MATUKIO MAKUBWA KUTOKA MAHAKAMANI MWAKA 2010

Na Happiness Katabazi

LEO ndio Ijumaa ya mwisho ya mwaka 2010. Kesho panapo majaliwa tunaukaribisha mwaka mpya wa 2011.

Ungana nami mwandishi wa habari za mahakamani ili uweze kupata mtiririko wa matukio makubwa yaliyotokea mahakamani kuanzia Januari hadi Desemba mwaka huu.

Desemba 29
Chenge atiwa hatiani

ALIYEKUWA Waziri wa Miundombinu na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Andrew Chenge alihukumiwa kwenda jela miaka mitatu au kulipa faini ya sh 700,000 baada ya kutiwa hatiani na Mahakama ya Wilaya ya Ilala kwa makosa matatu ya kuendesha gari kwa uzembe, kusababisha vifo vya watu wawili na kuendesha gari lililokuwa na bima iliyokwisha muda wake. Chenge alifanikiwa kukwepa kwenda jela baada ya kulipa faini na sasa yupo huru.

Desemba 28
Jaji Mkuu Agustino Ramadhani astaafu
JAJI Mkuu Agustino Ramadhani alistaafu rasmi kazi hiyo kwa mujibu wa sheria baada ya kushika wadhifa huo kwa miaka mitatu na nusu.Na siku hiyo ndiyo alikuwa akitimiza umri wa miaka 65.

Desemba 27
Jaji Mkuu Chande aapishwa
JAJI Mkuu mteule,Mohamed Othman Chande aliapishwa rasmi katika viwanja vya Ikulu na Rais Jakaya Kikwete kushika wadhifa huo.

Desemba 26
Kikwete amteua Chande kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania
RAIS Jakaya Kikwete alimteua Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mohamed Othman Chande kuwa Jaji Mkuu mpya wa Tanzania.

Desemba 21
Mahakama yalidhia hukumu ya Liyumba

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam ilisema hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Mei 24 mwaka huu, dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu (BoT), Amatus Liyumba ya kwenda jela miaka miwili ni sahihi na imekidhi matakwa ya sheria.

Hukumu hiyo ilitolewa na Jaji wa Mahakama Kuu, Emilian Mushi, wakati akitoa hukumu ya rufaa namba 56 ya mwaka 2010 iliyokatwa na mrufani Liyumba dhidi ya Jamhuri.

Desemba 16
Jaji Mkuu Mstaafu akataliwa
kesi ya Samaki wa Magufuli

UPANDE wa Jamhuri katika rufaa iliyokatwa na raia 36 wanaokabiliwa na kesi ya uvuvi haramu katika Mahakama ya Rufani nchini kwa kutumia meli ya meli ya Tawaliq 1 inayowakanili raia 36 wa kigeni ilimwomba aliyekuwa Jaji Mkuu Augustino Ramadhani kujitoea kwenye kesi hiyo kwasababu aliwahi kuizungumzia kesi hiyo nje ya mahakama kwa kutumia magazeti.

Desemba 6
Mahakama Tanzania yazindua tovuti yake
MAKAMU wa Rais, Dk.Mohamed Gharib Bilal alizindua uanzishwaji wa mfumo wa kurekodi mashauri kwa kompyuta na tovuti ya mahakama www.judiciary.go.tz., na kusema kuwa utaboresha mazingira na hadhi ya mahakama nchini.

Oktoba 4
Mahalu aibwaga serikali
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam,ilitamka kuwa kifungu cha 36(4)(e) sua ya 200 ya Sheria ya Uhujumu Uchumi ya mwaka 2002, ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Kesi hiyo ya Kikatiba ilifunguliwa mahakamani hapo na aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali .

Hukumu hiyo ilitolewa na jopo la majaji watatu waliokuwa wakiongozwa na Jaji Kiongozi, Fakhi Jundu, Agustine Mwarija na Prejest Rugazia ambapo kwa kauli moja walisema wanakubaliana na hoja za mawakili wa mlalamikaji (Mahalu),dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali akitetewa na mawakili wa kujitegema, Alex Mgongolwa kwamba kifungu hicho kinakwenda kinyume na Katiba ya nchi na kinaleta ubaguzi.

Julai 2
Kesi kubwa ya ufisadi yafutwa

HATIMAYE Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, ilimwaachia huru Ofisa Ugavi kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Elias Mziray, na maofisa wenzake wanne waliokuwa wakikabiliwa na makosa matatu ya kula njama ya wizi wa sh milioni 119.
Mahakama hiyo, ilifikia uwamuzi huo baada ya kuwaona washtakiwa wote kwa pamoja hawana kesi ya kujibu.

Mbali na Mziray, washtakiwa wengine ni Ofisa Manunuzi, David Kakoti, Gene Moshi na Mhasibu Joseph Rweyemamu ambao wote ni watumishi wa wizara hiyo, Uamuzi huo ulitolewa na Hakimu Mkazi Stewart Sanga

Julai 9
Waziri Maua aamuliwa kulipa sh mil. 100
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, ilimwamuru Naibu Waziri wa Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Mawasiliano, Dk. Maua Daftari, kumlipa mfanyabiashara Fatma Salim, sh milioni 100.7 baada ya kubaini alivunja mkataba na mdaiwa huyo.

Hukumu hiyo, ilikuwa ni mara ya pili ikiwa chini ya Jaji Fedrica Mgaya, ambapo mwaka juzi hukumu hiyo, ilisomwa na jaji Laurian Kalegeya ambaye kwa sasa ni Jaji wa Mahakama ya Rufaa ya Tanzania.

Juni 11
Korti Kuu yatengua masharti ya dhamana

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, ilitengua masharti ya dhamana yaliyotolewa na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Agnes Mchome, kwa aliyekuwa Mkurugenzi wa Benki Kuu(BoT), Simon Jengo na wenzake wawili ambao wanakabiliwa na kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma baada ya kubaini hakimu huyo hakufuata sheria husika kutoa masharti hayo ya dhamana. Uamuzi huo ulitolewa na Jaji Emilian Mushi.

Juni 21
Mafisadi wa Lukuvi mahakamani
OFISA Ardhi wa Manispaa ya Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, Magesa Magesa (33), alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na shtaka moja la kughushi dondoo ya barua ya kumilikishwa ardhi inayoonyesha imetolewa na Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Noel Mkomola Mahyenga.

Juni 23
Rufaa ya Kasusura yagonga mwamba

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, ilitupilia mbali rufaa iliyokatwa na aliyekuwa dereva wa Kampuni ya ulinzi ya Knight Support, Justine Kasusura, kwa maelezo kwamba sababu sita alizozitumia kukata rufaa zimeshindwa kuthibitisha na kwamba hukumu ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu iliyomtia hatiani kwa makosa ya unyang’anyi wa kutumia silaha na wizi dola milioni mbili za Marekani mali ya Citibank ilikuwa na dosari za kisheria. Hukumu ya Rufaa hiyo ilitolewa jana na Jaji mstaafu Thomas Mihayo.

Juni 8
Utumbo wa samaki wa Magufuli uteketezwe- Mahakama

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, iliamuru utambuzi wa utumbo wa samaki waliokamatwa wakivuliwa na wavuvi haramu 36 ambao ni raia wa kigeni katika meli ya Tawaliq katika eneo la Bahari ya Hindi, uharibiwe kutokana na kutoa harufu mbaya.

Juni 17
Majaji Saba wamgwaya mgombea binafsi

MAHAKAMA ya Rufaa Tanzania, ilitengua hukumu ya kuruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi katika uchaguzi, iliyotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na kusema suala hilo litaamuliwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akisoma hukumu hiyo kwa zaidi ya saa moja, Jaji Ramadhani alisema suala la mgombea binafsi limekaa kisiasa sana, sio kisheria kama ilivyoaminika.

Mei 28
Liyumba akata rufaa korti kuu

ALIYEKUWA Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba(62) aliyehukumiwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwenda jela miaka miwili alikata rufaa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam akipinga hukumu hiyo.

Mei 24
Liyumba afungwa miaka miwili jela

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, ilimuhukumu kwenda jela miaka miwili, aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba baada ya kumtia hatiani kwa kosa la matumizi mabaya ya ofisi za umma.

Mei 13
Liyumba hana hatia -Wakili
MAWAKILI wa upande wa utetezi katika kesi ya matumuzi mabaya ya ofisi ya umma inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatusi Liyumba waliiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imuone mteja wao hana hatia kwasababu hakuwa na mamlaka ya kuamua jambo lolote ile katika mradi wa ujenzi wa mradi wa majengo pacha.

Mei 8
Mkurugenzi BoT afutiwa kesi
MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam,ilimuachia huru aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Sheria katika Benki Kuu(BoT), Bosco Kimela aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi na kuisababishia serikali hasara ya Sh bilioni 104 ambaye amesota rumande kwa miezi nane sasa kwaajili ya kesi hiyo.

Mei 7
Vigogo BoT waachiwa, wakamatwa

MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam, iliwafutia mashtaka ya uhujumu uchumi yaliyokuwa yakiwakabili wakurugenzi wanne wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), lakini wakurugenzi hao walijikuta wakikamatwa tena baada ya kutuhumiwa mashtaka matatu ya matumizi mabaya ya ofisi za umma.

Washtakiwa hao ni Mkurungezi wa BoT, Simon Jengo, Naibu Mkurugenzi wa Fedha za Nje, Kisima Mkango, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Kitengo cha Sheria, Bosco Kimela na Mkurugenzi wa Huduma za Benki, Ally Bakari.

Mei 10
Waziri Daftari ashinda kesi
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, ilimfutia kesi ya madai ya kashfa iliyokuwa ikimkabili Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia,Dk.Maua Daftari kwasababu hati ya madai ina dosari za kisheria.

Juni 17
Majaji Saba wamgwaya mgombea binafsi


HATIMAYE Mahakama ya Rufaa Tanzania, ilitengua hukumu ya kuruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi katika uchaguzi, iliyotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na kusema suala hilo litaamuliwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aprili 23
Liyumba atumia hoja za Yesu kujitetea

ALIYEKUWA Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba (62), aliyekuwa akikabiliwa na shtaka moja la matumuzi mabaya ya ofisi ya umma, alidai serikali haijui itendalo dhidi ya kesi iyomfungulia.

Liyumba aliiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, izingatie ukweli wakati wa kutoa hukumu dhidi yake Mei 24 badala ya kuwasikiliza watu wasiojua watendalo.Maneno hayo mawili ‘hawajui watendalo’ yanafanana na yale aliyotumia Yesu Kristo, anayeaminika kuwa ni Mwokozi wa waumini wa Kikristo wakati akieleza kitendo cha Wayahudi waliokuwa wakimsulubisha (Luka 23:34).

Aprili 5
Maranda aanza kujitetea kesi ya EPA

MWEKA Hazina wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kigoma, Rajabu Maranda, aliieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kuwa alichokizingatia katika mchakato wa kudai deni lake la Sh bilioni 1.8 katika Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu ya Tanzania ni kupata fedha na si kutazama nyaraka.

Aprili 13
Wazee EAC waiteka Mahakama Kuu Dar

WAZEE wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) walizusha tafrani katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, muda mfupi baada ya Jaji Njengafibili Mwaikugile kutoa maelekezo ya kuwataka waende wakatafakari upya na kumletea taarifa sahihi zitakazomwezesha kufikia uamuzi wa kutoa haki katika shauri lao.

Aprili 9
Liyumba apangua shtaka kuu

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, ilimfutia shitaka moja kati ya mashitaka mawili yaliyokuwa yakimkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba, kwa maelezo kuwa upande wa mashitaka umeshindwa kupeleka ushahidi wa kuthibitisha shitaka mojawapo.

Uamuzi huo ulitolewa na kiongozi wa Jopo la Mahakimu Wakazi, Edson Mkasimongwa, aliyekuwa akisaidiana na Lameck Mlacha na Benedict Mwingwa.

April 9
Mgombea binafsi bado alitesa taifa

MAHADHIRI wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Palamagamba Kabudi na Profesa Jwani Mwaikusa, wakishirikiana na Mkurugenzi wa Mashitaka wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (DDP), Othman Masoud.Walikuwa wanaishauri Mahakama ya Rufaa kabla haijatoa hukumu ya rufaa iliyofunguliwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali mwaka jana kupinga hukumu ya Mahakama Kuu iliyoruhusu mgombea binafsi, katika kesi ya msingi iliyofunguliwa na Mchungaji Christopher Mtikila.

Aprili 9
Babu Seya, mwanaye waomba
hukumu yao ipitiwe upya

MWANAMUZIKI mahiri wa muziki wa dansi nchini Nguza Vikings “Babu Seya na mwanaye Johnson Nguza ‘Papii Kocha” walirusha karata yao ya mwisho katika Mahakama ya Rufaa Tanzania wakiomba mahakama hiyo ipitie upya hukumu iliyotolewa mahakama hiyo ambayo ilisisitiza kwamba warufani hao waendelee kutumikia kifungo cha maisha jela na kuwaachilia huru watoto wake wawili baada ya kuwaona hawana hatia.

Aprili 8
Majaji waitoa serikali jasho Kortini Dar

RUFAA ya kesi ya Mgombea binafsi ilianza kusikilizwa rasmi na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju, aliyedai kuwa hakuna mahakama yoyote nchini ambayo inaweza kusikiliza kesi ya kutaka kuwepo kwa mgombea binafsi.Masaju alitoa madai hayo wakati akiwasilisha hoja zake za kupinga hukumu ya Mahakama Kuu.

Machi 30
Mkurugenzi wa Easy Finance Kortini

MMOJA wa Wakurugenzi wa Kampuni ya kutoa mikopo nchini ya Easy Finance, Aloycious Gonzaga (43) na mkewe, Magreth Gonzaga (38), walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka manne ya kula njama na kuwasilisha hati ya kiwanja ya kughushi na kisha kujipatia isivyo halali sh milioni 50.

Machi 29
Serikali yamng’ang’ania Liyumba

UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya matumizi mabaya ya Ofisi ya Umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba uliiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imuone mshitakiwa ana kesi ya kujibu.

Machi 22
Mawakili wataka Liyumba aachiwe

UPANDE wa utetezi katika kesi ya matumizi mabaya ya Ofisi ya Umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumushi na Utawala wa BoT ,Amatus Liyumba, uliiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imuone mshitakiwa hana kesi ya kujibu na imuachirie huru kwasababu upande wa mashitaka umeshindwa kuthibitisha kesi yao(prima facie case).

Februali 11
Babu Seya,Papii wakwama tena

MWANAMUZIKI mahiri wa muziki wa dansi nchini, Nguza Viking (Babu Seya) na mwanaye Papii Kocha walishindwa kujinasua kwenye hukumu ya kifungo cha maisha jela.

Mahakama ya Rufaa Tanzania jana ilikazia hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, lakini iliwaachia huru watoto wawili wa Babu Seya ambao ni Nguza Mbangu (Mashine) na Francis Nguza (Chichi).

Januari 15
Mahakama Kuu yatengua uamuzi wa kesi ya Jeetu Patel
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam ilitengua uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wa kusimamisha usikilizaji wa kesi ya wizi wa sh bilioni 7.9 katika Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu, inayomkabili Mfanyabiashara maarufu Jayantkumar Chandubhai Patel maarufu ‘Jeetu Patel na wenzake wawili.

Januari 14
Washtakiwa wizi NBC Ubungo huru

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam imewaachiria huru Ramadhani Dodo na wenzake nane waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya wizi wa sh milioni 168 kwa kutumia silaha mali ya Benki ya Taifa ya Biashara(NBC)Tawi la Ubungo maarufu kama ‘kesi ya mtandao’baada ya kuwaona hawana hati.

Januari 11
Mtikila atupwa rumande

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, ilimtupa rumande Mwenyekiti wa Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila baada ya kumfutia dhamana kwa kukiuka masharti. Amri ya kumfutia dhamana na kutupwa rumande ilitolewa baata ya Hakimu Mkazi, Waliarwande Lema, kusikiliza utetezi wa Mtikila aliyechelewa kuhudhuria kesi ya uchochezi iliyomkabili.

Nawatakieni wasomaji wote wa gazeti hili na wale wadau wote wa mhimili wa mahakama ya Tanzania, maandalizi mema ya kuukaribisha mwaka mpya wa 2011.

0716- 774494
www.katabazihappy.blogspot.com

CHENGE ATIWA HATIANI

*HUKUMU YAKE YAIBUA MASWALI

Na Happiness Katabazi

MBUNGE wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge, jana alihukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela au kutozwa faini ya jumla ya sh 700,000 huku hukumu hiyo iliyotokana na makosa matatu yaliyokuwa yakimkabili ikizua maswali kwa watu wa kada mbalimbali wakiwemo wanasheria na baadhi ya watu wengine waliowahi kushtakiwa kwa makosa kama hayo.

Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni ilimtia hatiani Chenge kwa makosa matatu yaliyokuwa yakimkabili yakiwemo ya kuendesha gari kizembe na kusababisha vifo vya watu wawili: Victoria John na Beatrice Costatino.


Chenge alisababisha vifo hivyo baada ya gari alilokuwa akiliendesha kuigonga pikipiki ya miguu mitatu (Bajaj) ambayo marehemu walikuwa wamepanda.


Shtaka la tatu ni la kuendesha gari wakati bima ya gari hiyo ikiwa imekwisha muda wake. Hata hivyo, mshtakiwa huyo alikana mashtaka yote.


Hukumu hiyo ambayo ilikuwa ikisubiriwa kwa shauku na wananchi wengi, ilisomwa jana saa nne asubuhi na Hakimu Mfawidhi Kwey Lusema ambaye alisema amefikia uamuzi wa kumtia hatiani mshtakiwa huyo kwa sababu upande wa Jamhuri uliweza kuthibitisha kesi yake bila kuacha mashaka yoyote.


Upande wa Jamhuri ulikuwa ukiwakilishwa na wakili wa kujitegemea Richard Rweyongeza ambaye aliteuliwa na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kuendesha kesi hiyo akisaidiwa na wakili David Mwafwimbo.


Hakimu Lusema alisema endapo mshtakiwa huyo ataamua kutumikia adhabu ya kulipa faini, basi atapaswa kulipa faini hiyo kama ifuatavyo: 'Katika shtaka la kwanza na pili atalazimika kulipa jumla ya faini ya sh 500,000 na katika shtaka la tatu ambalo ni la kuendesha gari wakati bima yake imemalizika muda wake atalipa faini ya sh 100,000 pamoja na sh 100,000 kama faini ya uharibifu wa mali, hivyo kufanya jumla ya fidia anayotakiwa kuilipa kuwa ni sh 700,000.'
Chenge alinusurika kwenda jela baada ya kulipa sh 700,000 iliyotakiwa kama fidia kwa kuonekana na hatia kwa makosa yote hayo matatu; kiasi ambacho ni visenti tu kwake.


Kwa malipo hayo ya fidia, Hakimu Lusema alisema mshtakiwa huyo kuanzia jana yuko huru na anaweza kuendelea na shughuli zake kama kawaida.


Hata hivyo, Deus Mallya mmoja wa watu waliowahi kushtakiwa kwa makosa yanayofanana na ya Chenge, alielezea kushangazwa kwake na hukumu hiyo huku akidai kuwa mbunge huyo amependelewa kupewa fursa ya kulipa fidia.


Deus Mallya aliwahi kuhukumiwa kuendesha gari kwa uzembe na bila leseni na kusababisha kifo cha aliyekuwa mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe na kudai kwamba alihukumiwa moja kwa moja kwenda jela miaka mitatu bila kupewa fursa ya kutoa faini kama alivyopewa Chenge.


'Nchi hii ina sheria za matabaka! Wengine hawastahili kugusa mlango wa gereza na wengine ni wa kufungwa hata kwa maneno ya wanasiasa. Makosa yetu yanafanana, tena mwenzangu amekutwa na makosa matatu zaidi, mimi nilishtakiwa kwa makosa mawili lakini lilithibitika moja tu, la kuendesha gari kizembe na kusababisha kifo, kosa ambalo limo katika orodha ya makosa matatu ya Chenge. Inatia aibu, hukumu ya Chenge ni hukumu ya kishikaji,' alisema Mallya.


Aidha, baadhi ya wananchi waliozungumza na gazeti hili kwa sharti la kutotajwa majina yao walihoji uhalali wa mtu kutozwa faini wakati alisababisha kifo.


Mapema mwaka jana Chenge alifikishwa mahakamani hapo akikabiliwa na mashtaka hayo lakini wakati kesi ikiendelea mshtakiwa alikuwa nje kwa sababu aliweza kutimiza masharti ya dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Desemba 30 mwaka 2010

AUGUSTINE RAMADHANI:KESI YA MGOMBEA BINAFSI SITAISAHAU


Na Happiness Katabazi


“KESHOKUTWA, nitakuwa nikikumbuka siku yangu ya kuzaliwa na nitakuwa ninatimiza umri wa miaka 65, siku hiyo pia itakuwa ya kihistoria kwangu kwani ndiyo nitakuwa nastaafu kazi ya utumishi wa umma kwa mujibu wa sheria na Katiba ya Nchi.”


Hii ni nukuu ya maneno ya Jaji Mkuu, Agustino Ramadhan, alipoanza kuzungumza na jahazi Jumapili kuhusu maisha yake na kazi


Anasema kuwa katika kipindi chote cha utawala wake amefanya kazi kwa ushirikino mkubwa na watendaji wa serikali pamoja na wale wa mahakama.


Anabinisha kuwa anajivunia kuwa katika uongozi wake aliheshimu sheria na Katiba na hata watendaji wenzake kwa kiasi kikubwa walijitahidi kufuata mambo hayo Yafuatayo ni mahojiano ya Jaji Ramadhani na Jahazi Jumapili.
Swali:
Ulijisikiaje wakati ukiteuliwa kuwa jaji mkuu mwaka 2007 na changamoto zipi ulizozikuta?
Jibu:
Nilifarijika kuteuliwa kushika wadhifa huo wa kuongoza mhimili wa mahakama kwa sababu ni nadra kupata nafasi kuu kama hii.


Changamoto kubwa niliyoikuta ni uhaba wa watendaji, ambapo majaji wa Mahakama Kuu na Rufaa kwa wakati huo walikuwa 11 na hivi sasa tuko 16.


Katika Mahakama Kuu, Rais Kikwete, aliteua majaji 30 kuanzia mwaka 2008 hadi sasa ambapo ni wastani wa majaji 10 kila mwaka.


Mahakimu wa mahakama za mwanzo wapatao 100 wameajiriwa kuongoza mahakama hizo jambo ambalo kwa kiasi fulani limeharakisha usikilizaji wa kesi.


Hivi sasa Mahakama Kuu ina Kanda 13 na kanda hizo zina majaji wawili wawili isipokuwa Kanda ya Tabora, Mwanza majaji wanne, Arusha watatu.


Changamoto nyingine ni uhaba wa vitendea kazi na teknolojia za kizamani za kurekodi mashauri lakini nashukuru Desemba 6 mwaka huu, tulizindua mfumo wa kidigitali wa kurekodia mwenendo wa kesi pamoja na tovuti ya mahakama.


Teknolojia hiyo ya kidijitali imeishafungwa inatumika kwenye Mahakama ya Rufaa, Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na vitengo vyake vya Kazi, Ardhi na Biashara.
Swali: Ushirikiano wa mahakama na mhimili mingine ulikuwaje Jibu: Kimsingi wakati nikiingia mambo yalikuwa si mazuri, watendaji wa mahakama tulikuwa tukilalamikiwa na wabunge, wakuu wa mikoa na viongozi wengine wa serikali.


Jibu: Tatizo hilo nililitatua kwa kushirikiana na viongozi wa Serikali na Rais Jakaya Kikwete pamoja na aliyekuwa Spika wa Bunge, Samuel Sitta kwenye shehere zetu mbalimbali.
Nami pia nilikuwa nikihudhuria sherehe za kiserikali pamoja na vikao vya Bunge hasa vile vya bajeti.


Kupitia ushirikiano huo mpya tuliweza kuhabarishana changamoto zinazotukabili na namna ya kuzitatua kulingana na uwezo tuliokuwa nao.


Swali: Kwa nini mahakama huchelewesha usikilizaji wa kesi?


Jibu: Kuna aina mbili za ucheweshwaji wa kesi, mosi mahakama pili ni Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), ofisi ya Mwanasheria, polisi na mawakili wa kujitegemea.
Wakati mwingine hakimu au jaji anakuwa yuko tayari kusikiliza kesi lakini upande wa mashtaka unadai haujakamilisha upelelezi au unashindwa kuleta mashahidi kwa wakati.
Sababu nyingine ni baadhi ya mawakili wa kujitegemea wanakuwa hawajajiandaa kuendesha kesi husika sasa kwa sababu hizo ndiyo maana kesi zinashindwa kumalizika mapema.
Wananchi wengi hawatambui mchakato wa uendeshaji wa kesi ndiyo maana mwisho wa siku huishia kuitupia lawama mahakama kuwa inachelewesha kesi.


Lakini pia mhimili wa mahakama umeweza kusimamia sheria na Katiba. Pia mfumo wenyewe na baadhi ya sheria kwani tumeweza kubadilisha kanuni za uendeshaji wa kesi za Mahakama ya Rufani.


Kanuni za awali zilizotungwa mwaka 1979 zikafutwa na kanuni hizo mpya zilizopitishwa mwaka 2009 zimeanza kutumika Februari mwaka huu.
Swali: Wazee wa baraza wa mahakama wamekuwa wakilalamika kutolipwa posho kwa nini hali hiyo inajitokeza?


Jibu: Ni kweli kulikuwa na malalamiko hayo na wazee wa baraza walikuwa wanapata posho ya sh 1,500. Ila kuanzia Julai mwaka huu posho yao imeongezeka wanapata posho ya sh 5,000.
Wakati mwingine wazee hao walikuwa wanakopwa na mahakama wanakwenda kusikiliza kesi, hili lilikuwa linasababishwa na ufinyu wa bajeti ya mahakama.


Swali: una maana gani unaposema uongozi wako mahakama ilizingatia sheria na Katiba?


Jibu: Aah! Namaanisha kwamba mahakama imeangalia Katiba kwa mtizamo mpya unaopaswa uwe, ibara za Katiba zinazohusu majaji na ajira zao.
Huko nyuma majaji wa mahakama kuu walikuwa wanastaafu kwa mujibu wa sheria wakiwa na umri wa miaka 60 na wale wa mahakama ya rufaa miaka 65, halafu wanapewa mafao yao na kisha wanaweza kurejeshwa kufanya kazi hiyo kwa mkataba.
Hivi sasa hivi Rais wa nchi anaweza kuongeza umri wa kustaafu wa jaji anayekaribia kustaafu, Mfano Jaji wa Mahakama Kuu ana miaka 59;
Rais anaruhusiwa kumuongezea hata miaka mitatu mbele ya utumishi kabla ya umri wa miaka 60 kustaafu na akishastaafu katika umri huo alioongezewa na rais ndiyo anatapewa mafao yake yote.
Swali: Serikali imefanya jambo gani kwa mahakama mbalo utalikumbuka?
Jibu: Kubwa zaidi ni kukubali ombi letu la kutaka tuwe na mfuko wa mahakama ambao tunaamini utatusaidia kutatua matatizo yetu yanayokwamishwa na uhaba wa fedha.
Kilio chetu kikubwa kilikuwa ni kuiomba serikali ituwekee angalau asilimia mbili ya bajeti ya seriakli katika mfuko huo, sasa hivi mahakama inapewa asilimia 0.4 ya bajeti ya serikali.
Kiwango hiki ni kidogo sana kwani hata mikoa ya Lindi na Mtwara bajeti yake ni kubwa kuliko bajeti ya mahakama ambayo ina ofisi katika kata, wilaya na mkoa.


Pia naishukuru serikali kwa kutujengea mahakama za mwanzo mbili za kisasa zilizopo Kerege na Lugoba mkoani Pwani ambazo zimezinduliwa mapema wiki hii na ujenzi wake umegharimu zaidi ya sh milioni 600.
Swali: Kipi unajivunia katika utawala wako?


Jibu: Ni kuanzisha mchakato wa mahakama kupata mfuko wake na ninaamini hadi kufikia Julai mwakani mwakani mfuko huo utapatikana.

Jibu: Ikumbukwe kwamba licha ya kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania, mimi ni Jaji wa Mahakama ya Haki za Binadamu na za watu ya Afrika yenye makao makuu yake jijini Arusha.
Katika mahakama hiyo tuko majaji 11. Ila majaji wa mahakama hiyo hatufanyi kazi muda wote, tunakutana mara nne kwa mwaka na kwa siku 10.
Kwa hiyo nafasi hiyo ya ujaji wa mahakama hiyo ya Afrika nayo itaniwezesha kuniingizia kipato. Pia nitakuwa nikilipwa pesheni za kustaafu na serikali yetu.
Nakusudia kuwa mhadhiri wa sheria (Visiting Lecturer), katika baadhi ya vyuo vikuu na ninakusudia kuandika vitabu.


Swali: Ni kesi gani ulishiriki kuisikiliza na kuitolea maamuzi ambayo hutoisahau?
Jibu: Ni kesi ya Kikatiba ambayo mwanasheria mkuu wa serikali alikata rufaa katika Mahakama ya Rufaa, dhidi ya Mchungaji Christopher Mtikila, kwamba mahakama inaweza kutamka kwamba ibara ya Katiba inaweza kuvunja ibara nyingine ya Katiba?


Nitaikumbuka kesi hiyo kwa sababu ni mara ya kwanza kwa mahakama ya rufani nchini kuketi majaji saba kusikiliza rufaa moja , pia ni mara ya kwanza kwa mahakama ya rufaa kuwaita marafiki wa mahakama-Mkuu wa Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Paramaganda Kabudi.


Alikuwapo pia aliyekuwa mhadhiri mwandamizi wa sheria wa UDSM, marehemu Profesa Jwani Mwaikusa na Mkurugenzi wa Mashtaka wa Zanzibar (DPP), Masoud Othman Masoud.
Sababu hasa inayonifanya niikumbuke kesi hiyo ambayo mimi nilikuwa kiongozi wa jopo hilo la majaji ni muda niliotumia kufanya utafiti na hatimaye tukafikia uamuzi wa kutoa hukumu; kesi ile ambayo wananchi wengi hupenda kuita kesi ya mgombea binafsi.
Ila mimi siiti kesi ya mgombea binafsi bali naiita kesi ya Kikatiba.


Swali: Wosia gani unautoa kwa majaji na mahakimu?


Jibu: Ninawaasa waendelee kuzingatia sheria na Katiba ya nchi katika utendaji wao wa kila siku kwani wakumbuke wao ndiyo kimbilio la wananchi wenye kudhulumiwa au kuminywa haki zao.
Ni vema wakaendelea kuilinda heshima ya mahakama kwa kutoa haki bila upendeleo wowote.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Desemba 26 mwaka 2010

LIYUMBA AGONGA MWAMBA

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam imesema hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Mei 24 mwaka huu dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu (BoT), Amatus Liyumba, ya kwenda jela miaka miwili ni sahihi na imekidhi matakwa ya sheria.

Hayo yalisemwa jana na Jaji wa Mahakama Kuu, Emilian Mushi, wakati akitoa hukumu ya rufaa namba 56 ya mwaka 2010 iliyokatwa na mrufani Liyumba dhidi ya Jamhuri.
Liyumba alikuwa akiomba mahakama hiyo ya juu kutengua hukumu ya Mahakama ya Kisutu kwa hoja kuwa ilijielekeza vibaya kisheria katika kutoa hukumu yake.

Jaji Mushi alisema upande wa mrufani ambao ulikuwa ukiwakilishwa na mawakili wa kujitegemea, Jaji Mstaafu Hillary Mkate, Majura Magafu, Onesmo Kyauke na Hudson Ndusyepo, kupitia hoja zao 12 za kupinga hukumu ya Mahakama Kisutu, umeshindwa kuishawishi mahakama kuu ifikie uamuzi wa kutengua hukumu ya mahakama ya chini.

“Baada ya kupitia kwa kina hoja 12 zilizowasilishwa mahakamani na hoja za upande wa Jamhuri mahakama hii inakubaliana na hoja za Jamhuri kwamba iliweza kuthibitisha kesi yao hivyo inatupilia mbali rufaa hii iliyokatwa na mwomba rufaa (Liyumba),” alisema Jaji Mushi.

Jaji Mushi alisema kutokana na uhalisia wa kesi hiyo mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilikuwa sahihi kufikia uamuzi wa kuona jamii isingeridhika endapo ingempatia adhabu ya kulipa faini tu bila kwenda jela kutumikia kifungo.

“Nimejiridhisha kwamba hukumu iliyotolewa na Mahakama ya chini dhidi ya Liyumba ilikidhi matakwa ya kisheria na wala haikupitiliza matakwa ya kisheria katika mazingira ya kesi …na nimeshindwa kubaini misingi ya kisheria niweze kutengua hukumu ya mahakama ya chini na kwa sababu hiyo zile saa 12 za kupinga hukumu hii zilizotolewa na Liyumba mahakama hii inazitupilia mbali na kama hajaridhishwa na hukumu hii anaruhusiwa kukata rufaa.

“Mshtakiwa anayetiwa hatiani kwa kosa la matumizi mabaya ya ofisi ya umma kwa mujibu wa kifungu cha 35 cha Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 atafungwa jela miaka miwili au kulipa faini au kutumikia adhabu zote mbili kwa pamoja…lakini kwa uhalisia wa kesi hii nakubaliana na mahakama ya Kisutu kwamba mshtakiwa alistahili kwenda jela kwa sababu jamii na taifa liko kwenye mapambano dhidi ya rushwa,” alisema Jaji Mushi.

Liyumba kupitia kwa mawakili wake alikuwa amepinga hoja ya mahakama ya Kisutu ambayo ilisema wameamua kumfunga jela kwa sababu nchi iko kwenye mapambano ya rushwa na kwamba kiwango cha rushwa kiko juu.

Akitoa ufafanuzi wake juu ya hilo, Jaji Mushi alisema anaamini mahakimu wa mahakama hiyo ya chini peni zao ziliteleza kuandika hilo na kusisitiza kwamba hawakuwa wakimaanisha hivyo.
“Ukweli ni kwamba mshtakiwa alikuwa akikabiliwa na shtaka moja la matumizi mabaya ya ofisi ya umma kinyume na kifungu cha 96(1) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 na siyo shtaka la rushwa,” alisema Jaji Mushi.

Aidha, alisema anakubaliana na hukumu hiyo kwamba hakukuwa na uharaka wa Liyumba na aliyekuwa Gavana wa BoT, marehemu Daudi Balali kufanya mabadiliko ya ongezeko la mradi wa ujenzi wa majengo ya Minara Pacha kabla ya kupata idhini ya Bodi ya Wakurugenzi kwani kufanya hivyo ni kinyume cha sheria ya BoT inayoruhusu uwepo kwa bodi hiyo.

Kisha aliongeza, “Kitendo cha Balali na Liyumba kuruhusu mabadiliko ya ujenzi halafu baada ya mabadiliko kutekelezwa ndiyo wanaleta taarifa kwa bodi ili iwape idhini ni udhalilisha kwa bodi hiyo.”

Liyumba ambaye hadi sasa ameshatumikia robo ya kifungo chake, alikata rufaa Mahakama Kuu mwezi Juni mwaka huu akipinga hukumu ya Mahakama ya Kisutu akitaka mahakama hiyo ya juu imwachilie huru.

Mei 24 mwaka huu, jopo la mahakimu wakazi watatu lililokuwa likiongozwa na Edson Mkasimongwa aliyekuwa akisaidiwa na Benedict Mwingwa na Lameck Mlacha lilitofautiana katika kutoa hukumu hiyo.

Mkasimongwa aliandika hukumu peke yake ambayo ilifikia uamuzi wa kumwachilia huru mshtakiwa kwa hoja kuwa upande wa Jamhuri ulishindwa kuthibitisha kesi yake.

Hukumu hiyo ilibaki kwenye rekodi za mahakama, huku hukumu iliyoandikwa na mahakimu wawili Mwingwa na Mlacha ikibaki kuwa ndiyo hukumu rasmi ya Mahakama ya Kisutu. Hukumu hiyo ndiyo iliyomtia hatiani Liyumba kabla ya kukata rufaa hiyo iliyogonga mwamba.

April 9 mwaka huu jopo la mahakimu hao wakazi lilimfutia shtaka moja la kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 lakini lilimuona ana kesi ya kujibu katika shtaka moja la matumizi mabaya ya ofisi ya umma.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Desemba 22 mwaka 2010

SIKU NILIPOHITIMU KOZI YA USALAMA NA UTAMBUZI...


Mwandishi wa Habari za Mahakamani wa Gazeti la Tanzania Daima, Happiness Katabazi akipokea cheti kutoka kwa Ofisa wa The Protection Desk of Uganda, Yona Wanjala baada ya kuhitimu mafunzo ya Usalama na Utambuzi wa Mazingira hatarishi kwa watetezi wa haki za binadamu yalifofanyika katika Hoteli ya East African All Suit, mkoani Arusha, mwishoni mwa wiki.Mafunzo hayo yaliandaliwa na kufadhiliwa na The Protection Desk Of Uganda. (Picha na Mpiga Picha).

KUMBUKUMBU YETU


Nikiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wenzangu wa mazufuzo hayo , ikiwa ni muda mfupi baada ya kukabidhiwa vyetu vyetu kwa kuhitimu mafunzo hayo.

TOVUTI YA MAHAKAMA KUPUNGUZA KERO

Na Happiness Katabazi

DESEMBA 6 mwaka huu, Mahakama ya Tanzania iliandika historia mpya ya kimaendeleo kwa uzinduzi wa mfumo wa shughuli za mahakama na mradi wa kutoa elimu ya nadharia itumiayo mfumo wa kompyuta kurekodi na kutengeneza tovuti ya mahakama za Tanzanzia.


Makamamu wa Rais wa Seriakali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk.Mohamed Gharib Bilal ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo,kupitia hotuba yake yake alisema kuwa uanzishwaji wa mfumo wa kurekodi mashauri kwa kompyuta na tovuti ya Mahakama, utaboresha mazingira na hadhi ya mhimili wa mahakama nchini.

Katika uzinduzi huo uliohudhuriwa na viongozi wakuu akiwemo Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani, Jaji Mkuu, Agustino Ramadhani, Ofisa Mtendaji Mkuu wa (ICF) Omar Issa, majaji wa mahakama ya rufaa na mahakama kuu, Dk.Bilal aliizindua tovuti ya mahakama itakayotambulika kwa kwa jina la ‘www.judiciary.go.tz’.

“Kabla ya mfumo huu kuuzindua,ile haki iliyoainishwa katika Katiba ya nchi, yaani haki za binadamu zilikuwa hazipatikani kwa wakati kutokana na mahakama zetu kurekodi mwenendo wa kesi na huduma nyingine kwa kutumia mkono…

“Lakini sasa napenda niipongeze mahakama kwani imepiga hatua kwa kuanzisha mfumo huu ambao umefadhiliwa na Shirika la ICF nawapeni hongera sana mahakama kwa sababu hii ni hatua bora zaidi,” alisisitiza Dk. Bilal.

Na kwa upande wake Jaji Mkuu Agustino Ramadhani, alisema hadi sasa Mahakama Kuu na vitengo vyake ambavyo ni Biashara, Ardhi na Kazi, vimewekewa vifaa vya kisasa vya kurekodi na kufanya huduma ya kuandika kwa mikono kuwa historia na kuongeza kuwa Mahakama ya Rufaa nayo imeboresha huduma zake na kuwa ya kisasa huku zaidi.

Kwa uzinduzi huo, Fukuto la Jamii ambalo lilikuwa ni miongoni mwa watu walioudhulia hafla fupi ya uzinduzi huo uliofanyika katika kordo ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, na pia ni mdau mkubwa wa mahakama kwasababu ni mwandishi wa habari za mahakamani nchini, linapongeza hatua hiyo ya kimaendeleo iliyopigwa na mhimili wa mahakama.

Kwani Fukuto la Jamii,linaamini kufungwa kwa teknolojia hiyo katika mahakama ni wazi kutapunguza kwa kiasi kikubwa urasimu wa upatikanaji bahari za wazi za mahakama ikiwemo maamuzi yanayotolewa na majaji mbalimbali.

Na pia itaondoa adha kwa wananchi wenye kesi kwenye mahakama hizo kujua kesi zao zimepangwa kwa jaji nani na tarehe ngapi na siku ya tarehe hiyo kesi yake inakuja kwaajili gani, Je kutajwa,kusikilizwa,kuwasilisha ombi,kutolewa maamuzi au kutolewa hukumu.

Kwani wananchi wengi wenye kesi katika mahakama hizo wengine wanaishi mikoa ya mbali hivyo wamekuwa wakitumia gharama nyingi kufika mahakama kuu,mahakama ya rufaa kwaajili ya kufuatilia kesi zao zimepangwa kwa jaji nani na itatajwa au kuanza kusikilizwa tarehe ngani?

Na Fukuto la Jamii, ambayo siku zote za jumaa ufanya shughuli zake mahakama mara kwa mara imekuwa ikiwashuhudia wananchi hao wakitokea mikoa mbalimbali wakishinda kwenye ofisi za makarani wa kesi za jinai na madai katika mahakama ya rufaa na mahakama kuu Kanda ya Dar es Salaam,wakitaka kujua hatima za kesi zao na wengine wamekuwa wakilalamika kesi zao zimekuwa zikichelewa kupangwa hivyo wamekuwa wakitumia nauli mara kwa mara lakini kupitia tovuti hiyo sasa wananchi wenzetu ambao watakuwa na uwezo wa kutumia teknolojia hiyo wataondokana na msalaba wa kutumia nauli kuja mkoa mmoja hadi mwingi kwaajili ya kujua maendeleo ya kesi zao.

Hakuna ubishi kwamba mahakama nchini imekuwa ikilalamikiwa kuwa imekuwa ikichelewa kutoa maamuzi katika kesi mbalimbali kwasababu imekuwa ikifanyakazi kwa kutumia teknolojia ya zamani ya majaji na mahakimu kurekodi mwenendo wa mashauri kwa kutumia karamu na peni wakati mahakama za wenzetu majaji na mahakimu wao wamekuwa wakitumia teknolojia ya kisasa kurekodi mwenendo wa kesi zinazofunguliwa katika mahakama zao.

Na siyo tu imekuwa ikilalamikiwa tu katika hilo, pia imekuwa ikilalamikiwa na washtakiwa waliohukumiwa na mahakama kuu ambao wanataka kukata rufaa katika mahakama ya rufaa kwa kuchelewesha kuwapatia nakala ya kuhumu warufani hili waweze kutumia nakala hiyo kukataa rufaa katika mahakama ya rufaa, kwa kisingizio kwamba mahakama haina haina fungu la kuchapa haraka nakala za hukumu na kwamba teknolojia waliyokuwa wakiitumia si ya kisasa, hali iliyosababisha wananchi waliohukumuwa kuendelea kusota rumande muda mrefu bila kukata rufaa kwasababu uongozi wa mahakama kuu unawaeleza teknolojia ya kuchapa mwenendo wa hukumu siyo ya kisasa.Hiki kisingizio kuanzia mahakama ulipozindua mfumo huo wa kisasa, kife mara moja.

Na siyo kundi hilo tu limekuwa likilalamika, pia sisi waandishi wa habari za mahakama wakati mwingine tumekuwa tukipata wakati mgumu kupata nakala ya hati ya kesi ya madai hata kama kesi hiyo imefunguliwa asubuhi kwa kigezo kwamba, nakala ipo moja na nakala hiyo inapelekwa kwa Jaji Mfawidhi Kanda ya Dar es Salaam, Semistocles Kaijage ili aiidhinishe kesi hiyo mpya sambamba na kuipangia jaji wa kuisikiliza.

Naamini kupitia mfumo huo mpya wa teknolojia, hicho kisingizio ambacho mara nyingi kimekuwa kikitolewa na baadhi ya makarani wa masijala ya kesi za madai pale Mahakama Kuu,kitakwisha.

Aidha naamini teknolojia hiyo mpya itawasaidia wadau wa mahakama na sheria wakiwemo mawakili wa serikali na binafsi, wanafunzi wanaosoma sheria na wale wananchi wanaopenda kufuatilia maamuzi na hukumu mbalimbali kupata na kuzisoma kwa urahisi hukumu mbalimbali zinazotolewa na majaji wetu ambazo katika uzinduzi huo tuliambiwa kuwa zitakuwa zikiwekwa ndani ya tovuti ya mahakama ili wananchi waweze kuzisoma.

Na katika hilo, Fukuto la Jamii linaupongeza uongozi mzima wa mahakama nchini chini ya Jaji Mkuu Ramadhani ambaye pia ni Brigedia mstaafu wa JWTZ, Msajili wa Mahakama ya Rufaani Francis Mutungi, Mkuu wa Teknohama wa Mahakama ya Tanzania, Jaji Robert Makaramba,majaji wa mahakama ya rufaa na mahakama kuu na watendaji wote wa mhimili huo kwa kushirikiana kikamilifu kimawazo na vitendo na kuakikisha wanafikia lengo la kufungwa kwa teknolojia hiyo ya kurekodi mashauri katika mahakama zetu.Tunawapongeza sana.

Aidha safu hii inampongeza Ofisa Mtendaji Mkuu wa (ICF) Omar Issa na shirika lake hilo kwa msaada wake wa kufunga mfumo huo na kutoa mafunzo kwa watumishi wa mhimili huo ya jinsi ya kutumia mfumo na hadi kufanikisha leo hii mahakama yetu kwenda sambamba na sayansi ya teknolojia kwa kufunga mfumo katika Mahakama ya Rufaa , Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi, Aridhi na Biashara ambazo tayari zimefungwa mtandao huo, ni wazi kumerejesha heshima ya mahakama zetu hapa nchini.

Nimalizie kwa kuwaasa watumishi waliokwenye nafasi ya kutumia mfumo huo mahakamani kuwa waangalifu na kutumia vizuri kwani hata kama mfumo huo umefungwa kutokana na fedha za wahisani tukumbuke kuwa , utabaki kuwa ni mali ya watanzania wote.Nimesema hivyo kwasababu kuna mifano hai ya baadhi ya watumishi wanaopewa dhamana ya kutumia mali za umma hawazingalii mali hizo kwa umakini na matokeo yake wanazifuja na baada ya muda mfupi tunashuhudia uharibu wa hali ya juu.Msitufikishe huko.

Mwisho, safu hii inawatakieni wasomaji wake kheri na fanaka katika kusherehekea Siku Kuu ya Kristmasi ambao uazimishwa duniani kote Desemba 25, kila mwaka. Pia Fukuto la Jamii ninawaalika wasomaji wa safu hii kusherekea na kufurahi pamoja na mwandishi wa safu hii siku hiyo ya Kristmasi, kwani siku hiyo mwandishi wa safu hii(Happiness Katabazi) nitakuwa naazimisha siku yangu ya kuzaliwa na nitakuwa nikitimiza miaka 32.Namshukuru Mungu kwa kunipa afya njema.

Mungu ibariki Tanzania,Mungu ibariki Afrika
0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Desemba 19 mwaka 2010

Katabazi akiwa na mtetezi wa haki za wafugaji mkoani Morogoro, Mr.Adamu .Ambaye naye alishiriki mafunzo hayo yaliyoandaliwa na The Protection Desk Of Uganda.

Katikati ni (Happiness) , katika igizo la kuonyesha utu wa binadamu, ambapo katika igizo hilo alikuwa ni mama wa watoto ambao wanamtazama ,na walikuwa wakimsikiliza na aliwapatia fedha sawa bila ubaguzi na fedha hizo zilitokana na kilimo cha mahindi.

Happiness Katabazi, nikiwasilisha majibu wa swali ya Human Diginity kwa njia ya mchoro.katika mafunzo ya Usalama na Utambuzi wa mazingira hatarishi kwa watetezi wa Haki za Binadamu yaliyoandaliwa na The Protection Desk of Uganda, Desemba 13-17 mwaka huu, yaliyofanyika katika Eas African All Suit Hotel jijini Arusha, na kushirikisha watetezi wa haki za binadamu toka Tanzania na Ethiopia.

TANZANIA YAPONGEZWA KUHESHIMU HAKI ZA BINADAMU

Na Happiness Katabazi, Arusha

SERIKALI ya Tanzania imepongezwa kwa rekodi yake nzuri ya kuheshimu haki za binadamu na kuwalinda watetezi wa haki hizo.


Hayo yamesemwa na Ofisa wa Protection Desk of Uganda, Yona Wanjala, jana wakati akifungua mafunzo ya siku tano juu ya Usalama na Utambuzi wa Mazingira Hatarishi kwa watetezi wa haki za binadamu yanayoshirikisha watetezi wa haki hizo kutoka Ethiopia, Zimbambwe na Tanzania yanafanyika mjini Arusha.

“Hakuna ubishi kwamba Tanzania ni nchi ambayo bado ina rekodi nzuri ya kuheshimu haki za binadamu na kuwalinda watetezi wa haki za binadamu ukilinganisha na nchi nyingine kama Rwanda, Uganda, Ethiopia na Somalia kwani kila kukicha tumekuwa tukisikia watetezi wa haki za binadamu wakiuawa katika nchi hizo.

“…Kwani hadi sasa serikali ya Tanzania haina rekodi ya kutumia vyombo vyake vya dola kuwanyanyasa, kuwatesa au kuwaua watetezi wa haki za binadamu ukilinganisha na nchi nyingine… katika hili napenda kuipongeza serikali ya Tanzania,” alisema Wanjala ambaye pia ni mkufunzi katika mafunzo hayo.

Alisema, lengo ni kuwaelimisha watetezi wa haki za binadamu wa Tanzania kufahamu vema, mafunzo ya usalama na utambuzi wa mazingira hatarishi na jinsi gani wanavyoweza kujilinda kwa kuwa siku zote watetezi wa haki za binadamu wanakabiliana na hatari za kuuawa au kuteswa na serikali zao au matajiri wakubwa.

Jumla ya washiriki 14 ambao ni watetezi wa haki za binadamu toka taasisi mbalimbali za binafsi wanashiriki mafunzo hayo.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Desemba 14 mwaka 2010

VYOMBO VYA HABARI VITATUMIWA HADI LINI?

Happiness Katabazi

MAPEMA wiki iliyopita Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, alinukuliwa na gazeti moja la kila siku akikemea vikali tabia ya baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari, wafanyabiashara na wanasiasa nchini kuvitumia vyombo vya habari kuwachafua wenzao.

Bila kumung’unya maneno, alisema hivi sasa imeshajengeka tabia miongoni mwa makundi ya watu yanayokinzana kuwatumia baadhi ya wanahabari legelege kuandika habari ambazo hazina tija kwa taifa isipokuwa zina lengo la kuwachafua kisiasa au kibiashara mbele ya jamii.

Membe ambaye alitoa karipio hilo Novemba 27 mwaka huu, muda mfupi kwenye hafla ya kuapishwa kwa baraza jipya la mawaziri katika viwanja vya Ikulu, ambapo kila waziri alikuwa akizungumza matarajio yake au kile kinachomkera.

Binafsi baada ya kusoma habari hiyo iliyomnukuu Membe, niliguswa kwani alichokisema kiongozi huyo ni kweli tupu, sisi tunaoshinda kwenye vyumba vya habari kila siku, hayo yaliyosemwa na Membe tumekuwa tukiyashuhudia na kuyasikia na yalishatupa kichefuchefu na sasa yametukinai.

Hakuna ubishi kwamba miongoni mwa wanabari wana hulka ya kutofuata maadili ya fani ya uandishi wa habari na wamegeuka kuwa wachumia tumbo zaidi kuliko kuangalia maadili na masilahi ya taifa.

Naweza kuwaita watu wa aina hii ni Manyang’au. Hawa wamekuwa wakijirahisi kwa baadhi ya wanasiasa, wafanyabiashara ambao wamekuwa wakiwapata fedha au ahadi fulani ili waandike habari za kuumiza watu wanaowakusudia.

Waandishi hao hudiriki hata kutoboa siri ya habari fulani za uchunguzi ambazo zinatarajia kuchapishwa au kutangazwa kwenye chombo fulani kwa lengo la kujikomba ili waonekane bora.

Mchezo huo binafsi naouna ni hatari kwa fani ya habari na usalama wa baadhi ya waandishi ambao wako mstari wa mbele kuandika habari za uchunguzi kwa lengo la kufichua maovu.

Tabia hiyo imewafanya baadhi ya waandishi wa habari mahiri na wale wanaochipukia kuandika habari za uchunguzi kuamua kupunguza kasi na wengi hufikia hatua ya kuacha kabisa kuandika habari za aina hiyo.

Kimsingi tukubaliane kuwa tasnia ya uandishi wa habari ina mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa letu, sasa inapofika baadhi ya wanahabari wenyewe kushindwa kusimamia maadili ya taaluma yao na kuwa wahujumu kwa wanahabari wenzao taifa halitoweza kuendelea kwa kiwango kinachotakiwa.

Sote tunafahamu kuwa mwanasiasa chakula chake ni vyombo vya habari, yaani wanapenda kuandikwa mazuri yao tu lakini yanapoandikwa mabaya yao huwa mbogo na kuziita habari hizo ni uzushi wenye lengo la kuwachafulia jina.

Uswahiba wa wanasiasa na waandishi wa habari katika kupanga na kuandika habari za kuwachafua watu fulani kamwe haupaswi kupewa nafasi katika jamii iliyostaarabika.

Urafiki huo huo ndiyo unaowafanya viongozi kuwa vinara wa kuingia na simu, vinasa sauti kwenye vikao vya siri vya vyama vyao na hata vikao vya serikali, kurekodi mazungumzo yao na mara baada ya kikao kumalizika yote yaliyozungumzwa humo huingia kwenye vyombo vya habari.

Vinasa sauti vilivyotumika hukabidhiwa kwa wanahabari wasikilize yote yaliyozungumzwa kwenye vikao bila kujali kuwa kilichozungumzwa mle ni siri au mkutano wa ndani.

Aina hii ya viongozi ambao hawajui nini maana ya kutunza siri ya vyama au ya serikali ndiyo inayochangia nyaraka muhimu za serikali kuanikwa juani na kila mtu kuanza kuzijadili kulingana na upeo wake na mwisho wa siku kuweza kuathiri mustakbali wa taifa.

Wanaofanya mchezo huu haramu wa kuvujisha siri wengine tuliwashuhudia wakila viapo mbele ya Rais Jakaya Kikwete na kushika Msaafu na Biblia kwamba watatunza siri na kuihifadhi Katiba ya nchi. Hivi viongozi wenye tabia hii nikisema wana laana nitakuwa nakosea?

Nchi inayoongozwa na viongozi ambao wanakiuka viapo vyao vya kutunza siri au kuwahudumia wananchi pasi upendeleo haiwezi kuendelea kwa sababu wale waliopewa madaraka tayari watakuwa na laana ya kukiuka maagizo waliyoapa kuyalinda kwa kutumia vitabu vyao vya dini.

Wanasiasa tulionao hivi sasa wamekuwa wakitumia fimbo ya fedha zao au zile wanazosaidiwa na marafiki zao kutengeneza mtandao kwenye vyombo vya habari na dola ili kutimiza mambo yao maovu.

Tasnia ya habari itaiangamiza nchi kama itaendelea na tabia hii ya kutumiwa na watu wachache wenye masilahi binafsi iwe yawe ya kibiashara au ya kisiasa.

Fukuto la Jamii, linasema Membe umenena uliposema baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari nao wamekuwa wakiingilia uhuru wa wanahabari kwa kuelekeza habari ipi ichapishwe au itangazwe na ipi isichapishwe au kutangazwa.

Kuna baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari hapa nchini wameanzisha vyombo hivyo si kwa lengo kutaka kukuza taaluma ya habari, uhuru wa habari, kutoa ajira, kufanya biashara bali wamevianzisha kwa malengo la kuwachafua wale wasiokubaliana nao.

Wameanzisha vyombo hivyo pia kwa lengo la kuficha maovu yao na maswahiba zao, hawa masilahi ya taifa kwao ni msamiata mgumu kueleweka katika vichwa vyao.

Katika taifa linalojali usalama wa wananchi wake na sheria za nchi yake, haliwezi kuvumilia uanzishwaji wa utitiri wa magazeti tena kwa msimu ambayo baadhi yao yanachapisha habari zinazomkashifu mtu kwa maslahi fulani.

Tumeshuhudia wakati wa uchaguzi mkuu hasa mwaka 2005, magazeti mengi yalianzishwa bila udhibiti ukilinganisha na harakati za uchaguzi mkuu wa Oktoba 31, mwaka huu.

Katika kipindi hicho magazeti mengi yalianzishwa na baadhi ya waandishi wenzetu katika magazeti hayo ama walikuwa wanajua au hawajui walijikuta wakiwa na kazi ya kuandika makala za kuwachafua baadhi ya wagombea urais na wabunge.

Hali kadhalika kwa mwaka huu, pia kuna baadhi ya wanahabari wenye utashi wa kimaamuzi kwenye vyombo vya habari wanavyovitumikia nao walijikuta wakitumika kuwachafua baadhi ya wanasiasa na vyama fulani badala ya kusimamia maadili ya taaluma yao.

Hivyo basi umefika wakati mwafaka kwa wamiliki wanaoanzisha vyombo vya habari kama hawana dhamira ya dhati ni vyema wakaachana na biashara hiyo wakaenda kuwekeza katika biashara nyingine kuliko kuanzisha kitu kwa dhamira mbaya.

Idara ya Habari (Maelezo) chini ya Wizara ya Habari, Vijana na Michezo, ilishindwa kuvichukulia hatua madhubuti baadhi ya vyombo hivyo ambavyo vimekuwa vikizua habari za kuwachafua viongoni au wananchi wasio na hatia.

Habari za aina hii kwa namna moja au nyingine zimechangia watendaji wa serikali na wa sekta binafsi kupunguza morali ya kufanyakazi hasa pale wananchi wanapoamua kuhukumu utendaji wao wa kazi wakitumia ushahidi unaotolewa na vyombo vya habari.

Watendaji hawa wamekuwa wakisikika wakilalamika Idara ya Habari (Maelezo) kwa kuyashughulikia baadhi ya magazeti yanayokiuka maadili ya uandishi wa habari huku wakiyaacha mengine yanayomilikiwa na watu wenye ushawishi ndani na nje ya serikali.

Waziri Membe, ni kiongozi wa siku nyingi serikali na kwenye chama tawala ambaye ameona uozo huo na kutoa angalizo, kilichobaki hivi sasa ni kwa wahusika kuchukua hatua.

Kwa hiyo Fukuto la Jamii, linatoa rai kwa Waziri wa Wizara ya Habari Vijana na Michezo, Dk. Emmanuel Nchimbi na Naibu wake Dk. Fenella Mukangara kuona uozo huo, ni miongoni mwa changamoto kubwa inayoikabili ofisi yao.

Sio siri kwamba Dk. Nchimbi, ana mahusiano mazuri na wanahabari wengi, lakini tunaomba mahusiano hayo mazuri yasimpofushe macho na kushindwa kuyachukulia hatua baadhi ya magazeti yanayokiuka maadili ya taaluma zao.

Waziri huyo anapewa meno makali zaidi na sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 ambayo inampa mamlaka kulifungia gazeti pale anapobaini kuwa limechapisha habari iliyokiuka maadili.

Sheria hiyo imekuwa ikilalamikiwa na wadau wengi kuwa imepitwa na wakati na inatoa fursa kwa kiongozi husika kuyafungia magazeti ama kwa kukiuka maadili au kwa sababu nyingine ikiwemo za binafsi.

Wanahabari tunapaswa kujirekebisha kwa kutokubali kutumiwa na wanasiasa au wafanyabiashara wenye masilahi binafsi ili tuweze kuheshimika mbele ya jamii inayotuzunguka.
Leo hii waandishi wa habari wametolewa thamani na jamii kutokana na kutumiwa na watu wenye malengo binafsi.

Wanahabari wakifanikiwa kujirekebisha wageukie kwenye sheria hiyo ya magazeti ya mwaka 1976 kwa kufungua kesi ya Kikatiba Mahakama Kuu, kuiomba mahakama hiyo iibatilishe.

Kama hatutalisimamia jambo hilo, sheria hiyo itaendelea kutumiwa na waziri husika hata pale pasipokuwa na ulazima wa kulifungia gazeti sambamba na kuamua kutoyafungia magazeti yanayokiuka maadili.

Fukuto la Jamii linasema vyovyote iwavyo, mwisho wa siku mwanahabari ndiye mwenye taaluma ya habari hivyo ni vyema baadhi ya wanahabari ambao maisha yao na akili na utu wao wameamua kujibinafsisha kwa wanasiasa ambao wamekuwa na hulka za kupenda kuandikwa kwa mazuri na mabaya yafichwe wakaachana na tabia hiyo kwani wakumbuke wanasiasa ni watu wa kupita na hayo madaraka yao na taaluma za waandishi wa habari zitabaki kuwa pale pale.

Hivyo ni vyema kila mmoja wetu atimize wajibu wake kwa maslahi ya taifa letu na maadili ya taaluma inavyotutaka na si vinginevyo.

Tuna mifano hai ya machafuko yaliyotokea kwenye nchi za za Rwanda na Burundi ambako makala na habari za kichochezi zilizokuwa zikichapishwa na kutangazwa kwenye vyombo vya habari zilikuwa chanzo cha kuleta machafuko.

Fukuto la Jamii leo linampongeza Waziri Membe kwa kukemea uozo huo na linamtaka aendelee kukemea maovu mengine yanayofanywa na baadhi ya wanasiasa wenzake wenye hulka za kinyang’au ambao wanapenda kupambwa kwenye magazeti wakati hawana udhu na vigogo wengine.

Sisi wanahabari wakorofi haya anayoyasema Membe leo tuliyasema miaka minne iliyopita katika makala zetu lakini tulipuuzwa na kuonekana ni maamuma, lakini leo Mungu ni mkubwa kwani ameishaanza kuwafumbua macho hata viongozi wetu kuuona uozo huo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Desemba 12 mwaka 201o

HAPPINESS KATABAZI AITIMU KOZI YA CHETI CHA SHERIA

Pichani ni Mwandishi Mbobevu wa Habari za Mahakamani nchini, Happiness Katabazi katika mahali yake ya kumaliza Kozi ya Cheti cha Sheria iliyokuwa ikitolewa na Shule ya Sheria Tanzania ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City,Novemba 27 mwaka huu.Mahafali hayo ni mahafali ya 40 ya chuo hicho.
Remove Formatting from selection
Nikiwa na mwanangu kipenzin Queen Mwaijande(Malkia) nyumbani kwetu Sinza 'C',baada ya kurejea kwenye mahafali.
Happiness Katabazi at Mliman City Shop

Baada ya kumalizika mahafali niliingia Mlimani City kupiga picha na kununua bidhaa mbalimbali ikiwemo (Wine)Mvinyo.

Nikiwa na Svea Mchome muda mfupi baada ya kuvalishwa mataji

Nikimvisha taji mhitimu mwenzangu Svea Mchome ambaye ni walikiwa ni miongoni mwa marafiki zangu wa karibu wakati tukisoma kozi hiyo ya cheti cha Sheria, UDSM,ikiwa ni muda mfupi baada ya mahafali kumalizika.
Nikiwa nimekaa chini chini na wahitimu wenzangu tukisubiri kuingia ukumbini kwaajili ya mahafali.

Tabazi na Kumbukumbu

Katabazi akiwa nyuma ya bango hilo lilokuwa linatumiwa na wapiga picha wa kujitegemea nje ya ukumbi wa Mlimani City , siku ya mahafali yake.

JAJI WARIOBA NA MAANDAMANO YA WASOMI


JAJI Joseph Warioba ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Na Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Rwekaza Mukandara wakiongoza maandamano ya wanataaluma kuingia katika ukumbi wa Mlimani City, jumamosi iliyopita ambapo siku hiyo ndiyo yalikuwa mahafali ya 40 ya chuo hicho.

KATABAZI-TUMEHITIMU


Happiness Katabazi(Kulia) akifurahia jambo na wahitimu wenzake wa kozi ya cheti cha sheria iliyokuwa ikitotolewa na Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wa katikati ni Zawadi na akifuatiwa na Anna Lyamuya, nje ya ukumbi wa Mlimani City ,Dar es Salaam, Novemba 27 mwaka huu, katika mahafali ya 40 ya chuo hicho yalifanyika ukumbini hapo

ASHA BILAL:'USIMPIGE MWANAMKE PIGA MPIRA'

Mke wa Makamu wa Rais Mama Asha Bilal, akiwa na zawadi ya mpira aliokabidhiwa na waratibu wa maonyesho ya Kazi za Wake wa Mabalozi ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kusaidia watu wasiojiweza yaliyoandaliwa na Kikundi cha Wake wa Mabalozi yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Shule ya Tanganyika International Masaki jijini Dar es Salaam leo Nov 20. Mpira huo ulikuwa na Ujumbe usemao ‘USIMPIGE MWANAMKE PIGA MPIRA’. Picha na Muhidin Sufiani

ASHA BILAL NA UTAMADUNI

Mke wa Makamu wa Rais Mama Asha Bilal, akivishwa beji ya kampeni ya kutokomeza ugonjwa wa Vistula na mwakilishi wa ‘MABINTI Vistula’, Katia Geurts, kutoka CCBRT, wakati alipoalikwa kufungua rasmi maonyesho ya Kazi za Wake wa Mabalozi yaliyoandaliwa na Kikundi cha Wake wa Mabalozi nchini kwa ajili ya kuchangisha fedha za kuwasaidia watoto na watu wasiojiweza na NGO’s, yaliyofanyika kwenye Viwaanja vya Shule ya Tanganyika International Masaki Jijini Dar es Salaam, Nov 20 mwaka huu. Picha na Muhidin Sufiani

KAMISHNA TRA:MRAMBA HAKUITIA HASARA SERIKALI

Na Happiness Katabazi

NAIBU Kamishna wa Kodi za Ndani wa Mamlaka ya Mapato nchini(TRA), Christine Shekidele(54), katika kesi ya matumuzi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 11.7 inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba na wenzake,amesema kampuni ya Alex Stewart Bussiness Corporation haijailetea serikali hasara.

Mbali na Mramba, ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu Mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja.Ambao kesi yao inasikilizwa na Jaji John Utamwa anayesahidiana na Hakimu Mkazi Sam Rumanyika na Saul Kinemela na wanatetewa na mawakili wa kujitegemea Hurbet Nyange, Elisa Msuya na Profesa Leonard Shahidi na upande wa Jamhuri unawakilishwa na Wakili Kiongozi, Fredrick Manyanda na Ben Lincoln.

Shekidele ambaye ni shahidi 13, alitoa maelezo hayo jana wakati akijibu swali la wakili wa upande wa utetezi, Elisa Msuya alilomtaka aieleze mahakama kwamba endapo kampuni imepewa msamaha wa kutokulipa kodi na serikali kwa kufuata kanuni na sheria za nchi ,je kiasi hicho cha kodi alichosamehewa kitahesabika kuwa ni hasara kwa taifa?

“Kwa mujibu wa sheria za Kodi, pale serikali inapotoa msamaha wa kodi kwa kampuni husika , kile kiwango cha kodi kilichosamehewa katu hakiwezi kuhesabiwa kuwa kimeletea hasara kwa serikali, hivyo kampuni hiyo ya Alex Stewart ambayo Mramba aliidhinisha ipewe msamaha wa kodi na serikali yetu kwa ujumla ikakubali kutoa vibali vya kuisamehe kodi kampuni hiyo kwa kufuata sheria, nasisitiza serikali yetu haikupata hasara kwasababu kampuni hiyo ilisamehewa isilipe kodi.”alisema Shekidele.


Aidha Shekidele akijibu swali la Jaji Utamwa lilomtaka kuieleza mahakama mahakama kwamba juzi alieleza kuwa TRA ilikuwa haina kumbukumbu za ripoti ya fedha ya kampuni hiyo na iweje jana aimbie mahakama hiyo kuwa TRA inayo taarifa za fedha za kampuni hiyo, na ninani mwenye jukumu la kuandaa ripoti ya taarifa za fedha kodi za makampuni pale TRA?

“Mhh! Nikweli Jaji unavyosema lakini …toka mwaka 2004,TRA ilikuwa haina ripoti za fedha za kampuni hiyo lakini ilipofika mwaka 2007, TRA ndiyo ikapata ripoti za fedha za kampuni hiyo na TRA na hizo ripoti za fedha za kampuni hiyo zililetwa TRA na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Dk.Edward Hosea…..lakini hata hivyo mwenye jukumu la kuandaa taarifa za fedha za kodi ni mlipa kodi na msaidizi wake” alieleza Shekidele huku akionekana kubabaika babaika.

Shahidi huyo ni shahidi wa mwisho wa upande wa Jamhuri katika kesi hiyo, ila upande wa utetezi umeiomba mahakama imuite shahidi wa kwanza wa upande wa Jamhuri ambaye alishatoa ushahidi wake ili afike tena mahakamani hapo ili upande wa utetezi uweze kumuhoji na mahakama hiyo ilikubali ombi hilo na kuairisha kesi hiyo hadi Desemba 17 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya kutajwa na Januari 19-20 mwaka 2011 itakuja kwaajili ya kumalizia kusikiliza ushahidi wa shahidi wa kwanza.

Mbali na Mramba washtakiwa wengine ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mipango na Uchumi, Gray Mgonja ambao wanatetewa na mawakili wakujitegemea , Hurtbet Nyange, Elisa Msuya na Professa Leonard Shahidi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Novemba 25 mwaka 2010

KESI YA MRAMBA YASHIKA KASI

Na Happiness Katabazi

NAIBU Kamishna wa Kodi za Ndani wa Mamlaka ya Mapato nchini(TRA), Christine Shekidele(54), katika kesi ya matumuzi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 11.7 inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba na wenzake, ameimbia mahakama kuwa Kampuni ya Alex Stewart Bussiness Corporation ilikuwa haifuati sheria za kodi.

Mbali na Mramba, ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu Mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja.

Shekidele ambaye ni shahidi wa 13 wa upande wa jamhuri katika kesi , alitoa madai hayo mbele ya Jaji John Utamwa aliyekuwa akisaidiwa na Mahakimu Wakazi Sam Rumanyika na Saul Kinemela katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam,jana wakati akiongozwa kutoa ushahidi wake na Wakili Kiongozi wa Serikali Fredrick Manyanda.

Shekidele aliambia mahakama kuwa mwaka 2007 wakati akiwa na wadhifa huo pia alikuwa ni Kaimu Kamishna wa Kodi za ndani, na majukumu yake yalikuwa ni kuangalia utendaji wa makusanyo ya kodi za ndani na kujijbu mawasiliano na barua zitokazo nje ya Idara yake na kwamba kampuni hiyo ilikuwa haileti ripoti za mahesabu yake.

Hata hivyo Shekidele alianza kubabaika baada ya kubanwa maswali na wakili wa Mramba, Hurbert Nyange kwamba ana ushahidi gani kama zile ripoti za mahesabu za mwaka za kampuni hiyo ambazo zilitolewa na TAKUKURU kwa TRA kama kweli ni za kampuni hiyo.

“Mh! sikuziona hizo ripoti ya mahesabu ya kampuni hiyo.....aah waheshimiwa mahakimu naomba nibadili jibu langu la awali, nimekumbuka niliziona hizo ripoti ila sijui ni nani alizisaini...na sifahamu kama wakati TRA inaandaa ripoti hizo za mahesabu za kampuni hiyo sifahamu kama kampuni hiyo ilituma mwakilishi wake kushiriki kushirikiana na TRA kuandaa mahesabu hayo”alidai Shekidele.Kesi hiyo inaendelea kusikiklizwa tena leo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Novemba 24 mwaka 2010

KESI YA MARANDA NA EPA YASHIKA KASI

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya wizi ya sh bilioni 2.2 katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) Benki Kuu ya Tanzania, (BoT), inayomkabili Mweka Hazina wa CCM, Mkoa wa Kigoma, Rajabu Maranda, na ndugu yake, Farijala Hussein, umefunga kesi yake rasmi.


Mbele ya Jaji, Fatma Masengi, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Wakili Kiongozi wa Serikali, Fredrick Manyanda, aliiambia mahakama hiyo kuwa upande wa Jamhuri umefunga rasmi kesi hiyo baada ya mashahidi wake sita kumaliza kutoa ushahidi wake jana.

“Sisi upande wa Jamhuri leo tunatangaza rasmi kuifunga kesi yetu baada ya kuleta idadi hiyo ya mashahidi,” alidai Wakili Kiongozi Manyanda.

Kwa upande wake wakili wa utetezi, Majura Magafu aliomba mahakama iuamuru upande wa Jamhuri umpatie mwenendo mzima wa kesi hiyo ili aweze kwenda kuupitia na kuweza kumsaidia kujenga hoja itakayoweza kuishawishi mahakama iwaone wateja wake hawana kesi ya kujibu na Jaji Masengi alikubaliana na ombi hilo.
Jaji huyo aliiahirisha kesi hiyo hadi Desemba 13 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya kutajwa na kuona kama tayari upande wa Jamhuri umeishawapatia mwenendo huo upande wa utetezi.

Awali shahidi wa sita wa upande wa Jamhuri, ambaye ni Msajili Msaidizi (BRELA), Noel Shani, akiongozwa kutoa ushahidi wake na Manyanda aliambia mahakama kuwa yeye ndiye aliyelisajili jina la Kampuni ya Money Planner ambayo ilitumiwa na washitakiwa kuchota fedha za EPA.

Alisema anachokifahamu yeye ni kwamba alisajili jina hilo la kampuni ambayo wamiliki wake ni Paul Nyingo na Fundi Ayeshi Kitunga na si Maranda na Farijala kama washitakiwa wanavyodai kuwa kampuni hiyo ni yao.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Novemba 17 mwaka 2010

DK.SLAA AUKACHA USULUHISHI KORTINI

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, jana ilishindwa kuanza kuendesha usuluhushi katika kesi ya madai ya kupora mke wa mtu inayomkabili aliyekuwa mgombea urais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kupitia chama (CHADEMA), Dk.Willbroad Slaa baada ya mdaiwa na wakili wake kutotokea mahakamani.

Kesi hiyo ambayo jana ilikuja kwaajili ya usuluhishi lakini katika hali isiyotarajiwa mdaiwa huyo wala wakili wake Mabere Marando walishindwa kufika mahakamani hapo wala kutoa taarifa za udhuru.

Hali hiyo iliyomsababisha msuluhishi wa kesi hiyo(Jaji )Zainabu Muruke kusema kuwa kitendo hicho kimetafsiriwa na mahakama kuwa mdaiwa Dk.Slaa hayuko tayari kwaajili ya usulushi kwahiyo ataandika taarifa kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Semistocles Kaijage ili aweze kupanga jaji mwingine wa kuanza kuisikiliza kesi hiyo.
“Kutokana na mdaiwa (Dk.Slaa) na wakili wake Marando kutokufika leo(jana) mahakamani hapa kwaajili ya usuluhishi kama walivyokuwa wamekubali awali kushiriki katika meza ya usuluhishi tena bila hata kutoa taarifa ya udhuru , mahakama hii imetafsiri kitendo hicho kuwa mdaiwa hayupo tayari kwaajili ya usuluhishi na hivyo nitaandika taarifa kwa Jaji Mfawidhi ili aweze kupanga jaji mwingine kwaajili ya hatua zitakazofuata ili ianze kusikilizwa..”alisema Jaji Muruke.
Awali pande zote mbili katika kesi hiyo zilikubalina kushiriki katika meza usulushi na kwamba kama usuluhishi huo ukishindika , kila upande utaleta mashahidi wa nne pindi kesi hiyo itakapoanza kusikilizwa.
Kisheria kesi za madai kabla haijaanza kusikilizwa kunakuwa na usuluhishi ambapo jaji ndie anakuwa msuluhishi na endapo mdaiwa akikubali madai anayolalamikiwa,kesi humalizikia hapo na endapo mdaiwa atakwepa kushiriki kwenye usuluhishi au akashiri kwenye meza ya usulushi lakini wakashindwa kufikia mwafaka kesi hiyo uendelea kusikilizwa mahakamani.

Katika kesi hiyo ya madai inayomkabili Dk.Slaa ambaye pia ni Katibu Mkuu wa (CHADEMA). Aminiel Mahimbo amemshitaki Dk. Slaa akidai kuwa amempora mke wake Josephine Mushumbusi na kuwa anamnadi katika majukwaa ya kisiasa katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, kuwa ni mchumba wake, hoja ambazo Dk .Slaa alizipinga katika majibu yake na kudai kuwa hakufahamu kuwa mwanamke huyo ni mke wa mtu.

Mahimbo anaomba mahakama imwamuru Dk.Slaa amlipe Sh.bilioni moja ikiwa ni fidia ya kudhalilishwa kiongozi huyo wa kisiasa. Mahimbo katika madai yake anadai kuwa Septemba 7, 2002 alifunga ndoa na mwanamke huyo katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ushirika wa Kijitonyama na wala ndoa yao haijawahi kuvunjwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano,Novemba 17 mwaka 2010

WAKILI KESI YA ZOMBE AFARIKI DUNIA

Na Happiness Katabazi

ALIYEKUWA Mwanasheria Mwandamizi wa Serikali, Jasson Kaishozi katika kesi ya mauji ya wafanyabiashara wa nne iliyokuwa ikimkabili aliyekuwa Mkuu wa Upelele Mkoa wa Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi, (ACP),Abdallah Zombe na wenzake nane amefariki dunia jana.

Akizungumza na Tanzania Daima jana, Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Elizer Feleshi alisema ofisi yake ilipata taarifa za kifo hicho jana mchana kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mbeya na kwamba alikwenda hospitalini hapo kwa ajili ya kumuona daktari, alipomaliza aliishiwa nguvu na kufariki dunia wakati akipatiwa matibabu.

“Nikiwa kama DPP wa Tanzania na timu yangu wa waendesha mashtaka nchini, tumepokea kwa masikitiko na mshtuko mkubwa taarifa za kifo cha Kaishozi kwani alikuwa ni miongoni mwa mawakili mahiri wa serikali hasa kwa upande wa uendeshaji wa mashauri ya jinai,” alisema Feleshi kwa masikitiko.

Alisema taratibu za mazishi zinafanywa na mwili wa marehemu utasafirishwa kupelekwa nyumbani kwao Bukoba Vijijini kwa mazishi. Hadi kifo chake Kaishozi alikuwa Wakili wa Serikali Mfawidhi wa Kanda ya Mbeya.

Mbali na Zombe, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Christopher Bageni, Ahmed Makele, WP 4593 PC Jane Andrew, D 1406 Koplo Emmanuel Mabula, D 8289 DC Michael Shonza, D. 2300 Abeneth Saro, D.4656D/Koplo Rajabu Bakari na D.1317D/XP Festus Gwasabi.

Washitakiwa hao walidaiwa kuwa Januari 14, mwaka 2006 waliwaua wafanyabiashara watatu wa madini wa wilayani Ulanga, mkoani Morogoro; Ephraim Chigumbi, Sabinus Chigumbi na Mathias Lukombe pamoja na dereva teski Juma Ndugu, mkazi wa Dar es Salaam kwa madai kuwa walikuwa majambazi
Agosti 17 mwaka jana, Jaji wa Salum Massati aliwaachilia huru washtakiwa wote kwa maelezo kuwa upande wa Jamhuri ambao ulikuwa ukiwakilishwa na marehemu Kaishozi, Mwipopo, Mgaya Mtaki, Mzikila umeshindwa kuthibitisha kesi hiyo ambayo ilikuwa ikivuta hisia za watu wengi hapa nchini.

Kaishozi ambaye katika kesi ya Zombe alikuwa akisaidiana na mawakili wenzake wa serikali, Angaza Mwipopo, Mgaya Mtaki na Alexanda Mzikila ni wakili wa pili kufariki dunia katika kesi hiyo wa kwanza alikuwa wakili aliyekuwa akimtetea Zombe, Moses Maira.

Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Novemba 16 mwaka 2010

GIRE AIKANA RICHMOND KORTINI

Na Happiness Katabazi

MSHITAKIWA, Naeem Adam Gire, anayekabiliwa na mashitaka ya kughushi hati ya nguvu ya kisheria na kutoa taarifa za uongo kwa watumishi wa serikali kuhusu Kampuni ya kuzalisha umeme ya Richmond LLC ya Texas, Marekani amekana kuwa miongoni mwa wakurugenzi wa kampuni hiyo na kwamba wala hakutoa taarifa za uongo.


Gire alikanusha tuhuma hizo zilizoelekezwa kwake na upande wa Jamhuri katika kesi hiyo jana mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi, Walirwande Lema, muda mfupi baada ya Wakili Mkuu wa Serikali, Fredrick Manyanda, kumaliza kumsomea maelezo ya awali mshitakiwa huyo ambaye anatetewa na wakili wa kujitegemea, Richard Rweyongeza.

“Nakanusha mbele ya mahakama hii kuwa mimi si mkurugenzi wa kampuni hiyo ila nakubali kwamba mfanyabiashara anayeishi Marekani, Mohamed Gire, ambaye ni Mwenyekiti wa Richmond Development Company Limited, Liabilities Company (LLC), ni kaka yangu na mimi pia ni mfanyabishara ninayemiliki Richmond Internet CafĂ© iliyopo Mtaa wa Kipata nyumba Na.66 Dar es Salaam,” alidai Naeem Gire.

Manyanda aliendelea kueleza kuwa Machi 13, 2006, jijini Dar es Salaam, mshitakiwa akiwa na dhamira ya kutenda kosa, alighushi hati ya nguvu ya kisheria (power of attorney) inayoonyesha imetolewa na Mohamed Gire, ambaye ni Mwenyekiti wa Kampuni ya Richmond LLC ya Texas, Marekani, kwamba amemruhusu kufanya shughuli za kampuni hiyo hapa nchini.

Aliendelea kuieleza mahakama kuwa mshitakiwa huyo Machi 20 mwaka 2006, katika eneo la Ubungo, Umeme Park, Barabara ya Morogoro, alitoa hati hiyo ya nguvu ya kisheria inayomuidhinisha yeye kwamba ameruhusiwa kufanya kazi ya kampuni hiyo ya Marekani hapa nchini.

Manyanda aliendelea kuieleza mahakama kuwa Juni 2006 hapa jijini, mshitakiwa huyo pia alitoa taarifa za uongo kwa wajumbe wa timu ya majadiliano ya serikali, kuwa Kampuni ya Richmond LLC ya Texas, Marekani, ina uwezo wa kuzalisha umeme kwa kiwango hicho ili apewe tenda hiyo.

Wakili Mkuu huyo wa serikali Manyanda, aliendelea kuieleza mahakama kuwa Julai, 2006, ambapo mshitakiwa akifahamu na kwa ulaghai, alitoa hati ya nguvu ya kisheria iliyotolewa Machi 3, mwaka huo iliyokuwa ikimuonyesha kuwa ameruhusiwa na Mwenyekiti wa Kampuni hiyo, Mohamed Gire, kufanya kazi za kampuni hiyo hapa nchini.

Aidha, wakili Manyanda alisema baada ya mshitakiwa huyo kukamatwa na kuhojiwa na vyombo vya dola Oktoba 13 mwaka 2008, alikiri kutenda makosa hayo aliyoshitakiwa nayo mahakamani.
Hakimu Lema baada ya kusikiliza maelezo hayo ya awali aliahirisha kesi hiyo hadi Desemba 8 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwa ajili ya kutajwa.

Kwa mara ya kwanza mshitakiwa huyo alikamatwa na kufikishwa mahakamani Januari 13 mwaka jana na Gire amefikishwa mahakamani ikiwa ni mwaka mmoja baada ya aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi na mwenzake aliyekuwa Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Ibrahim Msabaha, walilazimika kujiuzulu nyadhifa zao kwa kashfa hiyo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Novemba 16 mwaka 2010

UBAGUZI KATIKA CHAGUZI USILIVURUGE TAIFA

Na Happiness Katabazi

KWA takribani miezi miwili mwandishi wa safu hii nilishindwa kuwaletea makala kama ilivyoada kwasababu ya kuwa kwenye kampeni za uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 31 mwaka huu, hapa nchini.


Katika kipindi chote hicho nilikuwa nikizunguka nchini nzima na aliyekuwa mgombea mwenza wa Chama cha Mapinduzi(CCM), ambaye kwa sasa ndiye Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk.Mohamed Ghalib Bilal ,nikiwa miongoni mwa waandishi wa habari wachache tuliochaguliwa kuunda timu ‘Press Team Bilal 2010 Campaign’.

Namshukurumu mungu tumeweza kumaliza kazi hiyo salama na kurejea ofisini kwangu tayari kabisa kwaajili ya kuendelea kulitumikia taifa hili kupitia kalamu yangu.Hivyo nawaomba radhi wasomaji wangu kwa kushindwa kuwaletea makala kwa kipindi chote hicho.

Mbali na maelezo hayo leo katika safu hii, nitajadili kwakina mchakato mzima wa uchaguzi mkuu uliopita pamoja na makandokando yake.
Watanzania tumeuona uchaguzi mkuu wa 2010 ukimalizika kwa taswira ambayo ni ya mchanganyiko.Wapo waliofurahi kwa kuwa ama wameshinda ama wagombea wao wameshinda.

Lipo kundi jingine la walioshindwa ambao wao wameshindwa ama wagombea wao wameshindwa .Lakini hivyo ndivyo ilivyotazamiwa iwe katika mazingira ya kinyang’anyiro ambacho kinapelekea kupatikana kwa mshindi mmoja tu kati ya wengi.Kura moja ni ushindi na hiyo ndiyo falsafa ya ushindi .

Sasa uchaguzi mkuu ulimalizika hivi karibuni ni wa tatu kufanyika tangu vyama vingi vianzishwe hapa nchini Julai 1992.

Je, tukiondoa mazingira tuliyoyataja hapo juu, Watanzania tumejifunza nini cha kuweza kujivunia kuwa sasa tunaelekea kwenye demokrasia bora iliyokomaa?

Mosi; nililoliona ni kukosekana kwa mazingira bora ya kisheria ya uchaguzi huru na wa haki.Jambo hili ni kubwa kwasababu chanzo chake ni Katiba ya nchi ,ambacho ni kilio cha wananchi wengi tangu mwaka 1992.
Hatujapa Katiba mpya inayopiganiwa na wana mageuzi na wala hatujapata Katiba nzuri kutokana na viraka vinavyobandikwa mara kwa mara na watawala waliopo madarakani.

Hivyo hatuna Tume huru ya Uchaguzi , hatuna sheria inayoweka mazingira sawa ya ushindani wa vyama vya siasa na hatuna uwezeshwaji wa washiriki wa uchaguzi ili kuakikiasha kila raia ana faidi haki yake ya binadamu na Katiba ya kuchagua au kuchaguliwa.

Pili;uchaguzi wa mwaka 2010,umeonyesha udhaifu mkubwa wa misingi kitaifa tuliokuwa tunajivunia kuwa tunayo na tunaheshimu sana.Msingi wa kwanza ambao ufa wake umeshindikana kuzibwa katika uchaguzi huu ni udini.Ghafla baadhi ya wagombea wakuu na wafuasi wa vyama vya siasa hasa wa CCM na CHADEMA walijikuta wakirushiana makombora ya udini .Kila mmoja akimlaumu mwenzake akitumia udini kujipatia udini kujipatia ushindi.

Ni kweli kwamba katika nchi yetu wengi wetu tuna dini kwa hiyo ni vigumu kumpata mgombea asiye na dini.Lakini ni hatari dini inapotumika kama mbinu halali ya kusaka uongozi.

Hilo halina mjadala kuwa ni baya ,la kukemewa vikali na ni la aibu na lina hatarisha usala wa taifa.Ila wasiwasi wangu ni viongozi wanapaswa wawe mstari wa mbele kukemea pepo huyo wa udini ,baadhi yao walitumia mbinu hiyo ya ubaguzi wa udini katika kampeni zao na kufanikiwa kupata madaraka na kwakuwa wanasiasa hao wenye hulka za kinyang’au wamefanikiwa kisiasa kwa kutumia mbinu hiyo ambayo ina hatarisha usalama wa taifa letu.

Sasa tujiulize katika chaguzi nyingine za kiasa wanasiasa hawa wataacha kutumia mbinu hiyo hatari ya udini katika chaguzi nyingine za kisiasa ili waweze kutwaa tena madaraka ya kisiasa?

Tayari hivi sasa watu wanangojea kuona serikali itakayoundwa na Rais Jakaya Kikwete itakuwa na sura kutokana na balaa hilo la udini?.

Kila mara mteuaji atakapoweka usawa au uwiano wa kidini ,haina maana kwamba hatumii kigezo cha udini.
Tatu; ukabila,ukanda,sehemu anakotoka mgombeaji. Tanzania ni nchi mmoja na Watanzania ni taifa moja linalojitambua kuwa ni ndugu moja.

Pamezuka hatari kubwa ya watu kuulizana asili,koo,kabila zao,ukanda anakotoka au sehemu anapotokea mgombeaji.

Kwa hiyo imefika mahali sasa imekuwa nongwa mfano mgombea atokee Karagwe mkoani Kagera aje kugombea udiwani au ubunge jijini Dar es Salaam, au atoke mkoa wa Mbeya aende akagombee katika moja ya jimbo au Kata mkoani Tanga.Mgombea atakayeenda kugombea Tarime ataulizwa kabila na anatokea ukoo gani?
Kwa hiyo mgombea ubunge wa mfano jimbo la Ubungo,Kawe na majimbo mengi atapata ushindi kwasababu watu wengi wanaoishi katika majimbo wa kabila lake.

Hivi tangu lini tumeulizana makabila?Hata unapoenda kununua kiwanja ujenge nyumba ,kweli ni nani anauliza kwanza ni eneo gani watu wa kabila lake wanaishi wengi?

Huu ni puuzi na umaamuma.Na kama utamaduni wa aina hii utapewa nafasi uote mizizi ,kwa sababu tayari umeishaanza kuchipua, ni wazi hatuwezi kuamisha vijiji vyetu tulikozaliwa huko mikoani tukaviamishia Dar es Salaam.

Nne; jinsia , baada ya miaka 15 ya vyama vingi bado taifa letu halijaweza kuimarisha uwiano wa kijinsia katika siasa za nchi. Kwa hiyo wanawake hawajapewa nafasi katika fikra za kisiasa kwa wa wananchi kuwa ni watu wanaostahili kuongoza kwa hiyo tumezidi kuimarisha mfumo wa Viti Maalum badala ya kuimarisha mafunzo ya kiungozi kwa wanawake ili waweze kuwa na ushindani uliobora katika Nyanja ya siasa.

Kwa hiyo japo kuwa wanawake wenzangu wamekuwa wakidai kwamba Viti Maalum viongezwe hadi kufikia asilimia 50; uwiano huo hautuakikishii sisi wanawake uwezo endelevu wa kiungozi.

Hivyo inabidi turejee suala hili kwa kudai mafunzo ya kiuongozi kwa wanawake yatolewe katika shule za msingi , sekondari na vyuoni ili kuwaandaa wawe washindani bora katika mfumo wa sasa wa siasa za ndani na nje ya nchi.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.
0716-774494


Chanzo:Gazeti la Tanzania la Jumapili, Novemba 15, mwaka 2010

MAHAKAMA YA KISUTU YALITUPA PINGAMIZI MURRO

Na Happiness Katabazi

HATIMAYE Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, ilitupilia mbali pingamizi la upande wa utetezi katika kesi ya kuomba rushwa ya sh mil. 10 inayomkabili aliyekuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Tanzania (TBC1), Jerry Murro na wafanyabiashara wawili.


Uamuzi huo ulitolewa jana na Hakimu Mkazi Gabriel Mirumbe, ambapo alisema baada ya kusikiliza malumbano ya kisheria yaliyoibuliwa na pande zote mbili juzi, amefikia uamuzi wa kutupilia mbali pingamizi za mawakili wa utetezi, Richard Rweyongeza, Majura Magafu na Pascal Kamala, waliotaka mahakama hiyo ikatae kupokea kielelezo cha pili cha upande wa Jamhuri, kwa sabababu pingamizi hilo halina hoja za msingi.

Juzi Wakili wa Rweyongeza aliwasilisha pingamizi la kutaka kielelezo hicho ambacho ni picha za CCTV zinazomuonyesha mshitakiwa wa kwanza, Murro, Deogratius Mugassa na aliyekuwa Mweka hazina wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Wage, wakiwa wanaingia na kutoka ndani ya Hoteli ya Sea Cliff, siku ya Januari 31 mwaka huu, saa 7:31 wakiingia katika hoteli hiyo na picha nyingine inaonyesha walitoka hotelini hapo saa 8:27 ya siku hiyo, kilichotolewa na shahidi wa pili wa upande wa mashitaka ambaye ni Meneja wa Teknolojia ya Mawasiliano wa Hoteli ya Sea Cliff, Pounama Kumar, kwa madai kwamba picha hizo ni kivuli na si halisi.

Hakimu Mirumbe, alisema amefikia uamuzi wa kukubalina na hoja za Wakili Kiongozi wa Serikali, Boniface aliyeiomba mahakama hiyo ipuuze pingamizi la utetezi, kwa madai kuwa kwa mujibu wa kifungu cha 40A cha Sheria ya Ushahidi ya mwaka 2002, kinairuhusu mahakama kupokea ushahidi wa kielektroniki, video na redio unaomhusu mshitakiwa na wala kifungu hicho hakiizuii mahakama kupokea ushahidi wa aina hiyo ambao ni kivuli au halisi.

“Mahakama hii inatupilia mbali pingamizi la upande wa utetezi na linakubaliana na hoja za upande wa jamhuri, kwa sababu ni za msingi na ni za kisheria, hivyo mahakama hii inapokea picha hizo za CCTV kama kielelezo cha pili kilichotolewa na upande wa Jamhuri na inaahirisha usikilizaji wa kesi hii hadi Januari 17,18 na 19 mwaka kesho,” alisema Hakimu Mkazi Mirumbe.

Katika shitaka la kwanza, watuhumiwa hao wanadaiwa kula njama kwa mujibu wa kifungu cha 32 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Novemba 13 mwaka 2010

MAHAKAMA KISUTU KUPOKEA VIELELEZO KESI YA MURRO

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, mjini Dar es Salaam, imesema leo itatoa uamuzi wa kupokea au kutopokea kielelezo cha pili kilichotolewa na upande wa Jamhuri jana katika kesi ya kuomba rushwa ya sh mil. 10 inayomkabili aliyekuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC1), Jerry Murro na wafanyabiashara wawili.


Hakimu Mkazi, Gabriel Mirumbe, alifikia uamuzi huo baada ya kuibuka malumbano makali ya kisheria baina ya pande hizo katika kesi hiyo. Upande wa utetezi unaowakilishwa na wakili wa kujitegemea, Richard Rweyongeza, Majura Magafu na Pascal Kamala na kuiomba mahakama isipokee picha za CCTV zilizotolewa mahakamani hapo, kama kielelezo na shahidi wa pili wa Jamhuri ambaye ni Meneja Teknolojia ya Mawasiliano wa Hoteli ya Sea Cliff, Apaumr, kwa madai picha hizo ni kivuli na si halisi .

Kwa upande wake Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, aliomba mahakama ipuuze pingamizi hilo la utetezi, kwa madai kuwa kwa mujibu wa kifungu cha 40A cha Sheria ya ushahidi ya mwaka 2002, kinairuhusu mahakama kupokea ushahidi wa kielektroniki, video, redio unaomhusu mshitakiwa na wala kifungu hicho hakiizuii mahakama kupokea ushahidi wa aina hiyo ambao ni kivuli au halisi.

Awali shahidi huyo wa pili kabla ya kutoa kielelezo hicho cha picha ya CCTV ambazo zinawaonyesha washitakiwa hao wakiwa kwenye Hoteli ya Sea Cliff, Januari 29, mwaka huu, kipokewe mahakamani kama kielelezo.

Akiongozwa kutoa ushahidi wake na wakili Kiongozi wa Serikali, Boniface, shahidi huyo alieleza kuwa Februali 2, mwaka huu, meneja mkuu ambaye ni bosi wake alimuita ofisini kwake akimtaka aongozane na maofisa watatu wa polisi waliokuwa wakiongozwa na Mkuu wa Upelelezi Kanda ya Dar es Salaam (ZDCO), Charles Mkumbo, awapeleke kwenye chumba maalumu cha kurekodi (CCTV) ili waweze kuangalia wageni waliofika kwenye hoteli hiyo siku ya Januari 28-31 mwaka huu.

Mbali na Murro, washitakiwa wengine ni Edmund Kapama na Deogratius Mugasa, ambao Februari 15 mwaka huu, walifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza wakikabiliwa na mashitaka matatu ya kula njama za kutaka kupokea rushwa kutoka kwa aliyekuwa Mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Karoli Wage. Kati ya mashitaka matatu yaliyofunguliwa dhidi yao, Murro anakabiliwa na mashitaka mawili.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Novemba 12 mwaka 2010

HEKO MAHALU,HEKO KORTI KUU

Happiness Katabazi

JUMATATU ya wiki hii, Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, iliandika historia mpya katika tasnia ya sheria nchini, baada ya kutoa hukumu iliyotamka bayana kuwa kifungu cha 36(4)(e) sura ya 200 cha Sheria ya Uhujumu Uchumi ya mwaka 2002, ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.


Sambamba na hiyo, mahakama hiyo ilitoa maelekezo kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ndani ya mwaka mmoja kuanzia siku hiyo awe amefanyia marekebisho kifungu hicho ama sivyo mahakama hiyo itakitamka kifungu hicho ni batili.

Kifungu hicho kilikuwa kinatamka kila mwenye kushitakiwa au kutuhumiwa kwa kosa la uhujumu uchumi ili apate dhamana ni lazima adhaminiwe kwa nusu ya kiwango anachotuhumiwa nacho.

Mfano, mtu mwenye kutuhumiwa kuiingiza hasara serikali ya sh bilioni 12 atatakiwa apatiwe au atoe dhamana ya sh bilioni sita, kinyume na hapo ataendelea kusota rumande.

Hukumu hiyo ya kesi ya kikatiba ya mwaka 2008, iliyofunguliwa mahakamani hapo na aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu, dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ilitolewa Oktoba 5, mwaka huu, saa nane mchana na jopo la majaji watatu.

Jopo hilo lilikuwa likiongozwa na Jaji Kiongozi, Fakhi Jundu, aliyekuwa akisaidiwa na Jaji Agustine Mwarija na Projest Rugazia, ambaye hakuwepo mahakamani hapo wakati hukumu hiyo ikisomwa.

Akisoma hukumu hiyo, Jaji Jundu alisema kimsingi Mahakama Kuu inakubaliana na hoja za mawakili wa mlalamikaji (Mahalu), aliyekuwa akitetewa na mawakili mahiri wa kujitegemea, Alex Mgongolwa na Cuthbert Tenga kwamba kifungu hicho cha 36 (4)(e) sura ya 200 cha Sheria ya Uhujumu Uchumi kinakwenda kinyume na Katiba ya nchi na kinaleta ubaguzi.

Alisema wanakubaliana na hoja za mawakili wa Mahalu, kwamba uwepo wa kifungu hicho unafanya mshitakiwa mwenye fedha ndiye apate dhamana na mshitakiwa ambaye hana fedha kutoweza kutimiza masharti hayo ya dhamana, hivyo kuishia kusota gerezani.

Hata hivyo, Jaji Jundu alisema kwa mujibu wa Ibara ya 30 (5) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mahakama Kuu inapoona kifungu chochote cha sheria kinakiuka ibara za Katiba, ina mamlaka ya kutoa maelekezo kwa Mwanasheria Mkuu kukifanyia marekebisho.

Hii ni kesi ya pili ya kikatiba kufunguliwa na wananchi katika mahakama hiyo hiyo dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na mwisho wa siku, wanashinda tangu serikali ya awamu ya nne iingie madarakani.

Kesi ya kikatiba ilifunguliwa na kituo cha Haki za Binadamu, ambapo pia kituo hicho kilikuwa kikitetewa na wakili Alex Mgongolwa waliomba mahakama hiyo itamke takrima katika uchaguzi ni rushwa.

Mwaka 2006 Mahakama Kuu ilikubaliana na hoja za wakili Mgongolwa ambapo ilitamka Takrima ni rushwa na ikamwagiza Mwanasheria Mkuu akafanyie marekebisho katika kifungu hicho kinachoruhusu takrima katika Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1985.

Mahalu, alilazimika kufungua kesi ya kikatiba Mahakama Kuu, ikiwa ni muda mfupi baada ya mwaka 2006, kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi ya sh bilioni tatu, ambapo hata hivyo kesi hiyo usikilizwaji wake unashindwa kuendelea katika mahakama hiyo kwa sababu jalada la msingi la kesi hiyo lipo katika Mahakama ya Rufani nchini.

Mahalu aliwasilisha ombi la kuiomba mahakama hiyo ya juu nchini ifanye mapitio ya uamuzi uliotolewa na aliyekuwa Jaji wa Mahakama Kuu (mstaafu), Juxon Mlai, ambaye alitupilia mbali ombi la Mahalu lililokuwa likiomba mahakama hiyo imuache huru kwasababu utaratibu wa kisheria haukufuatwa kabla ya yeye kufunguliwa kesi hiyo ya uhujumu uchumi.

Kwa mujibu wa maelezo hayo hapo juu, napenda kutoa pongezi zangu za dhati Profesa Mahalu kwa moyo wake wa ujasiri wa kufungua kesi hiyo tena kwa kutumia gharama zake kwa kuwaweka mawakili mahiri.

Nawapongeza mawakili hao kwa kazi nzuri ambayo iliweza kuwashawishi Jaji Kiongozi Fakhi Jundu na wenzake kukubaliana na hoja zao na mwisho wa siku wakatoa hukumu ambayo nalazimika kusema itawasaidia wananchi wengi ambao watapatwa na mabalaa ya kufunguliwa kesi za uhujumu uchumi .

Kwa wale wananchi ambao si waumini wa tasnia ya sheria au hawajawahi kufika mahakamani na kuona baadhi ya watu wanaokabiliwa na kesi za uhujumu uchumi na mahakama inapowatamkia washtakiwa wa kesi za aina hiyo kwamba ili wapate dhamana ni lazima watoe nusu ya kiasi cha fedha wanachotuhumiwa kuiba au kusababisha hasara, naamini itawawia vigumu kuona uzito, maana na faida ya hukumu hii.

Vyombo vingi vya habari havijaipa uzito wa kipekee hukumu hii, kama vyombo hivyo vilivyokuwa vizipata uzito wa kipekee hukumu ya rufaa ya mgombea binafsi au kesi ya mauaji ya watu wafanyabiashara wa nne iliyokuwa ikimkabili aliyekuwa mkuu wa upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi, Abdallah Zombe na wenzake na kesi za wizi wa akaunti ya madeni ya nje katika Benki Kuu (EPA). Na si vyombo vya habari peke yake pia jamii kwa ujumla na hizo taasisi zinazojinasibu kila kukicha kwamba ni taasisi za kiharakati za kutetea wanyonge na maskini.

Hili ni jambo la kusikitisha kama si la kushangaza kwani ndani ya jamii yetu hasa kwa sisi tunaotokea kwenye familia za kimaskini, kama si leo, basi kesho, mimi, wewe au mwingine tunaweza kujikuta mikononi mwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Eliezer Feleshi.

Tunaweza kuangukia katika mikono hiyo na baadaye kufikishwa mahakamani kwa kesi za uhujumu uchumi iwe tumetenda kweli kosa hilo au tumebambikiziwa kesi na mahakama italazimika kutumia kifungu hicho cha sheria ya uhujumu uchumi kwa ajili ya sisi maskini ndiyo tupate dhamana.

Nayaandika haya kwa hisia kali kwani kwa takriban miaka 11 sasa nimekuwa mwandishi wa habari za mahakamani hapa nchini, nimekuwa nikishuhudia wananchi wenzetu wakishindwa kumudu na kutimiza masharti ya dhamana kwa makosa ya uhujumu uchumi.

Watu hawa wamejikuta wanaozea magerezani miaka nenda miaka rudi wakati kesi zikiendelea kuunguruma, tena kwa kasi ya mwendo wa kinyonga kiasi kwamba zinachukua mpaka miaka minne hadi kutolewa uamuzi.

Msingi mmoja wapo wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, unapiga marufuku mtu yeyote kuchukuliwa kuwa na hatia mpaka pale mahakama itakapothibitisha kuwa mtu huyo ana hatia. Sasa kwa msingi huo wa Katiba ni dhahiri kifungu hicho cha 36(4) cha Sheria ya uhujumu uchumi ya mwaka 2002, kinapingana na msingi huo wa Katiba ambayo ndiyo sheria mama.

Wakati mwingine hukumu za washitakiwa hao zinapotoka mahakama inawaachilia huru washitakiwa hao kwasababu mahakama hiyo haijaletewa ushahidi unaojitosheleza.

Lakini vyovyote iwavyo, nadiriki kusema kuwa uwepo wa rushwa unatokana na mfumo wetu dhahifu katika masuala ya utoaji haki.Tuna matatizo makubwa kwa wale tuliowakabidhi majukumu ya kupambana na rushwa kwani baadhi yao watendaji wake wanakubali kutumiwa vibaya na wanasiasa wenye hulka za kinyang’au, kula rushwa na kisha kubambikia kesi watu wasio na hatia.

Watu hao wasio na hatia wakishaburuzwa mahakamani hujikuta wanabanwa na masharti ya kifungu hicho kilichotamkwa na Jaji Jundu na wenzake kuwa kinakwenda kinyume na Katiba ya nchini.

Ni hatari kwa sheria kumkabidhi binadamu yeyote mamlaka makubwa kiasi hicho. Leo na kesho itakapotokea kwamba mtu alifikishwa kortini na kuswekwa gerezani kwa kunyimwa dhamana kwasababu ya masharti ya kifungu hicho cha sheria ya uhujumu uchumi, na baadaye kubainika hana hatia, ana kuwa amedhalilishwa na kutopetezwa muda wake mwingi.

Kwa bahati mbaya, wengi wetu bado hatujajifunza thamani ya uhuru wa binadamu wenzetu.

Ni vyema sheria zetu zibadilishwe ili wale wanaoonekana mapema upande wa Jamhuri hauna sababu ya kuwafungulia mashtaka walipwe fidia kwa sababu thamani ya uhuru na heshima ya binadamu ni kubwa kuliko kiasi cha fedha chochote kinachohusika kwenye hizo kesi za uhujumu uchumi.

Kwenye tasnia ya sheria tunasema hivi ‘ni afadhali wahalifu tisa waachiliwe huru kuliko mtu mmoja asiye na hatia kuwekwa hatiani’.

Aidha, nimalizie kwa kumpongeza Profesa Costa Mahalu kwa uzalendo wake wa kufungua kesi hiyo na kisha kushinda, matunda ya hukumu hiyo si yake pekee, ni ya Watanzania wote watakaopatwa na matatizo ya kufunguliwa kesi za uhujumu uchumi.

Nina matumaini kuwa hukumu hii itawasaidia wanafunzi wa fani ya sheria vyuoni kwani watatumia hukumu hiyo kujibu maswali kweye mitihani, pia ni faida pia kwa majaji, mahakimu na mawakili ambao sasa watalazimika kutumia hukumu kama kielelezo cha kuunga mkono hoja zao za kisheria na kuitumia kutolea maamuzi katika kesi mbalimbali.

Hukumu hii iwe ni changamoto kwetu sisi waandishi wa habari hapa nchini kwani tumekuwa na kasumba ya kuinung’unikia sheria ya magazeti kuwa ni moja ya sheria mbaya lakini tunashindwa kupiga hatua moja mbele ya kutafuta mawakili watusaidie kufungua kesi ya kikatiba Mahakama Kuu, kutaka sheria hiyo ifanyiwe marekebisho.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Oktoba 10 mwaka 2010