CCM Inawachimbia kaburi Wabunge Wake

Na Happiness Katabazi

WANAFALSAFA wa masuala ya sayansi ya jamii, wanaamini kuwa nyakati zinafundisha binadamu kufikiri na kutenda kulingana na mahitaji ya watu na mabadiliko.

Kwa nini wanafalsafa hao wanadhani na kufikiri hivyo? Wanaamini kwamba ushujaa wa jana, waweza ukaonekana kuwa ufisadi leo.

Nayasema haya kutokana na mwenendo wa Bunge letu la Bajeti linaloendelea mjini Dodoma, dhidi ya mwenendo wa kiongozi wa serikali bungeni, Waziri Mkuu, Edward Lowassa na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yusuf Makamba.

Kwa nafasi yake Lowassa, kama kiongozi wa serikali bungeni anayetokana na chama tawala cha CCM, amekuwa akiwaita wabunge wa chama chake na kukaa kama kamati kwa lengo la kuwafunda kila linapotokea tatizo linaloonyesha udhaifu ndani ya serikali.

Lowassa na Makamba, Jumamosi iliyopita waliongoza kikao cha wabunge wa CCM kwa lengo la kufanya tathmini ya mjadala wa hotuba ya bajeti ya Wizara ya Fedha.

Katika kikao hicho, wabunge wa CCM wanadaiwa kuzibwa midomo ili wasiikosoe serikali kwenye vikao vya Bunge kwani ukosoaji huo eti unamkera Mwenyekiti wa CCM ambaye pia ni Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete.

Kikao hicho kilitawaliwa na mazungumzo ya kuwatisha wabunge wa CCM ambao walikosoa bajeti ya mwaka 2007/2008 wazi wazi.

Mbunge wa Nzega, Lucas Selelii, alitishia kuondoa shilingi katika mshahara wa Waziri Mkuu kwa kutoonekana kwa baadhi ya barabara katika bajeti ya mwaka huu ambazo zimeainishwa katika bajeti ya mwaka wa fedha unaoishia Juni mwaka huu.

Akichangia hotuba ya Wizara ya Fedha katika majadiliano yanayoendelea bungeni, Selelii alisema katika bajeti ya awamu iliyopita barabara hizo ziliainishwa, lakini kwenye bajeti ya awamu hii hazionekani.

Akiwa amekwisha kutamka kuwa na mwongozo wa Mungu katika mchango wake huo, mbali na kutamka nia yake ya kutoa shilingi katika mshahara wa Waziri Mkuu, Selelii pia alizishambulia Wizara ya Nishati na Madini na Wizara ya Miundombinu kuwa mipango yake kwa mwaka 2007/2008, hairidhishi. Nako alitishia kuondoa shilingi.

Hata hivyo alisema analazimika kukubaliana na bajeti hiyo kwa shingo upande kwa kuwa hana jinsi ya kuipinga kutokana na kubanwa na ilani ya uchaguzi ya chama chake.
Inawezekana kabisa kwamba CCM inafanya hivyo kwa nia njema kabisa, lakini, kwetu sisi tulioko nje na ambao ni wengi na tuliowatuma wabunge wetu kusema hayo wanayodadisi, hatuwezi kuwa na tafsiri nyingine juu ya mwenendo huo wa kufinya sauti ya umma.

Katika mfumo wa demokrasia ya uwakilishi, jamii inawategemea wabunge wao wakawasemee yale wanayohitaji kwa ajili ya maendeleo yao na pia yanayowakwaza, bungeni.

Katika mfumo wa demokrasia ya uwakilishi, jamii inategemea kusikia hoja za wawakilishi wao zikipatiwa majibu sahihi kutoka katika serikali yao ambayo wao ndio wameiweka madarakani.

Kinyume cha hapo kama serikali itataka kila inachokisema na inachokitaka kipite tu bila vikwazo, tena kwa lazima, basi hilo halitakuwa jumuiko la Bunge kwa maana ya mkusanyiko wa watu waliofikishwa huko kwa njia ya demokrasia.

Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kusema kwamba ‘ukweli una tabia moja nzuri sana. Haujali mkubwa wala mdogo na wala haujali adui wala rafiki.’

Ieleweke nayaandika haya si kwa kuwachukia Lowassa, Makamba au kiongozi yeyote yule wa serikali anayeingilia uhuru wa maoni ya wabunge wetu. Nasisitiza mawazo ya wabunge wetu lazima yaheshimiwe.

Tunasema hivyo kwa sababu serikali, kama serikali inaweza isiyajue mahitaji halisi au wananchi na hivyo hata mipango yake ikawa ni ya mbali sana na wananchi.
Lakini wabunge kama wawakilishi wa wananchi, wanaishi nao na hivyo wanayajua mahitaji na vipaumbele vya wananchi.

Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, alikuwa kiongozi wa shughuli za serikali bungeni pekee kwa kipindi cha miaka kumi ambaye alimudu vyema kufanya kazi yake bila ya kuitisha vikao vya falagha kuwafunga midomo wabunge ambao walikuwa wakiichambua serikali.

Sote tutakumbuka Bunge la mwaka 1995-2000 lilikuwa na idadi kubwa ya wabunge wa kambi ya upinzani kama kina Ndimara Tigambagwe, James Mbatia, Dk. Masumbuko Lamwai, Mabere Marando, Agustine Mrema na wengine, hakika walilichachafya Bunge na serikali.
Lakini kamwe hatukuwahi kusikia kwenye vyombo vya habari kwamba Sumaye alikuwa akifanya pilikapilika za kuitisha vikao na kutumia mbinu za kuwaziba midogo.

Sasa ajabu tunayoiona hivi leo ambapo ndani ya Bunge kuna idadi ndogo ya wabunge wa upinzani lakini tunashuhudia wabunge wakiminywa sauti zao.

Narejea kauli ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema) mapema mwaka huu alidiriki kusema wazi wazi kwamba serikali imekuwa kikwazo cha demokrasia ndani ya Bunge. Hakika hii si sifa nzuri hata kidogo.

Hatari ninayoiona hapa ni kwamba endapo CCM itaendelea na utaratibu wake huo wa kuwakusanya wabunge wa CCM, na kuwafunda pindi wanapoonekana kuibana serikali, basi itambue ajira za wabunge zitakuwa shakani katika uchaguzi ujao.

Inachokifanya CCM leo ni sawa na kuwachimbia kaburi wananchi, kwani hawataeleweka kwamba chama kimeweka msimamo wa kutohoji kushindwa kutekelezwa kwa baadhi ya miradi na ahadi za wakati wa kampeni.

Kwa vyovyote vile, ipo siku watasimama na kumhoji mbunge wao aliyesimama ndani ya Bunge, akatoa hoja zake nzito za utetezi wa wananchi wake hadi povu likamtoka mdomoni, lakini akaishia kupitisha bajeti ya wizara kwa asilimia 100 wakati hatapewa majibu ya hoja zake.

Ikifika hapo, ajue ajira yake hiyo ya kisiasa, itakuwa halali kwa kambi ya wapinzani kwa kuwa jamii kwa ujumla na wapinzani wa kisiasa wa mbunge husika wa ndani na nje ya chama chake, wanamsikia na kumpima kwa umakini mkubwa sana.

Kwa bahati nzuri sana, hivi sasa Watanzania wengi wameamka.Yote haya yanayotendeka ndani ya Bunge na yote yanayofanywa na viongozi wa CCM, wanayatambua. Wanaweza wasiyaseme leo, lakini 2010 hawatakaa kimya.

katabazihappy@yahoo.com; www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamis.Juni 28,2007

MWANAMKE WA SHOKA JESHI LA POLISI TANZANIA


KUTANA NA MWANAMKE WA SHOKA JESHINI…
Sydney Mkumbi:
Mwanamke ‘mzito’ pekee Jeshi la Polisi
.Ndiye aliyeongoza kumhoji Abdallah Zombe
.Ni bosi kitengo cha makosa dhidi ya binadamu

KUTANA na mwanamke wa kwanza ndani ya Jeshi la Polisi anayeongoza Kitengo cha Makosa dhidi ya Binadamu, Kamishna Msaidizi Mwandamizi (SACP), Sydney Ramadhani Mkumbi, ambaye katika makala hii amepata fursa ya kuelezea masuala mbalimbali yanayohusu jeshi hilo na historia ya maisha yake kama alivyofanya mahojiano mapema wiki hii na Mwandishi Wetu, Happiness Katabazi.

Swali: Ni kitu gani kilikusukama hadi ukajiunga na Jeshi la Polisi?

Jibu:
Ukakamavu waliouonyesha askari wa kike walipofika kutembelea Shule ya Sekondari ya wasichana Tabora mwaka 1960. Jinsi walivyokuwa wanatembea, hata walivyokuwa wanajieleza mbele ya kadamnasi, walinivutia sana.

Swali: Wewe kama mama wa familia unawezaje kumudu kazi ya jeshi na familia?
Jibu: Kupanga ni kuchagua. Kazi yoyote utakayoifanya bila kupanga huwezi kuimudu. Hivyo wakati wa kazi ni kazi kweli, na familia ina muda wake wa kuiangalia. Hata hivyo namshukuru mume wangu aitwaye Ramadhani Mkumbi, ambaye naye pia ni Ofisa wa Polisi, kuwa ni mwelewa na ni mvumilivu, anathamini kazi yangu na amekuwa bega kwa bega nami kwa kila ninachokifanya, namshukuru sana.

Swali: Inasemekana kwamba nafasi za kujiunga na jeshi hivi sasa ni lazima uwe na kigogo akukingie kifua ndipo upate nafasi. Unalizungumziaje hili?


Jibu: Siyo kweli, binafsi naelewa kwamba kuna ushindani mkubwa katika kujiunga na Jeshi la Polisi hivi sasa. Kwa sababu watu wengi wanapenda kujiunga na jeshi na nafasi ni chache. Aidha, kuna masharti ambayo yameainishwa kwa waombaji. Wakiyatimiza wanateuliwa.

Swali: Kuna wasichana uraiani wanapenda kazi ya jeshi, lakini wamejaribu kutafuta kazi hiyo hawajafanikiwa unawashauri nini wasichana hawa?

Jibu: Kama wana elimu inayohitajika na kama wanatimiza masharti kama vile urefu wa futi 5 nchi 3 na miaka isiyozidi 25 wasikate tamaa. Aidha waepukane na makundi ya uovu bali wawe karibu na Jeshi la Polisi kufichua maovu.

Swali: Unafikiri idadi ya wanawake waliobahatika kupata uongozi ndani na nje ya jeshi wanatosha, na kama hawatoshi nini kifanyike?

Jibu: Hawatoshi. Na tuliobahatika kupata uongozi tuonyeshe kumudu vema madaraka yetu. Na hao walio nyuma yetu waonyeshe uwezo ili viongozi wetu na serikali kwa ujumla wazidi kuwa na imani na utendaji kazi wetu.

Swali: Wewe ni askari mwanamke mwenye cheo cha juu kuliko askari wanawake ndani ya Jeshi la Polisi nchini, unafikiri askari wa kike waliojiunga na jeshi katika karne ya 21 ni tofauti na askari wa kike ukiwemo wewe mmoja wao mliojiunga na jeshi hilo katika karne ya 20?

Jibu
: Tofauti iliyopo kati ya askari waliojiunga karne ya 20 na hii karne ya 21 haiwahusu askari wa kike tu, bali askari wote kwa sababu askari wengi waliojiunga katika karne ya 20 walijiunga kwa wito, hivyo wanaipenda kazi yao na kuifanya kwa uadilifu. Tofauti na wa karne ya 21 ambao baadhi ya wameingia kukidhi haja ya ajira tu.

Swali: Unafikiri idadi ya wanawake waliobahatika kupata uongozi ndani na nje ya jeshi wanatosha na kama hawatoshi nini kifanyike?

Jibu:
Awali ya yote niishukuru serikali iliyomo madarakani kwa kutambua umuhimu wa jinsia na kusema kweli maeneo mengi yaliyopewa wanawake kuongoza, wameonyesha umahiri wa uongozi. Hivyo basi tuliopewa nafasi ya uongozi tuitumie vizuri ili iwe kivutio/hamasa na kigezo kwa serikali kuendelea kutupa uongozi.

Swali: Binafsi tueleze jambo lililowahi kukutokea ambalo hutalisahau katika maisha yako?

Jibu: Nakumbuka kati ya mwaka 1976/1977 nikiwa Mwendesha Mashitaka Mahakama ya Mkoa wa Dodoma mbele ya aliyekuwa Hakimu wa Mkoa Mh. Kajeri, alimhukumu mtuhumiwa mmoja (jina nalihifadhi) kwenda jela miaka mitatu kwa kosa la unyang’anyi wa kutumnia nguvu na mara baada ya mahakama kwisha mtuhumiwa alimrukia mlalamikaji na kumkaba koo nusura amtoe roho, ndipo nilipovua kiatu aina ya gongo na kumtwanga nacho sehemu ya hatari (pressure point) na kumfanya aone giza na kumnusuru mlalamikaji. Nina sisitiza sitalisahau tukio hili.

Swali: Imekuwa ikidaiwa kwamba ndani ya majeshi yetu askari wa kike wamekuwa wakinyanyaswa kijinsia na askari wanaume, unalizungumziaje?

Jibu:
Binafsi, nakubaliana kabisa na wewe kwamba miaka ya nyuma sisi askari wa kike tulikuwa tukinyanyaswa sana na askari wanaume kwa sababu tulikuwa na mipaka ya kufanya kazi kwa mfano ilikuwa si rahisi kumkuta askari wa kike akifanya kazi wilayani, ilikuwa tunafanyia kazi makao makuu ya mkoa tu.
Lakini hivi sasa wanaume hawatunyanyasi kwa kuwa tunajua haki zetu hivyo tunafanya kazi nao sambamba.

Swali: Unazungumziaje mwaka mmoja wa utawala wa Mkuu wa Jeshi la Polisi Inspekta Jenerali (IGP), Said Mwema?

Jibu: Isitoshe tu kusema kwamba pamoja na mambo mengine, serikali kutambua umuhimu wa kuunda wizara inayoshughulikia mambo ya kipolisi, kuwepo na uwezo zaidi wa kiuchumi serikalini.

Wananchi kutambua matatizo yanayoikabili idara hasa baada ya uhalifu wa kimataifa kuibuka nchini ghafla na la muhimu zaidi Inspekta Jenerali wa Polisi wa sasa kuwahi kufanya kazi Shirikisho la kimataifa la Jeshi la Polisi (Interpol) kumemsaidia kuleta ubunifu na maboresho zaidi katika jeshi letu ili liwe la kisasa.

Mabadiliko katika Jeshi la Polisi yanachangiwa na mkakati wake wa ulinzi shirikishi na ulinzi jirani ambao umesaidia kuliweka Jeshi la Polisi kuwa karibu na wananchi, hivyo wananchi wamejitokeza kutoa taarifa za uhalifu.
Mwisho, lakini si katika umuhimu, mabadiliko katika Jeshi la Polisi yanachangiwa na kaulimbiu ya serikali ya Awamu ya nne ya Ari mpya, Nguvu mpya na Kasi mpya, nayo yamesaidia mahitaji ya polisi ambayo hayakuwepo hapo nyuma kupatikana.

Swali: Wewe ni miongoni mwa askari wanawake wachache ndani ya Jeshi kuteuliwa kuwa mkuu wa kitengo cha makosa dhidi ya binadamu yakiwamo makosa ya mauaji, ubakaji na malalamiko, unadhani unapewa ushirikiano wa kutosha na askari wanaume?

Jibu: Ninapewa ushirikiano mkubwa sana na wanaume kwani watendaji kazi wakuu wengi wao ni wanaume.

Swali: Lini umeteuliwa kuwa mkuu wa kitengo cha makosa dhidi ya binadamu?
Jibu: Niliteuliwa kuwa mkuu wa kitengo hicho mwaka 2004 ambapo hadi sasa nakiongoza kitengo hiki.

Swali: Ni changamato gani zinakikabili kitengo chako unachokiongoza?

Jibu: Kama mkuu wa kitengo cha makosa dhidi ya binadamu, changamoto ambayo inanikabili katika kitengo hiki hasa ni pamoja na ucheleweshaji wa upelelezi hususan makosa ya mauaji, ubakaji na kadhalika, hivyo kusababisha mlundikano wa mahabusu magerezani na hata malalamiko kuwa mengi kana kwamba kwa sababu uchunguzi umekwama, basi mtuhumiwa anadai kubambikiwa kesi.
Hivyo kama mkuu wa kitengo ninalazimika kuwahimiza wakuu wa upelelezi wa mkoa kusimamia upelelezi na wakati mwingine kufanya semina kukumbushana/kuelimishana na wakati mwingine kukemea ucheleweshaji wa upelelezi wa makosa ya jinai kwa ujumla na athari zake.

Swali: Ni askari wanawake wangapi kwa sasa wana cheo kama chako cha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP)?

Jibu: Kwa sasa ni mwanamke peke yangu ndiye mwenye cheo hiki cha (SACP), na ninaweza kusema mimi ni mwanamke wa tano kushika cheo hiki kwani tayari hapo nyuma kulikuwa na maofisa wanawake wanne ambao wamestaafu kwa muda tofauti walikuwa na cheo hiki cha Kamishna Msaidizi Mwandamizi.


Swali: Tupatie siri ya mafanikio yako hadi ukakikwaa cheo cha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) kwa kuwa ni nadra mno kwa askari wa kike kupata cheo hicho?

Jibu: Ukweli wanawake ni wachache, sana ambao tumefikia cheo hiki cha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) na siri ya mafanikio yangu hadi kufikia hapa nilipo ni kufanya kazi kwa uaminifu, uadilifu na kufuata taratibu zote zilizopo katika jeshi letu ikiwa pamoja na kuwatii viongozi wangu na kutekeleza maagizo/amri halali ninazopewa.
Aidha, niwashukuru kwa dhati kabisa wazazi wangu Bwana na Bibi Nathaniel Mpena (ambao wote ni marehemu “Mungu awaweke mahali pema peponi)’ ambao walinilea katika maadili ya dini na kunisimamia hadi kupata elimu ambayo ilikuwa adimu kwa wanawake wa wakati ule.

Swali:Tupatie takwimu za makosa ya binadamu ambayo umewai kuyapokea na yakafanyiwa kazi?

Jibu:
Nisikufiche, kwasasa siwezi kukutajia idadi kamili ya makosa ya binadamu kwani makosa yanayoletwa hapa ni mengi mno. Ila ninachokumbuka mwaka 2006 mimi nilikuwa ni Mwenyekiti wa Tume ya Polisi ya kumhoji aliyekuwa Kamanda wa Upelelezi Kanda ya Dar es Salaam, ACP- Abdallah Zombe, na wenzake 12, wanaokabiliwa na tuhuma za mauaji ya watu wanne ambao ni wafanyabiashara ya madini na wakazi wa Mahenge mkoani Morogoro, ambao kabla ya mimi kuongoza tume ya kuwahoji, Tume ya Rais ya kuchunguza mauaji ya watu hao iliyokuwa ikiongozwa na Jaji Kipenga Mussa, ambayo tume hiyo baada ya uchunguzi wake ilibaini kwamba wafanyabiashara wale hawakuwa majambazi kama ilivyokuwa imedaiwa awali na Jeshi la Polisi.

Swali: Naomba kufahamu historia ya maisha yako kwa mapana.

Jibu: Mimi ni mtoto wa tano katika familia ya watoto saba kwa mzee Nathaniel Mpena, mzaliwa wa Kijiji cha Lukula wilayani Sikonge, Tabora. Nimesoma Shule ya Msingi Iwensato II, kati ya mwaka 1958-1960. Shule ya wasichana ya kati Usoke, na mwaka 1961-1964 nilijiunga na kuhitimu Shule ya Sekondari ya wasichana Tabora mwaka 1965-1968.
Nilipohitimu shule Februari 18, 1969 nilijiunga rasmi na Jeshi la Polisi katika Chuo cha Polisi (CCP) Moshi na kufanya kazi mikoa mbalimbali ikiwemo CCP Moshi, Dodoma, Mtwara, Kilimanjaro na Makao ya Polisi Idara ya Upelelezi.
Aidha, nimefanya kazi mbalimbali ikiwa pamoja na uendeshaji wa mashitaka ambao naweza kusema kwamba robo tatu ya maisha yangu katika Jeshi la Polisi nimekuwa mwendesha mashitaka katika mahakama za mikoa ya Dodoma na Kilimanjaro.
Nimeolewa, nina watoto watano, wa kwanza anaitwa Hussein (35), huyu anafanya kazi Umoja wa Mataifa (UN), Kulwa na Dotto (32), Adili (35) ambaye kwa sasa yupo masomoni Poland, Bahati (18), ambaye ni mtoto wa kike pekee niliyemzaa, na kwa sasa ni mwanafunzi wa kidato cha tano katika Shule ya Sekondari ya Loyola.

Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0755 312 859, barua pepe: katabazihappy@yahoo.com au www.katabazihappy.blogspot.com.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili la Juni 17,2007

Mwelekeo wa Taifa Sasa Taabani

Na Happiness Katabazi

NATUMAINI wasomaji wote ni wazima wa afya. Nisiwachoshe, leo nitaanza makala yangu kwa kuandika nukuu moja ya muasisi wa taifa hili, Mwalimu Julius Nyerere.

Nukuu hiyo inapatikana miongoni mwa hotuba zake maarufu, katika kitabu kiitwacho ‘Moyo kabla ya silaha’, aliyoitoa mwanzoni mwa miaka ya 1960. Na nitaichambua kwa mapana.

Jifunze wakati ni huu: “Afadhali tuwe na taifa ambalo halina silaha za kisasa, lakini tuna moyo wa ushujaa, kuliko kuwa na taifa lenye silaha, lakini vijana wake ni waoga. Tuwe taifa la binadamu, tujue wapi tunatoka na wapi tunakwenda.

“Kuwa na moyo safi ni jambo jema sana kwani tukiwa na moyo safi silaha zitafuata baadaye. Afadhali kuwa maskini, lakini tunajitegemea, kuliko kuwa matajiri kwa kuomba na kutegemea taifa jingine. “Tujiamini kwa nguvu zetu zote na tunajitegemea. Taifa linaloshiba makombo siyo taifa hata.

“Tuwe na tabia ya ushujaa, tusiwe waoga. Tuwe na tabia ya kujitegemea na kusaidiana. Ni afadhali kuwa na chakula kidogo, lakini tukagawana kidogo kidogo kuliko kuwa na chakula kingi na tukaanza kukigombea. Tanzania iwe na tabia mpya. Inawezekana, timiza wajibu wako.”

Aya ya kwanza ya nukuu hiyo Mwalimu Nyerere, alikuwa anaona kwamba vijana wengi walikuwa wanadai wapewe silaha, watakomboa taifa na kukomboa Bara la Afrika kutokana na ukoloni na ubeberu.

Hasa wakati huo vita ya uhuru ilikuwa inarindima katika nchi za Msumbiji, Angola, Zimbambwe na kwingineko.

Nchi hizo zilikuwa chini ya ukoloni na ubeberu na Tanzania ilikuwa makao makuu ya kamati ya ukombozi ya Afrika ya Umoja wa Nchi Uhuru za Afrika.
Na wakati huo ndege za Wareno zilikuwa zikivuka mpaka na kudondosha mabomu nchini mwetu.

Mwalimu Nyerere aliona upungufu katika mtazamo wa vijana wale kwamba silaha ndiyo njia sahihi ya kukomboa ukoloni na ubeberu.

Yeye aliona ni tofauti, kwani alichokuwa anakihitaji yeye ni commitment, uwe unaliamini hilo jambo kwa moyo wako wote na akili zako zote na ujitoe mhanga kulitetea Bara la Afrika. Hiyo ndiyo nadharia ya upambanaji na huo ndio msingi wa upambanaji.

Mwalimu alizungumzia katika mazingira hayo. Je, leo hii kauli hiyo inatugusa vipi Watanzania, umma ambao idadi kubwa ya Watanzania ni vijana? Na je, tuna amini kwa moyo wote kuhusu vita dhidi ya ubeberu? Ukweli ni kwamba hatuamini.

Walio wengi hawaamini kama kuna ubeberu, wanaamini kwamba kuna utandawazi kwa maana kwamba mtaji wa kibeberu unaweza ukatumika kulikomboa taifa na kufuta umaskini.

Kwa Watanzania wengi wa leo wanatofautiana sana na Mwalimu Nyerere, hawana moyo wala ushupavu wa kupambana na ufisadi, rushwa na mtaji wa kibeberu nchini. Na kwa hakika sera nzima ya uwekezaji ni tamko la kukumbatia ubeberu.

Kwa msingi huo vijana hawana budi kupambana na hata kuhitaji kuwa na moyo wa ushujaa. Tumeishakubali kwamba wageni wana haki kubwa hata kuliko wananchi kuwekeza na kuvuna rasilimali zetu.

Wajibu wetu na nafasi tuliyonayo ni kuomba ajira. Na katika hilo hakuna cha ushupavu wala cha woga, cha msingi ni kumpigia magoti na kumlamba miguu tajiri ili upate mradi wako.

Mwalimu Nyerere alisisitiza kwamba ili tuwe na taifa la binadamu linalostahili heshima lazima tujue wapi tunatoka na wapi tunakwenda: Kwa hilo Watanzania wa leo hatumo kwa sababu hatuna sera.

Tunachokiabudu leo hii ni kupewa misaada na wafadhili ambao sasa ndio wanatupangia mipango yetu na uchumi wa maendeleo. Kazi kubwa ya watendaji wa serikali ni kuandika michanganuo (proposals) ili kupewa fedha, na kweli kazi hiyo ya watumishi wa serikali inafanikiwa na kila wanapopewa pesa inafuatia kazi kubwa (shokoa) ya kuandika ripoti na kuwapelekea wakubwa waliotoa fedha zao kwa nchi yetu.

Mwalimu Nyerere alisema, afadhali kuwa maskini, lakini tunajitegemea kuliko kuwa matajiri kwa kuomba kutegemea taifa jingine, kwa maana hilo taifa linalostahili heshima ni lile linalojiamini, linalotegemea nguvu zake kwa maendeleo yake badala ya taifa linaloshiba ‘makombo’ linayopewa kwa jina la misaada.

Hebu tujiulize, Tanzania tunajitegemea kwa kitu gani? Vijana wetu hawajui tena kilimo wala hawapendi ufugaji, kwa hiyo chakula kilicho sokoni na kwenye supermarket kinaagizwa kutoka nje ya nchi.

Na hawapendi kwa sababu hakuna mazingira mazuri yatakayowashawishi wakijikite kwenye sekta hiyo.

Tanzania haina tena viwanda vya nguo, japo inazalisha pamba. Tanzania haisindiki kahawa wala matunda japo ina uwezo mkubwa wa kuzalisha mazao hayo. Tanzania haizalishi mafuta ya kula, inanunua mafuta hayo kutoka nje ya nchi ambazo nyingine ni jangwa japo Tanzania inazalisha zao la alizeti, karanga na mbegu nyingine za mafuta ya kula.

Viwanda vyetu tunaviuza, tena kwa wingi, vingine vinafungwa na vilivyopo ni vya jua kali vinavyozalisha bidhaa duni zisizo na tija wala thamani kwenye masoko ya kitaifa na kimataifa.

Kwa mantiki hiyo, Tanzania sasa ni jalala la kila kitu, kuanzia mitumba na kila uchafu unaotoka nje hasa nchi za Asia.

Je, kwa staili hii ni kiburi gani tunaweza kuwa nacho wakati tumeshindwa kujitegemea kwa kila kitu? Cha msingi nikuona jinsi taifa letu lilivyo taifa la waoga kiuchumi, kwani badala ya kuanzisha miradi ya kuzalisha mali, tunaanzisha miradi ya uchuuzi ya kuuza karanga na takataka kutoka nje.

Kwetu maendeleo ya uchumi ni kuligeuza taifa kuwa la wachuuzi wa aina ya wamachinga. Sasa ujasiri gani tutakuwa nao wakati sote ni maskini wa mali, kauli, maadili na elimu na afya mgogoro?

Taifa la aina hii ni taifa duni ambalo litatugeuza kuwa taifa la watumwa wa mataifa mengine.

Sasa hivi Watanzania wamechoka hata kufikiri, wanaogopa kufikiri na wako tayari kufuta Utanzania wao ili angalau watawaliwe na Wakenya au taifa lolote linalopenda kututawala. Hiyo ndiyo dhima la Shirikisho la Afrika Mashariki.

Unapoona mtu anakwenda sokoni kwa mikikimikiki na makelele wakati hana fedha wala bidhaa anayokwenda kuiuza sokoni, basi ujue mtu huyo kama si ‘maaruni’ ni Mtanzania.

Wengi wa Watanzania wa leo ni watu wanaopenda kutumia njia za mkato zisizo sahihi, hawapendi kufanya kazi wakatoka jasho wanapenda sana starehe na kucheza (Ngwasumaa, mipasho) na matokeo ya taifa kuwa na watu kama hawa ni kuwa na taifa la matapeli, wasanii, wala rushwa, wapika majungu, mafisadi, wazandiki na watu wasioaminika kabisa na hii sasa imeanza kuwa sifa kuu ya Watanzania kimataifa.

Kwa hiyo hivi sasa ukikutana na Mtanzania awe rais, mbunge, viongozi, mawakili, wafanyabiashara, matajiri, walemavu na wananchi wa kawaida unaanza kuwa na wasiwasi kwamba huyo si mmoja mwenye sifa kama hizo nilizozitaja hapo juu.

Si siri tena, zile zama za Mtanzania ni kioo cha uadilifu duniani zimekwisha kabisa.

Mungu ibariki Afrika, Mungu inusuru Tanzania.

0755 312 859: katabazihappy@yahoo.com au www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Juni 10,2007, ukurasa wa nane

Mwelekeo wa Taifa Sasa Taabani

Na Happiness Katabazi

NATUMAINI wasomaji wote ni wazima wa afya. Nisiwachoshe, leo nitaanza makala yangu kwa kuandika nukuu moja ya muasisi wa taifa hili, Mwalimu Julius Nyerere.
Nukuu hiyo inapatikana miongoni mwa hotuba zake maarufu, katika kitabu kiitwacho ‘Moyo kabla ya silaha’, aliyoitoa mwanzoni mwa miaka ya 1960. Na nitaichambua kwa mapana.
Jifunze wakati ni huu: “Afadhali tuwe na taifa ambalo halina silaha za kisasa, lakini tuna moyo wa ushujaa, kuliko kuwa na taifa lenye silaha, lakini vijana wake ni waoga. Tuwe taifa la binadamu, tujue wapi tunatoka na wapi tunakwenda.
“Kuwa na moyo safi ni jambo jema sana kwani tukiwa na moyo safi silaha zitafuata baadaye. Afadhali kuwa maskini, lakini tunajitegemea, kuliko kuwa matajiri kwa kuomba na kutegemea taifa jingine. “Tujiamini kwa nguvu zetu zote na tunajitegemea. Taifa linaloshiba makombo siyo taifa hata.
“Tuwe na tabia ya ushujaa, tusiwe waoga. Tuwe na tabia ya kujitegemea na kusaidiana. Ni afadhali kuwa na chakula kidogo, lakini tukagawana kidogo kidogo kuliko kuwa na chakula kingi na tukaanza kukigombea. Tanzania iwe na tabia mpya. Inawezekana, timiza wajibu wako.”
Aya ya kwanza ya nukuu hiyo Mwalimu Nyerere, alikuwa anaona kwamba vijana wengi walikuwa wanadai wapewe silaha, watakomboa taifa na kukomboa Bara la Afrika kutokana na ukoloni na ubeberu.
Hasa wakati huo vita ya uhuru ilikuwa inarindima katika nchi za Msumbiji, Angola, Zimbambwe na kwingineko.
Nchi hizo zilikuwa chini ya ukoloni na ubeberu na Tanzania ilikuwa makao makuu ya kamati ya ukombozi ya Afrika ya Umoja wa Nchi Uhuru za Afrika.
Na wakati huo ndege za Wareno zilikuwa zikivuka mpaka na kudondosha mabomu nchini mwetu.
Mwalimu Nyerere aliona upungufu katika mtazamo wa vijana wale kwamba silaha ndiyo njia sahihi ya kukomboa ukoloni na ubeberu.
Yeye aliona ni tofauti, kwani alichokuwa anakihitaji yeye ni commitment, uwe unaliamini hilo jambo kwa moyo wako wote na akili zako zote na ujitoe mhanga kulitetea Bara la Afrika. Hiyo ndiyo nadharia ya upambanaji na huo ndio msingi wa upambanaji.
Mwalimu alizungumzia katika mazingira hayo. Je, leo hii kauli hiyo inatugusa vipi Watanzania, umma ambao idadi kubwa ya Watanzania ni vijana? Na je, tuna amini kwa moyo wote kuhusu vita dhidi ya ubeberu? Ukweli ni kwamba hatuamini.
Walio wengi hawaamini kama kuna ubeberu, wanaamini kwamba kuna utandawazi kwa maana kwamba mtaji wa kibeberu unaweza ukatumika kulikomboa taifa na kufuta umaskini.
Kwa Watanzania wengi wa leo wanatofautiana sana na Mwalimu Nyerere, hawana moyo wala ushupavu wa kupambana na ufisadi, rushwa na mtaji wa kibeberu nchini. Na kwa hakika sera nzima ya uwekezaji ni tamko la kukumbatia ubeberu.
Kwa msingi huo vijana hawana budi kupambana na hata kuhitaji kuwa na moyo wa ushujaa. Tumeishakubali kwamba wageni wana haki kubwa hata kuliko wananchi kuwekeza na kuvuna rasilimali zetu.
Wajibu wetu na nafasi tuliyonayo ni kuomba ajira. Na katika hilo hakuna cha ushupavu wala cha woga, cha msingi ni kumpigia magoti na kumlamba miguu tajiri ili upate mradi wako.
Mwalimu Nyerere alisisitiza kwamba ili tuwe na taifa la binadamu linalostahili heshima lazima tujue wapi tunatoka na wapi tunakwenda: Kwa hilo Watanzania wa leo hatumo kwa sababu hatuna sera.
Tunachokiabudu leo hii ni kupewa misaada na wafadhili ambao sasa ndio wanatupangia mipango yetu na uchumi wa maendeleo. Kazi kubwa ya watendaji wa serikali ni kuandika michanganuo (proposals) ili kupewa fedha, na kweli kazi hiyo ya watumishi wa serikali inafanikiwa na kila wanapopewa pesa inafuatia kazi kubwa (shokoa) ya kuandika ripoti na kuwapelekea wakubwa waliotoa fedha zao kwa nchi yetu.
Mwalimu Nyerere alisema, afadhali kuwa maskini, lakini tunajitegemea kuliko kuwa matajiri kwa kuomba kutegemea taifa jingine, kwa maana hilo taifa linalostahili heshima ni lile linalojiamini, linalotegemea nguvu zake kwa maendeleo yake badala ya taifa linaloshiba ‘makombo’ linayopewa kwa jina la misaada.
Hebu tujiulize, Tanzania tunajitegemea kwa kitu gani? Vijana wetu hawajui tena kilimo wala hawapendi ufugaji, kwa hiyo chakula kilicho sokoni na kwenye supermarket kinaagizwa kutoka nje ya nchi. Na hawapendi kwa sababu hakuna mazingira mazuri yatakayowashawishi wakijikite kwenye sekta hiyo.
Tanzania haina tena viwanda vya nguo, japo inazalisha pamba. Tanzania haisindiki kahawa wala matunda japo ina uwezo mkubwa wa kuzalisha mazao hayo. Tanzania haizalishi mafuta ya kula, inanunua mafuta hayo kutoka nje ya nchi ambazo nyingine ni jangwa japo Tanzania inazalisha zao la alizeti, karanga na mbegu nyingine za mafuta ya kula.
Viwanda vyetu tunaviuza, tena kwa wingi, vingine vinafungwa na vilivyopo ni vya jua kali vinavyozalisha bidhaa duni zisizo na tija wala thamani kwenye masoko ya kitaifa na kimataifa. Kwa mantiki hiyo, Tanzania sasa ni jalala la kila kitu, kuanzia mitumba na kila uchafu unaotoka nje hasa nchi za Asia.
Je, kwa staili hii ni kiburi gani tunaweza kuwa nacho wakati tumeshindwa kujitegemea kwa kila kitu? Cha msingi nikuona jinsi taifa letu lilivyo taifa la waoga kiuchumi, kwani badala ya kuanzisha miradi ya kuzalisha mali, tunaanzisha miradi ya uchuuzi ya kuuza karanga na takataka kutoka nje.
Kwetu maendeleo ya uchumi ni kuligeuza taifa kuwa la wachuuzi wa aina ya wamachinga. Sasa ujasiri gani tutakuwa nao wakati sote ni maskini wa mali, kauli, maadili na elimu na afya mgogoro?
Taifa la aina hii ni taifa duni ambalo litatugeuza kuwa taifa la watumwa wa mataifa mengine. Sasa hivi Watanzania wamechoka hata kufikiri, wanaogopa kufikiri na wako tayari kufuta Utanzania wao ili angalau watawaliwe na Wakenya au taifa lolote linalopenda kututawala. Hiyo ndiyo dhima la Shirikisho la Afrika Mashariki.
Unapoona mtu anakwenda sokoni kwa mikikimikiki na makelele wakati hana fedha wala bidhaa anayokwenda kuiuza sokoni, basi ujue mtu huyo kama si ‘maaruni’ ni Mtanzania.
Wengi wa Watanzania wa leo ni watu wanaopenda kutumia njia za mkato zisizo sahihi, hawapendi kufanya kazi wakatoka jasho wanapenda sana starehe na kucheza (Ngwasumaa, mipasho) na matokeo ya taifa kuwa na watu kama hawa ni kuwa na taifa la matapeli, wasanii, wala rushwa, wapika majungu, mafisadi, wazandiki na watu wasioaminika kabisa na hii sasa imeanza kuwa sifa kuu ya Watanzania kimataifa.
Kwa hiyo hivi sasa ukikutana na Mtanzania awe rais, mbunge, viongozi, mawakili, wafanyabiashara, matajiri, walemavu na wananchi wa kawaida unaanza kuwa na wasiwasi kwamba huyo si mmoja mwenye sifa kama hizo nilizozitaja hapo juu.
Si siri tena, zile zama za Mtanzania ni kioo cha uadilifu duniani zimekwisha kabisa.
Mungu ibariki Afrika, Mungu inusuru Tanzania.

0755 312 859: katabazihappy@yahoo.com au www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima, Juni 10,2007. ukurasa wa nane