QUEEN KISSA MWAIJANDE


Pichani mtoto wangu Queen Mwaijande, akifurahia jambo muda mfupi baada ya kubatizwa katika Kanisa la Kiintili la Kilutheri Tanzania Usharika wa Ubungo, Dar es Salaam, Desemba 26 mwaka 2008.Picha na Happiness Katabazi

MIAKA MITATU YA SERIKALI YA AWAMU YA NNE


RAIS KIKWETE AMESHINDWA KUTIMIZA NDOTO ZAKE
Na Happiness Katabazi
JUMAPILI iliyopita Rais Jakaya Kikwete ametimiza miaka mitatu tangu alivyoapishwa Desemba 21 mwaka 2005, kuwa rais wa awamu nne wa taifa letu.

Wakati rais Kikwete akiadhimisha miaka mitatu ya uongozi wake, pia mimi kesho Desemba 25 mwaka huu, naadhimisha siku yangu ya kuzaliwa ambapo nitakuwa natimiza miaka 30.Namshuruku mungu kwa kunipa uhai na afya njema.

Leo katika makala hii nitazungumzia mafanikio, mapungufu yaliyoonyeshwa na serikali ya awamu ya nne katika kipindi hiki cha miaka mitatu tangu alipoapishwa na Jaji Mkuu Mstaafu Barnabas Samatta ,tarehe hiyo ikiwa ni muda mfupi baada ya asilimia 80 ya Watanzania kumpa ridhaa ya kuwaongoza katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwaka 2005.

Katika makala yangu hii nitataja sababu tano ambazo nitazianisha hapa chini ambazo zitatusaidia sote kutathimini utendaji kazi wa rais na serikali yake.

Majukumu ya rais kama yalivyoanishwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.Moja ya kigezo cha kutathimini jinsi rais wetu anavyomudu majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hiyo.

Pili,kutathimini utendaji wa Kikwete jinsi hali ya nchi alivyoikuta wakati anakabidhiwa madaraka na hali ilivyo sasa baada ya miaka mitatu ya uongozi wake.

Tathimini yangu ya tatu; inaangalia yale ambayo Kikwete aliwahaidi Watanzania wakati anaomba kura endapo ameweza kuyatekeleza au ajayatekeleza bado au kashindwa kuyatekeleza.

Tathimini yangu ya nne;ninachoweza kutathimi akiwa yeye aliyechukua urais kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi(CCM), utekelezaji wa Ilani ya chama chake.

Tathimini yangu ya tano;ni kumtathimini rais kulingana na matukio mbalimbali yaliyotokea chini ya utawala wake na jinsi alivyoweza kuyashughulikia.

Nianze na tathimini yangu ya kwanza;Ibara ya 33 ya Katiba ya nchi inatamka majukumu ya rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ,kwa mujibu wa Sheria ya mwaka 1984 Namba 15 ibara ndogo ya (9).Ibara ya 33(2)inasema rais atakuwa Mkuu wa nchi,kiongozi wa serikali na Amir Jeshi Mkuu.

Kikwete akiwa Amir Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama ameweza kutekeleza mambo mbalimbali ikiwemo litakalo kumbukwa mno ni pale alipolituma jeshi lake la Ulinzi la Wananchi(JWTZ) kwenda kisiwa cha Anjoun-Komoro na lilifanikiwa kumng’oa muasi Kanali Mohamed Bacar.

Aidha Kikwete ameweza kusimika viongozi wa Majeshi yake, Mkuu wa (JWZT) Jenerali Davis Mwamunyange,Inspekta Jeneli wa Jeshi la Polisi(IGP)Said Mwema,Kamisnha Mkuu wa Jeshi la Magereza Agustino Nanyaro ambao utendaji wao una kwenda vizuri kwani nchi haijavamiwa na maadui, usalama wa mipaka yetu kwa kiasi kikubwa upo salama na hatujasikia wafungwa au mahabusu wamevunja magereza yetu na kutoroka.

Kwa upande wa Kiongozi wa Serikali; ukweli ni kwamba rais wetu kwa kipindi hiki cha miaka mitatu ameongoza serikali inayoteteleka.Ni serikali iliyokumbwa na kashfa nyingi kuliko wakati wowote katika historia ya nchi yetu.

Na mfano mzuri katika hili ni kashfa ya mkataba wa kufua umme ambao ulimlazimisha kujiudhuru nyadhifa zao aliyekuwa waziri Mkuu Edwar Lowassa,waziri wa Nishati na Madini,Nazir Karamagi, Waziri Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk.Ibrahim Msabaha.Wakati aliyekuwa waziri wa Miundombinu Endrew Chenge naye alijiudhuru baada ya kukumbukwa na kashfa ya mkataba mbovu wa ununuzi wa Rada ambaye hata hivyo ianelezwa kwamba anaendelea kuchunguzwa.

Aliyekuwa waziri wake wa Fedha Zakhia Meghji aliwahi kukaririwa akisema kwamba alidanganywa na wasaidizi wake kuhusu kampuni ya Kagoda Agricultural ambayo kampuni hii inatajwa kuwa ni kampuni ya kifisadi na ilichota sh bilioni 40 katika Benki Kuu. Lakini kabla ya Meghji kusema hayo aliwahi kukaliliwa akijinasibu kwamba Kampuni ya Kagoda ilichota fedha hizo kwaajili ya kununulia vifaa vya usalama wa majeshi yetu.

Kashfa ya wizi wa Fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje katika Jiko letu la Uchumi(Benki Kuu), kashfa ambalo ilimlazimu rais kuunda tume kuchunguza wizi huo na hatimaye tunaendelea kushuudia baadhi ya watuhumiwa wameanza kuburuzwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Huu ni udhibitisho kwamba serikali anayoingoza rais wetu huyu ina viongozi na watendaji wasiyo makini,ingawa si wote.Vile vile katika kipindi chake cha uongozi , kina kuwa ni kipindi cha kupata historia nyingine ya kuwa na Baraza kubwa la mawaziri licha mapema Februari mwaka huu, alilazimika kulipunguza.

Ni serikali hii ilifanya kituko cha aina yake cha mawaziri wake kujimegea fedha za walipa kodi na kuanza kuzunguka mikoani kuwaelezea wananchi uzuri wa bajeti.Uamuzi ambao ulipingwa vikali na wananchi hadi kufikia mawaziri hao kukatisha ziara hizo kwani walikuwa wakikutana na wakati mgumo sambamba na kuzomewa na wananchi.

Hivyo wakati tukiazimisha miaka mitatu ya uongozi wa Kikwete nilazima tumweleze bayana kwamba uamuzi huu mawaziri wake kulandalanda mikoani kuelezea uzuri wa bajeti haukuwa sahihi kwani ulilenga kufuja fedha za walipa kodi.

Tathimini ya hali ailivyoikuta na hali ilivyo hivi sasa kijamii, kiuchumi na kisiasa;ukweli ni kwamba hali ya maisha imekuwa ngumu kuliko ilivyokuwa miaka mitatu nyuma kwani gharama za maisha zimepanda bei ya mafuta,vyakula ni ghali.Nikipindi ambacho tumeshuhudia kupanda kwa kasi bei za mafuta,ada za watoto mashuleni, ongezeko la uhalifu hususani uhalifu wa mtandao.Hali inazidi kuwa mbaya wakati rais aliwaaidi wananchi maisha bora.

Aliyoaidi wakati anagombea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, aliaidi wananchi mambo lukuki na miongoni aliyoyahaidi ni kushughulikia mpasukuko wa kisiasa Zanzibar ili kurejesha imani lakini hadi Jumapili miaka mitatu imetimia,jitihada zake za kumaliza mpasuko hazijazaa matunda.

Ahadi nyingine aliyowahadi wananchi , ni kujenga Vvyuo Vikuu vingi ili wananchi wake wapate elimu,ukweli ni kwamba hadi leo ameweza kutekeleza kwa kiasi fulani ahadi hiyo kwa kuanzisha Chuo Kikuu cha Dodoma.Hata akiondoka leo madarakani tutamkumbuka kwa kuanzisha chuo hicho.

Pamoja na hayo sera ya mtangulizi wake Benjamin Mkapa, ya Ubinafsishaji katika sekta mbalimbali ambayo imewezesha kuanzishwa Vyuo Vikuu kadhaa nchini.Kwa hiyo ukweli idadi ya wananchi wanaoingia vyuo ikuu imeongezeka.

Hata hivyo ubora wa elimu utolewao katika vyuo hivyo unaelekea kushuka zaidi kwasababu wakati idadi ya wanafunzi kujiunga vyuoni humo inaongezeka , idadi ya wahadhiri,miundombinu na vifaa vingine vya kujifunzia havijaongezeka. Mathalani uanzishwaji wa Chuo Kikuu cha Dodoma umethiri baadhi ya vyuo vingine kwani baadhi ya wahadhiri wa chuo hicho wametolewa kwenye vyuo vikuu hivyo kuviacha vikiwa vimepwaya.

Kimsingi kuna kuwa hakuna mantiki ya kuanzisha utitiri wa vyuo wakati vyuo tulivyonavyo tumeshindwa kuviendesha na ubora wake unaporomoka.Mbaya zaidi ongezeko la vyuo hivi unatokea wakati ambapo kuna sera tata ya uchangiaji gharama wa elimu ya juu.

Sera ambayo inazidi kuathiri Elimu ya Juu na hadi naandika makala hii, vyuo zaidi ya vitano vimefungwa kutokana na wanafunzi kupinga sera hiyo ya uchangiaji mikopo.Bahati mbaya zaidi tatizo hili linagusa moja ya ahadi aliyoitoa Kikwete katika Ukumbi wa Dimond Jubilee mwaka jana, wakati akizungumza na wana vyuo, alisema hakuna mtoto wa maskini atakayefukuzwa chuo kwakukosa ada.Hii ni ahadi ya pili ya rais Kikwete ambayo ameshindwa kuitekeleza.

Katika kipindi hiki cha uongozi wake kumekuwa na chipuko mithili ya uyoga kwa shule za sekondari al maarufu “sekondari za Kata’.Hili ni ongezeko la kupigiwa mfano na pengine ukilitizama kwa juu juu ni la kujivunia lakini ukilitizama kinachoendelea ndani ya shule hizi ni aibu.

Badala ya kuwa na shule halisi,nyingi zina ripotiwa zimekuwa ni kambi ya za watoto wetu kwenda kukuza umri.Ni shule zilizoghubikwa na uhaba wa walimu na vifaa kiasi cha kutisha.Kwa ujumla kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wa rais wetu kimekuwa ni kipindi cha kuporomoka kwa ubora wa elimu.

Rais Kikwete aliahidi kuleta usawa wa kijinsia katika uongozi kwa kuongeza nafasi za wanawake katika uongozi,kwa kiasi fulani ameweza kutekeleza ahadi hii na mifano ya hili ipo wazi kwani ameweza kuteua wanawake zaidi kuwa majaji wa Mahakama Kuu na Rufaa,wanawake 12 amewateua kuingia kwenye Baraza la Mawaziri, idadi ya wakuu wawilaya na wakuu wa mikoa ,wajumbe wa bodi mbalimbali imeongezeka ukilinganisha na miaka ya nyuma na awamu zilizopita.

Ahadi yake nyingine ya kutoa ajira kwa vijana na maisha bora ,pamoja na jitihada alizozifanya hazijaweza kuzaa matunda yakutosha kwani hadi leo vijana wasiyo na ajira ni wengi na watanzania kwa ujumla hawawezi kuyaona maisha bora.

Kuhusu Ilani ya Chama chake, katika Ilani hiyo moja wapo ya mambo mazito ambayo CCM iliaidi yangeshughulikiwa na Kikwete, ni uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi;hadi hivi sasa ahadi hii imekuwa ni kaa la moto kwa rais wetu maana alijipatiwa ufumbuzi kama Ilani ya chama tawala ilivyotamka.

Na hadi hivi sasa ahadi hiyo inaedelea kuleta mtafaruku miongoni mwetu. Wakati baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu wanaendelea kudai kwa nguvu wanataka mahakama ya Kadhi sasa na siyo kesho, Wakristo kupitia kwa viongozi wao wa kidini,hawataielewa serikali endapo itaridhia uanzishwaji wa mahakama hiyo.

(Hata hivyo ni maaskofu hawa hawa wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka 2005 kupamba moto ,walibariki Ilani ya CCM na kusema Kikwete ni chaguo la mungu).

Hata hivyo nitakuwa sijatenda haki kama sitatoa pongezi kwamba katika utawala wake uhuru wa habari,uhuru wa wananchi kariba mbalimbali kutoa maoni yao bila kubughudhiwa unaendelea kukua kwa kasi ukilinganisha na tawala zilizopita.Tunamuomba mungu rais Kikwete aendelee kuwa na moyo huu wa kuwa mstahimilivu anapokosolewa.Licha kuna baadhi ya watendaji wake wachache ambao hawataki kubadilika wamekuwa wakijitahidi bila mafanikio kuzuia uhuru huo wa kutoa maoni.

Kuhusu tathimini yangu ya tano;kipindi cha uongozi wa Kikwete hali ya utulivu wa ndani umeteteleka na ishara ya kuteteleka kwake ni ongezeko la migomo watu wa kariba mbalimbali wakiwemo baadhi ya watumishi wa serikali,wanavyuo,madaktari , walimu kuiburuza mahakamani serikali na hata wanafunzi wa shule za msingi waliandamana kupinga ongezeko la nauli na mahabusu kugomea kula na kwenda mahakamani kusikiliza kesi zao.

Hii hali ya mitafaruku siyo ishara njema kwa taifa kwasababu inaweza kusababisha kujengeka kwa utamaduni mpya kwamba haki haipatikani hapa nchini hadi watu wagome.Huu ni udhaifu mwingine wa serikali hii kwamba watendaji wake hawapo tayari kutimiza wajibu wao mpaka washinikizwe kwa migomo na kubebewa mabango na kufungiwa maofisini.

Aidha kuhusu uhusiano wa Tanzania na mataifa mengine; pengine rais katika kipindi hiki ameweza kuongeza uhusiano mwema na mataifa kwa manufaa ya taifa letu ingawa utaratibu alioutumia una lalamikiwa na wengi kwamba ni rais aliyevunja rekodi ya marais waliopata kuliongoza taifa hili aliyedhuru nchi za nje kwa muda mfupi mno hadi akapachikwa jina la msafiri maarufu wa karne ya 15 “Vasco Da Gamma’.

Watanzania tungependa kuona rais wetu akitulia ofisini au nchini na kushughulikia matatizo yanayowahusu wananchi moja kwa moja.

Pengine tukio jingine kubwa la kijamii linaloendelea katika utawala wa rais Kikwete ni ongezeko la vitendo na imani za kishirikina hususani mauaji ya wenzetu wenye ulemavu wa ngozi Albino.

Mauaji haya yamedhibitika kuwa na uhusiano wa watu kadhaa wanaotaka mali na utajiri wa chapchap.Tathimini ya utendaji wa serikali yake pia inaweza kufanywa kwa kuangalia ni jinsi gani imelishughulikia jambo hili la kikatili.

Ni wazi kwamba jitihada zilizofanywa hadi sasa hazijaweza kuikomesha aibu hii ya nchi ambayo pia inakwenda sambamba na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu.

Laiti serikali ingekuwa na nguvu thabiti pengine ingeweza kuwaakikishia mara moja Albino wote nchini usalama wa maisha yao kwa kutengeza mpango wa dharula wa kuwalinda wenzetu hawa na siyo kuishia kulizungumzia suala hili majukwaani na kusubiri Albino wengine wauwawe ndipo Jeshi la Polisi lingilie kati.

Hivyo basi rais Kikwete hana budi kukaa pamoja na wasaidizi wake ili wayabaini mapungufu katika utendaji wao na kuyarekebisha mara moja kwa maslahi ya taifa letu.Akumbuke pia kwamba kadri utendaji wa serikali yake utakavyoendelea kutowaridhisha Watanzania ndivyo wananchi watakavyopoteza imani naye na pengine watafikia hatua yakunyima ridhaa ya kuwaongoza wananchi katika kipindi kijacho.

Tunampongeza rais wetu katika yale yote ambayo ameweza kuyatekeleza yenye alama za kuonekana na yasiyoonekana kwa Watanzania walio wengi ambao wapo nje ya mfumo wa utendaji wa serikali ya awamu ya nne.Mwisho nawatakieni wasomaji wote sikuu njema ya Christmas na Mwaka mpya.

Mungu ibariki Tanzania,Mungu ibariki Afrika

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano,Desemba 24 mwaka 2008




TUNASUBIRI MAAFA MAHAKAMANI

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, ina umaarufu wa pekee nchini. Ina sifa nzuri na mbaya ambazo mara kadhaa zimeripotiwa katika vyombo vya habari.
Baadhi ya hukumu zilizowahi kutolewa na mahakama hiyo dhidi ya viongozi wa taasisi mbalimbali au watu maarufu kwenye jamii yetu, ni moja ya sababu zinazoipa umaarufu mkubwa mahakama hiyo.
Ushahidi wa hili ni hukumu za kwenda jela za watu wa aina ya Rafiki Baghdad, mfanyabiashara maarufu, aliyekuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Ismail Aden Rage, Padri wa Kanisa Katoliki, Parokia ya Mlandizi, Sixtus Kimaro, mwanamuziki Babu Seya na wanawe na kadhalika.
Ni katika mahakama hii ambako kesi ya aliyekuwa Waziri wa Ujenzi katika serikali ya Awamu ya Tatu, Nalaila Kiula, kesi ya wanajeshi wawili wa Uingereza waliokuwa wakituhumiwa kumbaka msichana Mtanzania baharini hadi kufa, zilizosikilizwa.
Ni Kisutu hapo hapo ambako kesi zinazowakabili vigogo za wizi wa mabilioni ya fedha katika akaunti ya madeni ya nje (EPA) na kesi ya matumizi mabaya ya madaraka inayowakabili mawaziri mawili waandamizi wa serikali ya Awamu ya Tatu - Basil Mramba na Daniel Yona - zinapoendeshwa.
Mlolongo wa matukio yanayoijengea umaarufu wa pekee mahakama hii ni mrefu, ikiwa ni pamoja na kesi ya mauaji ya watu wanne inayomkabili aliyekuwa Kamanda wa Upelelezi wa Mkoa wa Dar es Salaam, ACP Abdallah Zombe.
Na kama alivyoahidi Mkuregenzi wa Mashitaka Tanzania (DPP), Eliezer Feleshi, kuwa bado anashughulikia mafaili ya watuhumiwa wa EPA, haina shaka akikamilisha kazi hiyo tunazidi kushuhudia watuhumiwa zaidi wakiwamo vigogo wakifishwa mahakamani hapo.
Zaidi ni kwamba inasifika kwa utoaji hukumu kwa umakini katika baadhi ya kesi ambazo hazina umaarufu, hususan kesi za mirathi na migogoro ya ndoa, ingawa baadhi ya hukumu zimekuwa zikitenguliwa na Mahakama Kuu.
Lakini pia mahakama hii ina sifa mbaya ikiwa ni pamoja na tuhuma za watumishi wake kugubikwa na rushwa, uchafu wa vyoo, uchakavu wa majengo ya mahakama hiyo, ucheleweshwaji wa kutoa maamuzi katika mashauri mbalimbali yaliyopo mahakamani hapo, usalama hafifu na mahakama hiyo kukosa uzio unaoleweka.
Baada ya kuainisha sifa za Mahakama ya Kisutu, nieleze sasa lengo la makala hii. Lengo la makala hii ni kujulisha mamlaka husika changamoto zinazoikabili mahakama hii na mahakama zetu nyingine.
Kwa waandishi wa habari za mahakama mimi ambao sehemu kubwa ya saa za kazi huzitumia tukiwa mahakamani, sina shaka tutakubaliana kwamba chumba Namba 2 cha Mahakama ya Kisutu kina hewa chafu ya mikojo inayotokea katika baadhi ya vyoo vya mahakama hiyo, hali inayosababisha wananchi wanaohudhuria kesi mbalimbali katika chumba hicho kupata usumbufu mkubwa.
Chumba hiki ni doa kwa mahakamani hii, mapangaboi yake ni machakafu, paa lake limevamiwa na ndege walioligeuza kuwa maskani yao, lakini ni ndani ya chumba hicho hicho ambao utakuwata mawakili na waendesha mashitaka, wasomi waliovalia nadhifu, bila kuwasahau waandishi wa habari wakifanya shughuli zao.
Usalama mahakamani hapo nao hauridhishi ingawa kwa kipindi cha hivi karibuni Jeshi la Polisi limejitahidi kumwaga makachero wake katika mahakama hiyo, baada ya kesi za EPA na ukiukwaji wa maadili kuanza kusikilizwa.
Kazi kubwa wanayoifanya makachero hawa ni kunusanusa huku na kule kinachosemwa na kinachotokea wakati kesi hizi zikisikilizwa. Hawa hawako kwa ajili ya kuweka ulinzi wa kudumu.
Ukifika mahakamani hapo utashuhudia ulinzi wa kizamani, watu wa aina tofauti wanaingia na kutoka pasipo kuulizwa wala kupekuliwa. Kwa mtu mwenye kufikiri vizuri, hali hiyo itampa picha ya hatari hasa kwa jinsi mahakama hiyo ilivyo na wateja wengi wakubwa na maarufu ambao ni lazima wana maadui ambao si ajabu siku moja wakaamua kuwadhuru hadharani.
Ushahidi wa hili ni tukio la hivi karibuni la wananchi kuwazonga na kuwazomea Mramba na Yona wakati wakiondoka mahakamani hapo, baada ya kupewa dhamana. Kwa jinsi hali ilivyokuwa, kama kuna kikundi cha watu waliokuwa wamedhamiria kuwadhuru watu hao wangeweza kufanikisha dhamira yao kirahisi.
Hii ndiyo hali halisi, tukifikiria sababu ya wananchi kufanya mahakamani kitendo ambacho hakiruhusiwi kikatiba kwa sababu Yona na Mramba ni watuhumiwa tu, hawajatiwa hatiani na mahakama. Hivyo, kwa wananchi kufikia hatua ya kuwazonga kiasi kile ni wazi kwamba uwezo wa kudhurika kwao (Mramba na Yona) ni mkubwa kwa sababu moja tu, uvumilivu wao umefikia kikomo.
Hapa nieleweke kuwa sitetei watuhumiwa au wahalifu, ninazungumzia sheria tulizojiwekea na tukakubali kuzitii. Kama Mramba na Yona wangechanwa hata na wembe katika mshikemshike huo, halafu baadaye mahakama ikaja kuwaona hawana hatia au DPP akaamua kutumia kifungu cha 91 sura ya 20 cha Sheria ya Makosa ya Jinai kuondoa kesi zao mahakamani, ingekuwaje?
Mbali na tukio hilo, matukio ya watuhumiwa kutoroka wakiwa chini ya ulinzi wa polisi, baada ya kujipaka kinyesi au lile la mwaka jana lililotokea mahakamani hapo la mtuhumiwa mmoja wa kesi za wizi wa kutumia silaha katika benki za NMB, NBC na katika duka la kubadilisha fedha la Namanga, kujirusha kutoka ghorofani, yanaonyesha umuhimu wa kuimarisha ulinzi mahakamani hapo.
Kinachohitajika kwa serikali ni kuhakikisha inaongeza bajeti ya mahakama ya Tanzania ili iweze chombo hicho kiweze kufanya kazi katika mazingira yanayokubalika. Serikali inapaswa kuachana na kasumba ya kupeleka fedha nyingi katika masuala ya kisiasa kuliko mahakama na sekta nyingine muhimu.
Hii iwe changamoto kwa serikali, ilichukulie hili kama jambo la dharura kwa sababu ni wazi kuwa uwezo wa kuboresha mahakama zetu upo. Nasema upo kwa sababu sijawahi kusikia vikao vya Bunge au semina elekezi kwa makatibu wa kuu wa wizara, mawaziri na wakuu wa mikoa vinashindwa kufanyika kwa sababu ya uhaba wa fedha.
Lakini ni jambo la kawaida kwa Mahakama Kuu kuendesha vikao vichache au kesi chache kwa sababu ya uhaba wa fedha. Tatizo la msongamano wa mahabusu magerezani, linachangiwa kwa kiasi kikubwa na uhaba wa fedha, wakati Watanzania wanashuhudia kila kukicha ongozeko la magari ya kifahari yakitolewa kwa viongozi.
Serikali ina kila sababu ya kufanya jitihada za makusudi kama ilizofanya katika kuboresha maslahi ya vitendea kazi kwa Jeshi la Polisi.
Mungu ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika

0755 312859
katabazihappy@yahoo.com:www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano Desemba 17 mwaka 2008

ZAMU YA MGONJA KEKO

*Apanda kizimbani kwa mashtaka manane
*Akabiliwa na tuhuma za Mramba na Yona
*Mtuhumiwa wa 21 EPA apanda kizimbani

Na Happiness Katabazi

ALIYEKUWA Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Uchumi ambaye yuko kwenye likizo ya kustaafu, Gray Mgonja, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na mashtaka manane ya matumizi mabaya ya madaraka na kulisababishia taifa hasara ya sh. 11,752,350,148
Mgonja, alifikishwa mahakamani hapo jana majira ya saa 7:20 mchana, chini ya ulinzi mkali wa makachero wa polisi, waliokuwa wakiongozwa na Msaidizi wa Mkuu wa Kituo cha Polisi Kati, Inspekta Gewe Ninga.
Mgonja ambaye aliwahi kutajwa na Mbunge wa Karatu, Dk. Willibrod Slaa (Chadema), kwenye orodha ya watu 11 wanaodaiwa kuhusishwa na tuhuma za ufisadi, alitinga mahakamani hapo kwa gari aina ya Toyota, Rav 4, yenye namba za usajili T123 ATW kuingizwa moja kwa moja kwenye mahabusu ya mahakama hiyo.
Kabla ya kufikishwa kwa Mgonja mahakamani hapo, makachero wa polisi, wale wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), askari wa Kikosi cha Mbwa cha Kilwa Road, walikuwa wametanda kila pembe ya mahalama kwa ajili ya kuimarisha ulinzi na kuwa tayari kukabiliana na hali yoyote ya vurugu kama ingelitokea.
Ulinzi huo uliimarishwa ili kuzuia kile kilichowahi kutokea wakati Waziri wa Fedha wa zamani, Basil Mramba, na Waziri wa Nishati na Madini Serikali ya awamu ya tatu, Daniel Yona, walipofikishwa mahakamani hapo Novemba 25 mwaka huu, wakikabiliwa na mashtaka kama ya Mgonja.
Ilipofika majira ya saa 7:52, Mgonja aliingizwa kwenye ukumbi namba mbili wa mahakama hiyo, tayari kwa kusomewa mashtaka yake.
Mwanasheria Mwandamizi wa Serikali, Fredrick Manyanda, ambaye alikuwa akisaidiana na mwanasheria wa Takukuru, Joseph Ole, mbele ya hakimu Henzron Mwankenja, alidai kuwa, mshtakiwa huyo, anakabiliwa na mashtaka manane ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisabababishia serikali ya Jamhuri ya Muungano hasara ya sh 11,752,350,148.
Manyanda alidai kuwa Oktoba 10 mwaka 2003, katika ofisi ya Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam, mshitakiwa akiwa mtumishi wa serikali na wadhifa wa Katibu Mkuu wa wizara hiyo, alitumia madaraka yake vibaya kwa kuipatia msamaha wa kodi kampuni ya M/S Alex Stewart (Assayers), Government Bussiness Corporation, kinyume na maelekezo ya Mamlaka ya Mapato (TRA).
Alidai kuwa kati Desemba 18-19 mwaka 2003, katika wizara hiyo na wadhifa huo, mtuhumiwa alitumia madaraka ya ofisi ya umma vibaya kwa kutoa notisi ya serikali yenye namba 423 ya mwaka 2003 ya kusamehe kodi kampuni hiyo ya M/S Alex Stewart (Assayers) Government Bussiness Corporation, kinyume na mapendekezo ya TRA ambayo yalikataza kampuni hiyo isipewe msamaha wa kodi.
Katika shitaka la tatu, alidai kuwa, Desemba 19 mwaka 2003, mshitakiwa huyo akiwa na wadhifa huo, alitoa notisi ya serikali yenye namba 424 ya mwaka 2003 ambayo ilitoa msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo, kinyume na TRA.
Aidha alidai kuwa, katika shtaka la nne, Oktoba 15 mwaka 2004, alitoa notisi ya serikali yenye namba 497 ya mwaka 2004 kwa kampuni hiyo na katika shtaka la tano, wakili Manyanda alidai kuwa, Oktoba 14-15 mwaka 2004, akiwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, alitoa alitoa notisi ya serikali yenye namba 4198 cha 2004 ya kusamehe kodi kampuni hiyo.
Aliendelea kudai kuwa, Novemba 15 mwaka 2005, mshtakiwa akiwa mtumishi wa umma, alitoa notisi ya serikali yenye namba 377 ya mwaka 2005, iliyotoa msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo, kinyume na mapendekezo ya TRA.
Mwanasheria wa Takukuru, Joseph Ole, ambaye alisoma maelezo ya shtaka la saba na nane, alidai kuwa Novemba 15 mwaka 2005, katika Wizara ya Fedha, mshtakiwa akiwa mtumishi wa umma na Katibu Mkuu wa wizara hiyo, alitoa notisi ya serikali namba 378, yenye kuisamehe kodi kampuni hiyo hiyo.
Aidha katika shtaka la nane, Ole alidai kwamba kati ya mwaka 2003-2007, katika Wizara ya Fedha, mshitakiwa huyo akiwa mwajiriwa wa serikali, kwa makusudi au kwa kushindwa kuchukua tahadhari katika utendaji wake, aliidhinisha notisi za serikali namba 423/2003 na 424/2003, 497/2004 na 498/2004, 377/2005 na 378/2005 ya kuisamehe kodi kampuni ya M/S Alex Stewart (Assayers) Government Bussiness Corporation na kuisababishia serikali hasara ya jumla ya sh 11,752,350,148.
Hata hivyo upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika.
Mshtakiwa huyo ambaye anatetewa na jopo la mawakili wa kujitegemea, Profesa Leonard Shaidi, Dk. Alex Nguluwe, Pius Kisarika na Silvanus Mlola, alikana mashtaka yote.
Kiongozi wa jopo hilo la mawakili wa Mgonja, Profesa Shaidi, alidai mahakamani hapo kuwa kesi ya mteja wake inafanana na kesi ya jinai namba 1,200 ya mwaka huu, inayomkabili Mramba na Yona, hivyo anaomba masharti ya dhamana yaliyotolewa kwa washtakiwa hao yatolewe kwa mteja wake (Mgonja).
Hata hivyo Hakimu Mwankenja alimuuliza swali wakili wa serikali Manyanda kwa nini Mgonja asingeunganishwa katika kesi ya Mramba na Yona kwa sababu mashtaka anayokabiliwa nayo, yanafanana na yanayowakabili mawaziri hao wastaafu.
Akijibu hoja hiyo, Wakili Manyanda alidai kuwa upelelezi wa kesi ya Mramba na Yona haujakamilika na endapo utakamilika, wanaweza kuunganishwa kwenye kesi moja itakayojumuisha washtakiwa wote watatu.
Baada ya kusikiliza hoja za pande hizo mbili, Hakimu Mwankenja, aliahirisha kesi hiyo kwa dakika 15 ili aende akaandike uamuzi wa dhamana na alirejea mahakamani hapo majira ya saa 8:52.
Hakimu huyo, alisema kuwa dhamana kwa mshtakiwa huyo ipo wazi na anatakiwa adhaminiwe kwa fedha taslimu sh bilioni 5.9 au hati ya mali yenye thamani hiyo.
Mwankenja alisema amefikia uamuzi wa kumtaka mshtakiwa apate dhamana kwa kiasi hicho cha sh bilioni 5.9 kwa sababu yupo peke yake kwenye kesi hiyo na kuongeza kwamba, endapo kesi ya kina Mramba na Yona ikivunjwa na kuundwa kesi moja, dhamana hiyo itapungua.
Katika sharti la pili alimtaka mshtakiwa kusalimisha hati ya kusafiria mahakamani, kutotoka nje ya Dar es Salaam hadi aombe kibali cha mahakama na kwamba awe na wadhamini wawili wa kuaminika.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Desemba 29 mwaka huu, kwa ajili ya kutajwa.
Hata hivyo walijitokeza wadhamini wawili waliojitambulishwa kwa majina ya Ramadhani Mlinga na Devina Mlaki ambao walidai kwamba wanafanya kazi pamoja na mshtakiwa.
Hata hivyo Mgonja alishindwa kutimiza masharti ya dhamana, hivyo kufanya apelekwe rumande katika Gereza la Keko ; aliondoka mahakamani hapo majira ya saa 10:08, huku akiwa amepandishwa kwenye gari alilokuja nalo asubuhi.
Katika safari ya Keko, Mgonja alisindikizwa na Land Rover Defender mbili za polisi, zenye namba za usajili T220 AMV na PT 0940 ambalo lilikuwa limebeba mbwa watatu, ikiwa ni mara ya kwanza kuletwa tangu kuanza kwa kesi zinazohusiana na tuhuma za ufisadi.
Mngonja anakuwa kiongozi wa tatu mkubwa wa Serikali ya Awamu ya Tatu iliyokuwa ikiongozwa na rais mstaafu, Benjamin Mkapa, kufikishwa mahakamani kwa makosa ya matumizi mabaya ya madaraka.
Wakati huo huo mshitakiwa mwingine wa kesi ya wizi wa EPA, Mfanyabiashara, Jonathas Munisi alifikishwa mahakamani hapo jana, akikabiliwa na mashtaka ya wizi na kujipatia ingizo kwenye akaunti lenye thamani ya sh bilioni 2.6, mali ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).
Mwanasheria Kiongozi wa Serikali, Staslaus Boniface, alidai mbele ya hakimu, Addy Lyamuya kwamba, Julai 25 mwaka 2005, mshtakiwa huyo alijipatia ingizo la kiasi hicho cha fedha kwa madai kwamba Kampuni ya Njake Enterprises, ilipewa kibali cha kurithi deni la Kampuni ya Elton ya Japan. Hata hivyo mshtakiwa alikana shtaka hilo.
Lyamuya alisema ili mshtakiwa apate dhamana, lazima atoe nusu ya fedha anazotuhumiwa kuiba, yaani sh bilioni 1.3 au kuwasilisha hati ya mali yenye thamani sawa na kiasi hicho, sharti ambalo alishindwa kulitimiza, kesi hiyo kuahirishwa hadi Desemba 30 mwaka huu.
Kufikishwa kwa mtuhumiwa huyo kunafanya idadi ya watuhumiwa wa wizi wa EPA, kufikia 21.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima,Jumanne ya Desemba 16 mwaka 2008

ZAMU YA MGONJA KEKO

*Apanda kizimbani kwa mashtaka manane
*Akabiliwa na tuhuma za Mramba na Yona
*Mtuhumiwa wa 21 EPA apanda kizimbani

Na Happiness Katabazi

ALIYEKUWA Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Uchumi ambaye yuko kwenye likizo ya kustaafu, Gray Mgonja, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na mashtaka manane ya matumizi mabaya ya madaraka na kulisababishia taifa hasara ya sh. 11,752,350,148
Mgonja, alifikishwa mahakamani hapo jana majira ya saa 7:20 mchana, chini ya ulinzi mkali wa makachero wa polisi, waliokuwa wakiongozwa na Msaidizi wa Mkuu wa Kituo cha Polisi Kati, Inspekta Gewe Ninga.
Mgonja ambaye aliwahi kutajwa na Mbunge wa Karatu, Dk. Willibrod Slaa (Chadema), kwenye orodha ya watu 11 wanaodaiwa kuhusishwa na tuhuma za ufisadi, alitinga mahakamani hapo kwa gari aina ya Toyota, Rav 4, yenye namba za usajili T123 ATW kuingizwa moja kwa moja kwenye mahabusu ya mahakama hiyo.
Kabla ya kufikishwa kwa Mgonja mahakamani hapo, makachero wa polisi, wale wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), askari wa Kikosi cha Mbwa cha Kilwa Road, walikuwa wametanda kila pembe ya mahalama kwa ajili ya kuimarisha ulinzi na kuwa tayari kukabiliana na hali yoyote ya vurugu kama ingelitokea.
Ulinzi huo uliimarishwa ili kuzuia kile kilichowahi kutokea wakati Waziri wa Fedha wa zamani, Basil Mramba, na Waziri wa Nishati na Madini Serikali ya awamu ya tatu, Daniel Yona, walipofikishwa mahakamani hapo Novemba 25 mwaka huu, wakikabiliwa na mashtaka kama ya Mgonja.
Ilipofika majira ya saa 7:52, Mgonja aliingizwa kwenye ukumbi namba mbili wa mahakama hiyo, tayari kwa kusomewa mashtaka yake.
Mwanasheria Mwandamizi wa Serikali, Fredrick Manyanda, ambaye alikuwa akisaidiana na mwanasheria wa Takukuru, Joseph Ole, mbele ya hakimu Henzron Mwankenja, alidai kuwa, mshtakiwa huyo, anakabiliwa na mashtaka manane ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisabababishia serikali ya Jamhuri ya Muungano hasara ya sh 11,752,350,148.
Manyanda alidai kuwa Oktoba 10 mwaka 2003, katika ofisi ya Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam, mshitakiwa akiwa mtumishi wa serikali na wadhifa wa Katibu Mkuu wa wizara hiyo, alitumia madaraka yake vibaya kwa kuipatia msamaha wa kodi kampuni ya M/S Alex Stewart (Assayers), Government Bussiness Corporation, kinyume na maelekezo ya Mamlaka ya Mapato (TRA).
Alidai kuwa kati Desemba 18-19 mwaka 2003, katika wizara hiyo na wadhifa huo, mtuhumiwa alitumia madaraka ya ofisi ya umma vibaya kwa kutoa notisi ya serikali yenye namba 423 ya mwaka 2003 ya kusamehe kodi kampuni hiyo ya M/S Alex Stewart (Assayers) Government Bussiness Corporation, kinyume na mapendekezo ya TRA ambayo yalikataza kampuni hiyo isipewe msamaha wa kodi.
Katika shitaka la tatu, alidai kuwa, Desemba 19 mwaka 2003, mshitakiwa huyo akiwa na wadhifa huo, alitoa notisi ya serikali yenye namba 424 ya mwaka 2003 ambayo ilitoa msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo, kinyume na TRA.
Aidha alidai kuwa, katika shtaka la nne, Oktoba 15 mwaka 2004, alitoa notisi ya serikali yenye namba 497 ya mwaka 2004 kwa kampuni hiyo na katika shtaka la tano, wakili Manyanda alidai kuwa, Oktoba 14-15 mwaka 2004, akiwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, alitoa alitoa notisi ya serikali yenye namba 4198 cha 2004 ya kusamehe kodi kampuni hiyo.
Aliendelea kudai kuwa, Novemba 15 mwaka 2005, mshtakiwa akiwa mtumishi wa umma, alitoa notisi ya serikali yenye namba 377 ya mwaka 2005, iliyotoa msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo, kinyume na mapendekezo ya TRA.
Mwanasheria wa Takukuru, Joseph Ole, ambaye alisoma maelezo ya shtaka la saba na nane, alidai kuwa Novemba 15 mwaka 2005, katika Wizara ya Fedha, mshtakiwa akiwa mtumishi wa umma na Katibu Mkuu wa wizara hiyo, alitoa notisi ya serikali namba 378, yenye kuisamehe kodi kampuni hiyo hiyo.
Aidha katika shtaka la nane, Ole alidai kwamba kati ya mwaka 2003-2007, katika Wizara ya Fedha, mshitakiwa huyo akiwa mwajiriwa wa serikali, kwa makusudi au kwa kushindwa kuchukua tahadhari katika utendaji wake, aliidhinisha notisi za serikali namba 423/2003 na 424/2003, 497/2004 na 498/2004, 377/2005 na 378/2005 ya kuisamehe kodi kampuni ya M/S Alex Stewart (Assayers) Government Bussiness Corporation na kuisababishia serikali hasara ya jumla ya sh 11,752,350,148.
Hata hivyo upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika.
Mshtakiwa huyo ambaye anatetewa na jopo la mawakili wa kujitegemea, Profesa Leonard Shaidi, Dk. Alex Nguluwe, Pius Kisarika na Silvanus Mlola, alikana mashtaka yote.
Kiongozi wa jopo hilo la mawakili wa Mgonja, Profesa Shaidi, alidai mahakamani hapo kuwa kesi ya mteja wake inafanana na kesi ya jinai namba 1,200 ya mwaka huu, inayomkabili Mramba na Yona, hivyo anaomba masharti ya dhamana yaliyotolewa kwa washtakiwa hao yatolewe kwa mteja wake (Mgonja).
Hata hivyo Hakimu Mwankenja alimuuliza swali wakili wa serikali Manyanda kwa nini Mgonja asingeunganishwa katika kesi ya Mramba na Yona kwa sababu mashtaka anayokabiliwa nayo, yanafanana na yanayowakabili mawaziri hao wastaafu.
Akijibu hoja hiyo, Wakili Manyanda alidai kuwa upelelezi wa kesi ya Mramba na Yona haujakamilika na endapo utakamilika, wanaweza kuunganishwa kwenye kesi moja itakayojumuisha washtakiwa wote watatu.
Baada ya kusikiliza hoja za pande hizo mbili, Hakimu Mwankenja, aliahirisha kesi hiyo kwa dakika 15 ili aende akaandike uamuzi wa dhamana na alirejea mahakamani hapo majira ya saa 8:52.
Hakimu huyo, alisema kuwa dhamana kwa mshtakiwa huyo ipo wazi na anatakiwa adhaminiwe kwa fedha taslimu sh bilioni 5.9 au hati ya mali yenye thamani hiyo.
Mwankenja alisema amefikia uamuzi wa kumtaka mshtakiwa apate dhamana kwa kiasi hicho cha sh bilioni 5.9 kwa sababu yupo peke yake kwenye kesi hiyo na kuongeza kwamba, endapo kesi ya kina Mramba na Yona ikivunjwa na kuundwa kesi moja, dhamana hiyo itapungua.
Katika sharti la pili alimtaka mshtakiwa kusalimisha hati ya kusafiria mahakamani, kutotoka nje ya Dar es Salaam hadi aombe kibali cha mahakama na kwamba awe na wadhamini wawili wa kuaminika.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Desemba 29 mwaka huu, kwa ajili ya kutajwa.
Hata hivyo walijitokeza wadhamini wawili waliojitambulishwa kwa majina ya Ramadhani Mlinga na Devina Mlaki ambao walidai kwamba wanafanya kazi pamoja na mshtakiwa.
Hata hivyo Mgonja alishindwa kutimiza masharti ya dhamana, hivyo kufanya apelekwe rumande katika Gereza la Keko ; aliondoka mahakamani hapo majira ya saa 10:08, huku akiwa amepandishwa kwenye gari alilokuja nalo asubuhi.
Katika safari ya Keko, Mgonja alisindikizwa na Land Rover Defender mbili za polisi, zenye namba za usajili T220 AMV na PT 0940 ambalo lilikuwa limebeba mbwa watatu, ikiwa ni mara ya kwanza kuletwa tangu kuanza kwa kesi zinazohusiana na tuhuma za ufisadi.
Mngonja anakuwa kiongozi wa tatu mkubwa wa Serikali ya Awamu ya Tatu iliyokuwa ikiongozwa na rais mstaafu, Benjamin Mkapa, kufikishwa mahakamani kwa makosa ya matumizi mabaya ya madaraka.
Wakati huo huo mshitakiwa mwingine wa kesi ya wizi wa EPA, Mfanyabiashara, Jonathas Munisi alifikishwa mahakamani hapo jana, akikabiliwa na mashtaka ya wizi na kujipatia ingizo kwenye akaunti lenye thamani ya sh bilioni 2.6, mali ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).
Mwanasheria Kiongozi wa Serikali, Staslaus Boniface, alidai mbele ya hakimu, Addy Lyamuya kwamba, Julai 25 mwaka 2005, mshtakiwa huyo alijipatia ingizo la kiasi hicho cha fedha kwa madai kwamba Kampuni ya Njake Enterprises, ilipewa kibali cha kurithi deni la Kampuni ya Elton ya Japan. Hata hivyo mshtakiwa alikana shtaka hilo.
Lyamuya alisema ili mshtakiwa apate dhamana, lazima atoe nusu ya fedha anazotuhumiwa kuiba, yaani sh bilioni 1.3 au kuwasilisha hati ya mali yenye thamani sawa na kiasi hicho, sharti ambalo alishindwa kulitimiza, kesi hiyo kuahirishwa hadi Desemba 30 mwaka huu.
Kufikishwa kwa mtuhumiwa huyo kunafanya idadi ya watuhumiwa wa wizi wa EPA, kufikia 21.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima,Jumanne ya Desemba 16 mwaka 2008