HUKUMU KESI YA EPA KUSOMWA LEO

.MARANDA NA MWENZAKE KUCHEKA AU KULIA KISUTU
Na Happiness Katabazi

JOPO la Mahakimu Wakazi watatu leo linatarajia kuketi katika viti vitatu vya enzi ndani ya ukumbi namba mbili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam kumsomea hukumu Mweka Hazina wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Mkoa wa Kigoma, Rajabu Maranda (53) na mpwa wake Farijala Hussein ambao wanakabiliwa na kesi ya wizi wa Sh bilioni 1.8 katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania.

Jopo hilo linaloundwa na Mahakimu wakazi Saul Kinemela, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Focus Bambikya na Hakimu Mkuu Mfawidhi wa Mahakama ya Kisutu, Elvin Mgeta.

Washtakiwa hao ambao wanatetewa na wakili machachari Majura Magafu wanakabiliwa na kesi ya jinai Namba 1161/2008 kwa makosa ya kula njama,kuwasilisha nyaraka za uongo, za kughushi, wizi na kujipatia ingizo la Sh 1,864,949,294.45.

Katika shitaka hilo, washtakiwa hao wanadaiwa kuwasilisha nyaraka zilizoghushiwa Benki Kuu zilizoonyesha kampuni yao ya Kiloloma & Brothers ambayo hata hivyo haijawahi kusajiliwa kwa msajili wa makampuni nchini (BRELA), kwamba imepewa idhini na kudai deni la kampuni ya nje ya M/S BC Cars Export huku wakijua si kweli.

Wakati macho na masiko ya Watanzania yameelekezwa mahakamani hapo katika kesi hiyo itakayotolewa hukumu leo, pia kesi nyingine mbili zinazowakabili washtakiwa hao zitakuja mahakamani hapo kwaajili ya kuendelea kusikilizwa. Nyingine itakuja kwaajili ya upande wa jamhuri kuwasilisha majumuisho yao ya kumuona mshtakiwa huyo ana kesi ya kujibu.

Ikiwa hukumu hiyo itatolewa kama ilivyopangwa na jopo hilo Januari 26 mwaka huu, kesi hiyo ya jinai Na.1161/2008 itakuwa ni kesi ya kwanza kati ya jumla ya kesi 11 za wizi wa akaunti ya EPA kufunguliwa mahakamani hapo.

Kesi hizo zilifunguliwa na Mkurugenzi wa Mashtaka (DDP), Eliezer Feleshi kwa kishindo kuanzia Novemba 4 mwaka 2008 dhidi ya washtakiwa mbalimbali wakiwemo mfanyabiashara maarufu nchini Jayantkumar Chandubhai Patel ‘Jeetu Patel na wenzake na baadhi ya maofisa wa BoT ambao bado kesi zao zinaendelea kusikilizwa mahakamani hapo.

Mbali na kesi hiyo, Maranda na Farijala wanakabiliwa na kesi nyingine ya wizi wa Sh milioni 207 ambapo anashtakiwa yeye na maofisa wa BoT, Mkuu wa Idara ya EPA, Iman Mwakosya na Kaimu Mkurugenzi wa idara hiyo Ester Komu, na Katibu wa Benki Bosco Kimela.

Katika kesi hiyo ya wizi Maranda anadaiwa kutumia nyaraka za kughushi kuonyesha kampuni yake ya Rashaz Tanzania kuwa imepewa idhini ya kudai deni la kampuni ya Rashaz T Ltd na kisha kujipatia ingizo hilo la Sh milioni 207 huku akijua si kweli.

Kesi ya tatu ya jinai ni kesi Na. 1164/2008 ya wizi wa shilingi bilioni 3.8 katika akaunti hiyo ambayo inasikilizwa mbele ya jaji Beatrice Mutungi, Hakimu Mkazi Samwel Karua na Elvin Mugeta.

Katika kesi hiyo, washitakiwa Farijala, Maranda, Iman Mwakosya, Ester Komu, Ajay Somani na Sophia Lalika walitumia kampuni ya Mibale Farm kuonyesha imepewa idhini ya kudai deni la kampuni ya Lakshmi Textile Mills co. Limited ya India huku wakijua si kweli.

Juni 11 mwaka 2009, mahakama hiyo ilimuona Maranda na Farijala ambao wanakabiliwa na jumla ya kesi nne za wizi katika EPA, kuwa wana kesi ya kujibu na kwamba upande wa Jamhuri unaowakilishwa na Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka nchini, Stanslaus Boniface aliyekuwa anasaidiwa na Timon Vitalis, Frederick Manyanda, Ephery Cedrick na Michael Lwena na Oswald Tibabyekomya, umeweza kuthibitisha kesi yao.

Juni 6 mwaka 2009, Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka, Boniface aliwasilisha majumuisho ya kesi hiyo akiiomba mahakama hiyo iwaone washtakiwa wote hao wana kesi ya kujibu, kwani Jamhuri imeweza kuthibitisha kesi hiyo na kwa hiyo washtakiwa hao wana kila sababu ya kujibu kesi inayowakabili.

Aidha, Aprili 29 mwaka 2010, Rajabu Maranda alipanda kizimbani kutoa utetezi wake katika kesi hiyo ambayo leo inatolewa hukumu ambapo aliieleza mahakama hiyo kuwa alichokuwa akikizingatia katika mchakato wa kudai deni katika (EPA) ni kupata fedha na si kutazama nyaraka.

Itakumbukwa kuwa serikali kupitia Mkurugenzi wa Mashtaka (DDP) Feleshi iliwaburuza mahakamani watuhumiwa wa wizi katika akaunti ya EPA, baada ya tuhuma kuibuliwa na Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Ludovick Utoo, kelele za wananchi na wafadhili, hali iliyosababisha Rais Kikwete kuunda Tume ya uchunguzi wa wizi huo ambayo ilimshirikisha Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP-Said Mwema, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Dk. Edward Hosea na aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye kwa sasa amestaafu, Johnson Mwanyika.

Tume hiyo iliwahoji watuhumiwa na hatimaye kuwafikisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Aprili 29 mwaka 2011.

BALOZI MAHALU KUANZA KUJITETEA

Na Happiness Katabazi

HATIMAYE Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, umesema kwamba aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia,Profesa Costa Mahalu na Meneja Utawala wa Ubalozi huo Grace Martin wanaokabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi na wizi wa zaidi ya Euro milioni mbili wataanza kujitetea Mei 31 mwaka huu.


Amri hiyo imetolewa jana na Hakimu Mkuu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Ilvin Mugeta wakati kesi hiyo ilipokuja kwaajili ya kutajwa na kuangalia kama uongozi wa mahakama hiyo umeishampanga hakimu mpya wa kuendelea kusikiliza kesi hiyo kwasababu Machi 28 mwaka huu, Jaji Sivangilwa Mwangesi ambaye ndiye alikuwa akiisiliza kesi hiyo tangu awali kujitoa kwasababu mawakili wa washtakiwa waliwasilisha sababu sita kumtaka ajitoe kwasababu hawana imani naye kwani amekuwa akiendesha kesi hiyo kwa maslahi yake binafsi badala ya misingi ya kisheria.

“Tayari kesi hii imeshapangiwa hakimu wa kuendelea kuisikiliza na mimi (Mgeta) ndiye nimejipangia kusikiliza kesi hii na kwamba washtakiwa wataanza kujitetea Mei 31 na kesi hii itakuja kwaajili ya kutajwa Mei 18 mwaka huu… na mahakama hii imekubaliana na maombi ya Profesa Mahalu kwenda Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino jijini Mwanza kati ya Mei 12-22 na
Limekubali ombi la Grace la kwenye kijijini kwao mkoani Kilimanjaro kwa shughuli za kifamilia kuanzia Mei 4-15 mwaka huu”alisema Hakimu Mgeta.

Machi 28 mwaka huu, Jaji Sivangilwa Mwangesi alijitoa kuendelea kusikiliza kesi hiyo kufuatia sababu sita zilizowasilishwa mbele yake na jopo la mawakili wa utetezi linaoloongozwa na Mabere Marando, Alex Mgongolwa, Beatus Malima na Cuthbert Tenga Machi 25 mwaka huu, ambapo walimuomba jaji huyo ajitoe kwasababu hawana imani naye kwani amekuwa akiendesha kesi hiyo kwa malengo yake binafsi badala ya sheria.

Miongoni mwa sababu sita zilizowasilishwa na wakili Marando mbele ya Jaji Mwangesi siku hiyo ni kwamba upande wa utetezi ulishatoa mahakamani Kumbukumbu ya Bunge ‘Ansard’ ya Agosti 24 mwaka 2004 inayomnukuu aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa katika serikali ya awamu ya Tatu, Jakaya Kikwete akiliambia bunge kuwa taratibu za utafutaji, ununuaji wa jengo la ubalozi wa Tanzania ,Rome nchini Italia ulifuata taratibu zote za kisheria na kwamba fedha za ununuzi huo zilitumwa kwa awamu kwenye akaunti ya muuzaji na zilimfikia na kwamba hakukuwepo na wizi wowote lakini jaji huyo hakuzingatia ansard hiyo.

Sababu nyingine ya jaji huyo kukataliwa ni kwamba Jaji Mwangesi alipindisha kwa makusudi sheria ya Ushahidi ya mwaka 2002 na akaamua kuchukua ushahidi wa shahidi wa Jamhuri aliyekuwa nchini Italia kwa njia ya video wakati sheria hiyo ya ushahidi ya hapa nchini inakataza na kwamba ndiyo maana hivi sasa serikali ipo kwenye mchakato wa kupelekwa mswaada bungeni wa kuifanyia marekebisho sheria iliyopo hivi sasa,ili ushahidi kwa njia video(video conference) uweze kuruhusiwa na mahakama zetu.

Mapema mwaka 2006 ,Jamhuri kupitia mawakili wake toka Taasisi ya Kuzia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU), Ben Lincoln na Ponsian Lukosi iliwafikisha mahakamani hapo kwa mara ya kwanza washtakiwa hao kwa makosa ya uhujumu uchumi, wizi wa zaidi ya Euro milioni mbili wakati wakisimamiza ununuzi wa jengo la ubalozi mjini Rome nchini Italia.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Aprili 29 mwaka 2011.

DECI HAIKUWA NA JUKUMU LA KUKUSANYA FEDHA-SHAHIDI

Na Happiness Katabazi
NAIBU Msajili wa Wakala wa Usajili wa Makampuni(BRELA), Neol Shani ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa kampuni ya Deci Tz Ltd haikuwa na jukumu la kukusanya amana kwa watu na kuwarudishia kwa riba.


Shani ambaye tisa wa upande wa Jamhuri katika kesi ya kuendesha na kusimamia mradi wa upatu na kupokea amana za umma bila leseni inayowakabili wakurugenzi wa kampuni ya DECI Tz Ltd , alitoa maelezo hayo wakati akiongozwa na wakili wa serikali Prospa Mwangamila mbele ya Hakimu Mkazi Stewart Sanga kutoa ushahidi wake ambapo alidai kuwa yeye ndiye aliyeshughulia fomu za kuomba kampuni hiyo isajiliwe isajiliwe na yeye ndiyo aliyeidhinisha isajiliwe kama kampuni baada ya waombaji ambao ni washtakiwa kukidhi vigezo.

Shahidi ambaye ni mwanasheria kitaaluma alieleza pia kuifahamu kampuni ya kigeni ya Deci Africa Ltd yenye makao makuu nchini Kenya kwasababu ilileta maombi BRELA ya kutaka kufungua tawi lake hapa nchini na maombi hayo ya kampuni ya kigeni aliyashughulikia yeye na kwamba yalikuwa yamekidhi vigezo vyote na akaisajili na kuongeza kuwa kwa mujibu wa maombi hayo yanaonyesha wawakili wa kampuni hiyo ya kigeni hapa nchini wakili wa kujitegemea Alex Mgongolwa na Jackson Mtales.

Akihojiwa na wakili wa washtakiwa Hudson Ndusyepo kwamba majukumu ya kampuni ya kigeni ya Deci Africa Ltd ni yapi ,na ofisi za makampuni hayo zipo maeneo gani hapa nchini , shahidi huyo akajibu kuwa hayakumbuki hali iliyosababisha wakili Ndusyepo kumhoji kuwa yeye ni mwanasheria na alikuwa anafahamu jana alikuwa anakuja mahakamani kutoa ushahidi na kwamba ndiyo yeye aliyeshughulikia usajili wa makampuni hayo inakuwaje anashindwa kufahamu majukumu ya kampuni hizo na ofisi zake jambo ambalo shahidi huyo aliendelea kusisitiza kuwa anashughulikia maombi mengi ya usajili wa makampuni hivyo siyo rahisi kukumbuka majukumu ya kila kampuni.

Mwaka 2009, washtakiwa katika kesi hiyo ni Jackson Mtares, Dominic Kisendi, Timotheo ole Loitgimnye, Samuel Mtares, Arbogast Kipilimba na Samuel Mtalis,walifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza na Jamhuri ilidai kuwa washtakiwa wanamakosa ya kuendesha na kusimamia mradi wa upatu kinyume na sheria pamoja na kupokea amana za umma bila leseni na Na upande wa Jamhuri unawakiliwa na Mwanasheria wa Kanda ya Dar es Salaam, Justus Mulokozi na Prosper Mwangamila.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa Aprili 29 mwaka 2011.

KESI YA SAMAKI WA MAGUFULI YAPATA JAJI

Na Happiness Katabazi

HATIMAYE Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, umempanga Jaji Agustine Mwarija kuendelea usikiliza kesi ya uvuvi haramu katika Bahari ya Hindi Ukanda wa Tanzania inayowakabili raia 36 wa kigeni maarufu kama ‘kesi ya samaki wa Magufuli’.


Hatua ya kupangwa kwa jaji Mwarija kusikiliza kesi hiyo kunatokana na uamuzi uliotolewa Machi 3 mwaka huu, na Jaji Razia Sheikh wa kujitoa ambapo alisema anajitoa kusikiliza shauri hilo si kwasababu ya hoja zilizowasilishwa na wakili wa washtakiwa John Mapinduzi na Ibrahim Bendera kwamba hawana imani naye, bali anajitoa ili haki ionekane inatendeka na kwamba jalada la kesi hiyo analipeleka kwa Jaji Mfawidhi Semistocles Kaijage ili aweze kumpanga jaji mwingine.

Kwa mujibu wa hati ya wito ya mahakama hiyo inayoihalifu ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka(DPP),Eliezer Feleshi na mawakili wa utetezi , mahakama hiyo imezitaka pande hizo mbili kufika mahakamani Mei 5 mwaka huu, mbele ya jaji Mwarija ambapo kesi hiyo itakuja kwaajili ya kutajwa.

Akizungumza kwa njia ya simu na Tanzania Daima jana wakili wa washtakiwa John Mapinduzi alithibitisha kupokea wito huo na kwamba siku hiyo watafika mahakamani hapo bila kukosa wao pamoja na wateja wao.

Februali 25 mwaka huu, washtakiwa hao kupitia wakili wao Mapinduzi walimwomba jaji huyo ajitoe ikiwa ni saa chache tu baada ya jaji huyo kutoa uamuzi wa kuwanyima dhamana licha makosa yanayowakabili yanadhamana kwa mujibu wa Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 ila akasema kwa mazingira ya kesi hiyo mahakama hiyo imetumia mamlaka yake kuwanyima dhamana.

Machi 9 mwaka 2009 washtakiwa hao walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na makosa ya uvivu haramu katika kina kirefu cha habahari ya Hindi Ukanda ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuharibu mazingira ya ukanda huo.Hadi sasa washtakiwa wanaendelea kusota rumande kwa kukosa dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Aprili 28 mwaka 2011.

NNAUYE TAZAMA ULIPOTOKA,ULIPO NA UNAPOKWENDWA


Na Happiness Katabazi

“TEMBEA pole pole kama Kobe eeh… akinywa maji lazima ainuie kichwa juuu.” Hayo ni baadhi ya maneno yanayopatikana kwenye wimbo wa Kizimungala uliopo kwenye albamu ya ‘Dunia Kigeugeu’ ya bendi maarufu ya muziki wa dansi nchini ya FM Academia ‘Wazee wa Ngwasuma.’


Nimelazimika kutumia nukuu ya maneno hayo machache yanayopatikana kwenye kibao hicho cha Kizimungala kwa sababu naamini kabisa maneno hayo machache na mengine yatakayoendelea kwenye makala hii yanafikisha ujumbe uliomo katika makala hii.

Watanzania wote hususan wale wanaofuatilia mustakabali wa masuala ya kisiasa hapa nchini, watakumbuka hivi karibuni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete aliendesha vikao vya chama chake mjini Dodoma.

Wakati akiendesha vikao hivyo Rais Kikwete alitangaza kuivunja sekretarieti ya chama hicho kwa madai kuwa imeshindwa kumsaidia kazi tangu alipoiunda miaka michache iliyopita.

Waliokuwemo kwenye sekretarieti iliyovunjwa ni Katibu Mkuu, Yusuf Makamba, Katibu wa Uchumi na Fedha, Amos Makalla, Katibu wa Itikadi na Uenezi, John Chiligati, Naibu Katibu Mkuu, George Mkuchika na Mkuu wa Idara ya Mambo ya Nje , Bernad Membe.

Na alipoivunja aliwaacha wote na kumchukua John Chiligati kumpatia wadhifa wa Naibu Katibu Mkuu katika sekretalieti ya sasa, Katibu Mkuu ni Willson Mkama, Mkuu wa Idara ya Mambo ya Nje, Januari Makamba na Katibu wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi ni Nape Nnauye na Mweka Hazina ni Mchemba.

Hakuna ubishi tangu mwenyekiti wa chama hicho alipoiunda rasmi sekretarieti mpya, mara kwa mara tumekuwa tukimsikia Nnauye kwenye vyombo vya habari akinukuliwa akisema kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC ) kimetoa siku 90 kwa watuhumiwa wa ufisadi wajivue madaraka, chama kimezaliwa upya na kadhalika.

Kwa hakika kasi ya Nnauye ya kutoa matamko kwenye vyombo vya habari imekuwa kubwa ukilinganisha hata ile ya wajumbe wenzake wa Sekretarieti.

Binafsi naya fahamu majukumu ya Katibu Mwenezi kwenye vyama vyote vya siasa. Na nina fahamu uhuru wa mtu yeyote, akiwemo Nape mwenyewe kutoa maoni yake kama wanavyoruhusiwa na Ibara ya 18(a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Na moja ya kazi ya katibu mwenezi katika chama ni kuwa mshereheshaji katika mikutano ya hadhara ya chama husika.

Ninavyojua mimi chama chochote makini cha siasa uwa kinatoa ahadi kwa wananchi kuhusu jambo fulani kwamba kitatekeleza na kabla hakijatoa ahadi kwa umma au kwa wananchama wake ni lazima vikao husika vimeketi vimelipisha hilo na ahadi hiyo imeandikwa kwenye miniti za vikao husika.

Na si leo hii tunavyoona vioja vinavyofanywa na baadhi ya vyama vya siasa kusimama majukwaani kusema vitatekeleza hili na lile wakati hata kwenye ilani za uchaguzi wa vyama vyao hakuna na hata kwenye kumbukumbu za vikao vyao vya juu hakuna. Ni uhuni na uzandiki wa kupindukia.

Sasa kuhusu kasi ya Nnauye kuzungumza kwenye vyombo vya habari kwa kasi tena kwa kipindi hiki kifupi, sisi wachambuzi wa mambo tumeanza kujiuliza kichini chini hivi anafahamu kuwa yote anayoyazungumza kupitia vyombo vya habari wananchi wanayarekodi kwenye vitabu vyao vya kumbukumbu?

Na siku ikifika hayo anayoyasema yasipotekelezwa na chama chake, waananchi watawabana kwamba ni kwanini chama chake kimeshindwa kutekeleza yale yote anayoyasema kwenye vyombo vya habari hivi sasa?

Kama yote anayonukuliwa kwenye vyombo vya habari hivi sasa yapo kwenye rekodi za vikao vya chama hicho, basi mwisho wa siku hata kama hayatatekelezwa basi mwanasiasa huyo anaweza akasalimika kisiasa, ila kama hizo ahadi hazipo kwenye rekodi za vikao vya CCM, ila yeye kupitia wadhifa wake ameamua kuyazungumza kwa kuwa chama kimezaliwa upya, basi wakati ukifika wanachama wa CCM watamfuata kutokana na matamko yake ambayo hayakuwa yametekelezeka.

Mabadiliko ya uongozi wa juu wa chama hicho yaliyofanywa na Mwenyekiti wa chama hicho na matamko ya Nape kwenye vyombo vya habari yamebadilisha upepo mbaya uliokuwa ukivuma ndani ya chama hicho.

Chama hicho kilikuwa kikiandamwa na wakosoaji wa masuala ya kisiasa kwamba ni chama kilichozeekana na kimekosa dira na kwamba baadhi ya viongozi wake wamefilisika kisiasa.

Na wakati wote tuhuma hizo zimekuwa zikirushiwa chama hicho chenye makada wake ambao wana mafunzo na mbinu za kila aina za kuweza kukabiliana na mikikimiki ya wapinzani wake, lakini kwa kipindi chote hicho chama hicho kilishindwa kujipanga vema na kuweza kujisahihisha hadi heshima yake kuporomoka mbele ya jamii.

Ila siwezi kusema moja kwa moja chanzo cha kuporomoka kwa heshima ya chama hicho chanzo ni sekretarieti iliyopita.

Hata baadhi ya wanachama na viongozi wa CCM ngazi ya matawi, kata, wilaya na mikoa nao walikuwa chanzo kikubwa cha tatizo hilo kwani baadhi ya matendo yao, uzalendo wao kwa wananchi wenzao na wale wafuasi wa vyama vingine ulikuwa ukilalamikiwa kila kukicha.

Sasa kuhusu Nape, akumbuke kipindi kile alichokuwa akiungurumisha kile alichokiita ni ufisadi katika upangishwaji wa jengo la UVCCM kwa mwekezaji, ambapo alidai kuna ufisadi katika upangishwaji wa jengo hilo na matokeo ya madai yale aliyapata kutoka katika vikao vya UVCCM.

Kwa hiyo basi hana budi kutazama alikotoka, alipo na anakokwenda. Ningefarijika kukuona Nnauye unatumia muda mwingi kubuni mbinu thabiti ya kukinadi chama na hiyo idara yako kujipanga upya kwa kuandika maombi ya fedha kwa mweka hazina wenu za kuandaa mafunzo au semina hata ya wiki moja ya makatibu wenezi wa mikoa yote na wilaya maana wewe ni ndiye kiongozi wao ukawaeleza umejipanga vipi na wewe unataka wafanye nini na waache kipi ili mwendelee kukijenga chama chenu, badala yake karibu kila kukicha tunakusikia kwenye vyombo vya habari ukitueleza yale yale mliyoyajadili kwenye chama ya kujivua gamba.
Nilitegemea Nnauye sasa hivi uwe unaumiza kichwa kwa kubuni mkakati ule wa chama chenu mliouasisi miaka ya nyuma ya kuwa na chipukizi wengi kutoka mikoani na kwenda kuimarisha matawi ya chama chenu kwenye vyuo vikuu sambamba na kujenga nguvu za hoja zitakazowashawishi wana vyuo vikuu ambao wamekitema chama chenu na kujiunga kwa wingi na Chadema.

Nilitegemea Nnauye na UVCCM sasa hivi na nyie mngeanzisha mitandao mbalimbali na kuanza kukinadi chama na kuonyesha kwa miaka sita hii ya utawala wa Rais Kikwete amefanya nini, ameshindwa wapi na ana kusudia kufanya nini kwa mujibu wa ilani ya uchaguzi ya mwaka 2010?

Wakati mwingine huwa najiuliza, hivi hiyo mishahara na posho wanayopewa na chama pamoja na kutanua na magari ya kifahari kila kukicha na matokeo yake wanashindwa kukitetea chama kwa yale mazuri waliyofanya na kuweka bayana udhahifu ili kesho na kesho kutwa wasirudie udhahifu huo, wanalipwa za nini?

Matokeo yake hivi sasa tumekuwa tukiona nguvu ya vijana wa chama hicho ikitumika kwa nguvu zote nyakati za uchaguzi wa ndani wa chama hicho.

Hii ni kasumba ambayo ndiyo sasa inaanza kuwatafuna vijana wengi wa nchi ambao hata wengine hawana hadhi ya kuwa viongozi lakini wanajitumbukiza kwenye ulingo wa siasa kwa lengo moja tu la kupata madaraka harakaharaka na si kuvitumikia vyama vyao na taifa kwa ujumla.

Ikiwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) si chama tawala na hakina ruzuku kubwa kama CCM, kwa kipindi kifupi tu kimeweza kuwa na viongozi vijana hata ndani ya vyuo vikuu wenye uthubutu wa kulisimamia lile wanaloliamini, inakuwaje CCM vijana wake wawe goigoi na wawe mabingwa wa kutoa matamko wakati wa chaguzi za ndani zinapofika?

Binafsi nilishawahi kuandika makala zaidi ya nane huko nyuma kuitahadhalisha CCM ijitazame upya na isome alama za nyakati kwamba Watanzania wa sasa si wa jana na kweli hivi karibuni chama hicho kikaamua kukikiri kwamba tuhuma za ufisadi zimekiathiri, lakini kukiri tu hakutoshi tunataka kama kweli kuna wanachama wake wana tuhuma za aina hiyo basi wafikishwe kwenye vyombo vya dola kama wengine licha ya kuwa hayo ni maamuzi ya chama chenyewe na sisi watu wa nje hatupaswi kuyaingilia.

Tungali tukikumbuka Nyerere Foundation miaka miwili iliyopita ilifanya mdahalo wake pale ukumbi wa Karimjee na washiriki ambao wengi walishawahi kushika nyadhifa za juu serikalini waliikosoa wazi wazi serikali na kusema kwamba inakabiliwa na tuhuma za ufisadi.

Lakini kwa kuwa siku hazigandi, Aprili mwaka huu, kwenye kikao cha NEC Rais Kikwete na wajumbe wa mkutano huo walikiri wazi wazi kwamba upepo wa kisiasa dhidi ya chama chao ni mbaya sana, kwani tuhuma za ufisadi zinazowakabili viongozi wake nazo zimechangia chama hicho kupatwa na msukosuko wa kisiasa na hivyo kuwataka wanachama wanaokabiliwa na tuhuma hizo wajivue madaraka.

Sasa tuwahoji wale makada wote waliojitokeza kuwakebehi kina Jaji Joseph Warioba, Joseph Butiku kuwa ni wazi, leo hii wanaziweka wapi sura zao? Maana mwenyekiti wao amekiri kashfa za ufisadi zimekipaka matope chama chao.

Kwa hiyo nimalizie kwa kumuasa Nnauye kwamba cheo ni dhamana, asikubali kutumika kuwaumiza wenzie na kwamba kuna msemo usemao: “Yaliyomkuta mamba na kiboko yatamkuta” kwa sababu wote wanaishi majini.

Hivyo yaliyoikuta Sekretarieti na Kamati Kuu iliyopita mwisho wa siku yanaweza kuikuta hata sekretatieti ya sasa, kwani tungali tukikumbuka mwaka 2006 aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Benjamin Mkapa alistaafu wadhifa huo kabla ya muda wake kule Dodoma na akamkabidhi kiti Rais Kikwete, ambaye dakika chache baada ya kukabidhiwa kiti aliichagua sekretarieti mpya ambayo iliundwa na Katibu Mkuu, Yusuf Makamba, Naibu Katibu Mkuu, Jaka Mwambi, Mweka Hazina, Rostam Aziz, Mambo ya Nje, Dk. Asha-Rose Migiro, hivyo kuiacha sekretarieti ya Mkapa ambayo Katibu Mkuu alikuwa Philip Mangula, Naibu Katibu Brigedia Jenerali Hassan Ngwilizi, Katibu wa Itikadi na Uenezi , Omar Ramadhani Mapuli na Mweka hazina marehemu Salome Mbatia.

Sote tunamkumbuka aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM, Philip Mangula, enzi za Mkapa. Mangula alikuwa si aina ya kiongozi wa kupayuka payuka na kuzungumza ovyo ovyo na vyombo vya habari kama alivyokuwa Yusuf Makamba.

Tuliokuwa kwenye fani ya uandishi wa habari enzi zake ni mashahidi kwamba siku CCM ikitoa mwaliko kwa vyombo vya habari kwamba Katibu wake Mangula siku fulani atazungumza na waandishi wa habari, basi wahariri ndani ya vyumba vya habari nao hujipanga kwa kumwandaa mhariri au mwandishi mwandamizi makini ambaye pia wanamwandaa na kumpatia maswali ya kumuuliza katibu mkuu huyo. Na katika hili tutabaki tukimkumbuka Mangula.

Na kama Nnauye asipokuwa makini na kuikwepa sifa hiyo mbele ya safari itakuja kumghalimu.

Kwa mifano hai hiyo, Nape unapaswa uzifahamu vyema siasa za chama chako zikoje kwamba ni za kupanda na kushuka, tena wakati mwingine unashuka kwa ajili ya mizengwe na uzushi na matamanio ya kisiasa ya wakati huo, kuliko hali halisi au kutibu tatizo.

Hivyo Nnauye , January na Mchemba mtambue bado mna maisha marefu kwenye ulingo wa siasa hapa nchini, kama mtapenda hivyo ni vyema mjiepushe kujiingiza au kuingizwa kwenye magomvi binafsi na wakubwa wenu ambayo yamepewa misamiati ya kila aina.

Watanzania na wanachama wa chama chako wanataka kuona una fanyakazi kwa vitendo na si maneno majukwaani na kwenye vyombo vya habari.

Kama kweli NEC iliazimia viongozi hao wajivue nyadhifa zao na azimio hilo likaandikwa kwenye kumbukumbu za kikao hicho, basi ni wakati mwafaka sasa wananchi kusubiri hizo siku 90 zifike tuone kama kweli watu hao watakuwa wameishajivua madaraka na hilo likishindikana, basi Nape na viongozi wenzake wa chama chake tutawaweka kwenye kapu lilelile la viongozi wanaopenda kusema majukwaani, lakini utendaji ni sifuri.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Aprili 26 mwaka 2011.

KWANINI WANAHABARI TUZUIE KURIPOTI KESI HII?


Na Happiness Katabazi
IJUMAA ya wiki iliyopita Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, Elvin Mugeta alitoa amri ya kushangaza iliyovipiga marufuku vyombo vya habari nchini kuripoti mwenendo wa kesi ya madai Na.85/2009 ya kashfa ya shilingi moja iliyofunguliwa mahakamani hapo na Mfanyabishara Yusuf Manji dhidi ya Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi na ITV.


Mapema mwaka 2009, Manji anayetetewa na mawakili maarufu nchini, Mabere Marando, Richard Rweyongeza, Dk.Ringo Tenga na Beatus Malima alimfungulia kesi ya madai ya kashfa Mengi na kituo cha televisheni cha ITV akitaka amlipe fidia ya shilingi moja kwa madai kuwa Mengi alitumia televisheni yake hiyo kumkashfu kwa kumuita ‘Fisadi Papa’ na kwamba mmoja wa watu wanaopora rasilimali za Tanzania.

Maelekezo hayo ambayo yalitushtua baadhi ya waandishi wa habari za mahakamani waliokuwa ndani ya chumba hivyo, yalitolewa na Hakimu Mgeta ambapo siku hiyo kesi ilikuja kwaajili ya kutajwa.Mshangao huo uliotukumba wanahabari ulisababisha baada ya hakimu huyo kutoka mahakamani kumfuata ofisini kwake ili aweze kutufafanulia kwa mapana hayo maelekezo yake na kweli hakimu huyo alitufafanulia.

“Naomba mnisikilize kwa makini na utulivu kabisa na nitaongeza sauti ili muweze kunisikia vizuri licha kuna kelele za mafundi ujenzi ...maelekezo hayo ni kama yafuatavyo ni kwamba kuanzia sasa vyombo vya habari yaani magazeti na vile vya electroniki havitaruhusiwa kuripoti mwenendo wa kesi hii kwasababu kufanya hivyo kuna athiri uhuru wa hakimu na mahakama na sababu za maelekezo hayo hatuna sababu ya kuzitaja adharani kwani imefika mahala mahakama ya kisutu haipumui.

Kwa wale wananchi waliokuwa wakifuatilia kesi hii, watakumbuka kuwa Aprili 8 mwaka huu, Hakimu Mkazi , Alocye Katemana alitangaza kujitoa kuendelea kusikiliza kesi hiyo na kusema kuwa hawezi kutaja sababu za kujitoa kwa umma.

Katemana alitoa uamuzi huo ikiwa ni mara ya kwanza siku hiyo tangu jalada la kesi hiyo lilipotoka kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Semistocles Kaijage Machi 29 mwaka huu ambaye aliamuru jalada la kesi hiyo lirudishwe Mahakama ya Kisutu kwa hakimu Katemana ambaye ndiye amekuwa akisikiliza kesi hiyo kwaajili ya kuendelea kusikilizwa.

Jalada la kesi hiyo ambayo lilitua katika Mahakama Kuu Mwishoni mwa mwezi Machi mwaka huu, likitokea Mahakama ya Kisutu kutokana na barua ya Februali 23 mwaka huu, iliyoandikwa na wakili wa mdaiwa(Mengi) , Michael Ngaro kwa Jaji Mfawidhi Kaijage ambapo ndani ya barua hiyo Ngaro alimuomba jaji huyo apitie mwenendo mzima wa kesi.


Uamuzi wa Hakimu Katemana wa kujitoa, kulikuja siku mbili baada ya mdaiwa katika kesi hiyo Mengi kufanya mkutano na waandishi wa habari na kulalamikia baadhi ya vichwa vya habari vilivyotokana na habari inayohusu kesi hiyo sambamba na kutoa matangazo katika magazeti kadhaa ambapo ndani ya matangazo hayo alilikuwa akilalamikia baadhi ya magazeti yanavyoripoti kesi hiyo na mambo mengine.

Februali 15 mwaka huu, Hakimu Katemana alitupilia mbali ombi la Mengi lililotaka mahakama hiyo iwapatie nakala ya uamuzi iliyotolewa na hakimu huyo Februali 11 mwaka huu,ambapo hakimu huyu alikazikataa nyaraka vivuli 14 zikiwemo nyaraka ambazo zinaonyesha ni mali ya TAKUKURU,Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na mkataba wa kukopeshana fedha baina ya kampuni ya Kagoda Agriculture Ltd na Kampuni ya Quality Finance Corporation Ltd , ili aweze kwenda Mahakama Kuu kuomba ufanyiwe mapitio kwa sababu Sheria ya Mabadiliko ya Kanuni ambazo Na. 25 ya mwaka 2002, zinakataza upande wowote katika kesi yoyote kwenda mahakama ya juu kupinga amri za muda zinazotolewa na ya chini .

Kwa muktadha huo hapo juu binafsi nimeshangazwa ana amri hiyo licha nafahamu fika kuwa mahakama inaweza kutoa amri kadhaa kwenye masuala kadha wa kadha kwasababu mahakama zetu zimepewa nguvu ya kipekee(discretion Power) ambazo si lazima ziwe zimeanishwa kwenye vitabu vya sheria.Na ndiyo maaana hakimu huyo wakati akitoa maelekezo hayo hakunukuu kifungu chochote cha sheria.

Maelekezo hayo ambayo hayakutaja wazi sababu za kutuzuia kuripoti kesi hiyo siyo tu yamenyima haki vyombo vya habari ya kuchapisha habari ya kesi hiyo pia unanyima umma wa watanzania kufahamu kinaochendelea kwenye kesi hiyo ambayo hadi sasa ni shahidi mmoja tu (Manji) ambaye ndiye ametoa utetezi wake.

Ieleweke kwamba makala hii haina lengo la kuidharau au kuipinga amri hiyo la hasha kwani mwandishi wa safu hii ana heshimu uhuru wa mahakama na utawala wa sheria.Ila katika akili yake amekuwa akijiuliza Je ni kwanini Hakimu Mgeta kabla ya kutoa amri hiyo ambayo inaacha maswali mengi kuliko majibu hakueleza bayana sababu za kufikia uamuzi huo?

Uenda uamuzi huo umetokana na baadhi ya sisi waandishi waandishi wa habari za mahakamani tumeripoti kinyume ,lakini kama hivyo ndivyo,Je ni kwanini hakimu huyo asingeona haja ya kabla ya kufikia uamuzi huo wa kushtusha angewaita wahariri na waandishi waliondika visivyo kuwahoji,kutuelekeza tumekosoa wapi ili kesho tusirudie makosa hayo?

Fukuto la Jamii kila siku linaamini mahakama ni kama shule ambapo kwa wananchi wanaofuatilia mashauri mbalimbali upata fursa ya kujifunza vitu vipya vya kisheria kila siku, sasa Hakimu Mgeta haoni amri yake hiyo kwa njia moja ama nyingine inanyima fursa ya wananchi kujifunza kupitia kesi hiyo matajiri wawili yaani Manji anamtaka Mengi amlipe shilingi moja ili hali Manji amekodi mawakili maarufu nchini wamtetee?

Mgeta alisema eti kesi hiyo imeripotiwa sana na vyombo vya habari.Binafsi uwa sipendi unafki na katika hili sitamung’unya maneno hoja ya kesi hiyo minaiita ni hoja mfu,isiyo na mantiki ya kisheria na haina ukweli wowote kwani Watanzania wote wakiwemo mabosi wake Mgeta ni mashahidi kwamba hakuna kesi iliyoandikwa sana tena kwa miaka miaka minne mfululizo kama kesi ya Mauji ya watu wanne iliyokuwa ikimkabili , ACP-Abdallah Zombe na wenzake, kesi za EPA, kesi za matumuzi mabaya ya ofisi za umma iliyokuwa ikimkabili Amatus Liyumba,Profesa Costa Mahalu, Bazir Mramba na wenzake.

Sote tungali tukikumbuka jinsi ya vyombo vingi vya habari vilivyokuwa vikiripoti kesi ya Zombe kishabiki na upotoshaji wa hali ya juu hali iliyosababisha kabla ya hata Jaji wa Mahakama ya Rufaa Salum Massati kutoa hukumu yake Agosti 17 mwaka 2009, tayari umma na vyombo hivyo vya habari vilikuwa vimeishamhukumu Zombe kuwa ni muaji na anastahili adhabu ya kunyongwa na kamba hadi kufa.

Na siku zote hizo hatukuusikia mhimili wa mahakama ukitokeza adharani kukemea vyombo vya habari wala kuvizuia na wala hatukumsikia Jaji Massati akikemea hali hiyo zaidi jaji huyo alikuwa akivumilia vituko vyote vilivyokuwa vikitendeka ndani na nje ya mahakama hadi mwisho wa siku alivyokuja kutoa hukumu yake ya kushtusha ambapo aliwaachiria huru washtakiwa wote kwani alibaini ushahidi uliotolewa na jamhuri ulikuwa ni dhaifu.

Na wakati yote hayo yakitendeka Hakimu Mgeta alikuwa yumo ndani ya mhimili wa mahakama, tumuulize je alishawahi kutoa maoni kwa wakubwa zake wavizuie vyombo vya habari visiripoti kesi hiyo?

Kwa kuwa Hakimu Mgeta amevipiga marufuku vyombo vya electroniki na magazeti, tumuulize je wale waandishi wanaotafuta habari na kutawanya kwenye mitandao ‘on line’ kama Jamii Forum, blogg nao hawataruhusiwa kuripoti ushahidi wa kesi hiyo?

Mbona baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti kesi ya mauji ya mtoto Salome Yohana inayomkabili Ramadhani Mussa na mama yake na vyombo hivyo vilikuwa havimtendei haki mtoto huyo vinamuita ‘Rama Mla watu”,iliyofunguliwa mahakama ya Kisutu kabla ya kuamishiwa Mahakama Kuu, mbona hatujakusikia ukitoa amri kama hiyo?.Maana maandishi hayo yalikuwa yameishamhukumu Ramadhani kuwa anakula vichwa vya watu wakati bado kesi yake haijatolewa hukumu.?

Kwa watu kama sisi tunaofikiri sawa sawa , tuna hoji ni kwanini Hakimu Mgeta ambaye hajabainisha wazi kwamba yeye ndiye atasikiliza kesi hiyo au atampanga hakimu mwingine, ni kwanini amekuwa mwepesi mno kutoa amri hiyo na mbona kuna kesi nzito zinazohusiha waliokuwa vigogo wa serikali, watuhumiwa wa ujambazi wanaokabiliwa na kesi za unyang’anyi wa kutumia silaha,rushwa ya ngono,kesi za ndoa ambazo baadhi mashahidi wamekuwa wakitoa ushahidi ambao unafichua mbinu za kipelelezi zilizotumiwa na makachero ‘manusanusa,machatu’ wetu kuwakamata wahalifu lakini hatujamsikia hakimu huyo akitoa maelekezo kuzuia tusiripoti ?

Kwani siyo siri ushahidi unotolewaga na baadhi ya wapelelezi unakuwa mbinu na mikakati inayotumiwa na ‘manusanusa’ wetu kuwakamata wahalifu hivyo ushahidi huo unakuwa unatoa faida kwa wahalifu ambao hawajatiwa nguvuni kuwakwepa ‘manusanusa’.?

Mbona mabosi wako kule Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa hawajawi kutupiga marufu kuripoti kesi wanazoziendesha?Maana kesi nzito kama za mauji, kesi mgombea binafsi,kesi ya ubakaji inayomkabili mwana muziki nguli wa dansi, Nguza Vicking ‘Babu Seya na Papi Kocha,kesi ya kusajiliwa tuzo ya kampuni ya Dowans dhidi ya Tanesco,kesi ya madai dhidi ya Dk.Wilbroad Slaa ya kudaiwa kuiba mke wa mtu,kesi za kupinga matokeo ya uchaguzi wa mwaka 2010,kesi wizi wa samaki wa Magufuli’zimekuwa zikiendeshwa huko na kuudhuliwa na mamia ya wananchi ukitofautisha na kesi hiyo ya manji na mengi ambayo uudhuliwa na watu wachache sana.

Wanahabari tumebaki tukijiuliza kuhusu uamuzi huo kwamba uenda hakimu huyo amepata taarifa za Kiintelijensi kwamba kuripotiwa kesi hiyo kutaatarisha usalama wa wafanyabiashara hao na taifa?.

Hatukusikia uongozi wa mahakama nchini ukitoa maelekezo ya kuvikataza vyombo vya habari kutoripoti kesi, zaidi zaidi sisi waandishi wa habari za mahakama tumekuwa tukishuhudia mawakili wa washtakiwa wenyewe pindi wanapoona baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti uongo, wamekuwa wakifika na magezeti hayo mahakamani na kuiomba mahakama iyaonye magazeti hayo na ndiyo maana amri hiyo ya mahakama imetushangaza sana kwani ni mpya.

Siyo siri tena kwamba tumeanza kupatwa na wasiwasi kuwa huko mbele ya safari baadhi ya mahakimu wetu ambao siyo waadilifu wanaweza wakatumia gia kama ya hakimu Mgeta ambaye sisemi siyo mhadilifu kuvizuia vyombo vya habari visiripoti kesi nyingine ambazo zinafuatiliwa hatua kwa hatua na jamii ambazo zinaonekana kumuelemea mlalamikaji au mdaiwa ambao wana ukaribu nao.

Fukuto la Jamii linasisitiza kuwa lina heshimu uhuru wa mahakama ila amri ya hakimu Mgeta imetuachia maswali mengi kuliko majibu.Na amri hiyo inataka kufanana na amri ‘shindwa’ iliyowahi kutolewa na mtangulizi wako Addy Lyamuya ,Februali mwaka juzi, siku ya kwanza kabisa kesi ya wizi wa Sh bilioni 1.8 katika akaunti ya EPA inayomkabili Kada wa CCM, Rajabu Maranda na Farijara Hussein ilipoanza kusikilizwa rasmi kuwataka waandishi wa habari waweke peni chini eti si kila mtu anaruhusiwa kuripoti kesi.

Lyamuya alitoa amri hiyo ambayo ni amri ‘kihoja’ ambayo ilisababisha waandishi wa habari kuchachamaa na kesho yake asubuhi alimtuma karani wake kuwaita waandishi wahabari ofisini kwake bila ya kutoa ufafanuzi wowote akasema hataki malumbano akasema ni lazima kila siku tujiandikishe majina kabla ya kuingia mahakamani utaratibu ambao halishindwa kuusimamia hadi anastaafu kwani mimi , Grace Michale wa Majira na Faustine Kapama wa Dailnews kwa kauli moja tulimweleza utaratibu wake utatuwia vigumu kuutekeleza na kweli utaratibu huo ulikufa ndani ya siku mbili.

Tunamuomba Mgeta kufikiria upya amri yake.Pia tunamuomba Jaji Mkuu Chande Othman, Jaji Kiongozi Fakhi Jundu,Jaji Mfawidhi Semistocles Kaijage na Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,Amir Msumi kuutazama upya amri ya hakimu huyo kwani wakae wakijua siku hizi hakuna siri hapa nchini, sisi waandishi wachokonozi ambao tunaouwezo mkubwa tu wa kutafuta kilichomsukuma hakimu huyo kutoa maelekezo hayo na hatimaye tutakianika na mwisho wa siku itayochafuka ni mhimili mzima wa mahakama na siyo hakimu huyo.

Ieleweke kuwa tangu amri hiyo itolewe tayari mitaani baadhi ya wananchi wameanza kuwa na fikra mbaya kuhusu amri hiyo.Ila tunavyoifahamu mahakama yetu ni mahakama isiyona ubaguzi wakati wakuzishughulikia kesi mbali mbalimbali.Kesi zinazowahusu watoto chini ya umri wa miaka 18 kwa mujibu wa sheria vyombo vya habari haviruhusiwi kuziripoti lakini tunashangwazwa kesi hii ambayo ni ya madai y ash moja ambayo hata serikali yake haijashtaki au kushtakiwa mahakama ya Kisutu kwa nguvu ilizonazo imeamua kuingilia kati na kutupiga marufuku tusiripoti ushahidi utakaotolewa mahakamani.Inashangaza sana.

Namalizia kwa kujiuliza tena na tena hivi ni kwanini Hakimu Mgeta atupige marufuku kuripoti ushahidi wa kesi ya Manji na Mengi tu?Mahakama ya Kisutu ina nini katika kesi hiyo ya madai ya shilingi moja hadi kufikia uamuzi wa kutoa amri hiyo ambayo ni ngeni kutolewa na mahakama zetu hapa nchini?Hivi kesi hii ina unyeti gani ? Wakati ukifika tutakuja kujua chanzo cha kutolewa maelekezo hayo nini. Naomba kutoa hoja.
Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Aprili 19 mwaka 2011.

NG'UMBI AAMRILIWA KULIPA MIL 9/-

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imemwamuru imemwamuru aliyekuwa mgombea ubunge wa Jimbo la Ubungo (CCM), Hawa Ng’umbi kulipa jumla ya Shilingi milioni tisa ndani ya 14 kuanzia jana fedha ambazo ni dhamana ya kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ambayo yalimtangaza John Mnyika (Chadema) kuwa mbunge wa jimbo hilo .


Mbali na Mnyika , Ng’umbi ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Bukombe katika kesi hiyo anamshtaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali na aliyekuwa Msimamizi wa Uchaguzi wa jimbo hilo ambapo Mnyika anatetewa na wakili wa kujitegemea, Edson Mbogoro. Ng’umbi ambaye anatetewa wakili Issa Maige alifungua kesi hiyo Na. 107/2010 Machi 22 mwaka huu, akitaka mahakama hiyo itengue ushindi wa Mnyika kwa sababu sheria ya uchaguzi ilikiukwa.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Jaji Upendo Msuya ambapo alisema alisikiliza kwa makini ombi la mlalamikaji(Ng’umbi) la kutaka apunguziwe kiwango cha kulipa dhamana ya kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2002 inamtaka mlalamikaji alipe sh milioni tano kwa kila anamshtaki na kwamba alisikiliza hoja za mawakili wa wadaiwa zilizowasilishwa na Mbogoro ambazo zilitaka ombi la mlalamikaji litupwe kwasababu mlalamikaji ni mkuu wa wilaya na ana uwezo wa kifedha wa kuweza kulipa sh milioni 15 na kwamba mlalamikaji hakutoa vielelezo vinavyoonyesha yeye hana uwezo wa kulipa shilingi milioni 15.

Jaji Msuya alisema baada ya kupitia hoja za pande zote mbili amebaini kuwa Ng’umbi ameshindwa kuleta vielelezo vinavyoonyesha kuwa hana uwezo wa kiuchumi ambao haumruhusu kulipa dhamana ya shilingi milioni 15 hivyo mahakamana hiyo inamwamuru kulipa shilingi milioni tatu kwa kila mdaiwa ambayo jumla yake ni shilingi milioni tisa badala ya milioni 15 na kwamba fedha hizo anapaswa awe ameziliwakilisha mahakamani hapo ndani ya siku 14 kuanzia jana.

“Ng’umbi ameshindwa kuleta vielelezo vinavyounga mkono ombi lake la kutaka apunguziwe dhamana ya shilingi milioni 15 na kwa maana hiyo mahakama hii inamwamuru mlalamikaji huyo alipe shilingi milioni tatu kwa kila mdaiwa na fedha hizo anatakiwa azilipe ndani ya siku 14 kuanzia leo(jana) kama Sheria ya Uchaguzi ya Taifa ya mwaka 2002 inavyotaka.”alisema Jaji Msuya.

Aprili nane mwaka huu,Wakili wa Ng’umbi, Issa Maige, aliiomba mahakama hiyo impunguzie kulipa jumla ya shilingi milioni 15 ambapo kwa upande wake wakili wa wadaiwa Mbogoro na wakili wa serikali Sehel, waliomba mahakama hiyo itupilie mbali ombi hilo kwa sababu mlalamikaji anajiweza kiuchumi, hivyo ana uwezo wa kulipa kiasi hicho cha fedha kama sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2002 inavyomtaka.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Aprili 19 mwaka 2011.

WAANDISHI WAPIGWA MARUFUKU KESI YA MANJI,MENGI


Na Happiness Katabazi
KATIKA hali ya kustaajabisha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam,jana ilitoa maelekezo ya kuvizuia vyombo vyote vya habari nchini kuripoti mwenendo mzima wa kesi ya madai ya kashfa ya shilingi moja iliyofunguliwa mahakamani hapo na Mfanyabiashara Yusuf Manji dhidi ya Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Ltd, Reginald Mengi na ITV.
Maelekezo hayo yalitolewa jana saa nane mchana na Hakimu Mkuu Mkazi wa mahakama hiyo, Elvin Mugeta wakati kesi hiyo ya madai Na. 85/2009 ilikuja kwaajili ya kutajwa.
“Kesi hii imekuja leo(jana) kwaajili ya kutajwa lakini naomba mnisikilize kwa makini na utulivu kabisa na nitaongeza sauti ili muweze kunisikia vizuri...maelekezo hayo ni kama yafuatavyo ni kwamba kuanzia sasa vyombo vya habari yaani magazeti na vile vya electroniki havitaruhusiwa kuripoti mwenendo wa kesi hii kwasababu kufanya hivyo kuna athiri uhuru wa hakimu na mahakama;

“Vyombo vya habari katika hili tunaomba mtuwie radhi sana kwani tumevumilia mno hivyo mahakama ina sababu za msingi za kutoa maelekezo hayo na haina sababu ila haitaki kuzitaja sababu hizo adharani kwani taarifa mbili zinazokithana yaani ushahidi unaotolewa na shahidi mahakamani na ushahidi unaoandikwa kwenye vyombo vya habari kuhusu kesi hii zimeathiri hakimu na mahakama kwa ujumla kwani ilifika mahala mahakama haipumui;

Aidha Hakimu Mugeta alisema mahakama hiyo ni mahakama ya wazi hivyo wananchi wataruhusiwa kuudhuria kesi hiyo ila mashahidi wakati wanaotoa ushahidi wao vyombo vya habari havitaruhusiwa kuripoti ushahidi huo badala yake vitaruhusiwa kuripoti tarehe za kesi hiyo zilizopangwa, maamuzi madogo madogo yatakayotolewa na hukumu itakapotolewa”alisema Hakimu Mgeta na kuwafanya waandishi wa habari kushikwa na butwaa.

Baada ya kutoa maelekezo hayo Hakimu Mugeta alipanga tarehe ya kesi hiyo kuendelea kusikilizwa ambayo ni Juni 3 mwaka huu, lakini akazieleza pande hizo mbili kuwa hakimu mpya ambaye amepangwa kuendelea na kesi hiyo baada ya yule hakimu wa mwanzo kujitoa, watamjua siku ya tarehe hiyo kesi itakapoja kwaajili ya kusikilizwa.
Hata hivyo waandishi wa habari za mahakama walivyotoka nje ukumbi wa mahakama hiyo walisema wanashangazwa na maelekezo hayo na kuhoji ni kwanini maelekezo ya aina hiyo yametolewa kwenye kesi hiyo na siyo kesi nyingine ambazo zina maslahi ya umma moja kwa moja.

Aprili 8 mwaka huu, Hakimu Mkazi , Alocye Katemana alitangaza kujitoa kuendelea kusikiliza kesi hiyo kesi hiyo na kusema kuwa hawezi kutaja sababu za kujitoa kwa umma na kwamba jalada la kesi hiyo analipeleka kwa Hakimu Mkuu Mkazi Elvin Mgeta kumpangia hakimu mwingine.

Katemana alitoa uamuzi huo ikiwa ni mara ya kwanza siku hiyo tangu jalada la kesi hiyo lilipotoka kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Semistocles Kaijage Machi 29 mwaka huu ambaye aliamuru jalada la kesi hiyo lirudishwe Mahakama ya Kisutu kwa hakimu Katemana ambaye ndiye amekuwa akisikiliza kesi hiyo kwaajili ya kuendelea kusikiliza baada ya ukaguzi wake alioufanya katika jalada hilo akabaini kuwa hakimu huyo hakuwa amepindisha sheria yoyote wakati akiisiliza kesi hiyo.

Jalada la kesi hiyo ambayo lilitua katika Mahakama Kuu Mwishoni mwa mwezi Machi mwaka huu, likitokea Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutokana na barua ya Februali 23 mwaka huu, iliyoandikwa na wakili wa mdaiwa(Mengi) , Michael Ngaro kwa Jaji Mfawidhi Kaijage ambapo ndani ya barua hiyo Ngaro alimuomba apitie mwenendo mzima wa kesi kwani hawaridhishwi.


Uamuzi wa Hakimu Katemana wa kujitoa, kulikuja siku mbili baada ya mdaiwa katika kesi hiyo Na.85/2009, Reginald Mengi kufanya mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, na kulalamikia baadhi ya vichwa vya habari vilivyotokana na habari inayohusu kesi hiyo sambamba na kutoa matangazo katika magazeti kadhaa ambapo ndani ya matangazo hayo alilikuwa akilalamikia baadhi ya magazeti yanavyoripoti kesi hiyo na mambo mengine.

Februali 15 mwaka huu, Hakimu Mkazi Katemana alitupilia mbali ombi la Mengi lililotaka mahakama hiyo iwapatie nakala ya uamuzi iliyotolewa na hakimu huyo Februali 11 mwaka huu,ambapo hakimu huyu alikazikataa nyaraka vivuli 14 zikiwemo nyaraka ambazo zinaonyesha ni mali ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU),Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na mkataba wa kukopeshana fedha baina ya kampuni ya Kagoda Agriculture Ltd na Kampuni ya Quality Finance Corporation Ltd , ili aweze kwenda Mahakama Kuu kuomba ufanyiwe mapitio kwa sababu Sheria ya Mabadiliko ya Kanuni ambazo zimeandikwa Na. 25 ya mwaka 2002, zinakataza upande wowote katika kesi yoyote kwenda mahakama ya juu kupinga amri za muda zinazotolewa na mahakama ya chini hadi kesi ya msingi itakapomalizika na kutolewa hukumu.

Hakimu Katemana alisema siyo tu sheria hiyo ina kataza maamuzi madogo kama hayo aliyoyatoa kuyakatia rufaa pia nyaraka hizo 14 haziusiani na kesi iliyopo mbele yake, ni nyaraka vivuli ambazo hazijathibitishwa kisheria na pia hazionyeshi kama ofisi hizo za serikali zimetoa kibali kwa mdaiwa kutumia nyaraka hizo katika kesi hiyo na kuongeza kuwa nyaraka hizo zimewasilishwa nje ya muda mwafaka kwani kisheria zilipaswa kuwasilishwa kabla ya mlalamikaji kupanda kizimbani kuanza kutoa ushahidi wake.

Mapema mwaka 2009, Manji anayetetewa na mawakili maarufu nchini, Mabere Marando, Richard Rweyongeza, Dk.Ringo Tenga na Beatus Malima alimfungulia kesi ya madai ya kashfa Mengi na kituo cha televisheni cha ITV akitaka amlipe fidia ya shilingi moja kwa madai kuwa Mengi alitumia televisheni yake kumkashfu kwa kumuita ‘Fisadi Papa’ na kwamba mmoja wa watu wanaopora rasilimali za Tanzania.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Aprili 16 mwaka 2011.

KESI YA MPENDAZOE YAFIKA PATAMU

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Mei 25,26 na 27 mwaka huu, itaanza rasmi kusikiliza kesi ya kupinga matokeo ya Jimbo la Segerea uliofanyika mwaka jana yaliyomtangaza Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, Dk.Makongoro Mahanga kuwa ndiye mbunge iliyofunguliwa na aliyekuwa Mgombea Ubunge wa Jimbo hilo kwa tiketi ya (Chadema), Fred Mpendazoe.


Mbali na Dk.Mahanga wadaiwa wengine ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali na aliyekuwa Msimamizi wa Uchaguzi wa jimbo hilo na katika madai yake mlalamikaji ambaye ni Mpendazoe anataka mahakama kuu itengue ushindi wa Dk.Mahanga kwakuwa taratibu za sheria ya uchaguzi ya mwaka 2010 hazikufuatwa

Kwa mujibu wa hati wito wa kuitwa mahakamani iliyotolewa na mahakama ambayo Gazeti hili limefanikiwa kuona nakala yake, wahusika wa pande zote katika kesi hiyo wameishapewa nakala hiyo ya wito wa kufika mahakamani siku hiyo mbele ya Jaji Profesa Ibrahim Juma.

Kwa upande wake wakili Mpendazoe, Peter Kibatala alilithibitishia gazeti hili jana kwamba tayari ameishapokea kwaniaba yake nakala hiyo ya wito na kwamba watafika bila kukosa siku hiyo ambapo kesi yao itaanza kuunguruma rasmi.

Kesi hiyo ya Mpendazoe ni kesi ya kwanza kati ya kesi tisa za kupinga matokeo ya Uchaguzi wa ubunge wa mwaka 2010 kufikia hatua hiyo ya juu ya kuanza kusikilizwa.Kwani kesi nyingine za aina hiyo bado zipo katika hatua za awali mbele ya Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Aprili 15 mwaka 2011.

KESI YA ZOMBE YAPANGIWA JAJI

Na Happiness Katabazi

UONGOZI wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, umempangia Jaji Upendo Msuya kusikiliza kesi ya madai ya fidia ya sh bilioni tano iliyofunguliwa na aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Abdallah Zombe (57) dhidi ya serikali.


Kwa mujibu wa hati ya kuitwa mahakamani iliyotolewa na mahakama hiyo Machi 16, inazitaka pande zote katika kesi hiyo wafike mahakamani hapo Mei 16 mwaka huu, ambapo kesi hiyo itatajwa kwa mara ya kwanza tangu ilipofunguliwa.

Tanzania Daima ilipowasiliana na Zombe alithibitisha kupokea hati ya wito iliyotolewa na mahakama hiyo.

“Kwa sasa nipo Morogoro kwenye shughuli zangu za kujiingizia kipato ila ni kweli nimeishapokea hati hiyo ya kuitwa mahakamani Mei 16 mwaka huu, siku hiyo ya kesi nitahudhuria,” alisema Zombe.

Machi 7 mwaka huu, Zombe kupitia wakili wake, Richard Rweyongeza, alifungua kesi namba 35/2011 dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Jeshi la Polisi na akataja sababu 21 za kufungua kesi hiyo ya madai ya fidia ya kutaka alipwe sh bilioni tano na riba ya sh milioni 200.

Zombe anadai Jeshi la Polisi lilikiuka sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 inayotaka kabla ya mtu kukamatwa ni lazima aelezwe anakamatwa kwa sababu gani na akifikishwa kituo cha polisi ni lazima ahojiwe na kuchukuliwa maelezo yake ambayo baadaye hutumika mahakamani kama kielelezo, lakini jeshi hilo lilitenda kinyume cha sheria hiyo.

Zombe anadai sababu nyingine iliyosababisha afungue kesi hiyo ni Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Said Mwema kushindwa kulijibu kusudio lake la kuishitaki serikali ambalo lilipaswa kujibiwa ndani ya siku 90.

Agosti 17, mwaka 2009, Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ilimwachia huru Zombe na wenzake wanane waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya mauaji ya wafanyabiashara watatu na dereva teksi mmoja.

Baada ya hukumu hiyo, serikali ilikata rufaa Oktoba 7 mwaka 2009 katika Mahakama ya Rufaa kupinga hukumu hiyo, hata hivyo ilishindwa baada ya mahakama kueleza kuwa serikali ilishindwa kuthibitisha mashitaka hayo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatatu, Aprili 11 mwaka 2011.

SIRI ZA RICHMOND ZAZIDI KUFICHUKA

Na Happiness Katabazi

SHAHIDI wa tatu wa upande wa Jamhuri katika kesi ya kutoa taarifa za uongo kwa watumishi wa serikali kuhusu kampuni ya kufua umeme ya Richmond LLC, Injinia Simon Jilima ameileza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa hafahamu kuwa Mkurugenzi wa Kampuni hiyo aliyepo Marekani Mohamed Gile amewahi kulalamika kuwa mshtakiwa Naeem Gile ameghushi hati ya nguvu ya kisheria ya kampuni yake kufanyakazi hapa nchini chini ya mshtakiwa huyo.


Jilima ambaye ni Mhandishi wa Shirika la Umeme(TANESCO) alitoa maelezo hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema wakati akihojiwa na wakili wa utetezi Alex Mgongolwa ikiwa ni muda mfupi naada ya shahidi huyo kumaliza kuongozwa kutoa ushahidi wake na Wakili Mkuu wa Serikali Fredrick Manyanda ambapo pia shahidi huyo alidai kuwa hamfahamu ni nani aliyekuwa akiiwakilisha kampuni ya Richmond hapa nchini licha yeye aliteuliwa na Meneja Mkuu wa Idara ya Uzalishaji ya shirika hilo kuwa mhandishi msimamizi wa mradi wa kufunga mashine za kuzalisha umeme zilizoletwa na kampuni ya Richmond nchini.

“Namfahamu Mohamed Gile kupitia makabrasha kwamba yeye ndiye mkurugenzi wa Richmond yenye makao makuu nchini Marekani lakini sijawahi kuonana naye ana kwa ana...na sifahamu kuwa hiyo kampuni kama ilikuwa na mwakilishi wake hapa nchini”alidai mhandisi Jilima.

Awali akihojiwa na wakili mkuu wa serikali Manyanda, shahidi huyo Jilima alieleza mahakama kuwa mwaka 2006 alikuwa ni mhandisi katika katika kitengo cha uzalishaji umeme Tanesco na kwamba majukumu yake yalikjuwa ni kusimamia mitambo ya kuzalisha umeme na kwamba anaifahamu Richmond.

Jilima alieleza kuwa kwa mara ya kwanza aliifahamu kampuni hiyo wakati akiwa mjumbe wa kamati ya tathimini ya makampuni Machi 2006.Kwani kampuni hiyo ni miongoni mwa makampuni nane yaliyoleta maombi kwenye kamati hiyo ambaye naye alikuwa ni mjumbe na kwamba kamati hiyo ilikuwa na wajumbe 12 ilianzishwa na Bodi ya Manunuzi ya shirika hilo na hatimaye kamati hiyo ilibaini hakuna kampuni iliyotimiza vigezo na matokeo yao hayo waliyafikishwa kwenye bodi ya Tanesco.

“Baada ya Bodi kupokea taarifa yetu hiyo bodi hiyo iliagiza tena kamati yetu iangalie upya kampuni hiyo na kweli kamati yetu kwa mara ya pili ikaya tathimini tena makampuni yale na ikabaini tena kuwa makampuni hayo hayakuwa yametimiza vigezo walivyokuwa wakivitaka na kamati hiyo ikaandika tena ripoti yake kwa bodi na baada ya hapo kilichoendelea huko mbele sikufahamu”alidai Jilima.

Aidha alidai baada ya hapo aliteuliwa na Meneja Mkuu wa Idara ya Uzalishaji wa Shirika hilo Steven Babaga kusimamia mradi wa kufunga mashine za kufua umeme zilizoletwa na kampuni ya Richmond na akapewa mkataba wa kufunga mitambo hiyo na kwamba mkataba ulikuwa ni baina ya Tanesco na Richmond wa mwaka 2006 na kwamba majukumu yake yalikuwa kusimamia ufungaji mitambo licha mitambo hiyo ililetwa na Richmond ikiwa imechelewa.

‘Na awali nilikuwa nimeelezwa kwamba mitambo hiyo italetwa na Richmond kupitia kampuni ya Tratt-Whirtacy lakini baadaye kutokana na mabadiliko ambayo nilikuwa kuarifiwa na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini Dk. Ibrahim Msabaha ambaye ni miongoni mwa mawaziri waliojiuzulu kutokana na kashfa ya mkataba huo kwamba kampuni Tratt-Whirtacy haitaileta mitambo hiyo na kwamba mitambo hiyo italetwa na kampuni nyingine iitwayo GE Electric na kweli mitambo hiyo yenye megawati 100 ililetwa na tukaifunga”alidai shahidi huyo.

Kesi hiyo ambayo ilipangwa kuzisilikizwa mfululizo kwa siku tatu, kuanzia juzi na kwamba ingemalizika leo, katika hali isiyotarajiwa Wakili Mkuu wa Serikali Manyanda aliyaambia mahakama kuwa itawawia vigumu kuwapata mashahidi wengine hivyo akaiomba mahakama iarishe kesi hiyo jana hadi tarehe nyingine ambapo Hakimu Lema aliarisha shauri hilo hadi Mei 9-10 mwaka huu, na akautaka upande wa Jamhuri uakikishe unawaleta mashahidi wengi kadri iwezekanavyo.

Februali 2009 ilidaiwa mahakamani hapo kuwa Juni, 2006 jijini Dar es Salaam, mshitakiwa (Naeem) alitoa taarifa za uongo kwa wajumbe wa timu ya majadiliano ya serikali, kuwa Kampuni ya Richmond LLC ya Texas, Marekani, ina uwezo wa kuzalisha umeme kwa kiwango hicho ili apewe tenda hiyo.Aidha, alidai katika shitaka la tano mshtakiwa akifahamu na kwa ulaghai, alitoa hati ya nguvu ya kisheria iliyotolewa Machi 3, mwaka 2006 iliyokuwa ikimuonyesha kuwa ameruhusiwa na Mwenyekiti wa Kampuni, Hemed Gile ambaye ni kaka yake kufanya kazi za kampuni hiyo hapa nchini.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Aprili 13 mwaka 2011.

MABADILIKO YA KATIBA YASIVURUGE AMANI YETU


Na Happiness Katabazi

BABA wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere, alisema: “Uhuru bila nidhamu ni sawa uendawazimu na nidhamu bila uhuru ni sawa na utumwa.”


Nimelazimika kuyatumia matamshi hayo kwasababu kwa wale ambao ni wafuatiliaji wa masuala yahusiyo mustakabali wa taifa hususan hili la taifa liandike Katiba, mtakubaliana nami kwamba baadhi ya wananchi wanatumia uhuru bila nidhamu.

Matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea Aprili 7, mwaka huu yalitokea katika Ukumbi wa Karimjee Dar es Salaam wakati wa mjadala wa mabadiliko ya Katiba na kusababisha mjadala huo kuvunjika.

Tukio jingine lilitokea siku hiyo hiyo katika viwanja vya Bunge Dodoma na kusababisha wanausalama kutumia mabomu ya machozi, risasi, virungu na mabango ya kuikebehi serikali baada ya wananchuo wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kudaiwa kutishia hali ya usalama katika eneo hilo.

Pia matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea katika Ukumbi wa Shule ya Haile Selassie mjini Zanzibar.

Inaelezwa kuwa polisi wa Kutuliza Ghasia (FFU) na wanausalama walilazimika kutumia nguvu kuwatawanya wanachuo hao waliotaka kutumia nguvu kuingia katika Ukumbi wa Bunge wa Pius Msekwa kushiriki mjadala huo.

Amri ya kupiga mabomu ilitolewa na Mkuu wa Mkoa, Dk. James Msekela baada ya wanachuo hao kuanza kurusha mawe na kumjeruhi mpiga picha wa gazeti la Mwananchi, Edwin Mjwahuzi na askari mmoja.

Wanachuo hao waliokuwa wakiimba nyimbo na mabango ya kuikebehi serikali kwa zaidi ya saa tatu, waliamua kuvurumisha mvua ya mawe ndani ya eneo la Bunge, wakipinga wadau wengine kuendelea na mjadala wakati wao wako nje.

Kwa upande wake Katibu wa Bunge, Thomas Kashilila, alilaani vurugu hizo na kusema wanachuo hao walikuja kwa shari maana hata kukaguliwa walikataa.

Kama maelezo ya viongozi hao ni sahihi basi yale matamshi ya Mwalimu Nyerere kwamba: “Uhuru bila nidhamu ni sawa na wendawazimu,” ni sahihi kabisa.

Nchi yetu imeridhia taifa linaloongozwa na Katiba, kanuni mbalimbali za serikali, taratibu na mazoea ya serikali; hivyo kila mwananchi anatakiwa kufuata sheria hizo anapodai dai lake.

Aidha kitendo cha mwakilishi wa Chama cha Mapinduzi (CCM-Tambwe Hizza na Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba wakati wakitoa maoni yao kuzomewa na kupigiwa makelele wasiendelee kutoa maoni yao, ni wazi miongoni mwetu tunaohitaji hitaji hilo la katiba, tuna ajenda zetu za siri ambazo tumezivika kilemba cha dai la Katiba mpya.

Aiingii akilini kwa mtu mwenye akili timamu anayeelewa nini maana ya demokrasia na Ibara ya 18(a) ya Katiba ya mwaka 1977 inayosema: “Kila mtu anao uhuru wa kuwa na maoni na kueleza fikra zake,” kufanya uhuni kama uliofanywa na baadhi ya wanachuo hao na wale washiriki wa mdahalo wa Karimjee uliosababisha uhairishwe kwa ajili ya wananchi kumkatiza kwa makusudi Hizza asiendelee kutoa maoni aliyotumwa na chama chake.

Kila mtu ana uhuru wa kutoa maoni yake bila kuvunja sheria na ana haki ya kusikilizwa hata kama maoni yake yanatofautiana na mawazo ya watu wengine na hiyo ndiyo demokrasia.

Kitendo cha baadhi ya washiriki kushindwa kumvumilia Hizza amalize kutoa mawazo yake, wamekosa nidhamu, hawajakomaa kidemokrasia na wana ajenda yao binafsi.

Katika mdahalo wa Karimjee imeelezwa kuwa baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wastaafu wa serikali na waliopo serikalini kwa sasa na wasomi walikuwepo na kudiriki kuleta fujo za kutupiana maneno ndani ya ukumbi huo.

Siku nyingine wanaoandaa mdahalo huo, kama hawatawaita vyombo vya usalama, ipo siku washiriki wataingia na silaha za jadi kama fimbo, wembe na nyinginezo.

Suala la mjadala wa mabadiliko ya Katiba ni suala nyeti sana kwani ni la ustawi wa taifa letu sasa kama serikali na vyombo vyetu vya dola kama havitakaa imara katika mijadalo hiyo ni wazi kabisa uvunjifu wa amani utakuwa ukitokea mara kwa mara.

Katiba haijaundwa mmeishaanza kuleta vurugu je, huko mbele ya safari ikaundwa halafu hao washiriki wakorofi wakabaini maoni yao hayakuingizwa kwenye Katiba hiyo, si watatuletea vurugu hapa nchini?

Ieleweke kwamba kila sehemu kuna viongozi na sheria na taratibu zake. Sasa kitendo kilichofanywa na wanachuo wa UDOM eti kwa sababu wamezuiliwa kuingia ndani ya ukumbi huo, kimeshusha heshima ya wasomi hao na kimetushangaza na kuona huenda wasomi hao walikuwa na ajenda nyingine zaidi ya kuruhusiwa kuingia kwenye mdahalo huo.

Siku zote jamii inaamini wasomi ni watu waliostaarabika na wawe mfano kwa jamii.
Haiingii akilini kabisa wanafunzi hao kuelezwa kwamba ukumbi huo ni mdogo hauwezi kubeba tena idadi hiyo ya wanafunzi ambao wanakisiwa kuwa ni zaidi ya 9,000 na badala yake wakaruhusu wanafunzi wachache waingie lakini wanafunzi hao wakaamua kuzua tafrani hilo eti kwa kigezo cha kuzuiiliwa kuingia ukumbini.

Watanzania tukumbuke ni hawa hawa wanafunzi wa vyuo vikuu nchini wamekuwa wakilalamika kuwa madarasa na mabweni wanayosemea na kulala yameelemewa na idadi kubwa ya wanafunzi na kuishinikiza serikali itanue vyuo hivyo kwa kujenga majengo zaidi, lakini ghafla wiki iliyopita wanafunzi hao wakakengeuka na kutaka waruhusiwe kujazana kwenye ukumbi huo licha ya kuambiwa umejaa.

Tuwahoji wanafunzi hawa endapo Dk. Msekela na uongozi wa ukumbi wa Msekwa wangekuwa legelege na wangewaruhusu wanachuo hao wote wakajazane kwenye ukumbi huo na kwa bahati mbaya hewa ingekosekana na watu kupoteza maisha kutokana na kukosekana kwa hewa, wangemlaumu nani?

Na ambao wangenusurika kifo hicho ndiyo wangekuwa wa kwanza kuishutumu serikali kuwa ilishindwa kudhibiti mapema idadi ya watu kuingia ukumbini humo?

Tuwaulize wasomi hawa hadi walifikia hatua ya kushupalia kuingia kwa nguvu kwenye ukumbi huo, hivi wanafikiri huyo aliyekuwa anaendesha mdahalo huo angeweza kutoa nafasi kwa kila mwanachuo wa UDOM kutoa maoni yake?

Sasa swali ni je hivi kama wanafunzi hao walikuwa na lengo moja la kushiriki mdahalo huo, yale mabango waliyobeba waliyapata wapi katika kipindi kifupi namna ile?
Huko ni kukosa ni dhamu mbele ya viongozi waliowazidi umri waliokuwa ndani ya ukumbi na jamii kwa ujumla.

Ni kweli wanafunzi hao walikuwa na haki ya kushiriki na kutoa maoni yao kwenye mdahalo huo na midahalo mingine itakayokuja, lakini haki hiyo iligeuka kuwa ghasia kwa wapita njia na wakazi wa maeneo hayo kutokana na vurugu walizozifanya.

Tunaamini wao ni wasomi na wengine wanasomeshwa na kodi za wananchi kama waliona haki yao imeporwa si vyombo vya dola vipo wangeenda kulalamika.

Mkae mkijua mlichokifanya kimeishajengeka vichwani mwa watu kwamba wanafunzi wa UDOM ni wakorofi wanatumiwa na wanasiasa kirahisi na mwisho wa siku sifa hiyo mbaya hata kama mtakuwa mmefaulu vizuri itawawia vigumu kupata ajira kwenye soko la ajira.

Tunafahamu si wanafunzi wote ni wakorofi ila kuna baadhi yao wamesahau dhiki za majumbani kwao na matokeo yao wamejisahau kilichowapelekea chuoni hapo ni kupata elimu na si huo mdahalo wa mabadiliko ya Katiba ambao haupo hata katika mtahala wa masomo yanayotolewa na Chuo hicho.

Lakini wasomi hao busara hiyo hawakuichukua wakaamua kutumia njia ovu ya kurusha mawe na kutoa maneno ya kashfa dhidi ya serikali na CCM.

Tuwaulize wanafunzi hao hivi ndani ya ukumbi ule ulihudhuriwa na wana CCM peke yao?
Mbunge wa Arusha Mjini (CHADEMA), Godbless Lema, alisema yeye ndiye aliyekwenda katika Chuo Kikuu cha Dodoma kuwahamasisha wanafunzi hao waje kwa wingi katika mdahalo huo.

Kwanza kabisa wanafunzi hao kabla ya kufika katika viwanja hivyo walipaswa kumuuliza Lema kwamba yeye ndiye mratibu wa mdahalo huo?

Na je, ameweka utaratibu upi ambao ungewawezesha mamia ya wanafunzi hao kuweza kushiriki katika mdahalo huo?

Kama maswali hayo yote wangemuuliza mapema mbunge huyo ni wazi wasingekubali kuswagwa namna ile ambapo mwisho wa siku wakajikuta yule aliyewaalika (Lema) amepata nafasi ya kuingia ukumbini na wao kuishia nje na kupata mkong’oto toka kwa Jeshi la Polisi.

Kama wangeondokana na mawazo mgando baada ya kupata mwaliko wa mdomo toka kwa mbunge huyo ambaye naye alikuwa ni mwaliko kama walivyokuwa waalikwa wengine, serikali ya wanafunzi wa chuo hicho ingeteua wawakilishi wachache waende kushiriki kwa niaba ya wanafunzi wote.
Mwanachuo yoyote aliyekuwa ana mawazo yake angeandika wazo lake na kuwapatia wawakilishi hao ambao wangelifikisha kwenye mdahalo huo ama kwa mdomo au kwa maandishi.
Hivyo idadi kubwa ya wanafunzi wangebaki chuoni na kuendelea kujisomea kwani sisi tunachojua kilichowapeleka wanafunzi hao pale UDOM ni masomo na si ujuha kama ule.
Wanafunzi na wananchi wengine wanaoleta vurugu kwenye midahalo hiyo wajue kwamba wao si waamuzi wa kuruhusu muswada wa mabadiliko ya Katiba upite au usipite.
Waamuzi ni wabunge wetu wanaotuwakilisha bungeni ambapo Alhamisi na Ijumaa wiki hii wataujadili muswaada huo na kuupigia kura za muswada huo upite au usipite.
Hivyo kazi yetu sisi ni kutoa maoni kwa njia ya amani na kazi ya kuamua kuamua mswaada huo upite au usipite ni ya Bunge.
Hivyo msituvurugie amani kwaajili ya ajenda zenu za siri.
Fukuto la Jamii linawaasa wafuasi wa vyama vya siasa hapa nchini vinavyodaiwa vimekuwa vikiwatumia wanachama wao kuleta vurugu kwenye midahalo hiyo, viache tabia hiyo, kwani muswada huo hauna vyama bali unawahusu Watanzania.
Desemba 31 mwaka jana, Rais Jakaya Kikwete wakati akizungumza na wananchi kupitia hotuba yake ya kila mwisho wa mwezi, alisema anakubali hoja ya kuundwa kwa Katiba mpya.
Kila mmoja wetu amelichukulia hilo kivyake, na hii ndiyo tabia ya Watanzania ambo hawajajenga mila, desturi na utamaduni wa kushiriki katika mjadala wa kitaifa.
Mjadala wa kitaifa ni mchakato wa kujenga hoja kwa masilahi ya taifa. Kamwe hauendeshwi kwa kila mtu kujenga hoja kutetea tumbo lake.
Kwa hiyo wengi wanaojenga hoja ya kutaka kuundwa kwa Katiba mpya, wanafikiri matumbo yao, masilahi binafsi na umaarufu binafsi.
Vipo vyama na wapo watu na vikundi ambavyo bila kujali umaarufu binafsi wameendeleza hoja hii hadi leo.
Wapo baadhi ya wanasiasa watakaojaribu kuibinafsisha hoja hiyo ili waonekane ni waasisi wa hiyo hoja.
Wanaamini kwamba kumbukumbu za Watanzania ni duni hawawezie kukumbuka hoja hii ilianza lini na waasisi ni kina nani.
Tena katika hali ya kushangaza kama sio kustaajabisha wanachama wa vyama vya siasa na baadhi ya viongozi wao hawajui katiba za vyama vyao ambazo zimeandikwa kwa lugha ya Kiswahili na wala hawafahamu zimeandikwa nini ndani yake.
Sasa iweje leo hii wawe na ukereketwa wa kudai Katiba mpya ikiwa tu ibara za katiba ya vyama vyao hawazijui zinasema nini?
Wengine hata gamba la Katiba ya Jamhuri hawajawahi kuliona na duka la vitabu vya serikali ambapo ndipo sheria zote za Katiba ya nchi zipo yapo wapi?
Rais Kikwete katika hotuba yake ile pia alitamka kwamba mwaka huu ni wa Watanzania kujadili hoja ya Katiba mpya na yeye ataunda tume ya kuongoza mchakato wa kupata Katiba mpya.
Na kweli ahadi hiyo ya rais imetimia katika kipindi kifupi, kwani tayari muswada umeshaandaliwa na kupelekwa bungeni tayari kwa kuanza kujadiliwa.
Ni vema tukampongeza Rais Kikwete kwa kutekeleza ahadi hiyo katika hatua hii ya awali kwa kuzingatia kwamba hatua hiyo ni ya kijasiri sana kwani ukweli ni kwamba kundi kubwa la wanaopinga hoja hiyo wapo katika chama anachokiongoza cha CCM na serikali anayoingoza.
Sasa Watanzania tuko wapi? Je, tunaelewa kilichomsibu rais hadi akubali hoja ya Katiba mpya?
Kabla ya kupinga na kuona nia ya rais wetu ni mbaya eti kama ana jaribu kuteka hoja au kupora hoja ya wapinzani, tujiulize ni wangapi wanaelewa maana kamili ya mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar yaliyofanyika mwaka 2010?
Ni wangapi miongoni mwetu wameishaisoma Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977?
Nimalizie kwa kuwakumbusha wale wote wanaoleta vurugu kwenye mijadala hiyo kwamba utawala wa serikali yetu ni utawala unaoongozwa na sheria na Katiba na kamwe utawala huo haufanani na ule utawala wa samaki aina ya kambale ambao baba, mama na mtoto wote wana ndevu.
Hivyo sote tunapaswa tufuate sauti moja ya misingi tuliyojiwekea.
Hakuna ubishi, yale matamshi ya Mwalimu Nyerere kuwa “Uhuru bila nidhamu ni sawa uendawazimu,” yametimia kutokana na matukio hayo niliyoyataja na mengine sijayataja ambayo yametokea na yanaoendelea kutokea chini ya uongozi wa serikali ya awamu ya nne.
Sasa unapokuwa na taifa lenye wananchi wanaotumia vibaya uhuru wa kutoa maoni ni wazi kabisa muda si mrefu taifa hilo litajikuta linafuga na kuwalinda wananchi wengi ambao ni wendawazimu.
Navyo vyombo vya habari visifanye ushabiki katika suala hili la mchakato wa mabadiliko ya Katiba.
Kwa sababu hoja hiyo si mali binafsi ya Rais Kikwete, CCM, CHADEMA, NCCR-Mageuzi wala vyama vingine vya upinzani bali ni hoja ya Watanzania wote kwa masilahi yao.

Mungu ibariki Tanzania,
Mungu ibariki Afrika.

0716 774494
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Aprili 12 mwaka 2011.

SHAHIDI SERIKALI ILIIBEBA RICHMOND

Na Happiness Katabazi

MTAALAMU wa manunuzi wa Shirika la Umeme (TANESCO), Nicholaus Suke ameileza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam kuwa Kamati maalumu iliyoundwa na Shirika hilo kuchambua washiriki walijitokeza katika zabuni ya kununua mashine ya kufua umeme wa megawati 100 ilibaini hakuna aliyekidhi vigezo vilivyowekwa ikiwemo kampuni ya Richmond Development Company LLC.


Suke mbaye ni shahidi wa kwanza wa upande wa Jamhuri mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema alitoa maelezo hayonjana wakati akiongozwa na Wakili Mkuu wa Serikali Fredrick Manyanda kutoa ushahidi wake katika kesi ya kutoa taarifa za uongo kwa maofisa wa serikali kuhusu kampuni ya Richmond inayomkabili Naeem Gire ambapo shahidi huyo alidai kuwa licha ya kamati hiyo kuchambua makampuni yale , lakini ilibaini hakukuwa na kampuni yenye uhafadhari.

Alidai kuwa mwaka 2005 alikuwa na wadhifa wa Afisa na Katibu wa Bodi ya Zabuni na kwamba anaitambua kampuni hiyo ambayo mwaka 2006 ilikuwa ni miongoni mwa makampuni nane yaliyojitokeza kuomba zabuni hiyo iliyotangazwa na serikali kutoka na taifa kukumwa na tatizo la umeme.

Alitaja baadhi ya washiriki waliowasilisha makabrasha ya maombi ya kupatiwa tenda ya zabuni hiyo ambayo ilitangazwa kwenye magazeti, mbali ya Richmond ni Aggreco, Real Energy, Gapco, Apgum, Quatus, Recno.

Shahidi huyo alidai zabuni hiyo ilikuwa ya wazi ya ushindani wa kimatafa ambapo ilitangazwa Februari mwaka 2006, baada ya Bodi ya manunuzi ya serikali kupitisha nyaraka za kuanzisha mchakato wa kuitangaza.Hata hivyo, zabuni hiyo ilitangazwa kwa siku 10, kinyume na sheria ya manunuzi ya umma ya mwaka 2004 inayotaka iwe ya siku 45 na ilifanyika hivyo kutokana na maelekezo ya aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini Dk. Ibrahim Msabaha ambaye baadaye alikuja kujiudhulu kutokana na kashfa ya mkataba huo wa Richmond.

Alidai siku ya ufunguzi wa zabuni hiyo, kulikuwa na marumbano baina ya TANESCO na serikali. Alidai Richmond ilifuata taratibu zote za kushiriki kwenye zabuni. Baada ya washiriki hao kuwasilisha makabrasha yao, kamati maalumu iliundwa kuchambua washiriki hao ikiwa chini ya mwenyekiti Boniface Njombe akisaidiwa na washauri kutoka kampuni ya Lamahye kutoka Ujerumani ambao ni Poule na Hunae.

Shahidi huyo alieleza kuwa matokeo matokeo ya uchambuzi yaliweka wazi kwamba hakuna mshindi katika zabuni hiyo kwasababu hakuna hata kampuni moja kati ya zote zilizoomba zilitimiza vigezo vilivyowewa.Alidai bodi ya zabuni ilipopelekewa taarifa na kamati hiyo, iliridhia matokeo hayo, na kwa sababu nchi ilikuwa na matatizo ya umeme Bodi ya TANESCO kupitia menejimenti ilijulishwa kuhusu hilo ambapo iliiagiza kamati hiyo kuangalia kama kuna kampuni yenye uhafadhali.

Shahidi huyo, alidai kamati hiyo ilifanya uchambuzi tena ambapo ilibaini hakuna mwenye hafadhali na serikali ilijulishwa kwa kupitia bodi ya TANESCO. Alidai serikali ilielekeza kupelekewa kwa nyaraka za zabuni ambapo ili ziende bodi ya TANESCO ilifuta zabuni na kuzipeleka nyaraka.Mtaalamu huyo, alidai serikali ilitengeneza kamati yake maalumu na kuendelea na mchakato huo, ambapo yeye hakuwepo.

Yafutayo ni mahojiano baina ya shahidi huyo na wakili wa mshtakiwa Alex Mgongolwa:
Mgongolwa: Ulisema kulikuwa na malumbano kati ya TANESCO na serikali ni malumbano gani?

Shahidi: Yalikuwa ni ya aidha zabuni itangazwe ya siku 10 au ifiatwe sheria ya manunuzi inavyosema. Malumbano hayo ilikuwa ni kuhakikisha sheria uinafuatwa.

Alidai TANESCO baada ya kuona sheria inavunjwa walitaarifu Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), ambayo ilishauri kufuatwa kwa njia nyingine ya kutangazwa kwa siku 14.

Shahidi huyo, alidai wao waliitaarifu serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini na kusisitiza agizo lao na siku 10 litekelezwe.

Shahidi wa pili kwenye kesi hiyo, alikuwa Wakili wa kujitegemea Silvester Shayo, ambaye alidai Machi 13, 2006 alikuwa shuhuda wa waraka wa kuteua mwakilishi baina ya kampuni ya Richmond na Gire ambaye aliteuliwa kuwa mwakilishi wa kampuni hiyo.

Alidai waraka huo aliletewa ofisini kwake na karani wa wakili mwenzake Emmanuel Kisusi na kwamba haukutilia shaka kwa kuwa anamuamini wakili huyo.Hakimu Lema aliairisha kesi hiyo hadi leo ambapo shahidi wa tatu atapanda kizimbani kuanza kutoa ushahidi wake.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Aprili 12 mwaka 2011.



MAHABUSU WATOROKA CHINI YA ULINZI MAHAKAMA YA KISUTU

Na Happiness Katabazi

MAHABUSU wawili wanaokabiliwa na kesi ya unyang’anyi wa kutumia silaha Na. 253/2010 , Shida Luanda na Samuel Oyugi, wametoroka wakiwa katika harakati za kufungwa pingu na askari Maregeza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jiji Dar es Salaam.


Tukio hilo la aina yake lilitokea jana saa 3.30 asubuhi mahakamani hapo, ikiwa ni muda mfupi baada ya mahabusu hao wakiwa na wenzao wengine wawili Hakimu Mkazi Sundi Fimbo kuarisha kesi yao.Washitakiwa hao ambao walitoroka kwa kuruka ukuta wa mahakama hiyo, hata hivyo askari wanaolinda mahakama hiyo walifanikiwa kumkamata Luanda, nje ya eneohilo na Oyugi alifanikiwa kutoroka moja kwa moja hajapatikana hadi saa tisa alasiri wakati gazeti hili linaondoka mahakamani hapo.

Wanausalama hao baada ya kufanikiwa kumkamata Luanda walimpandisha kizimbani mbele ya Hakimu Mkazi Mustapher Siyani na kufunguliwa kesi mpya ya kutoroka akiwa chini ya ulinzi wa askari wa Jeshi la Magereza.

Wakili wa serikali Zuberi Mkakuti ndiye aliyesoma hati mpya ya dhidi ya mshtakiwa huyo ambapo alidai Luanda anakabiliwa na kosa la kutoroka chini ulinzi wa askari Magereza Rashid Gwakisa na Ibrahim na kwamba kosa hilo alilitenda jana saa tatu asubuhi mahakamani hapo.

Mshitakiwa huyo ambaye shati lake alilokuwa amelivaa mwilini lilikuwa limechanika kwa nyuma na hivyo kumfanya kulifunga huku akiwa hana viatu mguuni, alikana shtaka hilo ambapo Wakili Mkakatu alidai upelelezi wa shauri hilo umekamilika na jana hiyo akamsomea maelezo ya awali mshtakiwa huyo.

Katika maelezo hayo, inadaiwa Luanda , Oyugi, Ismail Shabani na Hati Jawadu, walifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Fimbo, kusomewa mashitaka katika kesi ya jinai Na. 253/2010.Mkakatu alidai baada ya washitakiwa hao kutoka kwa Hakimu Fimbo, wakiwa kwenye ‘korido’ la mahakama chini ya ulinzi wa askari hao ambao walikuwa wanawafunga pingu, Luanda na Oyugi walitumia nguvu na kujinasua kutoka kwenye pingu.

Ilidaiwa washitakiwa hao walimpiga kifuani askari Rashid na kukimbia ambapo katika harakati za askari hao kuwafukuza, waliruka ukuta wa mahakama ya Kisutu na kurukia upande wa pili ambao ni jingo la Maktaba ya Taifa. Mkakatu alidai askari walifanikiwa kumkamata Luanda nje ya eneo hilo na kufikishwa mahakamani hapo kwa kosa la kutoroka akiwa chini ya ulinzi.

Katika maelezo hayo ya awali aliyosomewa, Luanda alikubali kuwa jina na umri ni vyake. Upande wa mashitaka ulidai una mashahidi watatu ambao ni askari waliotorokwa na washitakiwa.Luanda na Oyugi walitoroka mahakamani hapo kwa kupanda katika vyuma vilivyofungwa na mafundi wanaofanya ukarabati ndani ya ofisi za mahakama hiyo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Aprili 12 mwaka 2011.

HAKIMU KESI YA MANJI,MENGI AJITOA


Na Happiness Katabazi
HAKIMU Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Alocye Katemana ametangaza kujitoa kuendelea kusikiliza kesi ya madai ya kashfa ya shilingi moja iliyofunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na mfanyabiashara Yusuf Manji dhidi ya Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Ltd, Reginald Mengi na ITV.


Uamuzi huo aliutoa jana mahakamani wakati kesi hiyo ilipokuja kwaajili ya kutajwa.Kesi hiyo ilikuja kutajwa kwa mara ya kwanza jana tangu jalada la kesi hiyo lilipotoka kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Semistocles Kaijage Machi 29 mwaka huu ambaye aliamuru jalada la kesi hiyo lirudishwe Mahakama ya Kisutu kwa hakimu Katemana ambaye ndiye amekuwa akisikiliza kesi hiyo kwaajili ya kuendelea kusikiliza baada ya ukaguzi wake alioufanya katika jalada hilo akabaini kuwa hakimu huyo hakuwa amepindisha sheria yoyote wakati akiisiliza kesi hiyo.

Jalada la kesi hiyo ambayo lilitua katika Mahakama Kuu Machi 23 mwaka huu, likitokea Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutokana na barua ya Februali 23 mwaka huu, iliyoandikwa na wakili wa mdaiwa(Mengi) , Michael Ngaro kwa Jaji Mfawidhi Kaijage ambapo ndani ya barua hiyo Ngaro alimuomba apitie mwenendo mzima wa kesi kwani hawaridhishwi.

Hakimu Mkazi Katemana jana aliingia mahakamani hapo na wakili wa mlalamikaji(Manji), Dk.Ringo Tenga alianza kwa kujitambulisha kama ulivyo utaratibu wa kimahakama na wakili huyo alipomaliza Hakimu Katemana alieleza kuwa anafahamu kuwa kesi hiyo imekuja kwaajili ya kutajwa ila anatangaza kujitoa kuendelea kusikiliza kesi hiyo na kusema kuwa hawezi kutaja sababu za kujitoa kwa umma na kwamba jalada la kesi hiyo analipeleka kwa Hakimu Mkuu Mfawidhi wa mahakama hiyo ili aweze kumpangia hakimu mwingi.

“Kabla ya mawakili kuendelea naomba niwatangazie kuwa kuanzia leo(jana) najitoa kuendelea kusikiliza kesi hii na sababu za kujitoa sitazitangaza kwa umma hivyo basi nalirudisha jalada hili kwa hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama hii ili aweze kumpanga hakimu mwingine ili aweze kuendelea kusikiliza kesi hii na ninaiarisha kesi hii hadi Aprili 15 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya kutajwa.”alisema Hakimu Katemana huku akionyesha kujiamini.

Uamuzi wa Hakimu Katemana wa kujitoa kuendelea kusikiliza kesi hiyo, kunakuja siku mbili baada ya mdaiwa katika kesi hiyo Na.85/2009, Reginald Mengi kufanya mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, na kulalamikia baadhi ya vichwa vya habari vilivyotokana na habari inayohusu kesi hiyo sambamba na kutoa matangazo katika magazeti kadhaa ambapo ndani ya matangazo hayo alilikuwa akilalamikia baadhi ya magazeti yanavyoripoti kesi hiyo na mambo mengine.

Februali 15 mwaka huu, Hakimu Mkazi Katemana alitupilia mbali ombi la Mengi lililotaka mahakama hiyo iwapatie nakala ya uamuzi iliyotolewa na hakimu huyo Februali 11 mwaka huu,ambapo hakimu huyu alikazikataa nyaraka vivuli 14 zikiwemo nyaraka ambazo zinaonyesha ni mali ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU),Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na mkataba wa kukopeshana fedha baina ya kampuni ya Kagoda Agriculture Ltd na Kampuni ya Quality Finance Corporation Ltd , ili aweze kwenda Mahakama Kuu kuomba ufanyiwe mapitio kwa sababu Sheria ya Mabadiliko ya Kanuni ambazo zimeandikwa Na. 25 ya mwaka 2002, zinakataza upande wowote katika kesi yoyote kwenda mahakama ya juu kupinga amri za muda zinazotolewa na mahakama ya chini hadi kesi ya msingi itakapomalizika na kutolewa hukumu.

Hakimu Katemana alisema siyo tu sheria hiyo ina kataza maamuzi madogo kama hayo aliyoyatoa kuyakatia rufaa pia nyaraka hizo 14 haziusiani na kesi iliyopo mbele yake, ni nyaraka vivuli ambazo hazijathibitishwa kisheria na pia hazionyeshi kama ofisi hizo za serikali zimetoa kibali kwa mdaiwa kutumia nyaraka hizo katika kesi hiyo na kuongeza kuwa nyaraka hizo zimewasilishwa nje ya muda mwafaka kwani kisheria zilipaswa kuwasilishwa kabla ya mlalamikaji kupanda kizimbani kuanza kutoa ushahidi wake.

Mapema mwaka 2009, Manji anatetewa na mawakili maarufu nchini, Mabere Marando, Richard Rweyongeza, Dk.Ringo Tenga na Beatus Malima alimfungulia kesi ya madai ya kashfa Mengi na kituo cha televisheni cha ITV akitaka amlipe fidia ya shilingi moja kwa madai kuwa Mengi alitumia televisheni yake kumkashfu kwa kumuita ‘Fisadi Papa’ na kwamba mmoja wa watu wanaopora rasilimali za Tanzania.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Aprili 9 mwaka 2011.

KORTI KUU YASIKILIZA OMBI LA NG'UMBI

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, jana ilisikiliza ombi dogo la aliyekuwa mgombea ubunge wa Jimbo la Ubungo kwa tiketi ya CCM, Hawa Ng’umbi, la kuomba mahakama impatie msamaha wa kutolipa sh milioni 15 kama dhamana ya kesi yake ya kupinga ushindi wa mbunge wa jimbo hilo, John Mnyika (Chadema).


Ng’umbi katika kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ambayo yalimtangaza Mnyika kuwa mshindi, ana mshtaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali, John Mnyika na aliyekuwa Msimamizi wa Uchaguzi wa jimbo hilo ambapo Mnyika anatetewa na wakili wa kujitegemea, Edson Mbogoro. Ng’umbi alifungua kesi Na. 107/2010 Machi 22 mwaka huu, akitaka mahakama hiyo itengue ushindi wa Mnyika kwa sababu sheria ya uchaguzi ilikiukwa.

Wakili wa Ng’umbi, Issa Maige, aliiomba mahakama hiyo chini ya Jaji Upendo Msuya anayesikiliza kesi hiyo imsamehe mteja wake asilipe kiasi hicho cha fedha kwa sababu hata Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2002 haijaweka kigezo cha mteja wake kwamba ana uwezo wa kifedha, hivyo ni lazima alipe kiasi hicho cha fedha.

“Mheshimiwa Jaji tunaomba mahakama ilikubali ombi la mlalamikaji (Ng’umbi) la kutaka asamehewe asilipe dhamana hiyo na kwamba mahakama itupilie mbali pingamizi la wadaiwa ambao wanataka ombi la mteja wangu litupwe,” alidai wakili Maige.

Kwa upande wake wakili wa Mnyika, Edson Mbogoro na wakili wa serikali Sehel, waliomba mahakama hiyo itupilie mbali ombi hilo kwa sababu mlalamikaji anajiweza kiuchumi, hivyo ana uwezo wa kulipa kiasi hicho cha fedha kama sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2002 inavyomtaka.

Jaji Msuya alisema amesikiliza hoja za pande zote mbili na ameahirisha kesi hadi Aprili 18 mwaka huu atakapotoa uamuzi wake.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Aprili 9 mwaka 2011.

DOWANS YAWAJIBU LHRC

Na Happiness Katabazi

KAMPUNI ya Dowans Holding SA na Dowans Tanzania Ltd, zimeiomba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam itupilie mbali mapingamizi waliyowekewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) na wengine, kwa madai kuwa hawana haki ya kisheria kupinga tuzo waliyopewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara (ICC) isajiliwe na mahakama hiyo.


Mbali na LHRC, wengine walioweka mapingamizi ya kutaka Mahakama Kuu ya Tanzania isisajili tuzo hiyo ni mwandishi wa habari mwandamizi, Timothy Kahoho, Lawyers Environment Action Team na Sikika Company.

Ombi hilo la kutaka mapingamizi hayo yatupiliwe mbali liliwasilishwa hivi karibuni mahakamani hapo na wakili wa Kampuni ya Dowans, Kennedy Fungamtama, kwa madai kuwa LHRC na wengine wanaopinga tuzo hiyo hawana haki kwa sababu hawakuingia nao mkataba wa kufua na kuzalisha umeme.

Nakala ya mapingamizi hayo ya Dowans ambayo Tanzania Daima inayo, inaeleza kuwa wenye haki ya kupinga tuzo hiyo ni TANESCO ambao waliingia nao mkataba na si watu, ama taasisi nyingine.

Nakala hiyo ya Dowans imechambua kuwa; Kahoho hana haki wala masilahi yoyote ya kisheria yanayompa nguvu ya kisheria ya kupinga tuzo, kwa sababu mkataba uliingiwa na pande mbili ambazo ni Dowans na TANESCO na kuongeza kuwa hata TANESCO ilipovunja mkataba huo ni Dowans ndiyo ilikwenda ICC kuifungulia kesi TANESCO na hatimaye Oktoba 15 mwaka jana, mahakama hiyo ilitoa hukumu ambapo Dowans ndiyo ilishinda kesi hiyo.

Wakili huyo wa Dowans, Fungamtama anadai kuwa hata katika mkataba walioingia Dowans na TANESCO , Kahoho hawakuwa sehemu ya mkataba huo (Power Off –Take Agreement (POA) ambapo kwa mujibu wa mkataba huo, pande hizo mbili zilikubaliana kuwa endapo itatokea tofauti miongoni mwao, mgogoro wao utatatuliwa na Mahakama ya ICC.

Alisema pande zote zilikubaliana kwamba mkataba huo ni mzuri na kwa mazingira hayo, Mahakama ya Tanzania haitakuwa na mamlaka ya kuona mkataba huo ni batili, hivyo wapingaji hao hawana mamlaka ya kuupinga.

Kuhusu hoja ya Kahoho kwamba Dowans isilipwe, Fungamtama alidai kuwa si ya msingi na haina mantiki kisheria, kwani tayari Mahakama ya ICC ilishatoa hukumu yake na ikaiamuru TANESCO kuilipa fidia Dowans, ikiwa ni hasara waliyoipata baada ya TANESCO kuvunja mkataba kinyume cha makubaliano.

Aidha, kuhusu mapingamizi ya LHRC, Lawyers Environment Team na Sikika Company Ltd, dhidi ya Dowans, kwanza Fungamtama alihoji uwezo wao kisheria, uwakilishi wao kwa watu wasiofahamika kama walivyodai kuwa wanawawakilisha wananchi na kuongeza kuwa hawana sababu ya kisheria ya kusema kuwa wao ni wawakilishi wa wananchi wanaopinga tuzo hiyo isisajiliwe na kulipwa.

Wakili Fungamtama alidai kuwa walalamikaji hao walikosea kutaja kiwango cha tuzo aliyoshinda mteja wake. Tuzo aliyoshinda mteja wake ni dola za Marekani 65,812,630.33 na si dola 123,223,270.98 kama walivyoainisha kwenye hati yao ya madai na kuongeza kuwa si kwamba mkataba ulioingiwa na TANESCO na Dowans hauwabani .

Baada ya mahakama kupokea mapingamizi hayo ya Dowans, iliitaka TANESCO ijibu pingamizi lililowekwa dhidi yake na Dowans Mei 27, mwaka huu.

Kadhalika LHRC na Kahoho nao wajibu mapingamizi waliyowekewa na Dowans Mei 20 mwaka huu, na kwamba majibu yote hayo yajibiwe kwa njia ya maandishi na akaiahirisha kesi hiyo hadi Julai 28 mwaka huu, ambapo kesi hiyo itakuja kwa ajili ya kutajwa.

Januari 25 mwaka huu, Dowans iliwasilisha ombi lake la kutaka Mahakama Kuu ya Tanzania iisajili tuzo waliyopewa na Mahakama ya ICC na siku chache baadaye TANESCO, LHRC na Kahoho wakawasilisha hati ya nia ya kupinga ombi hilo la kutaka tuzo hiyo isajiliwe.

Mahakama ya ICC, ilitoa hukumu ya kesi ya Dowans dhidi ya TANESCO, Novemba 15 mwaka jana, ambapo mahakama iliitia hatiani TANESCO kwa kosa la kuvunja mkataba na Dowans na ikaiamuru iilipe fidia ya shilingi bilioni 94, hukumu ambayo imezua mjadala mkali hapa nchini kuanzia kwa viongozi wa serikali, vyama vya siasa na makundi mengine, ambapo wengine wanataka Dowans ilipwe huku wengine wakitaka kampuni hiyo isilipwe.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Aprili 7 mwaka 2011.

KESI YA N'GUMBI,MNYIKA KUSIKILIZWA APRIL 8

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Ijumaa ya wiki hii itasikiliza ombi dogo la aliyekuwa mgombea Ubunge wa Jimbo la Ubungo kwa tiketi ya (CCM) la kuomba mahakama hiyo impatie msamaha wa kutolipa sh.milioni 15 kama dhamana ya kesi yake ya kupinga ubunge wa mbunge wa Jimbo la Ubungo(CHADEMA), John Myika.


Ng’umbi katika kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ambayo yalimtangaza Mnyika kuwa mshindi, ana mshtaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali, John Mnyika na aliyekuwa Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo ambapo Mnyika anatetewa na wakili wa kujitegemea Edson Mbogoro. Ng’umbi alifungua kesi Na.107/2010 Machi 22 mwaka huu, akitaka mahakama hiyo itengue ushindi wa Mnyika kwasababu sheria ya Uchaguzi ilikiukwa.

Msajili wa wilaya ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salam , Amir Msumi aliyasema hayo jana wakati kesi hiyo ilipokuja kwaajili ya kutajwa na akasema tayari uongozi wa kesi hiyo umeishampanga jaji wa kuisikiliza kesi hiyo na kwamba kesi hiyo itasikilizwa na Jaji Upendo Msuya.

Juzi Mnyika aliwasilisha pingamizi mahakamani hapo dhidi ya ombi hilo dogo la mlalamikaji(Ng’umbi) la kutaka asamehewe kiasi hicho cha fedha , ambapo aliomba mahakama hiyo itupilie mbali ombi la mlalamikaji kwasababu mlalamikaji ana jiweza kiuchumi hiyo anauwezo wa kulipa kiasi hicho cha fedha kama sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2002 inavyomtaka mlalamikaji katika kesi ya uchaguzi kuweka mahakamani shilingi milioni tano kwa kila mdaiwa anayemshtaki.

Mnyika katika pingamizi hilo ambalo Tanzania Daima linalo nakala yake anadai kuwa sababu nyingine ya kuwasilisha pingamizi dhidi ya Ng’umbi ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Wilaya ya Bukombe ni kwamba ombi hilo la msamaha mlalamikaji ameshindwa kutaja sababu zinazoonyesha yeye hana uwezo wa kulipa kiasi hicho cha fedha.

“Tena tunaomba mahakama kuu ilitupe ombi kwasababu naamini huyu mlalamikaji kwanza alishawahi kuwa mkuu wa wilaya ya Mvomero na sasa ni Mkuu wa Wilaya ya Bukombe na ana vyeo vingine hivyo.... ana uwezo wa kiuchumi ambao unamruhusu kulipa mahakamani dhamana hiyo hivyo naomba mahakama hii tukufu isikubali huo msamaha wake kwasababu naamini anao uwezo wa kulipa kiasi hicho cha fedha.”alidai Mnyika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Aprili 6 mwaka 2011.

FEDHA ZA MISAADA ZISIVURUGE WANATAALUMA


Na Happiness Katabazi

HABARI za mtandao wa Wiki leaks zinazosema kwamba fedha za Marekani za Millennium Challenge Account zimekuwa zikitumika kuiwezesha Taasisi ya Kuzia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kutekeleza mpango wake wa kufungua kesi zenye mvuto kwa waandishi wa habari na vyombo vya habari kila siku; ni jambo la kushangaza na kutia aibu.


Katika mfumo wa jamii ya Kidemokrasia na Utawala Bora huzingatia mgawanyo wa madaraka baina ya mihimili mitatu ambayo ni Serikali, Bunge na Mahakama.Takukuru ni chombo cha serikali kilicho chini ya Ofisi ya Rais.

Inapotokea habari iliyojaa tuhuma kwamba chombo hicho kina mkakati wa kuwaburuza mahakamani baadhi ya wananchi, ni kashfa kubwa na uonevu wa hali ya juu.

Tunapozungumzia ufisadi, tunamaanisha uozo ndani ya serikali basi kitendo hicho ni cha kifisadi, udhalimu na kwa maana hiyo endapo chombo cha serikali cha ufisadi na uonevu kwa baadhi ya raia wetu wasiyo na hatia, ina maana kwamba baadhi ya kesi tunazosikia na kuziona si kesi zilizofanyiwa uchunguzi makini.

Ni kesi za kubambikiza ili tupate sifa Marekani na nchi nyingine.

Hivi sasa kumekuwa na tuhuma zinazotolewa chinichini na wanataaluma ya sheria nchini kuwa baadhi ya vigogo serikalini wamekuwa wakitoa maelekezo kwa baadhi ya mahakimu na majaji wetu kuamua kesi kwa kupendelea upande wa Jamhuri.

Kwa maana hiyo tuhuma hizo ambazo zimedhirisha katika mtandao wa Wiki leaks hivi karibuni zimetuambia kwamba mahakamani siku hizi si shwari tena.

Ile imani tuliyokuwa nayo kwamba mahakama ni hekalu la haki sasa haina msingi tena wa kuegemea.

Ikiwa ni kweli baadhi ya majaji na mahakimu wetu wanaelekezwa au kushawishiwa na serikali angalau kuwatia hatiani katika mahakama za chini ili waje kuachiliwa kwenye rufaa.

Kutokana na kuwepo kwa taarifa za mtandao huo hivi karibuni, serikali yetu haijazikanusha hadi sasa kwamba fedha za Millennium Challenge Account zinatumika nchini kwa minajili ya kidhalimu.

Kwa kuwa serikali ya Marekani haijakanusha pia tuhuma hizo, sisi tumebakiwa midomo wazi kuhusu Uhuru wa Mahakama zetu na kuhusu mustakabali wa utawala bora nchini.

Tuna historia ya muda mrefu ya kuwa na Takukuru lakini hakuna kipindi cha historia cha taasisi hiyo kuwa na manung’uniko ya uonevu, ubambikiaji kesi kama kipindi hiki.

Kwa namna ya pekee wakati mwingine tunaona Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, nayo imekuwa ikituhumiwa chini chini kuwa imebaki kuwa kituo cha kupitisha maamuzi ya mashtaka yaliyokwisha chukuliwa na ngazi za juu serikalini badala ya maamuzi hayo kuchukuwaliwa kwa misingi ya kitaaaluma.

Tumeona jinsi baadhi ya waliokuwa watuhumiwa wa wizi wa fedha katika Akaunti ya Madeni ya Nje(EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania(BoT), walivyoshughulikiwa kwani kuna wengine walipewa msamaha kabla ya kushtakiwa eti kwasababu walirudisha fedha na wengine wakaburuzwa pale Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Sasa kwa mktadha huo kuna uchaguzi wa nani ashtakiwe na nani asishtakiwe wakati wote walituhumiwa kuvunja sheria za nchi kama hao walioshtakiwa mahakamani.

Kamwe hakutufanyi tuheshimu baadhi ya taasisi zetu za seriakali kwa kuwa inaonyesha wazi zimehusika katika udhalimu huo.

Fukuto la Jamii linahitimisha kwa kusema kama tuhuma hizo zilizotandazwa kwenye mtandao huo, na zile zinazotolewa na baadhi ya mawakili wa kujitegemea na maofisa wengine wa serikali kwamba kuna baadhi ya kesi zinafunguliwa kwaajili ya vigogo fulani kulipiza kisasi na kwamba katika kesi hizo ofisi ya DPP na baadhi ya majaji na mahakimu waoga wanakuwa wanashindwa kutenda haki kwa ajili ya kuogopa vitisho.

Basi makundi hayo yote hayana budi kuondokana na udhalimu huo kwani wakumbuke vyeo ni dhamana na walipokuwa vyuoni wanasoma sheria hawakufundishwa kuonea watu kwa ajili ya kuwafurahisha waliowateua au kupokea rushwa.

Licha baadhi ya mawakili wa kujitegema kuwa miongoni mwao nao wamekuwa wakilalamikiwa na baadhi ya mawakili wa serikali kuwa wamekuwa wakikwamisha kesi zinazofunguliwa na Jamhuri kwa makusudi kwa kuwasilisha pingamizi mahakamani kila kukicha ili waweze kukata ngebe ya ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Eliezer Feleshi na Takukuru kwa madai kwamba ofisi hizo zimekuwa zikitumiwa na serikali kuwabambikizia kesi baadhi ya wateja wao ili serikali ionekane haifanyi kazi.

Lakini kwa kufanya hivyo ni kuendelea kuwachochea baadhi ya wananchi waendelee kuichukia serikali yao na mahakama.

Na ikumbukwe kuwa mwananchi yoyote anayeamini amedhurumiwa haki yake kimbilio lake ni mahakamani.

Lakini kwa watu wenye akili timamu huwa tunajiuliza hivi huo udhalimu wote unaofanywa na baadhi ya wanataaluma ya sheria na wapelelezi una tija gani kwa taifa hili?

Binafsi naona hauna tija kwa taifa letu hata kidogo zaidi ni kujenga taifa la wananchi wenye wenye moyo wa visasi na kuleteana umaskini kwenye familia.

Kila mwanataaluma atimize wajibu wake kwa mujibu wa maadili ya kazi yake na asikubali kutumiwa vibaya kwani vitabu vya dini vinatueleza kuwa Mungu yupo; na kesho kwa Mungu kuna moto kwa wale wote wanaokwenda kinyume na matakwa yake.

Hivyo mhimili wa mahakama nao hauna budi kujiondoa katika kashfa za tuhuma hizo kwani ningali nikikumbuka wosia uliotolewa na Rais Jakaya Kikwete, katika Siku ya Sheria nchini iliyofanyika Februari 2 mwaka huu katika Viwanja vya Mahakama Kuu, aliitaka mahakama ijisafishe kwani ndani ya mhimili huo kuna baadhi ya mahakimu na majaji wanatuhumiwa kukiuka maadili ya kazi yao na viapo vyao.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

0716 774494
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Aprili 5 mwaka 2011.

MNYIKA APINGA N'GUMBI KUSAMEHEWA ADA YA KESI

Na Happiness Katabazi

MBUNGE wa Jimbo la Ubungo kwa tiketi ya (CHADEMA), John Mnyika ameiomba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kutupilia mbali ombi la mlalamikaji katika kesi ya kupinga ubunge wake Hawa Ng’umbi(CCM) linalotaka mahakama hiyo impatie msamaha wa kutolipa Sh milioni 15 kama dhamana ya kesi aliyoifungua kwasababu hana uwezo wa kulipa kiasi hicho.


Ng’umbi katika kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ambayo yalimtangaza Mnyika kuwa mshindi, ana mashtaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali, John Mnyika na aliyekuwa msimamizi wa uchaguzi wa jimbo hilo ambapo Mnyika anatetewa na wakili wa kujitegemea Edson Mbogoro.

Kwa mujibu ya Mnyika ambayo anapinga ombi hilo la mlalamikaji(Ng’umbi) la kutaka asamehe kulipa kiasi hicho ambayo yamewasilishwa Mahakama Kuu na wakili wake Mbogoro, Mnyika ametaja sababu tano za kutaka ombi hilo likataliwe kwasababu mlalamikaji huyo katika maombi yake hajataja sababu zinazoonyesha yeye hana uwezo wa kulipa kiasi hicho cha fedha.

“Tena tunaomba mahakama kuu ilitupe ombi kwasababu naamini huyu mlalamikaji kwanza ni Mkuu wa Wilaya ya Bukombe na ana vyeo vingine hivyo ana uwezo wa kiuchumi ambao unamruhusu kulipa mahakamani gharama hiyo ya fedha ….hivyo tunaiomba mahakama hii tukufu isikubali huo msamaha wake wa kukataa kulipa kiasi hicho cha fedha kwakuwa ana uwezo wa kulipa gharama hiyo”alidai Mnyika.

Kesi hiyo inakuja leo kwaajili ya kutajwa mbele ya Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.Ng’umbi ambaye naye alikuwa ni mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM, alifungua kesi hiyo Na.107/2010 Machi 22 mwaka huu, akitaka mahakama hiyo itengue ushindi wa Mnyika.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Aprili 5 mwaka 2011.