Header Ads

HEKO OFISI YA DPP,POLE WAFUASI WA SHEIKH PONDA

 
 
 

Na Happiness Katabazi

MACHI 21 mwaka huu, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Sundi Fimbo aliwahukumu wafuasi 53 wa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Sheikh Ponda Issa Ponda kwenda jela mwaka mmoja baada ya kuwatia hatiani kwa makosa matatu likiwemo kosa la kufanya maandamano haramu ya kutaka kwenda ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP),Dk.Eliezer Feleshi kumshinikiza ampatie dhamana Ponda.

Hakimu Fimbo alisema alianza kwa kuikumbusha mahakama kuwa washitakiwa hao wanakabiliwa na makosa manne ambapo mshitakiwa Salum Bakari Makame na wenzake 52 wanaotetewa na wakili wa kujitegemea Mohamed Tibanyendera.

Kosa la kwanza ni la kula njama kutenda kosa kinyume na kifungu 384 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002, kosa la pili ni la kufanya mkusanyiko haramu kinyume na kifungu cha 74 na 75 cha sheria hiyo ambavyo vinasomwa pamoja na kifungu cha 43(2)(4) na 46 cha Sheria ya Jeshi la Polisi ya mwaka 2002 , kuwa Februali 15 mwaka huu, walitenda kosa hilo la kutaka kuandama kwenda katika ofisi ya Mkurugenzi Mkuu wa Mashitaka ,Dk.Eliezer Feleshi kumshinikiza ampatie dhamana Sheikh Ponda,kwani Feleshi amemfungia dhamana Ponda tangu Oktoba 18 mwaka jana hadi leo hii.

 Kosa la tatu ni la kukaidi amri ya jeshi la polisi iliyowataka watawanyike ambalo ni kinyume na kifungu 79 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu na kinachosomwa pamoja na kifungu cha 44 cha Sheria ya Jeshi la Polisi ya mwaka 2002 na kosa la nne ni la uchochezi ambalo lilikuwa likiwakabili washitakiwa watatu tu ambao ni Makame, Said Idd, Ally Nurdin Nandumbi ambao wote hawa Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP), aliwafungia dhamana tangu walipofikishwa kwa mara ya kwanza mahakama ni hapo Februali 18 mwaka huu.

Hakimu Fimbo alisema ili kuthibitisha kesi yao upande wa jamhuri uliokuwa ukiwakilishwa na mawakili waandamizi wa serikali Bernad Kongora,Peter Ndjike,na Joseph Mahugo na walileta jumla ya mashahidi 10 na upande wa utetezi walileta jumla ya mashahidi 54.

 “Baada ya kujiuliza maswali hayo mahakama hii imefikia uamuzi wa kuwaona washitakiwa 52 walitenda kosa la kula njama isipokuwa mshitakiwa wa 48 (Waziri Omar Toli) hakutenda kosa hilo kwa sababu alikutwa akitoka kununua mabeseni, mahakama hii imewatia hatiani kwa kosa hilo kwani kwa mujibu wa vielelezo vilivyoletwa mahakamani yaani barua iliyoandikwa na Taasisi ya Jumuiya ya Maimamu kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dar es Salaam kuomba kibari cha maandamano na polisi wakawakataza ila wakaandamana, washitakiwa wengine walikamatwa na vipeperushi, mabango,vipaza sauti vinavyosema ‘Dpp ukristo utakuponza’:

“Kwa vielelezo hivyo mahakama hii imeridhika kwamba walitenda kosa la kwanza, la pili na la tatu na kosa la nne ambalo ni la uchochezi mahakama hii imeona upande wa jamhuri umeshindwa kulithibitisha na kwasababu hiyo mahakama hii imewatia hatiani kwa washitakiwa wote kwa makosa matatu isipokuwa mshitakiwa 48 ametiwa hatiani kwa kosa la tatu tu” alisema Hakimu Fimbo.

Akilichambua kosa la pili ambalo ni la kufanya mkusanyiko haramu, hakimu huyo alisema pia mahakama inamuachilia huru mshitakiwa wa 48 katika kosa hilo,isipokuwa washitakiwa wengine wote wametiwa hatiani kwa kosa hilo kwasababu walikutwa katika maeneo tofauti wakitenda kosa hilo na katika utetezi wake walitoa walitoa ushahidi unaopishana ambao wengine walidai kuwa wa walikuwa wameenda kununua bidhaa,na walikuwa na fedha mfukoni lakini hata hivyo kiwango cha fedha walichokitaja polisi,na mahakamani ni tofauti ‘alisema hakimu Fimbo.

Hakimu huyo alisema kila kosa alilowatia nalo hatiani watalitumikia kifungo ha gerezani kwa mwaka mmoja,hivyo washitakiwa hao watatumikia adhabu ya mwaka mmoja jela.

Baada ya kumuliza kutoa hukumu hiyo, ndugu na jamaa wa washitakiwa hao waliigeuza mahakama na viunga vyake ni sehemu ya msiba kwani walianza kuangua vilio kwa sauti ya juu na kusababisha wanausalama kuwatoa nje.

Kesi hii ya kihistoria ilifunguliwa rasmi Februali 18 mwaka huu,saa nane mchana na siku hiyo hiyo upande wa jamhuri uliwasomea mashitaka na siku hiyo hiyo ukasema upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.


Februali 19 mwaka huu,upande wa jamhuri uliwasomea maelezo ya awali washitakiwa hao na shahidi wa kwanza wa upande wa Jamhuri ambaye ni Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Hemed Msangi na mashahidi wengine walianza kutoa ushahidi wao.

Februali 26 upande wa jamhuri ulifunga ushahidi wake. Februali 28 washitakiwa walianza kujitetea na Machi 19 upande wa utetezi ulifunga utetezi.

Februali 20 mawakili wa pande zote mbili waliwasilisha mahakamani kwa maandishi majumuisho ya mwisho ambapo mawakili wa upande wa Jamhuri waliomba mahakama iwatie hatiani washitakiwa wakati wakili wa utetezi aliomba mahakama iwaachilie huru kwa sababu hawana hatia.

Machi 21 mwaka huu mahakama hiyo ilitoa hukumu yake ambapo iliwahukumu washitakiwa wote kwenda jela mwaka mmoja.


Kwanza kabisa napenda kuipongeza timu ya mawakili wa serikali waandamizi iliyokuwa ikiongozwa na Bernad Kongora,Peter Ndjike,na Joseph Mahugo kwa kuweza kuleta ushahidi thabiti ambao umeweza kuishawishi mahakama hadi ikawatia hatiani washitakiwa.

Pili,nalipongeza jeshi la polisi ambao ndiyo walikuwa wakipeleleza kesi hiyo kwani waliweza kufanyakazi yao ya kipelelezi kwa kasi ya ajabu ukilinganisha na upelelezi wanaoufanya katika baadhi ya kesi nyingine ambao uwachukua muda mrefu kukamilisha upelelezi huku wakiacha watuhumiwa wa kesi mbalimbali kuendelea kusota gerezani.

Tatu, naupongeza uongozi wa Mahakama nchini kwa kutoa agizo maalum la kutaka kesi hiyo na ile kesi ya inayomkabili Ponda ambayo itatolewa hukumu Aprili 18 mwaka huu na hakimu Mkazi Victoria Nongwa, kusikilizwa mfululizo kila siku wakati kesi nyingine ambazo zimefunguliwa miaka mitano nyuma hazipata bahati hii ya mtende ya kusikilizwa mfululizo.

Lakini pia nawapongeza mawakili wa upande wa jamhuri na wakili wa utetezi Mohamed Tibanyendera kwa kuwaweza kutimiza wajibu wao wa kitaaluma wa kuisaidia mahakama kutoa haki bila kuingiza mbinu chafu za kuchelewesha kesi ambazo zimekuwa zikitumiwa na baadhi ya mawakili wahuni na wababaishaji(Delay Ethnics).

Lakini pia binafsi napenda kujipongeza mimi na waandishi wenzangu wa habari za mahakamani kwani tumeweza kuiripoti kesi hii mwanzo hadi mwisho.

Pia kuvipongeza vyombo vya ulinzi na usalama yaani askari wa Jeshi la Magereza na Polisi kwa kuimarisha ulinzi wa hali ya juu mahakamani hapo siku zote wakati kesi hiyo ilipokuwa ikisikilizwa tena katika mazingira magumu kwani ukumbi uliokuwa ukiendeshewa kesi hiyo ulikuwa hauna viti vya kutosha, hakuna feni.Na ninaomba nisisitize ushirikiano wa waandishi wa habari za mahakamani,mawakili ,wanausalama uzidi kuimarika.

Aidha napenda kutoa pole kwa washitakiwa 53 waliohukumiwa kwenda jela mwaka mmoja, pamoja familia zao, kwani ni wazi jela siyo sehemu nzuri ya kwenda kuishi ila kwasababu nchi yetu inaongozwa kwa utawala wa sheria basi yule yoyote anayetiwa hatiani kwa makosa mbalimbali mahakama inaweza kumpatia adhabu ya kwenda jela ambapo unapokuwa gerezani ni wazi uhuru wako unakuwa umezuiwa.

Kwanza kimsingi napenda mkubaliane na hesabu zangu kuwa kesi hiyo ya jinai Na.125/2013 ilidumu mahakamani hapo kwa siku 32 tu tangu ilipofunguliwa rasmi Februali 18 na kutolewa hukumu Machi 21 mwaka huu.

Kwa hiyo binafsi umalizikaji wa kesi hiyo haraka kiasi hicho binafsi umenifundisha mambo kadhaa ya msingi kuwa, kumbe mahakama, ofisi ya DPP na jeshi la polisi vikiamua kufanyakazi yao kikamilifu vinaweza sana, ila wakati mwingine uwa vyombo hivi ni kama vinaamuaga kujitoaga fahamu kwa kushindwa kutoa vipaumbele katika kesi za mbalimbali ili nazo zisikilizwe mfululizo kama hii ili watuhumiwa wajue hatia yao hali inayosababisha msongamano magerezani.

Itakumbukwa kuwa mwishoni mwa mwaka jana hadi Mwanzoni mwa mwaka huu, Tanzania iliingia katika historia chafu ya baadhi ya wananchi wake kujihusiasha na malumbano ya na vurugu za kidini hali iliyosababisha hata makanisa kuchomwa mto,na viongozi wa dini kuuwawa na kujeruhiwa lakini serikali iliweza kuwakamata wahusika na kuwafikisha mahakamani watuhumiwa na moja ya kesi inayooendana na madai ya udini ni hii ambapo imetolewa hukumu.

Najua makala hii itawakera baadhi ya watu ila napenda ieleweke wazi kuwa hukumu ya kesi hii ni funzo kwa wale wote wanaofikiri Tanzania ni chini ya kiuni na ambayo haiongozwi kwa utawala wa sheria,pia ni funzo kwa wale wote wanaofikiri dini ya kiislamu au kikristo ndiyo zinazoliongoza dola la Tanzania.

Lakini pia hukumu hii ni funzo kwa wale wote wanaoleta chokochoko za kidini pia kwa wale wafuasi wa vyama wa baadhi ya vyama vya upinzania hapa nchini ambao wamejiwekea kasumba ya kufanya maandamano haramu kwa kisingizio kuwa mahakama haiwezi kuwafunga jela washitakiwa wanaokabiliwa na kesi za maandamano haramu kwani magereza yamezidiwa na idadi kubwa ya watu na kwamba serikali haina uwezo wa kuwatunza wafungwa wengine wa kesi za maandamano haramu.

Nalisema hili kwasababu kuna wafuasi wa chama kimoja cha upinzani huko mitaani wamekuwa wakijifariji kuwa mahakama haiwezi kuwafunga jela washitakiwa wengi wanaokabiliwa kwa makosa ya maandamano na mkusanyiko haramu.

Leo hii wenzetu hao 53 waliofungwa jela, wale waliowatuma watenda makosa hayo wala hatukuwaona kuja mahakamani kuwasaidia zaidi ya ndugu na wake wa washitakiwa ndio kila siku walikuwa wakifika mahakamani kufuatilia kesi .

Watu hao 53 wanafamilia zao,wameziacha familia yao kwa mambo ya kijinga tu ya kukaidi sheria za nchi, leo hii nani atazihudumia familia zenu wakati nyie mpo gerezani?

Hukumu hii iwafumbue macho wafuasi wa vyama vya siasa ambao ni wao na familia zao ni malofa wa kutupa kama mimi wasikubali kushiriki maandamano haramu yanayoandaliwa na vyama vyao, kwani siku zote viongozi wa kubwa wa vyama visiasa ni kama mashetani ambao wamekuwa wakipenda kuwaamasisha watoto wawenzao washiriki kwenye vurugu ,maandamano haramu mwisho wa siku mtajikuta mnaangukia kwenye mikoni ya dola.Na muwajibu viongozi hao waende kuwachukua watoto wao wa kuwazaa na wake zao ndiyo washiriki maandamano hayo haramu ili wakutane na mkono wa dola.

Maana imekuwa ni desturi kwa wanasiasa hasa wa upinzani kuwakataza watoto na wake zao kushiriki kwenye maandamano haramu ila siku wanasiasa hao wakienda kuapishwa,au kwenye vikao vya bunge ndiyo uwachukua wake na watoto zao kwenda kustarehe ila kwenye maandamano haramu ambapo kule kuna virungu vya polisi na mabomu ya machozi hawazipeleki familia zao.

Ikumbukwe kuwa Watanzania wengine tunajifanya tunapenda wakati tukiwa na afya njema, tuna madaraka au uwezo fulani,hatuna matatizo na hatujafunguliwa kesi mahakamani ila ukiishaondoka madarakani, mali na fedha hauna,una ugua na umefunguliwa kesi mahakamani wale wote waliokuwa wanajifanya wapo karibu yao wanakukimbia na kuanza kukusema vibaya.Mifano ya haya ninayasema ninayo kwani nimeishuhudia na imenifundisha sana tu.

Mwisho, kasi hii ya kutisha ya kuimaliza kesi hii pia ipelekwe kwenye kesi za maandamano na mkusanyiko haramu zilizofunguliwa katika Mahakama za Arusha,Dar es Salaam na kwingineko ambazo zinawakabili viongozi wa siasa na wafuasi wao ili nazo kesi hizo ziweze kumalizika kwa haraka na hatimaye watuhumiwa wapatiwe haki yao na mahakama.
 
Chanzo:www.katabazihappy.blogspot.com ; Aprili 3 mwaka 2013. 

No comments:

Powered by Blogger.