Header Ads

HATIMA YA PONDA MACHI 4



Na Happiness Katabazi

UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya uchochezi na wizi wa malighafi ya Sh.milioni 59 inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda na wenzake 49 wameiomba  Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imuone Ponda na wenzake wanakesi ya kujibu kwasababu umeweza kujenga kesi yao.

Kesi hiyo ambayo jana ilikuja kwaajili ya upande wa jamhuri unaowakilishwa na wakili Mwandamizi wa Serikali Tumaini Kweka na Inspekta wa Polisi,  Hamisi Said na upande wa utetezi unaowakilishwa na Juma Nassor na Njama kuwasilisha majumuisho yao kwa njia yam domo ya kuomba mahakama iwaone washitakiwa wanakesi ya kujibu au la.

 Kwa upande wake wakili Kweka aliikumbusha mahakama kuwa washitakiwa wanakabiliwa na makosa matano ambayo ni kula njama kutenda kosa, kuingia kwa nguvu kwenye kiwanja cha Chang’ombe Markas ambacho ni mali ya Kampuni ya Agritanza Ltd, kujimilikisha kiwanja hicho, wizi na uchochezi.

Wakili Kweka alidai kuwa washitakiwa wote ni kweli walitenda makosa hayo na ndiyo maana walikuingia kwa jinai tangu Oktoba 12 hadi walipokuja kukamatwa usiku wa kuamkia katikaOktoba 17 mwaka jana katika kiwanja hicho na uwepo wao katika kiwanja hicho katika siku hizo zote ni ndiyo walitenda kosa la kujimilikisha kiwanja hicho isivyo halali.

Akilichambua kosa la wizi alidai kuwa wakati washitakiwa wameingia kwa jinai katika kiwanja hicho walikuta kokoto, mchanga mali ya Agritanza na kwa makusudi wakaamua kutumia malighafi hizo kwaajili ya kujenga msikiti mdomo ndani ya kiwanja hicho bila idhini ya mmiliki wa kiwanja hicho ambacho ni kampuni hiyo.

Kuhusu kosa la uchochezi wakili Kweka alidai kielelezo cha 13 kilichotolewa na Shahidi 17 ,F 8586/DC Ismail ambaye alimhoji mshitakiwa aitwaye Fiswaali ambaye ni mkazi wa Mlandizi ambaye katika maelezo yake ambayo yalipokelewa na mahakama kama kielelezo cha 13, alimweleza shahidi huyo kuwa yeye alisikia wito toka Redio Iman ambayo ilikuwa ikiwataka waislamu wote waende wakaongeze nguvu ya kujenga msikiti  katika kiwanja cha Chang’ombe Markas kwasababu kiwanja hicho mali ya waisilamu na kilikuwa kimeibwa.

“Kwa maelezo hayo ya mshitakiwa Fiswaali ambayo maelezo hayo yalipokelewa na mahakama kama ushahidi tosha kwa mshitakiwa wa kwanza(Ponda) na mshitakiwa wa tano (Mkadamu) walitenda kosa hilo la kuchochea washitakiwa waende kutenda makosa yanayowakabili katika kiwanja hicho.

Aidha Kweka ambaye alitumia dakika kumi tu kuwasilisha majumuisho alidai upande wa jamhuri umeweza kujenga kesi yake kupitia mashahidi wake 16 na vielelezo 13 walivyovileta mahakamani ambapo waamini kisheria vitawafanya washitakiwa wapande kizimbani kujitetea.

Kwa upande wake wakili wa utetezi Nassor Juma akiwasilisha majumuisho yake, aliomba mahakama iwaone washitakiwa hawa kesi ya kujibu na waachiliwe huru kwasababu kesi hiyo imefunguliwa na polisi kwa jazba na upande wa jamhuri umeshindwa kujenga kesi yao na kwamba mahakama kuwaambia washitakiwa wanakesi ya kujibu ni kuwasumbua bure washitakiwa.
Wakili Nassor alidai wanachokiona katika kesi hiyo ni kuwa kuna mgogoro wa ardhi ambao ulitakiwa ukatatuliwa kwanza na Mahakama ya Ardhi kwa mujibu wa kifungu cha 167 cha Sheria ya Ardhi Na.4 ya mwaka 1999.

Nassor alidai kuwa katika hati ya mashitaka ,kosa la kwanza ni la kula njama kutenda kosa na kwamba jamhuri imeshindwa kuanisha ni kosa gani hilo la jinai au madai lililotendwa na washitakiwa na kwamba hata hilo kosa la tano la kushawishi au uchochezi upande wa jamhuri umeshindwa kuanisha wazi washitakiwa walishawishiwa kutenda kosa lipi ambalo limesababishwa kufunjwa kwa sheria.

Akichambua kosa  kosa la pili, tatu na nne la kuingia kwa jinai, kujimilikisha kiwanja hicho isivyo halali na wizi, wakili huyo alidai washitakiwa hawakuingia kwa jinai kwani hata shahidi wa jamhuri ambaye ni mlinzi  alieleza kuwa Ponda alifika katika eneo hilo  akawasalimia Asalamaleku na  Asalamaleku manaake amani iwe  na kisha mlinzi huyo akampatia simu Ponda akaongea na shahidi wa tatu ambaye ni mmiliki wa kiwanja hicho Sulemain Hilary na kuhoji kuwa kama Ponda aliwasalimia vizuri , je huko ndiko kuingia kwa jinai?

Kuhusu kosa la wizi alidai washitakiwa hao hawajatenda kosa na upande wa jamhuri umeshindwa kulithibitisha kwani Hilal alitoa ushahidi unaosema ndani ya kiwanja chake kulikuwa na kokoto, mchanga ambazo hata hazijaletwa kama kielelezo na kwamba washitakiwa walichokifanya ni kutumia malighafi hizo kujengea msikiti mdomo na kwamba huo sio wizi.

“Sisi upande wa utetezi tunaiomba mahakama hii iwaachirie huru washitakiwa wote na iwaone hawana kesi ya kujibu kwasababu kesi hii imefunguliwa kwa jazba na polisi na upande wa jamhuri umehindwa kuleta ushahidi ambao utaweza kuishawishi mahakama iwaone washitakiwa wote wana kesi ya kujibu”alidai wakili Nassor.
Kwa upande wake Hakimu Nongwa aliarisha kesi hiyo hadi Machi 4 mwaka huu, ambapo atakuja kutoa uamuzi wa ama kuwaona washitakiwa wana kesi ya kujibu au la na kuamuru Ponda na Mkadamu warudishwe rumande kwasababu bado Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Dk.Eliezer Feleshi hajaondoa hati yake ya kuwafungia dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Machi Mosi mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.