DECI WAKWAMA TENA KISUTU


Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imekataa kurudia kutoa uamuzi wa dhamana wa kesi ya vigogo wa Taasisi ya Entrepreneurship for Community Initiative (DECI) kwa sababu tayari Hakimu Mkuu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, Addy Lyamula alishaitolea uamuzi.


Hayo yalisemwa jana na Hakimu Mkazi, Mteite, muda mfupi tu baada ya mawakili wa utetezi kuwasilisha ombi la kutaka mahakama hiyo iziondoe sababu zilizosababisha DPP-Eliezer Feleshi, Juni 17 mwaka huu, kutoa hati ya kuzuia dhamana ya washitakiwa, kwa madai sababu hizo hivi sasa hazipo tena.

Kitululu alidai sababu hizo hazipo tena kwani awali shauri hilo lilikuja kwa ajili ya kutajwa kwa mara ya kwanza, na upande wa mashitaka ukawa umejengewa uwoga, hivyo DPP akafikia uamuzi wa kutoa hati hiyo ya kuzuia dhamana, ili kulinda usalama wa washitakiwa na maslahi ya Jamhuri.

“Siku hiyo kulikuwa na Maaskari wengi hapa Mahakamani hata wale wa kutuliza ghasia, ni ni dhahiri leo pia hawapo (jana), jambo ambalo limedhihirisha kuwa upande wa serikali umeridhika na hakuna wasiwasi wa kiusalama dhidi ya wateja wetu;

“Na kwa misingi hii tunaomba upande wa mashitaka uiondoe hati hiyo ya DPP ya kuzuia dhamana kwa washitakiwa ili wateja wetu waweze kupata dhamana kwani shitaka linalowakabili linadhamiwa” alisema Kitululu.

Akipangua hoja hizo wakili wa serikali, Biswalo Mganga, alianza kwa kusema yeye ana majibu mafupi kwamba upelelezi huo bado haujakamilika.

Mganga alidai kesi hiyo ilipokuja kwa mara ya pili Juni 17, mwaka huu, pamoja na mambo mengine yote, Hakimu Mkazi Lyamuya alitoa uamuzi kuhusu dhamana ya washitakiwa, uamuzi ambao alidai umemfunga mikono hata Hakimu Mteite na mahakama hiyo kwa kuwa haina mamlaka ya kutengua hati ya DPP.

Mganga akipangua hoja hizo huku akionyesha kujiamini, alidai hati hiyo ni ya DPP na bado DPP hajawasilisha taarifa ya kuiondoa.

Kuhusu hoja ya sababu za kiusalama baina ya washitakiwa na jamhuri , alidai sababu hizo zilitolewa na DPP na wala siyo Kitululu hivyo ni vema DPP mwenyewe akatoa taarifa ya kuiondoa hati hiyo.

Kuhusu hoja kwamba FFU na wanausalama kutokuwepo kwa wingi jana mahakamani hapo, alisema

“Hivi wale nyuma ni Mgambo?si maofisa wa polisi na wakili huyo asitake kuvifundisha kazi vyombo vya ulinzi na usalama kazi kwani vyenyewe vinajua ni jinsi gani vinavyofanyakazi” alidai Mganga na kusababisha watu kuangua kicheko.

Akitoa uamuzi wake, Hakimu Mkazi Mteite, alisema kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya kutajwa tu na kwamba amesikiliza hoja za pande zote mbili na kueleza kuwa kuhusu hoja za upande wa utetezi kutaka wateja wake wapatiwe dhamana, hawezi kutolea maamuzi ombi hilo kwa mara ya pili kwani Hakimu Lyamuya alishalitolea uamuzi .

Lakini Mteite aliutaka upande wa mashitaka uangalie kama zile sababu zilizoainishwa kwenye hati ya DPP kama hivi sasa hazina nguvu tena, basi waziondee ili washitakiwa waweze kupatiwa dhamana na akaiahirisha kesi hiyo hadi Julai 10 mwaka huu.

Washitakiwa katika kesi hiyo ni Jackson Mtares Dominic Kisendi, Timotheo ole Loitgimnye, Samwel Mtares, Arbogast Kipilimba na Samwel Mtalis ambao wote wanaendelea kusota rumande.

Juni 12 mwaka huu, Wakili Kiongozi wa Serikali Justus Mlokozi alidai washitakiwa wote wanakabiliwa na mashitaka mawili, shitaka la kwanza ni kuendesha na kusimamia mradi wa upatu kinyume na kifungu 111A(1)(3)cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu , na shitaka la pili ni kupokea amana za umma bila leseni kinyume na kifungu cha 6(1,2) cha Sheria ya Mabenki na Taasisi za Kifedha Na.5 ya 2006.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumatano, Julai mosi, 2009

SERIKALI YAWEWESEKA MGOMBEA BINAFSI

Na Happiness Katabazi

KWA mara ya pili, serikali imekata rufaa dhidi ya Mwenyekiti wa Chama cha Democrat (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, katika Mahakama ya Rufani nchini, kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, ulioruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi katika uchaguzi mkuu.


Kwa mujibu wa rufaa hiyo namba 45 ya mwaka huu, inaonyesha serikali iliwasilisha rufaa hiyo, Ijumaa iliyopita mahakamani hapo ikipinga hukumu ya iliyotolewa na waliokuwa majaji wa Mahakama Kuu, ambao ni Jaji Mstaafu Amir Manento, Salum Massati, Jaji wa Mahakama ya Rufani na Thomas Mihayo (Mstaafu), ambao walikubaliana na ombi na Mtikila na kuruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi nchini.

Katika rufaa hiyo, serikali imetoa sababu sita za kukata rufaa hiyo zikiwemo; Mahakama Kuu ilikosea kujipa mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo, ilikosea kutengua vifungu vya Katiba ya nchi, na kukosea kisheria kwa kupunguza matakwa ya lazima ya Ibara 30(5) na 13(2) ya Katiba ya nchi.

Sababu nyingine ni kujipachika mamlaka ya kibunge ya kutunga sheria, kukosea kisheria kwa kuiweka Katiba ya nchi katika vyombo vya kimataifa na pia ilikosea kuitolea maamuzi kesi hiyo bila kuweka suala hilo bayana.

Mara ya kwanza, serikali ilikata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama Kuu, katika Mahakama hiyo ya Rufaa mwaka 2007, ambapo ilidai mahakama hiyo ya chini ilikosea kisheria kutafsiri Ibara ya 21(1)(c), 39(1)(c) (b) na 69(1)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano.

Hata hivyo, rufaa hiyo ilitupwa na Mahakama ya Rufaa baada ya kukubalina na ombi la wakili wa Mtikila, Richard Rweyongeza kwamba, rufaa hiyo haina msingi na kwamba imejaa dosari za kisheria.

Awali katika hukumu ya Mahakama Kuu uliotolewa Mei 2006, ililiruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi katika uchaguzi, kwa sababu Katiba ya nchi inatoa haki hiyo.

Mahakama Kuu ilibainisha kuwa Katiba inatamka wazi kuwa, kila mwananchi ana haki ya kuchagua au kuchaguliwa kuwa kiongozi na haiweki masharti kuwa hilo lifanyike kwa mtu kujiunga na chama fulani.

Mwaka 1993, Mtikila alishinda kesi kama hiyo katika Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, lakini licha ya uamuzi huo wa mahakama, Bunge lilishindwa kutunga sheria ya kuruhusu mgombea binafsi hivyo alifungua kesi hiyo ya kikatiba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na kushinda tena.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumatano, Julai mosi, 2009

TUWE MAKINI MBINU CHAFU ZA UCHAGUZI MKUU ZIMEISHAANZA

Na Happiness Katabazi

WATANZANIA wenzangu kaeni mkao wa kula, msimu wa uchaguzi (mavuno) umewadia, hilo ndilo ambalo naweza kulisema kuhusu pilikapilika na hekaheka za maandalizi ya wagombea uenyekiti wa serikali za mitaa na vijiji, udiwani, ubunge na urais.

Mara nyingi, wananchi tumekuwa hatupo makini katika kuchagua viongozi kwa kuwa tunauona uchaguzi kama sehemu ya kuvuna fedha kutoka kwa wagombea.

Lakini tayari Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameshabainisha kuwa, serikali imeandaa mabadiliko ya sheria ya uchaguzi ili kuondoa vifungu vinavyohalalisha takrima (rushwa).

Kauli hiyo ya Pinda inaonekana kukosa mashiko wa wagiga kura na wagombea kwa kuwa kila mmoja anajiona ana haki ya kutoa au kupokea takrima.

Tayari huku mitaani hivi sasa zimeshaanza pilikapilika kabambe kwa wagombea watarajiwa kutoa hongo kwa namna mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kufadhili timu za mipira ya miguu, kuanzisha mashindano na kutoa vikombe vinavyopachikwa majina yao, kutoa misaada kwa vikundi vya waathirika vya ukimwi na SACCOS.

Walengwa wakuu wa takrima hizo ni vijana na wanawake kwa kuwa wao ndio wanaonekana kuwa ni rahisi kurubuniwa na kupokea rushwa.

Si jambo la kushangaza hivi sasa wapanbe wa wagombea hao kuanza kubisha hodi misikitini na makanisani kwa lengo la kutoa misaada mbalimbali pamoja na kujenga nyumba hizo za ibada.

Katika kipindi hiki, wagombea watakuwa wacha-mungu zaidi pamoja na kutembelea maeneo mbalimbali ilimradi wawe karibu na wananchi kwa lengo la kuwapumbaza.

Tunatakiwa tujiulize maswali magumu, fedha hizi wanazozigawa wapambe wa wagombea hao watarajiwa wamezipata wapi? Au kuna EPA mpya ambayo hatujaigundua?

Sina shaka kuwa kuna uhusiano wa karibu wa wingi huo wa fedha hizo zinazoanza kutapanywa na kupungua kwa mapato ya serikali yanayokusanywa na TRA.

Sababu zinazotolewa za kuyumba kwa uchumi kuwa ndiyo kiini cha kupungua kwa mapato ya nchi, yaweza kuwa kiini macho. Wakati ukifika tutabaini hilo.

Lakini pia tutupie macho yetu kwenye eneo ambalo limekuwa likilindwa na serikali kwa usiri mkubwa, yaani mikataba ya uwekezaji na tenda za manunuzi ya umma.

Naamini kwamba ufisadi katika maeneo haya haujaguswa kana kwamba haupo, lakini najua mabilioni ya serikali hulipwa kila mara kwa mikataba isiyo na tija kwa taifa, kuna kandarasi na tenda za manunuzi ya umma zinazosukwa kwa madhumuni ya kuiba mabilioni ya fedha za umma.

Miradi mingi inayofanywa hivi sasa na serikali inakuwa na mazingira ya watu kunufaika zaidi (ufisadi), ujenzi wa barabara, utengenezaji wa vitambulisho vya uraia vimetengewa fedha nyingi, lakini ukija kuangalia gharama halisi unaweza kuzimia.

Wakati mwingine ufisadi huu wa kuibia umma ufanyika mchana kweupe, kwani barabara zinazojengwa huharibika kabla ya kipindi kifupi tu baada ya kuanza kutumika.

Kwa nini jamii isiamini kwamba baadhi ya wanasiasa na watendaji serikalini wameshajichotea mabilioni ya fedha kwa ajili ya kampeni za uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika mwakani?

Kuna tatizo gani katika kufuatilia mambo hayo? Mbona tuna vyombo vya usalama vingi? Idara ya Usalama wa Taifa inayoongozwa na kiongozi shupavu, Rashid Othman ipo, TAKUKURU chini ya Dk. Edward Hosea ipo. Je, hawajatambua maovu hayo?

Nina uhakika itakapofika mwaka 2011 zitaibuliwa kashfa za watu waliojichotea fedha za wananchi na kuzitumia katika uchaguzi.

Binafsi sijaona tija yoyote ya fedha zilizotolewa na Rais Jakaya Kikwete, maarufu kama ‘mabilioni ya JK’, kwa ajili ya kuwasaidia wajasiriamali. Pia nina shaka hata hizo sh trilioni 1.5 zilizotengwa kwa ajili ya kukabiliana na mtikisiko wa uchumi, zinaweza ziende ninakotarajia.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Beno Ndulu, Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustapha Mkulo, walishawahi kuliambia taifa kuwa nchi yetu haitaathirika na mtikisiko wa uchumi, lakini sasa ni tofauti je, nani aaminike?

Najua hakuna atakayeweza kuzuia fedha zilizotengwa na Rais Kikwete kwa ajili ya kukabiliana na mtikisiko wa uchumi zisitumike vibaya, wadadisi wa mambo wanaona fedha hizo zimewekwa kwa ajili ya uchaguzi, hasa kwa chama tawala ili waseme wameshinda kwa kishindo.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Julai 28,2009

WAZEE WA BARAZA WAMTETEA ZOMBE

*Waiambia korti hana hatia
*Wengine ushahidi wawabana
*Sasa yasubiriwa hukumu

Na Happiness Katabazi

WAZEE wa Baraza katika kesi ya mauaji ya wafanyabishara watatu na dereva taksi mmoja inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam, ACP Abdallah Zombe na wenzake nane, wameiomba Mahakama Kuu imwachie huru Zombe kwa kuwa hana hatia.


Wazee hao wa baraza, Magreth Mossi na Nicolus Kimolo, walitoa kauli hizo jana alipokuwa wakitoa maoni yao kulingana na ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo na pande zote mbili.

Mbali na kuomba Zombe kuachiwa huru wazee hao pia wameimba mahakama kumwachia huru mshitakiwa mwinigine katika kesi hiyo, Festus Gwasabi (mshitakiwa wa 13) kwa maelezo kuwa ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo dhidi ya washitakiwa hao haukuweza kudhibitisha kuhusika na mauaji hayo.

Kabla ya wazee hao kutoa maoni hayo jana, Jaji wa Mahakam ya Rufani, Salum Massati, anayesikiliza kesi hiyo juzi aliwatahadharisha kutoa maoni yao kwa kutozingatia yaliyoandikwa katika vyombo vya habari kwani yameandikwa mengi kuhusiana na kesi hiyo.

Hata hivyo, katika kutoa hukumu ya kesi hiyo, Jaji anaweza kuzingatia au kutozingatia maoni ya wazee hao.

Mzee wa baraza aliyeanza kutoa maoni yake ni Kimolo ambaye alieleza kuwa kulingana na ushahidi wa upande wa mashitaka, hakuna shahidi aliyedhibitisha kwamba Zombe alishiriki katika mauaji hayo na pia hakuna shahidi aliyethibitisha alimuona Zombe kwenye eneo la tukio.

Mzee wa Baraza Kimolo ndiye aliyaanza kutoa maoni na mapendekezo yake kuhusu mshitakiwa wa kwanza(Zombe), alikumbusha upande wa mashitaka ulileta mashahidi 37 na hakuna udhibitisho kwamba mshitakiwa huyo alishiriki katika mauji hao na kwamba hakuna shahidi hata mmoja aliyeweza kusema wala kuthibitisha kwamba walimuona Zombe kwenye eneo la tukio.

Kimolo alidai kuhusu hoja iliyotolewa na upande wa mashitaka kwamba Zombe alikwenda kituo cha Polisi Urafiki, yeye ameona mshitakiwa huyo alikwenda kutatua utata wa fedha na alitoa amri kwamba kielelezo hicho kitimie na kuongeza hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Zombe aende kituoni hapo.

Kuhusu hoja ya mashitaka kwamba Zombe aliwapa mkono wa pongezi askari kuwa alikuwa anajua kilichokuwa kinaendelea kwani asingeweza kutoa pongezi kwa baadhi ya askari; alidai kwa maoni yake Zombe alikuwa hajui chochote kilichokuwa kinaendelea.

Alikumbusha kuwa mahakama hiyo ilielezwa na mshitakiwa wa 12,Rajabu Bakari jinsi walivyofundishwa na Zombe kujibu maswali kwenye Tume ya ACP-Mgawe na Jaji Mussa Kipenka, pia aliendelea kueleza kuwa mshitakiwa wa kwanza aliwapa vikaratasi vya kujitetea lakini Rajabu wakati akijitetea alidai hata hayo aliyofundishwa kujitetea hayakumsaidia na hata alipotakiwa na mahakama atoe hivyo vikaratasi alishindwa kuwasilisha mahakamani vikaratasi hivyo.

“Maoni yangu katika hilo hilo , kushindwa kwa Rajabu kuwasilisha vikaratasi hivyo hayana ukweli” alidai Kimolo huku akionyesha kujiamini.

Akichambua ushahidi wa shahidi wa 36 wa upande wa mashitaka,Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Sidney Mkumbi ambaye ndiye alikuwa Mpelelezi Mkuu wa kesi hiyo, alikiri mbele ya mahakama hiyo kuwa Zombe akuandika maeleszo ,pia alieleza mahakama kuwa mshitakiwa wa kwanza ameunganishwa tu kwenye kesi hiyo kutokana na maelezo ya nyongeza yaliyotoka kwa washitakiwa wenzake.

“Baada ya washitakiwa wote kupewa haki yao ya msingi ya kujitetea katika mahakama hii tukufu,hatukuweza kusikia hayo maelezo ya nyongeza yaliyofanya Zombe aunganishwe kwenye kesi hii.

“Jaji ili mahakama yako iweze kumtia hatiani kwa kosa kubwa kama hili mauji nilazima upande wa mashitaka uthibitishe bila kuacha shaka yoyote kesi yake.Hivyo basi upande wa mashitaka katika kesi hii umeshindwa kuthibitisha mashitaka manne ya mauji kwa Zombe kwa sababu zifuatazo:alidai Kimolo.

Sababu ya kwanza alieleza kuwa hakuna shahidi hata mmoja katika mashahidi 37 aliyedai Zombe kuwa alihusika.Pili, Tume zote zilizoundwa,hazikupendekeza mshitakiwa huyo wa kwanza ashitakiwa.Tatu, mpelelezi Mkuu wa kesi hiyo, SACP- Mkumbi naye alithibitisha kwamba Zombe aliunganishwa katika kesi hiyo kwa maelezo ya nyongezo yaliyotolewa na washitakiwa wenzake.

“Kwa maoni na mapendekezo yangu, naiomba mahakama hii imuone Zombe hana hatia kwa makosa ya mauji aliyoshitakiwa nayo” alidai Kimolo.

Kwa upande wake Magreth Mossi, akitoa maoni na mapendekezo yake kuhusu Zombe,alieleza kuwa ni ukweli usiopingika mashahidi wote wa upande wa mashitaka ,hakuna shahidi aliyeweza kuthibitisha shitaka hili kuhusu mshitakiwa huyo.

“Jaji, kuanzia kukamatwa kwa marehemu na hadi walipofikwa na umauti wao hata shahidi mmoja hakuweza kumnyoshea kidole Zombe kuwa alikuwepo eneo la tukio.Mahakama hii ilipokea ushahidi wa jinsi mshitakiwa huyo alivyokuwa akitoa taarifa alizokuwa amezipata kutoka kwa askari wake waliokuwa eneo la tukio” alidai Mossi.

Kuhusu hoja ya Zombe aliwapongeza askari kwamba ilionyesha alikuwa akifahamu tukio hilo, alidai ukweli usiopingika kiongozi yoyote anapoona askari wake wamefanyakazi ya ushupavu sio vibaya kutoa mkono wa pongezi,kwani alipata taarifa askari wake walikamata majambazi na silaha waliopora roli la kampuni ya Bidco.

“Naona hicho ndicho kilimfanya Zombe kutoa mkono wa pongezi na tume zote mbili zilioundwa , hazikumuona mshitakiwa huyo ana kesi ya mauji hivyo naungana na mzee wa baraza mwenzangu, kuiomba mahakama hii tukufu umuone mshitakiwa wa kwanza hana hatia” alidai Mosi, na kusababisha Zombe awe anajifuta machozi mara kwa mara kizimbani.

Kuhusu mshitakiwa 13, Festus Gwasabi, wazee hao wote kwa pamoja waliomba mahakama imuone hana hatia kwani ushahidi umeonyesha alishiriki katika upekuzi wa kwa marehemu wakati wakiwa hai Sinza Palestina, na baada ya zoezi hilo alipewa amri na mkubwa wake aendeshe gari la marehemu hao ambapo alipanda gari hilo na aliyekuwa mshitakiwa sita, Moris Nyangerela ambaye aliachiliwa huru na kulipeleka gari hilo kituo cha Urafiki.

Aidha walidai haya Gwasabi wakati akijitetea alikubali kushiriki kukamata na kuwapekua marehemu lakini aliamuriwa na mkuu wake apelike gari hilo Urafiki na mshitakiwa huyo alimleta shahidi wake, Nyangerela ambaye alikuja kudhibitisha hayo.

Hivyo wakaiomba mahakama hiyo itumie kifungu kile kile ilichokitumia kumwachia Nyangerela pia kitumike kumwachia Gwasabi na hivyo maoni na mapendekezo yao kwa mshitakiwa huyo wanaomba mahakama imwone hana hatia.

Wazee hao wakitoa maoni na mapendekezo yao dhidi ya mshitakiwa wa pili,SP-Christopher Bageni, wote kwa kauli moja wanakubaliana na upande wa mashitaka kwamba umeweza kudhibitisha kesi dhidi ya mshitakiwa na wakaiomba mahakama imuone ana hatia ya makosa anayoshitakiwa kwakuwa, ushahidi wa mazingira unaoyesha alitenda kosa hilo.

Kuhusu mshitakiwa tatu,SP- Ahmed Makelle, wazee hao kwa kauli moja waliomba mahakama imwone ana hatia kwasababu mashahidi wa upande wa mashitaka walimtambua mshitakiwa huyo alifika eneo la tukio na wakati mshitakiwa akijitetea alikiri kufika eneo la tukio na kwamba mashahidi hao walieleza walimtambua baada ya Makelle kuwa anagombea fuko la fedha.

Aidha wakitoa maoni yao kuhusu mshitakiwa wa tano, Jane Andrew,wazee hao pia waliomba atiwe hatiani kwani wanakubaliana na mashahidi wa upande wa mashitaka kwamba walimtambua kuwa ndiye aliyefika Sinza Palestina na alikuwa akigombea mfuko wa fedha.

Lakini katika hali isiyo tarajiwa na wengi, wakati wazee hao wa baraza walipomaliza kutoa maoni yao dhidi ya Mabula, Bageni, Makelle na Jane walikuwa wakiangua vicheko kizimbani.

Kuhusu mshitakiwa wa saba,Emmanuel Mabula, wazee hao pia walikubaliana na upande wa mshitaka kuwa umeweza kudhibitisha kesi kwa mshitakiwa huyo, kwani hakuna hata shahidi aliweza kuiambia mahakama siku ya tukio mshitakiwa huyo alipangiwa doria eneo la Makongo Juu.

“Mshitakiwa mwenyewe(Mabula) aliambia mahakama kuwa alikuwa ni miongoni mwa askari walioenda kupewa mkono wa pongenzi wa RCO-Zombe, huku akijua kuwa hakuwa hakuwa katika mapambano na majambazi lakini akakubali pongezi hizo, sisi tunasema aliku na lake jambo alilokuwa akilificha hivyo tunaomba hatiwe hatiani” alidai.

Wazee hao ambao walionyesha kujiamini wakati wakitoa mapendekezo yao, wakitoa maoni yao dhidi ya mshitakiwa tisa, Michael Shonza, walisema maoni yao kwa mshitakiwa hayo yanafanana na maoni waliyoyatoa kwa mshitakiwa saba, kwani siku ya tukio Mabula na Shonza walikuwa pamoja, hivyo wanameomba naye atiwe hatiani.

Aidha kuhusu mshitakiwa kumi, Koplo Abeneth Salo, wazee hao walisema baadhi ya mashahidi wa mashitaka walimtambua japo kuwa Januari 16/1/2006 Sinza Palestina alivalia nguo za kiraia na siku hiyo walimuona akiwa amekaa kwenye gari la mshitakiwa tatu(Makelle) ila mashahidi hao walimwona Jane na Makelle pale Sinza Palestina ila Abeneth alkuwa ndani ya gari.

Walikumbusha kuwa mshitakiwa 12(Rajabu) alieleza mshitakiwa tano(Jane) na Abeneth wote walifika barabara ya Samunujoma kwenye roli la Bidco, vile vile alimshuhudia Jane na Abeneth wakiondoka pamoja na gari la Makelle, na aliendelea kufahamisha mahakama kuwa gari hilo ndiyo lilikuwa la kwanza kuondoka .

Walisema Abeneth alipopewa haki ya kujitetea alidai yeye alishushwa Ubungo Terminal kwaajili ya kuendelea na doria na wala hakuweza kuleta shahidi ili adhibitishe madai hayo, hivyo walidai kushindwa kwa mshitakiwa huyo kufanya hivyo wanakubaliana na upande wa mashitaka kwamba wameweza kuthibitisha kesi dhidi yake na wakaiomba mahakama imwone ana hatia.

Aidha wazee hao wakichambua ushahidi wa mshitakiwa wa 12,Rajabu Bakari, walisema kwa hiari yake mwenye bila kulazimishwa na mtu yoyote ,mshitakiwa huyo akiwa ana akili timamu alikiri kuwa alikuwepo eneo la mauji msitu wa Pande na kwamba alipopewa haki ya kujitetea,mshitakiwa huyo alidai alikuwa chini ya amri ndiyo maana alikwenda katika msitu huo.

“Jaji huyu ni askari polisi na moja ya kazi ya majukumu yake ni kulinda usalama wa raia na mali zake,hivi kweli bosi wake anampa amri ya kuwa watu wasiyo na hatia, akanyamaza kimya?Mtukufu jaji huyu mshitakiwa anahusika moja kwa moja na tukio hili la mauji na tunaomba atiwe hatiani”alidai Magreth Mossi.

Baada ya wazee hao kuitimisha kutoa maoni na mapendekezo yao , Jaji wa Mahakama ya Rufani, Salum Massati, huo ndiyo mwisho wa kesi hiyo na kwamba hukumu ataitoa kutokana tarehe itakayopangwa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Mbali na Zombe, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni SP Christopher Bageni, SP Ahmed Makelle, Jane Andrew, Emmanuel Mabula, Michael Shonza, Koplo Abeneth Saro, Rajabu Bakari na Festus Gwasabi.

Zombe na wenzake, wanadaiwa kufanya mauaji hayo Januari 14 mwaka 2006, eneo la Mbezi Luis, katika msitu wa Pande, ambapo waliwaua Ephraim Chigumbi, Sabinus Chigumbi na Mathias Lukombe, ambao ni wafanyabiashara wa madini kutoka Mahenge, Ulanga na Juma Ndugu, ambaye ni dereva teksi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Juni 27 ,2009

SERIKALI YASISITIZA ZOMBE ANA HATIA

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa serikali katika kesi ya mauaji ya wafanyabiashara watatu na dereva teksi mmoja inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam (ACP), Abdallah Zombe na wenzake wanane, umejigamba kuwa umethibitisha kesi hiyo pasipo shaka, hivyo kuiomba mahakama kuwatia hatiani washitakiwa hao kwa makosa waliyoshitakiwa.


Akiwasilisha majumuisho ya kesi hiyo jana katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Wakili wa Serikali, Mugaya Mtaki aliyekuwa akisaidiana na Angaza Mwipopo, Alexander Msikila na Justus Kaishozi, alidai katika kuthibitisha kesi hiyo, walileta mashahidi 37 na kutoa vielelezo 23.

Akichambua ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo, Mtaki, alidai ushahidi uliotolewa na daktari umethibitisha kuwa marehemu hao walikuwa wamepigwa risasi na kuitaka mahakama kuondokana na dhana kwamba walipambana na polisi.

“Wakili wa utetezi, Majura Magafu, alitoa hoja ya kuwa hakukuwa na ubishi marehemu wote walikamatwa wakiwa hai. Sisi tunakubaliana na ukweli huo kwani umethibitishwa na shahidi wa 2, 6 na 7 wa upande wa mashitaka.

“Jambo jingine ambalo tunaomba mahakama yako ikubaliane na sisi kuwa halina ubishi, ni washitakiwa Zombe, Christopher Makele na Hemed Makele walikwenda Kituo cha Polisi Urafiki kushughulikia kielelezo cha fedha,” wakili wa serikali alimweleza Jaji Salum Massati.

Pamoja na hayo, wakili huyo aliiomba mahakama kuzingatia ushahidi wa mshitakiwa Makale uliodai Zombe ni muongo kwa kusema kuwa alikuwa hajui kilichokuwa kikitendeka, na kwamba yeye (Makele) aliandika taarifa za uongo kwa Tume ya Jaji Mussa Kipenka na ACP-Mgawe kwa maelekezo yake.

“Kwa muhtasari ushahidi huo ndiyo unamuhusisha Zombe kwa sababu alikuwa anajua tukio japo hakuwepo msitu wa Pande. Ni rai yetu Zombe aonekane na hatia kama washitakiwa wengine.

“Na hatua ya Msemwa (Wakili wa Zombe) kumfananisha Zombe na Yesu, kwamba anasulubiwa bila hatia, sisi tunasema mshitakiwa huyo hastahili kufananishwa na Yesu, kwani katika kesi ya Yesu, yule jaji wa Kirumi alikuwa na roho ya kikatili, ndiyo maana hakamtia Yesu hatiani licha ya Pilato aliuliza kuna ushahidi gani wa Yesu kutiwa hatiani.

“Katika kesi hii upande wa mashitaka tumethibitisha kesi yetu na wewe ni jaji unayesimamia haki, hivyo usifananishwe na jaji aliyemsulubu Yesu,” alidai Mtaki na kusababisha watu kuangua kicheko mahakamani.

Aliendelea kueleza kuwa, ushahidi wa utetezi unaonyesha kuwa Zombe hakuwapo msitu wa Pande, lakini alihoji ni kwa nini upande huo unashindwa kueleza wakati huo Zombe alikuwa wapi.

“Mtukufu Jaji, common intention siyo lazima washitakiwa wakae pamoja kupanga kabla ya kutenda kosa, kwa hiyo mahakama hii iuzingatie ushahidi uliotolewa kuwa washtakiwa wana hatia.

“Endapo Zombe na Gwasabi hawataonekana na hatia katika kesi ya mauaji, basi tunaomba washitakiwa hawa waonekane na hatia kwamba walishiriki kuficha kosa wakati likitendeka,” alieleza.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Salum Massati, aliwaasa wazee wa baraza, Magreth Mossi na Nicolas Kimolo, kutoa maoni yao kuhusu kesi hiyo kwa kuzingatia ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo.

Pia aliwataka kutozingatia yale yaliyoripotiwa na vyombo vya habari, kwani yameandikwa mengi kuhusu kesi hiyo. Leo wazee hao wa baraza wanatarajiwa kutoa maoni yao ya mwisho katika kesi hiyo.

Mbali na Zombe, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni SP Christopher Bageni, SP Ahmed Makelle, Jane Andrew, Emmanuel Mabula, Michael Shonza, Koplo Abeneth Saro, Rajabu Bakari na Festus Gwasabi.

Zombe na wenzake, wanadaiwa kufanya mauaji hayo Januari 14 mwaka 2006, eneo la Mbezi Luis, katika msitu wa Pande, ambapo waliwaua Ephraim Chigumbi, Sabinus Chigumbi na Mathias Lukombe, ambao ni wafanyabiashara wa madini kutoka Mahenge, Ulanga na Juma Ndugu, ambaye ni dereva teksi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima, Juni 26,2009

TUHARAKISHE KUTENGANISHA BIASHARA NA SIASA

Na Happiness Katabazi

HIVI karibuni kundi la wananchi wa Kijiji cha Sing’isi, wilayani Arumeru walivamia shamba la Mbunge wa Vunjo mkoani Kilimanjaro, Aloyce Kimaro (CCM), na kuchoma moto nyumba 20 na mazao mbalimbali yaliyokuwamo.


Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Basilio Matei, uharibifu huo mpaka hivi sasa unakadiriwa kusababisha hasara ya kiasi cha sh milioni 500.

Kamanda Matei ameahidi kuwa uchunguzi wa kujua thamani halisi ya mali zilizoteketea unaendelea na kuna uwezekano wa hasara kuongezeka.

Wakati uchunguzi huo ukiendelea tayari watu 86 wamekamatwa wakihusishwa na tukio hilo na 38 wameshafikishwa mahakamani na kusomewa mashitaka.

Naamini kuwa matukio ya namna hiyo yanayozidi kushamiri siku hadi siku ni matokeo ya mfumo wa kisiasa ulioparaganyika kiitikadi na kimaadili hapa nchini.

Kujinasibu kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ndani na nje ya nchi kuwa ni watetezi wa wanyonge, wakati hawatendi hicho wanachokisema, ni moja ya mambo yanayowafanya watu wachoshwe na kuamua kufanya mambo ambayo ni kinyume cha sheria.

Kuwapo kwa sera nzuri na mipango ya serikali isiyo na utekelezaji pamoja na viongozi kuhubiri kile wasichokitenda, hubomoa daraja la mawasiliano baina yao na wananchi.

Wananchi huona viongozi wao kama wasaliti na wanyonyaji wa rasilimali zao kwa kujilimbikizia mali nyingi ilhali maisha ya wananchi yakizidi kuwa magumu kadiri siku zinavyosonga mbele.

Tujiulize, viongozi wa kujilimbikizia mali wameingia kwa utashi wa kuwahudumia wananchi au wajinufaishe kibiashara kupitia mwamvuli wa siasa?

Kuchanganya biashara na siasa ni mtego unaotakiwa kuteguliwa kwa uangalifu zaidi, kwa kuwa hata ikulu hivi sasa imekuwa ikitumika kwa manufaa ya viongozi, fulani wasiozingatia maadili ya viongozi wa umma.

Tunaweza kuendelea kama viongozi wataweza kujiepusha na mgongano wa kimasilahi kama ambavyo tunaona kila kukicha.

Inawezekana vipi rais mfanyabiashara akubali muswada wa kuibana biashara anayoifanya yeye au familia yake?

Tukifanikiwa kutofautisha na kutenganisha biashara na siasa tutaweza kuwadhibiti viongozi mbalimbali, kuanzia ngazi za chini mpaka juu kujihusisha na biashara na hapo tunaweza kurejesha angalau maadili ya viongozi wa umma.

Nimefarijika baada ya kumsikia Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuwa kabla ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwakani sheria hiyo itakuwa imeshaanza kufanya kazi.

Mifumo ya kiutendaji ndiyo inayowafanya wananchi kujiona ni wakimbizi katika ardhi yao, hatuna sababu za kuzidisha pengo kati ya walionacho na wasionacho ambalo mwisho wa siku ni vurugu miongoni mwa jamii.

Wananchi wanapenda viongozi wao washiriki katika shughuli za kilimo au nyingine za uzalishaji mali, lakini wasingependa kuona viongozi hao wanatumia madaraka yao kujineemesha.

Tusingependa nchi ikumbane na matatizo ya ardhi kama yale tunayoyaona Zimbabwe, Sudan na kwingineko.

Sina haja kuuhisha uvamizi wa Kimaro na itikadi za kisiasa, lakini ni vizuri dola ikaendesha jambo hilo bila kuingiza utashi wa kisiasa ili haki ipatikane.

Kimaro na kiongozi mwingine yeyote kwa hivi sasa hawazuiwi kufanya biashara, hivyo ni vema kwa wakati huu wakapatiwa ulinzi wa kisheria.

Mwisho, nimalizie kwa kuitaka serikali iliyo madarakani chini ya Chama Cha Mapinduzi iachane na utawala wa kiimla na mfumo wa kuwindana kama ule wa paka na panya.

Kama wataendelea na utaratibu huu, basi mbele ya safari hali itakuwa mbaya zaidi na tutabaini yupi ni panya na yupi ni paka.


Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Juni 21, 2009

MAPAPARAZI WA MAHAKAMA:ACP-KENYELA KARIBU TENA KORTI YA KISUTU


Kushoto, Happiness Katabazi Mwandishi wa Gazeti la Tanzania Daima na (kulia) ni mwandishi wa Gazeti la Uhuru, Furaha Omar, tukiwa tumepiga picha ya kumbukumbu na ACP-Charles Kenyela, jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, iki ni sekunde chache baada ya (njagu) huyo kufika katika mahakama hiyo kwa shughuli za kikazi alilakiwa kwa furaha na waandishi wa habari za Mahakamani.
Awali Kenyela ndiye alikuwa Mkuu wa Waendesha Mashitaka Kanda ya Dar es Salaam lakini hivi sasa ameamishiwa Makao Makuu ya Polisi Kanda Polisi jijini, kama Mkuu Kitengo cha Fedha.(Picha imepigwa Juni 16,2009)

LIYUMBA KIZUNGUMKUTI

*Mahakama Kuu yatengua kumlegezea masharti
*Yatoa masharti mapya ya dhamana ya bil 110/-

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetengua uamuzi uliotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wa kulegeza masharti ya dhamana kwa aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba.

Aidha, mahakama hiyo imetoa masharti mapya ya dhamana kwa Liyumba na kuutaka uongozi wa Mahakama ya Kisutu usimamie utekelezwaji wake badala ya jukumu hilo kuachiwa Hakimu Mkazi Nyigulila Mwaseba kwa madai kuwa amepotosha matakwa ya kifungu 148(5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Uamuzi huo ulitolewa jana saa tatu asubuhi na Jaji Geofrey Shaidi baada ya kusikiliza hoja za upande wa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Eliezer Feleshi uliowakilishwa na wakili kiongozi wa serikali, Justus Mulokozi na John Rwabuhanga pamoja na upande wa mjibu rufaa (Liyumba) uliowakilishwa na mawakili wa kujitegemea; Majura Magafu, Hudson Ndyusepo na Onesmo Kyauke.

Jaji Shaidi alisema ametengua uamuzi wa Mahakama ya Kisutu uliotolewa na hakimu mkazi Mwaseba ambaye alilegeza masharti ya dhamana dhidi ya Liyumba kwani uamuzi wa mahakama hiyo umepotosha matakwa ya kifungu hicho cha 148(5)(e) ya CPA mwaka 2002.

Alisema kifungu hicho kipo wazi na kinamtaka mshitakiwa kutoa fedha au nusu ya mali anayotuhumiwa kuiba.

“Mengi yamesemwa kuhusu kifungu hicho, pande zote mbili katika shauri hili wamekubaliana, na lugha iliyotumika katika kifungu hicho haina utata wowote, hivyo sina tatizo na tafsiri ya neno fedha.

“Nakubaliana na tafsiri ya neno fedha iliyotolewa na Mulokozi, ambaye tafsiri yake aliinukuu kutoka kwenye kifungu Na.5 cha Kanuni ya Adhabu inayosema fedha maana yake ni ‘warrants’, ‘funds’, ‘bank cheque’, ‘current notes or request of payment’.

“Naomba ieleweke wazi kwamba kifungu hicho hakijataja kosa lolote moja kwa moja, kwani kinatamka kuwa mtu anayeshitakiwa kwa kosa lililohusisha fedha au mali ambayo inazidi sh milioni 10, atalazimika kutoa fedha au nusu ya mali anayotuhumiwa kuiba.

Hivyo kifungu hiki kinapaswa kitumike kwenye kesi inayomkabili Liyumba,” alisema Jaji Shaidi.

Kuhusu hoja ya mawakili wa utetezi iliyokuwa ikiomba mahakama hiyo isikubaliane na matumuzi ya kifungu hicho, kwani kinatumika kwenye makosa ya wizi na kujipatia mali kwa njia ya udanganyifu, alisema:

“Kwa heshima na taadhima kabisa, sikubaliani na ombi hilo la mawakili wa utetezi, kwani halina msingi wowote kwenye macho ya sheria na endapo ningekubaliana nalo, nami ningekuwa natafsiri vibaya, na katika uelewa wangu shitaka linalomkabili Liyumba ni kusababisha hasara baada ya kuongeza kiwango cha fedha katika mradi wa ujenzi wa minara pacha bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa BoT, hivyo kusababisha hasara ya sh bilioni 221 mali ya BoT.”

Alisema kwa sababu hiyo kiwango kilichoipatia BoT hasara ni fedha na wala siyo makisio ya kifedha kama ilivyodaiwa na mawakili wa utetezi.

“Mwaseba alikosea kusema kifungu hicho cha 148(5)(e) cha CPA, hakiendani na makosa anayokabiliwa nayo mshitakiwa, na kwamba usemi huo kamwe haukubaliki kwenye macho ya sheria…na kifungu hiki bado ni kifungu halali cha sheria na kitaendelea kutumika kama kilivyo,” alisema Jaji Shaidi huku akionyesha kukerwa na uamuzi huo.

Akijibu hoja ya utetezi iliyodai kuwa kifungu hicho kinakwenda kinyume na katiba ya nchi inayotoa uhuru wa mtu binafsi kuwa huru, jaji huyo aliwataka mawakili hao wafuate utaratibu wa kuhoji sheria na kwamba katika rufaa hiyo si mahali pake.

“Nasisitiza kifungu hicho kipo wazi na ninaamuru kitumike ipasavyo kama nilivyotoa sababu hapo juu, hivyo nakubaliana na rufaa ya DPP na ninatengua uamuzi wa Mahakama ya Kisutu kwani ulitafsiri vibaya matumizi na matakwa ya kifungu hicho.

“Ninaelekeza Mahakama ya Kisutu impatie dhamana Liyumba kwa kuzingatia masharti ya kifungu hicho, yaani atoe fedha taslimu au hati ya mali inayolingana na nusu anayotuhumiwa kusababisha hasara ambapo nusu itakuwa sh bilioni 110.

“Liyumba asalimishe hati ya kusafiria kwa Mkuu wa Polisi Kanda ya Dar es Salaam, asisafiri nje ya mkoa huu bila kibali cha mahakama. Utekelezaji huu ufanywe na Mahakama ya Kisutu na si Hakimu Mkazi Nyigulila Mwaseba ambaye mahakama imemwona alitafsiri vibaya kifungu hicho,” alisema Jaji Shaidi.

Baada ya umuzi huo kutolewa, Magafu aliwasilisha ombi la kutaka kukata rufaa dhidi ya uamuzi huo, lakini jaji huyo alimjibu kwa mkato kwa kumtaka apeleke maombi hayo kwa njia ya maandishi.

“Mheshimiwa Jaji sisi tutakata rufaa haraka iwezekanavyo na tunaomba utusikilize maombi yetu haya kwa njia ya mdomo, kwani sheria inakutaka wewe jaji utusikilize kwa njia ya mdomo na tunaomba ombi hili uliweke kwenye rekodi zako,” alizungumza kwa jazba wakili Magafu.

Akijibu, Jaji Shaidi alisema: “Nipo tayari nendeni mkakate rufaa, lakini Magafu nimekwambia nendeni kisha mlete ombi lenu hilo kwa maandishi na si vinginevyo.”

Wiki iliyopita, Wakili Kiongozi wa Serikali, Mulokozi, aliiambia mahakama hiyo kuwa, DPP hakuridhishwa na uamuzi wa Mahakama ya Kisutu na ndiyo maana wameamua kukata rufaa.

Aliongeza kuwa, rufaa yao ipo katika sehemu kuu mbili. Mosi, wanaamini Mwaseba alikosea kutoa dhamana bila kuzingatia kifungu hicho; pili hakimu huyo alipotosha matakwa ya kifungu hicho.

Huku akionyesha kujiamini, Mulokozi alianza kwa kuichambua sababu ya pili, kuwa shitaka linalomkabili mjibu rufaa ni kusababisha hasara na kwa mujibu wa maelezo ya kosa yanaonyesha kuwa makosa hayo aliyafanya akiwa ni mtumishi wa umma kwani alizidisha kiwango cha fedha za ujenzi wa minara pacha (Twin Towers) bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa BoT.

“Mtukufu Jaji, mradi wa ujenzi wa minara pacha, kiwango cha fedha kiliainishwa rasmi, lakini Liyumba akiwa mtumishi wa benki hiyo alikizidisha kiwango kingine cha fedha na kwa kitendo chake hicho mwenye mali ambaye ni BoT aliingia hasara ambayo ni fedha halisi, hivyo tunaomba kifungu hicho kitumike kuamua dhamana ya Liyumba,” alidai Mulokozi.

Aidha, alidai kuwa maana halisi ya kifungu cha 284(a)(6) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, inatamka wazi endapo mahakama inapomtia hatiani mshitakiwa, kwa kuanzia, mahakama hiyo itachukua fedha taslimu au hati ya nusu ya mali iliyowekwa na mshitakiwa kama dhamana.

“Kwa hiyo, kwa kifungu hicho cha 284(a)(6) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, sisi tunasema kinasaidia utekelezaji wa masharti yanayotamkwa katika kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai 2002.

“Hivyo, tunaomba Mahakama Kuu iingilie kati kutafsiri kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Makosa ya Jinai kisha itengue uamuzi wa Mahakama ya Kisutu kwa sababu kifungu hicho ndicho kinapaswa kitumike kwenye dhamana ya mshitakiwa,” alidai Mulokozi.

Mei 28 mwaka huu, Mwaseba alitangaza kumwachia Liyumba kwa dhamana ya sh milioni 300 badala ya sh bilioni 110 kama ilivyotakiwa na kifungu hicho cha sheria, wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh milioni 50 kila mmoja, zuio la kutoka nje ya Dar es Salaam hadi kwa kibali maalum na kusalimisha hati ya kusafiria mahakamani.

Masharti hayo ni tofauti na yale ya awali, alipotakiwa kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, ambao wangesaini bondi au kuwasilisha hati yenye thamani ya nusu ya kiasi cha sh bilioni 221, anachotuhumiwa kuisababishia serikali hasara.

Hata hivyo, uamuzi wa kulegezewa masharti ya dhamana, ulimfanya Liyumba apumue, hasa pale Hakimu Mwaseba aliposema amesikiliza hoja za pande zote mbili na kulazimika kukubaliana na hoja za mawakili wa utetezi kwamba, ni kweli kifungu hicho kamwe hakipaswi kutumika katika mashitaka mapya yanayomkabili mshitakiwa huyo.

Liyumba anakabiliwa na makosa mawili ya jinai katika kesi namba 105/2009 kwa matumuzi mabaya ya ofisi ya umma ambapo anadaiwa kuwa kati ya mwaka 2001-2006 akiwa mwajiriwa wa serikali, aliidhinisha ujenzi wa minara pacha, bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu.

Aidha, anadaiwa kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 kwa uamuzi wake wa kuidhinisha ujenzi wa minara hiyo pacha kosa linaloangukia kwenye shitaka la kwanza.

Liyumba alisomewa mashitaka mapya baada ya Hakimu Mkazi Walirwande Lema, aliyekuwa akisikiliza kesi namba 27/2009 iliyokuwa ikimkabili mshitakiwa huyo na Meneja Miradi wa BoT, Deogratius Kweka, kuwaachia huru baada ya kubaini hati ya mashitaka ilikuwa ina makosa kisheria.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye, walikamatwa tena na Liyumba kusomewa mashitaka mapya, na Kweka kuachiliwa huru.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Juni 16,2009

VIGOGO DECI KIZIMBANI

*Wanadaiwa kuendesha shughuli za upatu bila leseni
*Watupwa rumande, ndugu zao waangua kilio kortini
*Kamati ya dharura DECI sasa wapanga kuandamana

Na Happiness Katabazi

BAADA ya vuta nikuvute kati ya viongozi na wanachama wa Kampuni Development Entrepreneurship for Community Initiative (DECI), inayojihusisha na shughuli za kuvuna na kupanda pesa, hatimaye jana viongozi watano wa kampuni hiyo, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijni Dar es Salaam.

Viongozi hao walifikishwa mahakamani hapo, majira ya saa nane mchana, chini ya ulinzi wa askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) ambao waliambatana na makachero wa polisi kutoka Makao Makuu ya Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam na Makao Makuu ya Upelelezi ya jeshi hilo.

Kwa mujibu wa taarifa za kuaminika toka ndani ya jeshi hilo, watuhumiwa hao walikamatwa tangu juzi na kuchukuliwa maelezo na hatimaye jana kufikishwa mahakamani.

Wakili Kiongozi wa Serikali, Justus Mlokozi, akisaidiana na Prosper Mwangamila, mbele ya Hakimu Mkuu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Addy Lyamuya, alidai kuwa washitakiwa wote ni wachungaji wa Kanisa la Pentekoste.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Jackson Sifael Mtares, Dominick Kigendi, Timotheo Saigaran ole Loitginye, Samwel Sifael Mtares, Arbogast Francis Kipilimba na Samwel Mtalis.

Washitakiwa hao ambao walirudishwa rumande, wanatetewa na mawakili wa kujitegemea Simon Kitululu, Onesmo Michael, Shambwee Shitambala na Hudson Ndusyepo.

Kwa mujibu wa Mwangamila, washitakiwa hao wanakabiliwa na mashitaka mawili ambayo ni kuendesha na kusimamia mradi wa upatu kinyume na kifungu 111A(1,3) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16.

Alidai kuwa, kati ya mwaka 2007 na Machi 2009, katika makao makuu ya DECI, yaliyopo Mabibo Mwisho, jijini Dar es Salaam, washitakiwa waliendesha na kusimamia mradi wa upatu katika sehemu tofauti nchini kwa ahadi ya kuwapa wanachama wake fedha zaidi ambazo katika mazingira ya kibiashara ni kubwa kuliko mradi waliokuwa wakiufanya.

Mwangamila alidai kuwa, shitaka la pili ni kupokea amana za umma bila kuwa na leseni kinyume na kifungu cha 6(1,2) cha Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha Na.5 ya mwaka 2006 na kwamba, washitakiwa wote katika kipindi hicho, wakiwa kwenye ofisi zao za DECI, walipokea amana kutoka kwa umma bila leseni.

Washitakiwa wote walikana mashitaka hayo na wakili huyo wa serikali alidai kuwa upelelezi bado haujakamilika na kuomba tarehe ya kutajwa kesi hiyo.

Hata hivyo, wakili wa utetezi, aliomba wateja wake wapewe dhamana kwa kuwa ni wakazi wa Jiji la Dar es Salaam na ni wachungaji wa dhehebu la Pentekoste.

Ombi hilo lilipingwa na wakili kiongozi wa serikali, Mulokozi na kutoa hati ya kiapo cha mpelelezi mkuu wa kesi hiyo, Kamishna Msaidizi wa Polisi, Essack Mugassa ambacho kinataka washitakiwa wasipewe dhamana.

Alidai kuwa, endapo washitakiwa hao watapewa dhamana, wanaweza kuvuruga upelelezi na kuongeza kwamba tayari wameshawapatia upande wa utetezi hati hiyo ya kiapo.

Kesi hiyo inayovuta hisia za wengi, imeahirishwa hadi Juni 17 na washitakiwa wote walirejeshwa rumande.

Wakati washitakiwa hao wakipandishwa kwenye karandinga tayari kwa ajili ya kupelekwa rumande, baadhi ya ndugu na jamaa zao waliokuwa kwenye viunga vya mahakama hiyo, walishindwa kuvumilia na kuanza kuangua kilio, huku ndugu wengine pamoja na baadhi ya wanachama, wakiwa wamekaa vikundi wakitafakari hali hiyo.

Mapema mwaka huu, Kampuni ya DECI iliyowanufaisha watu wengi hasa wale waliojiunga mwanzoni, iliibua malumbano kati ya serikali, viongozi wa kampuni hiyo na wanachama wao, waliopinga hatua ya serikali kusitisha shughuli zake kwa madai kuwa haiko kihalali.

Kusimamishwa kwa shughuli za kampuni hiyo, kulitokana na uamuzi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kutoa taarifa ya kuwataadharisha Watanzania waliojiunga na upatu huo kuwa, taasisi hiyo haiko kisheria na wanaweza kupoteza fedha zao walizopanda.

Shughuli za kupanda na kuvuna mbegu DECI, zilisitishwa baada ya serikali kusimamisha akaunti za kampuni hiyo hadi hapo uchunguzi utakapokamilika, hali ambayo baadaye ilisababisha uvunjifu wa amani katika ofisi za kampuni hiyo, baada ya wanachama wake kuamua kuchukua sheria mkononi kwa kuvunja vioo vya magari ya viongozi, wakitaka warejeshwe fedha zao.

Katika hatua nyingine, kamatai ya dharura ya wanachama wa DECI, wamefanya kikao cha ghafla jana mara baada ya viongozi wao kutupwa rumande, wakipinga hatua hiyo.
Kamati hiyo inayoongozwa na Isack Kalenge, inawataka wanachama wa DECI nchi nzima kuandamana Jumatano ijayo ili kuishinikiza serikali kuwaachia huru viongozi wao.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Juni 13, 2009

KORTI KUU KUAMUA DHAMANA YA LIYUMBA JUNI 15

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imesema Juni 15 mwaka huu, itatoa uamuzi wake kuhusu rufaa ya Mkurugenzi Mashitaka(DPP),Eliezer Feleshi, dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi wa Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba, ya kupinga uamuzi wa kulegezewa masharti ya dhamana.


Jaji Geofrey Shaidi ambaye jana alisikiliza rufaa hiyo sambamba na kusikiliza hoja za upande wa DDP na mawakili wa mjibu rufaa ,na kwamba anairisha shauri hilo tarehe hiyo ambapo atakuja kutoa uamuzi kulingana na malumbano ya kisheria yaliyozuka wakati akisikiliza hoja hizo.

“Nimesikiliza kwa kina hoja zote hivyo naomba namimi mnipe muda hadi Juni 15 mwaka huu, saa tatu asubuhi,tukutane pale ukumbi namba moja katika mahakama hii,kwani siku hiyo ndiyo nitautumia kutolea uamuzi wa rufaa hii namba 44/2009” alisema Jaji Shaidi.

Awali jana asubuhi Wakili Mwandamizi wa Serikali Justus Mlokozi akiksaidiana na John Rwabuhanga alianza kwasema hakuliridhishwa na uamuzi huo ndiyo maana wameamua kukata rufaa kwasababu kuu mbili,mosi,wanaamini Mwaseba alikosea kutoa dhamana bila kuzingatia kifungu hicho,pili hakimu huyo alipotosha matakwa ya kifungu hicho.

Huku akionyesha kujiamini, Mulokozi alianza kwa kuichambua sababu ya pili,alidai kuwa shitaka linalomkabili mjibu rufaa ni kusababisha hasara na kwamujibu wa maelezo ya kosa yanaonyesha kuwa kakosa hayo aliyafanya akiwa ni mtumishi wa umma kwani alizidisha kiwango cha fedha cha ujenzi wa Minara Pacha”Twin Towers” bila idhini ya mwenye mali ambaye ni BoT.

“Mtukufu Jaji mradi wa ujenzi wa ujenzi wa Minara Pacha kiwango cha fedha kilichoanishwa rasmi lakini Liyumba akiwa mtumishi wa benki hiyo alikizidisha kiwango kingine cha fedha na kwa kitendo chake hicho mwenye mradi mali ambaye ni BoT aliingia hasara ambayo ni fedha halisi:

‘Hivyo basi katika misingi hiyo shitaka lililopo katika kesi ya msingi pale Kisutu hiki kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 ,kinatakiwa kitumike kikamilifu katika kuamua dhamana ya Liyumba na sivinginevyo.” alidai Mulokozi huku akionyesha kujiamini.

Mulokozi ambaye jana alilazimika kutumia kifungu cha 5 cha Sheria Kanuni ya Adhabu ili kutetea hoja yake, alidai kuwa kifungu hicho kinatoa tafsiri maana ya neno fedha ambapo alisema kwa mujibu wa kifungu hicho kinasema fedha maana yake warrants,funds,hundi ya benki,current notes or request of payment .

“Kwa tafsri hiyo haina maana neno fedha taslimu peke yake kama ilivyodaiwa na Mwaseba kwahiyo hakimu huyo tunaamini kabisa hakimu huyo alipotoka kusema shitaka la kusababisha hasara halihusiani na fedha taslimu” alidai Mulokozi.

Aidha alidai maana halisi ya kifungu cha 284(a)(6) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu,inatamka wazi endapo mahakama inampomtia hatiani mahakama inaanza kuchukua ile nusu ya mali iliyowekwa mahakama na mshitakiwa kama dhamana.

“Kwahiyo kifungu hicho cha 284(a)(6) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kwahiyo sisi tunasema kifungu hicho kinasaidia utekelezaji wa masharti yanayotamkwa katika kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai 2002.

“Kwa hiyo tunaomba Mahakama Kuu iingilie kati kutafsiri kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Makosa ya Jinai kisha itoe itengue uamuzi mahakama ya Kisutu kwasababu kifungu hicho ndicho kinapaswa kitumike kwenye dhamana ya mshitakiwa’ alidai Mulokozi.

Kwa upande wake mawakili wa utetezi Onesmo Michael na Majura Magafu waliendelea kusisitiza msimamo wao kuwa uamuzi wa kulegezwa kwa masharti ya dhamana uliotolewa na mahakama ya Kisutu ni sahii na kutaka rufaa ya DPP itupiliwe mbali.

Mei 28 mwaka huu,Mwaseba alitangaza kumwachia kwa dhamana ya sh milioni 300 badala ya sh bilioni 110 kama ilivyokuwa awali,wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh milioni 50 kila mmoja, zuio la kutoka nje ya Dar es Salaam hadi kwa kibali maalum na kusalimisha hati ya kusafiria mahakamani.

Masharti hayo ni tofauti na yale ya awali, alipotakiwa kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, ambao wangesaini bondi au kuwasilisha hati yenye thamani ya nusu ya kiasi cha sh bilioni 221, anachotuhumiwa kuisababishia serikali hasara.

Sharti lingine la awali, lilikuwa ni kuacha hati za kusafiria mahakamani hapo, kuripoti katika ofisi za Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kila Ijumaa na zuio la kutoka nje ya Dar es Salaam bila ya kibali maalum cha mahakama.

Hata hivyo, uamuzi wa kulegezewa masharti ya dhamana, ulimfanya Liyumba apumue, hasa pale Hakimu Maseba aliposema amesikiliza hoja za pande zote mbili na kulazimika kukubaliana na hoja za mawakili wa utetezi kwamba, ni kweli kifungu hicho kamwe hakipaswi kutumika katika mashitaka mapya yanayomkabili mshitakiwa huyo.

Liyumba anakabiliwa na makosa mawili ya jinai katika kesi namba 105/2009 kwa matumuzi mabaya ya ofisi ya umma ambapo anadaiwa kuwa kati ya mwaka 2001-2006 akiwa mwajiriwa wa serikali, aliidhinisha ujenzi wa minara pacha, bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu.

Aidha, anadawa kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 kwa uamuzi wake wa kuidhinisha ujenzi wa minara hiyo pacha kosa linaloangukia kwenye shitaka la kwanza.

Liyumba alisomewa mashitaka mapya baada ya Hakimu Mkazi Walirwande Lema, aliyekuwa akisikiliza kesi namba 27/2009 iliyokuwa ikimkabili mshitakiwa huyo na Meneja Miradi wa BoT, Deogratius Kweka, kuwaachia huru baada ya kubaini hati ya mashitaka ilikuwa ina makosa kisheria.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye, walikamatwa tena na Liyumba kusomewa mashitaka mapya, huku Kweka akiendelea kuhojiwa na Takukuru.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi,Julai 11,2009

WATUHUMIWA WA UVUVI WA MELI HARAMU WACHARUKA MAHAKAMANI

Na Happiness Katabazi

RAIA 32 wa kigeni ambao Machi mwaka huu, walikamatwa kwenye meli ya Tawariq 1 wakifanya uvuvi haramu katika Bahari ya Hindi ambao wanakabiliwa na kesi ya uvuvi haramu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jana walicharuka mahakamani hapo na kutishia kuanza mgomo wa kutokula chakula.


Hali hiyo ambayo haikutarajiwa ilitokea jana mahakamani hapo mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema, ikiwa ni takribani sekunde chache tangu hakimu huyo aseme kuwa hataweza kuandika kurekodi chochote kwasababu jarada la kesi ya washitakiwa bado lipo Mahakama Kuu na kwamba anaairisha kesi hiyo hadi Juni 23 mwaka huu, na wakili wa serikali Rose Chilongola kuanza kuondoka

Baada hakimu huyo kusema hayo washitakiwa wote walinyosha vidole juu huku wakisema kwa lugha ya Kiingereza kama ilivyotafrisiliwa na gazeti hili kwa lugha ya Kiswali‘no no no’.

“Tangu mapema Machi mwaka huu tupo rumande hakutajapa dhamana wala kutolewa uamuzi wa vigezo gani tutizimize tupate dhamana sisi tunateseka,hatutendewi haki na nchi hii kwani hata kama kweli tumekamatwa tunavua samaki kwenye ardhi ya Tanzania bila kibali tunaomba tupatiwe dhamana ili tuweze kufanya mambo mengine kwani sisi pia tuna haki ya kupata dhamana kwa wakati.Na tumeamua sisi sote washitakiwa kuwa kitu kimoja hadi haki itendeke’alidai mshitakiwa huyo.

Na kwa upande wa wakili wa washitakiwa ho Elias Nawela alidai kuwa anashangazwa hadi kufikia jana jarada la kesi kutokuwa limefika Mahakama ya Kisitu kwani tayari Mahakama Kuu ilishalitolea uamuzi.

Hata hivyo Lema baada ya kusikiliza malalamiko ya washitakiwa hao ambao awali walidai hawafahamu lugha ya Kiingereza lakini jana waliitumia kufikisha kilio chao, alisema anawaidi atakapomaliza kusikiliza kesi alizokuwa akizikiliza jana atafuatilia jarada hilo Mahakama Kuu.

Mei mwaka huu, upande wa mashitaka katika kesi hiyo ulipeleka jarada la kesi hiyo Mahakama Kuu, ili mahakama hiyo iamuru samaki hao wauzwe au la , Jaji Gerofrey Shaidi katika uamuzi wake kuhusu ombi hilo alisema hilo siyo jukumu la mahakama na kuwa jukumu hilo ni la Maofisa Uvuvi.

Washitakiwa hao ni mabaharia, Jiojwen Chang (34), Jia Yin Zhao 26), Gexi Zhao (36), Zongmin Ma (36), Dong Liu (25), Yongiao Fang (22), Nguyen Tuan(23), Hsu Sheng Pao (55), Zhao Hanquing (39), Zho Hanging (39) ambaye wote ni wakala na raia wa China.

Wengine ni Tran Van Phuon (33), Pham Dinn Suong (31), Tran Van Thanh (23), Cao Vuong (27), Kristofer Padilla (29) raia wa Vietnam. Wengine ni Mohamed Kiki (61), Anul Mani (24) raia wa Taiwani.

Aidha, Wakili Mganga alisema washtakiwa wengine ni Jejen Priyana (22), Kuntoto Suratno (27), Tusi Ame (25), Ifan Herman Pandi (21), raia wa Indonesia, Silvano Garanes (32), Benjie Rosano (34), Ignacio Dacumos (31), Marlon Maronon (33), Jhoan Belano (34), Rolando Nacis (35) raia wa Philipins, Wakati Ali Ali Mkota (32), Juma Juma Kumu (40), Jackson Toya(39) raia wa Kenya.

Machi 10 mwaka huu, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa washtakiwa wote wanakabiliwa na mashtaka mawili, shitaka la kwanza ni kuvua samaki bila leseni kinyume na sheria ya Uvuvi wa Samaki katika kina kirefu ya mwaka 2009.

Alidai Machi 8 mwaka huu, washtakiwa wote kwa pamoja, saa sita usiku katika ukanda wa bahari ya Hindi ndani ya eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, walikamatwa wakiwa wakivua samaki bila leseni.Na washtakiwa wote walikana mashtaka na wapo rumande kwaajili ya wameshindwa kutimiza masharti dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Julai 11, 2009

MAHAKAMA:MARANDA ANA KESI YA KUJIBU

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, imesema Mweka Hazina wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kigoma Rajabu Maranda na mpwawe, Farijala Hussein, wanaokabiliwa na kesi ya wizi wa sh bilioni 1.8 za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), mali ya Benki Kuu ya Tanzania, (BoT), wana kesi ya kujibu.


Uamuzi huo ambao ni wa kwanza kutolewa katika kesi za EPA zaidi ya saba zilizofunguliwa mahakamani hapo, ulitolewa jana na jopo la mahakimu wakazi watatu, Cypriana William, Saul Kinemela na Phocus Bampikya wa mahakama hiyo.

Akisoma uamuzi huo kwa niaba ya jopo hilo, Bampikya ambaye ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, alianza kusoma majumuisho ya ushahidi uliotolewa wiki iliyopita na kumalizia majumuisho ya ushahidi uliowasilishwa na Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface.

“Jopo hili baada ya kupitia kwa makini majumuisho ya pande hizo mbili katika kesi hii namba 1161/2008, kwa kauli moja limekubaliana na majumuisho ya ushahidi yaliyotolewa Ijumaa iliyopita na upande wa mashitaka, kwamba washitakiwa wana kesi ya kujibu,” alisema.

Baada ya kumaliza kusoma uamuzi huo, wakili wa utetezi, Majura Magafu, aliiomba mahakama itoe amri ya kupatiwa nakala ya uamuzi huo ili ajue hoja zilizotumiwa na mawakili wa upande wa mashitaka na kujipanga kwa utetezi.

Alidai kuwa, wanatarajia kuleta mashahidi kumi na washitakiwa wenyewe watatoa ushahidi, hivyo kufanya idadi ya mashahidi katika upande wa utetezi kuwa 12. Hata hivyo, alikataa kutaja majina ya mashahidi hao.

Mahakama ilikubali ombi la Magafu na kuahirisha kesi hiyo hadi Juni 24, itakapokuja kwa ajili ya kutajwa na kupangiwa tarehe ya kuanza kusikilizwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamis, Juni 11,2009

DPP ALIA NA LIYUMBA

*Apinga kupunguziwa masharti ya dhamana
*Amtuhumu hakimu kwa kupotosha ukweli

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, leo inaanza kusikiliza rufaa iliyokatwa na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Eliezer Feleshi, dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba, kupinga uamuzi wa kulegezewa masharti ya dhamana.


Rufaa hiyo namba 44 ya mwaka 2009, itasikilizwa mbele ya Jaji Geofrey Shaidi.
Katika maombi yake, DPP anapingana na uamuzi uliotolewa Mei 28 na Hakimu Mkazi Nyigumalila Maseba wa Mahakama ya Kisutu Dar es Salaam, wa kumpunguzia masharti ya dhamana mtuhumiwa huyo.

Katika maelezo yake, DPP amebainisha kwamba, Hakimu Maseba, amepotosha na kukiuka matakwa ya kifungu cha 148 kifungu kidogo cha 5E cha sheria za makosa ya jinai iliyorekebishwa mwaka 2002, inayomlazimu mtuhumiwa kulipa kama dhamana, nusu ya mali anayodaiwa kuiba.

Kwa mujibu wa hakimu huyo, aliieleza mahakama kwamba, kifungu hicho hakiangukii kwenye makosa yanayomkabili Liyumba. Hivyo alitangaza kumwachia kwa dhamana ya sh milioni 300 badala ya sh bilioni 50 kama ilivyokuwa awali.

Kabla ya kusoma uamuzi wake kwa Liyumba anayekabiliwa na tuhuma za matumizi mabaya ya ofisi na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221, Hakimu Maseba, alikumbusha kuwa katika shauri hilo dhamana ilikuwa haibishaniwi bali kilichokuwa kikibishaniwa ni masharti ya dhamana.

“Kwa uamuzi huu, Liyumba sasa atatakiwa atoe fedha taslimu au hati ya mali yenye thamani ya sh milioni 300, wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh milioni 50 kila mmoja, zuio la kutoka nje ya Dar es Salaam hadi kwa kibali maalum na kusalimisha hati ya kusafiria mahakamani,” alisema.

Masharti hayo ni tofauti na yale ya awali, alipotakiwa kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, ambao wangesaini bondi au kuwasilisha hati yenye thamani ya nusu ya kiasi cha sh bilioni 221, anachotuhumiwa kuisababishia serikali hasara.

Sharti lingine la awali, lilikuwa ni kuacha hati za kusafiria mahakamani hapo, kuripoti katika ofisi za Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kila Ijumaa na zuio la kutoka nje ya Dar es Salaam bila ya kibali maalum cha mahakama.

Hata hivyo, uamuzi wa kulegezewa masharti ya dhamana, ulimfanya Liyumba apumue, hasa pale Hakimu Maseba aliposema amesikiliza hoja za pande zote mbili na kulazimika kukubaliana na hoja za mawakili wa utetezi kwamba, ni kweli kifungu hicho kamwe hakipaswi kutumika katika mashitaka mapya yanayomkabili mshitakiwa huyo.

Alisema, hakuna ubishi kwamba mashitaka yanayomkabili Liyumba ni yale ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia hasara serikali ya sh bilioni 221, hivyo mashitaka hayo ni tofauti kabisa na yanayoainishwa kwenye kifungu hicho.

“Nakubaliana na hoja za mawakili wa utetezi kuwa, kifungu hicho kamwe hakipaswi kutumika katika mashitaka yanayomkabili mshitakiwa na kwa sababu hiyo, natupilia mbali ombi la upande wa mashitaka lililotaka mahakama hii itumie kifungu hicho katika kumpatia dhamana mshitakiwa na endapo upande wa mashitaka haujaridhika na uamuzi wake, unaweza kukata rufaa,” alisema Maseba Mei 29 katika Mahakama ya Kisutu na kusababisha mawakili wa serikali kujiinamia.

Liyumba anakabiliwa na makosa mawili ya jinai katika kesi namba 105/2009 kwa matumuzi mabaya ya ofisi ya umma ambapo anadaiwa kuwa kati ya mwaka 2001-2006 akiwa mwajiriwa wa serikali, aliidhinisha ujenzi wa minara pacha, bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu.

Aidha, anadawa kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 kwa uamuzi wake wa kuidhinisha ujenzi wa minara hiyo pacha kosa linaloangukia kwenye shitaka la kwanza.
Liyumba alisomewa mashitaka mapya baada ya Hakimu Mkazi Walirwande Lema, aliyekuwa akisikiliza kesi namba 27/2009 iliyokuwa ikimkabili mshitakiwa huyo na Meneja Miradi wa BoT, Deogratius Kweka, kuwaachia huru baada ya kubaini hati ya mashitaka ilikuwa ina makosa kisheria.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye, walikamatwa tena na Liyumba kusomewa mashitaka mapya, huku Kweka akiendelea kuhojiwa na Takukuru.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumatano,Juni 10,2009

SHAHIDI AUGUA GHAFLA MAHAKAMANI

Na Happiness Katabazi

SHAHIDI wa kwanza Mary Kiwia ,katika kesi ya wizi wa Sh bilioni 6.3 wa Fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu ya Tanzania, inayowakabili mtu na mdogo wake Johnson Lukaza na Mwesigwa Lukaza jana alishindwa kupanda kizimbani kuanza kutoa ushahidi wake baada ya hali ya afya kubadilika ghafla akiwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam.


Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface mbele ya Mahakimu wa Kazi wanaosilikiza kesi hiyo Prophir Lyimo,Emilius Mchauru na Edson Mkasimongwa alieleza mahakama kuwa kesi hiyo ya jinai namba 1156/2008, jana ilikuja kwaajili ya kuanza kusikilizwa na kuwa walileta shahidi mmoja ili aweze kuanza kutoa ushahidi wake.

“Lakini kwa bahati mbaya shahidi huyo ambaye amefika leo(jana) mahakamani hapa presha imepanda hivyo tunaomba tupewe muda ili tuweze kuwatafuta mashahidi wengine” alidai Boniface.

Hata hivyo Tanzania Daima katika uchunguzi wake imebaini shahidi huyo aliyepandisha presha wakati akisubiri kupanda kizimbani kutoa ushahidi wake anaitwa Maria Kiwia mbaye ni Mwanasheria Kitaaluma.

Hata hivyo kiongozi wa jopo la mahakimu hao wakazi, Lyimo alisema wanakubalina na hoja ya wakili utetezi Alex Mgongolwa na Richard Rweyongeza kuwa jarada la kesi hiyo linadosari na kwamba dosari hizo haziwezi kufanyiwa marekebisho na mahakama ya Kisutu isipokuwa Mahakama Kuu hoja ambayo iliingwa mkono na Wakili Boniface ambaye aliiongeza kuwa jarada hilo lipelekwe mahakama hiyo ya juu lipewe maelekezo.

“Kwa hiyo kimsingi sisi jopo limebaini jarada lina dosari zinazotakiwa kutolewa maelekezo hivyo tunaamuru jarada la kesi hii lipelekwe Mahakama Kuu kwaajili ya maelekezo na naninaairisha kesi hii hadi Julai 8 mwaka huu.” alisema Prophir Lyimo.

Novemba mwaka jana , ilidaiwa mahakamani hapo kuwa kati ya Novemba –Desemba 2007 washitakiwa hao walikula njama,kughushi hati ya kuamisha deni na kuibia sh 6,300,402,224.64 mali ya BoT, ambapo walighushi hati ya kuamishia mali iliyoonyesha kampuni yao ya Kernel Limited imepewa idhini ya kukusanya deni la kampuni ya Marubeni Corporation ya Japan.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne,Juni 9,2009

SERIKALI:MARANDA ANA KESI YA KUJIBU

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa mashitaka katika kesi ya wizi wa sh bilioni 1.8 za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), inayomkabili Mweka Hazina wa CCM Mkoa wa Kigoma na wenzake, umejigamba kuwa wameweza kuthibitisha kesi hiyo, hivyo kuiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam iwaone wana kesi ya kujibu.


Akiwasilisha majumuisho ya ushahidi katika kesi hiyo jana, Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface ambaye alikuwa akisaidiana na Timon Vitalis, Frederick Manyanda, Ephery Cedrick na Michael Lwena, alidai upande wa mashitaka umedhibitisha kesi hiyo, hivyo washitakiwa wa na kila sababu kujibu kesi inayowakali.

Aidha, Bonifacena alieleza kusikitishwa na wakili wa utetezi, Majura Magafu aliyedai kuwa upande wa mashitaka umeshindwa kudhibitisha kesi hiyo licha ya kutoa vielelezo 17.

Mbele ya Mahakimu Wakazi, Cypriana William, Saul Kinemela na Phocus Bampikya, Wakili huyo wa serikali alidai miongoni mwa vielelezo hivyo kuna vielezo vya washitakiwa wawili katika kesi hiyo (Maranda na Farijala Hussin) ambavyo vinaonyesha walitoa maelezo ya ungamo kwenye Kikosi kazi kilichoundwa na Rais Jakaya Kikwete kuchunguza wizi huo.

“Maungamo hayo ni maneno yalitoka kwenye vinywa vya washitakiwa wenyewe na wala si kwenye vinywa vyetu wala vyenu…licha ya juzi Magafu kuyapinga maungamo hayo, lakini sisi tunasema hayo ni maungamo ya washitakiwa na yamekidhi kifungu cha 3 cha sheria ya ushahidi ya mwaka 2002,” alidai Wakili huyo.

Akichambua ungamo la Maranda, alidai ingawa mshitakiwa huyo alikana kutofahamu Farijala alitoa wqapi fomu hizo, hapo panahitajika kutumika ushahidi wa mazingira na kusema kuwa upande wa mashitaka unaamini nyaraka hizo zilitengenezwa na washitakiwa hao.

Akijibu hoja ya Wakili Magafu kwanini hakueleta shahidi toka kampuni ya MS/BC Cars Eport ya Mumbai India, ili idhibishe kuibiwa, alidai wakili huyo analiangalia suala hilo juu juu.

“Ukiangalia hati ya kuhamisha mali inaonyesha BC Cars Eport imeridhia kampuni ya Kiloloma & Brothers idai deni lake na ukiangalia chini ya hati hiyo umewekwa muhuri wa Kiloloma & Bro’s Enterprises na saini imewekwa na mtu wa kufirika (Chares Kissa), sasa huu ni mkorogo wa kughushi na tukumbuke tunapoitaja Kiloloma & Bros tunaona sura ya Farijala Hussein,” alidai na kusababisha watu kuangua vicheko.

Aidha, alidai kama washitakiwa walikuwa wameingia makubaliano na kampuni hiyo iweje Farijara atumie jina la kufikirika na kueleza kwa sababu hiyo hawakuona umuhimu wa kumuita mtu kutoka kampuni hiyo kutoa ushahidi mahakamani.

Akichambua shitaka la tano, la kuwasilisha hati za uongo, alidai wa shahidi toka BoT unaonyesha Maranda ndiye aliyekuwa akifika katika benki hiyo na kuwasilisha nyaraka zilizoghushiwa ambazo ni kilelezo cha 12 zilizokuwa zikionyesha anatakiwa alipwe deni kwaniaba ya kampuni hiyo ya nje.

Akipangua hoja ya Magafu kuwa hakuna mtu aliyetoka BoT kuja kulalamika kwamba waliibiwa fedha, alidai dosari ya majumuisho ya wakili huyo ni kwamba hakuangalia upande wa pili, kwani kuna nyaraka toka Benki Kuu ambazo zinaonyesha zilituma fedha kwenye kampuni ya washitakiwa na kwamba upande wa mashitaka haukuona haja ya kumleta Gavana kuja kudhibitisha wizi kwani nyaraka walizozitumia kujipatia fedha, kusajili jina la biashara ni za kughushi.

“Kwa hiyo tunaomba mahakama hii tukufu iwaone washitakiwa wanakesi ya kujibu kwani tunataka wapande kizimbani na kuleza bila kificho sh bilioni 1.8 waliipataje” alidai Boniface.

Aidha, alidai ungamo la Farijala linaonyesha yeye ndiye aliyejaza fomu ya kuomba kupatiwa jina la biashara la Kiloloma & Bro’s Enterprises na kwamba ndiye aliyepeleka fomu hiyo BRELA na kulipia ada ya usajili sh 6,000.

Wakili huyo wa Serikali alidai pia mshitakiwa huyo wakati anasajili kampuni hiyop alikiri kutumia jina la kufikirika la Chares Issac Kissa.

Akichambua shitaka la kwanza la kujipatia usajili kwa njia ya udanganyifu, Boniface alidai Farijara alipata usajili wa kampuni hiyo kwa udanganyifu, kwani alitumia jina la kufikirika.
Pia alieleza udanganyifu mwingine aliokiri kuufanya mshitakiwa huyo ni kudanyanya kuwa ofisi ya kampuni hiyo ipo nyumba Na. 7 Mtaa wa Iramba, Magomeni.

Sambamba na hayo, alieleza kuwa ushahidi wa mtaalam wa maandishi umebainisha kuwa fomu hiyo ilikuwa imejazwa na Farijala.

Baada ya kumaliza kuwalisha majumuisho hayo, Hakimu Cypiriana William alisema atatoa uamuzi wa suala hilo Jumatano ijayo iwapo washitakiwa wanakesi ya kujibu au la.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumamosi, Juni 6,2009

MAHAKAMA KUU YAMNG'ANG'ANIA PROFESA MAHALU

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imeyatupa maombi ya aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu na Meneja Utawala wa Fedha, Grace Martin, wanaokabiliwa na kesi ya kuisababishia serikali hasara ya zaidi ya sh bilioni 2.
Katika maombi hayo, washitakiwa hao walitaka mahakama hiyo iwaachilie huru kwa sababu mwenendo mzima wa kesi yao ya msingi, una dosari za kisheria.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Jaji Juxon Mlayi baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili wiki iliyopita.

Katika uamuzi huo, Jaji Mlayi alisema ombi la Mahalu kuwa upande wa mashitaka ulikosea kufungua kesi hiyo kabla ya kuwaondolea kinga ya kidiplomasia, haina msingi kwa kuwa katiba ya nchi inatamka wazi kwamba mwenye kinga ya kutokushtakiwa ni rais pekee.

Alisema washitakiwa hao kweli wana kinga, lakini inatumika kuwakinga wanapokuwa Italia na kwamba serikali ile isingekuwa na mamlaka ya kuwashitaki hadi hapo Serikali ya Tanzania ingewaondolea kinga, lakini kwa kuwa washitakiwa hao ni watumishi wa umma, serikali ina mamlaka ya kuwashitaki bila hata ya kuwaondolea kinga.

Kuhusu hoja kuwa walifunguliwa kesi bila ya kuwapo kibali cha Mkrugenzi wa Mashitaka (DPP), Jaji Mlayi alisema baada ya kupitia jalada la kesi hiyo, ameona vibali viwili vya DPP, kimoja kikionyesha kesi hiyo ilikuwa ikiwakabili washitakiwa watatu na kibali cha pili, kinaonyesha washitakiwa wawili.

Alisema kibali hicho cha pili, kiliwasilishwa baada ya mshitakiwa mmoja ambaye alikuwa akishitakiwa pamoja na washitakiw hao, kufutiwa mashitaka na DDP.

Aidha, akichambua ombi kuwa Mahakama ya Kisutu, haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo kwa sababu makosa ya washitakiwa yalitendeka nchini Italia na si hapa nchini, Jaji Mlayi alisema kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002, inatoa mamlaka ya kumshitaki mtu aliyefanya makosa hata nje ya Tanzania.

Kuhusu ombi la waombaji waliokuwa wakipinga uamuzi wa Hakimu Mkazi, Sivangilwa Mwangesi wa kuchukua ushahidi kwa njia ya video, Jaji Mlayi alisema hawezi kulitolea uamuzi kwa sababu lilikwishatolewa uamuzi na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Hata hivyo, alitupa ombi la pingamizi la upande wa mashitaka, lililotaka mahakama hiyo isikubali kusilikiza maombi hayo.

Baada ya uamuzi huo kutolewa, wakili wa utetezi, Alex Mgongolwa, aliwaambia waandishi wa habari kuwa, hawajaridhishwa na uamuzi huo, na wanakwenda kujiandaa kwa ajili ya kukataa rufaa katika Mahakama ya Rufani.

Juni 3, mwaka huu, mawakili wa utetezi, Mabere Marando aliyekuwa akisaidiwa na Mgongolwa, Bob Makani na Cuthbert Tenga wanaowatetea waombaji, waliomba Mahakama Kuu iwaachie washitakiwa hao kwa madai kuwa kesi hiyo ilifunguliwa bila kibali cha DPP.

Marando alifafanua kuwa, washitakiwa walifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Januari 22 mwaka 2007 na wakati wote huo, hati ya mashitaka haikuwa na kibali cha DPP hadi Aprili 25, mwaka huo, DPP Eliezer Feleshi, alitoa kibali.

Marando alitumia kifungu cha 26(1) cha Sheria ya Uhujumu Uchumi iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002, ambayo inatamka bayana kuwa, shauri lolote linaloangukia kwenye makosa ya uhujumu uchumi, alipaswi kufunguliwa mahakamani bila kibali cha DPP.

Wakili Mgongolwa alidai kuwa, dosari ya tatu ni kwamba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, haikuwa na mamlaka ya kuendesha kesi inayowakabili washitakiwa hao, kwa madai kuwa makosa yanayowakabili, yalifanyika nchini Italia na kwamba Italia haijumuishi mahakama hiyo.

Akijibu pingamizi la upande wa mashitaka la kutaka mahakama hiyo isisikilize ombi la Mahalu, kwa sababu hakukuwa na ulazima wa kusikiliza, Mgongolwa alidai kuwa kwa mujibu wa kifungu 43(1),44(1),(a) cha Sheria ya Mahakimu na kifungu cha 372 na 373(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, zinatoa nguvu kwa Mahakama Kuu kusikiliza ombi la mapitio ya jalada la kesi, ambalo kesi ya msingi imefunguliwa katika mahakama ya chini.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Juni 9,2009

NANI MWEKEZAJI HALALI TRL?

Na Happiness Katabazi

NADHARIA ya kubinafsisha ni pana.Inajumuisha dhana ya kuuza mali ya walipa kodi kwa mtu binafsi ili mtu huyo aendeshe huduma hiyo iliyokuwa ikiendeshwa na umma kwa ubora na ufanisi zaidi.


Mauzo kama hayo yanatakiwa yazingatie uwezo wa mtu kununua rasilimali inayouzwa kwa bei ya hali ya soko kwa mtindo ama wa shindani kitenda au kwa mtindo wa upendeleo kwa wafanyakazi wa kampuni hiyo ya umma.

Ama kwa mtindo wa upendeleo wa wazawa kwa vile siyo halali kumshindanisha mzawa na mgeni katika mazingira ya kitenda.

Nadharia hii ya ubinafsishaji inahusu pia ukodishaji wa rasilimali za umma kwa mwendeshaji binafsi pale ambapo rasilimali husika haifai kuuzwa kwa mtu binafsi kwa maslahi ya taifa ama rasilimali hiyo ni kubwa mno kiasi kwamba mwekezaji hawezi kupata mtaji wa kutosha kununua rasilimali hiyo.

Kwa ujumla nadharia ya ubinafsishaji inaiondoa dola katika uendeshaji wa shughuli za kiuchumi ili dola izingatie wajibu wake wa utawala, ulinzi na usalama wa taifa.

Tulipoamua kubinafsisha miundombinu yetu na hasa shirika la ndege ilitubidi kuzingatia misingi hiyo niliyoitaja.

Kwa kuwa Kampuni yetu ya reli(TRL) ndiyo chombo mwafaka cha uchukuzi wa bidhaa na abiria chenye usalama na chenye uwezo wa kusafirisha binadamu na bidhaa kwa wingi, mataifa yaliyomengi hayapendelei kubinafsisha muundombinu huo.

Hivyo mtindo wa kukodisha reli kwa waendeshaji binafsi umekuwa ukitumika nchini Ujerumani,Swedeni,Uingereza,Marekani.Mtindo huo umetumika kwa ufanisi mkubwa.

Lakini ieleweke kwamba bado dola katika nchi hizo halijajiondoa kwenye wajibu wa kufanya reli za kisasa zinazotumia umeme na kuvipa nguvu viwanda vikubwa vinavyotengeneza Injini na mabehewa ya kisasa ya uchukuzi wa bidhaa na abiria.

Hivyo siku hadi siku raia katika mataifa hayo wanakuwa wakitegemea zaidi reli kama chombo kikuu cha usafirishaji wa mizigo na binadamu.Treni za kisasa zenye mabehewa ya kisasa yanayompatia abiria burudani,starehe zinazofanya usafiri huu kushindana na usafiri wa anga yaani ndege.

Spidi ya treni hizi zinazoendeshwa kwa spidi ya ya umeme ni kati ya km 250 hadi 650 kwa saa.Hizo ndizo treni tunazoziona katika nchi hizo kupitia mitandao au Televisheni katika kila nchi ambayo ni makini katika sekta ya uchukuzi.

Tanzania haina sababu ya kugundua taili katika eneo hili la Sayansi na Teknolojia kwani tayari dunia imeshapiga hatua hizo za kimaendeleo.

Tunapo binafsisha mfumo wetu wa reli lazima tuzingatie kukabidhi mfumo kwa kampuni yenye uwezo wa Kisayansi,Teknolojia na mtaji ili kuweza kuendesha reli zetu kwa viwango vya juu.

Ni ajabu! badala ya hayo tuliyoyataja nchi yetu imechagua kampuni RITES ambayo kisayansi na teknolojia bado ipo kwenye enzi za ujima na kimtaji ni sifuri.

Tuambiwe kama Rais Jakaya Kikwete aliamua kujitengea sekta hiyo ya reli ndiyo chaguo lake la uwekezaji binafsi, atuambie kwani tunaona sasa mlipa kodi ametishwa mzigo wa kumlipia mishahara mwendeshaji maelezo yoyote na rais yupo kimya.

Sasa kama rais hana hisa katika mradi huu atueleze ni kwanini anamkumbatia mwekezaji wa sasa TRL?

Na hizo fedha serikali inazomkopesha kila mwezi anamkopesha kwa idhini ya nani na kwa maslahi ya nani?

Ni serikali hii hii inashindwa kuboresha mishahara watumishi wa umma hususani sekta ya afya , walimu na hata kuwapa mikopo ya uhakika wanafunzi wa elimu ya juu, kuweka dawa katika mahospitali yake lakini ina fedha za kumjaza huyu mwekezaji wa TRL.

Hivi tunajikomba nini kwa huyu mwekezaji au ni shemeji yetu kutoka India?

Tumechoka, serikali isijaribu kutulazimisha tuitukane.Serikali isitulazimishe tuwe wakorofi na waaasi. Serikali itekeleze wajibu wake wa kuongoza kwa kuzingatia misingi ya Utawala bora kisiasa,kiuchumi na kiutamaduni.Katika hili la mwekezaji wa TRL tunaona kunanuka ufisadi mkubwa.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Juni 7,2009

SOS:SHIRIKA LILILOJENGA KIJIJI CHA WATOTO YATIMA



*NIA NI KUWALEA KATIKA FAMILIA ZENYE UPENDO

TATIZO la watoto wa mitaani wanaoishi katika mazingira hatari hapa nchini kadri siku zinavyozidi kusonga mbele linaanza kukua. Katika makala hii Mwandishi Wetu HAPPINES KATABAZI, amezungumza na Mkurugenzi wa Kijiji cha Watoto cha SOS Dar es Salaam, Dk. Alex Lenguju,(Pichani) na anatuelezea zaidi jinsi kijiji hicho kilivyojipanga kuwaokoa watoto wanaoishi katika mazingira mahumu.


Swali: Tueleze kwa mapana SOS Children Villages International nini?

Jibu: Shirika la SOS Children’s Villages International ni Shirika huru la Maendeleo ya Jamii lisilo la Kiserikali wala la Kidini, shirika hili linalenga hasa matunzo ya muda mrefu ya watoto yatima na waliotelekezwa katika mfumo wa familia mbadala. Katika mfumo huu, watoto wanalelewa kwa muda mrefu katika nyumba za familia zinazojitegemea ambazo kwa pamoja zinaunda Kijiji cha SOS.

Swali: Shirika lilianzishwa lini?

Jibu:
Shirika hili lilianzishwa na Herman Gmeiner wakati alipojenga kijiji cha kwanza cha Watoto cha SOS mwaka 1949 katika mji wa Imst huko Austria. Katika vijiji vya SOS vya watoto tumejitolea kabisa katika ustawi wa watoto. Lakini pia tumejitolea kwa dhati kabisa kuimarisha familia na jamii kwa ujumla kama njia madhubuti ya kuzuia utelekezaji wa Watoto.

Shirika hili shirika la kwanza kuanzisha huduma kabambe ya malezi muda mrefu ya watoto yatima na waliotelekezwa katika mfumo wa familia mbadala ambapo hadi sasa linaongoza duniani katika utekelezaji wa mfumo huu. Mfumo wetu wa malezi ya watoto umejengwa juu ya kanuni kuu nne za msingi za Muundo wa Malezi wa SOS:

Kila mtoto anapata mzazi mmoja anayemjali, kumtunza na aliyekaribu naye kabisa wakati wote. Katika Kijiji cha Watoto cha SOS, watoto wanaishi katika nyumba za familia kila na kila nyumba inaongozwa na mama. Mama wa SOS anajenga uhusiano wa karibu na kila mtoto aliyekabidhiwa kwake akimpatia kila mtoto usalama, upendo na uthabiti ambao kila mtoto anahitaji ili aweze kukua vyema. Mahusiano ya kifamilia yanajengeka yenyewe kama kaka na dada. Katika nyumba za familia chini ya uangalizi wa mama, watoto wanakuwa pamoja kama kaka na dada wa familia moja, kwa namna hii wanajenga muunganiko wa kudumu kati yao.

Kila nyumba inatengeneza nyumbani kwao wenyewe, hapo ndipo wanapotoka na hapo ndipo wanaporudi. Chini ya paa la nyumba hii watoto wakiwa na mama yao wanapata kujisikia salama na kuwa wako kwao kweli kweli.

Famila ya SOS ni sehemu ya jamii. Familia imo ndani ya Kijiji ambacho ndicho kinachoipa familia mazingira ya jamii pana ambamo watoto wanapata fursa ya kufurahia utoto kwa furaha na wakati huo huo wanajifunza kushiriki kikamilifu katika maisha ya kijumuiya. Mkurugenzi wa Kijiji ndiye pia Baba wa Kijiji, watoto wanamtambua kuwa ni baba yao. Baba wa kijiji pamoja na wafanyakazi wenza wa kiume wanawapatia watoto mambo muhimu wanayohitaji.

Swali: Matarajio yenu ya baadaye ni yapi?

Jibu: Matarajio ya SOS kwa ajili ya watoto wote duniani ni kufika hatua ambapo kila mtoto yumo ndani ya familia na anapata fursa ya kukua kwa upendo, heshima na usalama. Katika SOS tumepania mambo matatu makuu ikiwemo kujenga familia mbadala kwa watoto ambao hawana familia ili waweze kutengeneza mustakabali wao na kushiriki katika maendeleo ya jamii ambako watoto hawa wanatoka. Tunataka kila mtoto anayeingia katika malezi yetu afike hatua ya kuwa mtu mwenye mafanikio na mwanajamii anayeweza kutoa mchango wa maana katika jamii anamoishi. Sisi katika SOS tunaheshimu dini na tamaduni mbalimbali na tunafanya kazi kwa kuzingatia Mkataba wa Umoja wa Mataifa Juu ya Haki za Mtoto.

Swali: SOS ina fanyakazi katika nchi zipi?

Jibu: Kwa sasa SOS inafanya kazi katika nchi zaidi ya 132 duniani kote; ikiwa na Vijiji vya Watoto zaidi ya 470 na pia vituo mbalimbali vya huduma vya SOS kama vile Shule, Vituo vya Kijamii, Vituo vya Afya na Shule za Ufundi. Hivyo, kwa miaka zaidi ya 50 sasa wale wanofuata nyayo za mwanzilishi wa SOS wamesambaza wazo la SOS hadi kufika katika nchi mbalimbali, tamaduni, dini na mitindo ya maisha. Hapa Tanzania kijiji cha kwanza cha SOS kilifunguliwa Zanzibar mwaka 1991 katika eneo la Mombasa. Mei 2000, kijiji cha pili hapa nchini ambacho ni cha kwanza Tanzania bara kilifunguliwa huko Arusha katika eneo la Ngaramtoni.

Swali: Tueleze kijiji cha SOS Dar es Salaam kina jumla ya watoto wangapi?

Jibu: Kijiji cha SOS cha Dar es Salaam tunachokitambulisha sasa ni cha tatu katika nchi yetu. Kijiji hiki kinapokea watoto wachanga hadi wa miaka 6, ambao wanatunzwa hadi kufikia utu uzima ili nao wajitegemea wenyewe. Kijiji hiki kina jumla ya nyumba za familia 13, zenye uwezo wa kutunza watoto 130 kikiwa kimejaa. Kwa sasa tuna watoto 122 katika kijiji hiki, lakini tunatarajia kufikia watoto 120 hadi mwisho wa mwezi huu na kutimiza idadi kamili ya watoto 130 kabla ya mwisho wa mwaka 2010. Pamoja na mpango wa malezi ya watoto ya muda mrefu katika mfumo wa familia, shirika pia lina mpango wa kuimarisha familia hapa Dar es Salaam.

Mpango huu unalenga kuwasaidia watoto wenye uhitaji ambao hawakuweza kupata nafasi katika Kijiji na ni sehemu muhimu sana ya mkakati wa SOS wa kuzuia utelekezaji wa watoto.

Kwa wakati huu mpango wa kuimarisha familia unahudumia familia 52 zenye jumla ya watoto 202 na walezi wao, wengi wakiwa kutoka Manispaa ya Temeke, Kinondoni, Ilala na Bagamoyo. Hawa wanapewa huduma za chakula, matibabu, mahitaji ya shule na mafunzo mbalimbali kwa walezi.

Aidha SOS inasaidia familia kuandaa maendeleo ya mpango miaka 3-5 ili baada ya miaka hiyo ziweze kujitegemea. Na tumekuwa zikipatiwa misaada ya chakula, tiba, elimu na mafunzo ya ujasiriamali, malezi na afya.

Lengo kuu la mpango huu ni kuzuia utelekezwaji watoto kwani watu wengine wanatelekeza watoto kwasababu ya kushindwa kuwahudumia na mpango huo unapofanikiwa, idadi ya watoto wa mitaani na wanaolelewa kwenye vituo itapungua.
Lengo jingine la mpango huo wa kuimarisha familia ni kutetea haki za wa watoto. SOS pia inashirikiana na mashirika mengine ili kuhakikisha watoto kwenye jamii wanapata haki stahili kama vile chakula, mahali pa kulala na ulinzi salama. Hili halijaanza hapa Tanzania, lakini SOS inataka kuwa sauti ya watoto katika jamii ili familia ifahamu katika kulinda, kusimamia na kutetea haki za watoto.

Swali: Serikali inaisaidiaje SOS?

Jibu: Mchango mkubwa wa serikali ni pale ilipotoa idhini ya shirika la SOS lifanye kazi hapa nchini. Pia ilitoa ardhi kwetu hadi vijiji vikajengwa hapa Sinza C, inatupatia msamaha wa kodi wa vifaa vya watoto na kadri ya uwezo wake inatoa ruzuku. SOS inategemea michango kutoka kwa jamii kwa asilimia 100 kwaajili ya kuendelea kujenga na kuendesha kijiji hicho. Kila kitu kinatoka kwa watu wenye mapenzi mema katika jamii.

Hadi sasa sehemu kubwa ya misaada inakuwa ikitoka kwa wanajamii nje ya nchi lakini hivi karibuni Watanzania wameanza kupata mwamko wa kujitokeza, kusaidia watoto wetu kwa aina ya kuchangia fedha au mali na mashirika machache yameonyesha nia ya kutaka kusaidia kama vile Commercial Bank of Afrika, Zain, Vodacom, Kibo Trade na Hoteli ya Kempiskin Kilimanjaro inayotusaidia kwa kukusanya michango toka kwa wateja wake na kisha kutuletea hapa kijijini.

0716-774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Juni 6, 2009

WAKILI ATAKA WASHITAKIWA EPA WAACHIWE HURU

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa utetezi katika kesi ya wizi wa sh bilioni 1.8 za Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), umeiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kuwaachia huru washitakiwa wa kesi hiyo, kwa madai kuwa ushahidi ulitolewa na upande wa mashitaka ni dhahifu na umeshindwa kuonyesha kiasi cha fedha walichoiba.


Washitakiwa katika kesi hiyo ni Mweka hazina wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kigoma, Rajabu Maranda na mpwa wake, Farijala Hussein ambaye ni mfanyabiashara na wote ni wakazi wa jijini Dar es Salaam.

Wakili wa utetezi, Majura Magafu alitoa madai hayo mbele ya Hakimu Cypriana William, ambaye ni Naibu Mwenyekiti wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ambaye anasaidiana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Phocus Bambikya na Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Saul Kinemela, kusikiliza kesi hiyo.

Katika kesi hiyo, jana, upande wa utetezi ulikuwa ukiwasilisha majumuisho ya ushahidi, ikiwa ni siku chache baada ya upande wa mashitaka kufunga ushahidi wake.
Magafu alieleza kuwa, kwa mujibu wa hati ya mashitaka, washitakiwa hao wanakabiliwa na makosa ya kula njama, kughushi, wizi na kujipatia ingizo kwenye akaunti isivyo halali. Upande wa mashitaka ulileta jumla ya mashahidi tisa.

Alidai kuwa, mashahidi walioletwa na upande wa mashitaka, wameshindwa kuithibitishia mahakama kuwa washitakiwa hao na wengine ambao hawapo mahakamani, walipanga njama ya kuiibia BoT.

Akitolea mfano shahidi wa sita ambaye ni Ofisa wa Jeshi la Polisi, Salum Kisai, alidai kuwa licha ya kuwa ni mpelelezi, haukueleza wakati gani, mahali washitakiwa walipanga njama za kuibia Benki Kuu.

Akizungumzia hati ya kuhamisha deni lililotumiwa na washitakiwa kuonyesha MS/BC Cars Export Limited imewapatia idhini ya kukusanya deni la Kampuni ya Kiloloma & Brother inayomilikiwa na washitakiwa, kuwa hati hiyo ilighushiwa, alidai hakuna ushahidi uliothibitisha hilo.

Aidha alieleza kuwa, kosa la kula njama linaambatana na makosa mengine ya kujipatia usajili kwa njia ya udanganyifu na kughushi, kwa hiyo hakuna shahidi aliyekuja kuithibishia mahakama kwamba hati ya kuhamisha deni ‘deed of assignment’ ilighushiwa.

Magafu akifafanua kuwa, katika shitaka la wizi, hadi sasa hakuna mtu yeyote, awe Gavana, Naibu Gavana au Mkurugenzi wa Fedha toka BoT, aliyefika mahakamani hapo kueleza fedha za benki hiyo zilivyoibwa na kuongeza kuwa, waliokuja kutoa ushahidi walionyesha utaratibu wa kutoka kwa fedha ambao si shida ya mahakama.

Kuhusu shitaka la kujipatia ingizo la fedha kwa njia ya udanganyifu, Magafu alidai hakuna shahidi toka BoT au MS/BC Cars Exports Limited, aliyekuja kusema fedha zilizoingizwa kwenye kampuni ya washitakiwa ya Kiloloma & Brothers na hazikuingizwa kihalali.

Novemba mwaka jana, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, washitakiwa hao wanakabiliwa na mashitaka sita, kwamba mwezi Mei mwaka 2005 waliiba zaidi ya sh bilioni 1.8, mali ya BoT.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Juni 5, 2009

KESI YA MAHALU NGOMA NZITO

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa utetezi katika kesi ya kuisababishia hasara serikali, ya zaidi ya sh bilioni 2, inayomkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu na Meneja Utawala na Fedha, Grace Martin, umedai kuwa upande wa mashitaka ulikosea kufungua kesi hiyo kabla ya kuwaondolea kinga ya kidiplomasia washitakiwa hao.


Hoja hiyo ni miongoni mwa hoja nne ziliozowasilishwa jana katika Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, mbele ya Jaji Juxston Mlayi na kiongozi wa jopo la mawakili wa utetezi, Mabere Marando aliyekuwa akisaidiwa na Alex Mgongolwa, Bob Makani na Cuthbert Tenga.

Jana, Mahalu na mwenzake, waliwasilisha ombi namba 2/2009, dhidi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), la kuomba mahakama hiyo ipitie mwenendo wa kesi ya msingi inayowakabili, ambayo ilifunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Marando aliiambia mahakama hiyo jana kuwa, walifikia uamuzi wa kuwasilisha ombi hilo la mapitio mahakamani hapo baada ya kubaini dosari kubwa tatu za kisheria licha ya kumweleza Hakimu Mkazi, Sivangilwa Mwangesi, anayesikiliza kesi hiyo ambaye hajazipatia ufumbuzi.

Kwa mujibu wa Marando, dosari ya kwanza ni kwamba washitakiwa wote ni wanadiplomasia, hivyo wana kinga ya kidiplomasia kwa mujibu wa sheria.

Alidai kuwa, mtu mwenye kinga ya aina hiyo, ataendelea kuwa nayo, na itaendelea kumlinda kwa mambo aliyoyafanya akiwa nayo, hadi pale mamlaka husika itakapomuondolea.

‘Sasa cha kushangaza, upande wa mashitaka ulikurupuka na kuwafungulia kesi washitakiwa hawa, ambao hadi sasa wana kinga ya kibalozi, kwa sababu mamlaka husika haijawaondolea kinga, hivyo kitendo cha serikali kuwashitaki, huku ikijua fika haijawaondolea kinga, ni makosa na hawakupaswa kushitakiwa,” alidai Marando.

Alitaja dosari ya pili kuwa, washitakiwa walifunguliwa kesi bila ya kibali cha DPP.

Marando alifafanua kuwa, washitakiwa walifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Januari 22 mwaka 2007 na wakati wote huo, hati ya mashitaka haikuwa na kibali cha DPP hadi Aprili 25, mwaka huo, DPP Eliezer Feleshi, alitoa kibali.

Marando alitumia kifungu cha 26(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002, ambayo inatamka bayana kuwa, shauri lolote linaloangukia kwenye makosa ya uhujumu uchumi, alipaswi kufunguliwa mahakamani bila kibali cha DPP.

“Mheshimiwa Jaji Mlayi, kifungu hicho kinakataza makosa kama haya yanayowakabili washitakiwa, yasifunguliwe bila kibali cha DPP, lakini upande wa mashitaka walifungua kesi hii bila kibali cha DPP. Na hili lipo wazi kabisa, kwani kesi ilifunguliwa Januari 22 mwaka 2007 na kibali cha DPP kikaja kuwasilishwa mahakamani Aprili 25, mwaka huu, hii ni ni kosa kisheria,” alidai Marando.

Wakili Alex Mgongolwa alidai kuwa, dosari ya tatu ni kwamba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, haikuwa na mamlaka ya kuendesha kesi inayowakabili washitakiwa hao, kwa madai kuwa makosa yanayowakabili, yalifanyika nchini Italia na kwamba Italia haijumuishi mahakama hiyo.

“Na kwa mujibu wa kifungu cha 59(3) cha Sheria ya Mahakimu inayoainisha mipaka ya mahakama za hakimu mkazi nchini kuendesha kesi, kwa hiyo kabla ya kesi ya msingi kufunguliwa, walipaswa kuomba kibali toka kwa Jaji Mkuu ili Mahakama ya Kisutu iongezewe mipaka ya kuendesha kesi hiyo, pia uamuzi ule wa Mahakama ya Kisutu kupokea ushahidi wa shahidi wa upande wa mashitaka, anayeishi Italia kwa njia ya video, ni wazi kabisa Mahakama ya Kisutu ilivuka mipaka yake bila kupata kibali cha kuongezewa mipaka na Jaji Mkuu,” alidai Mgongolwa.

Akijibu pingamizi la upande wa mashitaka la kutaka mahakama hiyo isisikilize ombi la Mahalu, kwa sababu hakukuwa na ulazima wa kusikiliza, Mgongolwa alidai kuwa kwa mujibu wa kifungu 43(1),44(1),(a) cha Sheria ya Mahakimu na kifungu cha 372 na 373(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, zinatoa nguvu kwa Mahakama Kuu kusikiliza ombi la mapitio ya jalada la kesi, ambalo kesi ya msingi imefunguliwa katika mahakama ya chini.

“Kwa sababu hiyo, tunaomba mahakama hii itupilie mbali mwenendo mzima wa kesi, kwa sababu umejaa dosari za kisheria ambazo zipo wazi na kisha iwaachilie huru washitakiwa,” alidai Mgongolwa.

Wakati mawakili wa utetezi wakibainisha dosari hizo kwa vielelezo, upande wa mashitaka ulionekana kukumbwa na wakati mgumu wa kupangua hoja hizo kwa vielelezo.
Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, akijibu hoja hizo alidai kuwa, hakukuwa na umuhimu wa mahakama hiyo kufanya mapitio.

Kuhusu hoja kwamba Mahakama ya Kisutu haikuwa na mamlaka ya kuendesha kesi hiyo, wakili huyo alidai kuwa Ubalozi wa Tanzania nchini Italia ni Tanzania.

Hoja hiyo ilisababisha Jaji Mlayi kumtaka Boniface ampatie ushahidi unaoonyesha kuwa Ubalozi wa Tanzania nchini Italia ni Tanzania, ambapo Boniface alimweleza jaji kuwa anamtuma Mwanasheria wa Takukuru, Ponsian Lukosi ambaye alikuwa akisaidiana naye, kwenda maktaba ya mahakamani hapo kwa muda ili akachukue ushahidi huo, lakini hadi ombi lilipomalizwa kusikilizwa jana saa saba mchana mahakamani hapo, Lukosi alirudi bila kuwa na ushahidi huo.

“Upande wa Mashitaka sijasahahu, nipatie huo ushahidi, mlioenda kuusaka unaonyesha Ubalozi wa Tanzania nchini Italia ni Tanzania,” alisema Jaji Mlayi na kusababisha mawakili wa upande wa mashitaka kujiumauma bila kutoa maelezo yanayoeleweka, hali iliyosababisha watu kuangua vicheko.

Akijibu hoja ya washitakiwa hao kwamba hawakupaswa kushitakiwa kwa sababu hawajaondolewa kinga ya kidiplomasia, Boniface alijibu kwa kifupi bila kuonyesha vielelezo vyovyote, kwa kudai wana haki ya kushitakiwa.

Mgongolwa akijibu hoja hizo, alidai yote yaliyowasilishwa na upande wa mashitaka hayana msingi, na kwamba hakuna kitu muhimu katika sheria kama mamlaka na kusisitiza kuwa jambo likifanyika nje ya mamlaka husika ni batili.

Kuhusu hoja kuwa Ubalozi wa Tanzania nchini Italia ni Tanzania, Marando alidai kuwa, hoja hiyo si sahihi kwa kuwa ubalozi wetu kuwa Italia ni upendeleo na kutolea mfano kuwa mwaka 1998 Ubalozi wa Marekani ulivyolipuliwa hapa nchini Tanzania, iliamua kuipatia Marekani eneo jingine la Msasani na kujenga tena ubalozi wake na kuhoji kwamba ina maana sehemu zote hizo ni nchi ya Marekani, jambo liloibua vicheko tena mahakamani hapo.

Kutokana na malumbano hayo ya hoja za kisheria, Jaji Mlayi alisema atatoa uamuzi kuhusu wa hoja hizo Juni 8.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Juni 4, 2009

KESI YA ZOMBE KUUNGURUMA TENA JUNI 15

Na Happiness Katabazi

KESI ya mauaji ya wafanyabiashara watatu na dereva teksi mmoja, inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam (ACP), Abdallah Zombe na wenzake, imepangwa kuanza kunguruma tena Juni 15, Tanzania Daima imebaini.


Vyanzo vya kuaminika toka ndani ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, vimelihakikishia gazeti hili jana kuwa, kesi hiyo imepangwa kuanza kusikilizwa Juni 15 hadi 19 na itasikilizwa mfululizo.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, tayari ratiba ya vikao vya kesi za mauaji ambayo ndani yake imepangwa kesi ya Zombe, tayari imeishaanza kugawiwa kwa mawakili wanaowatetea washitakiwa na wale wa serikali.

‘Ni kweli kesi ya Zombe itakuwa tarehe hiyo na tayari ratiba ya kesi hiyo imeishaanza kutolewa kwa mawakili wa pande zote,” kilisema chanzo chetu.

Kutokana na kupangwa kesi hiyo Juni 15, upande wa mashitaka unatarajiwa kuwasilisha majumuisho ya ushahidi wa kesi hiyo mbele ya Jaji wa Mahakama ya Rufani, Salum Massati baada ya kikao kilichopita kushindwa kuwasilisha kwa madai ya kutokuwa na muda wa kutosha.

Mbali na upande wa mashitaka, pia wazee wa baraza katika kesi hiyo, nao watapata fursa ya kuwasilisha majumuisho yao.

Mei 7, mwaka huu, mawakili wa utetezi waliwasilisha majumuisho ya ushahidi wa kesi hiyo baada ya washitakiwa kumaliza kutoa ushahidi wao katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, na ikafunga rasmi kupokea ushahidi upande wa utetezi.

Mawakili wa utetezi, Jerome Msemwa, Majura Magafu, Denis Msafiri na Ishengoma, waliiomba mahakama hiyo kuwaachia huru wateja wao kwa kuwa ushahidi uliotolewa mahakamani hapo, umejaa mkanganyiko mkubwa na pia ni wa kuungaunga.

Pia walisema mashahidi katika kesi hiyo, wameshindwa kuthibitisha kama washitakiwa hao walihusika kufanya tukio hilo la mauaji, Januari 14, mwaka 2006.

Wakili Jerome Msemwa ambaye anamwakilisha Zombe, alidai kitendo cha mteja wake kutoa taarifa za mauaji ya watu hao kwenye vyombo vya habari, si kosa, kwani alifanya hivyo baada ya kupokea taarifa kutoka kwa askari wake wa chini.

Mbali ya Zombe na ASP Christopher Bageni, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni SP Ahmed Makelle, Jane Andrew, Emmanuel Mabula, Michael Shonza, Koplo Abeneth Saro, Rajabu Bakari na Festus Gwasabi.

Washitakiwa hao wanadaiwa Januari 14 mwaka 2006, eneo la Mbezi Luis, katika msitu wa Pande, waliwaua Ephraim Chigumbi, Sabinus Chigumbi na Mathias Lukombe, ambao ni wafanyabiashara wa madini kutoka Mahenge, Ulanga na Juma Ndugu, ambaye ni dereva teksi, mkazi wa Manzese, jijini Dar es Salaam.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Juni 4,2009

WAKILI WA LIYUMBA ACHARUKA

Na Happiness Katabazi

WAKILI wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba, anayekabiliwa na kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221, Majura Magafu, amecharuka mahakamani na kudai kuwa upande wa mashitaka una hila, na unafurahia kuona mshitakiwa huyo anaendelea kusota mahabusu.


Wakati wakili huyo akicharuka, Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imeitisha jalada la kesi hiyo namba 105/2009, inayomkabili Liyumba, ili iweze kupitia uamuzi wa kulegeza masharti ya dhamana, uliotolewa na Mahakama ya Kisutu, Ijumaa iliyopita.

Hatua hiyo ya Mahakama Kuu, imetokana na upande wa mashitaka kuwasilisha ombi hilo la mapitio katika mahakama hiyo ya juu.

Wakili wa utetezi, Magafu anayesaidiana na Hudson Ndusyepo na Profesa Gamalieli Mgongo Fimbo, aliikumbusha mahakama hiyo kuwa shauri hilo jana lilikuwa limekuja kwa ajili ya mahakama kuhakiki hati za masharti ya dhamana ili mshitakiwa aweze kudhaminiwa.

Magafu alidai kuna wadhamini wawili ambao ni wafanyakazi wa BoT watakaosaini bondi ya sh milioni 50 kila mmoja, na kivuli cha hati ya nyumba iliyopo kitalu 2232 na 3233 Mtaa H, Mbezi Beach, yenye thamani ya sh milioni 882, mali ya mshitakiwa na kivuli cha hati ya kusafiria.

Alisema wamefikia kuwasilisha vivuli hivyo na si nyaraka halisi kwa kuwa bado zinahifadhiwa mahakamani hapo kwani zilitumika katika kesi Na 27/2009, iliyofutwa Jumatano iliyopita, na kwamba licha kuwasilisha maombi ya kutaka warejeshewe hati hizo, bado hawajarejeshewa.

“Tumefikia uamuzi wa kuwasilisha vivuli vya hati hizo kwa kuwa hati halisi bado zipo mikononi mwa mahakama hii na Ijumaa iliyopita tuliomba turejeshewe, lakini bado hatujarejeshewa.

“Pia Ijumaa tuliwawasilisha hati nyingine kwa upande wa mashitaka na pia leo asubuhi tuliwapatia hati nyingine ili wahakiki, lakini hadi tunaingia mahakamani hapa, hawajatupatia jibu, hivyo tunaomba mahakama hii ikubali kupokea hati hizo, huku tukisubiri kupata hati halisi ili mshitakiwa leo apate dhamana,” alisema Magafu.

Akijibu hoja hizo, Wakili Mwandamizi wa Serikali, Justus Mlokozi, ambaye alikuwa akisaidiana na Prosper Mwangamila na John Wabuhanga, alidai kuwa bado hawajathibitisha usafi wa hati hizo ambazo upande wa utetezi unataka zitumike kumdhamini mshitakiwa.

Mulokozi alidai kuwa, hati waliyopewa Ijumaa, inaonyesha ilifanyiwa tathimini Agosti mwaka 2008 na kuongeza kuwa, kuanzia wakati huo hadi jana, ni kipindi kirefu na chochote kinaweza kutokea kuhusu hati hiyo, hivyo aliomba wapewe muda kujiridhisha.

“Mheshimiwa hakimu, kilichosemwa na Mulokozi kimeonyesha wazi serikali ina hila, na inafurahia Liyumba anavyoendelea kusota mahabusu,” alidai Magafu.

Kauli hiyo ilisababisha Mulokozi kuinuka na kuiomba mahakama imwamuru Magafu atoe tuhuma hizo chini ya kiapo na aache kuikashifu serikali.

Hali hiyo ilimfanya Magafu ainuke tena kwenye kiti chake, na kuendelea kudai kuwa jukumu la kuhakiki masharti ya dhamana ni la mahakama, si upande wa mashitaka, na limetamkwa wazi katika kifungu cha 148(6,7) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai iliyofanyiwa marekebisho 2002.

“Kama nyumba ya mshitakiwa ambayo hati yake bado inashikiliwa na mahakama, kwanini upande wa mashitaka una wasiwasi? Mei 28 mwaka huu, mshitakiwa kaachiliwa huru akakamatwa tena, akapelekwa huko wanapojua serikali, na nyaraka zote zilizotumika kumdhamini awali bado zipo mahakamani, sasa anataka kusema mahakama imeiba hizo nyaraka?

“Sisi tunaamini kitu kikihifadhiwa mahakamani, kinakuwa katika mikono salama, na kama upande wa mashitaka una wasiwasi, ulete ushahidi kama nyumba hiyo imeuzwa na ndiyo maana leo tumeomba hizo nyaraka zitumike kumdhamini mshitakiwa,” alidai Magafu.

Alidai kuwa, kama kweli serikali haina nia mbaya dhidi ya mashitakiwa, nyaraka hizo zitumike kumdhamini mteja wake na mambo mengine yatafuatia, na wapo tayari kwenda kujibu ombi la mapitio Mahakama Kuu.

Magafu alidai kuwa, anachokiona kwenye kesi hii ni upande wa mashitaka kutumia mbinu za kuchelewesha kesi ili mshitakiwa aendelee kusota rumande.

“Sasa tunaanza kuhisi kuna kitu kwenye hii kesi…mbona hila zote zinafanywa na upande wa mashitaka katika kesi hii hii tu?” alihoji Magafu.

Akitoa uamuzi wake baada ya malumbano makali ya hoja za kisheria, Hakimu Mkazi Mwaseba alisema kuwa, mahakama inatakiwa ajiridhishe na nyaraka hizo ambazo zimewasilishwa na upande wa utetezi.

“Ili niweze kutoa dhamana kwa mshitakiwa, lazima nijiridhishe na hizi barua za wadhamini mlizoleta leo, hakuna polisi wa kuzihakiki, hivyo siwezi kutoa dhamana,” alisema na kuamuru mshitakiwa arudi rumande hadi Juni 15.

Uamuzi huo wa Mwaseba wa kumnyima dhamana Liyumba, ulisababisha ndugu na jamaa wa mshitakiwa waliokuwa wamekuja kuhudhuria kesi hiyo, kushikwa na simanzi na kuondoka kwenye chumba cha mahakama wakiwa wamejiinamia.

Ijumaa iliyopita, Mwaseba alilegeza masharti ya dhamana kwa Liyumba, ambapo sasa atatakiwa atoe fedha taslimu au hati ya mali yenye thamani ya sh milioni 300, wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh milioni 50 kila mmoja, kutotoka nje ya Dar es Salaam hadi kwa kibali maalum na kusalimisha hati ya kusafiria mahakamani.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Juni 2, 2009