ANDREW CHENGE ACHA WANAHABARI

Na Happiness Katabazi

MARA zote mama yangu mzazi Oliva Ndimugeita, amekuwa akiwaambia ndugu, jamaa na sisi watoto wake kwamba tukimuona au kumsikia binadamu awaye yeyote anadai heshima kwa nguvu, tujue binadamu huyo ana matatizo.

Jumamosi iliyopita nyakati za asubuhi baada ya kumaliza kusoma habari kubwa kwenye moja ya gazeti la kila siku (si Tanzania Daima) iliyokuwa na kichwa cha habari kisemacho “Chenge ageuka Mbogo’, niliamini maneno ya mama yangu kuwa yamejaa ukweli na hekima.

Ndani ya habari hiyo Andrew Chenge, amenukuliwa aking’aka kwamba wandishi wa habari siku hizi hawamheshimu, lakini ipo siku atawafunza adabu.

Kwa mujibu wa habari ile, Chenge alionekana mwenye hasira, alipotoa kauli hiyo baada ya kuulizwa juu ya maoni yaliyotolewa na wananchi, asasi za kijamii na wanasiasa kwamba hakustahili kuwepo katika timu ya kurekebisha kasoro kadhaa kwenye mradi wa Jengo la UVCCM.

Maoni hayo yanatokana na ukweli kwamba, Chenge anakabiliwa na tuhuma za ufisadi ambazo hadi sasa zinachunguzwa na Taasisi ya Makosa Makubwa ya Jinai(SFO) ya Uingereza.

“Kwa nini waandishi wa habari hamniheshimu? Naomba tafadhali mniheshimu. Siku hizi hamniheshimu kabisa, lakini kuna siku nitawafunza adabu,” alisema.

Kwanza nataka ieleweke wazi kwamba matamshi haya ya Chenge, kusema ipo siku atawafunza adabu waandishi wa habari ni matusi na vitisho, anapaswa atuombe radhi. Pia ni kauli ya kitisho ili wanahabari wasiwe na ujasiri, waingiwe woga wasiandike maovu yake.

Chenge anaposema atawafunza adabu waandishi wa habari ni dhahiri shairi kwamba waandishi wa habari wa kada zote hawana adabu!.

Leo hii Watanzania wa makundi mbalimbali wanapolalamikia serikali imeingia mikataba ya kihuni na mibovu ambayo inawanufaisha wawekezaji wa kigeni kuliko raia wa nchi hii, ni lazima tumtaje Chenge, Baraza la Mawaziri wa Serikali ya awamu ya tatu na rais Benjamin Mkapa.

Tunamtaja na tutaendelea kumtaja kwa sababu Chenge ndiye alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kipindi chote cha awamu ya tatu hivyo alikuwa mshauri mkuu wa masuala ya sheria kwa serikali.

Mikataba yote ya ‘kihuni’ ambayo leo hii inaigharimu serikali na wananchi wake imesababishwa na viongozi wenzake na yeye akiwemo.

Katika hili, hana ujanja kwani yeye ni mwanasheria kitaaluma alipaswa kuifahamu kwa undani mikataba hiyo kuwa ni mibovu kabla haijaingiwa na serikali.

Chenge lazima atambue kuwa tutaendelea kumwandika, wananchi wanateseka na gharama za maisha kwa sababu ya fedha za walipa kodi ambazo serikali ilikuwa ikizilipa kwa kampuni ya IPTL. Fedha hizo zingewekwa kwenye sekta ya afya bila shaka wananchi tungepata huduma bora katika hospitali zetu.

Lakini, Chenge na wataalam wengine wa serikali aidha kwa kukosa uzalendo katika taifa lenu au kwa uzembe mkaliingiza taifa kwenye mikataba ya kinyonyaji yenye harufu ya rushwa kama IPTL, Netgroup Solution na mingine ambayo inawanufaisha wawekezaji wa kigeni.

Najiuliza ni kwa nini Chenge hana huruma na waandishi wa habari hadi atake tena kuwafunza adabu kwani wanahabari ni wananchi ambao nao wanasulubika katika mikataba hiyo ambayo nalazimika kusema mbunge huyu mbaye aliwahi kuwa Waziri katika serikali ya awamu ya nne na wenzake walishawashikisha adabu wananchi kwa kuiliingiza taifa kwenye mikataba hiyo.

Wakati umefika sasa wanahabari tumhoji Chenge ni adabu ipi nyingine anataka kutufunza? Kwa mtazamo wangu kauli ya yake inamrudi kwa sababu alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali lakini alishindwa kuishauri vema isiingie mikataba dhalimu.

Hivyo Chenge ambaye pia ni Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), aelewe wazi wanahabari hawana chuki nae anaandikwa kwa mazuri na mabaya yake na siku zote za maisha atambue kwamba tunapolalamikia mikataba mibovu, lazima tuihusishe serikali ya awamu aliyokuwa Mwanasheria wake Mkuu.

Wananchi wa kada mbalimbali waliojitokeza kupinga uteuzi wake wa kuwa mjumbe wa timu ya kurekebisha kasoro kadhaa za jengo la UVCCM, wanayo haki ya kuhoji uteuzi wake kwa sababu alishindwa kuona ubovu wa mikataba ya IPTL, Netgroup Solution, Rada na mingine.

Leo, baada ya kujitoka kwenye uwaziri kutokana na kashfa ya ufisadi wa ununuzi wa rada ndiyo anaweza kuona kasoro katika mkataba wa mradi wa jengo la UVCCM?

Hivyo kutokana na mlolongo wa tuhuma nilizoziorodhesha zinamhusisha Chenge, ndizo zinazosababisha adai heshima kwa nguvu na hapo ndipo maneno ya mama yangu mzazi yanapotimilika kwamba ‘binadamu yeyote anayedai heshima kwa nguvu ana matatizo’.

Hivyo naomba uwe mstahimilivu na ungetaka mabaya yako yasiandikwe basi tangu mwanzo katika utendaji wa kulitumikia taifa hili, usingejiingiza kwenye kashfa ambazo leo tuhuma hizo zinakutafuna kila kukicha.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika

0755312859
katabazihappy@yahoo.com:www.katabazihappy.blogspot.com

CHANZO.Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Septemba 17, 2008

KUMPINGA RAIS HADHARANI,LIPO TATIZO

Na Happiness Katabazi

AWALI ya yote, natoa salamu za shukrani kwa wasomaji wangu wapendwa, kwa sababu tulipoteana kwa takriban miezi mitatu. Nilikuwa kwenye likizo ya uzazi.

Aidha, namshukuru Mwenyezi Mungu, amenijalia uhai, afya njema pamoja na mtoto wangu Queen Mwaijande, aliyezaliwa Juni 8, mwaka huu katika Hospitali ya Jeshi la Wananchi (JWTZ) Lugalo, Dar es Salaam.

Nawashukuru pia wote waliokuwa karibu yangu kwa kipindi hicho, wakiwamo madaktari na manesi wa hospitali hiyo, kwa huduma nzuri na waliokuwa nami kimwili na kiroho.

Nikiachana na hayo, katika mtazamo wangu leo nitazungumza kuhusu tabia iliyoibuka kwa kasi hivi karibuni ya baadhi ya Watanzania kudiriki kumpinga Rais Jakaya Kikwete hadharani.

Kimsingi, licha ya kuwa ni haki ya kikatiba kutoa maoni kuhusu kile unachoamini au kukiona, lakini inapotokea mara kwa mara kuwa hivyo kwa kiongozi wa hadhi ya rais, hakika kuna jambo.
Hali hii inanisikitisha hasa nikiangalia maana halisi ya neno kiongozi. Kiongozi ni mtu wa kuonyesha njia, anapaswa kuwa mfano kwa walio nyuma yake.

Aidha, kiongozi ni dira na mwelekeo wa wale anaowaongoza, kiongozi ndiye aliyebeba matumaini ya anaowaongoza.

Hivyo basi, kitendo cha waongozwa kumkosoa kiongozi wao, tena kwa hoja, kwa kiongozi mwenye sifa za uongozi, anapaswa kujirudi na kurekebisha dosari. Ziwe zake au wasaidizi wake.

Kinyume cha hayo, matumaini na imani ya wanaoongozwa (wananchi), dhidi ya kiongozi wao (rais), yataanza kupotea taratibu kwa maana kwamba, licha ya hali ya mambo kwenda kombo, kiongozi wao haoni wala hasikii.

Nikija kwa rais wetu aliyeingia madarakani kwa kishindo, anapingwa mara kwa mara kimtizamo kutokana na hali ya mambo inavyokwenda katika utawala wake, inayochangiwa na yeye mwenyewe au wasaidizi wake.

Tatizo kubwa linaloonekana katika utawala wa Kikwete, ni kuangushwa na ‘uswahiba’ wa baadhi ya wasaidizi na wateule wake. Tabia hiyo inasababisha kila atakachosema kupingwa au kukosolewa wazi na wananchi wake.

Safu ya wasaidizi wa Rais Kikwete, baadhi yao hawajabobea kwenye nafasi hizo, hali inayosababisha rais kupingwa kwa hoja katika hotuba zake kadhaa anazozungumzia mambo mbalimbali kwa mustakabali wa taifa.

Kwa mtazamo wangu, hata kwenye nafasi mbalimbali ndani ya chama ambacho ni mwenyekiti wake, haonekani kupata mafanikio kutokana na uteuzi wa baadhi ya wanachama wenzake.

Na hii ndiyo maana baadhi ya ‘maswahiba’ wa rais wanasikika mitaani na kwenye vilabu vya pombe wakisema wanaowatuhumu kwa ufisadi, hawakuwafanyia mipango ya kuwateua.

Naamini, usingemteua Edward Lowassa kuwa waziri mkuu, aliyejiuzulu nafasi hiyo baada ya ofisi yake kukumbwa na kashfa ya kuiingiza serikali kwenye mkataba wa kampuni hewa ya Richmond, ungeweza kumpata msaidizi mwingine mzuri zaidi.

Rais asishangae wananchi wakimkosoa, ni kwa sababu wanayajua hayo, na si chuki, tunamtakia mema rais wetu na kamwe hatutavumilia kumkosoa, kumshauri na kumpongeza panapo stahili, tena bila kujali propaganda chafu za ‘maswahiba’ zake.

Ndiyo maana Rais Kikwete, aliwahi kusema wananchi wanampenda, timu yake inamuangusha. Hivi hiyo timu aliiteua nani?

Kauli ya wananchi kumpenda hivi sasa ni kumvika kilemba cha ukoka, kwa sababu kinachofanya wananchi wampende kiongozi wao ni matumaini aliyowapa. Yakipotea, watakuchukia tu.

Hivi sasa bidhaa hazikamatiki, iwe sokoni au madukani, bei zipo juu, na mbaya zaidi hivi sasa kila kukicha wanajiamulia kupanga bei za bidhaa watakavyo, kwa kuwa hakuna wa kuwadhiti, hali inayosababisha wananchi kuumizwa na bei hizo.

Rais Kikwete na CCM yake waliwaahidi wananchi kuwapatia maisha bora, lakini ghafla, amenukuliwa akisema, hali ya maisha ni ngumu na gharama zimepanda, hivyo kuwataka wananchi wavumilie hali hiyo.

Kabla ya kuwataka wavumilie hali hiyo, rais alipaswa kuwaeleze Watanzania ahadi ya maisha bora imetimia kwa kiwango gani au ameshindwaje, ili wananchi wajue pa kushika.

Ieleweke kwamba Kikwete ni rais wa Watanzania, si Afrika wala ulimwengu. Kimsingi Rais Kikwete si wa Warundi, Wazimbabwe, Wamarekani wala Shirika la Fedha Duniani (IMF).
Mkurugenzi wa IMF anaposema Kikwete anafanya vizuri ina maana ‘tumeuzwa’.

Mfano suala la Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA). Waliokuwa wanalifahamu ni baadhi ya wafanyabiashara wenye asili ya Kiasia, kwa sababu ndio waliokuwa wanakwenda kuzichota, kwa sababu walijua kwamba zipo.

Ulikuwa mlango kwa baadhi ya Waasia hapa mjini kununulia madeni. Tatizo si kuwepo kwa fedha za EPA ndani ya Benki Kuu. Bali ni ufisadi ulioibuka ndani ya CCM na serikali yake baada ya kuona hizo fedha zipo, wakazipigia mahesabu ya kisiasa.

Imeelezwa kwenye maeneo mbalimbali kwamba, CCM ilizitumia fedha za EPA inavyojua yenyewe. Hivyo kutokana na usiri na kauli mbalimbali za viongozi, suala hili ni pamoja ukweli huo.

Hivi karibuni Rais Kikwete alitumia saa tatu na ushei kuhutubia Bunge na kuwaficha wahusika wa EPA, ina nilazimisha binafsi kuamini kwamba rais alinufaika na fedha hizo ndiyo maana anazifumbia macho.

Sasa kwa kawaida serikali hupata fedha kwa njia nyingi za aina hiyo, ndiyo maana Baba wa Taifa Julius Nyerere, alipopata fedha za mfuko wa mali za adui (Enemy Property Fund) mwaka 1960 alizitumia kujengea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Ikumbukwe kwamba Nyerere aliweza kuzipeleka fedha hizo kwenye TANU zikaliwe, tusingejua lakini kwa uadilifu wake akazipeleka kwenye ujenzi.

Kwa hiyo ilikuwa ni wajibu wa serikali ya Tanzania kutumia fedha za EPA kuzilinda ili wananchi wa taifa hili wafaidike kwenye miradi kama ‘Schoolership’ ziwasaidie watoto maskini.

Kwa hiyo kuuziingiza kwenye bajeti ya kilimo ni ili ninaowaita mafisadi wazitafute tena ili zisiwafikie wakulima kama walivyozoea.

Binafsi, sikubali fedha hizo kwenda kwenye kilimo kwa sababu ilisemwa kwamba serikali haina sera thabiti ya kukuza kilimo kwa hiyo fedha za EPA haiwezi kukuza kilimo kama tulivyoambiwa.
Na tujiulize isingekuwepo fedha ya EPA ingekuwaje kwenye sekta ya kilimo? Mfano rais amesema fedha hizo zitatumika kwenye mfuko wa mbolea ina maana kilimo ni mbolea tu?
Sasa ametaka zitumike kwenye kilimo, basi kungekuwa na mpango kamili wa kuwapo vitu fulani, badala ya kusema zitumike kwenye mbolea.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Naomba kutoa hoja.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Septemba 10, 2008