MADARASA YA CHEKECHEA KUJENGWA KILA KTK SHULE ZA MSINGI-DK.BILAL


Na Mwandishi Wetu,Pwani
MGOMBEA mwenza wa Chama Cha Mapinduzi(CCM),Bilali amesema ifikapo mwaka 2015 kila shule ya msingi kote nchini itapaswa kuwa na darasa moja la wa chekechea.

Dk.Bilali aliyasema hayo leo wakati akiwahutubia wananchi wa wilaya ya Rufiji katika mkutano wa adhara uliofanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi ya Mhoro Kata ya Chumbi mkoani Pwani sambamba na kumnadi mgombea ubunge wa Jimbo la Rufiji Dk. Seif Rashid na mgombea ubunge wa Jimbo la KIbiti,Abdul Marombwa,alisema mpango huo mkakata umeainishwa katika Ilani ya CCM ya mwaka 2010-2015.

Dk.Bilali ambaye jana ndiyo alianza ziara ya kampeni yake rasmi mkoani hapa alisema lengo la mpango huo kuingizwa kwenye ilani hiyo ya CCM, ni chama hicho kupitia serikali yake inataka kuona wanafunzi wa shule wanaomaliza shule za awali wanajiunga na shule za msingi na sekondari na kisha kujiunga na vyuo vikuu.

“Hivi sasa taifa lisilo na wasomi ni dhahiri halitaweza kupiga hatua za kimaendeleo kwa wakati hivyo kwakuwa inapenda kuona wananchi wake wakubwa kwa wadogo wakipita elimu ndiyo maana ilani ya mwaka 2010-2015 imewekea mkazo suala la ukuzwaji wombea sekta ya elimu kwa ngazi zote hivyo nawasii sana wazazi na wananchi kote nchini muwaruhusu watoto wenu waende mashuleni kupata elimu kwani hakuna ulithi usiooza kama elimu.

Huku hotuba yake ikikatishwa mara kwa mara na vibwagizo vya nyimbo za kukisifu chama na kumpongeza rais Jakaya KDikwete kumchagua Dk.Bilali kuwa mgombea mwenza, alisema ili mpango huo utimie wananchi wa kada zote hawana budi kuinga mkono serikali ya ccm ilikuweza ujenzi huo wa madarasa ya wananfunzi wa shule za awali yanajengwa na kuongeza kwa kuwataka wananchi wote wanampatia kura za ndiyo mgombea urais wa ccm,Kikwete kesho mgombea mwenza ataendelea na ziara yake ya kampeni mkoani Kilwa.
.Hotuba ya Dk.Bilal,ya Agosti 24 mwaka huu.

DK.BILAL AITIKISA PWANI


Kamanda wa Chipukizi wa Wialaya ya Kilwa Masoko, Chekeni Omar, akimvisha Skafu Mgombea Mwenza, Mohamed Gharib Bilal, wakati wa mapokezi ya mgombea huyo eneo la Somanga, akitoka Wilaya ya Rufiji kuingia Wialaya ya Kilwa Masoko kuendele na Mikutano ya Kampeni(imepigwa leo Agosti 24 mwaka 2010).

NILIWAKAMATA WATUHUMIWA WAWILI-SHAHIDI

Na Happiness Katabazi

SHAHIDI wa kwanza wa upande wa Jamhuri Konstebo Shaha Mbengwa(31) katika kesi ndogo inayomkabili aliyekuwa Mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la (TBC1),Jerry Murro ya kuomba na kupokea rushwa ya sh milioni 10, ameieleza mahakama kuwa ni yeye ndiye aliyemkamata mshtakiwa wa pili na watatu Edmund Kapama na Deogratius Muggasa.


Mbengwa ambaye alikuwa akitoa ushahidi huo mbele ya Hakimu Mkazi Gabriel Milumbe huku akiongozwa kutoa ushahidi huo na Wakili Mkuu wa Serikali Stanslaus Boniface jana wakati kesi ndogo (trial within a trial) jana ilipoanza kusikilizwa ikiwa ni siku moja tu baada ya hakimu huyo kutoa amri ya kusimamisha usikilizwaji wa kesi ya msingi.

Mbengwa ambaye ni askari kanzu na anafanyakazi katika ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam(ZDCO),Charles Mkumbo, alidai kuwa Januari 31 mwaka huu, Mkumbo alimpatia kazi ya kuwasaka washtakiwa hao wawili na kisha awapeleke ofisini kwake na akaeleza kuwa siku hiyo hakufanikiwa kuwakamata lakini ilipofika Februali mosi mwaka huu, alifanikiwa kuwakamata washtakiwa hao maeneo ya Kinondoni saa nne asubuhi.

Alieleza kuwa baada ya kuwakamata washtakiwa,wakati wanaanza safari ya kuwalete Kituo Kikuu cha Polisi Kati(Central) , njiani Muggasa alianza kutaka kugoma kupelekwa kituoni kwa maelezo kwamba siku hiyo ilikuwa ni siku yake anayotakiwa kwenda Makao Makuu ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU) kuripoti kwani nako huko alikuwa anakabiliwa na tuhuma zingine zinazomkabili.

“Kwasasabu nilikuwa na ofisa mwenzangu ,tulimkubalia hilo ombi lake na tukampeleka hadi TAKUKURU kweli akaripoti kisha akarudi nje tulipokuwa tukimsubiri tukaanza safari ya kuelekea ofisini kwa ZDCO ambapo tulifika ofisini kwa afande Mkumbo saa saba mchana”alidai Konstebo Shaha Mbengwa.

Baada ya kutoa maelezo hayo, karani mmoja wa mahakamani hapo alipenyesha karatasi iliyokuwa ikienda kwa hakimu Milumbe ambapo hakimu huyo aliisoma karatasi hiyo na kisha kutangaza ndani ya chemba kwamba amepata ujumbe kutoka uongozi wa juu wa mahakama unaomtaka atoke ndani ya chemba aende kuendeshea kesi hiyo inayofuta umati mkubwa wa watu kwenye mahakama ya wazi na akairisha kesi hiyo hadi saa saba mchana.

Lakini katika hali isiyotarajiwa ilipofika saa 6:10 mchana, Hakimu Milumbe aliwaita washitakiwa na mawakili wa utetezi Pascala Kamala,Majura Magafu na wakili Mkuu wa Serikali, Stanslaus Boniface ambaye awali alisema upande wa Jamhuri katika kesi hiyo ndogo kwa jana umeleta mashahidi wa tano akiwemo ZDCO-Charles Mkumbo, kwamba hataweza kusikiliza kesi hiyo saa saba mchana kwasababu anajisikia vibaya hivyo akaiairisha hadi leo saa nne asubuhi.

Aidha tango hilo la kuamishwa kwa kesi hiyo toka chemba kupelekwa mahakama ya wazi, kuliwafurahisha umati wa watu wakiwemo waandishi wa habari za mahakama ,washtakiwa wenyewe, maaskari polisi, wanafunzi wa sheria ambao wanakuja mahakamani hapo kuudhulia mafunzo kwa vitendo na wananchi mbalimbali walisema wamefurahishwa sana na uamuzi huo wa uongozi wa mahakama kwani walikuwa wakisimama madirishani, na wengine kulazimika kusimama nje huku wasifahamu kinachoendelea ndani ya kesi hiyo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne Agosti 20 mwaka 2010

POLISI WALINILAZIMISHA NITOE MAELEZO YA KUMKANDAMIZA JERRY MURRO-MUGGASA

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa utetezi katika kesi ya kuomba rushwa ya Sh milioni 10 inayomkabili aliyekuwa Mtangazaji wa Shirika la Utangazaji wa Taifa(TBC1),Jerry Murro na wenzake, umeiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu , usipokee maelezo ya onyo ya mshtakiwa wa tatu(Deogratius Mugassa) kwa maelezo kama kielelezo kwa madai kwamba mshtakiwa aliteswa na polisi wakati akichukuliwa maelezo hayo.


Sambamba na hilo baadhi ya wananchi wakiwemo waandishi wa habari wamelalamikia hatua ya kesi hiyo ambayo inavuta hisia za watu wengi kuendeshewa chemba, kwani wananchi hao na waandishi wa habari wengi wanashindwa kuingia kusikiliza kesi hiyo kwasababu ya uhaba wa nafasi na kuongeza kuwa wanashangazwa na hatua hiyo kwani wakati mwingine mahakama za wazi za mahakama hiyo zinakuwa wazi lakini hakimu huyo anaendeshea kesi hiyo inaendeshewa chemba na kuuomba uongozi wa mahakama ufanye kila linalowezekana kesi hiyo iwe inasikilizwa katika mahakama ya wazi.

Ombi hilo liliwasilishwa kwa njia ya mdomo jana na wakili wa utetezi Majura Magafu mbele ya Hakimu Mkazi Gabrile Milumbe ikiwa ni sekunde chache baada ya shahidi wa kwanza wa upande mashitaka,Staff Sajenti Peter Jumamosi alikuwa akiongozwa na Wakili Mkuu wa Serikali Stanslaus Boniface kutoa ushahidi wake na akaomba atoe maelezo hayo ya onyo ya Muggasa kama kielelezo.

Magafu alidai mteja wake(Muggasa) anaiomba isipokee maelezo hayo kama kielelezo kwasababu Februali 3 mwaka huu, wakati anachukuliwa maelezo hayo na shahidi huyo, aliteswa na alikuwa akishinikizwa na Mkuu wa Upelelezi wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam(ZDCO),Kamishna Msaidizi wa Polisi, Charles Mkumbo na Kamishna Kasala ambao walimtaka mshtakiwa huyo atoe maelezo yatakayomgandamiza mshatiwa wa kwanza(Murro) ambaye jeshi la polisi limekuwa likimsaka muda mrefu kwasababu amekuwa akiwadhalilisha kwenye vyombo vya habari.

“Naomba mahakama isipokee kilelezo hiki kwani mteja wangu amenieleza alinyanyaswa wakati akichukuliwa maelezo na alilazimishwa na polisi akubaliane na maelezo wanayoyataka polisi..na manyanyaso aliyopata ni aliambiwa atoe maelezo yatakayomkandamiza Murro kwasababu polisi wanamtafuta muda mrefu kwani amekuwa akiwadhalilisha na wakati mteja wangu anachukuliwa maelezo hayo ZDCO-Mkumbo, Kamishna Kasala walikuwepo pembeni ambapo walikuwa wakimuamrisha shahidi huyo(Jumamosi) achukue maelezo ya mshtakiwa huyo ambayo yanamgandamiza Jerry Murro na kwamba hayo yalikuwa ni maelekezo maalum toka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi”alidai Magafu.

Baada ya Magafu kumaliza kuwasilisha pingamizi hilo la kupinga kielezo hicho kisipokelewe, Hakimu Milumbe alisema anatoa amri ya usikilizaji wa kesi ya msingi usimame na kuiairisha kesi hiyo hadi leo ambapo kesi ndani ya kesi(trial within a trial) itakapoanza kusikilizwa na kaumuru pande zote zilete mashahidi kama wanao.

Februali mwaka huu, Murro, Edmund Kapama na Muggasa walifikishwa mahakamani hapo wakikabiliwa na makosa ya kushawishi na kuomba rushwa toka kwa Mhasibu wa Halmashauri ya Bagamayo Michael Wage.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Agosti 19 mwaka 2010

DHAMANA YA MTOTO WA KINGUNGE YAZUA UTATA

Na Happiness Katabazi

IKIWA ni siku moja tu tangu Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Gabriel Milumbe atoe masharti ya dhamana kwa mtoto wa mwanasiasa mkongwe nchini,Kingunge Ngombale Mwiru, Tonny Mwiru(36),anayekabiliwa na makosa ya kula njama,kuwasilisha nyaraka za uongo,kughushi na kujipatia sh milioni 424 kwa njia ya udanganyifu baadhi ya mawakili wa serikali wamesema wanakusudia kukatia masharti hayo ya dhamana Mahakama Kuu haraka iwezekanavyo.


Juzi Hakimu Milumbe alisema ili mshitakiwa huyo apate dhamana ni lazima asaini bondi ya Sh milioni 10 na kuwasilisha hati ya mali yenye thamani ya Sh milioni kumi na mshtakiwa huyo alishindwa kutimiza masharti hayo ya dhamana akapelekwa mahabusu.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Tanzania Daima jana mahakamani hapo, Mawakili Waandamizi wa Serikali na wale wa kujitegemea kwa masharti ya kutotaka majina yao walisema wameshtushwa masharti hayo ya dhamana yaliyotolewa na hakimu Milumbe kwani ni wazi kabisa yanakwenda kinyume na masharti ya dhamana yaliyoainishwa kwenye kifungu cha 148((5)(e) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

“Kifungu hicho cha sheria ya jinai kinasema wazi mshitakiwa yoyote anayekabiliwa na makosa ya fedha taslimu au mali ambazo zinazaidi ya thamani ya Sh milioni ,basi mshitakiwa huyo atapaswa awasilishe nusu ya fedha taslimu au hati ya mali yenye nusu ya thamani hiyo na sivinginevyo:

“Sasa kwenye kesi ya mtoto wa Kingunge anakabiliwa na makosa hayo yakujipatia sh milioni 424 lakini cha kushangaza hakimu Milumbe ametoa masharti ambayo yanajumla ya thamani ya Sh milioni 20….hivi katika akili ya kawaida nusu ya sh milioni 424 ni sh milioni 20?....tunajipanga kukatia rufaa uamuzi wa hakimu huyo kwani sheria ya makosa ya jinai bado haijabadilishwa na bunge hivyo hatufikirii kwamba sheria hiyo ilibadilika juzi kwasababu ya mtoto wa Kingunge kushitakiwa na ikashindwa kubadilika kwa washtakiwa wengine ambao ni wananchi wa kawaida wanapofikishwa mahakamani”alisema Wakili Mwandamizi wa Serikali ambaye aliomba jina lake liifadhiwe.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama Democratic(DP),Mchungaji Christopher Mtikila alisema sheria ipo wazi na alishangazwa na uamuzi wa hakimu huyo ambao alisema umeipaka matope mahakama hiyo na kuongeza kwa kumuasa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP),Eliezer Feleshi pamoja na vijana wake wakakate rufaa Mahakama Kuu kupinga masharti hayo ambayo yanasigina sheria ya nchini.

“Au huyo Tonny ni kwasababu ni mtoto wa mzee Kingunge ndiyo maana hakimu alibabaika na kujikuta anatoa masharti yanayokinzana na kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002?Au inapofika watoto wa vigogo kuburuzwa mahakamani ndiyo basi baadhi ya mahakimu wetu wanaamua kupindisha sheria makusudi?.

“Hii aikubaliki DPP na vijana wake tunataka wafanye haraka wakatie rufaa masharti hayo kwani watanzania wote bado tunakumbuka ni aliyekuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Nyigulila Mwaseba alilegeza masharti ya dhamana kwa aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba ambaye alikuwa akikabiliwa na kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya Sh bilioni 221 na DPP alikata rufaa Mahakama Kuu na Jaji Geofrey Shahidi alitengua masharti hayo ya Mahakama Kisutu na kutaka Liyumba apewe dhamana kwa mujibu wa kifungu cha 148(5)(e) cha Sheria hilo, lakini hadi Mei 24 mwaka huu, Mahakama hiyo Kisutu ina mhukumu kwenda jela miaka miaka mwili alishindwa kutimiza masharti hayo ya dhamana.

Hata hivyo gazeti hili lilifanya jitihada za kuwasilisha na DPP-Feleshi ili kujua msimamo wa ofisi yake kuhusiana na madai hayo, simu zake ya kiganjani ilikuwa haipatikani.

Kabla ya hakimu Milumbe kutoa masharti ya dhamana,alimtazama usoni Tonny sekunde kadhaa na kisha alimuuliza kama mzee Kingunge Ngombale-Mwiru ni baba yake , naye alijibu kuwa ndiyo.

“Ujue baba yako tunamheshimu sana, sasa kwanini wewe mtoto wake unajihusisha na mambo kama haya?”.Alihoji Hakimu Milumbe.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Agosti 19 mwaka 2010

MTOTO WA KINGUNGE KORTINI KWA UTAPELI WA MIL.424/-

Na Happiness Katabazi

MTOTO wa mwanasiasa mkongwe nchini, Kingunge Kombale - Mwiru, Tony Mwiru (36), jana alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, akikabiliwa na makosa ya kula njama, kuwasilisha nyaraka za uongo, kughushi na kujipatia sh milioni 424 kwa njia ya udanganyifu.


Mbele ya Hakimu Mkazi, Gabriel Milumbe, Mwendesha Mashitaka, Inspekta wa Polisi, Emma Mkonyi, alidai kuwa mshitakiwa huyo anakabiliwa na mashitaka manne.

Shitaka la kwanza ni la kula njama ambapo yeye na wenzake ambao hawakuwepo mahakamani jana, waliwasilisha nyaraka za uongo katika Kampuni ya SCI (TZ) Ltd na kujipatia sh 424,488,799.29.

Inspekta Mkonyi alidai shitaka la pili ni la kughushi. Katika shitaka hilo, Mwiru anadaiwa kughushi maombi ya ujumbe kasi wa kuamishia fedha wenye namba 17 wa Agosti 27 mwaka 2008, kwa nia ya kuonyesha ujumbe huo ni halali na ulitolewa na Savishankar Resman ambaye ni Mkurugenzi wa SCI (TZ), Ltd wakati si kweli.

Aidha, alidai shitaka la tatu ni la kuwasilisha nyaraka za uongo. Inadaiwa kuwa Agosti 29, mwaka 2008 katika Benki ya Barclays (TZ), iliyopo Mtaa wa Ohio jijini, mshitakiwa aliwasilisha nyaraka za uongo ambazo ni fomu ya maombi ya ujumbe kasi yenye namba E7 kwa mfanyakazi wa benki hiyo, Bitun Chiza.

Shitaka la nne ni la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, ambapo inadaiwa kuwa Oktoba 9, mwaka 2008, katika Benki ya CRDB, Tawi la Kijitonyoma, alijipatia kiasi hicho kupitia akaunti namba 01j014293000, akionyesha Kampuni ya SCI (TZ), Ltd imeidhinisha ilipe kiasi hicho cha fedha kwa kampuni ya Temm Power Ltd.

Hata hivyo mshitakiwa alikana mashitaka yote na Inspekta Mkonyi alidai upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika na kuomba tarehe ya kutajwa.

Baada ya kumaliza kusikiliza mashitaka hayo, Hakimu Milumbe alimuuliza mshitakiwa kama mzee Kingunge Ngombale - Mwiru ni baba yake, naye alijibu kuwa ndiyo.

“Ujue baba yako tunamheshimu sana, sasa kwanini wewe mtoto wake unajihusisha na mambo kama haya?” alihoji Hakimu Milumbe.

Mshitakiwa huyo amerejeshwa mahabusu baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Agosti 18 mwaka 2010

KIZIMBANI KUJIFANYA POLISI

Na Happiness Katabazi

MSHTAKIWA wa tatu katika kesi ya kuomba rushwa ya Sh milioni 10 inayomkabili aliyekuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC1),Jerry Murro, Deogratius Mgassa kwa mara nyingine tena jana alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na kesi mpya ya kujifanya ni Ofisa wa Jeshi la Polisi na kisha kujipatia sh milioni 19 kwa njia ya udanganyifu.


Mbele ya Hakimu Mkazi Devota Kisoka, Wakili wa serikali Zuberi Mkakatu alidai kuwa Mugassa anakabiliwa na mashtaka matatu.Shitaka la kwanza ni la kula njama na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kwamba mshtakiwa huyo na wenzake ambao hawapo mahakamani.

Wakili Mkakatu alidai shtaka la pili ni la Mugassa kujifanya Ofisa wa Jeshi la Polisi kwamba Aprili 28 mwaka huu, katika Bar ya Rose Garden huko Mikocheni, yeye na wenzake walijitambulisha kwa Rose Azizi kuwa wao ni maofisa wa jeshi la polisi.

Mkakatu alidai shitaka la tatu ni la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kwamba kati ya Mei na Aprili mwaka huu, katika Bar hiyo ya Rose Garden walijipatia sh milioni 19 kutoka kwa Rose Azizi baada ya kujifanya wao ni maofisa wa jeshi hilo na kwamba fedha hizo walizopewa watazitumia kuweka mtego wa kuwakamata wezi walioiba matofari mawili wa madini ya dhahabu wilayani Nzega.

Hata hivyo mshtakiwa huyo alikana mashitaka yote matatu na wakili Mkakatu aliambia mahakama kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika hivyo anaomba kesi hiyo ipangiwe tarehe ya kutajwa.

Aidha Hakimu Mkazi Kisoka alisema ili mshtakiwa huyo apatiwe dhamana ni lazima yeye mwenyewe ajidhamini fedha taslimu sh milioni 10 au kuwasilisha hati yenye thamani hiyo na pia awe na wadhamini wawili ambao wanasaini bondi ya sh milioni 10.Hata hivyo mshitakiwa huyo alishindwa kutimiza masharti hayo ya dhamana na amerudishwa rumande hadi Agosti 25 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja tena kwaajili ya kutajwa.

Hii ni kesi ya pili tofauti inayomkabili Mugassa mahakamani hapo.Kesi ya kwanza ni ya kuomba rushwa ya sh milioni 10 inayomkabili yeye na Jerry Murro na Edmund Kapamba ambayo inasikilizwa na Hakimu Mkazi Gabrile Mirumbe, ambapo wanakabiliwa na mashitaka matatu, likiwemo la kula njama za kutaka kupokea rushwa kutoka kwa aliyekuwa mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Karoli Wage ambapo pia wanadaiwa kujifanya wao ni maofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU).

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Agosti 13 mwaka 2010

JAJI KIONGOZI NAYE APATA AJALI

Na Happiness Katabazi

SIKU mbili tu baada ya Jaji Mkuu wa Tanzania Agustino Ramadhani anusurike kifo katika ajali mbaya ya gari, jana Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu, Fakihi Jundu naye amenusurika kifo baada ya gari alilokuwa akisafiria kupata ajali mbaya ya gari.
Habari za kuaminika zilizopatikana kutoka ndani ya msafara wa Jaji Jundu, zinasema ajali hiyo ilitokea jana saa 7:45 mchana kilometa chache kufika Wilaya ya Kasuru mkoani Kigoma.


Msafara huo, ulikuwa ukitokea mkoani Shinyanga kuelekea mkoani Kigoma akitumia gari aina ya Toyota Land Cruser V8 akiwa na mlinzi wake, lilipinduka na kuingia porini.

Baada ya ajali hiyo, Jaji Jundu alikimbizwa kwenye hospitali ya Wilaya ya Kasuru kwa ajili ya matibabu.

Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Francis Mutungu, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema hali ya Jaji Jundu si nzuri kutokana na majereha aliyopata.

‘Ni kweli Jaji Jundu amepata ajali ya gari na hivi sasa ofisi yangu inafanya jitihada za kumrejesha Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu na kwamba hata Jaji Mkuu ambaye Jumatatu wiki hii naye alipata ajali ya gari akiwa kwenye msafara huo wa ziara ya kukakugua Tume ya Utumishi wa Mahakama nchini, tayari amerejeshwa Dar es Salaam kwa ajili ya kukaguliwa afya yake,” alisema Mutungi.

Jumatatu wiki hii, Jaji Mkuu Augustino Ramadhani, alipata ajali katika eneo la Simbo mkoani Tabora baada ya gari alilopanda kupinduka na kugonga kisiki.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi,Agosti 12 mwaka 2010





KESI YA JERRY MURRO YAAHIRISHWA


HATIMAYE Hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, Gabriel Milumbe, amekubali ombi la upande wa Jamhuri katika kesi ya kuomba rushwa ya sh milioni 10 inayomkabili aliyekuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC1), Jerry Muro na wenzake wawili la kuahirisha usikilizaji wa kesi hiyo hadi wiki ijayo.

Hakimu Milumbe alikubali ombi hilo kwa kuwa Wakili Mkuu wa Serikali Stanslaus Boniface ambaye anaendesha kesi hiyo yuko likizo.

Mbali na Muro, washitakiwa wengine ni Deogratius Mgasa na Edmund Kapama wanaotetewa na mawakili wa kujitegemea Richard Rweyongeza, Majura Magafu na Pascal Kamala.

Hakimu Milumbe pia alisema anaahirisha kesi hiyo kwa kuwa hali yake kiafya si nzuri, hivyo anajiandaa kwenda hospitali. Kesi imeahirishwa hadi Agosti 18.

Juzi, Hakimu Milumbe aliuchachamalia upande wa Jamhuri kwamba kama haupo tayari kuendelea na kesi hiyo, ataifuta na kuongeza kuwa hayupo tayari kuahirisha kesi hiyo kwa sababu ya wakili Stanslaus kutokuwapo mahakamani.

Washitakiwa hao wanakabiliwa na mashitaka matatu, likiwemo la kula njama za kutaka kupokea rushwa kutoka kwa aliyekuwa mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Karoli Wage.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Agosti 12 mwaka 2010


HAKIMU ATISHIA KUIFUTA KESI YA JERRY MURRO

Na Happiness Katabazi

HAKIMU Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Gabrile Milumbe, ameuchachamalia upande wa utetezi katika kesi ya kuomba rushwa ya sh milioni 10 inayomkabili aliyekuwa Mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC1), Jerry Muro, na wenzake kwamba kama haupo tayari kuendelea na kesi hiyo, ataifuta.
Mbali na Murro washtakiwa wengine ni Deogratius Mgasa na Edmund Kapama wanaotetewa na mawakili wa kujitegemea Richard Rweyongeza, Majura Magafu na Pascal Kamala.


Hakimu huyo alitoa angalizo hilo baada ya wakili wa Serikali Zuberi Mkakatu, kuiomba mahakama kuahirisha kesi hiyo iliyokuja kwa ajili ya kuanza kusikiliza ushahidi wa upande wa mashtaka kwa madai kuwa wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, ambaye amekuwa akiendesha shauri hilo tangu awali, yuko likizo.

Baada ya wakili huyo kutoa maelezo hayo, Hakimu Milumbe alisema hayuko tayari kuahirisha usikilizwaji wa kesi hiyo jana na kuongeza kuwa kama upande wa serikali hauko tayari kuendelea nayo, ataifuta kesi hiyo.

Hata hivyo hakimu huyo ambaye alionekana kukerwa na upande wa serikali kuahirisha kesi hiyo kila mara, aliamua kuiahirisha kwa nusu saa na baadaye kuamuru shahidi wa upande wa mashtaka aanze kutoa ushahidi wake.

Majira ya saa nne asubuhi, pande zote mbili ziliingia tena mahakamani, huku umati wa watu ukiwa umefurika kusikiliza kesi hiyo ambayo imekuwa ikivuta hisia za wengi.

Akitoa ushahidi wake, shahidi wa kwanza upande wa mashtaka, Staff Sajenti, Peter Jumamosi, alidai kuwa Februari Mosi mwaka huu wakati akiwa ofisini kwake katika Kituo Kikuu cha Polisi Kati, bosi wake ambaye ni Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Charles Mkumbo, alikuja na watuhumiwa wawili wa kesi hiyo ili achuke maelezo yao.

“Siku hiyo, nikiwa ofisini pale katika Kituo Kikuu cha Polisi Kati, ilipofika majira ya saa tisa, bosi wangu ambaye ni Mkuu wa Upelelezi wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam (ZDCO), Charles Mkumbo, alikuja na watuhumiwa wawili, akanipa mtuhumiwa wa pili, Deogratius Mgasa, nimhoji kuhusiana na madai ya kuomba rushwa,” alidai Peter Jumapili.

Wakati akitoa maelezo hayo, shahidi huyo alikatishwa na swali la Hakimu Milumbe ambaye alimuulizwa wakili wa serikali yalipo maelezo ya onyo ya mshtakiwa Mgassa na kujibiwa kwamba hawana maelezo hayo.

Wakili huyo wa serikali alidai kuwa maelezo hayo bado yako polisi, hali iliyosababisha hakimu kumtaka shahidi asitishe kutoa ushahidi kwa sababu mahakama haiwezi kusikiliza ushahidi wake bila kuwepo maelezo ya onyo.

“Lazima tufuate taratibu za kimahakama…mi’ sipendi kupoteza muda bure, awali tulikubaliana upande wa jamhuri mlete mashahidi watano kwa siku mkakubali …sasa hao mashahidi watano mliokubali kwamba mngewaleta leo (jana) wako wapi? Naairisha kesi hii hadi kesho (leo) na mashahidi watano hakikisheni wanafika bila kukosa,” alisema Hakimu Milumbe.

Washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka matatu, likiwemo la kula njama za kutaka kupokea rushwa kutoka kwa aliyekuwa mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Karoli Wage.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano Agosti 11 mwaka 2010

JAJI MKUU ANUSURIKA AJALINI

Na Happiness Katabazi

JAJI Mkuu wa Tanzania, Agustino Ramadhani, amepata ajali katika eneo la Simbo mkoani Tabora baada ya gari alilopanda kupinduka na kugonga kisiki.
Taarifa zilizolifikia Tanzania Daima jana asubuhi kutoka mkoani Tabora, zimedokeza kuwa Jaji Ramadhani alipatwa na ajali hiyo wakati akiendelea na ziara ya kukagua Tume ya Utumishi wa Mahakama.


Gari la Jaji Mkuu lilipinduka mara moja na kisha kuanza kuserereka lakini likazuiwa na kisiki; jambo ambalo kwa kiasi kikubwa limezuia kutokea kwa maafa zaidi.

Tanzania Daima, iliwasiliana na Jaji Ramadhani na alithibitisha kupata ajali katika eneo la Nzega alipokuwa akitokea mkoani Singida kwa shughuli za kikazi.

Alisema walipofika eneo la Nzega ndipo gari lake lilipopata ajali; lakini hata hivyo alisema hali yake inaendelea vizuri kwa sababu hakupata majeraha.

“Eh! Yaani tayari gazeti lenu limeishapata habari kuhusu mimi kupata ajali? Ni kweli gari nililopanda aina Land Cruiser V8 limepata ajali lakini nashukuru tumetoka salama,” alisema.

Jaji Mkuu aliongeza kuwa mlinzi na dereva wake pia wametoka salama katika ajali hiyo na walibadilishiwa gari jingine baada ya mkasa huo na kuendelea na safari.

Jaji Ramadhani alibainisha kuwa katika ziara hiyo ameongozana na Jaji Kiongozi, Fakihi Jundu, Jaji Ibrahim Juma, Wakurugenzi wa tume hiyo, na maofisa wengine wa mahakama.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Agosti 10 mwaka 2010

WASHITAKIWA FEDHA HARAMU WABADILISHIWA MASHITAKA

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya kula njama na kuhamisha fedha kwa njia haramu sh milioni 338.9 inayomkabili Ofisa wa Mamlaka ya Mapato (TRA), Justice Katiti na wenzake watano umebadilisha hati ya mashitaka.


Mbele ya Hakimu Mkazi, Alocye Katemana, jana Wakili Kiongozi wa Serikali, Fredrick Manyanda, aliyekuwa akisaidiana na Mkuu wa Idara ya Sheria kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ben Lincoln, waliiambia mahakama kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili kubadilisha hati ya mashitaka.

Wakili Kiongozi wa Serikali Manyanda alisema kwa mujibu wa hati hiyo ya mashitaka ambayo mashitaka yote kumi yalikuwa yakiwakabili washitakiwa wote na kwa mujibu wa mashitaka hayo washitakiwa wote hawapaswi kupewa dhamana lakini kutokana na mabadiliko hayo, wameamua kumuondoa mshitakiwa wa sita, Joseph Rutto, katika shitaka la sita na saba ambayo ni mashitaka ya kuhamisha fedha kwa mtandao kwa njia ya haramu na badala yake mshitakiwa huyo atakabiliwa na shitaka la kwanza ambalo ni la kula njama ambalo kisheria linadhaminika.

Manyanda alieleza kuwa kwa mabadiliko hayo washitakiwa wengine watano wataendelea kukabiliwa na mashitaka yote.

Aidha, Hakimu Katemana alisema ili Rutto apate dhamana ni lazima awe na wadhamini wawili wa kuaminika ambao watatoa nusu ya kiasi hicho cha fedha au watawasilisha hati za mali zenye thamani ya nusu ya kiasi hicho cha fedha.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti 9 mwaka huu, itakapotajwa tena kwa kuwa upelelezi haujakamilika.

Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Fortunatus Muganzi, Robert Mbetwa, Gidion Otullo na Godwin Paulla ambao kwa pamoja wanadaiwa Septemba 29 mwaka 2008, jijini Dar es Salaam, walighushi maombi ya ujumbe wa kasi wa kuhamisha fedha Na. E.17 wa Benki ya Barclays na unaoonyesha kwamba Kampuni ya Tourism Promotion Services (Tanzania) Limited unaiomba benki hiyo uilipe Kampuni ya East Africa Procurement Services Limited Tanzania, sh milioni 338.9 kwa sababu ilifanya kazi ya kuuza maturubai na vifaa vya hoteli, huku wakijua si kweli.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Agosti 5 mwaka 2010

UJAMBAZI HUU TUUWEKEE MIKAKATI KUUTOKOMEZA

Happiness Katabazi

HIVI sasa kumeibuka aina mpya ya ujambazi ambapo mtu anapotoka kwenye mihangaiko yake ya kila siku hufuatiliwa kila anakokwenda na hatimaye kuuawa.

Uhalifu huu unalitia doa taifa letu ambalo kwa miaka mingi limekuwa na sifa ya amani na utulivu licha ya kuwapo kwa matukio ya kinyama yanayotokea mara moja moja.

Aina hii ya uhalifu inafanywa na watu ambao naweza kusema si wenye kuhitaji mali za wahusika bali roho zao, kwa kuwa kila wanapofanya uvamizi hawachukui chochote isipokuwa kuyakatisha maisha yao.

Watu wanaouawa ni tegemeo kubwa taifa na familia zao kwa hiyo vifo vyao husababisha huzuni na kusuasua kwa maendeleo yaliyokusudiwa.

Kadiri tunavyozidi kwenda mbele ndivyo jamii inavyozidi kuingiwa na roho za kikatili zilizojaa tamaa ya fedha na kisasi ambavyo ni kukiuka maagizo ya Mungu ya kupendana, kushirikiana.

Mwingiliano wa jamii tofauti katika nchi zinazotuzunguka na ukuaji wa teknolojia ya sayansi (utandawazi), umasikini na sababu nyinginezo ni miongoni mwa mambo yanayochangia kushamiri kwa uhalifu hapa nchini na duniani kwa ujumla.

Uanzishaji wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki (EAC) unaweza kuwa chachu ya kuongezeka kwa vitendo hivyo, kwa kuwa wananchi wa nchi wanachama wana uhuru wa kuingia na kutoka katika nchi zilizomo kwenye jumuiya hiyo bila ya kuwepo kwa vikwazo kama vilivyokuwapo awali.

Baadhi ya wananchi niliozungumza nao wameanza kuingiwa na wasiwasi kwamba kuzuka kwa aina hiyo mpya ya ujambazi ni matokeo ya nia njema ya viongozi wetu kuridhia kutekelezwa na Itifaki ya Soko la Pamoja la nchi za EAC?

Ujambazi wa kutumia mabomu ambayo mara kwa mara tumekuwa tukisikia yakitumika nchini Somalia na hivi karibuni ulijikita katika mji wa Kampala nchini Uganda na raia wa Uganda 75 waliuawa na bomu lililolipuka wakati wananchi hao wakitazama fainali ya Kombe la Dunia zilizomalizika Julai 11 mwaka huu.

Baadhi ya wananchi wa Somalia wanaanza kufaidika na utekelezaji wa Soko la Pamoja ambalo moja ya misingi ya soko hilo inatoa haki watu kuzagaa katika nchi za Afrika Mashariki bila vizuizi na kufanya kazi.

Sasa tunapofungua mipaka ya nchi yetu watu waingie kutoka Kenya,Uganda, Rwanda na Burundi waingine Tanzania kutafuta ajira na kuwapatia haki ya kuhamia (right of establishment).

Lakini aina ya ujambazi wenye ukatili na unyama wa kupindukia kwa wanapoenda kuua watu bila kupora hata kitambaa cha kujifutia jasho, ni mpya, hatujawahi kuusikia hapa nchini ndiyo maana tunapata woga wa kufanya shughuli zetu.

Uhalifu ambao mara kwa mara umekuwa ukitumika hapa nchini ni ule wa watu kuvunja nyumba za watu na kupora mali, kuiba benki na wakati mwingine ukisikia kuna vifo vimetokea kwenye tukio la uporaji ujue kulikuwa na ubishani kati ya mporaji na mporwaji.

Matukio ya kukatisha maisha ya watu pasi kuchukua chochote ni nadra kuyasikia lakini sasa yanaanza kushamiri kwa kasi ya aina yake huku yakiwahusisha zaidi watu wenye nyadhifa fulani au wafanyabiashara wakubwa.

Tanzania inapaswa kuwa makini zaidi hivi sasa ambapo tumeingia kwenye jumuiya ya ushirikiano wa Afrika Mashari kwani kuna majirani zetu ambao baadhi yao bado mikono yao inachuruzika damu za mauaji ya kimbari.

Mfano katika mauaji ya kimbari yaliyotokea Rwanda mwaka 1994 , mauaji yote yaliyotokea kabla ya tarehe ile iliyowekwa na Umoja wa Mataifa(UN), yana sura ya kimbari vile vile.

Lakini ukiyachunguza mauaji hayo yatawanasa hawa ambao ni wahanga wa mauaji ya baadaye.

Kwa hiyo ina maana kama Wahutu waliua na Watutsi na wakalipiza kisasi. Unapotambua mauaji ya pili ya mwaka 1994 ambapo baadhi ya Watutsi waliuawa na Wahutu, bado haujagusa wala kuutoa mzizi wa fitina.

Sasa leo hii serikali iliyopo madarakani nchini Rwanda chini ya Rais Paul Kagame iliwahi kusikika ikilalamikia adhabu ndogo wanazopewa washitakiwa wa mauaji ya kimbari wanaoshtakiwa katika Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari (ICTR) yenye makao yake makuu mjini Arusha.

Serikali hiyo inaona adhabu hizo ni sawa na kuwapa huduma bora wauaji ambao hawakujali utu wa wenzao wakati wakifanya au kuhamasisha ukatili.

Ndiyo maana sasa tutaona vituko vya mauaji kwa mtindo mpya yanaanza kutokea hapa nchini. Na katika kuhamishia mtindo huo mpya wa uuaji hapa kwetu, ndipo Watanzania hata wanataaluma wetu kama aliyekuwa Mhadhiri mwandamizi wa Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Juani Mwaikusa (58) aliuawa wiki iliyopita.

Wapangaji wa mauaji ya kimbari ni sawa kama watuhumiwa na washtakiwa wa kesi za mauaji hayo, ambayo kimsingi ni sawa na ujambazi.

Kwa hiyo kila tukio la mauaji yakitokea litakuwa na sura ya ujambazi kama tukio la mauji ya Profesa Mwaikusa.

Sisi Watanzania tungependa kuliasa Jeshi la Polisi kwamba wanachoweza kufanya ni kutambua kwamba mazingira ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki yamebadilika. Ulinzi na usalama ni jambo gumu na nyeti.

Uwepo wa vitendo vya ujambazi vinavyolitikisa taifa letu hivi sasa visipojulikana chimbo lake ni nini, tutafikia hali ya mabomu kulipuana mitaani.

Sheria zetu za ulinzi na usalama nazo ni vema zikatupiwa jicho ili usalama wa raia na mali zao usiwe shakani kama ilivyoanza kujionyesha hivi sasa.

Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Jeshi la Polisi IGP), Idara ya Usalama wa Taifa, Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Jeshi la Magereza ni vizuri yakafanya kazi pamoja ili kudhibiti hali hii.

Yaweke mikakati mipya ya kukabiliana na wimbi la wahamiaji ambao baadhi yao wana hulka na kujihusisha na vitendo vya kihalifu.

Vyombo hivyo vya ulinzi na usalama vijaribu kuzuia watu ambao wana historia ya uhalifu nchini mwao, kwa kuwazuia kuingia nchini kufanya chochote, iwe ni kutembea, kufanya kazi au kufanya biashara.

Kwahiyo, mabalozi wetu wa nchi za nje wafanye hiyo kazi, hatutaki watu wenye historia za kihalifu kuja hapa nchini kwetu. Na hilo likifanikiwa litakuwa limefanikiwa kuvunja minyororo ya wahalifu hapa nchini.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili,Julai 25 mwaka 2010

KIFO CHA MWAIKUSA:PIGO KWA TASNIA YA SHERIA


Happiness Katabazi

WIKI hii tasnia ya wanasheria nchini, Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na taifa kwa ujumla lilipata pigo baada ya kuondokewa na gwiji la sheria nchini, Profesa Juani Timoth Mwaikusa (58), ambaye aliuawa kinyama kwa kumimiwa risasi mwilini mwake na watu wasiojulikana.

Licha ya wauaji hao kutojulikana, Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Charles Kenyela, ameuleza umma kuwa watu hao wanasadikiwa kuwa ni majambazi.

Vilio, mshtuko, kwiki, mshangao, wasiwasi na majonzi vilitawala ndani ya familia ya marehemu ambaye alikuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kada ya wanasheria na taifa kwa ujumla muda mfupi baada ya kupokea taarifa ya kifo hicho kilichotokea Julai 13 mwaka huu, saa nne usiku nyumbani kwa marehemu eneo la Salasala.

Katika mahojiano ya Tanzania Daima Jumapili na wanataaluma wa sheria walitoa maoni yao jinsi walivyomfahamu marehemu na mchango wake kwa taifa.

Jaji Mkuu wa Tanzania Agustino Ramadhani , alisema taifa limepoteza mtu hodari kwenye taaluma ya sheria.

Alisema wakati wa rufaa ya kesi ya mgombea binafsi iliyofunguliwa na Mchungaji Christopher Mtikila, marehemu alikuwa kiongozi wa jopo hilo akisaidiwa na Januari Msofe, Eusebio Munuo, Natalia Kimaro, Mbarouk Mbarouk, Sauda Mjasiri na Bernard Ruhanda kusikiliza rufaa hiyo.

Marehemu aliitwa mahakamani kama rafiki wa mahakama kutoa maoni yake katika kesi hiyo na alifanya hivyo katika hukumu ya Mahakama ya Rufaa iliyoandaliwa na yeye na majaji wenzake sita, hawakukubaliana na maoni ya gwiji huyo wa sheria nchini lakini kutokubalina na mawazo yake si kukosana naye.

Ikumbukwe kuwa Aprili 11 mwaka huu, siku hiyo mvutano wa kisheria uliendelea katika Mahakama ya Rufaa, miongoni mwa magwiji wa sheria, ambao waliitwa kutoa maoni yao kama marafiki wa mahakama kuhusu hukumu ya Mahakama Kuu iliyoruhusu mgombea binafsi nchini.

Magwiji hao ni Mkuu wa Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Palamagamba Kabudi, Mkurugenzi wa Mashitaka wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (DDP), Othman Masoud na marehemu Profesa Juani.

Walikuwa wanaishauri Mahakama ya Rufaa kabla haijatoa hukumu ya rufaa iliyofunguliwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali mwaka jana kupinga hukumu ya Mahakama Kuu iliyoruhusu mgombea binafsi, katika kesi hiyo.

Binafsi nimeguswa na msiba huo hasa ninapoikumbuka siku hiyo kwani Profesa Mwaikusa wakati akitoa maoni yake alikuwa pia akitumia mikogo ya wananasheria wanayoitumia wakati kesi zinaposikilizwa.

Mwaikusa alilieleza jopo lile kuwa ni suala la haki za binadamu na kwamba mahakama kwa mamlaka yake, haina kikomo cha kujadili haki hiyo.

Alisema Katiba ya nchi ipo kwa ajili ya kulinda haki za binadamu na kwa msingi huo haki za binadamu ni mama wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na kuongeza kuwa kama kuna kifungu kinavunja haki za binadamu. basi kifungu hicho ni wazi kinakiuka haki za binadamu.

“Kwa uamuzi ule wa Mahakama Kuu wa kubatilisha vifungu vya ibara 21(1) (c), 39(1) (c) (b) na 69(1) (b) za Katiba ya nchi, kama kuna ibara zinapingana, ibara inayopaswa kutumika ni ile inayolinda haki za binadamu na kuhusu hukumu ya Mahakama Kuu ilikuwa na mamlaka ya kutamka ibara hizo ni batili kwani Katiba inalinda haki za binadamu na haki hizo za binadamu zilianza, Katiba ikafuata, hivyo haki hizo ni sheria mama.”

Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP), Eliezer Feleshi, anasema yeye na ofisi yake wameshtushwa na taarifa hiyo, kwani Mwaikusa enzi ya uhai wake alifanya kazi kwa uadilifu mkubwa.

“Katika kesi hizo mbili Profesa Mwaikusa alikuwa akiudhuria kama rafiki wa mahakama wakati si wakili, hivyo umuhimu wake haukuwa kwenye taaluma yake ya uwakili bali hata rafiki wa mahakama.

Kifo chake ni changamoto kwa jamii kuwafichua waahalifu na kuviimarisha vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ili viweze kupambana uhalifu.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Fakihi Jundu, anasema Mhimili wa Mahakama nchini, ulimfahamu marehemu kuwa ni mchapa kazi shupavu, aliyetoa hoja zilizosaidia kupata ufumbuzi wa kesi mbalimbali.

Alisema marehemu alikuwa mwanataaluma aliyekuwa akijiandaa vyema kabla ya kuingia kwenye kesi, hivyo baadhi ya hukumu mbalimbali ambazo amepata kuzisimamia kama wakili, zitaendelea kuwa kumbukumbu na kutumika na mahakama kufikia maamuzi ya kesi mbalimbali na wanafunzi wa sheria vyuoni kuzitumia.

Mkuu wa Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Paramaganda Kabudi, anasema kifo hicho ni pigo kwani marehemu alikuwa mtafiti mahiri na msomi makini kwa wanafunzi na walimu wake na alikuwa mwenye vipaji vingi kwani mbali na taaluma yake ya sheria pia alikuwa mshahiri mzuri wa mashahiri aliyoyatunga kwa lugha ya Kiingereza ambayo ameyaweka kwenye kitabu cha ‘Summons Poems of Tanzania’.

Mwadhiri Mwandamizi kutoka kitivo hicho, Dk. Sengondo Mvungi, ambaye pia ndiye aliteuliwa na kitivo hicho kuongoza shughuli ya mazishi, anamwelezea marehemu kama mtaalamu mzuri na mwenye msimamo wa kutetea wananchi.

Wakili wa kujitegemea na mwanaharakati wa haki za binadamu nchini, Alex Mgongolwa, anamwelezea Profesa Mwaikusa kwamba alikuwa miongoni mwa mawakili walioendeleza sheria kwa kiwango cha juu na kutolea mfano kwamba alikuwa Waziri Mkuu mstaafu, Joseph Warioba (CCM) aliyefungua kesi ya kupinga matokeo ya ubunge wa Jimbo la Bunda ambayo yalimtangaza Steven Wassira (NCCR) katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1995 kuwa mshindi.

Wassira ambaye hivi sasa ni Waziri wa Kilimo , Chakula na Ushirika alishinda kesi hiyo na hivyo ushindi wa Wassira ulitenguliwa na Mahakama Kuu mwaka 1996.

“Na hoja ya rushwa kwenye uchaguzi ambayo ilitolewa kwenye kesi hiyo na Profesa Mwaikusa kwamba mgombea akitoa vitu vidogo vidogo kwa wapiga kula ni rushwa na hoja yake hiyo ilisababisha Bunge kutunga sheria ya Takrima ya mwaka 1998, kwakweli nimepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa ya kifo cha marehemu ambaye alikuwa mwalimu wangu na ninaomba polisi wafanye uchunguzi wa kina ili hatimaye washitakiwa wafikishwe mahakamani,” alisema Wakili Mgongolwa.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Ushindani nchini, Edson Mkasimongwa, anasema marehemu alikuwa mwalimu wake katika kipindi cha 1997-2000.

Anasema marehemu alikuwa muungwana, asiye na vishindo na aliyekuwa tayari kusaidia kitaaluma na kumshauri mtu yeyote alipomjia kumuomba msaada, alifanya kila aliloweza na kuonyesha uwezo wake katika kufundisha wanafunzi na kwa sababu hiyo, wanafunzi wa sheria wamepoteza mwalimu mzuri.

Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi (ACP), Charles Kenyela, anasema Jeshi la Polisi na yeye binafsi wamepokea kwa masikitiko makubwa ya kifo hicho na kuahidi kuwasaka kwa udi na uvumba wauaji hao.

Kenyela ambaye ni mwanasheria kitaaluma anasema binafsi anahuzunishwa na msiba huo kwani marehemu alikuwa ni mwalimu wake wa sheria.

Meja Jenerali mstaafu wa Jeshi la Wananchi (JWTZ), Alfred Mbowe, anasema anamlilia Profesa Mwaikusa kwa sababu marehemu alikuwa mwadilifu na siku zote alikuwa mwana taaluma anayesimamia haki na usawa na kuongeza kuwa kifo chake kimemshtua na kuomba vyombo vya dola vifanye upelelezi wa kina ili kuwabaini waliohusika na unyama huo.

Sisi tulimpenda sana Profesa Mwaikusa lakini Bwana amempenda zaidi. Bwana ametoa na bwana ametwaa, jina lake lihimidiwe. Amina.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Julai 18 mwaka 2010