Heri kuleta timu za taifa kuliko Real Madrid


Real Madrid ni wageni wa rais Kikwete binafsi au rais wa Tanzania?
.Ujio wake ni gharamazaidi kuliko faida
.Ni fahari ya kisiasa kuliko uchumi,kisoka
.Mamilioni yangewekezwa kwa soka la vijana

Na Happiness Katabazi

Kwani Klabu ya Real Madrid ina kuja Tanzania kama mgeni wa nani?
Ni mgeni wa Rais Jakaya Kikwete binafsi au wa rais wa Tanzania, kwa hiyo kwa gharama za nani? gharama ya mlipa kodi?
Kwa hiyo sisi Watanzania tunaishi kwa ufahari na pesa nyingi za kutupa kwa kuwalipa wachezaji nyota ambao baadhi yao wanalipwa Sh Milioni 200 kwa wiki.
Sasa hawa wachezaji wanakuja hapa nchini watatusaidia nini hata kama watacheza na timu yetu ya Taifa.
Real Madrid ni klabu wala siyo timu ya taifa fulani, sasa mimi sioni faida yake kwa kuwa hata timu yetu ikiifunga licha ni ndoto za mchana, haitaonyesha kama imeifunga timu ya taifa fulani. Sasa inakuja hapa kwa misingi gani?
Mimi nafikiri kila kitu lazima kiendane na uwezo, kwa hiyo hata kama Watanzania tungependa klabu hiyo ije icheze hapa, ni ndoto ambazo zikiingizwa kwenye mfuko wa mlipa kodi zitatupeleka pabaya.
Kwa sababu taifa lina mambo mengine ya kipaumbele kuliko kujiingiza kwenye anasa za michezo kama hii.
Kwa sababu kama ni suala la kukuza vipaji, basi fedha zitakazotumika kuwa ‘kirimu’ Real Madrid, zingetumika kuibua vipaji na kuendeleza michezo katika shule nyingi hapa nchini.
Lazima tuwe na maono ya mbali na kuweza kutofautisha michezo kama anasa na michezo kama elimu na uwezeshwaji wa wananchi.
Michezo inapokuwa kwenye ngazi ya klabu ni vyema tuiachie sekta binafsi ya michezo (klabu ikaalika klabu yenzake kwa kuwa itajua vema ni jinsi gani itagharamia hiyo lakini mlipa kodi halazimiki kuchangia).
Rais wetu Jakaya Halfan Mrisho Kikwete,, anaposafiri nje ya nchi, ajitambue ni kiongozi wa wananchi na wananchi wake wanaishi kwenye lindi la umaskini uliotukuka.
Ambao hawana chakula,tiba,umeme wa uhakika, barabara,maji safi na salama ya kunywa na hivyo,wanafunzi wamerejeshwa majumbani kwa kukosa mikopo, asijione yeye ni sawa na Mfalme wa Saudi Arabia, anayeongoza kutoa mialiko bila kujali athari zake kiuchumi kwa watu wake.
Kwa sera,mtindo huu wa Rais Kikwete, maskini wa Tanzania watapasuka mapafu.Anatupeleka kwa ari,kasi na nguvu ya kutuua kabisa.
Natoa mfano halisi pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wanafunzi hawana maji ya uhakika, vyoo vinanuka,hawana madarasa ya kusomea,mabweni hayatoshi wanapanga uraiani ,wahadhiri wanalalamika kwamba mishahara wanayopewa ni midogo na aikidhi mahitaji ,wanafunzi hawana mikopo,lakini rais wa watu hawa yupo tayari kumlipa star ya Real Madrid Sh.Milion 200 kwa wiki . Hakika hii ni busara isiyo na busara.
Mwishoni mwa mwaka jana, Soko la Mwanjelwa mkoani Mbeya, liliteketea kwa moto na kusababisha hasara ya mamilioni na wafanyabiashara wa soko hilo wengi ni raia wa kawaida wa kima cha chini.
Serikali ya awamu ya nne haijawajibika kwa namna yoyote ile. Na kama serikali inaweza kuchangisha wafanyabiashara wakubwa wawape fedha za bure klabu ya Real Madrid, kwa nini serikali hiyo isiwachangishe wafanyabiashara hao wakubwa wawasaidie wafanyabishara wa Soko la Mwanjelwa?
Tembelea hospital yaTemeke,Mwananyamala, utaona wakina mama wajawazito wanavyojifungua katika hali duni.
Hutaona wagonjwa wanavyoishi katika hali duni,utaona mitambo ya kawaida kama X-Ray haipo lakini Rais wetu, ndoto zake zipo kwenye starehe ya Real Madrid. Je huyu ni rais wa walala hoi?
Upo umaarufu wa bure wa kusikika kwamba wewe ndiye rais pekee uliyeleta timu hiyo na watoto wa kijiweni watakusifia kweli kweli bila kujali kwamba hata hiyo fedha ya kuingia langoni kuwaona mastar wa real Madrid wakilisakata kabubumbu hawatakuwa nayo.
Kwa hiyo JK kakosea, kama yeye alikuwa na akiba yake binafsi hivyo anaileta timu hiyo kwa gharama zake hiyo ni sawa, hatuna ubishi.
Lakini haiwezekani, hatutaki na tunakemea Rais wetu kualika klabu hiyo ya nje na kutumia wadhifa wa Urais kutoa maelekezo ya kuchangisha gharama za klabu hiyo.
Hilo hatulitaki kwa sababu ni kudhalilisha nafsi hiyo ya urais wa Tanzania.Kumbe rais wetu sasa ni wakala wa kawaida wa klabu za michezo za Ulaya?
Rais hakutakiwa kabisa kujiingiza katika biashara ya klabu za mpira,yeye kama raia angeweza akafanya mipango ya kualika timu za Mataifa mfano timu ya taifa ya Nigeria, Hispania, Italia, Afrika Kusini, Ujerumani, England na kadhalika.
Na hizo timu ingekuja hapa nchini,itakuja kama sehemu ya ushirikiano wa Utamaduni kati ya nchi yetu na nchi hiyo na isingekuwa na gharama za kibiashara kama hizi kwakuwa taifa ya timu yake ingechangia gharama na sisi taifa letu lingechagia gharama ukitofautisha na ujio wa Real Madrid, wananchi na makampuni ya hapa yataigharimia kwa asilimia mia moja.
Hivyo fikra hizi za kualika nyota wa klabu ya Real Madrid, kuja hapa nchini kupora kile kidogo kilichosalia mifukoni mwa

Watanzania, tunazipinga kwakuwa hazituakikishii maisha bora kwa kila Mtanzania, badala yake ina mwakikishia Mtanzania wa kawaida atakuwa maskini maradufu.

Mungu ibariki Afrika!
Mungu inusuru Tanzania.
katabazihappy@yahoo.com

Taaluma ya Habari:Inaandaliwa Kitanzi!



Taaluma ya Habari: inaandaliwa kitanzi!

Na Happiness Katabazi

DEMOKRASIA ni msingi wa utawala bora na utawala bora ni kutawala kwa misingi ya uwazi, ukweli na kuwashirikisha wananchi.
Uwazi katika Serikali ni nini? Uwazi katika uendeshaji wa serikali yoyote ile unamaanisha kwamba, shughuli zote za serikali ziwekwe wazi kwa wananchi.
Taasisi/mhimili unapojihusisha na kuhabarisha wanajamii ni vyombo vya habari. Kwa hiyo, serikali iwe tayari kutoa habari kwa waandishi wa habari wazifikishe kwa wananchi.
Sasa kilichotokea kwenye Rasimu ya Muswada wa Uhuru wa Habari wa mwaka 2006 nchini ni kwamba, habari zote zinazohusu uundwaji wa sera za nchi ni siri kwa mujibu wa kifungu cha 28 cha rasimu yenyewe.
Habari zote zinazowasilishwa na kujadiliwa ndani ya baraza la mawaziri na maamuzi ya baraza la mawaziri ni siri kwa mujibu wa kifungu cha 27 cha rasimu hiyo.
Habari zote zinazohusu usalama wa Taifa, Ulinzi wa Taifa, Ushirikiano wa Kimataifa ni siri kwa mujibu wa kifungu cha 29 cha rasimu hiyo.
Habari zote ambazo zimelindwa na sheria, kanuni au mila za usiri wa shughuli za usiri wa serikali ni siri kwa mujibu wa kifungu cha 31 cha rasimu. Pia habari zote zinazohusu siri za biashara na biashara ni siri kwa mujibu wa kifungu cha 33.
Habari zote zinazogusa maslahi ya uchumi wa nchi ni siri kwa mujibu wa kifungu cha 34. Habari zote zitokanazo na utafiti kwa mujibu wa kifungu cha 35 cha rasimu ni siri. Habari zote zilizopatikana kwa ahadi kwamba zitabaki siri nazo pia ni siri kwa mujibu wa kifungu cha 36.
Habari zote ambazo uchapishwaji wake unaweza ukaathiri maslahi ya Taifa, jamii ni siri kwa mujibu wa kifungu cha 38. Na Waziri husika anapewa mamlaka ya kutangaza habari fulani ni siri na isitolewe na vyombo vya habari kwa kuwa itaathiri maslahi ya taifa kwa mujibu wa kifungu cha 42 cha rasimu hiyo.
Wanahabari wenzangu na jamii kwa ujumla ukijumlisha vipengele vyote hivi na ukizingatia kwamba kwa mujibu wa sheria ya Uhifadhi wa Nyaraka za Taifa , muda wa usiri ni miaka thelathini.
Je, huo uwazi wa serikali yetu katika misingi ya utawala bora uko wapi? Kwanini serikali yetu inapenda ngonjera hata kwenye maswala nyeti kama haya?
Hebu viongozi tuliowapa dhamana ya kutuongoza, tuelezeni kwa fikra zenu uwazi katika shughuli za serikali ni kitu gani?
Au sasa tuseme mawaziri na viongozi wa serikali wanapofanya harusi kubwa za watoto wao, birthday ya Taifa, safari za Rais na Waziri Mkuu nje ya nchi ndiyo habari za kuwaambia wananchi?
Tuachane na hilo, rasimu ya mwasada huu ni mbaya pia kwasababu unaweka vipengele vitakavyounda baraza la habari la serikali, hilo limeitwa Media Standard Board kwa mujibu wa kifungu cha 57 cha rasimu hiyo.
Sasa baraza hili linaundwa ili kutawala na kudhibiti taaluma ya habari nchini kwa hiyo baraza hili ndilo litakuwa na uwezo wa kubuni maadili,kuyaweka na kuwadhibiti wanahabari kulingana na maadili hayo.
Baraza pia litakuwa na uwezo wa kutoa leseni za uandishi wa habari kulingana na masharti yatakayowekwa na baraza.
Mwenyekiti wa baraza hili atateuliwa na rais na litakuwa ni taasisi ya serikali. Pia baraza hili litakuwa na mamlaka ya kusikiliza malalamiko ya wanajamii dhidi ya wahandishi wa habari.
Taasisi ya Uandishi wa habari ni muhimili usio rasmi wa dola ambao ni vyema ukibaki huru bila kuingiliwa na dola.
Kwa rasimu hii kwa mara ya kwanza, muhimili huu una rasimishwa kwa mithili ya kutawaliwa na kufungwa minyororo badala ya kulindwa na kupewa uhuru kwa kutekeleza kazi zake.
Baraza la habari lililopo limeundwa na wadau wa habari baada ya serikali kushindwa kuunda baraza hilo mwaka 1993, kutokana na harakati za wadau kupinga kuundiwa habari na serikali.
Leo hii wanahabari tuna baraza letu tunalolitii na kulithamini ambalo utendaji wake ni wakusifika.
Baraza la habari la Tanzania lina ufanisi wa asilimia 97, kwamba mashauri yote yaliyoamriwa na baraza yametekelezwa kwa ufanisi huo.
Sasa kwanini serikali inataka kuiondolea jamii taasisi inayojiendesha yenyewe, inayofanyakazi kwa ufanisi ili kutuundia baraza la kikilitimba la serikali?
Shime wanahabari, tushike kalamu na Note Book, tujitome kwenye vyombo vyote vya habari kuhakikisha tunaandika makala na habari kwa mapana zaidi kuhusu hii rasimu ili wanajamii ambao nao wanaitaji kupata habari wajue serikali imedhamiria kuichinja chinja taaluma ya habari.
Nanimalizie makala hii kwakumwoma Rais Kikwete, aisome rasimu vilivyo aone vipengele vilivyowekwa ambavyo vinachinja taaluma ya uandishi wa habari wa hapa nchini kwake na kisha arejee maagizo na ahadi zake ambazo amekuwa akizitoa alipoingia madarakani kuwa serikali yake itashirikiana kwa karibu na vyombo vya habari na pia alikuwa akiwataka watendaji wake kutowakimbia na kutowanyima habari waandishi wa habari.
Binafsi naamini maagizo na ahadi zake hizo alikuwa akizotoa kwa moyo mmoja ila kama alikuwa akizitoa kwa malengo ya kufurahisha umma basi ukweli utadhihirika pale atakapo kubali rasimu hii iwe sheria na pia ndipo tutakapo amini msemo maarufu usemwao “hakuna urafiki wa kudumu baina ya wanasiasa na wanahabari’.
Mungu Ibariki Tanzania
0755-312859:katabazihappy@yahoo.com
mwisho

KARIBUNI WASOMAJI WANGU KATIKA SAFU HII

Ndugu Wasomaji,
Kwa mara nyingine tena ni yuleyule mwandishi wako mwenyefikra za Kimapinduzi Happiness Katabazi, nimejitokeza tena katika ulimwengu wa Sayansi na Teknolojia kwaajili ya kuwaletea makala za uchambuzi wa masuala mbalimbali hususani chambuzi za siasa hapa Tanzania.

Katika safu hii nitakuwa nikiwaletea chambuzi wasomaji wangu napia natoa nafasi kwenye ya kutoa maoni kuhusu makala hizo pia nakaribisha pongezi na mawazo mbadala kutoka kwenu

Naamini mtajifunza kupitia makala zangu nami pia nitajifunza kutokana na mawazo yenu.

Napatikana kwa simu Na:
0755 312859

ASANTENI