MIAKA MIWILI YA RAIS KIKWETE MADARAKANI:

MASWALI MENGI KULIKO MAJIBU
Na Happiness Katabazi

ALIPOINGIA Ikulu Desemba 21 mwaka 2005 Rais Jakaya Kikwete alikuwa mtu mwenye tabasamu lenye matumaini kwa taifa lake. Alikuwa anajivunia ushindi wa Tsunami wa zaidi ya asilimia 80.

Yeye alionekana ametimiza ndoto yake ya muda mrefu ya kuwa Rais wa Tanzania, ndoto ambayo ilififia mwaka 1995 aliposhindwa na Rais Mstaafu Benjamin Mkapa.

Kwa kipindi cha miaka kumi iliyopita Rais Kikwete alijizatiti kuwa rais wa taifa hili, inaelezwa alikusanya fedha na kujenga mtandao ili kushinda ndani ya chama chake na kushinda kwenye uchaguzi mkuu uliopita.

Pamoja na maandalizi hayo ambayo yaliingiza Taifa kwa mara ya kwanza katika matumizi makubwa ya kupindukia katika uchaguzi ilisadikiwa kwamba Rais Kikwete aliandaa timu ya wanamtandao, itakayompelekea Ikulu.

Miaka miwili sasa inatimia Ijumaa ijayo aiingie ikulu,Je Kikwete anatabasamu lilelile lenye matumaini kwa watanzania lenye kupatia maisha bora kila mmoja wao, milo mitatu kwa siku, ajira milioni moja kwa vijana,wanawake watawezeshwa?

Je wale wanamtandao wote walikuwa wakijitapa kuwa wameaidiwa vyeo na fursa za biashara wamevuna walichoaidiwa?.Na je watanzania waliompigia kura kwa asilimia 80 bado wapo nyuma ya rais wao?

Ili kujibu maswali haya yafaa kuiweka serikali ya awamu ya nne ya ari,nguvu na kasi mpya kwenye mizani na vitendo.Lazima tujue kama ahadi zile zilikuwa danganya toto au kweli na rais wetu na chama chake walikuwa wamejizatiti kuzitekeleza kwa vitendo.

Mtandao uliomweka madarakani una wana CCM na wasio wana CCM.Wasio kuwa wana CCM walijikuta wanakimbilia kadi haraka ili kujiweka imara kwenye mkao wa kula.

Na hao walikuwa wengi mno wenye elimu na wasiyo na taaluma na matapeli wa mtaani,wafanyabiashara, waandishi wa habari hata baadhi ya viongozi wa dini wote walijikuta wana matumani ya kufanyiwa hiki au kile kama walivyokuwa wakijitapa vichochoroni na kwenye mabar kwamba wameaidiwa na rais wetu.

Matokeo ya mategemeo haya yalikuwa kuteuliwa kwa baraza la mawaziri lenye wingi wa mawaziri kama darasa la chekechea.

Kweli mawaziri 61 ni wengi mno hawana tija kwa taifa ni kero,hasara kubwa na gharama.Hakuna jambo ambalo baraza hili kubwa limeweza kukamilisha katika kipindi hiki cha miaka miwili kwa sifa na unafisi ila baraza hili limejipatia sifa yakuwa wafalme wa matumizi ambao wamekiuka vigezo vyote vya matumizi makubwa ya fedha.

Kwa upande mwingine vyeo vya ukuu wa wilaya, Ukuu wa mkoa na makatibu wa kuu maana ni vichache mno kuwatosha wanamtandao walioaidiwa vyeo hivyo.

Hata tukiongeza vyeo vya mabalozi na wakurugenzi wa mashiriki bado haviwatoshi ,hivyo waliokosa wamekosa na waliopata wamepata,wanaomba ‘reshaffle’wanaomba lakini huo ndiyo ukomo wa mtandao.

Yawezekana tumejionea uroho na ugomvi wa madaraka ndani ya anachokiongoza rais wetu jambo ambalo alijawahi kutokea katika historia ya chama hicho tangu kianzishwe.
Wazee wamejikuta wakipigwa mweleka na vijana wadogo kwa jina la wanamtandao.Neno Mtandao limegeuka kuwa itikadi ya CCM ,ukiwa mwanamtandao unanafasi,ukiwa si mwanamtandao huna nafasi.

Kama watanzania wanajiuliza ni kwanini serikali ya awamu ya nne inaonekana kupoteza dira na sifa basi jibu watalipata kwa kuangalia taswira mpya ya CCM, chama hicho sasa ni zizi la viongozi wa ovyo ovyo na baadhi yao wapo kwaajili ya kujilimbikizia mali. Hiyo ndiyo CCM mpya tuliyonayo hivi sasa.

Tuhuma za ufisadi, miaka miwili ya uongozi wa rais Kikwete, aikupambwa na vitendo vya kikakamavu vinavyoliletea taifa tija kimaendeleo badala yake imekuwa ni miaka miwili iliyogubikwa na habari za vitendo vya ufisadi vinavyotuhumiwa kufanywa na viongozi.

Tulianza na kashfa ya mkataba wa Richmond ambapo wakati taifa linaumia kiuchumi kwakukosa nishati serikali ilijikuta ikipiga magoti mbele ya mafisadi waliotoka kujitoa mabilioni ya fedha kuleta vinu vya umeme hewa kutoka Marekani.

Mpaka leo kashfa hii haijapatiwa ufumbuzi.Inasadikika kuwa baadhi ya vigogo walio ndani ya serikali waliusika kwenye kashfa hiyo.

Imelichukua bunge muda mrefu mno kuunda kamati kuchunguza kashfa hiyo.Wakati kashfa ya Richmond ikitokea wananchi walijikuta wakilipukiwa na bomu jingine la ufisadi ambapo ilielezwa kwamba wanunuzi wa Rada iliyopingwa vikali na wananchi.

Inadaiwa kuwa walijipatia rushwa ya dola milioni 12 ambazo zinasadikiwa kuwa zilitolewa kama bahasha kwa vigogo ndani ya serikali.Hili nalo lipo na wala alijapatiwa ufumbuzi.

Kana kwamba kashfa hizo azitoshi hivi sasa tunazo kashfa mbili kubwa moja, ubadhirifu wa fedha ndani ya Benki Kuu (BOT) na nyingine kuhusu mikataba ya madini.

Kashfa ya BOT, ni ufisadi uliopita kipimo, hakuna Mtanzania anayeweza kuelewa jinsi gani taasisi hiyo ilijiingiza kwenye ubadhirifu kwa kiwango kile. Kweli kuwaambia wananchi kwamba vile viminara viwili vina thamani ya Sh milioni 523, ni jambo lisilowezekana.

Pia ukweli kwamba BOT imejiingiza katika bodi za makampuni yanayotajwa kuwa ni ya kifisadi ya Meremeta, Tangolg, Kagoda na Mwananchi Golg ambazo zimeingiza serikali kwenye hasara za mabilioni ya fedha za walipa kodi ni dhambi isiyosameheka.

Hata ilipogundilika Waziri wa Madini Nazir Karamagi amekiuka agizo la Rais Kikwete na kuweka saini katika mkataba wa madini unaolileta taifa hasara ya mabilioni ya fedha ni jambo lisilosameheka.

Tujiulize sasa sera ya awamu nne ni kuliangamiza taifa kiuchumi kwa ari,nguvu na kasi mpya? Haya siyo matumaini tuliyokuwa nayo tulivyompigia rais wetu kura katika uchunguzi mkuu wa mwaka 2005.

Inabidi sasa Rais Kikwete atueleze kama kweli yeye ni msafi na hana ushirika na hawa wanaoliangamiza taifa.Alisipofanya hivyo basi itakuwa alali kuamini na yeye ni mmoja wao, kwani mbona hatuoni Gavana wa Benki Kuu Daudi Balali akiguswa, mbona hatuoni Karamagi akiguswa?

Hata hivyo Rais Kikwete, akiwa anatimiza miaka miwili tangu aingie madarakani, napenda kumpongeza yeye binafsi kwa kuruhusu uhuru wa habari kupanuka katika muda mfupi tangu aingie madarakani, naomba aendelee na moyo huo kwani umedhiirisha ni jinsi gani ameiva kidplomasia na anaheshimu demokrasia.Hongera sana.

Lakini bado kuna viongozi wachache wamekuwa wakilitumia jina la rais kujaribu kuviziba mdomo vyombo vya habari huru visifichue maovu wala kumkosoa rais panapostahili hata hivyo kadri siku zinavyozidi kwenda jitihada hizo zinagongwa mwamba.

Kwenu nyie viongozi ambao nadiriki kusema ni wachafu kwani mngekuwa wasafi msingethubutu kupitapita na kupiga simu kwenye vyombo vya habari kwamba habari fulani isichapishwe, acheni tabia hiyo kwani April mwaka jana, rais aliutangazia umma kwamba yupo tayari kukosolewa kupitia vyombo vya habari na kupongezwa na baadhi ya watu wasigeuke kuwa wasemaji wake na mkumbuke huyu ni rais wa wananchi wote na siyo kikundi cha wanamtandao maslahi.

Mwisho Rais Kikwete,kumbuka wananchi tulikuamini tukakuweka madarakani kwanjia ya demokrasia, hivyo tunapenda kuona wewe na serikali yako mkisikiliza shida zetu na kuzitatua na pia viongozi wazembe ambao huo uzembe wao unakwamisha ufanisi wapumzishe,weka wengine ambao wanaipenda nchi yao na wako tayari kuilitumikia taifa hili wakati wowote.

Mungu ibariki Afrika,mungu inusuru Tanzania

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili Desemba 16,2007

BURIANI KANALI GODFREY MAKAYA


Kanali Makaya afariki dunia
Na Happiness Katabazi

ALIYEWAHI kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kinondoni enzi hizo wilaya hiyo ilikuwa ikiitwa Mzizima, Kanali Mstaafu Godfrey Kajana Makaya(63) amefariki dunia.
Akizungunza ba gazeti hili nyumbani kwa marehemu Sinza Madukani Dar es Salaam, jana, mtoto wa marehemu Doreen Makaya alisema kwamba baba yake alifariki Ijumaa iliyopita saa 4:20 katika hospitali ya Agha Khan Jijini Dare-es salaam. Kanali Mstaafu Godfrey Makaya alifanyiwa upasuaji mdogo wa Henia mapema Novemba 19 mwaka huu, na kuruhusiwa kutoka hospitali Novemba 25 Mwaka huu.

Hali yake ya afya ilibadilika ghafla Ijumaa, akiwa katika hospitali ya Agha Khan alipokwenda kwa ajili ya kuangaliwa maendeleo ya operesheni yake aliyokuwa amefanyiwa.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa alitakiwa arudi baadaye ili kumuona daktari majira ya saa nane mchana lakini akiwa anatembea kurudi kwenye gari, hali yake ilibadilika ghafla na kufariki muda mfupi baadaye saa nne asubuhi hospitalini hapo.

Kanali Mstaafu Makaya aliiongoza Wilaya ya Mzimzima sasa Kinondoni kwa Kipindi cha zaidi ya miaka 17 mfululizo kwa kuchaguliwa na wananchi na hadi mauti yalipomkuta alikuwa mjumbe wa Halmashauri kuu ya Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Kinondoni na Mjumbe wa Tawi la Sinza D.
Kanali Mstaafu Makaya alizaliwa Septemba mosi mwaka 1944. Alijiunga na jeshi la Wananchi wa Tanzania(JWTZ) na kustaafu kazi Desemba 9 mwaka1997 akiwa Mkuu wa Chuo cha Mgambo Mbeya.
Aidha mazishi yatafanyika kesho katika makaburi ya Kinondoni jijini Dar es Salaam na hataazikwa kwa heshima zote za kijeshi baada ya baada ya kutolewa heshima za mwisho nyumbani kwake Sinza Madukani.Marehemu ameacha watoto kumi na sita na wajuu 29.
Mungu ametoa na bwana ametwa jina la bwana liimidiwe.

KAMATI YA MADINI NI 'MAZINGAOMBWE' YA KIKWETE!


Na Happiness Katabazi

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete, asitake kuwadanganya wananchi kwa kuwa ndiye aliyeahidi maisha bora kwa kila Mtanzania, lakini katika siku za hivi karibuni ameonekana kuwa na ‘ndimi mbili’.

Anajaribu sasa kukwepa ahadi zake. Siku chache zilizopita alinukuliwa akiwaambia waandishi wa habari wa nchi za nje kwamba hafahamu ni kwanini Tanzania inakuwa maskini.
Huyu ni rais wa nchi ambayo bajeti yake ni tegemezi kwa fedha za wafadhili kwa asilimia 46! Huyu ni rais wa nchi ambayo haina uwezo wa kuwapatia elimu bora watu wake.
Hata vijana 27 waliokwama kule nchini Ukraine, serikali yake ilishindwa kuwaokoa, wakalazimika kukatisha masomo na kurudi nchini kwa nauli za kubahatisha.
Huyu ni rais wa serikali ambayo inaendesha hospitali zisizo na dawa za kutosha, madaktari na manesi wanaishi kwa mishahara isiyokidhi mahitaji.
Huyu ni rais ambaye mvua ikinyesha siku moja nchi nzima anayoiongoza inaogelea kwenye mafuriko na mijini magari na watu wanatembea kwa tabu. Lakini rais huyu hajui ni kwanini Tanzania ni maskini.Tanzania ina madini.
Tanzania ina rasilimali za wanyama na misitu, vyote hivyo Bunge limevitungia sheria ambazo zinawaruhusu wawekezaji wa nje ‘kupora’ mali hizo kupeleka nje bila kulipa kodi na kusamehewa kodi.
Lakini rais wetu ambaye amekuwa waziri kwa muda mrefu, hajui ni kwanini ni nchi yetu ni maskini. Rais Kikwete amesikika akisema kwamba wawekezaji katika sekta ya madini wakitulipa kodi kwa asilimia 30 na mrahaba wa asilimia tatu, inatutosha.Ebu tumuulize rais wetu, inamtosha nani hiyo kodi na huo mrabaha?

Kama inamtosha yeye, sawa, lakini kama taifa, hicho sicho tunachokitaka, sisi kama wananchi wa taifa hili tunataka ubia wa asilimia 51 na asilimia 49 zibaki kwa wakezaji na bado walipe kodi serikalini.
Hilo ndilo dai kuu la Watanzania, ingawa bado halijawekwa kwenye sheria na sera za nchi.
Sasa kama rais wetu anataka kucheza, acheze anavyotaka, lakini sisi tunataka tumiliki migodi kwa asilimia 51, na wawekezaji walipe kodi na ieleweke wazi, hatuna mjadala katika hilo.
Nasema kwamba, bila wazalendo kushirikishwa kwenye migodi na wakajenga hisa zao kwenye thamani ya madini yenyewe, hatutaweza kujikomboa na kujitoa hapa tulipo.
Pili, tunataka haki ya kutawala shughuli za migodi na kujua kiasi gani kinachimbwa na kupatikana, kinatokana na umiliki wa hisa. Sasa sisi tukiendelea kujikita kwenye kusubiri kupewa kodi kama anavyodai sasa rais wetu, tukae tukijua tumeliwa.
Ninachokiona ni kwamba, Rais anataka kukwepa mjadala huu na badala yake wiki iliyopita ameunda kamati ya kupitia mikataba ya madini, sijui kama wananchi wengi wanafahamu kwamba kamati hiyo haina mamlaka ya kubadilisha vipengele vya sheria vilivyopo kuhusu madini. Sasa kamati teule ya rais inaenda kuchunguza kitu gani?
Hapa ndipo busara ya baadhi ya wananchi wanapomnunia Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (CHADEMA) kukubali kujiunga na kamati hiyo, inapojionyesha.
Kwa sababu wananchi wanajua sheria ya madini ipo na ni mbaya na haijabadilishwa. Wananchi wanajua sera ya CCM kuhusu madini ipo na ni mbaya na haijabadilishwa hadi sasa.
Kwa hiyo, mikataba yoyote itakayotiwa saini na iliyokwishatiwa saini inatokana na vitu wiwili, navyo ni sera za CCM kuhusu madini na sheria ya nchi inayohusu madini.
Kwa hiyo sasa kupitia kamati hiyo tutapata nini? Hatutapata kitu, tumeingizwa kwenye ‘mazingaombwe na longolongo’ na anayefikiria tutapata kitu na aseme.
Hata kama hao wajumbe wote wa kamati teule ya rais ni maadui wa Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, bado hawataweza kuthibitisha kwamba waziri huyo na wenzake waliomtangulia waliingia mikataba kwa makosa kwa sababu atasema alifuata sheria za nchi ambazo wananchi tunasema ni mbaya kusaini mikataba hiyo. Lakini hoja hii haitusaidii kitu.
Hoja kuu ni kuhusu sheria ya madini ibadilishwe, Watanzania wawe wabia kwenye migodi kwa asilimia 51 na wawekezaji wabakie na asilimia 49 na walipe kodi, hivyo kama hatuwezi kupatiwa haya, rais na chama chake kinachounda serikali, itafika wakati tutawaita nao ni mafisadi.

Kwa mantiki hiyo, kama kamati yako hii ya kuchunguza mikataba ya madini haitaleta hilo, tutawashitaki kwa Mungu na yeye ndiye atajua cha kuwafanya, kwani tumekuwa tukilia kuhusu hili kila mara, lakini tunapuuzwa.
Kwakuwa tumepata taarifa kuwa kamati nne zilishaundwa kwa ajili ya kuchunguza sekta ya madini, tunataka serikali iweke wazi ripoti za kamati za kazi zilizotangulia ili tujue zilipendekeza nini na serikali yetu ilishindwa kutekeleza lipi katika hizo kamati ili kamati hii mpya isirudierudie kufanya yaliyokwishafanywa na kamati zilizotangulia.
Nasisitiza tena, rais cheza unavyotaka, lakini sisi wananchi tunataka kuona hiyo hoja kuu niliyokwisha itaja hapo juu inatekelezwa kwa vitendo.
Wewe ndiye rais wetu, tumekuamini kuwa unafaa kutuongoza, funga bao kwa kichwa, mkono, kifua na hata mguu, lakini hakikisha hoja hii kuu inatekelezwa na tena hatuna subira katika hili, tunataka kuona ukilitekeleza kwa Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili,uk.21.Novemba 25 mwaka 2007.

NIKIWA NA BINTI WA RAIS KARUME



Mwandishi wa Tanzania Daima, Happiness Katabazi (kushoto) akizungumza na binti wa rais, Aman Abeid Karume, ambaye ni wakili wa kujitegemea, Fatma Karume (kulia) nje ya Hoteli ya Regency Park, Dar es Salaam, juzi usiku kuhusu tuhuma zinazomkabili za kufanya vurugu mahakamani Jumatano ya wiki hii.Katikati ni mmoja wa wateja wa wakili huyo. (Picha na Francis Dande)

BINTI WA KARUME ARUSHA KOMBORA


*Adai Mahakama Kisutu inanuka rushwa
*Asema amewasilisha ushahidi Takukuru
*Asisitiza yu tayari kukabiliana na lolote

Na Happiness Katabazi

BINTI wa Rais, Amani Abeid Karume, ambaye ni wakili wa kujitegemea, Fatma Karume, anayedaiwa kufanya fujo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam juzi, ameibuka na kueleza kusikitishwa kwake na madai hayo huku yeye mwenyewe akitoa tuhuma nzito za rushwa dhidi ya mahakimu wa mahakama hiyo.

Fatma alitoa tuhuma hizo wakati alipofanya mahojiano ya ana kwa ana na Tanzania Daima jana jioni wakati alipotakiwa kueleza kile kilichotokea katika mahakama hiyo juzi na uamuzi wake, baada ya Chama cha Wanasheria Tanzania (TLS) kutoa tamko la kusikitishwa na tukio hilo na kutaka uchunguzi ufanyike.

Wakili huyo, alisema baadhi ya mahakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wanajihusisha na vitendo vya rushwa, jambo aliloeleza kuwa alikuwa tayari ameshalitolea malalamiko yake rasmi katika Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).

Akizungumzia matokeo ya mzozo wake huo wa juzi, Fatma alisema alikuwa tayari kukabiliana na hatua zozote zitakazochukuliwa dhidi yake kwa sababu tu ya kupigania haki anayoamini alidhulumiwa katika misingi isiyofaa.
“Niko tayari hata kufutwa uwakili. Natetea haki yangu ambayo naamini nilinyang’anywa, nimeingia kufanya kazi hii kwa sababu ya kutetea wananchi, hivyo siwezi kuona nikidhulumiwa nikanyamaza kimya. Enzi za utumwa zilishapitwa na wakati, ni bora nikalime nazi kuliko kupoteza haki yangu,” alisema Fatma kwa kujiamini.

Alisema hata kama yeye ni mtoto wa rais, bado anayo haki ya kudai kile anachodhani anadhulumiwa, kwani naye ni mtu kama walivyo watu wengine, na kimsingi akakataa suala lake kuhusishwa na urais wa baba yake.

Kuhusu kuwapo kwa rushwa, binti huyo wa Rais wa Zanzibar alisema anao ushahidi wa kutosha unaomuonyesha mmoja wa mahakimu waandamizi wa mahakama hiyo akiomba rushwa kutoka kwa mteja wake, Sadiq Walji.

“Ninao ushahidi wa uhakika hakimu (alimtaja jina), aliomba rushwa (akataja kiasi cha fedha zilizoombwa na hakimu huyo)…tena alimfuata mteja wangu katika Hoteli ya Sea Cliff Agosti 26 mwaka huu, na alimpatia fedha na akamrekodi bila ya yeye kujua ‘tape recorder’ (kinasa sauti). Hili ushahidi wa sauti yake tulishauwasilisha Takukuru na wamelifanyia uchunguzi kwa muda mrefu.

“Nasema hivi, Mahakama ya Kisutu inanuka rushwa. Inahusisha mahakimu na waendesha mashitaka. Rushwa imetawala pale, tena huyo hakimu kesho (leo) anapelekewa barua yake…mimi siyo mwehu hata kidogo, nasema hili kwa uhakika na serikali na watu wote wajue kuwa Mahakama ya Kisutu pana rushwa kila mahali,” alisisitiza wakili huyo wa kujitegemea.

Akizungumzia madai ya kufanya fujo ndani ya mahakama wakati kesi inaendelea, wakili Karume aliyefika kwa ajili ya kumuwakilisha Walji, kwenye kesi namba 60/2006 ya madai ya mtoto wa miaka miwili iliyokuwa ikisikilizwa mbele ya Hakimu Mwandamizi, Addy Lyamuya, alisema hakimu huyo alimkosea, hali iliyosababisha malumbano.

Alisema, Hakimu Lyamuya alitaka kuipanga kesi hiyo tarehe za mbali bila sababu za msingi, jambo ambalo wakili Karume alipingana nalo kwa kuwa Hakimu Adolf Mahay, alikwishatoa uamuzi Agosti mwaka huu kuwa mtoto huyo wa mteja wake anayeishi kwa Saeeda Hassam , awe akiruhusiwa kila Ijumaa kwenda kwa baba yake na kurudishwa kwa mama yake Jumapili.

Fatma alisema licha ya uamuzi huo, mama wa mtoto huyo alikuwa akikaidi amri hiyo, hali ambayo ilimfanya yeye awasilishe ombi la kutaka mwanamke huyo achukuliwe hatua za kisheria kwa kosa la kuidharau amri halali ya mahakama hiyo.

“Licha ya kumuomba hakimu aipange leo, alikataa na kunijibu kwa ukali na akanionyeshea kwa ishara kwamba mimi ni mwendawazimu….nikamuuliza, madaraka hayo nani kampa ya kunionyeshea kwa ishara mimi ni mwendawazimu? Akaanza kuniambia nisimpangie kazi…nikashikwa na hasira na kutoka mahala nilipokuwa nimesimama na kumwambia zama za utumwa zilishapita katika nchi yetu, hivyo siwezi kukubali kuona navunjiwa heshima nikanyamaza kimya na nikamweleza kabisa nakwenda kumshitaki kwa wakubwa wake wa kazi.

Alisema baada ya kumweleza maneno hayo, hakimu alikwenda kumshitaki kwa Hakimu Mkuu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Sivangilwa Mwangesi na pia alikwenda kumshitaki kwa Jaji Kiongozi Amir Manento lakini hata hivyo alisema malalamiko yake hakuwa ameyapeleka kwa viongozi hao kwa maandishi.

“Licha ya kumweleza yote haya, hakimu hakutaka kunisikiliza na badala yake akanionyeshea kwa ishara kwamba, mimi ni mwendawazimu….ndipo nilipomweleza kwamba hawezi kazi na kwamba naenda kumshitaki kwa wakubwa wake wa kazi,” alisema Karume.

Fatma alisema pia kuwa, juzi asubuhi alikwenda kumshitaki Lyamuya kwa Hakimu Mkuu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Sivangilwa Mwangesi, pia alikwenda kumshitaki kwa Jaji Kiongozi, Amir Manento, lakini hata hivyo alisema malalamiko yake hakuwa ameyapeleka kwa viongozi hao kwa maandishi.

“Habari zilizoandikwa jana kwakweli zimeniumiza sana…kwani Lyamuya aliniita mimi mwendawazimu na mbaya zaidi, Mahayi anasema kwamba alijitoa kwenye kesi ninayoitetea kwa sababu nilimfokea. Haya mambo si ya kweli,” alisema Fatma katika mahojiano jana.

Katika tukio la juzi, Fatma alikuwa akituhumiwa kutoa maneno makali dhidi ya Hakimu Lyamuya, hali iliyodaiwa kusababisha hakimu huyo ajitoe kuendelea kusikiliza kesi inayomhusu mwanasheria huyo.

Tukio hilo la aina yake lilitokea katika chumba cha mahakama, wakati hakimu huyo alipotaka kuanza kusikiliza kesi ya madai namba 60/2006 ambayo ilianza kujadiliwa na hakimu huyo juzi hiyo kwa mara ya kwanza, tangu apewe jalada hilo.

Katika kesi hiyo, Fatma anamwakilisha Sadiq Walji, ambaye ni mdaiwa katika kesi hiyo ya madai ya mtoto. Mdai katika kesi hiyo namba 60/2006 ni Saeeda Hassam.

Kabla Hakimu Lyamuya kuanza kusikiliza kesi hiyo, Wakili Fatma, aliiomba mahakama kuahirisha kesi hiyo hadi kesho, kwa ajili ya kuanza kusikilizwa kwa shauri hilo.

Kutokana na hali hiyo, hakimu alimtaka karani wake kuangalia kwenye kitabu cha kumbukumbu (diary) kama siku hiyo itafaa kusikilizwa kwa shauri hilo. Hata hivyo, karani alimweleza hakimu kuwa siku hiyo zimepangwa kesi nyingi za kusikilizwa, labda waipange Januari 13, mwakani.

Kwa mujibu wa taarifa za juzi, Hakimu Lyamuya alikubaliana na maelezo ya karani wake na kumweleza wakili huyo kwamba kesi hiyo itasikilizwa tarehe hiyo.

Baada ya hakimu kupanga tarehe hiyo, Wakili Fatma anadaiwa kuwa alianza kufoka kwa sauti ya juu akitaka mahakama isikilize kesi hiyo jana jambo ambalo Hakimu Lyamuya alilikataa kwa kueleza kuwa hakuwa na nafasi.

Wakili huyo aliendelea kuomba mahakama kupanga kesi hiyo Januari 2 mwakani, ombi ambalo hakimu huyo alilikataa na kumweleza tarehe hiyo mahakimu watakuwa mapumziko, ndipo wakili huyo alipoanza kutoa kauli kali dhidi ya hakimu huyo.

“Kwanza wewe hujui kazi na ni mara yako ya kwanza kuniona mimi… hunijui ni nani, sasa nitakuonyesha… nitaandika barua kwa wakubwa wako wa kazi na kuwaeleza kwamba hujui kazi,” alidaiwa kusema Fatma hiyo juzi.

Kutokana na tafrani hiyo, mahakama ilishindwa kuendelea kusikiliza shauri hilo wala kulipangia tarehe na badala yake jalada la kesi lilirudishwa kwa uongozi wa mahakama hiyo, ili limpangie hakimu mwingine kusikiliza kesi hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya tafrani hiyo juzi, Hakimu Lyamuya, alisema ameshangazwa na vitendo vya utovu wa maadili vilivyoonyeshwa na wakili huyo na kueleza hajafikiria kuchukua uamuzi wa kumfungulia kesi.

Chanzo;Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Novemba 23,2007








DK.MVUNGI:TULICHAGUA BORA VIONGOZI 2005

.Asisitiza Bunge linahitaji wanamageuzi wengi
.Amsifu Zitto Kabwe kwa ushujaa bungeni

Dk. Edmund Sengondo Mvungi, ni Mhadhiri Mwandamizi wa Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambaye pia alikuwa ni mgombea urais kwa tiketi ya Chama cha NCCR-Mageuzi katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, anazungumzia kwa mapana mustakabali wa mageuzi nchini.Ungana na Mwandishi Wetu Happiness Katabazi, aliyefanya mahojiano maalum na msomi huyo ofisini kwake hivi karibuni.

Swali: Miaka miwili imepita tangu uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 ambao wewe uligombea urais wa Tanzania na wewe na wagombea wenzako wa vyama vya mageuzi mlishindwa vibaya katika uchaguzi huo. Kwa nini umekuwa kimya kuhusu mambo mengi yanayotokea nchini?

Jibu: Sijui kama tulishindwa katika uchaguzi ule. Kama ni kushindwa, basi Watanzania tulishindwa vibaya katika uchaguzi ule. Tulishindwa kuchagua viongozi bora tukachagua bora viongozi, tulishindwa kuchagua sera bora za kutuletea mageuzi na maendeleo ya haraka kwa walio wengi tukachagua chama kilichochoka na ambacho hakina sera bora.

Kama kura asilimia 8o za mshindani wangu ni za kweli, basi tujionee wenyewe maana halisi ya kura zile katika utekelezaji wa yale aliyoahidi kwa kila Mtanzania. Maisha bora kwa kila Mtanzania! Bila shaka ukweli unajidhihirisha sasa, maisha bora kwa wawekezaji kutoka nje, kulia na kusaga meno kwa Mtanzania mlalahoi!

Ni kweli nimekuwa kimya kwa kuwa nimerejea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambapo nafundisha sheria. Mwajiri wangu amenipatia somo jipya la 'Maadili ya Taaluma ya Sheria" juu ya lile la "Sheria ya Katiba", hivyo kazi imeongezeka maradufu. Nautumia muda wangu mwingi kuandaa
mihadhara kwa ajili ya wanafunzi wangu.

Swali: Unataka kutuambia umeachana sasa na siasa za mageuzi?

Jibu: La hasha! Sijaacha siasa, kwani binadamu aliyeachana na siasa ni yule aliyekwisha
kufa. Binadamu ni mwanasiasa kwa asili na hulka yake. Kila jambo tunalotenda ni siasa.
Viongozi wa siasa ni aina moja tu ya wanasiasa tulionao. Mimi bado ni mjumbe wa
Halmashauri Kuu ya chama changu na mshauri wa sheria na haki za binadamu wa chama changu
cha NCCR-Mageuzi. Nashiriki katika michakato mbalimbali ya mageuzi inayofanywa na
wanamageuzi nchini pamoja na ile inayofanywa na wanaharakati katika asasi zisizo za
kiserikali.

Swali: Unasemaje sasa kuhusu ukimya wako kuhusu mambo kadha wa kadha yanayotokea katika nchi yetu yenye mguso wa kisiasa?

Jibu: Kimya kinaweza pia kuwa jibu. Ni vyema kujipa muda kukaa kimya na kusikiliza wengine
wanasema nini. Hiyo inawapa wananchi fursa ya kushirikiana na serikali kutekeleza yale
waliyoahidiwa. Pale utekelezaji unapokinzana na misingi ya demokrasia tunayojenga,
najitokeza kuelezea msimamo wangu, kwa mfano suala la muswada wa sheria ya haki ya kupata
habari na sheria ya huduma ya vyombo vya habari ulioletwa na serikali. Sikukaa kimya,
nilijitokeza kuzungumza na kushiriki katika harakati ya kuweka mambo sawa kwa mujibu wa
misingi ya taaluma ya sheria, haki za binadamu na maslahi ya wadau wa habari.

Swali: Unaonaje mwenendo wa mageuzi, tunapiga hatua au tunarudi nyuma, hasa ukitizama
kusimamishwa kwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto bungeni hivi karibuni?

Jibu: Swali lako kubwa kweli. Mimi binafsi naona tunapiga hatua kwenda mbele. Hakuna
nafasi kwa jamii kurudi nyuma, kwani kila hatua inayopigwa hata kama itaonekana ni mbaya
na yenye kuwaumiza wananchi, bado ni hatua yenye mafunzo mema au mabaya kwetu. Kwa mfano
naona jamii imekomaa zaidi, kwa kuwa imejionea yenyewe ukweli na uongo, haki na dhuluma
vikitendwa na serikali yao mbele ya macho yao na vikigusa maisha yao. Sihitaji kuendesha
darasa la haki za binadamu kwa ndugu zangu Wabarabaig kule Hanang kwa wao kujua kuwa
serikali imevunja haki yao ya kumiliki ardhi walimozaliwa na ambamo wamekuwa wakifugia
mifugo yao kwa zaidi ya karne moja.

Wabarbaig kule Hanang wamejionea wenyewe kuwa serikali ilithamini zaidi uwekezaji katika
kilimo cha ngano ni bora kuliko haki yao ya kuishi, kujenga utamaduni wao na kujipatia
riziki yao kwa kufuga. Sihitaji kuwakumbusha jinsi serikali ilivyotwaa ardhi yao kwa
mabavu kwa kuwachomea nyumba zao, kuharibu mali na mifugo yao. Wabarbaig wanajua kuwa hata
baada ya serikali kushindwa kuendelea kulima ngano haikuwarejeshea ardhi yao bali
ilitafuta wawekezaji wauziwe ardhi ile. Mashamba yale sasa yatauzwa kwa wawekezaji na
mawili yatagawiwa kwa wafugaji na wakulima ambao si wale walionyang'anywa ardhi mradi wa
ngano ulipoanzishwa. Hiyo ndiyo busara ya serikali yetu!

Vivyo hivyo sihitaji nguvu kubwa kuwaeleza wananchi wa Kijiji cha Nyamuma kule mkoani Mara
kuwa serikali yao ilifanya kitendo cha kifisadi kuwavamia na kuwachomea nyumba zao,
kuharibu mali zao na kuumiza wengine katika zoezi la kupanua mipaka ya hifadhi ya
Serengeti. Kule serikali iliona kuwa haki ya wanyama kuishi ni muhimu kuliko ile ya
wananchi wake. Wananchi wa Nyamuma wanajua kuwa serikali yao haiwathamini kwani hata baada
ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kuamua kesi yao na kuamuru serikali iwalipe
fidia ya jumla ya shilingi milioni 850, serikali imegoma kulipa.

Mimi ninayo mifano mingi tu ya kuonyesha kuwa somo kuhusu ufisadi, kutoheshimu sheria, ubadhirifu wa kodi na rasilimali za umma vinavyofanywa na serikali linaanza kueleweka sasa kwa matukio halisi
yanayowagusa wananchi moja kwa moja. Haya si mambo ya kuzua au ya kubuni. Mageuzi si
usanii bali ni mchakato halisi wa kupigania haki na maendeleo ya watu. Mimi naona mpaka
hapo tulipofikia ni hatua kubwa katika mageuzi ya nchi. Hapo zamani za kale, tulikuwa
tumegubikwa na ukiritimba wa chama kimoja na hatukuwa na haki ya kusema wala kujua. Sasa
tunayo haki ya kujua na kusema. Hapo kesho tutajinyakulia haki ya kujiamulia mambo yetu
sisi wenyewe. Haki hii itatuwezesha kuwaondoa madarakani hao Miungu Watu wanaovunja haki
zetu za msingi kwa kutumia nguvu za dola.

Kuhusu kufukuzwa kwa mbunge Kabwe Zitto, hilo ni tukio la kusikitisha, lakini
linaloelezeka. Tuko vitani kuleta mageuzi na Zitto kaumizwa na risasi ya adui vitani. Ni
shujaa wa vita hivi na tumpe moyo wa kuendelea kupambana. Waliomjeruhi wanadhania
wameshinda, la hasha! Kitendo chao kimewaamsha wananchi kujua ukweli wa demokrasia tuliyo
nayo kuwa haitoshi. Kumbe haitoshi kuchagua wanamageuzi wachache kutetea haki zetu kule
bungeni. Kumbe Bunge la Jamhuri halipo, badala yake tunalo Bunge la Chama Cha Mapinduzi!
Wanakutana kama kamati ya chama na kuamua kulindana na kisha wanaingia bungeni kulindana.
Tungelisema hili bila mfano huu halisi wa kusimamishwa vikao vya Bunge kwa Zitto ambao
wananchi wamejionea wenyewe kwenye luninga wangesema sisi ni wazushi! Sasa kila mmoja
amejua kuwa katiba, sheria na kanuni za Bunge vyote vina dosari nyingi za msingi.

Kumbe katiba, sheria na kanuni za Bunge vimeunda Miungu Watu ambao haipaswi wasemwe! Upo
msemo unaosema kwamba anayemsema mfalme kuwa yuko uchi, hata kama kweli mfalme yuko uchi
wa mnyama, ajue shingo yake ni halali ya mfalme. Ataitwa mzushi, asiye na adabu na kisha
ataadhibiwa kwa kukatwa shingo. Hicho ndicho alichofanya Kabwe Zitto. Alimshuku Waziri
Karamagi kuwa ni mla rushwa kwenye mkataba ule wa mgodi wa dhahabu wa Buzwagi na kwa kuwa
huyo ni Mungu Mtu, hata kama tuhuma za rushwa dhidi yake ni za kweli, Bunge la Jamhuri
limeona hakuna haja kuchunguza tuhuma hizo ila ni busara zaidi kumwadhibu aliyetoa tuhuma
hizo.

Tukio hilo ni moja tu katika matukio mengi yatakayotokea siku za usoni. Wamesema kuwa hizo
ni rasharasha tu. Inamaanisha nini tamko hilo? Mimi naona wamejipanga kulihujumu kabisa
taifa hili.

Waswahili wanasema "wamekaa mkao wa kula". Ile hoja ya Mbunge wa Karatu (CHADEMA) Dk.
Willbrod Slaa kuhusu ufisadi katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) inatisha. Angepata fursa
ya kuiwasilisha bila shaka vichwa vingepukutika! Kumbe Watanzania tutajionea mengi,
mabilioni ya fedha za umma kutafunwa bila maelezo, kodi za wananchi kutafunwa hivyo kwa
kisingizio cha kutoa mikopo ya kupunguza umasikini, mikataba mingi ya kufilisi rasilimali
za asili kuwekwa saini kwa siri ili umma using'amue na kuhoji. Tutajionea wenyewe vituko
na kashfa nyingi za kushangaza kama vile viongozi kupora mali za umma au kutumia nafasi
zao kujitajirisha, unyang'au na kila uchafu unaoendana na ubeberu! Baba wa Taifa
alitufundisha wakati ule wa uhai wake kuwa ubepari ni unyama, na hakuna ubepari mbaya kama
ubepari uchwara unaojegwa katika enzi za utandawazi.

Wale uwadhaniao kuwa siyo utagundua kuwa ndio. Waliokuwa wahubiri wa ujamaa na uadilifu
utagundua kuwa ndiyo mabepari wa leo wanaoshiriki katika kila namna ya umafia. Haya mambo
ni ya kweli, yapo na tusidhani ni uzushi au hadithi ya "Elfu lela ulela"!

Swali: Dk. Mvungi hayo unayosema yanatisha. Sasa wanamageuzi mmejipanga vipi kukabiliana na hayo uliyoyaelezea?

Jibu: Ni vyema kwanza kujiweka sawa kuyafichua maovu haya wananchi wayajue. Kulijua tatizo
ni hatua ya kwanza katika kulipatia jambo hilo ufumbuzi. Mimi siamini kuwa kule CCM kila
kiongozi au kila mwanachama ni fisadi. Wapo wenye nia njema kule ambao pia wanaumia
wakiona ufisadi huu. Kumbuka ufisadi ni uovu wa kupindukia na hauna itikadi. Hiyo ni sura
moja ya kukuonesha kuwa tatizo tulilonalo ni la kitaifa na linahitaji ufumbuzi wa kitaifa
siyo wa chama kimoja au vyama vya upinzani peke yake.

Tunahitaji sasa uhuru wa pili. Tunahitaji kuanzisha mchakato wa kulikomboa taifa kutoka
kwenye ufisadi unaojijenga hivi sasa. Hatunaye Baba wa Taifa kutuongoza na kutuonyesha
jinsi ya kulitekeleza hili. Lazima tukae chini tutafakari mambo haya ili kwa pamoja tuvute
kamba kuzuia maangamizi ya taifa letu. Mimi kweli naona wenzetu hawa hawana aibu kabisa
kufanya maovu haya. Tunazo rasilimali nyingi mno kiasi kwamba tunaweza kusema Tanzania ni
Bustani ya Eden. Lakini kumezuka waroho na mafisadi wakubwa wanaotumia nguvu za dola
kuruhusu uporwaji wake na wageni kwa kisingizio cha "uwekezaji". Tusipogundua kuwa lugha
ya "uwekezaji" ni lugha ya utandawazi inayohalalisha ubeberu, hatutagundua ukweli kuwa
"uwekezaji" ndio ufunguo wa umasikini wa mataifa ya dunia ya tatu. Sijui kama viongozi
wetu wa leo wanatofautiana sana na Sultani Mangungo wa Msovero. Afrika imefilisika
kiuongozi na tunahitaji sasa mapambano ya uhuru wa pili kuikomboa Afrika kutoka kwenye
ubeberu huu unaojiita utandawazi.

Kumbuka uhuru wa pili ni dhana kubwa na nzito kifalsafa. Tutakuwa tunajipanga kupambana na
Watanzania wenzetu ambao wamesimama upande mmoja na ubeberu. Hawa wanao ndugu, jamaa na
marafiki wa ndani na nje ya nchi. Hawa wameshikilia hatamu za dola. Hawa wamejilimbikizia
mabilioni ya fedha kuweza kumrubuni kila mtu mwenye roho nyepesi nyepesi. Kwa pamoja hawa
wanaunda tabaka la kinyonyaji na kifisadi linaloangamiza taifa. Tabaka hili halina aibu,
huruma wala uzalendo.

Linajali matumbo yao tu na likishapora huhifadhi fedha na rasilimali hizo nje ya nchi.
Hili ni tabaka hatari kabisa. Hivyo usiniulize kama wanamageuzi tumejipanga vipi, jiulize
wewe uko upande gani katika harakati hizi, na uko tayari kufanya nini kwa ajili ya nchi
yako. Mimi nikuulize: Je, kuna kabila la Watanzania linaloitwa "wanamageuzi"? Kama hakuna
kwa nini mwanamageuzi awe mimi, asiwe wewe?

Swali: Je, unadhani ushirikiano wa vyama vya CUF, CHADEMA, TLP na NCCR-Mageuzi ni jambo makini na litakalofanikiwa?

Jibu: Mimi naona ushirikiano huo ni jambo zuri na la kuungwa mkono. Tuwape moyo waimarishe
ushirikiano ule, labda utazaa mafanikio kama tutapata chama kimoja kikubwa cha upinzani
nchini.

Swali: Je, wataacha ubinafsi na kuweka mgombea mmoja wa urais?

Jibu:
Suala la mgombea mmoja wa urais si zito wala gumu kama kukubali kuunda chama kimoja.
Tunachopigania ni kuwa na upinzani unaoleta maana, unaoweza kuiondoa CCM madarakani au
kuligawa Bunge na serikali za mitaa ili chama kimoja kisiwe na ukiritimba wa siasa na
maamuzi nchini. Hatutaki kuwa na Bunge la chama kimoja ambapo wanakutana kama kamati ya
chama na kufanya maamuzi kisha wakaingia bungeni na kupiga muhuri maamuzi yao.

Swali: Kuna baadhi ya Watanzania wanasema wanaotaka katiba mpya wanataka kugawana vyeo, wewe unasemaje?

Jibu: Ah! Hayo ni mawazo yao kama wanasema hivyo na ninayaheshimu. Mimi nataka katiba mpya
na sina lengo la kugawiwa cheo chochote. Nataka katiba mpya kwa kuwa katika katiba ya sasa
misingi ya demokrasia ni finyu sana. Lazima tuwe na katiba ya taifa huru la kidemokrasia
ambapo kila raia ana haki sawa na fursa sawa. Nataka katiba inayoweka misingi ya
demokrasia ya umma hivyo kwamba umma uwe na nafasi ya kuidhibiti serikali badala ya
serikali kuudhibiti umma. Nataka katiba inayounda tume huru ya uchaguzi badala ya hii ya
sasa ambapo uchaguzi unaendeshwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama.

Swali: Kwani ni kweli kuwa Kamati ya Ulinzi na Usalama ndiyo inaendesha uchaguzi?

Jibu:
Sijui ni lipi zuri, kujua ukweli na ukaishi kwa taabu na mahangaiko au kutojua
chochote na ukaishi kwa amani mustarehe. Kamati ya Ulinzi na Usalama haina mamlaka ya
kuendesha shughuli za uchaguzi kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi na katiba ya nchi. Lakini
katika utendaji, kamati hiyo ndiyo inapanga kila kitu na kutekeleza mikakati yote ya nani
ashinde na nani ashindwe. Wananchi hupiga kura, lakini kamati hii huchagua nani awe
kiongozi.

Swali: Rais Kikwete amesema tayari mikataba ya madini inadurusiwa. Tutapata sasa asilimia
30 kupitia kodi na mrahaba. Je, huoni hiyo ni hatua nzuri?

Jibu: Mimi namsifu Rais Kikwete kwa kutambua ukweli kuwa mikataba ile na sheria ya madini
ina kasoro. Hilo ni jema kabisa. Sikubaliani naye kuwa asilimia 30 inatosha! Mimi nadhani
tungepata asilimia sabini wawekezaji wakachukua thelathini. Sasa mwenye rasilimali ni
nani, sisi au wawekezaji? Tatizo hapa ni woga tulionao kuwa wawekezaji hawatapatikana.
Hiyo si kweli. Ramani ya madini ipo, wao hawaji hata kutafuta madini hayo, wanakuja
kuchimba tu!

Nchi zenye sheria nzuri za madini huhakikisha kuwa migodi ni mali ya raia wake, hivyo hata
ukitoza asilimia 30 kodi na hata usipotoza mrahaba hupotezi kitu kwani rasilimali iko
mikononi mwa raia wako. Tatiz o hapa ni kuwa tunatoa bure rasilimali ya Watanzania kwa
wageni, jambo ambalo si la busara wala halali. Lakini kule migodini hatuna udhibiti kwa
kujua kiasi gani cha madini kimepatikana. Wanachimba na kumimina dhahabu na kuondoka nayo
bila sisi kujua wamepata kiasi gani. Wanachotuambia wamepata ndicho chetu. Watanzania
tunayo tanzanite, dhahabu, almasi, na sasa tunayo pia mafuta. Kwa nini sisi ni masikini
kuliko mataifa ambayo hayana kabisa rasilimali asili kama hizo? Kama mtu ataniambia kuwa
tunao uongozi bora, sasa tumwombe Mungu atupe nini zaidi?

Swali: Unasemaje kuhusu ubinafsishaji wa sekta ya umma, huoni kama sasa uchumi wa nchi
unapaa ukilinganisha na hapo zamani tulipokuwa tunafuata ujamaa?

Jibu: Wengi wanaozungumzia kushindwa kwa ujamaa hawaujui hata huo ujamaa ni kitu gani.
Hebu nieleze hao wanaotetea ubinafsishaji wanaweza kuonesha mradi gani mpya waliojenga
ukiacha hizo mali zetu walizogawiana bure kwa kisingizio cha ubinafsishaji? Mimi naona
ubinafsishaji ungeandaliwa vizuri ungetusaidia kwa maana kwamba rasilimali zile
tungeziweka mikononi mwa wazawa au kuzibakiza mikononi mwa umma, lakini tukaruhusu wageni
kuwekeza kama wabia. Tusingekubali kabisa kuwapatia rasilimali zile kwa asilimia zaidi ya
hamsini. Kwa kufanya vile tulijikata miguu ya kuingilia kwenye ubepari sasa tumekuwa
viwete kiuchumi kwenye nchi yetu wenyewe.

Si kweli kuwa uchumi unapaa. Uchumi unaopaa ni wa nani? Labda ule wa wageni tuliowapatia
rasilimali zetu bure. Kwa mfano serikali iliuza benki nzima ya Biashara ya Taifa kwa
shilingi bilioni 15 tu, thamani ambayo hailingani na hata lile jengo yalimo hivi sasa
makao makuu ya benki hiyo. Mara baada ya kukabidhi benki kwa wanunuzi, tuliwalipa wanunuzi
hao bilioni 15 kama fedha za huduma za kibenki kutoka benki ya NMB. Sasa tuliuza benki
hiyo kwa bei gani? Lakini pia tuliwapatia akaunti yetu ya dhamana za fedha za kigeni yenye
dola milioni 80 hivi, kule Marekani. Unaweza kusema sisi ni wafanyabiashara wazuri kwa
kufanikisha uuzwaji huo wa benki yetu? Naweza kuchukua mfano wowote wa ubinafsishaji na
nitakuonesha kuwa tulifanya madudu.

Swali: Hivi karibuni serikali imetangaza kuwa itapeleka shilingi bilioni 22 kila mkoa
katika mchakato wake wa kupunguza umasikini, hili nalo walionaje?

Jibu:
Ah, ndugu yangu acha tu wapeleke, hazitakosa walaji hizo. Mimi siamini kuwa kila mtu
anaweza kujiajiri au kuwa mwekezaji. Kuamini kuwa mtu ambaye hajawahi kufanya biashara na
ambaye hana hata uzoefu wa biashara ataandika andishi la mradi na kufaulu kuanzisha
biashara au mradi wa uzalishaji mali ni hatari. Ubepari haujengwi kiholela hivyo. Ubepari
ni mfumo wa kisayansi kabisa wa uchumi. Ukiuendea kichwa kichwa utapoteza rasilimali za
walipa kodi bure. Kumbe kwa kudra ya Mungu wako watakaoweza na pia wako wengi
watakoshindwa. Tusishangae hayo yote mawili yakitokea kwa kuwa kweli hakuna maandalizi ya
kutosha yamefanywa kwa mchakato huo.

Swali: Maandalizi gani hayo unadhani yangefanywa?

Jibu:
Kila jambo litafanyika vizuri kama watendaji au wadau wake wataandaliwa kwanza
kielimu. Mimi naona silaha dhidi ya umaskini ni elimu bora na afya bora. Mengine yanaweza
kuja kama ziada. Taifa ambalo linaweza kuamua kuwa vijana wake walioko nje ya nchi
kujitafutia elimu hawana haki ya kusaidiwa wanapokwama kama wale waliokwama kule Ukraine
bado halijajiweka sawa kupambana na umasikini. Tuko tayari kuchangia harusi, vifo, michezo
na kadhalika, lakini tunasita kutoa fedha za kodi zetu kuwasomesha vijana wachache tu
ambao wamekwama kule Ukraine.

Mimi sioni mfungamano wa kisera wa malengo yetu. Iko wapi mipango ya elimu ya ujasiriamali
kwa hao watakaokopesha mabilioni hayo? Je, ni kitu gani shilingi milioni moja katika
biashara au mradi wa kukimu familia ya kawaida yenye watu wanne hivi? Zipo nchi zinayo
miradi ya kujikimu kwa raia wake. Lakini nchi kama hizo hazitoi mikopo holela kwa kila
mtu. Zinatoa mikopo kwa watu waliokwishahitimu kiwango fulani cha elimu na pia utaalamu wa
mradi unaoombewa fedha. Kisha wameunda taasisi ya kifedha yenye wataalamu wa kusimamia
mafunzo ya miradi, uendeshaji wa miradi na usimamizi wa miradi kwa wanaokopeshwa hadi
miradi yao iweze kujiendesha. Hili si jambo dogo la kukurupuka.

Swali: Eleza mtazamo wako wa serikali ya awamu ya nne inayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete ambayo imebakiza miezi michache itimize miaka miwili tangu iingie madarakani.

Jibu:
Mimi naona wamewaahidi Watanzania mbingu, lakini tulichopata ni jehenamu. Maisha
yetu sasa ni hoi bin taabani. Wakubwa uchumi wao binafsi unapaa, sisi walalahoi tumechoka!
Kiutendaji inaonekana katika kila jambo kuna 'usanii' mwingi, lakini tunachokipata ni duni
kabisa. Sipendi kubeza wala kudanganya. Je, walimu bila elimu ni jambo jema kwa elimu ya
taifa? Mimi naona ni kujidanganya tu kudahili wanafunzi na kuwajaza kwenye madarasa bila
walimu. Si kila mtu anaweza kuwa mwalimu, hiyo kazi ni wito, lakini pia ni taaluma.

Unaweza kusifiwa kwa kuanzisha chuo kikuu kipya, lakini chuo hicho kina wahadhiri? Na je,
hivyo vyuo vikuu vilivyopo umevifikisha wapi? Mimi naona tumekwama hapo, vyuo vikuu
tulivyonavyo hatuna uwezo kuviendeleza, ila tunajenga vingine! Kwa nini hatuoni kwamba
kuendeleza na kupanua vyuo vilivyopo ni bora kuliko kujenga vipya? Sasa naona elimu ya juu
imevamiwa kimamluki. Wale binafsi wanatoa tu vyeti bila kujali viwango vya elimu kwani
akifeli mwanachuo watakula wapi? Mimi naona hayo si mambo mazuri kwa taifa letu. Maendeleo
ya taifa hutegemea elimu, na tukichezea elimu tunachezea uwepo wa taifa letu. Tutakuwa na
watu wenye vyeti, lakini wasio na elimu. Tutashindwa katika kila jambo tutakalotaka
kulifanya kwa kuwa hakuna jambo linaloweza kufanywa na mbumbumbu.

Mimi naona utendaji wa papara katika kila jambo, lakini kwa kweli hakuna serikali
inayoweza kufanya kila kitu. Wangechagua mambo machache wakayafanya vizuri badala ya
kupapasa kila kitu na kukifanya vibaya. Naona uchungu kabisa kuona jinsi wanavyoachia
rasilimali asili kuporwa na wageni. Hilo nina uchungu nalo na sioni woga kulisema. Sheria
ya madini ni bomu na viongozi wa awamu ya tatu na ya nne walaumiwe kwa hilo. Naona pia
uchungu kwa ubinafsishaji holela wa rasilimali zetu. Tulijiuza rahisi mno, hilo ni jambo
ambalo sioni cha kujivunia. Naona pia kuwa ufisadi umekithiri na umegubika serikali nzima.
Hii kashfa aliyoibua Zitto na ile anayoizungumzia Dk. Slaa ni ishara mbaya kwa taifa.
Wakubwa wengi wanadanganya na kulihujumu taifa. Mimi naona hayo yanatosha, hakuna haja ya
kuzungumza mengi kwani yanatia uchungu. Watanzania wawe tu na juhudi na ushujaa wa
kukabiliana na hayo, wasikate tamaa. Sisi wanamageuzi tutaendelea kueleza kasoro hizi,
siyo kwa nia mbaya ila kwa kuwa bila ukweli, hakuna haki na bila haki taifa huangamia.

Swali: Sasa ni jambo gani la kuwatia moyo Watanzania unaweza kulisema?

Jibu: Kwa Watanzania wenzangu sote tunajua hali tuliyofikia. Wengi hatuna chakula, mavazi,
tiba na watoto wao hawapati elimu. Hatuhitaji nguvu nyingi kuelezea hali mbaya tuliyomo
kijamii na kiuchumi. Lakini hali hii isitukatishe tamaa kwani hakuna shida isiyo na mwisho
na penye nia pana njia. Najua kila mwananchi sasa ni mwanamageuzi. Tulipoanza tulikuwa
wachache. Sasa kila mmoja ni mwanamageuzi. Hili halina rangi za vyama kwani umasikini
hauna chama. Lazima tujifunze sasa na kwa haraka jinsi gani ya kubadili hali zetu kwa
kujikomboa wenyewe badala ya kungojea ukombozi uletwe na serikali. Nadhani kwa hili tuko
mbioni kufikia hatua ya mgeuko kote nchini.

Lazima mbinu za mageuzi zibadilike haraka. Hatuwezi kufunzwa mbinu za mageuzi na walio
madarakani. Inawezekana sasa tukaamua kubadili kabisa mchakato wa mageuzi kwa jinsi ambayo
italeta tija na kupunguza hasara ya upotevu wa muda na rasilimali. Kwa kuwa wenzetu walio
madarakani wamejikita katika ufisadi, wizi wa kura, matumizi ya dola kubaki madarakani na
kila jitihada ya kuleta mageuzi kwa amani wanazipiga vita, inawezekana tukaziacha mbinu za
sasa na kuona jinsi nyingine ya kuleta mabadiliko. Sijui tutachagua njia ipi, lakini
wakati ukifika njia itapatikana. Hakuna linaloshindikana wananchi wakiamua.

Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu 0755 312 859; barua pepe;
katabazihappy@yahoo.com na tovuti; www.katabazihappy.blogspot.com.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Novemba 11,2007

BABA WA TAIFA TUNAENDELEA KUKUENZI


Na Happiness Katabazi

MWALIMU Julias Nyerere Baba wa Taifa letu,leo tunaadhimisha miaka nane tangu ulipotutoka Oktoba 14,1999, na tukakupumzisha kwa amani katika Kijiji ulichozaliwa cha Butiama.

Tunaendelea kukuenzi baba japo kwa staili mbalimbali.Tukikuita baba kwa sababu wewe ni mwasisi wa taifa letu la Tanzania .Baba,ulikuwa Mwalimu wetu na hata leo hii inaendelea kutufundisha katika yale yote uliyotuusia.

Nakuomba baba uchungulie toka uliko utuangalie hapa duniani katika taifa lako la Tanzania uone tunavyokuenzi hususan katika yale mambo kuntu(masuala mazito) sana uliyotufundisha na kutuhusia.

Wasia wako uliukita katika mtindo wako wa maisha binafsi,uongozi wako uliotukuka,matamshi na matendo yako.Miongoni mwa mambo uliyotuusia yanahusu elimu.Ulipenda watu wote wapate elimu na ukatuambia kila apataye elimu afanye nini.

Baba, uliwahi kutuambia kwamba;aliyepata bahati ya kusoma na akapata elimu ni kama mtu ambaye kijiji kimempa chakula chote kilichopo ili ale ashibe,avuke ng’ambo akakiletee kijiji chote chakula ,na asipofanya hivyo akajenga kiburi ni sawa na msaliti.Baba tunakuenzi kwa hilo.

Tunakuenzi kuanzia katika suala la elimu, ambalo baba ulibobea katika hilo ukiwa mwalimu na mwanafalsafa. Ulitufundisha falsafa ya Elimu ya Kujitegemea, uliyoiasisi mwenyewe; ulituusia kwamba elimu itujengee akili za udadisi.Leo tunakuenzi baba kupuuza kuwa wadadisi na wabunifu.Shuleni tunasoma kwa kukariri ili tufaulu mitihani.Baba,hata udadisi wa kisiasa umepigwa marufuku katika taasisi za elimu ya juu, ili tuwe mbumbumbu,mazumbuku,mzungu wa reli,wasioweza kuhoji lolote.

Hukuishia hapo ukaanzisha elimu ya watu wazima. Tunakuenzi baba kwa mipango na mikakati lukuki ya elimu.Baba, kupitia mipango mbalimbali ya elimu kuanzia ya msingi (MMEM), sekondari (MMES) na kadhalika, tumeongeza idadi ya shule nchini hususan za sekondari ambazo baadhi ya wajukuu zako wanaziita eti sekondari za Lowassa,na walimu wake wanaitwa ni ‘voda fasta’ bila shaka utamkumbuka huyu kijana wako,ndiye waziri wetu mkuu wa sasa.

Baba ukichungulia huwezi kuamini wingi wa shule hizo. Si unakumbuka idadi ya kata katika nchi hii uliotuachia. Tumekuenzi kwa kufungua sekondari kwa kutumia kanuni ya kata moja shule moja kama ulivyoacha tumekusudia katika sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995. yaani baba tumeanzisha shule nyingi kwelikweli kiasi kwamba hazina walimu.

Hilo baba usidhani ni tatizo si afadhali tunazo shule angalau tupate mahali ambapo wajukuu zako watakaa wapige soga kuliko kukaa bure nyumbani. Alafu baba kama tusingezifungua si wagombea uongozi wetu watakosa kura katika uchaguzi ujao.

Baba usijali masuala ya kitaaluma, tunaenzi uanasiasa wako kwa kuanzisha shule za kisiasa. Hata zisipozalisha wataalam, si wawekezaji wataendelea kuja na wataalam wao.

Tunajitahidi kwa kuhakikisha angalau kila shule tuliyoianzisha ina mwalimu mmoja,tena huyo huyo ndio mkuu wa shule, wasaidizi wake viranja. Kwa kawaida huyu mwalimu akisafiri usiwe na wasiwasi, anakabidhi mafaili ya ofisi na majukumu yote ya kufundisha kidato cha kwanza hadi cha nne kwa kiranja mkuu.

Usiwe na wasiwasi baba, viranja wanaimudu kazi hiyo vizuri sana, hii ni katika kuakikisha tunaienzi vyema taaluma yako ya ualimu kwa kuifanya si taaluma tena bali kichwa cha mwenda wazimu ambacho hata asiyejua kushika wembe anaweza kukinyoa, kwani baba, lazima mtu ajue kusoma ndio awe mwalimu?

Tunakuenzi baba kwa kuendelea kusoma tukiwa watu wazima na katika siku zote za maisha yetu. Chungulia baba uone jinsi wengi wetu walivyofanikiwa kusoma ukubwani na kujipatia shahada za juu kabisa. Tangia uondoke baba idadi ya wanao wenye shahada za falsafa (PhD) imeongezeka kwa kasi. Usishangae baba tumewezaje hilo, siku hizi kuna shahada tunazipata kiurahiiisi kwenye mtandao. Wenyewe baba wanaziita za ‘on line’.

Kwahiyo tunakuenzi baba kwa kurahisisha mambo, tunatafuta wenzetu wenye uwezo kichwani tunawapa visenti kidogo wanatufanyia ‘assignments’ na kutuandikia thesis, tunawasilisha kwenye vyuo vya ughaibuni, kisha kufumba na kufumbua tunaitwa ‘madokita’. Hicho cheo baba tunakitumia vilivyo kukuenzi katika siasa , maana kitaaluma hatuwezi kukitumia, samahani baba hatuna ujuzi wowote katika nyanja za shahada tunazotunukiwa.

Kukuenzi kwetu hakuishii hapo baba. Si unakumbuka ulituachia vyuo vikuu. Tumekuenzi si tu kwa kuviboresha bali tumeongeza na vingine vingi baba. Kwa sasa baba tuna universities zisizopungua therathini(30). Zaidi baba tumekuenzi kwa kuongeza kwa kiasi kikubwa udahili katika vyuo hivyo.

Hiyo ni mojawapo ya mikakati tunayoitumia kukuenzi kwa kuuporomosha kwa kasi ya roketi ubora wa elimu ya juu uliyotuanzishia baba. Kwa mfano baba katika chuo kikuu cha mlimani, tumekuenzi kwa kukigeuza mfano wa sekondari kuubwa!

Nikufafanulie kidogo baba, chungulia baba uone jinsi tulivyokuenzi kwa kuboresha mazingira ya kazi ya wafanyakazi wa chuo hicho kwa kuwarundika waadhiri na maprofesa watatu watatu au wawili wawili karibu katika kila chumba kinachofanana ofisi japo ni vyumba vidogo vidogo baba. Si unafahamu baba kwamba ualimu ni wito na uadhiri ni wito mkuu na afterall hatuna fedha zilizobaki baada ya kununua mashangingi hata tuwajengee ofisi zenye ‘vipupwe’ na nafasi.

Baba, fedha zimetutindikia tunawalipa mishahara ambayo haina tofauti sana na posho ya siku nne ya mheshimiwa mmoja anayetuwakilisha bungeni. Tumekuenzi enzi baba kwa kutambua kuwa siku moja ya mbunge aliyesinzia kwenye kiti cha kuzunguka kule dodoma ina thamani sawa na wiki nzima ya mhadhiri anayesugua kichwa na kula vumbi la vitabu akitoka jasho kuwaelimisha wanao.

Lakini baba, nisiseme sana maana wahadiri wenyewe baadhi yao wameamua kukuenzi kwa kuweka chaki chini na kukimbilia kuomba kura za wananchi. Wana ka-msemo eti siasa inalipa vizuri hasa ukiweza kupata takrima ya ‘kuinvest’ humo. Wengine wao wanakuenzi kwa kukalia kimya makosa ya watawala.

Wanachelea kufungua midomo yao wasije wakaikosa ahadi ya maisha bora waliyoahidiwa na kijana wako, japo wengi wao hawana nyumba za kuishi tuankaa nao mitaani ‘uswazi’ au ‘madongo poromoka’. Tunashangaa baba,wanawezaje kukaa chini wakafikiri na kuandika mambo ya akili,ya kisomi wakiwa wanaishi huku uswahilini kwetu ambako kila mpangaji ufungulia redio yake.

Wameshindwa baba kuandika chochote cha maana, wanakuenzi kwa kuwaelezea kila siku mawazo yako uliyoandika,wakitoka hapo wanahubiri na kukariri tu nadharia na mawazo ya wasomi wenzao wa nchi za ughaibuni. Si kosa lao baba, hivyo ndivyo watawala wamewataka wawe labda wasije wakahatarisha maslahi ya wenye nacho.

Baba, kwa kushindwa kuwajengea wasomi wetu hawa nyumba za kuishi, hatuwezi kukulaumu wewe,maana enzi zako nyumba zilijengwa pale mlimani zilizowatosheleza waliokuwepo. Na kwa kuona mbali baba ulitenga eneo kubwa la mlima ule kwa ajili ya ujenzi wa baadaye, bila shaka wa vyumba vya mihadhara, ofisi, makazi ya wahadhiri na wanafunzi wao.

Sisi baba, tumeamua kukuenzi kwa kulitumia eneo hilo ulilotutengea kwa staili mbadala kabisaa! Tumewekeza baba kwa kutumia sehemu ya eneo hilo kuwapa wageni makaburu; hapana ni ndugu zetu wa sauzi, wanyonyaji; sio – ni wawekezaji, makupe; no! ni wajasiriamali, tumewapa wajenge maduka ya kisasa ya bei mabaya kwa ajili ya wenyenazo kufanya shoping na walalahoi kwenda kujionea mambo! Usishangae baba, katika maduka hayo miwani ya jua bei yake ni sawa na mshahara wa kima cha chini ongeza noti kadhaa!

Tunaendelea kukuenzi baba kwa kutojali tena mwanafunzi wa chuo kikuu anaishi wapi,ni mtu mzima atajua mwenyewe. Anasomasomaje ‘madesa’ au vitabu shauri yake, anakula au ‘anadeshi’,kalala pazuri au ‘kabebwa’ no bode keaz. Samahani baba hiyo misamiati mitatu hukutuachia,imetungwa na wasomi wenyewe kutokana na maisha magumu yanayowakabili kutokana na harakati za kukuenzi.

Madesa wanasema ni makaratasi ya kuokoteza yanayofanana na kile kilichomo kwenye vitabu wasivyoweza kuvipata; kudeshi baba ni kushinda bila kula nakokufanya msomi ili aweze kumudu uchangiaji wa gharama za elimu ya juu. Wanachangia baba kwa mujibu wa sera iliyotungwa na wale wanaokuenzi kwa vile uliwasomesha bure elimu bora,ukawalisha bure chakula bora, ukawapatia vitabu bora na walimu bora. Wanakuenzi baba kwa kutanguliza adjective bora kabla ya nomino.

Baba, kule Dodoma ulikotuambia viongozi wetu wahamie wakakuenzi kwa kukataa kwenda huko hadi leo,sasa tunapatumia kukuenzi kwa mtindo mpya. Tumeanzisha Chuo Kikuu kipya huko. Hatukupata shida ya majengo ya kuanzia, tumetumia yale yale ambayo waliyatelekeza uliowaagiza waame Magogoni waende Ugogoni.

Eeh, tumetumia na mojawapo ya majengo ya chama ambayo awali kilikataa kuyarejesha kwa umma baada ya kuanzishwa mfumo wa vyama ulivyotwambia visiwe utitiri,mpaka sasa havijawa utitiri baba, tunavyo kumi na saba tu japo vingi vina tatizo la utapiaruzuku.

Baba, ulituachia uhuru wa kutoa kauli na ukavifanya vyuo vikuu mahali huru pa kujieleza. Tunakuenzi baba kwa kuua moyo huo. Kila anpojitokeza anyethubutu kuwa jasiri kama wewe tunamnyamazisha ili wewe tu ubakie mwenye kuenziwa. Kuna mjukuu wako mmoja, labda humjui vizuri kwani ni mdogo sana. Tumemwekea breki ya kuongea kwa niaba ya wananchi katika chombo cha uwakilishi. Haikutosha baba,juzi tu alialikwa chuo kikuu,lakini tukafanikiwa kumdhibiti maana tuliona ana fikra huru kama zako tukakuenzi kwa kumkatalia kuingia chuoni. Chungulia baba umwone huyo kijana.

Vilevile katika uwanja huo huo wa elimu,tunaendelea kukuenzi kwa kufanya midahalo isiyo na tija. Tunatajataja jina la lako,tunakunywa maji ya kilimanjaro,tunagahawana posho,tayari tunakuwa tumekuenzi.

Baba ulituhusia pia tuwe na umoja wa kitaifa,watoto wa baba mmoja wasiokuwa na ubaguzi wa kidini wala kikabila.Baba ukasema katika karne ya 20,wanangu mnazungumzia ukabila,ukatuuliza iwapo tunaka kutambika?Tunakuenzi baba,hasa linapokuja suala la uchaguzi.

Ni hivi juzi tu tu limchagua Rais wa Awamu ya Nne,Jakaya Kikwete, bila wewe kuwepo.Tunakuenzi kwa kukataa ukabila, lakini wapo baadhi ya wanao wanaouendekeza.Baba unamkumbuka yule motto wako kipenzi Dk.Salim Ahmed Salim? Wapo waliompigia kumbo asigombee kiti cha urais kwa sababu ya asili yake, ngozi ya rangi yake.Eti yeye ni Mwarabu,eti alikuwa mwanachama wa Hizbu!

Pia yule mwanao Joseph Mungai ambaye ni waziri tangu enzi za utawala wako hadi sasa, naye ameambia yeye si Mtanzania ni ‘mkikuyu’, na aliambia hivyo baada ya kugombea nafasi ya NEC kupitia mkoa Iringa ambapo mwaka huu chama chako ulichokiasisi kinafanya uchaguzi mkuu.

Dhambi ya pili baba tumetenda,utusamehe na utuombee kama ulivyotuahidi kabla hujatutoka, kuwa unajua tungelia sana baada ya kifo chako,lakini kwamba utatuombea.

Vile vile baba ulituasa kwamba serikali haina dini,na kila mtu awe na uhuru wa kufuata dini anayoipenda.Kwamba dini kamwe isitutenganishe.Baba ulikuwa Mkatoliki mwaminifu, lakini uliwapenda na kuwaheshimu wanao Waislamu na hata wengine waliofikia wakakubatiza jina la Musa!

Baba mwaka huu tunakuenzi kwa kukwaruzana kidini.Tunabisaha juu ya Mahakama ya Kadhi na kunyoosheana vidole machini huku chama ulichokiasisi mwenyewe kikiwa ndicho kinachokonoa udini huu kwa kuwaahidi dada na kaka zetu wa Kiislamu kwamba kina sera ya kuanzisha Mahakama ya Kadhi.Tuombee baba,amani uliyotuachia tusiipoteze kwa kuanzisha taasisi ambazo hukuturithisha na ambazo ni hatari.

Baba katika suala la uchumi tunaendelea kukuenzi kwa kuuza kila raslimali uliyotuachia. Ahsante baba kwa kutuachia mali. Alhamdulilahi hatujaanza kutoana roho – yarabi kwa mali ulizoacha baba. Ila tumeziuza kisawasawa.
Baba zile nyumba ulizotuachia ukasema wakae humo watumishi wa umma tumeziuza na pesa tulizopata tukazitumia kuwapangishia viongozi wetu vyumba katika mahoteli makubwa. Si unaona mwenyewe tulivyo na akili.

Baba yale mabenki uliyotuachia tunaendelea kuyauza, viwanda tunaendelea kuvinadi, mashirika hatujaacha kuyapiga bei, mahoteli hatujachoka kuyabinafsisha na madini tuayatoa zawadi kwa marafiki zetu wa ughaibuni kwa njia ya mikataba yenye kamrabaha. Baba, katika miaka michache ijayo almasi,dhahabu,tanzanite,,bati, uranium na vito vingine vya thamani ulivyotuachia tutakuwa hatunavyo tena. Hizo zote ni harakati za kukuenzi maana ulituachia mali nyingi kiasi kwamba zinatulewesha.

Tunakuenzi baba hata katika suala zima la uongozi bora.Baba,unamkumbuka yule kijana wako uliyempenda sana kwa tabia yake ya utanashati na usafi wa mwili na roho,hata akaitwa Mr.Clean?Naye amekuenzi hivyo.

Amekuenzi Baba kwa kutuhumiwa kufanya Ikulu ni mahala pa ujasiriamali japo wewe ulimhusia kwamba Ikulu ni mahala patakatifu.Uliuliza baba, ikulu pana biashara gani?’ Swali lako .Baba kijana wako kakuenzi kwa kulijibu kwamba ikulu pana biashara ya kutumia dhamana ya ukuu wa nchi kujipatia mikopo bila kuulizwa ulizwa ili ujasiriamali.Tunakuenzi baba,kwa kuisigina vilivyo sheria ya Maadili ya Viongozi.Baba,kalianzisha kaka, wadogo zake unatarajia wafanyeje?

Na wadogo nao wameamua kukuenzi.Wewe baba ulituambia ,’watu safi katika nchi hii wapo chungu nzima’ utuwie radhi baba mpaka sasa hatujaweza kuwatambua.Ila angalau tumewatambua hao wengine.Tumekuenzi baba kwa kuunda timu ya mchezo wa ufisadi, inaitwa”The list of shame’ aka “Jk eleven’.Hii timu inakuenzi vizuri sana baba,kwa kuongeza harufu chafu uliyoisikia uliposema ‘kanchi kananuka rushwa!’. Siku hizi baba siyo kunuka tu, bali ka-nchi kamevunda ufisadi’ kuanzia sebuleni hadi jikoni.Yaani baba huwezi kuamini, uvundo umefika hadi kwenye jiko la uchumi(Benki Kuu ya Tanzania).

Baba ungekuwepo endapo wala rushwa wangetiwa hatiani na vyombo vya sheria ungeamuru wachapwe viboko wakati wakuingia gerezani na wakati wa kutoka ili wakawaonyeshe wake zao makovu ya bakora hizo.Lakini sasa hakuna wakuamuru hilo.

Tunakuenzi Baba, tukikumbuka ulitufundisha hata kutunga mashairi, mfano ni tunaposoma kile kitabu chako cha ‘Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania’.usibishe baba ebu soma shairi hili uone tunavyofuata nyanyo zako:

“Mkataba wa Buzwagi, alisaini Karamagi,
Umezua hoja nyingi,tena hoja za msingi
Kulikoni Karamagi,akaiuza Buzwagi
Mbona hanywi Konyagi,na wala havuti Bangi”?

Buzwagi unaijua baba;ni eneo moja lenye utajiri wa madini uliyotuachia, kijana wako Karamgi kawagawia wazungu kwa kusaini mkataba ambao ukisoma baba utalia machozi.

Baba tunazidi kukuenzi kwelikweli, hadi ndani ya chama ulichotuachia.Baba ulituambia chama kiwe na matawi imara.Tumekuenzi baba kwa kuimarisha matawi hayo., ila si kama yale matawi ya kizamani, tumeanzisha matawi yanayoendana na wakati.Nikutajie matawi hayo Baba japo machache?Haya…moja linaitwa,mtandao-maslahi,jingine mtandao-halisi, la tatu mtandao-matumaini, la nne mtandao-dhuluma—yako mengi baba.

Halafu Baba unajua tunakuenzije kuhusu suala la alama za chama?Baba uliturithisha jembe na nyundo ukasema kwa maana hiyo chama ni cha wakulima na wafanyakazi.

Lakini tumekuenzi Baba, kwa kugundua kwamba hizo alama haziendi na wakati.Hatujazifuta,ila tumekigeuza chama kuwa cha wenye uwezo ,wafanyabiashara na mafisadi.Baba, hakuna wa kukwambia kwamba hili si kweli.

Akikwambia hivyo muulize mweka hazina wa sasa wa chama ni mkulima au mfanyakazi?Je hayumo kwenye Jk eleven? Muulize nini kilitokea kuhusu ufisadi wakati wa uchaguzi ndani ya chama.

Baba , watoto wadogo ambao hakukuona,wanachanganywa sana juu ya sura yazo.Kuna sanamu za ajabu kabisa zinachongwa na kuwekwa mitaani sasa, hadi wengine wakubwa wanakaribia kuisahau sura yako halisi.Wahurumie hao baba, njaa zao zinawatuma vibaya.

Baba, niruhusu niwakumbushe wanao wote kwamba hatuwezi kujivunia wewe kuwa baba yetu na kusema kwamba tunakuenzi, wakati kile tunachokifanya ni kinyume cha mafundisho,wasia na imani yako.

Tuombee baba, ili mfumo wa elimu yetu ukuenzi,ili mfumo wa uchumi wetu nao ukuenzi na mfumo wa siasa ukuenzi.Kadhalika viongozi wetu wakuenzi kwa maneno yao,mawazo yao na matendo yao.

Baba ,viongozi wetu inabidi wakumbuke maneno ya Yesu Kristo aliyowaambia watu wa taifa la Uyahudi,kwamba “Hamjui kwamba mnaye baba mwingine,ninyi si watoto wa Ibrahim,ninyi ni watoto wa ibili,kwa kuwa ibilisi amekuwa mwongo na mnafiki tangu mwanzo,nanyi mnayatenda hayo hayo kama baba yenu”.

Sasa baba ,wanao tunapojivunia ubaba wako,baadhi ya yetu wanaye baba mwingine ambaye si wewe!Baba yao ni beberu(bepari aliyekomaa),kwani bepari amekuwa mnonyaji,tangu mwanzo hata leo hii,angali akinyonya kwa kutumia utandawazi,unafsishaji na kuendekeza masilahi binafsi.

Viongozi wetu wa leo mnamuenzi baba yupi?Baba Mungu alikuumba na ukiisha kuifanya kazi yake hapa kwetu,akakutwaa.Jina la Bwana lihimidiwe na aipumzishe roho yako mahali pema peponi.Amina.

0755 312859:katabazihappy@yahoo.com;www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili , Oktoba 14, 2007

KWANINI MAWAZIRI WANAZOMEWA?

Na Happiness Katabazi

MTAJI Mkubwa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na serikali yake ni uoga na ukondoo wa Watanzania. CCM imekuwa ikidumisha ukondoo huo ili wananchi wabaki mbumbumbu wasio na uwezo wa kuona ukweli wa mambo na kuweza kukosoa sera, sheria na vitendo viovu wanavyofanyiwa na serikali.

Ningependa kuwapongeza Watanzania kwamba wameweza kuthibitisha katika wiki mbili hizi kwamba wamepevuka, si mbumbu tena kama baadhi ya viongozi walivyofikiria.
Wananchi wa Tanzania wameweza kuelewa hoja ya ufisadi iliyotolewa na Watanzania wenzao ambao nao wanaipenda nchi yao.

Pili, Watanzania wameweza kuwaadhibu viongozi wa serikali na CCM waliokwenda mikoani kubeza hoja ya wapinzani kwa kuwazomea adharani. Nawapongeza sana wananchi hasa wa Mkoa wa Mbeya.

Viongozi wa serikali wamekuwa wakitisha na kusema kwamba wapinzani ni wachochezi na hata vyombo vya habari vilivyoandika habari za ufisadi vimeitwa kuwa ni vya uchochezi.

Hii inamaanisha kwamba serikali ya CCM ina amini kwamba wenye haki ya kuwaambia Watanzania ukweli ni wao pekee.

Kwa hiyo, mtu mwingine yeyote akienda kuwaeleza wananchi taarifa zozote zile anaitwa mchochezi, mzushi, hana kazi za kufanya, asiye na hoja.

Lakini upo usemi unaosema kwamba unaweza kuwadanganya watu wote kwa muda fulani, lakini huwezi kuwadanganya watu wote kwa muda wote, kwani ukweli unaposimama, uongo hujitenga.

Sisi Watanzania tuna uwezo sasa wa kuchambua mchele na pumba, si mahala pake sasa kulishwa kasumba na propaganda za CCM wakati fedha zetu zinaporwa, mali na rasilimali zetu zinafujwa na nchi inakwenda mrama na gharama za maisha zimepanda.

Jambo la kusikitisha ni kwamba serikali inawasikia wageni au wafadhili, lakini haiwasikilizi wananchi wake. Kwa hiyo serikali imeanza kuzijibu hoja za wapinzani kijuujuu baada ya wafadhili kuchachamaa.

Hii inamaanisha kwamba wafadhili wasingechachamaa, hoja za wapinzani zingepuuzwa, ukweli ungefichwa na ufisadi ungeendelea.

Kipimo cha heshima ya serikali yoyote duniani na viongozi wake, ni jinsi wananchi wanavyowapokea na kuwa tayari kuwasikiliza. Wimbi la zomeazomea ni ‘tsunami’ inayoizengea CCM na serikali yake.

Ipo hatari serikali hii ikasombwa na tsunami hiyo, kwani wananchi wanapokosa imani nayo, hawaiheshimu tena na wala viongozi wake hawaonekani kuwa viongozi wenye heshima.

Ukiangalia uendeshaji wa dola, mihimili mikuu ya dola imepoteza sifa. Mhimili wa kwanza ni Bunge, limepoteza umaarufu na sifa yake baada ya kujigeuza kuwa kama kamati tendaji ya CCM.

Matukio kadhaa ya hivi karibuni, yamedhihirisha kuwa Bunge letu kwa kiasi fulani halisikilizi hoja wala kufuata kanuni, kwa kuwa CCM ina vita ya kuangamiza wapinzani.

Kumbe fursa ya sauti ya wanyonge kusikika bungeni imepotea na mfano halisi ni jinsi Bunge lilivyojadili hoja ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, kuhusu utata wa mkataba wa Buzwagi.

Mbunge huyu kijana alifikisha hoja bungeni akimtuhumu Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, alivyotia saini mkataba huo hotelini nchini Uingereza.

Basi, hata kama Bunge lingeona hakuna haja ya kuunda tume huru ya uchunguzi wa mkataba ule, basi hoja hii isingesababisha Zitto kuadhibiwa, maana hakuwa amemdhalilisha mtu.

Mhimili wa pili ni serikali, nao umepoteza sifa kwa kujiingiza kwenye kashfa nyingi za kiutendaji, kashfa za namna hiyo zinaashiria ufisadi mkubwa ndani ya serikali yetu.

Mhimili huu una kashfa nyingi, ikiwemo kashfa ya IPTL ambayo hadi sasa tunaendelea kuilipa kampuni hiyo dola 100,000 kila siku, kwa mradi wa ovyo, na hatujui ni lini kashfa ya Richmond itachunguzwa ili wananchi waambiwe ukweli.

Kwa mtazamo wangu, hata chombo cha kukabiliana na rushwa kimekuwa chombo cha kusafisha na kupaka rangi ufisadi, kama kilivyofanya kwenye Richmond, baada ya Watanzania kuteseka sana kwa kukosa umeme na fedha nyingi kulipwa kwenye makampuni yasiyo na uwezo wa kuzalisha umeme.

Na hata hatujaambiwa nani amewajibishwa, tulichoambiwa ni kwamba hapakuwepo na rushwa. Hivi nani anaamini maelezo hayo?

Takukuru sasa inachunguza kashfa ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BOT) na mkataba wa Buzwagi. Hivi Takukuru ina ubavu wa kuchunguza kashfa hizo? Watanzania tungoje tu kuambiwa Buzwagi na BOT hapakuwa na vitendo vya rushwa wala ufisadi.

Sasa matokeo ya aina hii ya utendaji wa dola ndiyo yanayopelekea wananchi kukosa imani na serikali, CCM na viongozi wake na kuamua kuwazomea na kuwapiga mawe.

Kama viongozi wetu wa serikali wasipobadili tabia na wakashirikiana na wananchi kutokomeza ufisadi na kuwaletea wananchi maendeleo ya kweli, nasisitiza tena viongozi wa CCM na serikali wasije kushaanga wakicharazwa bakora mitaani.

Wananchi wamechoshwa na ufisadi unaofanywa na baadhi ya viongozi, wamechoka na uroho wao wa mali usio na kipimo. Na hakika nasema, wakiacha kuzomea, watabeba bakora na kuanza kuwacharaza viongozi wetu, hatua ambayo sitaki tuifikie.

Mungu Ibariki Afrika,Inusuru Tanzania

Chanzo:Gazeti la Tanzania la Alhamis ya Oktoba 11,2007

WAANDISHI WA HABARI WAKIWA KAZINI


Pichani nipo na Mwanahabari mwenzagu toka gazeti la The Citzen,Bernad James, nje ya jesngo la Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam,kufuatilia wa kesi ya madai iliyofunguliwa Ijumaa ya Oktoba 5 mwaka 2007, na vyama vinne vya siasa dhidi ya Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali. James ni mwandishi mwenzangu ninayeripoti naye kesi mbalimbali katika mahakama hiyo.(Picha na Kassim Mbarouk wa Gazeti la Mwananchi).

ZIARA ZA MAWAZIRI SI JIBU LA HOJA ZA WAPINZANI

Na Happiness Katabazi

HOJA ya wapinzani kuhusu tuhuma za ufisadi, ukiukwaji wa maadili kwa viongozi, ugumu wa bajeti na ufujwaji wa rasilimali za nchi, zimeichanganya Serikali kiasi cha mawaziri na makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwenda mikoani kujaribu kuondoa sumu hiyo.

Utetezi unaotakiwa utolewe na serikali si kwenda kuhutubia wananchi mikoani, ni kukaa chini na kuangalia wapinzani wametoa hoja zipi na serikali kuzijibu kwa vitendo na kitaaluma.

Mfano, Mbunge wa Karatu Dk. Willibrod Slaa, (CHADEMA) anaposema kwamba Mkaguzi Mkuu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG), alinyimwa mikataba ya ujenzi wa minara pacha ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), hawezi kujibiwa kwa mawaziri, manaibu wao na makada wa CCM kwenda kuwahutubia wananchi.

Nasisitiza na kutoa ushauri wa bure kwa Serikali, dawa ya hoja za wapinzani si kuwatoa viongozi hao wa serikali katika ofisi zao na kwenda kutangatanga mitaani kuhutubia wananchi, tena kwa kutumia fedha za walipa kodi na fedha za CCM wakati baadhi ya wana CCM wanalia njaa.

Na hata hivi karibuni vyombo vya habari viliripoti habari kwamba uchaguzi wa CCM Mkoa wa Mara ulishindwa kufanyika baada ya kukosekana kwa posho za wajumbe hadi kada mmoja na mfanyabiashara wa mkoa huo, kuokoa jahazi kwa kutoa mamilioni ya fedha zake kwa ajili ya posho za wajumbe wa mkutano huo na hatimaye ukafanyika.

Ziara hizo hazina maana yoyote zaidi ya ufujaji wa fedha za umma. Binafsi najiuliza kama ni kwenda kunadi Ilani ya CCM leo hii, ina maana wakati wa uchaguzi wa mwaka 2005, iIlani hiyo haikunadiwa, na kama haikunadiwa vizuri ni vipi CCM ilishinda kwa kishindo?

Serikali ijibu hoja na kama inaona wapinzani hususan Dk. Slaa amechafua jina la viongozi, basi akamatwe na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria. Hiyo ndiyo dawa ya kujibu hoja za wapinzani.

Dk. Slaa anaposema Kampuni ya Meremeta haimilikiwi kwa asilimia 100 na serikali, badala yake inamilikiwa kwa asilimia 50 na asilimia 50 iliyobaki inamilikiwa na Kampuni ya Trinex ya Afrika Kusini, je, uzushi uko wapi katika hili?
Je, hati ya Brela ya kutambua usajili wa kampuni hiyo uliofanywa kwenye visiwa vya wakwepa kodi huko Uingereza je, ni uongo?

Dk. Slaa ameuliza katika hoja yake kwamba, je, Serikali ya Tanzania haikushiriki kwenye ufisadi kwa kufungua kampuni ya wakwepa kodi, kwanini serikali haitaki kueleza ilipofungua kampuni Uingereza katika visiwa vya Ilse of Man ilikuwa inakwepa kodi ya nani?

Na je, ni halali kwa serikali yetu kuanzisha kampuni hizo zinazotuhumiwa kuwa ni za kifisadi? Hoja kama hii isipojibiwa vizuri Watanzania tutaichoka serikali.
Labda ni vizuri pia kuuliza Kampuni ya Meremeta ilifanya biashara gani kustahili kulipwa mabilioni kutoka BoT na iliingizia taifa faida gani?

Sisi wananchi wa kawaida tukiamini kwamba Kampuni ya Meremeta iliundwa kwa madhumuni ya kuchota fedha za BoT na kuzipeleka nje ya nchi, tutakuwa tumekosea?
Kwaninii hata ilipofilisika hatuambiwi nani aliteuliwa kama mufilisi wa kampuni hii? Kwani serikali haijaeleza kuhusu madeni yote ya kampuni hiyo mufilisi.

Watanzania tunataka kujua, hiyo Trinex ya Afrika Kusini iliyolipwa kwa fedha za walipa kodi ni ya nani? Sasa haisaidii serikali kutapatapa na kukurupuka kujibu kashfa hii wala kuwahutubia wananchi hakutasaidia serikali kujikosha.

Hoja ya Dk.Slaa tumeielewa na hii ni mara ya pili nasisitiza inahijati majibu thabiti na si ya ‘mipasho’. Serikali ijue kwamba wananchi si mbumbu kiasi cha kutong’amua ukweli wa mambo.

Alipozungumza na waandishi wa habari Ikulu Dar es Salaam, Mzee Kingunge Ngombare-Mwiru, aliwabeza wapinzani na kusema hoja zao zimejaa uzushi, uongo na wana wivu, kwa sababu CCM iliwashinda katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, na sasa wanaona wivu kwamba serikali inatekeleza ahadi za kuleta maisha bora, imejenga shule nyingi za sekondari.

Kitu ambacho mzee Kingunge amesahau ni kwamba tayari serikali ipo madarakani na yeye ni waziri na hakuna mpinzani aliyekwenda mahakamani kupinga kutokuitambua serikali iliyopo madarakani.

Kwa hiyo, hoja ya Kingunge hata kama alitumwa na serikali kama alivyodai, ni ya kukurupuka na ailengi wala kujibu hoja ya vigogo wanaotuhumiwa kwa ufisadi.

Kwa kuwa hoja ya wapinzani ni ufisadi, wizi wa mali za umma na uvunjwaji wa maadili ya viongozi unaofanywa na viongozi wakuu wa ngazi za juu za serikali na CCM, jibu la mzee Kingunge liko nje ya mada.

Hata pale Kingunge alipo wadharau na kusema serikali ina mengi ya kufanya na kwamba haitawafuatilia wapinzani mikoani kujieleza kwa wananchi, tayari serikali hiyo hiyo ya kina mzee Kingunge imesalimu amri na imeteua timu yake ya viongozi kwenda kuzima moto wa wapinzani.

Kwani Mawaziri, Manaibu Waziri na Bendi ya TOT-Plus, Katibu Mkuu wa CMM Yusuf Makamba na makada wengine , wamepangwa mikoani wakijaribu bila mafanikio makubwa kujikosha mbele ya wananchi na kujaribu kukanusha hoja za wapinzani.

Kinachojidhiirisha ni jinsi serikali inavyojikang’anya katika suala hili. Haionekani serikali ina majibu yanayoeleweka kukanusha hoja za wapinzani. Hivyo kila kigogo aliyeguswa na tuhuma hizo anakurupuka na kutoa maelezo yake yanayopingana na vigogo wenzake kana kwamba serikali haina msemaji mmoja wa kueleweka.

Chakuchekesha zaidi ni pale baadhi ya watuhumiwa wa ufisadi walipotishia bila mafanikio makubwa kumshitaki Dk. Slaa, gazeti la Mwanahalisi na Mbunge wa Kigoma Kaskazini Kabwe Zitto.

Kitendo cha kutotimiza vitisho vyao kinaonyesha uwoga walionao wa siri nyingi zinazowahusu kufichuliwa mahakamani.

Tunawapa ushauri waheshimiwa watuhumiwa wa ufisadi kwamba wakubali kujiuzulu badala ya kungoja wananchi kufumuka kwa maandamano yanayoweza kusababisha ghasia na wao wenyewe kucharazwa bakora na umma wenye 'hasira takatifu'.

Ieleweke wazi kwamba japo Watanzania wanasemekana kuwa ni binadamu ambao nyonga yao ya hasira iliondolewa na wakunga walipozaliwa, itafika siku vifuko vyao ya nyonga vitajaa nyongo ya hasira takatifu na watakapoanza maandamano itakuwa ni vigumu kuwadhibiti.

Tunaamini bado nchi yetu ina viongozi angalau wachache wenye busara ya kutambua ukweli, hivyo kuwashauri watuhumiwa wa ufisadi kung’oka madarakani.

0755 312859;katabazihappy@yahoo.com;www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Alhamisi ya Oktoba 4,mwaka 2007

BILA KAZI YA ZIADA,HADHI YA MAHAKAMA YA TANZANIA INAKWISHA!

Na Happiness Katabazi

JULAI mwaka huu Rais Jakaya Kikwete alimteua Jaji Augustine Ramadhani(62) kuwa Jaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa Jaji Mkuu, Barnabas Samatta, aliyestaafu kwa mujibu wa sheria.

Na ni kwa mabadiliko ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.Mahakama iliongezewa nguvu na kubadilishwa jina kutoka kuwa Idara tu ndani ya Wizara ya Katiba na Sheria na kuwa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Mabadiliko haya yalikuwa na maana kwamba sasa mahakama inatambilika rasmi kama muhimili wa dola. Muhimili ambao kwa muda mrefu ulikuwa umegandamizwa na serikali(executive) kwani mahakama ilikuwa inapangiwa kila kitu ikiwemo bajeti yake.

Pamoja na dhana ya uhuru wa mahakama lakini bado katika mazingira ya utendaji wake isingeweza kujidadavua na kufanya mambo yake kama inavyotaka.

Kwa hali ilivyo sasa mahakama yetu ya Tanzania ina kazi kubwa sana ya kufanya. Zipo changamoto nyingi ambazo inabidi izitatue ili kufikia uhuru wa kweli wa mahakama na utaoaji wa haki kwa haraka na pasipo malalamiko.

Ni miaka 28 sasa tangu Mahakama ya Rufani ilipoanzishwa lakini hadi sasa bado hakuna mabadiliko makubwa. Mh.Jaji Mkuu; mahakama nyingi za mwanzo huko vijijini zinatisha ukiyaangalia majengo yake, ukiachilia mbali samani zilizomo humo ndani.

Hakuna sehemu za kuweka mafaili, vitendea kazi hakuna,nyumba za mahakimu n.k. ambapo hakimu anatembea umbali mrefu kufika kazini na mara nyingine hakimu anapoendelea na kesi kunyeshewa na mvua au upepo.

Hali hii imetokea pia huko Biharamulo ambako pia wakati mwingine mahakama hufanyika kwenye wodi la zamani la hospitali ya Biharamulo. Haya yote yanafanya mahakama zetu zikose uhuru wake na ukiachia hayo mahakimu wengi kutoripoti vituo vya kazi walivyopangiwa au kuhama hasa kipindi hiki ambacho mahakimu wengi wanaoenda huko ni wale wenye Stashahada.

Ifike wakati sasa mahakama hizi za mwanzo ziangaliwe na kwa kuwa pesa za serikali kuu hazitoshi basi nashauri iendeshwe harambee na Mahakama Kuu kuwahamasisha wananchi kujenga mahakama kama inavyokuwa kwa vituo vya polisi ili wajijengee mahakama zao wenyewe.

Aidha, katika mahakama zetu za chini kuna ukosefu mkubwa wa samani,vitendea kazi kama vile karatasi,n.k na upungufu wa majengo ambao unafanya mahakimu na wengine kukosa mahali pa kukaa, mifumo ya maji taka ni mibovu, vyoo vinatia kinyaa.

Ukienda mathalani pale Kisutu utakuta mahakimu wawili wanakaa chumba kimoja, hakimu mwingine hata kiti anachokalia utamwonea huruma aidha hata chumba cha kukaa mawakili nacho hakitoshi, hali inayofanya utendaji kazi kuwa mgumu sana.

Katika mahakama nyingine kama huko Kigoma Hakimu Mfawidhi anawajibika kutembea umbali mrefu na saa nyingine kupanda treni wakati anapokwenda kukagua mahakama za mwanzo. Mambo haya yote yanaathiri sana uhuru wa mahakama.

Kutokana na kukosekana mazingira mazuri ya kufanyia kazi unakuta mahakimu wengi wanaamua kutokwenda wanakopangiwa kazi au kuwa wavivu au saa nyingine kupewa lifti na wadaiwa katika kesi, au kufadhiliwa mahitaji muhimu kitu ambacho kinaathiri utoaji haki.

Unategemea nini hakimu ambaye anatoka Bunju na kuja kuendesha mahakama ya Kisutu huku akitumia usafiri wa daladala?

Humo humo kwenye daladala wamepanda watuhumiwa au wadaiwa ambapo saa nyingine anajikuta amelipiwa nauli au mwenye nyumba wake. Naam! yaweza kuwa ni ukarimu lakini kwa nini uwe kwa hakimu?

Je unategemea mwenye nyumba huyu au mtu aliyemlipia nauli ya daladala hakimu mara atakapopatwa na kosa kuhukumiwa kwa haki?

Hali hii ndivyo ilivyo hata kwa makarani wetu ambao mishahara yao ni midogo, wakati kazi wanayofanya ni kubwa sana. Kila kukicha wanacheza na mafaili ambayo pamoja na vumbi wanalolipata hawapati hata ‘allowance’ ya maziwa.

Hali hiyo inapelekea kuanza kuwaomba wateja pesa, mara nyingine kwa nia njema tu si kwa lengo la rushwa. Mara nyingi hata rushwa zinazolalamikiwa mahakamani si za mahakimu kama mahakimu ni bali nyingi zinapokelewa na makarani kwa kisingizio kwamba mahakimu wanataka chochote ili wateja washinde kesi zao.

Mara nyingine makarani wamekuwa wakituhumiwa kwa makusudi kuwa wanaficha majalada ya wateja ili tu kulazimisha rushwa kwani mteja akisumbuka sana mwisho huamua kutoa chochote.
Mara nyingi rushwa hizi ni za kati ya Sh. mia tano, elfu moja, elfu mbili hadi elfu tano.Inasikitisha sana kuona kwamba hukumu imetolewa lakini inachukua miezi mitano hadi sita kupata hukumu yake, na bado hukumu ikishachapwa kule kukabidhiwa tu na karani utasugua viatu weeeee mpaka uchoke.

Baadhi ya Makarani hata imefikia wanathubutu kuwaacha wateja na kwenda kunywa chai au kupiga soga tu na ndugu zao kwa zaidi ya masaa mawili huku wananchi wakisota tu kwenye korido za mahakama.

Kisingizio kompyuta mbovu mara mafaili mengi n.k.Yupo rafiki yangu mmoja ambaye alifungua kesi yake katika mahakama ya Kisutu hapa Dar-es-salaam, ilichukua zaidi ya mwezi kupata tu wito wa mahakama(summons) kila siku anaambiwa njoo mchana mara njoo asubuhi.Cha ajabu kesi hii ilikuwa kwa Hakimu Mkuu Mkazi Mfawidhi kabisa,lakini utendaji wa makarani wake ukaongoza kuwa mbovu. Watumishi wa mahakama hawajali kabisa.

Wengine wamefikia hatua kuomba rushwa mchana kweupe pee hata kwa kulazimisha kana kwamba ni halali. Tatizo kubwa linalotokea hapa ni kwamba hakuna hata mfumo mzuri wa kupeleka malalamiko katika mahakama zetu.

Ukiachilia malalamiko ya rushwa hakuna mfumo mzuri wa kiutendaji wa kupeleka malamiko yanayohusu utendaji wa watumishi wa mahakama,na hata kama upo basi au haujulikani au walio na wajibu hawataki kufanya wajibu wao, kwani utakuta baadhi ya wakuu wa makarani wenyewe ndiyo wanaongoza kwa kupokea rushwa au kulalamikiwa kwa utendaji mbovu.

Ukichunguza sana utakuta kama vile makarani hawawajibiki kwa mahakimu na hivyo wanakuwa hawawaheshimu. Kwa ufupi makarani wanaharibu sifa ya mahakama kuliko mahakimu wenyewe hasa wanapokuwa na ujuzi kidogo wa sheria basi hapo hujifanya mahakimu au majaji wenyewe.Ukimkuta karani mzuri basi ni yule aliye chini ya hakimu aliyemakini na mkali sana,vinginevyo karani atakuchezea anavyoweza.

Unakuta hadi saa nyingine wanashindana na wanasheria kwa kukosoa hati zao mbalimbali wanazoziwasilisha mahakamani kana kwamba wao ndio wataalamu wa sheria.

Kundi jingine linaliochangia kuipaka matope na kuharibu uhuru wa mahakama ni Waendesha Mashitaka (PP)ambao ni watumishi wa Jeshi la Polisi chini ya IGP-Said Mwema, lakini wanafanya kazi za ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka nchini inayoongozwa na Eliezer Feleshi,chini ya utaratibu wan chi uliopo.

Yaani baadhi ya Waendesha Mashitaka Mahakamani wanaongoza katika kuomba na kuporushwa mahakamani toka kwa ndugu na jamaa wa washtakiwa.

Hali hii hujitokeza sana pale ambapo Hakimu ametoa dhamana tena ya wazi na bure kabisa lakini mara akiachiwa tu anapokwenda kusaini na kukamilisha taratibu nyingine za polisi kama kutaka waandikiwe amri ya kutolewa gerezani, baadhi ya Waendesha Mashtaka(PP) na ndiyo huchukua nafasi yao wakishirikiana na karani husika kuwazungushazungusha na kuweka urasimu kibao na hata mara nyingine kuwatishia ndugu kwamba karandinga linakuja ili tu ndugu watoe chochote.

Pia Baadhi ya Waendesha Mashitaka wamekuwa wakituhumiwa kuaribu ushaidi katika kesi mbalimbali pindi wanapopewa rushwa na washitakwa, nasijawai kusikia wakikanusha hili, hakika ili ni tatizo na viongozi wao hawana budi kulikemea hili ili lisiendelee kuichafua mahakama zetu.

Mahakama zetu zinahitaji mabadiliko makubwa ili kukabiliana na changamoto hizi.

Ofisi za Mahakimu Wafawidhi zinapaswa kuwa wazi ili kukaribisha malalamiko ya watu na kupewa uwezo wa kudhibiti makarani wasio waaminifu katika kazi zao.

Na siyo ofisi za mahakama za Wafawidhi tu bali kuanzia ngazi zote za mahakama ziwe wazi kupokea malalamiko pia mahakama zote zitengeneze masanduku ya maoni ambayo yatawezesha raia kutumbukiza maoni na malalamiko kuhusu watumishi mbalimbali wa mahakama.

Na kuwe na tume au kamati ya utumishi wa mahakama ambayo itachukua maoni hayo na kuyafanyiakazi kama alivyokuwa kuwa akifanya Jaji wa Mahakama ya Rufaa Jaji Laurian Kalegeya, alipokuwa Jaji wa Mahakama Kuu na Mfawidhi wa Mahakama za Dar es Salaam.

Jaji Kalegeya enzi akiwa Jaji Mfawidhi alisaidia sana kuleta nidhamu mahakamani kwa kuzitembelea mahakama mara kwa mara hasa za mwanzo,kuongea na watumishi na kupokea malalamiko ya wananchi dhidi ya watumishi wake wasiyowaaminifu na kuwashughulikia kikamilifu,na ili ninaushaidi nalo.

Kazi ya kudhibiti rushwa ni kweli wanaweza kuachiwa (TAKUKURU) lakini hata masuala ya kiutendaji nayo mathalani uzembe wa makarani kupoteza mafaili tunahitaji kuwaachia TAKUKURU? La hasha huu ni wajibu wa mahakama moja kwa moja na haukwepeki.

Mahakama zetu zinapaswa kuwa na kompyuta za kutosha, printa, magari au walau hata pikipiki kwa mahakimu na vitendea kazi vingine ili kazi ziweze kufanyika kwa urahisi. Aidha ilipaswa kila hakimu wa mahakama ya wilaya kuwa na kompyuta kwajili ya kurahisisha ufanisi wake wa kazi mathalani uchapaji wa maamuzi madogo madogo ya mahakama kama vile ruling na order mbalimbali.

Aidha ni jambo la aibu sana hadi sasa kwa mahakama kutokuwa na tovuti(website) ambayo maamuzi na hukumu mbalimbali za mahakama zingekuwa zinapatikana.

Nasema ni jambo la aibu kwa sababu mahakama nyingi duniani tayari zina mitandao na tovuti na idara nyingi za serikali yakiwamo mashirika na taasisi binafsi yana tovuti kwaajili ya kutolea na kupokelea taarifa mbalimbali.

Leo hii hakimu au jaji anataka asome hukumu labda ya kesi ya Takrima, mgombea binafsi nk. ina mlazimu atafute ‘Law report’ au aingie gharama ya kuja Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,ndiyo apate nakala hizo za hukumu.Mahakama ingekuwa imefungua tofuti yake hakimu au jaji huyo asingelazimika kufunga safari kuja hapa hapa na badala yake kule mkoani alipo angefungua tovuti ya Mahakama ya Tanzania na angeweza kupata na kuisoma vema hukumu hizo na nyingine nyingi.

Je, nini kinashindikana kwa mahakama zetu, je,ni kukosekana kwa vipaumbele au kutojua?

Kuwepo kwa mtandao wa kompyuta, tovuti(website) kungesaidia mambo mengi sana kwani mahakama zilizoko wilayani na mikoani zingeweza kupata mawasiliano moja kwa moja na Mahakama Kuu.Mahakimu wangeweza kupata rejea za kesi mbali mbali ambazo hazijaripotiwa kupitia katika mtandao huu.

Aidha kusingekuwa na haja ya kusubiri muda mrefu uamuzi utoke kwani ukishasomwa tu unawekwa kwenye mtandao,mtumiaji anaufungua na kuutumia.
Vilevile Jaji wa chumba kimoja angeweza kujua jaji mwenzie ameamua nini na hivyo kuepusha mlundikano wa maamuzi mengi yanayotofautiana kuhusu jambo moja.

Baadhi ya ufisadi nilioutaja katika makala hii si wa kubuni wala kutunga.Upo na unatokea kila siku mashaidi ni wananchi wanao hudumiwa na mahakama hizo ,mimi mwenyewe ni Mwandishi wa Habari wa gazeti hili kwa miaka zaidi ya mitano sasa nimekuwa nikiandika habari za mahakamani toka mahakama za Mwanzo hadi mahakama ya Rufaa hivi sasa nimeshuudia baadhi ya ufisadi huo na hasa umekithiri katika mahakama za chini ukiachilia mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa.

Naweza kusema kwamba kupungua kwa matatizo niliyokwisha yataja hapo juu kunatokana kwa namna moja na udhibiti na usimamizi wa karibu uliopo kutoka kwa Majaji,Wasajili wa mahakama na uchache wa mashauri yanayofika Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu.

Kwa aina nyingine uwepo wa vitendea kazi vya kisasa japo havikidhi maitaji, umechangia sana kuleta ufanisi katika mahakama hizo mbili .Hivyo niimani yangu kwamba iwapo maslahi ya watumishi wa mahakama yataboreshwa kama ya wenzao wa mahakama Kuu na Rufaa,vifaa vikaongezwa,mazingira ya utendaji kazi yakaboreshwa na usimamizi mzuri ukawepo basi hata mahakama za chini zitakuwa na ufanisi mzuri ukilinganisha na sasa.

Binafsi nina imani na Jaji Mkuu Agustine Ramadhani ambaye pia ni Brigedia Mstaafu wa Jeshi la Wananchi(JWTZ) ambaye kabla ya kuapishwa nilifanya naye mahojiano maalum ofisini kwake kuhusu historia ya maisha yake na amejipanga vipi kuongoza Mahakama ya Tanzania, ambapo aliniambia kwamba kwake ni mapema mno kutamka kuwa amepanga kufanya jambo gani na kuomba Watanzania wampe muda aingie kwenye ofisi mpya ya (Ujaji Mkuu),aangalie ofisi hiyo ina miba gani, na akae na wenzake wajadiliane mambo mbalimbali kisha anaweza kutamka kwamba amejipanga kufanya mambo gani.

Jaji Mkuu umeishaingia ofisi mpya na kiti umeishakikalia na sasa umeishaanza kukizoea na hata ile miba uliyosema nafikiri umeishaanza kuiona.

Sisi kama wananchi tuna wajibu wa kukusaidia kwa kukuonesha wapi uozo ulipo, na wapi panatukera na kutuchefua ili wewe na timu yako mjue pa kuanzia. Ombi letu kwako ni hili mahakama ifungue Tovuti yake,itandaze masanduku ya maoni katika kila makahakama na watumishi wasiyowaaminifu washughulikiwe mara moja bila kuoneana haya.

Hizo ni changamoto zinazokabili mahakama zetu na Jaji Mkuu Ramadhan unapaswa kuzifanyiakazi ili hadi ya mahakama iweze kuwepo kama ilivyoelezwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.Bila kazi ya ziada,hadhi ya mahakama ya Tanzania inakwisha.

Mungu Afrika,Mungu inusuru Tanzania

0755 312859; Email:katabazihappy@yahoo.com,website:www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Jumapili Septemba 30, mwaka 2007

LOWASSA AMENICHANGANYA


Na Happiness Katabazi

BABA wa Taifa Mwalimu Julias Kambarage Nyerere aliwai kusema ili nchi iendelee yahitaji mambo manne, nayo ni watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora.

Wahaya na sisi Wanyambo tuna msemo: “Omukama ainduka anketo tainduka alulimi.” Kwa Kiswahili: “Mfalme hujigeuza kitini, si katika ulimi (kauli).”

Kwa kawaida kiongozi anatakiwa kuwa na kauli thabiti na msimamo katika ayasemayo.
Uchumi unapaa ni kauli iliyotolewa na Waziri Mkuu Edward Lowassa aliyoitoa kabla na wakati wa kufunga kikao cha Bunge la bajeti, la mwaka wa fedha 2007/2008, mjini Dodoma.

Waziri Mkuu Lowassa, akisoma hotuba yake ya kufunga kikao cha Bunge, alilalamika kuwa kuna baadhi ya waandishi wa habari, wachora katuni na wanaharakati wamekuwa wakipinga hilo.

Alisisitiza tena kuwa uchumi unapaa, kutoa vigezo na kuwataka wanaopinga hoja hiyo pia kuleta vigezo vya kupingana na hali hiyo.

Lakini mwishoni mwa wiki akiwa kwenye ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza, akijibu swali la wananchi wa Sengerema waliotaka kujua ni kwanini mfumko wa bei umeshika kasi katika kipindi kifupi tangu Rais Benjamin Mkapa aondoke madarakani.

Pia walitaka kujua ni lini ahadi ya maisha bora kwa kila Mtanzania itatimizwa.
Lowassa akijibu swali hilo alisema mfumuko wa bei unaoendelea hivi sasa umesababishwa na uchumi wa nchi kutokuwa mzuri. Na kuhusu ahadi ya maisha bora itatimizwa lini, aliwajibu kuwa maisha bora hayaji kwa wananchi wake kutofanya kazi kikamilifu katika sehemu zao za kazi.

Hapa waziri mkuu amenichanganya, kwani ni yeye aliyeuambia umma kupitia Bunge kuwa uchumi wa nchi unapaa kwa kasi ya ndege, lakini mwishoni mwa wiki iliyopita anawaambia wananchi wa Sengerema walipodai awaonjeshe huo uchumi unao paa, anasema vinginevyo.

Hivi waziri mkuu tukuelewe vipi? Ni mtu yuleyule uliyezungumza bungeni ndiye uliyezungumza Sengerema mwishoni mwa wiki?

Tuambizane ukweli kwamba wataalamu wako walilidanganya taifa kwa kukupa taarifa zisizo sahihi na hali halisi ya uchumi.

Kumbuka wakati wa kampeni jinsi CCM walivyoliimbia taifa ngonjera ambazo kiutekelezaji ni sawa na ndoto za Abunuasi. kwani hazitekelezeki.

Kwa jinsi hali ya mambo inavyokwenda, unaweza kuona kabisa uwezekano wa serikali kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania.

Mfano, nia njema ya kujenga shule lazima iendane na taaluma ya elimu katika kujenga shule. Shule ni walimu wanafunzi, majengo, madawati, mahabara, vitabu n.k.
Sasa kila kimoja kwa nafasi yake. Tukijenga darasa, tukaweka wanafunzi ndani bila kupata walimu, tukae tukijua tunajenga genge la wahuni.

Na hizo ndizo shule zako Lowassa tunazoambiwa kwamba hazina walimu wa kutosha, hao ni wale walimu wako wa wiki nne. Tuambizane ukweli la sivyo taifa hili tutalipeleka pabaya.

Hao Watanzania wenzetu wanaojazwa upumbavu katika shule za kata bila walimu, watalipeleka taifa hili kuzimu.

Shule bila vitabu, madaftari, karamu, chaki, na vifaa vya maabara, si shule, hawa wanafunzi ni kiwango gani cha elimu ambacho wanapata?

Twende kwenye vyuo vikuu, serikali ina vyuo vikuu vinne, Mzumbe, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Sokoine na Chuo Kikuu Uhuria. Hivyo vyuo vikuu kwanza ni vidogo na serikali haifanyi juhudi ya kupanua ili viweze kupokea wanafunzi wengi.

Uwezo wa vyuo vikuu hivyo kuvipanua ni mkubwa na unahitaji ongezeko la walimu, mishahara waboreshewe, inahitaji vifaa vya elimu ya juu, kompyuta na maabara za kisayansi.

Badala ya kulifanya hili, serikali inakurupuka na kuanzisha chuo kikuu kipya cha Dodoma. Ili kuanzisha Chuo Kikuu cha Dodoma, serikali imelazimika kuchukua baadhi ya wahadhiri kutoka kwenye vyuo vikuu hivyo vine, ingawa vyuo vyenyewe havina walimu wa kutosha.

Je, hayo maendeleo yako wapi kama una bomoa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Sokoine, Mzumbe na Chuo Kikuu Huria ili ujenge Chuo Kikuu cha Dodoma maana yake nini? Au tunataka utitiri wa vyuo vikuu usio na viwango?

Twende kwenye sekta ya afya, huko vijijini tunaowajua ni waganga wa kienyeji na wakunga wa jadi, si madaktari ambao serikali inawasomesha kwenye vyuo vikuu na ndio wanaozalisha kina mama huko vijijini.

Badala hata ya kuwasaidia wakatoe huduma bora zaidi, mnakimbilia kujenga majengo ya zahanati bila kuweka wataalamu wa kutosha na dawa.

Wenzetu wa Kenya wanatengeneza dawa za mitishamba, tena wakati mwingine miti hiyo wanaivuna hapa kwetu na kwenda kutengeneza dawa hizo nchini mwao na kisha wanakuja kutuuzia hapa, na katika hili tukae tukijua tunapoteza na kukosa teknolojia.

Miti tunayo, waganga wa jadi na wakunga tunao, kitengo cha miti shamba kipo lakini akipewi fedha za kutosha badala yake fedha za walipa kodi zinanunulia mashangingi na kuishia kwenye ziara za viongozi.

Viongozi wakipata ajali wanapelekwa kutibiwa Afika Kusini, kwa matibabu ambayo waganga wetu wa hapa kupitia kitengo hicho cha tiba asilia kitengo cha MOI, kinaweza kutoa matibabu hayo.

Mheshimiwa Lowassa, wewe unawaambia wananchi wa Sengerema kwamba serikali ina mikakati ya kuboresha maisha yao, mikakati hiyo ni ipi tusiyoijua?
Au unataka kuzungumzia MKUKUTA, MKURABITA na mabilioni ya Kikwete? Kweli hiyo mikakati itatutoa kwenye umaskini?

MKURABITA ni mkakati wa walionacho na wanarasimisha mali walizonazo, kwa maana kama hauna mali, MKURABITA haukufikii.

MKUKUTA ni mpango wa kupunguza makali ya umaskini lakini umaskini una baki pale pale, hautuhakikishii kama tutaondoka kwenye umaskini kwa mikopo ya sh 50,000 au sh 100,000. Serikali itaondoaje umaskini kwa mikopo hiyo midogo?

Mabilioni ya Rais Kikwete hayawezi kutokomeza umaskini kwa sababu mikopo hii inatolewa kwa masharti na maskini hawezi kutekeleza masharti hayo, na si kila anayeomba anapata kutokana na masharti ya kibenki.Hata fedha hizo zingetolewa bila masharti, pia hazitoshi.

Kwa hiyo sisi tunachokusii Lowassa, usijalibu kupotosha wananchi kwasababu tayari wameishagundua siri ya sifuri.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima,Jumatano Septemba 26 mwaka 2007