'MAWAKILI KESI YA EPA WANAKIUKA SHERIA '

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa mashitaka katika kesi ya wizi wa sh bilioni 1.8 katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) inayomkabili Farijala Hussein na Shaban Maranda, umeelezwa kushangazwa na upande wa utetezi kung’ang’ania kukata rufaa Mahakama Kuu kupinga uamuzi wa Mahakama ya Kisutu, kuwaona washitakiwa hao wana kesi ya kujibu.


Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface aliyekuwa anasaidiana na Wakili Mwandamizi, Fredrick Manyanda, alidai kuwa kitendo hicho ni kinyume cha sheria.

“Msomi Magafu (Wakili wa utetezi) anafahamu sheria inakataza maamuzi yoyote kukatiwa rufaa hadi mahakama inapotoa hukumu, hivyo kinachofanywa na upande wa utetezi ni kukiuka sheria kwa makusudi na lengo hasa wanataka kuchelewesha kesi,” alidai Boniface.

Hata hivyo, madai hayo yalipingwa na wakili wa utetezi, Majura Magafu kwa maelezo kuwa msimamo wa kukata rufaa unabaki pale pale na kwamba nakala ya rufaa hiyo ipo kwenye maandalizi ya mwisho kwa ajili ya kuiwasilisha Mahakama Kuu.

Hakimu Mkazi, Cypriana William, alisema ombi la Magafu litaendelea kubaki kama lilivyo kuahirisha kesi hadi Agosti 28 mwaka huu, itakapotajwa.

Wakati huohuo, mshitakiwa wa pili katika kesi ya EPA, Amit Nandi, amewasilisha maombi mahakamani hapo akiiomba mahakama impatie hati yake ya kusafiria, ili aweze kumsindikiza mkewe nchini India kwa matibabu.

Ombi hilo liliwasilishwa katika kesi tatu tofauti tofauti zinazomkabili mshitakiwa huyo na wenzake na wakili wake, Gabriel Mnyere, ambapo jana kesi hiyo ilikuja kwa kutajwa.

Kwa upande wake, Wakili wa Serikali, Michael Lwena na Arafa Msafiri, waliiambia mahakama kuwa mshitakiwa huyo ni raia wa kigeni, hivyo akipewa ruhusa hiyo anaweza kutoroka na endapo atatoroka serikali itakuwa na wakati mgumu wa kumsaka. Uamuzi wa ombi hilo utatolewa Agosti 3.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Julai 30 ,2009

USIKILIZWAJI KESI YA MRAMBA WAKWAMA

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, ilishindwa kuendelea kusikiliza maelezo ya awali ya kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 11.7 inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba na wenzake, kwasababu kompyuta inayorekodi mwenendo wa kesi hiyo kupata tatizo la kiufundi.


Washitakiwa wengine ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu Mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja.

Kiongozi wa jopo la kesi hilo John Utamwa anayesaidiana na Sam Rumanyika na Saul Kinemela jana saa 8:58 baada ya kutoka mapumziko ya dakika 15 mahakamani hapo, alisema jopo hilo limelazimika kusitisha kuendelea kusikiliza maelezo ya awali kwakuwa mtaalamu wa kompyuta huyo amewaeleza kompyuta hiyo imepata hitirafu.

Utamwa alisema kimsingi kesi hiyo hawezi kuendelea bila ya kuwepo kwa kifaa hicho hivyo akautaka upande wa mashitaka kusitisha kuendelea kusoma maelezo hayo ya awali hadi Septemba 16-25 mwaka huu na kuongeza kuwa kesi hiyo itakuja kutajwa Agosti 31 mwaka huu, kwakuwa sheria inataka kesi itajwe ndani ya siku 30.

Aidha alikubali maombi ya washtakiwa wote ya kutoka nje ya Dar es Salaam yaliyowalishwa na mawakili wao Hurbet Nyange,Joseph Thadayo na Profesa Leonard Shaidi.

Mapema saa tano asubuhi hadi saa 7:30 mchana, Wakili Kiongozi wa serikali Stanslaus Boniface aliyekuwa akisaidiana na Fredrick Manyanda, Tabu Mzee, Beni Lincon alianza kusoma maelezo ya awali dhidi ya washitakiwa lakini hata hivyo alishindwa kumaliza kusoma maelezo hayo kwasababu ya kompyuta kuaribika.

Boniface alidai kuwa washitakiwa wote walikuwa ni watumishi wa wa umma wenye nyadhifa za juu serikalini, na kwamba kati ya 2000-2005 Mramba alikuwa Waziri wa Fedha, na kati ya 2002-2005 Yona alikuwa Waziri wa Nishati na Madini na kuwa 2002-2008 Mgonja alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha.

“Hivyo washitakiwa walipaswa kufanyakazi zao kwa uadilifu na kwa misingi ya sheria”alidai Boniface.

Akiendelea kueleza kupitia dokezo la Machi 2003 lenye kumbukumbu Na.CDA 111/338/01 ,mshitakiwa wapili(Yona) aliomba ridhaa ya Rais wa awamu ya tatu Benjamin Mkapa kupitia barua yenye Na.SHC/PP.340/P ya Machi 20 ya 2003 la kuletwa mkaguzi huru wa dhahabu.

Lakini barua ya Septemba 11 ya 2002 na Desemba 15 mwaka huo huo, iliyoandikiwa na Katibu Mkuu ofisi ya rais, Mrindoko na Kaimu Mkuu wa kitengo cha Sheria G.M.Nyelo ilikataa ombi la Yona na zikamtaka aheshimuwa sheria kwasababu mchakato uliotumika kumpata mkaguzi huru ni batiri na usitishwe na kumtaka watumie mahabara ya SEAMIC kutafiti jambo hilo kwa gharama kidogo.

Aidha mshitakiwa wa pili alishauriwa na Kamishna wa Madini G.L Mwakalukwa kuptia barua yake Na.CDA 111/338/01 ya Machi 21 2003 kwamba pafanyike uteuzi Assayers Licensing Board kwaajili ya upatikanaji ushauri kutoka Commonwealth Sekretarieti kuangalia jinsi ya kupunguzwa kwa gharama za kuingia mkataba na Alex Stewart (Assayers).

“Lakini Mei 11 ya 2003,Yona aliandika barua kwa rais Mkapa yenye kumbukumbu Na.CDA/11/338/01-M.100/5 aliomuomba rais airuhusu wizara ya Fedha na Benki Kuu zigharamie Golg Asseyers na rais alimjibu ombi hilo kupitia barua SHC/PP.340/Q ya Mei 13 ya 2003, ambayo alikataa ombi la Yona.”alidai Boniface.

Aidha aliendelea kueleza kuwa Mei 15,2003 Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha wakati huo, Abdisalaam Khatibu alimjulisha Yona kupitia barua Na.TYC/M/30/2 maazimio ya kikao kati ya Think Tank ya Wizara ya Fedha na Tax Review Committee ni kwamba uchunguzi zaidi ufanyike kuhuusu kuajili Gold Asseyers na akamshauri asitishe mchakato msima wa kumpata mkaguzi huyo goldi..

Alidai licha ya kupewa taarifa hizo, Yona alipuuza na Mei 20, 2003 ,kupitia barua yake yenye kumbukumbu Na.111/338/01.Na kuwa mshitakiwa wa tatu(Mgonja) naye pia alipuuza maazimio yaliyotolewa na Sekretarieti ya Commonwealth katika barua yake Na.5106/P/58 ya Mei 21 ya 2003.

Aidha washitakiwa kupitia mawakili wao walikubaliana na barua hizo na madokezo kuwa yapokelewe na mahakama ili zijekutumika kama vielelezo vya upande wa mashitaka wakati kesi hiyo itakapoanza kusikilizwa na hivyo kufanya jopo hilo jana kupokea jumla ya vielezo saba.

Washitakiwa hao walifikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani hapo mwishoni mwa mwaka jana, wakikabiliwa na makosa mawili ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kisababishia serikali hasara ya sh .bilioni 11.7, kwa kukudharau mapendekezo ya TRA yaliyokataza kampuni ya Alex Stewart isipewe msamaha wa kodi lakini washitakiwa hao walikaidi mapendekezo hayo na kutoa msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Agosti mosi, 2009

WAZUNGU WEZI ATM WAMKATAA MKALIMANI

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa mashitaka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jana ulishindwa kuwasomea mashitaka raia wawili wa Bulgaria ambao wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, kwa tuhuma za wizi wa sh milioni 70 mali ya Benki ya Barclays.


Mwendesha Mashitaka Mfawidhi, Edger Luoga, mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema, aliwataja washitakiwa hao kuwa ni Nedkolazarous’ Standaev (35) na Stela Peteva Nedelcheva (23).

Luoga alipokuwa akijiandaa kuanza kuwasomea mashitaka huku mkalimani aliyetafutwa na serikali kwa ajili ya kutafsiri lugha ya Kiingereza kwenda lugha ya Bulgaria, ndipo mshitakiwa wa pili, Nedelcheva, alinyosha mkono na kuiambia mahakama hiyo kwamba hawana imani na mkalimani huyo (jina tunalihifadhi kwa sababu za kiusalama).

Nedelcheva alidai kuwa wamefikia uamuzi wa kumkataa mkalimani huyo kwa sababu haifahamu vyema lugha ya Bulgaria na kwamba hata walipokamatwa hivi karibuni, mkalimani huyo aliletwa polisi na wakati wakihojiwa, alikuwa akitafsiri lugha yao isivyostahili.

“Mheshimiwa hakimu, mkalimani huyu hatumtaki, atafutwe mkalimani mwingine kwa sababu hatuna imani naye kwa kuwa hata tulivyokamatwa na kuchukuliwa maelezo na polisi, alikuwa akitafsiri tofauti na maelezo yetu tuliyokuwa tukiyatoa kwa lugha yetu ya Bulgaria,” alidai Nedelcheva ambaye alijifunga kanga aliyopewa na wasamaria wema baada ya kutinga mahakamani hapo akiwa na kaptula fupi iliyokuwa ikionyesha maungo yake.
Aidha, Hakimu Lema alisema amesikia ombi hilo na kuahirisha kesi hiyo hadi Julai 27, na kuamuru washitakiwa hao wakahifadhiwe kwenye mahabusu ya polisi.

Mapema wiki hii, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, aliwaambia waandishi wa habari kwamba wanawashikilia watuhumiwa wakiwa na kadi maalum zilizowawezesha kuiba kwenye ATM ya benki ya Barclays.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Julai 24,2009

KORTI YAWAPA DHAMANA WAVUVI HARAMU

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, imetupilia mbali pingamizi la serikali katika kesi ya uvuvi haramu inayowakabili raia 32 wa kigeni waliokamatwa kwenye meli ya Tawariq 1,lilokuwa likiiomba mahakama hiyo isipokee ripoti ya tathimi ya meli hiyo kwasababu ripoti hiyo ni ya uongo.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Hakimu Mkazi Waliarwande Lema, ambaye alianza kwa kusema kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya yeye kutoa uamuzi kuhusu malumbano ya kisheria yaliyoibuka Ijumaa iliyopita kuhusu ripoti ya tathimini ya meli hiyo.

Hakimu Lema alisema baada ya kupitia kwa kina malumbano hayo ya hoja za kisheria, amefikia uamuzi wa kutupilia mbali ombi la upande wa mashitaka lilokuwa likitaka mahakama hiyo isipokee ripoti hiyo kwasababu amebaini halina msingi.

Alisema mahakama hiyo ilichokuwa ikikitaka ni katika ripoti hiyo ni tathimini na si dosari za uandaaji wa ripoti kama inavyodaiwa na upande wa mashitaka na kuongeza kuwa ripoti hiyo imeiwezesha mahakama hiyo kufikia uamuzi wa kutoa dhamana kwa washitakiwa hao ambao wamesota rumande kwa miezi mitano sasa.

Lema alisema kwa mujibu wa ripoti hiyo ya tathimini iliyofanywa na Dar es Salaam Marine Instute, endapo meli hiyo itauzwa kwenye soko nchini India ni dola 280,000 na katika soko la hapa nchini ni dola 122,000.

‘Pingamizi hilo la serikali kwamba ripoti hiyo ina dosari nyingi na kwamba ni ya uongo, mahakama hii imeliona halina msingi kabisa kwasababu mahakama hii ilichokuwa ikiitaji ni tathimini ya meli ili iweze kutoa dhamana kwa washitakiwa na tathimini hiyo imeainishwa kwenye ripoti hii, hivyo ripoti hii ndiyo imeiwezesha mahakama hii leo (jana) imeifikisha mahakama hii kutoa masharti ya dhamana kwa washitakiwa.”alisema Lema na kufanya mawakili wa serikali kujiinamia.

Akitoa masharti ya dhamana alisema meli hiyo na samaki ambao wanathamani ya sh bilioni 2.7, vitadhaminiwa kwa bondi ya dola za kimarekani 250,000, kila mshitakiwa anadhaminiwa na wadhamini wawili wanaotambulika na ofisi za balozi ambapo wadhamini hao wawili watasaini bondi ya dola 25,000.

Hata hivyo washitakiwa hao walishindwa kutimiza masharti ya dhamana hiyo jana na walirejeshwa rumande hadi Agosti 5 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya kutajwa.

Ijumaa iliyopita, wakili wa serikali Deo Nangela na Mganga Biswalo, walitumia saa moja na nusu kuichambua ripoti hiyo na kuishawishi mahakama isiipokee ripoti hiyo kwa kile walichokidai kuwa ina mapungufu mengi,ya uongo na kwamba haitaisaidia mahakama kufikia uamuzi wa kutoa dhamana kwa washitakiwa.

Naye wakili wa utetezi Ibrahimu Bendera aliyekuwa akisaidiana na Elias Nawela walipinga hoja hiyo na kudai kuwa ukweli unabaki pale pale kwamba upande wa mashita siyo wataalum wa masuala ya meli hivyo ni vyema wakaitwa wataalamu waliofanya tathimini na si vinginevyo na kusisitiza ripoti hiyo ni sahihi.

Washitakiwa hao ni mabaharia, Jiojwen Chang (34), Jia Yin Zhao 26), Gexi Zhao (36), Zongmin Ma (36), Dong Liu (25), Yongiao Fang (22), Nguyen Tuan(23), Hsu Sheng Pao (55), Zhao Hanquing (39), Zho Hanging (39) ambaye wote ni wakala na raia wa China.

Wengine ni Tran Van Phuon (33), Pham Dinn Suong (31), Tran Van Thanh (23), Cao Vuong (27), Kristofer Padilla (29) raia wa Vietnam. Wengine ni Mohamed Kiki (61), Anul Mani (24) raia wa Taiwani.

Aidha,washitakiwa wengine ni Jejen Priyana (22), Kuntoto Suratno (27), Tusi Ame (25), Ifan Herman Pandi (21), raia wa Indonesia, Silvano Garanes (32), Benjie Rosano (34), Ignacio Dacumos (31), Marlon Maronon (33), Jhoan Belano (34), Rolando Nacis (35) raia wa Philipins, Wakati Ali Ali Mkota (32), Juma Juma Kumu (40), Jackson Toya(39) raia wa Kenya.

Machi 10 mwaka huu, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa washtakiwa wote wanakabiliwa na mashtaka mawili, shitaka la kwanza ni kuvua samaki bila leseni kinyume na sheria ya Uvuvi wa Samaki katika kina kirefu ya mwaka 2009.

Alidai Machi 8 mwaka huu, washtakiwa wote kwa pamoja, saa sita usiku katika ukanda wa bahari ya Hindi ndani ya eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, walikamatwa wakiwa wakivua samaki bila leseni.Na washtakiwa wote walikana mashtaka na wapo rumande kwaajili ya wameshindwa kutimiza masharti dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Julai 23,2009

KORTI YAWAPA DHAMANA WAVUVI HARAMU

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, imetupilia mbali pingamizi la serikali katika kesi ya uvuvi haramu inayowakabili raia 32 wa kigeni waliokamatwa kwenye meli ya Tawariq 1,lilokuwa likiiomba mahakama hiyo isipokee ripoti ya tathimi ya meli hiyo kwasababu ripoti hiyo ni ya uongo.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Hakimu Mkazi Waliarwande Lema, ambaye alianza kwa kusema kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya yeye kutoa uamuzi kuhusu malumbano ya kisheria yaliyoibuka Ijumaa iliyopita kuhusu ripoti ya tathimini ya meli hiyo.

Hakimu Lema alisema baada ya kupitia kwa kina malumbano hayo ya hoja za kisheria, amefikia uamuzi wa kutupilia mbali ombi la upande wa mashitaka lilokuwa likitaka mahakama hiyo isipokee ripoti hiyo kwasababu amebaini halina msingi.

Alisema mahakama hiyo ilichokuwa ikikitaka ni katika ripoti hiyo ni tathimini na si dosari za uandaaji wa ripoti kama inavyodaiwa na upande wa mashitaka na kuongeza kuwa ripoti hiyo imeiwezesha mahakama hiyo kufikia uamuzi wa kutoa dhamana kwa washitakiwa hao ambao wamesota rumande kwa miezi mitano sasa.

Lema alisema kwa mujibu wa ripoti hiyo ya tathimini iliyofanywa na Dar es Salaam Marine Instute, endapo meli hiyo itauzwa kwenye soko nchini India ni dola 280,000 na katika soko la hapa nchini ni dola 122,000.

‘Pingamizi hilo la serikali kwamba ripoti hiyo ina dosari nyingi na kwamba ni ya uongo, mahakama hii imeliona halina msingi kabisa kwasababu mahakama hii ilichokuwa ikiitaji ni tathimini ya meli ili iweze kutoa dhamana kwa washitakiwa na tathimini hiyo imeainishwa kwenye ripoti hii, hivyo ripoti hii ndiyo imeiwezesha mahakama hii leo (jana) imeifikisha mahakama hii kutoa masharti ya dhamana kwa washitakiwa.”alisema Lema na kufanya mawakili wa serikali kujiinamia.

Akitoa masharti ya dhamana alisema meli hiyo na samaki ambao wanathamani ya sh bilioni 2.7, vitadhaminiwa kwa bondi ya dola za kimarekani 250,000, kila mshitakiwa anadhaminiwa na wadhamini wawili wanaotambulika na ofisi za balozi ambapo wadhamini hao wawili watasaini bondi ya dola 25,000.

Hata hivyo washitakiwa hao walishindwa kutimiza masharti ya dhamana hiyo jana na walirejeshwa rumande hadi Agosti 5 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya kutajwa.

Ijumaa iliyopita, wakili wa serikali Deo Nangela na Mganga Biswalo, walitumia saa moja na nusu kuichambua ripoti hiyo na kuishawishi mahakama isiipokee ripoti hiyo kwa kile walichokidai kuwa ina mapungufu mengi,ya uongo na kwamba haitaisaidia mahakama kufikia uamuzi wa kutoa dhamana kwa washitakiwa.

Naye wakili wa utetezi Ibrahimu Bendera aliyekuwa akisaidiana na Elias Nawela walipinga hoja hiyo na kudai kuwa ukweli unabaki pale pale kwamba upande wa mashita siyo wataalum wa masuala ya meli hivyo ni vyema wakaitwa wataalamu waliofanya tathimini na si vinginevyo na kusisitiza ripoti hiyo ni sahihi.

Washitakiwa hao ni mabaharia, Jiojwen Chang (34), Jia Yin Zhao 26), Gexi Zhao (36), Zongmin Ma (36), Dong Liu (25), Yongiao Fang (22), Nguyen Tuan(23), Hsu Sheng Pao (55), Zhao Hanquing (39), Zho Hanging (39) ambaye wote ni wakala na raia wa China.

Wengine ni Tran Van Phuon (33), Pham Dinn Suong (31), Tran Van Thanh (23), Cao Vuong (27), Kristofer Padilla (29) raia wa Vietnam. Wengine ni Mohamed Kiki (61), Anul Mani (24) raia wa Taiwani.

Aidha,washitakiwa wengine ni Jejen Priyana (22), Kuntoto Suratno (27), Tusi Ame (25), Ifan Herman Pandi (21), raia wa Indonesia, Silvano Garanes (32), Benjie Rosano (34), Ignacio Dacumos (31), Marlon Maronon (33), Jhoan Belano (34), Rolando Nacis (35) raia wa Philipins, Wakati Ali Ali Mkota (32), Juma Juma Kumu (40), Jackson Toya(39) raia wa Kenya.

Machi 10 mwaka huu, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa washtakiwa wote wanakabiliwa na mashtaka mawili, shitaka la kwanza ni kuvua samaki bila leseni kinyume na sheria ya Uvuvi wa Samaki katika kina kirefu ya mwaka 2009.

Alidai Machi 8 mwaka huu, washtakiwa wote kwa pamoja, saa sita usiku katika ukanda wa bahari ya Hindi ndani ya eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, walikamatwa wakiwa wakivua samaki bila leseni.Na washtakiwa wote walikana mashtaka na wapo rumande kwaajili ya wameshindwa kutimiza masharti dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Julai 23,2009

KASHFA YA NORTH MARA,VIONGOZI WAWAJIBIKE

Na Happiness Katabazi

HIVI karibuni wananchi waishio katika Wilaya ya Tarime wameulalamikia mgodi wa dhahabu wa North Mara, kwamba unatiririsha maji ya kemikali ambayo wamedai maji hayo yamedhuru afya za baadhi yao wanaoishi maeneo jirani na mgodi huo.


Kilio hicho cha wakazi hao kimeendelea kusambaa karibu pande zote za nchi, kwani baadhi ya viongozi wanaharakati na wasomi wamejitokeza kuishinikiza serikali kuingilia kati na kuyapatia ufumbuzi wa haraka madai ya wakazi hao.

Si hao pekee, bali hata Watanzania wazalendo waliokerwa na unyama huo wameendelea kulalamikia hali hiyo kwa nguvu zote na kuitaka seriakali kuingilia kati kunusuru janga hilo.

Binafsi nasema yanayofanywa na North Mara dhidi ya wananchi wenzetu wa Tarime, ni matokeo ya sera mbovu ya madini kwasababu mgodi hauna tofauti na migodi mingine hapa nchini.

Kwa hiyo, Watanzania wenzangu wasiitazame North Mara kama kisiwa, yale yanayotokea katika mgodi huo yapo katika migodi mingine nchini. Utaratibu wa kusafisha dhahabu unaofanywa na mgodi huo ni utaratibu unaofanywa pia na migodi mingine.

Kwa hiyo, tujiulize tuna sera ya uchimbaji wa madini inayowalinda wananchi wa taifa hili kutokana na athari za mifumo ya usafishaji wa madini? Je, tunasheria inayowalinmda wananchi dhidi ya utaratibu wa usafishaji wa madini isiyokidhi viwango vya dunia vya usalama wa afya za raia?

Tunachokiona North Mara ni kwamba wawekezaji wameamua kukiuka viwango vya dunia vya usalama wa afya za wananchi, ili kukwepa gharama za teknolojia za kisasa.

Matokeo yake wananchi wenzetu wanakunywa maji, wanaoga na mifugo pia mifugo yao inatumia maji hayo yenye kemikali yenye madhara kwa binadamu na hayo yote yanafanyika chini ya ulinzi wa polisi wa nchi hii, serikali ya nchi hii na sheria hizo zinawalinda wawekezaji.

Kumbe sheria za madini si tu zinawaruhusu wawekezaji kuchukua madini yetu kwa wingi sisi tubaki mikono mitupu, ila pia zinawaruhusu kutumia teknolojia duni inayoumiza au kujeruhi au kuathiri vibaya afya za binadamu na mifugo na viumbe hai vilivyopo.

Kashfa ya North Mara ni kubwa ambayo mapana yake yangemlazimisha Waziri wa Nishati na Madini ajiuzulu. Kwa kuwa awali serikali ilipinga kuwa hakuna athari zozote kwa binadamu, na kwamba hakuna yeyote wala mifugo iliyoathirika na maji hayo yanayotiririshwa na mgodi huo.

Na huo ndiyo umekuwa msimamo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na serikali yake. Hii ina maana kwamba CCM na seriakali yake katika Mkoa wa Mara imetupiwa mfupa ilikuficha ukweli.

Na kwa sababu wamekuwa wakificha ukweli huo ndiyo maana hata Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Balozi Khamis Kagasheki, alivyotumwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwenda mgodini hapo serikali Mkoa wa Mara ilimgeuza mwanaserere waziri huyo na kumficha ukweli.

Sasa tujiulize hao walioficha ukweli walikuwa na malengo gani? Je, ni watetezi wa wananchi au watetezi wa kampuni hayo ya migodi? Kwa nini wananchi walalamike kuathirika? Kiongozi akatae kama si rushwa ni nini?

Kwa hiyo watu wa Mara waendelee kusimama kidete kutetea haki zao kwa kuanzisha kesi kubwa ya madai ya fidia ya Mazingira ,mifugo,,mazao na afya zao.
Pili, watu wa Mara wawafichue viongozi ambao wamelishwa rushwa na makampuni ya migodi.

Mungu ibariki Tanzania,Mungu ibariki Afrika

0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Julai 23, 2009

WATUHUMIWA WA PEMBE ZA NDOVU WATINGA MAHAKAMANI

Na Happiness Katabazi

HATIMAYE vigogo sita wa makampuni binafsi ya kupakia na kusafirisha mizigo nchini, jana walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam wakikabiliwa na kesi za uhujumu uchumi, kwa kusafirisha nje ya nchi jumla ya kilo 11,061 za pembe za ndovu zenye thamani ya sh 791,514,020 kinyume cha sheria.


Mbele ya Hakimu Mkazi Anisetha Wambura, Wakili wa Serikali, Prosper Mwangamila, aliyekuwa akisaidiana na Michael Lwena, Shadrack Kimaro na Abubakar Mrisha, alidai kuwa kesi hiyo inamkabili Eladius Colonerio (39) ambaye ni Mkurugenzi wa Team Freight (T) Ltd, Gabriel Balua (33), Meneja Usafirishaji wa nje na ndani ya nchi wa kampuni hiyo, na Shaban Yabulula (44) ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kigoma M. N Enterprises (T) Ltd.

Wakili wa Mwangamila, alidai kuwa washitakiwa hao katika kesi hiyo namba Na. 3 ya mwaka huu, wanakabiliwa na mashitaka 11.

Alisema shitaka la kwanza ni kula njama, ambapo kati ya Desemba 22 mwaka jana na Januari 15 mwaka huu, jijini Dar es Salaam, washitakiwa kinyume cha sheria, walisafirisha kiasi cha kilo 9,578 za meno ya tembo kwenda Hai Pong, Vietnam, na Manilla Philippiness, zenye thamani ya sh 684,827,000 mali ya Serikali ya Tanzania.
Mwangamila alidai shitaka la pili ni uwindaji haramu kinyume na Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori ya mwaka 2002.

Katika shitaka hilo, alidai kuwa washitakiwa katika muda usiofahamika, ndani ya eneo la hifadhi linalolindwa na sheria hiyo, waliwinda tembo waliowahamisha kwenye jedwali bila kibali halali.

Aidha, alidai mashitaka mengine ni kujihusisha na biashara ya nyara za serikali, kusafirisha nyara nje ya nchi, kumiliki nyara hizo, na kushindwa kutoa taarifa za umiliki kwa ofisa wanyamapori.

Mwangamilia alidai shitaka la nane ni kuwasilisha hati za uongo, ambapo Desemba 2008 hadi Januari 2009 katika Bandari ya Dar es Salaam, kwa makusudi na kwa lengo la kudanganya, washitakiwa waliwasilisha hati za kuomba kusafirisha mizigo kwenye meli yenye Na. DAR001793 ya Desemba 22 mwaka jana.

Hati nyingine za uongo zilizowasilishwa na washitakiwa hao ni Bill of Lading Na. DAR 002348/1 na DAR 002348, tamko Na. DAR 002347 iliyotolewa na CMA CGM (T) Ltd na tamko la Ushuru wa Forodha lenye namba za usajili R 93832 ya Desemba 23, mwaka jana kwa kontena Na. ECMU 1721884 na ECMU 1642240, lililosafirishwa kwenye bandari ya Hai Phong, Vietnam na Manilla, Phillippiness.

Shitaka la tisa alidai ni kusafirisha nje ya nchi bidhaa zilizozuiliwa na kukatazwa na Sheria ya Ushuru wa Forodha ya Afrika Mashariki Na. 1 ya mwaka 2004.
Katika muda huo ndani ya Bandari ya Dar es Salaam, washitakiwa wanadaiwa kusafirisha nje ya nchi pembe za ndovu kinyume cha sheria.

Wakili huyo machachari, alidai shitaka la kumi ni kusafirisha nje ya nchi mali iliyofichwa kinyume cha sheria hiyo ya ushuru wa forodha, ikiwa ni pamoja na kusafirisha pembe hizo za ndovu kinyume cha sheria, huku wakidanganya kuwa ni mabaki ya plastiki kwenda Vietnam.

Katika shitaka la mwisho, washitakiwa walidaiwa kutengeneza au kutumia nyaraka za uongo za ushuru wa forodha kinyume cha Sheria ya Ushuru wa Forodha.

Hata hivyo, washitakiwa hao walipewa ruhusa kujibu tuhuma zinazowakabili katika shitaka la kwanza, saba, nane, tisa, 10, 11, kwa sababu mashitaka hayo hayaangukii katika Sheria ya Uhujumu Uchumi, ambapo walikana mashitaka hayo.
Mwangamila alidai upelelezi bado haujakamilika na kueleza kuwa shitaka la pili, tatu, nne, tano na sita ni makosa ya uhujumu uchumi hivyo, washitakiwa hawakupaswa kusema chochote kuhusu mashitaka hayo kwa sababu, dhamana ya mashitaka hayo, hushughulikiwa na Mahakama Kuu na si mahakama hiyo.
“Mheshimiwa hakimu, kifungu cha 29(4)(a) cha Sheria ya Uhujumu Uchumi kama ilivyofanyiwa mapitio 2002, kinatamka wazi kabisa Mahakama ya Hakimu Mkazi itatoa dhamana kwa kesi ya mali au fedha isiyozidi sh milioni 10, lakini katika kesi hii, kiwango hicho kimezidi hivyo tayari sheria hiyo imeifunga mikono mahakama hii na hivyo haiwezi kutoa dhamana kwa washitakiwa,” alisema Mwangamila.
Hoja hiyo ilipingwa na wakili wa utetezi, Juma Nassor ambaye alisema makosa yanayowakabili washitakiwa yanadhaminika na kuomba mahakama ipuuze madai ya serikali.
Hata hivyo, Hakimu Wambura, alisema hawezi kutoa maamuzi kuhusu malumbano hayo ya kisheria kwa sababu anahitaji muda wa kwenda kuzipitia hoja hizo.
Wambura aliiahirisha kesi hiyo hadi Agosti 6, ambapo atakuja kutoa uamuzi wa kama dhamana ipo au haipo kwa washitakiwa hao.

Wakati huo huo, mbele ya Hakimu Mkazi Mohamed Mchengelwa, Wakili wa Serikali, Abubakar Mrisha aliwataja washitakiwa watano kuwa wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi Na. 4 ya mwaka huu.

Katika kesi hiyo washitakiwa wanadaiwa kusafirisha pembe za ndovu kiasi cha kilo 1,483, zenye thamani ya sh 106,687,020 kwenda Manila, Phillippines kinyume cha sheria.

Wakili Mrisha aliwataja washitakiwa hao ambao pia ni wakurugenzi wa kampuni za kupakia na kusafirisha mizigo, kuwa ni Nebart Kiwale (45) ambaye ni Mkurugenzi wa Uplands Freight Forwarders (T) Ltd, Gabrile Balua (33) wa Team Freight, Issa Lweno (40) wa Uplands Freight Forwarders, Eladius Colonerio (39), Mkurugenzi wa Team Freight (T) Ltd na Abubakar Hassan (38).

Hata hivyo, washitakiwa hao walikana baadhi ya mashitaka yaliyo kinyume na sheria ya ushuru wa forodha na kanuni ya adhabu, isipokuwa hawakutakiwa kusema chochote kwenye makosa ya sheria ya uhujumu uchumi.

Wakili wa serikali Mrisha, naye alidai upelelezi bado haujakamilika na Hakimu Mchengelwa aliahirisha kesi hiyo hadi Julai 28, atakapotoa uamuzi kuhusu washitakiwa wapewe au wasipewe dhamana na mahakama hiyo.

Kufikishwa kwa washitakiwa hao jana, kumefanya washitakiwa waliokamatwa na pembe za ndovu jijini Dar es Salaam, kufikia kumi sasa.

Wiki mbili zilizopita, mahakamani hapo walifikishwa watuhumiwa wanne, mmoja akiwa raia wa China, waliokamatwa na pembe za ndovu katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, wakizisafirisha nje ya nchi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Julai 22,2009

KESI YA MRAMBA YAPIGWA KALENDA

Na Happiness Katabazi

KESI ya matumuzi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 11.7 inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba na wenzake, jana ilishindwa kuendelea kutokana na mahakimu wanaosikiliza kesi hiyo kutokuwapo mahakamani.


Hakimu Mkazi, Saul Kinemela, ambaye ni mjumbe wa jopo la mahakimu wakazi wanaosikiliza kesi hiyo, alisema jana kuwa kesi hiyo haitaweza kuendelea kutokana na Mwenyekiti wa jopo hilo, John Utamwa, kuwa safarini katika ziara ya Jaji Mkuu, Agustino Ramadhan na mjumbe mwingine wa jopo hilo, Fatma Masengi, kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu.

Kinemela alisema kutokana na Masengi kuteuliwa kuwa jaji, nafasi yake itajazwa na Hakimu Mkazi, Sam Rumanyika.

Alisema kwa sababu hizo, anaahirisha kesi hiyo hadi Julai 31 itakapokuja kwa ajili ya washitakiwa kusomewa maelezo ya awali.

Aidha, Wakili wa Mramba, Hurbet Nyange na Peter Swai, waliomba mahakama impatie ruhusa mteja wao, ili aweze kwenda jimboni kwake, jambo ambalo lilikubaliwa na kuruhusiwa kutoka nje ya Dar es Salaam kuanzia Julai 22-30 mwaka huu.

Mbali na Mramba, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja, ambao wote kwa pamoja wanakabiliwa na shitaka hilo la matumizi mabaya ya ofisi za umma ambapo walidharau ushauri wa Mamlaka ya Mapato (TRA) uliokuwa ukiwataka wasitoe msamahama wa kodi kwa Kampuni ya M/S Alex Stewart.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Julai 21,2009

LIYUMBA AFUNGUA KESI YA KIKATIBA

Na Happiness Katabazi

ALIYEKUWA Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania,Amatus Joachim Liyumba amefungua kesi ya Kikatiba katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, akiomba mahakama hiyo itamke kwamba kifungu 148(5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya 2002, kinapingana na Katiba ya Nchi.


Kesi hiyo ambayo imewasilishwa juzi na wakili wa Liyumba,Onesmo Kyauke tayari imeishapewa namba 36 ya mwaka huu. Na kwa mujibu wa hati hiyo, mdaiwa ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya 2002, kina mtaka mtuhumiwa anayedaiwa kuiba zaidi ya sh milioni kumi,atoe fedha taslimu au hati ya nusu ya mali anayotuhumiwa kuiba mahakamani ,ndipo apate dhamana.

Kwa mujibu wa hati ya madai ambayo Tanzania Daima ,imefanikiwa kupata nakala yake, Liyumba anaiomba mahakama hiyo itamke kifungu hicho kinapingana na Ibara ya 13(6)(b) ya Katiba ya nchi ya mwaka 1977, inayotamka bayana kwamba mtu asichukuliwe kuwa ana hatia hadi pale mahakama itakapomkuta na hatia.

Aidha hati hiyo ya madai inadai kuwa kifungu hicho cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, pia kinapingana na Ibara 17(1) ya Katiba ya Nchi, ambapo ibara hii inatamka bayana kuwa kila mtu ana haki ya kuwa huru.

Liyumba anadai hatua ya mtuhumiwa kutakiwa kutoa fedha taslimu au nusu ya mali wakati bado hajatiwa hatiani na kesi inayomkabili, ni wazi mshitakiwa anakuwa ameishahukumiwa jambo alilodai linakwenda kinyume na Ibara ya 13(6)(b) ya Katiba ya Tanzania.

“Kwa sababu hizo tunaiomba mahakama hii,itamke kifungu hicho kuwa ni batili kwani kinakwenda kinyume na haki za msingi zilizoainishwa kwenye ibara hizo za Katiba ya nchi ambayo ndiyo sheria mama” ilisomeka hati hiyo.

Aidha Liyumba aliendelea kudai kuwa yeye kama Mtanzania ana haki ya kuwa huru kwa mujibu wa ibara hiyo, lakini hivi sasa ameshindwa kupata haki hiyo ya uhuru kwasababu kushindwa kuwasilisha fedha au hati ya nusu ya mali ya bilioni 110, mahakamani ili apate dhamana.

“Hivyo haki zangu kwa mujibu wa ibara hizo za Katiba zimenyang’anywa na kifungu hicho cha Sheria ya Mwenendo wa Janai, hivyo naiomba mahakama iliangalie na hilo wakati ikisikiliza kesi hii ya Kikatiba niliyofungua”.alidai Liyumba.

Julai 15 mwaka huu, Jaji Geofrey Shaidi, alitengua masharti ya kulegeza dhamana ya mshitakiwa huyo yaliyowekwa na Hakimu Mkazi Kisutu, Nyigulila Mwaseba yaliyotaka mshitakiwa huyo atoe fedha au hati ya nusu ya mali yenye jumla ya sh milioni 300, wadhamini wawili watakaosaini bondi y ash milioni 50, kusalimisha hati ya kusafiria, na kutotoka nje ya Dar es Salaam.

Jaji Shaidi akilisema anatengea alikubaliana na rufaa ya DPP-Eliezer Feleshi, na akatengua masharti hayo kwasababu hakimu Nyigulila alipotosha matakwa ya kifungu cha 148(5)(e) ya Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai 2002.Na badala yake akatamka masharti mapya na kumtaka mshitakiwa huyo atapata dhamana kwa kutoa fedha au hati ya nusu ya mali ya sh bilioni 110.

Mei 28 mwaka huu, Liyumba alifikishwa tena Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, na kusomewa mashitaka mapya ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma chini ya kifungu 96(i) na kuisababishia serikali hasara serikali ya sh bilioni 221 kinyume na kifungu 284A(i) vya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho 2002.

Liyumba ni mtumishi wa pili mstaafu wa serikali kufungua kesi ya aina hiyo, wa kwanza ni aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia,Profesa Costa Mahalu anayekabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi katika Mahakama ya Kisutu, naye mwaka juzi, alifungua kesi ya Kikatiba Mahakama Kuu, akitaka mahakama hiyo ifute moja ya kifungu cha Sheria ya Uhujumu Uchumi, kinachomtaka mtuhumiwa kutoa fedha taslimu au nusu ya mali ndipo apate dhamana na kesi hiyo inaendelea.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima, Ijumaa, Julai 10, 2009

MSHITAKIWA ALIKIRI KUHUSIKA-SHAHIDI

Na Happiness Katabazi

SHAHIDI wa pili katika kesi ya wizi wa sh bilioni 2.2 wa Fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki ya Tanzania, inayomkabili Kada wa CCM, Rajabu Maranda na mpwa wake, Farijara Hussein, SSP-Salum Kisai, ameiambia mahakama Farijara alikiri kuhusu na kesi hiyo.


SSP-Kisai ambaye alikuwa akiongozwa kutoa ushahidi wake na Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, Fredrick Manyanda,Oswald Tibabyekoma na Michael Lwena, alidai kuwa Oktoba 20 mwaka jana, akiwa katika ofisi za Kikosi Kazi kilichoundwa na Rais Jakaya Kikwete kuchunguza wizi wa EPA, aliandika maelezo ya onyo ya Farijara na kwamba alifuata taratibu zote za kisheria zinazotakiwa kuchukua maelezo ya onyo kwa mshitakiwa.

Kisai ambaye ni Mtaalamu wa Maandishi toka Makao Makuu ya Upelelezi ya Jeshi la Polisi, alidai kuwa kimsingi maelezo Farijara alikiri kuhusika na wizi huo na akaomba mahakama ipokea maelezo hayo ya onyo ya mshitakiwa huyo kama kielelezo.

Lakini hata hivyo wakili wa mshitakiwa Majura Magafu alipinga kupokelewa kwa maelezo hayo kwasababu hati hiyo ya onyo haijakidhi matakwa ya kifungu cha 46 na 58 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya 2002.

Magafu alidai kuwa shahidi huyo wakati akichukua maelezo ya mshitakiwa alimfanyia ulaghai mteja wake kwani pia alipaswa kumweka sehemu nzuri mshitakiwa na angempatia peni na karatasi ili aweze kuandika maelezo yake mwenyewe na angemjulisha kuwa maelezo hayo yangekuja kutumika mahakamani.

“Hivyo napinga maelezo ya onyo yasipokelewe kwasababu Farijara alirubuniwa na shahidi huyu ambaye ni ofisa wa polisi wakati akimhoji mteja wangu kule katika ofisi za Kikosi Kazi” alidai Magafu.

Pingamizi lilosababisha jopo la mahakimu wakazi linaloongozwa na Fatma Masengi, Catherine Revocate na Benedict Muigwa,kukubaliana na pingamizi la Magafu na kutoa amri ya kusimamisha uendeshaji wa kesi ya msingi na kuamua kufanyika kwa kesi ndogo ambayo itaanza leo ambapo kila upande utaleta mashahidi wake kudhibitisha kama maeleazo hayo ya onyo hayakufuata taratibu za kisheria.

Novemba mwaka jana, ilidaiwa kuwa washitakiwa hao kati 2004-2005 walitumia kampuni yao hewa ya Money Planner Consaltant kuibia Benki Kuu, sh bilioni 2.2.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa,Julai 10,2009

WAISLAMU TULIENI,HUKUMU YA CCM 2010

Happiness Katabazi

JUMANNE wiki hii, serikali kupitia Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, ilitangaza kutounda Mahakama ya Kadhi na badala yake itatafsiri sheria za Kiislamu na kuzijumuisha kwenye sheria za nchi ili zitumike kwenye mahakama ya kawaida nchini.


Chikawe alisema uamuzi huo wa serikali, unatokana na mapendekezo yaliyowasilishwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na tume ya wataalamu waliochambua mapendekezo ya utafiti uliofanywa na Kamati ya Kurekebisha Sheria.

Kwanza Watanzania tujikumbushe; wakati serikali ikitangaza msimamo huo, ni Chama Cha Mapinduzi(CCM) kwa mujibu wa ilani yake ya 2005-2010 iliahidi kuwaletea Mahakama ya Kadhi Waislamu.

Ni ukweli usiopingika kwamba CCM ilidandia ahadi ya uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi kwa ajili ya kujipatia umaarufu na kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, wakati ikijua wazi isingeweze kutekeleza ahadi hiyo.

Kwa hiyo hata kwenye hoja ya Tanzania kuwa mwanachama wa Jumuiya ya Nchi za Kiislam(OIC), pia serikali yetu inajua wazi kabisa haiwezi kuingia katika jumuia hiyo; ila inaendelea kuwahadaa Watanzania na kuwafanyia mchezo wa danganya toto!

Kwa hiyo Waislam wameliwa na katika hilo ilikuwa ni siasa tu. Ahadi hiyo ni sawa na ile nyingine ya “Maisha bora kwa kila Mtanzania” tuliyoahidiwa na CCM lakini hadi hii leo imebaki kwa watu fulani. Maisha bora yameyeyuka kama theluji ya mlima Kilimanjaro.

Binafsi naweza kusema CCM si wakweli, kwani kwa kawaida chama chochote ambacho ni makini pale kinapotoa ahadi lazima kiitekeleza baada ya kukamata dola.

Nawasihi ndugu zangu Waislaam kwamba wakati wa kupiga kura katika uchaguzi mkuu ujao wawe makini kwa kuchagua chama makini kuliko kugeuzwa wanasesere.

Serikali yetu haishughuliki na mambo ya kiibada, kwani Ibara ya 19 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977,inaikataza.

Kwa hiyo serikali kama serikali kufikiria itachukua sheria za Kiislam na kuzitafsri na kuzijumuisha kwenye sheria za nchi , ni ‘uongo’ uliokubuhu.

Ila Waislam wanaoitaka Mahakama ya Kadhi watajua jinsi ya kuiadhibu serikali na CCM.Siyo siri Serikali ya Awamu ya Nne imejijengea sifa mbaya ya kutoa baadhi ya viongozi wakuu kutoa matamko na ahadi za uongo bila aibu.

Inasikitisha serikali kuwa na sifa kama hii kwani watoto wetu wanaona hali hiyo hivyo mwisho wa siku nao watakuwa viongozi; watarithi porojo kama hizi.

Lakini jambo la kushukuru Mungu baadhi ya wananchi wameishaanza kugundua tabia hiyo ya viongozi na kwa upande wa baadhi ya viongozi wa dini wamekuwa wakienda ibada za kuliombea taifa hili ili lisije likatumbukia kwenye machafuko yasiyo ya lazima.

Hivyo wananchi watambue lengo la CCM ni kung’ang’ania kubaki madarakani na siyo kuiletea nchi yetu maendeleo ya kweli na uhakika kama tunavyotamani iwe.

CCM siyo chama cha kuaminika tena.Kwanza Rais Jakaya Kikwete ni Muislamu na alizunguka nchini nzima kunadi ilani ya chama chake na kuahidi angeliingia madarakani angelianzisha mahakama hiyo.

Hivyo namuonea huruma kwani kwa msimamo huo wa serikali uliotolewa na Waziri Chikawe, umethibitisha pasipo shaka kwamba Rais Kikwete na chama chake walikuwa wanatambua kinachoendelea.

Katika hili Waislam waelewe hakuna mtu anapinga wao kufurahia uhuru wa dini yao vile vile wajue uhuru huo umepewa mipaka katika Katiba ya nchi, kwa hiyo wawe makini na aina hii ya wanasiasa.

Kama ni siasa, ni vizuri Waislam wachunguze kwa kina katiba na sera za vyama vyote kabla hawajaanza kupiga kula zao hovyohovyo.

Katika hili , ilani ya CCM iliandaliwa kiujanjaunjanja ili chama hicho kikiingia madarakani baada ya hapo kila mtu abebe mzigo wake.lakini hukumu ya hao waliyowadanganya inatoka mwaka kesho wakati watakapopita kuwaomba muwapigie kura tena.

Mungu Ibariki Tanzania,Mungu Ibariki Afrika

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Julai 5,2009