MATUKIO MAKUBWA MAHAKAMANI 2011




Na Happiness Katabazi

Kwa mara nyingine siku ya leo ambayo ni siku ya mwisho ya kufunga mwaka huu, Mwandishi wa Habari za Mahakama wa gazeti hili amekuandalia matukio makubwa yaliyotikisa katika baadhi za mahakama hapa nchini ungana nae kwa simulizi zaidi.


Desemba 27
Kafulila arejeshewa ubunge


Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Alise Chinguile amesikiliza na kutoa amri ya kukizuia chama cha NCCR-Mageuzi, kusitisha utekelezaji zaidi wa maazimio ya kikao chake cha Halmashauri Kuu kilichoketi Desemba 17 mwaka huu, ambacho kilimvua uanachama mbunge wa Kigoma Kusini kwa tiketi ya chama hicho, David Kafulila hadi pale kesi ya msingi iliyofunguliwa na mbunge huyo itakapotolewa uamuzi.Na kesi ya msingi itatajwa mbele ya Jaji.

Desemba 23
Kafulila afungua kesi kupinga kufukuzwa uanachama


David Kafulila afungua kesi ya madai Na. 218/2011 ya kupinga uamuzi wa kikao cha NEC cha Desemba 17 kilichomvua uanachama na pia akawasilisha ombi dogo chini ya hati ya dharula lilotaka mahakama hiyo itoe amri ya kuzuia utekelezwaji zaidi wa azimio la kikao hicho cha NEC.

Desemba 21
Kibanda afikishwa kizimbani


Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima, Absalom Kibanda afikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam mbele ya Hakimu Mkazi Stewart Sanga , akikabiliwa na kosa la uchochezi na alikana shtaka na yupo nje kwa dhamana.

Hii ni mara ya kwanza kwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imfungulie kesi ya uchochezi mwandishi wa habari na Mhariri kwa madai kuandika na kupitisha makala inayodaiwa kuwa ni ya kichochezi.

Desemba 14
Kesi ya Mramba bado hakieleweki


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam imesema kuwa mwendo wa kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya shilingi bilioni 11.7 inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha Basil Mramba na wenzake bado haujakamilika.

Jaji John Utamwa anayesaidiwa na Hakimu Mkazi Sam Rumanyika na Saul Kinemela alisema kesi hiyo ilikuja jana kwaajili ya kutajwa na kuangalia kama mwenendo wa kesi hiyo umekamilika lakini amebaini mwenendo wa kesi hiyo ambao ulishachapwa una makosa.

Desemba 8 mwaka huu,
Mwandishi Kortini kwa uchochezi


Mwandishi wa Safu ya ‘Kalamu ya Mwigamba’ ambayo inachapishwa kila siku ya Jumatano na gazeti la Tanzania Daima, Samson Mwigamba (36) alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na kosa moja la kuandimakala inayowashawishi maaskari na maofisa wa majeshi ya hapa nchini kuacha kuitii serikali iliyopo madarakani kwa sasa.

Wakili Mwandamizi wa Serikali Elizabeth Kaganda mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema alidai mshtakiwa huyo anakabiliwa na kosa moja la kuwashawishi askari na maofisa wa jeshi la polisi, magereza na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania(JWTZ) kutoendelea kuitii serikali iliyopo madarakani kwa sasa ambayo inaongozwa na Rais Jakaya Kikwete kinyume na kifungu cha 46(b),55(10(a) na 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Wakili Kaganda alidai Novemba 30 mwaka huu,gazeti la Tanzania Daima la siku hiyo toleo Na.2553 lilichapisha waraka uliokuwa na kichwa cha habari kisemacho “Waraka Maalum kwa Askari wote” ambao uliandikwa na mshtakiwa huyo kupitia safu yake ijulikanayo kwa jina la ‘Kalamu ya Mwigamba’.

Wakili huyo wa serikali alidai kuwa mshtakiwa huyo kupitia walaka wake huo kwa makusudi na kwa nia kuvunja sheria za mamlaka ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliwashawishi askari na maofisa wa jeshi la polisi, Magereza na JWTZ kutoendelea kuiiti serikali iliyopo madarakani.

Hata hivyo mshtakiwa huyo anayetetewa na Edson Mbogoro alishindwa kutimiza masharti ya dhamana na akarudishwa rumande hadi Desemba 20 mwaka huu, ambapo kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya kutajwa.

Hii ni mara ya kwanza kwa Tanzania kumfungulia kesi ya kushawishi au uchochezi mchangiaji wa makala kwenye magazeti ya hapa nchini. Pia hii itakuwa ni mara ya pili kwa serikali kumfungulia kesi ya jinai Mwigamba tangu mwaka huu ulipoanza.

Kwani Mwigamba na Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu Dk.Wilbroad Slaa , mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini Godbless Lema na Mbunge wa Moshi Mjini Philemon Ndesamburo na wanachama wengine wanakabiliwa na kesi ya mkusanyiko na maandamano haramu waliyoyafanya Januari 5 mwaka huu, katika jiji la Arusha na kesi hiyo ipo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha na imefikia hatua ya kuanza kusikilizwa.

Desemba 5 mwaka huu
Upelelezi kesi ya Mattaka tayari


Upande wa Jamhuri katika kesi ya matumizi mabaya ya madaraka na kununua magari ya mitumba kinyume na Sheria ya manunuzi ya umma ya mwaka 2004 inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Shirika la Ndege(ATCL), David Mattaka na wenzake umeileza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.


Wakili Mwandamizi wa Serikali Oswald Tibabyemokya alieleza hayo mbele ya Hakimu Mkazi Ritha Tarimo wakati kesi hiyo jana ilipokuja kwaajili ya kutajwa ambapo alieleza kuwa upelelezi huo umekamilika.Hakimu Tarimo alisema anaiarisha kesi hiyo hadi Januari 5 itakapokuja kwaajili ya kutajwa na kwamba usikilizwaji wa awali utafanyika Januari 23 mwaka 2012.

Desemba 5 mwaka huu
Meja JWTZ kortini kwa utapeli


Meja wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kikosi cha 511 cha Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam, Muhsini Kombo (39) na Devotha Soko (33), jana walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kwa tuhuma ya kujipatia sh milioni 100 kwa njia ya udanganyifu.

Mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema, wakili wa Serikali, Ladslaus Komanya, alidai katika shitaka la kwanza kuwa Kombo pamoja na Devotha Soko walikula njama na kughushi kati ya Januari-Machi mwaka 2008 na kwa nia ya udanganyifu washitakiwa walighushi mhutasari wa kikao cha Machi 25 mwaka 2008 na kujaribu kuonesha kuwa familia ya marehemu Awadhi Shoo imemteua Devotha Soko kuwa msimamizi wa mirathi.

Desemba 2
Mawakili wa Liyumba wakwamisha kesi


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jana ilijikuta ikishindwa kuanza kusikiliza pingamizi la awali lililotarajiwa kuwasilishwa na mawakili wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba (63), anayekabiliwa na kesi ya kukutwa na simu gerezani kwa sababu ya mawakili hao kutokuwepo mahakamani bila kutoa taarifa rasmi.

Novemba 30
Jerry Murro ashinda kesi


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, imemwachilia huru aliyekuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC 1), Jerry Murro (30) na wenzake ambao ni Deogratius Mugassa na Edmund Kapama ambao walikuwa wakikabiliwa na makosa ya kula njama na kuomba rushwa ya sh milioni 10 toka kwa aliyekuwa Mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Wage baada ya upande wa Jamhuri kushindwa kuthibitisha mashitaka yao.

Novemba 17
Shahidi:Mintanga hakustahili kushtakiwa kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya


Shahidi wa nne upande wa Jamhuri katika kesi ya kula njama na kusafirisha dawa za kulevya Kilo 4.8 inayomkabili aliyekuwa Rais wa Shirikisho la Ngumi la Ridhaa Tanzania (BFT), Alhaji Shaban Mintanga, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP), Charles Ulaya amedai mshtakiwa huyo alistahili kushtakiwa kwa kosa moja tu la kula njama na siyo kosa la kusafirisha dawa hizo.

Novemba 16
Maranda afunguliwa kesi mpya


Kada wa Chama cha Mapinduzi(CCM), Rajabu Maranda jana alifikishwa tena katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na kesi mpya ya kugushi na kujipatia ingizo la jumla ya Sh bilioni 5.9 toka Benki Kuu ya Tanzania, mali ya benki hiyo kinyume cha sheria.

Novemba 21
Washtakiwa ‘kesi ya samaki wa magufuli’ wamaliza kujitetea


Washtakiwa watano raia wa China wanaokabiliwa na kesi ya uvuvi haramu katika ukanda wa Tanzania kwa kutumia meli ya Tawariq 1 maarufu kama ‘Kesi ya Samaki wa Magufuli’ wamemaliza kujitetea katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.Washtakiwa hao Hsu Chin Tai, Zhao Hanguing, Hsu Shang Pao, Ca’ Dong Li na Chen Rui Hai wanatetewa na mawakili wa kujitegemea Ibrahim Bendera na John Mbele mbele ya Jaji Agustine Mwarija.Novemba 14, mwaka huu, washtakiwa hao walijitetea kwa lugha ya Kichina na kusaidiwa na mkalimani Mtanzania; walisema: “Mheshimiwa Jaji wateja wetu hao watano wamemaliza kujitetea na tumeona utetezi wao unatosha hivyo hatuhitaji kuleta mashahidi ili waje kuwatetea na kwa hiyo upande wa utetezi katika kesi hii tumefunga ushahidi wetu na tunaiachia mahakama.

Novemba 28
Waziri aongeza muda kesi ya Mbatia, Mdee


Hatimaye Waziri wa Katiba na Sheria Celina Kombani ameongeza muda wa miezi sita kuanzia jana katika kesi ya kupinga matokeo yaliyomtangaza mbunge wa Jimbo la Kawe, Halima Mdee(Chadema), kuwa mshindi kama alivyokuwa ametakiwa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kuongeza muda huo.

Kesi hiyo ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu mwaka 2010 iliyofunguliwa na aliyekuwa Mgombea Ubunge kwa tiketi ya (NCCR-Mageuzi), James Mbatia anayetetewa na wakiliwa Mohamed Tibanyendera dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mdee na Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Kawe.

Novemba 16
Hakimu azuia waandishi kuripoti kesi ya wanafunzi UDSM


Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Waliarwande Lema kwa mara ya pili jana aliendelea tabia yake kwa kuwazuia waandishi wa habari toka vyombo mbalimbali vya wasiingie kusikiliza kesi ya kufanya mkusanyiko usio halali inayowakabili wanafunzi 50 wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.Kesi hiyo ambayo jana ilikuja kwaajili wanafunzi 41 kati ya 50 kuja kupatiwa dhamana na hakimu huyo, ambapo waandishi hao wa habari walifika mahakamani hapo tangu saa mbili asubuhi na kuhudhuria kesi mbalimbali lakini ilipofika saa 6.30 mchana wanafunzi hao waliingizwa kwenye ofisi ya hakimu Lema kwaajili ya kuanza kutimiza masharti ya dhamana

Novemba 18
Kesi ya Mpendazoe, Mahanga kuanza kusikilizwa Machi 2


Hatimaye Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imesema kuwa Machi 2-Aprili 13 mwakani itaanza kusikiliza mfululizo kesi ya kupinga matokeo ya Ubunge wa Mbunge wa Jimbo la Segerea(CCM), Dk.Makongoro Mahanga.

Kesi hiyo ya uchaguzi ilifunguliwa mahakamani hapo mwaka jana na aliyekuwa mgombea ubunge wa jimbo hilo la Segerea kwa tiketi ya Chama cha Maendeleo na Demokrasia(CHADEMA), Fred Mpendazoe anayetetewa na wakili Peter Kibatara dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali(AG), Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo ambao wanatetewa na wakili wa serikali David Kakwaya na Dk.Mahanga ambaye ni Naibu Waziri wa Kazi na Ajira anayetetewa na wakili wa kujitegemea Jerome Msemwa, kwa madai kuwa taratibu za uchaguzi zilikiukwa na wanaiomba mahakama itengue matokeo yalimtangaza Mahanga kuwa mshindi.

Novemba Mosi
Mnyika akanusha madai ya Ng’umbi


MBUNGE wa Jimbo la Ubunge kwa tiketi ya chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA), John Mnyika ameiomba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, itupilie mbali hati ya madai iliyofanyiwa marekebisho na aliyekuwa mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya (CCM), Hawa Ng’umbi kwa madai kuwa tuhuma zilizoelekezwa kwake na Ng’umbi ni za uzushi na hazina ushahidi.

Katika kesi hiyo ya madai ya Na.107/2010 ,iliyopo mbele ya Jaji Upendo Msuya , Ng’umbi anayetetewa na wakili wa kujitegemea Issa Maige,anamshtaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Msimamizi wa uchaguzi wa jimbo la Ubungo na Mnyika, ambapo anadai Sheria ya Uchaguzi ilikiukwa katika uchaguzi huo na kwamba mwanasheria mkuu wa serikali na msimamizi wa uchaguzi jimbo hilo walishindwa

Oktoba 28
Jerry Murro ana hatia-Serikali


Upande wa Jamhuri uliwaowakilishwa mwanzo hadi mwisho wa kesi hii na Mkurugenzi Msaidizi katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini, Stanslaus Boniface uliwasilisha majumuisho yao kwa njia ya maandishi ambayo yalimuomba Hakimu Mkazi Frank Moshi amuone Murro na wenzake wanahatia.

Oktoba 28
Mdee akwaa kisiki kortini


Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetupilia mbali pingamizi lilowekwa na Mbunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA),Halima Mdee lililokuwa likitaka hati ya madai katika kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu mwaka 2010 iliyofunguliwa na aliyekuwa Mgombea Ubunge kwa tiketi ya (NCCR-Mageuzi), James Mbatia ifanyiwe marekebisho kwa maelezo kuwa haina msingi wa kisheria.

Uamuzi huo ulitolewa na Jaji John Utamwa ambaye baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili alifikia uamuzi wa kukubaliana na hoja za wakili wa mlalamikaji, Mohamedi Tibanyendela aliyetaka pingamizi hilo litupwe na mahakama.

“Hivyo mahakama hii haikubaliani na pingamizi la mdaiwa anayetetewa na Wakili Edson Mbogoro anayetaka hati ya madai ifanyiwe marekebisho kwa vile hawezi kujibu baadhi ya tuhuma alizotuhumiwa nazo kwasababu zinamkera, kumtia kichefuchefu…..kwa hiyo mahakama hii leo inasema tuhuma hizo hazikeri wala kutia kichefuchefu hivyo ina muamuru mdaiwa kuzijibu na inatupilia mbali pingamizi la mdaiwa”alisema Jaji Utamwa.

Oktoba 25
Kesi ya Jeetu Patel dhidi ya Mengi yatupwa


Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imeifuta kesi ya Kikatiba iliyofunguliwa na mfanyabiashara Jayantkumar Chandubai ‘Jeetu Patel’ na wenzake watatu dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi na Mkurugenzi wa Mashtaka(DPP) kwa maelezo kuwa kesi hiyo haina mantiki ya kisheria na Kikatiba.

Uamuzi huo wa kesi hiyo Na. 30/2009 ulitolewa jana asubuhi na jopo la majaji watatu Jaji Kiongozi wa Fakihi Jundu, Semistocles Kaijage na Profesa Ibrahim Juma ambao walisema licha wanaifuta kesi hiyo kwa sababu haina mantiki ya kisheria, pia walisema madai ya Patel kuhusu tamko la Mengi alilolitoa Aprili 23 mwaka 2009 kwa vyombo vya habari kuwa yaliingilia uhuru wa Mahakama Mkazi Kisutu na kuidharau mahakama hiyo kwa kuwa hukumu walalamikaji ambao wanakabiliwa na kesi nne za EPA kupitia vyombo vya habari kuwa ni ‘Mafisadi Papa’ yalipaswa yapelekwe katika mahakama hiyo ya chini kwani mahakama za chini zimepewa nguvu za kuwaadhibu wale wote wanaotenda makosa ya kuidharau mahakama na endapo uamuzi wa mahakama hiyo ya chini asingelidhika nao ndiyo Jeetu Patel angekatia rufaa uamuzi huo wa mahakama ya Kisutu katika Mahakama Kuu.
Oktoba 21
Jerry Murro hana hatia-Mawakili
Upande wa utetezi unaowakilishwa na mawakili wa kujitegemea Rweyongeza, Majura Magafu katika kesi inayomkabili Jerry Murro na wenzake uliwasilisha majumuisho yao kwanjia ya maandishi na kuiomba mahakama iwaachilie huru washtakiwa hao kwasababu hawana hatia kwani ushahidi ulioletwa na Jamhuri ni wa kuunga unga na hautoshelezi kuishawishi mahakama kuwatia hatiani.

Oktoba 23
Mbunge CCM kizimbani
Mbunge wa Nzega mkoani Tabora, Dk. Hamisi Kigwangalla (CCM) amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Nzega, akikabiliwa na mashitaka sita, yakiwemo ya kuvamia kituo cha Polisi wilayani Nzega.

Oktoba 10
Mbunge kortini, atupwa rumande
Mbunge wa Mbarali, Modest Kilufi (CCM) amewekwa rumande katika Gereza la Ruanda jijini hapa baada ya kunyimwa dhamana na Mahakama ya Mkoa wa Mbeya.

Alinyimwa dhamana hiyo na Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Michael Mteite, Kilufi (51), baada ya kufikishwa hapo akikabiliwa na mashitaka ya kutishia kumuua Mtendaji wa Kata ya Ruiwa wilayani Mbarali, Jordan Masweve (28).

Mbunge huyo alisomewa mashitaka na mawakili wa Serikali, Griffin Mwakapeje na Basilius Namkambe mbele ya Hakimu Mteite na kudaiwa kutishia kuua Machi 16, mwaka huu katika maeneo ya Ubaruku wilayani Mbarali.

Oktoba 19
Watuhumiwa wa mauji waachiwa
Mwekezaji wa Hoteli ya South Beach ya Kigamboni, Salim Nathoo ‘Chipata’ (53), na wenzake waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya kijana Lila Hussein (25), wameachiwa huru kufuatia Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP) Eliezer Feleshi kuwasilisha hati ya kuiondoa kesi hiyo mahakamani.

Nathoo aliyeshtakiwa pamoja na Meneja wake Bhushan Mathkar na John Mkwanjiombi (32) waliachiwa wiki hii na Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Temeke, Kassim Mkwawa.

Mwendesha mashtaka katika kesi hiyo, Dunstun Kombe, aliliambia Tanzania Daima kwamba amri ya kuachiwa huru kwa watuhumiwa hao ilitolewa Oktoba 10 na DPP kwa kutumia kifungu 91 (1) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai ya mwaka 2002, inayompa madaraka ya kuondoa kesi mahakamani ikiwa ataona ushahidi wa kesi husika hautoshelezi bila kuhojiwa na mtu wala taasisi yoyote.


Oktoba 20
Serikali yajichanga kesi ya Mahalu


Katika hali isiyotarajiwa jana upande wa Jamhuri katika kesi ya uhujumu uchumi wa zaidi ya Euro milioni mbili, inayomkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Dk.Costa Mahalu na Grace Martin ilijikuta ikitoa mpya baada ya kuieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa imepata nyaraka halisi za mawasiliano yaliyokuwa yakifanywa kati ya mshtakiwa huyo na serikali wakati hapo awali upande wa Jamhuri ulidai kuwa hauna nyaraka hizo.

Kesi hiyo ambayo jana ilikuwa imekuja kwaajili ya kuendelea kusikilizwa ambapo Wakili Mwandamizi wa Serikali Ponsia Lukosi alikuwa anatarajiwa kuja kuieleza mahakama amebaini nini kwenye zile nyaraka 11 zilizotolewa juzi na Mahalu ambaye aliomba mahakama hiyo izipokee kama vielelezo lakini wakili huyo wa serikali aliomba mahakama kabla ya kuvipokea kesi hiyo iarishwe hadi jana ili upande wa Jamhuri uweze kupata nafasi ya kuzipitia nyaraka hizo.

Oktoba 18
Mahalu afichua bei ya ununuzi jengo la Ubalozi, Rome Italia

Aliyekuwa balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa ripoti ya bei ya ununuzi wa jengo la Ubalozi wa Tanzania mjini Roma aliyokuwa ameipendekeza yeye ilikuwa ni ya bei ya chini ukilinganisha na ripoti ya ununuzi wa jengo hilo iliyokuwa imependekezwa na serikali kupitia Wizara ya Ujenzi.

Oktoba 4
Washtakiwa kesi ya Jerry Murro wamaliza kujitetea


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilitoa amri ya kuzitaka pande zote mbili katika kesi ya Jerry Murro iliyotolewa na Hakimu Moshi, Oktoba 4 mwaka huu, ambapo siku hiyo alizitaka pande zote kufanya hivyo.

Na siku ndiyo shahidi wa Murro alitoa ushahidi wake na washtakiwa wawili Deogratius Mugassa na Edmund Kapama nao walitoa utetezi wao na siku hiyo hiyo wakili wa utetezi Richard Rweyongeza aliambia mahakama kuwa huo ndiyo mwisho wa ushahidi wao.

Na kabla ya washtakiwa hao kuanza kutoa utetezi wao wakili wa serikali , Boniface aliwasilisha ombi la kutaka kubadilisha hati ya mashtaka ambapo ombi hilo lilikubaliwa na hakimu huyo ambapo alisema kuanzia siku hiyo hati ya mashtaka itasomeka kuwa washtakiwa waliomba rushwa Michael Wage Januari 29 mwaka jana katika hoteli ya Sea Cliff, tarehe ambayo inaoona na picha za CCTV ambazo zinawaonyesha washtakiwa hao walifika katika hoteli hiyo wakiwa na Wage.

Kabla ya kubadilisha hati hiyo,hati ya mashtaka ilikuwa ikisomeka kuwa washatkiwa hao walitenda kosa hilo Januari 28 mwaka jana, tarehe ambayo ilikuwa ikitofautiana na tarehe iliyokuwa ikionekana kwenye nakala ya picha ya CCTV kamera.

Novemba 14
Wanachuo UDSM 50 kortini kwa maandamano haramu


Jumla ya Wanafunzi 50 wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, wakikabiliwa na makosa mawili ya kufanya mkusanyiko usihalali na kukaidi amri ya Jeshi la Polisi liliwataka watawanyike.

Novemba 11
Mdogo wa Rostam Aziz kizimbani kwa dawa za kulevya

ASSAD Aziz Abdulasul ambaye ni mdogo wa mwanasiasa maarufu nchini, Rostam Aziz, anayetuhumiwa kusafirisha kilo 92.2 za dawa ya kulevya aina ya heroine yenye thamani ya sh bilioni 2, jana alifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama Kuu Kanda ya Tanga na kusomewa maelezo ya awali.

Mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tanga, Kipenka Mussa, wakili mwandamizi wa serikali Biswalo Mganga aliieleza mahakama hiyo kuwa kesi hiyo ya jinai Na.1/2011 ilikuja mahakamani hapo kwa mara ya kwanza jana ikitokea Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani Tanga kwa ajili ya maandalizi ya kuhamishiwa katika mahakama hiyo ya juu ambayo ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo na jana upande wa jamhuri uliwasomea washtakiwa hao maelezo ya awali.

Wakili wa mganga aliwataja washtakiwa hao mbali na Assad kuwa ni Kileo Bakari Kileo, Yahya Makame, Mwamadali Podadi ambaye ni raia wa Iran, Salum Mparakesi, Saidi Ibrahim Hamis na Bakari Kileo ‘Mambo’ ambao wanatetewa na mawakili wa kujitegemea Richard Rweyongeza na Edward Chuwa.

Akiwasomea maelezo hayo ya awali, Wakili Mganga alieleza kuwa washtakiwa wote kwa pamoja kati ya Januari mwaka 2009 hadi Machi 8 mwaka 2010 walikula njama na kusafirisha kiasi hicho cha dawa za kulevya na kuziingiza nchini.

Septemba 28
Dowans yaibwaga Tanesco


Jitihada za wanasiasa na wanaharakati kulizuia Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO), kulipa tuzo ya mabilioni ya shilingi kwa Kampuni ya kufua umeme, Dowans Tanzania, zimegonga mwamba baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam kutoa uamuzi wa kuiruhusu Dowans kusajili tuzo hiyo ili ilipwe.
Katika hukumu hiyo aliyoanza kuisoma kuanzia saa 3:31 asubuhi hadi 6:53 mchana, Jaji Mushi alisema kesi hiyo ya madai Na. 8/2011 iliyofunguliwa na TANESCO dhidi Dowans Tanzania, ilikuja kwake ili atoe hukumu ya ama kuiruhusu Dowans kusajili au kutokusajili tuzo hiyo. TANESCO katika pingamizi lake iliwasilisha sababu 12 za kupinga tuzo hiyo isisajiliwe.

Jaji Mushi alianza kwa kusema maneno yafuatayo:

“Kwanza, naishukuru TANESCO na zile taasisi nne za wanaharakati waliokuwa wakiongozwa na LHRC; walijitokeza mahakamani hapa kupinga tuzo ya Dowans isisajiliwe na kutumia muda wao kuchambua kesi mbalimbali na kuandaa mapingamizi yao, ambayo hata hivyo niliyatupilia mbali.

“Pili, nafahamu fika kuwa kesi hii ya Dowans ina sayansi nyingi sana za kisiasa, hivyo napenda niwafahamishe mapema kabisa kabla ya kuendelea kuwa hukumu yangu nitakayotoa leo haijatoa nafasi kwa sayansi hizo za kisiasa, kwa sababu imezingatia misingi ya sheria na haki.”

Jaji Mushi alisema miongoni mwa sababu zilizowasilishwa na mlalamikaji (TANESCO) za kutaka tuzo ya Dowans isisajiliwe ni pamoja na majaji wa Mahakama ya ICC kuipendelea Dowans, hukumu yake kuwa na upungufu wa kisheria, hukumu kutofuata sera na maslahi ya taifa na Mahakama Kuu ya Tanzania kutokuwa na mamlaka ya kuisajili tuzo hiyo. Dowans ilikuwa inatetewa na Wakili Kennedy Fungamtama, huku TANESCO ikitetewa na Kampuni ya uwakili ya Rex Attorney. Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali iliwakilishwa na Naibu Mwanasheria Mkuu, George Masaju na Dk. Hawa Senare.

Septemba 23
Amatus Liyumba atoka gerezani

Hatimaye aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba (63) ametoka jela katika gereza la Ukonga jijini Dar es Salaam , alikokuwa akiishi baada ya kumaliza kutumikia adhabu ya kifungo cha miaka miwili gerezani.

Kwa mujibu wa taarifa za kuaminika toka ndani ya familia ya Liyumba, zililiambia Tanzania Daima jana kuwa Liyumba alitoka gerezani hapo jana saa 3:30 asubuhi bila ya kuwepo kwa vikwazo vyovyote.

Septemba 20
Hati ya Kesi ya Ng’umbi ina makosa

Aliyekuwa mgombea ubunge wa Jimbo la Ubunge(CCM), Hawa Ng’umbi ambaye ni ndiye mlalamikaji katika kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 yaliyomtangaza John Mnyika kuwa mbunge wa jimbo hilo, amekiri kuwa hati yake ya madai aliyoifanyia marekebisho ina makosa ya kisheria na anaiomba mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imruhusu aende kuifanyia marekebisho.

Septemba 20
Wabunge Chadema wapanda kizimbani

Wabunge wawili na Mjumbe wa Baraza la Vijana la Chama cha (Chadema), wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Mkoa wa Tabora, wakikabiliwa na mashitaka manne likiwamo shambulio na kumshikilia Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Fatuma Kimario, kinyume cha sheria.

Waliofikishwa mahakamani hapo jana ni Mbunge wa Maswa Mashariki, Sylvester Kasulumbai, Mbunge wa Viti Maalumu, Suzan Kiwanga na Mjumbe wa Bavicha Wilaya ya Igunga, Anwar Kashaga. Watatu hao walifikishwa mahakamani hapo saa 4.55 asubuhi kwa gari la Polisi na kuingizwa katika chumba cha mahabusu saa 5.05, huku umati wa wananchi ukiwa umefurika katika Mahakama hiyo.

Septemba 8
Liyumba ashtakiwa tena


Aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania, Amatus Liyumba (63), ambaye Septemba 23 mwaka huu anamaliza kutumikia adhabu ya kifungu cha miaka miwili jela, jana alijikuta akipandishwa tena katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam kwa kesi mpya ya kukutwa na simu gerezani.

Septemba 6
Dowans haikamatiki


Hatimaye Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imeyafukuza maombi ya wanaharakati waliokuwa wakiongozwa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu(LHRC) ambao yaliyokuwa yakiomba mahakama hiyo ikatee kusajili tuzo iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa migogoro ya Kibiashara(ICC) kwa kampuni ya Dowans Holdings SA(Costa Rica) na na wenzake kwasababu wanaharakati hao hawana haki wala mamlaka ya kupinga hilo.

Septemba 8
Mtikila afungua kesi kuzuia mahakama isiuzwe


Mwenyekiti wa Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, amefungua kesi ya Kikatiba katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam jana, akiitaka izuie kuuzwa kwa jengo la Mahakama ya Rufaa lililopo eneo la Kivukoni Front, kwa mmiliki wa Hoteli ya Kempinski.

Kwa mujibu wa hati ya madai ambayo tayari imeshapewa namba 23 ya mwaka huu, Mtikila anamshtaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Katiba na Sheria na Jaji Mkuu wa Tanzania kwa kuruhusu jengo hilo la mahakama ya juu nchini liuzwe.

Agosti 18
Jerry Murro:Polisi wamenibambikizia kesi

Aliyekuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa(TBC1), Jerry Murro(30), anayekabiliwa na kesi ya kula njama na kuomba rushwa ya Sh milioni 10, ameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imuone hana hatia kwasababu kesi hiyo inayomkabili amebambikiwa na baadhi ya askari wa Jeshi la Polisi.

Agosti 17
Tao ‘akwaa kisiki’korti kuu


Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetupilia mbali ombi la aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha (TLP), Hamad Tao dhidi ya Mbunge wa Ilala(CCM), Mussa Hassan ‘Zungu’lilokuwa linataka mahakama hiyo imsamehe asilipe dhamana ya kesi hiyo ya uchaguzi kwa maelezo ombi hilo liliwasilishwa kabla ya wakati wake.

Uamuzi wa kesi hiyo ya uchaguzi Na.104/2010 iliyofunguliwa na Tao ambaye hivi karibu alifukuzwa uanachama wa chama hicho, ulitolewa jana na Jaji Dk.Fauz Twaibu ambaye alisema amefikia uamuzi baada ya kubaini ombi hilo la Tao lakutaka asamehewe kulipa dhamana ya kesi hiyo kwasababu ombi hilo pia halikukidhi matakwa ya Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2010.

Agosti 4
Mahalu aanza kujitetea


Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu ameileza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa alipofika katika ubalozi huo alikuta ofisi hizo zikiwa na hali mbaya hali iliyosababisha kutoa fedha zake mfukoni na kunua thamani zenye hadhi ya ofisi ya ubalozi.

Sambamba na hilo Balozi Mahalu mawasiliano kati ya rais wanchi, balozi,waziri wa Mambo ya Nje na Katibu uwa ya aina tatu.Aina ya kwanza ni mawasiliano ya maandishi yaani barua za kawaida, maandishi ya mafumbo na mawasiliano ya mdomo.Rais anamamlaka ya kumpigia simu balozi kokote alipo na kumpa maelekezo au kumwita balozi aje hapa nchini na kisha kumpa maelekezo ya ana kwa ana bila maandishi.

Julai 28
Bosi wa Richmond aibwaga serikali

Hatimaye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es salaam, imemwachiria huru mfanyabiashara Naeem Adam Gire aliyekuwa akikabiliwa na makosa ya kughushi, kutoa taarifa za uongo kwa maofisa wa serikali kuhusu kampuni ya Richmond LLC ya Texas ya Marekani kwasababu ushahidi ulitolewa na upande wa Jamhuri ni dhahifu.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Hakimu Mkazi Waliarwande Lema ambaye alisema kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya mahakama hiyo kutoa uamuzi wa ama mshtakiwa huyo Gire aliyekuwa akitetewa na wakili wa kujitegemea Alex Mgongolwa na Richard Rweyongeza ambapo Jamhuri ilikuwa ikiwakilishwa na Wakili Mkuu wa Serikali Fredrick Manyanda na Shadrack Kimaro ana kesi ya kujibu au la.

Lema alisema baada ya kupitia ushahidi wa mashahidi wote tisa na vilelelezo vilivyotolewa na upande wa Jamhuri, amebaini ushahidi na vielelezo hivyo ni dhahifu na una mapungufu ambao umeacha mashaka na maswali mengi na hivyo mahakama yake imefikia uamuzi wa kutumia kifungu cha 330 cha Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, ambacho kinaipa mamlaka mahakama ya kumwona mshtakiwa hana kesi ya kujibu na kumwachiria huru.

Julai 25
Maranda ana kesi ya kujibu

Kwa mara nyingine tena Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imemuomwona Kada wa CCM, Rajabu Maranda na mpwa wake Farijala Hussein kuwa wanakesi ya kujibu katika kesi ya pili inayowakili ya wizi wa Sh bilioni 2.2 katika Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu ya Tanzania.

Julai 15
Jaji Mkuu aongoza kusikiliza kesi ya askofu Mokiwa

Kanisa la Anglikana Tanzania, limeiomba Mahakama ya Rufaa Tanzania kutengua amri ya Mahakama Kuu Kanda ya Arusha iliyoamuru Askofu Mkuu wa kanisa hilo Dk.Valentino Mokiwa akamatwe na ashtakiwa kwa sababu ametenda kosa la jinai la kudharau amri ya mahakama.

Ambapo katika madai hayo ya msingi waliwasilisha kwa Jaji Sambo ambapo waliomba mahakama yake itoe amri ya kuzuia uchaguzi wa askofu wa dayosisi Mount Kilimanjaro usifanyike na askofu mteule wa dayosisi hiyo asiapishwe ambapo mahakama kuu baadaye ilitoa amri ya Mhashamu Dk.Mokiwa akamatwe na ashtakiwa na adhibiwe kwa sababu amedharau amri ya mahakama kwani amemwapisha mdaiwa wa pili (Hotay) wakati mahakama hiyo bado haijatoa maamuzi yake.

Ombi hilo la kanisa la Anglikana la kutaka amri hiyo itenguliwe liliwasilishwa jana wakili wa kanisa hiyo Joseph Thadayo mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Chande Othman aliyekuwa akisaidiwa na majaji wa mahakama ya rufaa William Mandia na Steven Bwana.

Julai 15
31 waachiwa ‘kesi ya samaki wa Magufuli’

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imewaachilia huru raia wa kigeni 31 kati ya 36 waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya uvuvi haramu bila leseni maarufu kama “kesi ya samaki wa Magufuli”katika ukanda wa Tanzania, baada ya kuwaona hanawana kesi ya kujibu.

Sambamba na hilo,mahakama hiyo imemwamuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na taasisi nyingine za serikali kuandaa haraka iwezekanavyo utaratibu wa usafiri ambao ni salama wa kuwarejesha katika nchi zao raia 31 wa kigeni iliyowaachilia huru ili waweze kwenda kuungana na familia zao.

Juni 24
Mahita aumbuka tena

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetupilia mbali rufaa iliyokuwa imekatwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) mstaafu, Omari Mahita, dhidi ya aliyekuwa msichana wake wa kazi anayedaiwa kuzaa naye.

Katika rufaa hiyo, Mahita alikuwa akiiomba Mahakama Kuu itengue hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni ambayo ilimuamuru kupeleka gharama za matunzo ya mtoto wake Juma Omary Mahita (14) mtoto anayedaiwa kuzaa na msichana huyo Rehema Shabani.

Juni 20
Mhindi aliyeua Mtanzania kunyongwa


Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imemhukumu kunyongwa kwa kamba hadi kufa raia wa India Vinoth Praveen kwa kosa la kumchoma visu hadi kufa Mtanzania, Abdul Basit.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Jaji Dk. Fauz Twaibu aliyesema kwamba mahakama imeridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri.

Katika kesi hiyo ya jinai namba 83/2009 upande wa Jamhuri uliwakilishwa na Wakili wa Serikali Shadrack Kimaro, wakati upande wa utetezi uliwakilishwa na Wakili wa kujitegemea Majura Magafu.

Juni 20
Diwani CCM jela miaka 10 kwa rushwa


Mahakama ya Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, imemhukumu kifungo cha mika 10 jela na faini ya sh milioni 6.7 Diwani wa Viti Maalum (CCM) Kata ya Mlingoti, Atindanga Mohammed kwa makosa 11 ya rushwa.

Hukumu hiyo ya aina yake ilitolewa leo na Hakimu Shemuli Cyprian baada ya mahakama hiyo kuridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka ambapo diwani huyo aligawa vitenge na kanga kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.Katika kesi hiyo upande wa mashtaka uliwakilishwa na wakili wa serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Christa Kadekenga.

Juni 18
Mfungwa msomi ashinda rufaa


Hatimaye Mahakama ya Rufani nchini imemfutia adhabu ya kifungo cha miaka 20 jela yule mfungwa aliyepata Shahada ya kwanza ya Sheria katika Chuo Kikuu Huria(OUT) akiwa gerezani,askari mpelelezi wa Jeshi la Polisi E.6937 D/C Haruna Pembe Gombela baada ya kubaini huku zote zilizotolewa na mahakama za chini zilimtia hatiani kimakosa.

Uamuzi huo wa Mahakama ya Rufani nchini unatokana na rufaa Na.44/2006 iliyokatwa mahakamani hapo na mrufani Gombela ambaye alikuwa akiishi katika Gereza Ukonga dhidi ya Jamhuri aliyoomba mahakama hiyo ya juu nchini itengue hukumu ya ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam iliyotolewa na Jaji Katherine Orioyo Oktoba 31 mwaka 2005, ambayo pia nayo ilikubaliana na hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Wilaya ya Ilala katika kesi ya unyang’anyi wa kutumia silaha Na.1426/1990 ambazo hukumu zote hizo zilimtia hatiani kwa kosa hilo na kumhukumu kwenda jela miaka 20.

Juni 8
Hakimu kortini kwa rushwa Dar

Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Ukonga jijini Dar es Salaam, Ndevera Kihangu na wenzake wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na makosa ya kushawishi na kupokea rushwa ya sh 100,000.Mbali na Hakimu Kihangu, washitakiwa wengine ni karani wa hakimu huyo, Eveline Mowo na mhasibu wa mahakama hiyo, Victoria Mtasiwa.

Juni 5
Serikali yashinda kesi tano mauji ya Albino


Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP),Eliezer Feleshi ameeleza kuwa hadi sasa ofisi yake imeshinda jumla ya kesi tano za mauji ya watu wenye ulemavu wa ngozi(Albino) walizokuwa wamezifungua katika Kanda mbalimbali za Mahakama Kuu hapa nchini na Mahakama Kuu nchini.

Sambamba na kushinda kesi hizo tano za mauji ya albino, pia imeweza kushinda kesi moja ya biashara haramu ya kusafirisha binadamu ( Human Traffick and Abduction) iliyomhusisha Robison Mukwena ambaye ni mlemavu wa ngozi.

Juni 1
Wabunge CCM waiburuza serikali mahakamani


Wabunge watatu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na raia wengine wanne wamefungua kesi ya Kikatiba katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na wenzake wakiiomba serikali izuiwe kulipa fidia ya sh bilioni 94 kwa Kampuni ya Dowans Holdings SA na Dowans Tanzania Ltd.

Mei 31
Kesi ya Mahalu:Ushahidi wa Mkapa tishio


Wakati Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imeahirisha kuanza kusikiliza kesi ya uhujumu uchumi wa zaidi ya euro milioni 2, sawa na sh bilioni 3 inayomkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu, na Grace Martin, ushahidi wa Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, umeivuruga serikali ya Rais Kikwete.

Mvurugano huo ulijionyesha jana mahakamani baada ya wakili mkuu wa serikali, Ponsian Lukosi, anayesaidiwa na wakili mwandamizi toka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ben Lincoln, kuwasilisha ombi la kuitaka mahakama itoe mwongozo wa kesi hiyo kwa madai kuwa mawakili wa Mahalu, Mabere Marando na Alex Mgongolwa, wamekuwa wakitoa mwenendo wa kesi hiyo kwenye vyombo vya habari kabla ya kusikilizwa na mahakama hiyo.

Mei 30
Jamhuri yafunga ushahidi kesi ya ‘Samaki wa Magufuri’

Hatimaye upande wa Jamhuri katika kesi ya uvuvi haramu katika kina kirefu cha ukanda wa Bahari ya Hindi maarufu kesi ya ‘Samaki wa Magufuri’ inayowakabili raia 36 wa kigeni umefunga ushahidi wake katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Wakili Mwandamizi wa Serikali Biswalo Mganga anayesaidiwa na Prosper Mwangamila mbele ya Jaji Agustine Mwarija alieleza mahakama hiyo kuwa mashahidi wake 13 walifika mahakamani hapo kutoa ushahidi wameona ushahidi wao umetosha na hivyo wamefikia uamuzi huo wa kuifunga kesi yao.

Mei 23
Hukumu kesi ya EPA:Yametimia


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam,ilitoa hukumu ya kwanza katika kesi ya wizi wa sh bilioni 1.8 zilizochotwa kwenye Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), mali ya Benki Kuu (BoT), ambapo ilimhukumu Kada wa CCM, Rajabu Maranda na mpwake wake Farijala Hussein kwenda jela miaka 5 baada ya kuwatia hatiani kwa makosa ya kugushi na kujipatia ingizo la kiasi hicho cha fedha toka BoT.

Hukumu hiyo ilizusha vilio na kuifanya mahakama hiyo kuzizima kwa muda baada ya Mweka Hazina wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kigoma Rajab Maranda na binamu yake Farijala Hussein kuhukumiwa kifungo cha miaka mitano jela.
Jopo la mahakimu wakazi likiongozwa Saul Kinemela lilianza kusoma hukumu hiyo kwa saa moja ndani ya ukumbi namba mbili wa mahakama hiyo.Mahakimu wengine ni Phocus Bambikya Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani na Elvin Mugeta, Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Aprili 15
Waandishi wapigwa marufuku kesi ya Manji,Mengi


Katika hali ya kustaajabisha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam,jana ilitoa maelekezo ya kuvizuia vyombo vyote vya habari nchini kuripoti mwenendo mzima wa kesi ya madai ya kashfa ya shilingi moja iliyofunguliwa mahakamani hapo na Mfanyabiashara Yusuf Manji dhidi ya Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Ltd, Reginald Mengi na ITV.

Aprili 10
Kesi ya Zombe yapangiwa Jaji

Uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, umempangia Jaji Upendo Msuya kusikiliza kesi ya madai ya fidia ya sh bilioni tano iliyofunguliwa na aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Abdallah Zombe (57) dhidi ya serikali.

Aprili 8
Hakimu kesi ya Manji,Mengi ajitoa

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Alocye Katemana ametangaza kujitoa kuendelea kusikiliza kesi ya madai ya kashfa ya shilingi moja iliyofunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na mfanyabiashara Yusuf Manji dhidi ya Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Ltd, Reginald Mengi na ITV.

Uamuzi huo aliutoa jana mahakamani wakati kesi hiyo ilipokuja kwaajili ya kutajwa.Kesi hiyo ilikuja kutajwa kwa mara ya kwanza jana tangu jalada la kesi hiyo lilipotoka kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Semistocles Kaijage Machi 29 mwaka huu ambaye aliamuru jalada la kesi hiyo lirudishwe Mahakama ya Kisutu kwa hakimu Katemana ambaye ndiye amekuwa akisikiliza kesi hiyo kwaajili ya kuendelea kusikiliza baada ya ukaguzi wake alioufanya katika jalada hilo akabaini kuwa hakimu huyo hakuwa amepindisha sheria yoyote wakati akiisiliza kesi hiyo.

Machi 30
Mengi akwaa kisiki korti kuu

Hatimaye Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imetoa ametoa amri ya kurudishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jalada ya kesi ya madai ya kashfa ya shilingi moja iliyofunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na mfanyabiashara Yusuf Manji dhidi ya Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Ltd, Reginald Mengi na ITV.

Jalada la kesi hiyo ambayo lilitua katika Mahakama Kuu Machi 23 mwaka huu, likitokea Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutokana na barua ya februali 23 mwaka huu, iliyoandikwa na wakili wa mdaiwa(Mengi) , Michael Ngaro kwa Jaji Mfawidhi Semistocles Kaijage ambapo ndani ya barua hiyo Ngaro alimuomba Jaji Kaijage apitie mwenendo mzima wa kesi hiyo kwani hakimu mkazi anayeisikiliza kesi hiyo Alocye Katemana ametoa maamuzi kadhaa yanaoonyesha anaupendelea upande wa mlalamikaji(Manji).
Machi 28
Jaji Mwangesi ajitoa kesi ya Mahalu
Hatimaye jaji Sivangilwa Mwangesi ambaye alikuwa akisiliza kesi ya uhujumu uchumi wa Euro zaidi ya milioni mbili inayomkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu na Meneja Utawala na Fedha, Grace Martin ametangaza kujiondoa kuendelea kusikiliza kesi hiyo.

Jaji Mwangesi alitangaza umuzi huo jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, ambapo kesi hiyo ilikuja kwaajili ya jaji huyo kutoa uamuzi wa ama kuendelea au kujiondoa katika kesi hiyo kufuatia sababu sita zilizowasilishwa Ijumaa iliyopita na washtakiwa ambayo yalimtaka ajitoe kwasababu hawana imani nae kwasababu amekuwa akiendesha shauri hilo kwa malengo yake badala ya sheria.
Machi 25
Mahalu amkataa jaji
Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu na Grace Martin ambao wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi ya zaidi ya Euro milioni mbili, jana walimwomba Jaji Sivangilwa Mwangesi ambaye anaendesha kesi hiyo hajitoe kwasababu amekuwa akikiusha sheria kwa makusudi kwasababu ya malengo anayoyajua yeye.

Ombi hilo limetolewa jana na mawakili wa washtakiwa haoMabere Marando aliyekuwa akisaidiwa na Beatusi Malima na Alex Mgongolwa ambapo kwakuanza waliiumbukusha mahakama hiyo kuwa wanafahamu kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya jaja huyo kupanga tarehe ya washtakiwa hao kuanza kujitetea.
Machi 23
Kesi ya Manji Vs Mengi:Jalada latua korti kuu
Jalada la kesi ya madai ya kashfa ya shilingi moja iliyofunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na mfanyabiashara Yusuf Manji dhidi ya Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Ltd, Reginald Mengi na ITV, limetua rasmi Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa vyanzo vya kuaminika toka ndani ya Mahakama Kuu vililithibitishia gazeti hili kuwa jalada hilo limefika mahakamani hapo jana asubuhi likitokea katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Vyanzo hivyo vilibainisha kuwa chanzo cha jalada hilo kuitwa katika mahakama hiyo ya juu ni kutokana na barua ya Februali 23 mwaka huu, iliyoandikwa na wakili wa mdaiwa(Mengi),Michael Ngaro kwa Jaji Mfawidhi Semistocles Kaijage ambapo ndani ya barua hiyo Ngaro anamuomba Jaji Kaijage alipitie mwenendo mzima wa kesi hiyo kwani hakimu mkazi anayeisikiliza kesi hiyo na akatolea maamuzi mbalimbali Alocye Katemana alionesha kuupendelea upande wa mlalamikaji(Manji).
Machi 18
Kesi ya wizi wa gari la DPP:sita wafutiwa shitaka la unyang’anyi
Hatimaye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imewafutia shtaka la unyang’anyi wa kutumia silaha washtakiwa sita katika kesi unyanganyi wa kutumia silaha, kupokea mali za wizi na wizi wa gari na kompyuta mali ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DDP) vyenye jumla ya thamani ya shilingi sh 111,500,000.

Sambamba na hilo Hakimu Mkazi Jenevitus Dudu ambaye ndiye anasikiliza kesi hiyo ambayo ina jumla ya washtakiwa 12, pia amewaachilia huru washtakiwa watatu ambao walikuwa wakikabiliwa na kosa la kupokea mali za wizi baada ya kuwaona hawana kesi ya kujibu.
Baada ya Hakimu Dudu kutoa uamuzi huo , Mkurugenzi wa Mashtaka(DPP), Eliezer Feleshi aliwasilisha mahakamani hapo hati ya kuzuia dhamana kwa washtakiwa sita walifutiwa shtaka la unyang’anyi kwa kutumia silaha ambalo kwa mujibu wa sheria za mwenendo wa makosa ya Jinai ya mwaka 2002, shitaka hilo halina dhamana na Wakili wa Serikali Zuberi Mkakati naye akawasilisha mahakamani hapo hati ya kusudio ya kukata rufaa katika Mahakama Kuu dhidi ya uamuzi wa hakimu huyo.
Machi 16
Gulam Dewji aburuzwa kortini
Shirika la Nyumba la Taifa(NHC), imeiburuza katika Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi ,Bodi ya Udhamini ya Federation of Khoja Ithna-Asheri Jamaats of Afrika na mfanyabiashara maafuru nchini Gulambhai Dewji wakiomba mahakama hiyo itamke jengo lililopo kitalu Na.39 mtaa wa Chuma-Chang’ombe jijini hapa ni mali halali ya shirika hilo na si la wadaiwa hao.
Kwa mujibu wa hati ya madai ambayo gazeti hili inayo nakala yake, mlalamikaji ambaye amefungua kesi hiyo chini ya hati ya hati ya dharula , na Mwanasheria wa Shirika hilo la Nyumba nchini, Martin Mdoe ndiye amekula kiapo kwaniaba ya Mkurugenzi Mkuu wa (NHC), anaiomba mahakama hiyo itamke kuwa jengo hilo ambalo lina thamani ya zaidi ya bilioni mbili ni mali ya shirika hilo.

Machi 8
Jerry Murro ana kesi ya kujibu
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, imemuona aliyekuwa Mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la TBC1, Jerry Murro na wenzake wanaokabiliwa na kesi ya kula njama, kushawishi na kuomba rushwa ya sh milioni 10, kuwa wana kesi ya kujibu.

Uamuzi huo wa kushtua ulitolewa leo na Hakimu Mkazi Gabriel Mirumbe ikiwa ni muda mfupi baada ya shahidi wa sita wa upande wa Jamhuri, D/C Koplo Lugano Mwampeta kumaliza kutoa ushahidi wake na Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka nchini, Stanslaus Boniface kueleza kuwa wamefunga ushahidi.

Machi 8
Zombe aishika pabaya serikali


Hatimaye aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Abdallah Mohamed Zombe(57),amemfungulia kesi ya madai ya fidia ya Sh bilioni tano serikali kwasababu ilimnyanyasa, kumdhalilisha,kumbakizia kesi na ilikiuka sheria na Katiba ya nchi wakati ilipomkamata na kumfungulia kesi ya mauji ya watu wa nne.

Machi 7
Raia wa kigeni kortini kwa dawa za kulevya


Kwa mara nyingine tena serikali imewaburuza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, raia wanne wa kigeni wakikabiliwa na mashtaka mawili ya kula njama na kuingiza dawa za kulevya aina ya Heroin zenye uzito wa gramu 81 zenye thamani ya Sh bilioni 2.8.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mustapher Siyani wakili mwandamizi wa serikali Biswalo Mganga aliyekuwa akisaidiwa Prosper Mwangamila na Theophili Mtakyawa aliwataja washtakiwa hao kuwa ni Dinnis Chukwudi Okechukwu,Paul Ikechukwu Obi ambao ni raia wa Naigeria, Stani Hycenth raia wa Afrika ya Kusini na Shoaib Mohammed Ayazi ambaye ni raia wa Pakstani ambao wanatetewa na wakili wa kujitegemea Brigson Sheiyo.

Machi 3
Jaji ajitoa ‘kesi ya Samaki wa Magufuli’


Hatimaye jaji Razia Sheikh anayesikiliza kesi ya uvuvi haramu katika Bahari ya Hindi ukanda wa Tanzania inayowakabili ryaia 34 wa kigeni maarufu kama ‘kesi ya samaki wa Magufuli’ amejitoa kuendelea kusikiliza kesi hiyo.

Jaji Sheikh alitoa uamuzi huo jana katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kufuatia ombi la washtakiwa hao walioliwasilisha mbele yake Ijumaa iliyopita ambapo washtakiwa walimwomba ajitoe kwasababu hawana imani naye.

Jaji Sheikh alisema anajitoa kusikiliza shauri hilo si kwasababu ya hoja zilizowasilishwa na wakili wa washtakiwa John Mapinduzi na Ibrahim Bendera bali anajitoa ili haki ionekane inatendeka na kwamba jalada la kesi hiyo atalipeleka kwa Jaji Mfawidhi Semistocles Kaijage ili aweze kumpanga jaji mwingine.

Februali 15
Nyaraka za Mengi kuhusu EPA,Kagoda zakatariwa tena kortini

Kwa mara ya pili Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imetupilia mbali ombi la Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP Ltd, Reginald Mengi, lililotaka mahakama hiyo iwapatie nakala ya uamuzi iliyoutoa Ijumaa iliyopita ili aweze kwenda Mahakama Kuu kuomba ufanyiwe mapitio.

Mengi kupitia wakili wake Michael Ngaro, wanapinga kutupwa kwa nyaraka zinazohusu wizi wa fedha kupitia Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), inayoihusisha kampuni ya Kagoda ambazo Mengi anadai ina uhusiano na Manji.

Uamuzi wa kulitupa ombi hilo, ulitolewa jana na Hakimu Mkazi, Aloyce Katemana, ambaye alisema baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili anakubaliana na hoja ya mawakili wa mlalamikaji (Manji), Mabere Marando, Dk. Ringo Tenga, Richard Rweyongeza na Beatus Malima, ambao walidai ombi lililowasilishwa na wakili wa mdaiwa Michael Ngaro na Deo Ringia, halina msingi wa kisheria.

Februali 10
Mawakili wa Mintanga wageuka mbogo

Upande wa utetezi katika kesi ya kula njama na kusafirisha dawa za kulevya inayomkabili aliyekuwa Rais wa Shirikisho la Ngumi za Ridhaa Tanzania (BFT), Alhaji Shabani Mintanga, umeiomba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kuifuta kesi hiyo kwasababu upande wa Jamhuri umeshindwa kuleta mashahidi.

Februali 4
Mhasibu mahakamu kuu kortini kwa wizi

Mhasibu Msaidizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kitengo cha Ardhi, Raymond Mazale, amefikishwa mahakamani akikabiliwa na kosa la wizi wa sh milioni 22 mali ya mwajiri wake.

Wakili wa Serikali Beatrice Mpangala mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu Dar es Salaam, Aloyce Katemana, alieleza mahakama kuwa mshtakiwa huyo anakabiliwa na mashtaka manne ya wizi.

Februali 3
Manji amvaa Mengi kortini

Mfanyabiashara maarufu nchini, Yusuf Manji(35) jana ameileza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa kashfa zilizotolewa na Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP Ltd,Reginald Mengi kuwa yeye ni Fisadi Papa zimemvunjia heshima na kusababisha asiaminiwe tena wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Manji ambaye siku hiyo ilikuwa ni mara yake ya kwanza kupanda kizimbani hapo , alitoa maelezo hayo wakati akiongozwa kutoa ushahidi wake na mawakili maarufu wa kujitegemea nchini, Mabere Marando, Dk.Ringo Tenga, Richard Rweyongeza, Sam Mapande na Beatus Malima mbele ya Hakimu Mkazi Aloyce.

Februali 2
Kikwete aitaka mahakama ijisafishe
Rais Jakaya Kikwete ameomba uongozi wa Mhimili wa Mahakama nchini kuondoa hisia za ukosefu wa uhadilifu zinazowakabili baadhi ya watendaji wa mahakama nchini.

Rais Kikwete aliyasema hayo leo katika sherehe ya siku ya Sheria nchini iliyofanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ambapo maudhui ya siku ya sheria mwaka huu ni “ Umuhimu wa elimu kuhusu mahakama kama hatua ya msingi ya utatuzi wa migogoro katika jamii”.

“Leo katika kusherekea siku hii ya sheria minauomba mhimili wa mahakama mambo mawili .Mosi; uadilifu katika utoaji haki…bado kuna hisia ya ukosefu wa uhadilifu kwa watoaji haki ambao ni mahakama kwamba wenye fedha ndiyo wanapata haki na wasiyo na fedha hawapati haki:

“….Uwezo wa kuondoa hisia hizo mbaya upo mikononi mwenu na ninatambua sifa za uadilifu mlizokuwa nazo majaji na mahakimu licha miongoni mwenu wamekuwa na sifa za ukosefu wa uhadilifu na kwa taarifa nilizonazo uongozi umekuwa ukiwashughulikia kiutawala”alisema Rais Kikwete.

Januari 27
Dowans yaipiga chenga serikali


Hatimaye kampuni ya kufua umeme ya Dowans Holdings SA na Dowans Tanzania Ltd zimewasilisha rasmi ombi la kuomba fidia ya sh bilioni 94 isajiliwe katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Fidia hiyo ni ile iliyoamriwa kulipwa na TANESCO kwa kampuni hiyo baada ya shirika hilo la ugavi wa umeme nchini kutiwa hatiani na mahakama ya kimataifa ya usuluhishi migogoro ya kibiashara (ICC), kwa kile kilichoelezwa kuwa ilivunja mkataba baina yake na kampuni hiyo kinyume cha taratibu.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana mchana jijini Dar es Salaam, Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Salvatory Bongole, alisema ombi hilo la Dowans dhidi ya TANESCO, liliwasilishwa Januari 25 mwaka huu mahakamani hapo na wakili wa kujitegemea ambaye anaiwakilisha kampuni hiyo, Kennedy Fungamtama.

Bongole alisema ombi hilo limepewa namba 8/2011 na jaji wa kulisikiliza ameshapangwa ingawa tarehe ya kuanza kusikilizwa kwa ombi hilo bado haijapangwa.

Januari 6
Vigogo wa Chadema kortini Arusha


Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA), Freemen Mbowe, Katibu Mkuu Dk.Wilbroad Slaa na wanachama wengine wafikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, wakikabiliwa na makosa kufanya mkusanyiko haramu Januari 5 mjini Arusha.
Nawatakieni wasomaji wote kheri ya mwaka mpya.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

0716 774494
www.katabazihappy.blogspot.com


Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Desemba 31 mwaka 2011.

JAJI MAKARAMBA UMENENA



Na Happiness Katabazi

KWANZA namshukuru mungu kwa kuweza kunipa uzima na afya njema na hadi Desemba 25 mwaka huu, nikaweza kutimiza umri wa miaka 33.

Nikiachana na hilo,leo nitajadili ushauri uliotolewa na Jaji wa Mahakama Kuu Kitengo cha Biashara Robert Makaramba alioutoa Desemba 26 mwaka huu kwa vyombo vya habari kabla ya kufungua tamasha la vipaji kwa vijana Wakatoriki.

Jaji Makaramba aliwataka waandishi wa habari nchini kuungana na kupiga kelele kwa serikali ili ibadilishe sheria ya uchochezi iliyorithiwa kutoka kwa wakoloni kwa kuwa ni hatari na inaweza kusababisha wengi wao kufungwa jela pamoja na vyombo vya habari kufilisiwa.

Alisema lazima waandishi waungane kupitia Press Club zao na kuhakikisha wanadai mabadiliko katika sheria hiyo kwani sheria ya uchochezi ipo na kwa namna yoyote mwandishi anaweza kuambiwa ameivunja na hivyo kujikuta akifikishwa mahakamani.

Mimi binafsi nikiwa kama mwandishi wa habari na mwanafunzi wa fani ya Sheria hivi sasa, napenda kuunga mkono ushauri huo wa Jaji Makaramba kwetu sisi waandishi wa habari kwani endapo waandishi wa habari hivi sasa tutaacha dharau, ubinafsi na ujinga tunaweza kuufanyia kazi kwa vitendo ushauri huo ulitolewa na jaji huyo ambaye alishawahi kuwa mwadhiri wa katika kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kabla ya kuteuliwa kuwa jaji.

Ni wazi kwamba Ibara ya 18(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inatoa uhuru wa kila mtu kutoa fikra zake.

Lakini hakuna ubishi kwamba licha haki hiyo imewekwa ndani ya Katiba kwa maandishi lakini wakati huu wa utawala wa Serikali ya Awamu ya Nne inayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete sote ni mashahidi, vyombo vya habari na waandishi wa habari tumekuwa na uhuru mpana sana wa kujadili masuala mbalimbali na mengine nyeti bila vyombo vya dola kuvamia vyumba vyetu vya habari na kufanya uharibifu au kuwadhuru waandishi wa habari wazi wazi kama tunavyoshuhudia nchi za wenzetu ambapo watawala wamekuwa wakitumia vyombo vya dola kubugudhi wanahabari na kuaharibu mitambo ya vyombo vya habari.
Sisi waandishi wa habari hapa nchini tunafahamiana vizuri tu kwani baadhi ya waandishi habari tumekuwa tukitumiwa na wanasiasa wanaoasimiana au wenye nia ya kuwania madaraka ya juu kupitia vyama vyao vya hasa wale wa Chama cha Mapinduzi(CCM) kuandika habari za kuwachafua wanasiasa wenzao.

Na wanasiasa hao wamekuwa wakati mwingine wamekuwa wakitupatia hata mazungumzo mbalimbali yanayojadiliwa kwenye vikao vya siri vya vyama vyao ambayo mazungumzo hayo yakichapishwa kwenye vyombo vya habari yanakuwa yamemchafua mwanasiasa wanawayehasimiana naye.

Na situ tumekuwa tukitumiwa na wanasiasa, bali hata wafanyabiashara na makundi mengine katika jamii nayo yamekuwa yakiwatumia baadhi ya waandishi wasio waadilifu ama kwa kujua au kutokujua kupenyeza ajenda zao zichapishwe kwenye vyombo vya habari kwa maslahi yao binafsi badala ya taifa.

Na wakati mwingine waandishi wa habari wa aina hiyo wamekuwa wakikubali kuaziandika habari hizo bila ya kuwa na vielelezo vyovyote mkononi jambo ambalo mwisho wa siku serikali au mtu binafsi anapoamua kulishtaki gazeti au kuwafikisha wahariri na waandishi wa habari mahakamani, wanajikuta hawana ushahidi ambao unaounga mkono habari au makala walizozichapisha ambazo zimeleta madhara kwa watu au serikali.

Ikumbukwe kuwa kifungu cha 9 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002, kinasema kutojua sheria siyo kinga ya kutokuadhibiwa.

Kwa hiyo sisi waandishi wa habari tukae tukijua sheria ya uchochezi ipo na ni kweli ni hatari kwetu sisi waandishi wa habari na endapo siku serikali itakapoamua kuanza kuitumia dhidi yetu ni wazi kabisa tutajikuta tukiangukia kwenye mkondo ule ule wa kufikishwa mahakamani na magerezani.

Somo zuri tumelipata kupitia hukumu mbalimbali zilizotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Mauji ya Kimataifa yenye makao makuu yake mjini Arusha,ambapo tulishuhudua waandishi wa habari walivyotiwa hatiani kwa makosa ya uchochezi na kuhukumiwa kwenda jela.
Lakini pia nimalizie kwa kutoa rai kwa wamiliki wa vyombo vya habari hapa nchini waondokane na uwekezaji uchwara katika sekta ya habari na badala yake waanze kuajili wanasheria kwa wingi ambao wanasheria hao ambao kutwa nzima watakuwa wakishinda ndani ya vyombo vya habari na kuzipitia habari zote zinazoandikwa na waandishi na kuhaririwa na wahariri ili kuweza kunusuru waandishi, wahariri na vyombo vya habari kukumbwa na kadhia ya kufikishwa mahakamani kwa kuandika na kupitisha habari ambazo ni za kichochezi.

Mwisho nimalize kwa kuwakumbusha waandishi wenzangu kuwa kila mmoja atimize wajibu wake kwa maslahi ya taifa hili na siyo kwa maslahi ya manyang’au kwani endapo tutakubali kuandika habari au makala za uchochezi mwisho wa siku tutaangukia mikononi mwa dola jambo ambalo si jema.

Hivyo wakati tukitafakari ushauri wa Jaji Makaramba,na sisi waandishi wa habari miongoni mwetu tujitazame upya na huu uhuru mpana wa kuandika na kuzungumza tuutumie vizuri kwaajili ya kuuletea tija taifa letu na siyo kuwaletea tija wanasiasa manyang’au ambao leo hii wameanza kupiga jalamba kuutaka urais wa Tanzania mwaka 2015 kwa gharama zozote kwani mwisho wa siku madhara ya kufunguliwa kesi yatakapotupata wanasiasa hao manyang’au hawatatusaidia kwa lolote na hiyo ndiyo tabia ya wasiasa wengi hapa nchini.

Nawatakia maandalizi mema ya kuukaribisha mwaka mpya wa 2012.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika
0716- 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Septemba 29 mwaka 2011.

KESI YA KAFULILA,NCCR-MAGEUZI-MAWAKILI WATUNISHIANA MISULI

Na Happiness Katabazi

CHAMA cha NCCR-Mageuzi nchini kimedai vyombo vya habari vilivyochapisha na kutangaza habari jana kuhusu amri ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam katika kesi ndogo Na.218/2011 iliyofunguliwa mahakamani hapo na Mbunge wa Kigoma Kusini kupitia chama hicho David Kafulila na wenzie saba.


Hayo yalisemwa jana na Katibu wa Idara ya Katiba na Sheria wa chama hicho, Dk.Sengondo Mvungi katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika jana katika makao makuu ya chama hicho ambapo alisema lengo la mkutano huo ni kutoa ufafanuzi zaidi wa kilichoamriwa na Jaji Alise Chinguile juzi jioni.

“Nyie vyombo vya habari hivi mmefikia hatua sasa ya kuchakachua hata amri za mahakama?Kumbukeni hata vita ya wenyewe kwa wenyewe iliyotokea Rwanda, waandishi wa habari walishiriki kuleta machafuko yale sasa nataka niwaeleze jambo moja mfahamu kuwa hii Tanzania ni yetu sote na kamwe mimi na chama changu hatuwezi kuona nyie waandishi wa habari mnachakachua hata amri za mahakama halafu tunanyamaze kimya”alisema Dk.Mvungi kwa sauti ya ukali.

Dk.Mvungi akitolea ufafanuzi wa kilichoamliwa na mahakama ni kuhusiana na yale waliyoyaomba ambapo hakuna hati yoyote inayoonyesha maombi ya kubatilisha maamuzi ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho yaliyotolewa Desemba 17 mwaka huu na kwamba suala la kuamuru upande katika kesi usifanye jambo zaidi ni katika mamlaka ya mahakama ambalo chama hakina tatizo na suala hilo.

“Ni vyema ieleweke wazi kwamba hakuna amri yoyote ya mahakama iliyotolewa ya kuwabakiza waliovuliwa uanachama katika chama.Wala hakuna amri ya kuwafutia adhabu yoyote waliyopewa wale waliodhibiwa . Hivyo maamuzi ya NEC yababaki kuwa sahihi na halali kwa mujibu wa sheria za nchi mpaka pale ambako mahakama itaamua vinginevyo.

“Msimamo wa chama chetu kwa sasa ni kwamba maamuzi yake ya NEC ambayo yalimvua uanachama Kafulila bado hayajatenguliwa wala kujadiliwa na mahakama yoyote ile.Isipokuwa kwa sasa tumepokea amri ya Mahakama Kuu ikizuia chama kisiendelee na hatua zaidi dhidi ya Kafulila na wenzake walioshirikiana kushitaki chama kwenye kesi Na.218/2011 mpaka shauri la msingi litakapoamriwa”alisema Dk.Mvungi.

Alisema msimamo wa chama chake ni kwamba hautaipinga amri hiyo ya mahakama licha amri hiyo imetolewa bila wadaiwa ambao ni Chama cha NCCR-Mageuzi na Mwenyekiti wake James Mbatia bila kujulishwa wala kupewa wito wa mahakama kuwa Kafulila amewafungulia kesi mahakamani hapo na kwamba wameshangazwa na hatua hiyo ya mahakama ya kusikiliza ombi hilo bila ya kutoa wito wa kuitwa kwa wadaiwa ili waje kujitetea na kwamba chama hicho kimeamua kitaenda kuudhulia kwenye kesi kubwa ambayo itatajwa Februali 21 mwaka huu.

Vyombo vya habari vingi jana viriripoti habari ambazo zilimkariri wakili wa Kafulila, Daniel Welwel kuwa mahakama imetoa amri ya kuzuia utekelezwaji wa uamuzi wa NEC ya chama hicho wakati amri ya mahakama haikusema hivyo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Desemba 29 mwaka 2011.
mwisho

KAFULILA AREJESHEWA UBUNGE

Na Happiness Katabazi

HATIMAYE Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetoa amri ya muda ya kusitisha utekelezwaji wa azimio la kikao cha Halmashauri Kuu ya Chama cha NCCR-Mageuzi, kilichomvua uanachama, David Kafulila (Kigoma Kusini), hivyo kupoteza kiti chake cha ubunge.

Amri hiyo ya muda ilitolewa jana na Jaji Alise Chinguilwe, muda mfupi baada ya kusikiliza ombi lililoletwa chini ya hati ya dharura na Kafulila kupitia kwa wakili wake, Daniel Welwel.

Akitoa uamuzi huo uliomwacha Kafulila akiwa na furaha isiyo kifani, Jaji Chinguilwe alisema, ametoa uamuzi huo baada ya kusikiliza na kuridhishwa na hoja za wakili huyo.

“Nimesikiliza hoja za wakili wa mlalamikaji (Kafulila) na mahakama hii inatoa amri ya kusimamisha utekelezaji wa azimio hilo la NEC ya Chama cha NCCR- Mageuzi ambalo lilimvua uanachama mlalamikaji kwa madai kuwa alikiuka katiba ya chama hicho,” alisema.

Akifafanua juu ya uamuzi huo, jaji huyo alisema kuwa mahakama yake imeona kuwa endapo itaruhusu utekelezwaji wa azimio la NEC ya chama hicho iendelee na uamuzi wake, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), italitangaza jimbo hilo kuwa liko wazi.

“Na ni wazi kuwa NEC ikishatangaza kuwa jimbo hilo liko wazi, itaitisha uchaguzi mdogo wakati kesi ya msingi iliyofunguliwa na Kafulila itakuwa bado haijatolewa uamuzi.

“Hivyo basi, mahakama yangu imezingatia mambo yote hayo, kwa hiyo inakubaliana na ombi la kuzuia utekelezwaji wa azimio la kikao hicho hadi kesi ya msingi iliyofunguliwa na Kafulila mahakamani hapo, itakapo malizika,” alisema Jaji Chinguile.

Kwa amri hiyo ya Mahakama, Kafulila ni Mbunge halali wa Kigoma Kusini hadi hapo mahakama itakapotoa hukumu ya kesi ya msingi iliyofunguliwa na mwanasiasa huyo kijana.

Ijumaa iliyopita Kafulila alifungua kesi ya madai dhidi ya chama hicho na Mwenyekiti wa chama hicho, James Mbatia, ya kupinga uhalali wa kikao cha NEC ya NCCR–Mageuzi, kilichoketi Desemba 17 mwaka huu, jijiji Dar es Salaam.

Kikao hicho pamoja na mambo mengine, kilimvua uanachama mbunge huyo kwa madai ya utovu wa nidhamu na kukiuka kanuni na taratibu za chama.

Kesi hiyo namba 218/2011, itakuja tena Februari 21mwakani ambapo itakuja kwa ajili ya kutajwa.

Kwa miezi kadhaa sasa, Kafulila amekuwa akiripotiwa na vyombo vya habari kuwa amekuwa akimshinika Mwenyekiti wa chama hicho, James Mbatia ajivue gamba kwa madai kuwa ameshindwa kukiongoza chama hicho.

Msimamo huo uliibua makundi ndani ya chama hicho na mwisho wa siku chama hicho kikafikia uamuzi wa kuitisha kikao cha NEC cha dharura, kisha kufanya uamuzi wa kumfukuza uanachama Kafulila.

Mbali ya Kafulila, chama hicho pia kilimvua uanachama kada wake aliyekuwa mgombea wa kiti cha urais katika uchaguzi uliopita, Hashim Rungwe, kwa madai kama hayo ya Kafulila.

Pia NEC ya chama hicho, ilitoa onyo kali kwa baadhi ya wabunge na wanachama wengine ambao wanadaiwa kuwa ni wafuasi wa kundi la Kafulila.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Desemba 28 mwaka 2011

KESI YA MRAMBA BADO HAKIELEWEKI

Na Happiness Katabazi


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam imesema kuwa mwendo wa kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya shilingi bilioni 11.7 inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha Basil Mramba na wenzake bado haujakamilika.


Jaji John Utamwa anayesaidiwa na Hakimu Mkazi Sam Rumanyika na Saul Kinemela alisema kesi hiyo ilikuja jana kwaajili ya kutajwa na kuangalia kama mwenendo wa kesi hiyo umekamilika lakini amebaini mwenendo wa kesi hiyo ambao ulishachapwa una makosa.
Jaji Utamwa alisema kwa sababu hiyo anaagiza mwenendo huo ukafanyiwe marekebisho na wahusika na endapo utakamalika basi mahakama hiyo itazipatia pande hizo mbili na akaiarisha kesi hiyo hadi Januari 13 mwakani ambapo kesi hiyo itakuja kwaajili ya kutajwa.
Mbali na Mramba washtakiwa wengine ni Katibu Mkuu Mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini Daniel Yona ambao wanatetewa na mawakili wa kujitegema Peter Swai, Hurbet Nyange na Elisa Msuya.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima, Desemba 15 mwaka 2011.

SERIKALI YASHAURIWA

Na Happiness Katabazi


SERIKALI imetakiwa kuzingatia matakwa ya kifungu cha 7 cha Sheria ya Ardhi ya mwaka 1999 na Katiba ya nchi kabla ya kuanza uchukua uamuzi wa kuwaondoa kwa nguvu wakazi wanaoishi kwenye makazi hatarishi yaliyoathiriwa na mafuriko yaliyosababishwa na mvua iliyonyesha wiki iliyopita.


Ushauri huo wa kisheria umetolewa jana na Mhadhiri toka Kituo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Onesmo Kyauke jana alipofanya mahojiano maalum na gazeti hili jijini Dar es Salaam, ambapo alisema endapo serikali haitazingatia hilo na badala yake ikatumia mabavu, mwisho wa siku itajikuta ikifikishwa mahakamani na wakazi hao na kuwalipa fidia kubwa.

Kyauke alisema kifungu cha 7 cha Sheria ya Ardhi Na.113 ya mwaka 1996, kinatamka watu wanaoishi kwenye makazi hatarishi yakiwemo maeneo ya mabondeni na kwamba kifungu hicho kinawatambua wakazi wanaoshi

“Kwa hiyo endapo serikali inataka kuwaondoa wakazi wanaoishi kwenye maeneo hayo kwanza inapaswa kuzingatia matakwa ya kifungu hicho cha sheria hiyo kwa Waziri mwenye dhamana ya ardhi kwa kuanza kutoa tangazo kwenye gazeti la serikali la kusudio la kulitangaza eneo fulani ni eneo hatarishi na kisha nakala hiyo ya hilo tangazo la waziri huyo linapaswa lipelekwe kwa wakazi wa eneo hilo waweze kulisoma;

“Na wakazi hao wakishalisoma tangazo hilo la waziri na kama hawakubaliani nalo, wakazi hao wa eneo hilo hatari watakuwa na haki ya kwenda kutoa malalamiko yao mbele ya Kamishna wa Ardhi na kamishna wa ardhi atawasilikiza na kuandika ripoti yake na kisha ripoti hiyo kumkabidhi waziri na kumshauri waziri kuwa eneo hilo kweli ni hatarishi;

“Ambapo waziri huyo ataisoma ripoti hiyo na ushauri huo na kama hataridhika na huo utetezi wao, waziri huyo ataipeleka ripoti hiyo kwa rais wa nchi na kisha rais wanchi ndiyo atakaye tangaza kulichukua eneo hilo kwasababu eneo hilo ni hatarishi na eneo hilo linakuwa ni mali ya serikali lakini pia wakazi hao watapaswa walipwe fidia”alisema Kyauke.
Alisema licha ya rais wa nchi kutangaza kulichukua eneo hilo hatarishi kwaajili ya kulibadilisha matumuzi yake ,wakazi hao watakuwa na haki ya kupewa fidia kwanza hata kama wakazi hao walikuwa wakimiliki maeneo hayo kwa kutumia hati za kimila au za wizara.

Kyauke ambaye ni wakili wa kujitegemea pia alisema kwa hiyo agizo lilotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Meck Sadick na Rais Jakaya Kikwete lilowataka wakazi hao wahame halikufuata taratibu hizo za kisheria ambapo mwisho wa siku serikali inaweza kujikuta ikifikishwa mahakamani na wananchi hao na kudaiwa fidia na wakazi hao kwani kifungu cha saba cha sheria ya ardhi kinawatambua wakazi wanaoishi kwenye maeneo hatarishi ambayo yamepimwa na ambayo hayajapimwa.

“Kwa hiyo naiomba serikali yetu ifuate taratibu hizo za kisheria kwani ieleweke wazi Katiba ya nchi ina mpa haki mwananchi ya kumiliki mali na ardhi hivyo, katika kukabiliana na tatizo hilo natoa ushauri kwa serikali ifuate taratibu za kisheria ambazo zipo wazi”alisema Kyauke.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Desemba 28 mwaka 2011

MAKALA YAMFIKISHA KORTINI KADA WA CHADEMA

Na Happiness Katabazi


MWANDISHI wa Safu ya ‘Kalamu ya Mwigamba (36)’ inayochapishwa kila siku ya Jumatano na gazeti la Tanzania Daima , Samson Mwigamba (36), jana alijikuta akifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kwa kosa la kuandika makala inayowashawishi maaskari na maofisa wa majeshi ya hapa nchini kuacha kuitii serikali iliyopo madarakani kwa sasa.


Mwigamba ni Mhasibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Makao Makuu na Mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Arusha na si mwandishi wa habari kitaaluma, alifikishwa hapo jana saa tatu asubuhi chini ya ulinzi mkali wa makachero wa Jeshi la polisi na kisha kuifadhiwa katika mahabusu ya mahakama hiyo wakati akisubiri kupandishwa kizimbani na kusomewa shtaka moja la kesi ya jinai Namba 289 ya mwaka huu.

Ilipofika saa 6:21 mchana Mwigamba ambaye si Mwandishi wa Habari Kitaaluma aliondolewa katika mahabusu ya mahakama huyo huku akisindikishwa na askari polisi na kisha kuuingizwa ndani ya chumba cha mahakama mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema na kisha Wakili Mwandamizi wa Serikali Elizabeth Kaganda alianza kumsomea shtaka linalomkabili.

Kaganda alidai mshtakiwa huyo anakabiliwa na kosa moja la kuwashawishi askari na maofisa wa jeshi la polisi, magereza na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania(JWTZ) kutoendelea kuitii serikali iliyopo madarakani kwa sasa ambayo inaongozwa na Rais Jakaya Kikwete kinyume na kifungu cha 46(b),55(10(a) na 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Wakili Kaganda alidai Novemba 30 mwaka huu,gazeti la Tanzania Daima la siku hiyo toleo Na.2553 lilichapisha waraka uliokuwa na kichwa cha habari kisemacho “Waraka Maalum kwa Askari wote” ambao uliandikwa na mshtakiwa huyo kupitia safu yake ijulikanayo kwa jina la ‘Kalamu ya Mwigamba’.

Wakili huyo wa serikali alidai kuwa mshtakiwa huyo kupitia walaka wake huo kwa makusudi na kwa nia kuvunja sheria za mamlaka ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliwashawishi askari na maofisa wa jeshi la polisi, Magereza na JWTZ kutoendelea kuiiti serikali iliyopo madarakani.

Hata hivyo mshtakiwa huyo ambaye alikuwa amevalia magwanda ya chama hicho alikana kosa hilo na wakili Kaganda alidai upande wa jamhuri hauna pingamizi la mshtakiwa kupewa dhamana kwasababu kosa linalomkabili lina dhamana kwa mujibu wa sheria nakuongeza kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.

Kwa upande wake Hakimu Waliarwande Lema alisema ili mshtakiwa apate dhamana ni lazima awe na wadhamini wawili wa kuaminika ambao kila mmoja atatakiwa asaini bondi ya shilingi milioni tano na mdhamini mmoja kati ya hao wadhamini wawili atapaswa awasilishe hati ya mali isiyoamishika yenye thamani ya shilingi milioni tano.

Hakimu Lema alisema sharti jingine ni kwamba mshtakiwa huyo atatakiwa kila mwisho wa mwezi aende kuripoti katika kituo Kikuu cha Polisi Kati(central) na mshtakiwa huyo atatakiwa asalimishe hati yake ya kusafiria mahakamani hapo.

Aidha wakili wa mshtakiwa Edson Mbogoro alieleza kuwa mshtakiwa ana wadhamini wawili ambao ni madiwani wa wilaya ya Ilala ambao wamekuja na barua zinazowatambulisha kuwa wao ni madiwani na kwamba hati hiyo ya mali isiyoamishika hawakuja nayo ila akaiomba mahakama impatie dhamana mteja wake.

“Ni hivi hapa hakuna kuombana omba masharti ya dhamana ndiyo hayo hapo juu nimeishayataja kwahiyo ninachotaka masharti hayo yatekelezwe kwa vitendo na siyo kuniomba sijui nini….kwanza nina kazi nyingi za kufanya siyo kesi hii moja…kwasababu mshtakiwa ameshindwa kutimiza masharti hayo ya dhamana naamuru amepelekwe gerezani hadi Desemba 20 mwaka huu, kesi hii itakapokuja kwaajili ya kutajwa”alisema kwa ukali Hakimu Lema na kufanya Mwigamba kunyong’onyea.

Baada ya hakimu huyo kusema hayo askari hao walimtoa kizimbani Mwigamba na kisha kumrudisha katika mahabusu ya mahakamani hapo tayari kwaajili ya kusubiri gari la kumpeleka gerezani.Gazeti hili lilimshuhudia mmoja wa ndugu wa mshtakiwa huyo akitoka ndani ya viwanja hivyo akienda kwenye maduka ya jirani na mahakama hiyo na kumnunulia maboksi ya juice mbili na kisha kumpelekea mstakiwa katika mahabusu hayo kabla ya kupakizwa kwenye gari na kupelekwa gerezani.

Hii ni mara ya kwanza kwa Tanzania kumfungulia kesi ya kushawishi au uchochezi mchangiaji wa makala kweny magazeti ya hapa nchini. Pia hii itakuwa ni mara ya pili kwa serikali kumfungulia kesi ya jinai Mwigamba tangu mwaka huu ulipoanza.

Kwani Mwigamba na Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu Dk.Wilbroad Slaa , mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini Godbless Lema na Mbunge wa Moshi Mjini Philemon Ndesamburo na wanachama wengine wanakabiliwa na kesi ya mkusanyiko na maandamano haramu waliyoyafanya Januari 5 mwaka huu, katika jiji la Arusha na kesi hiyo ipo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha na imefikia hatua ya kuanza kusikilizwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Desemba 9 mwaka 2011.

UPELELEZI KESI YA MATTAKA TAYARI

Na Happiness Katabazi


UPANDE wa Jamhuri katika kesi ya matumizi mabaya ya madaraka na kununua magari ya mitumba kinyume na Sheria ya manunuzi ya umma ya mwaka 2004 inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Shirika la Ndege(ATCL), David Mattaka na wenzake umeileza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.


Wakili Mwandamizi wa Serikali Oswalid Tibabyemokya alieleza hayo mbele ya Hakimu Mkazi Ritha Tarimo wakati kesi hiyo jana ilipokuja kwaajili ya kutajwa ambapo alieleza kuwa upelelezi huo umekamilika na kwamba wanaiomba mahakama hiyo ipange tarehe kwaajili ya kuja kuwasomea washtakiwa maelezo ya awali.

Kwa upande wake Hakimu Tarimo alisema anaiarisha kesi hiyo hadi Januari 5 kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya kutajwa na kwamba usikilizwaji wa awali utafanyika Januari 23 mwakani.

Novemba 22 mwaka huu, Mattaka anayetetewa na wakili Peter Swai na Kaimu Ofisa Mkuu wa Kitengo cha Fedha Elisaph Mathew Ikomba na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Ndani, William Haji anayetetewa na wakili Alex Mgongolwa walifikishwa mahakamabi hapo kwa mara ya kwanza wakikabiliwa na makosa kushindwa kutunza kumbukumbu za mawasiliano ya manunuzi waliyokuwa wakifanya na mtoa huduma kinyume na kifungu cha 55(3),87(1)(f) cha Sheria ya Manunuzi ya Umma Na. 21 ya mwaka 2004 na kanuni ya 17(1) ya Sheria ya Manunuzi (Goods,Works,Non-Consultant Services and Disposal of Public Asets by Tender) Regulation,G.N. No.97 of 2005.

Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa(TAKUKURU) alidai shtaka la pili ambalo linawakabili ni la kushindwa kutimiza matakwa ya vifungu vya Sheria ya Manunuzi ya Umma na Kanuni zake kinyume na kifungu cha 87(1)(f) cha Sheria ya Manunuzi ya umma ya mwaka 2004.

Shtaka la tatu lina mkabili Mattaka peke yake ni matumuzi mabaya ya madaraka kinyume na kifungu cha 31 cha Sheria ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa ya mwaka 2007 ambapo Mattaka alitoa idhini ya kununuliwa kwa magari hayo bila ya kuwepo kwa mkataba wa pande zote mbili na bila idhini ya Bodi ya ATCL.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Desemba 6 mwaka 2011.

MEJA JWTZ KORTINI KWA UTAPELI

Na Happiness Katabazi


MEJA wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kikosi cha 511 cha Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam, Muhsini Kombo (39) na Devotha Soko (33), jana walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kwa tuhuma ya kujipatia sh milioni 100 kwa njia ya danganyifu.



Mbele ya Hakimu Mkazi Waliarwande Lema, wakili wa Serikali, Ladslaus Komanya, alidai katika shitaka la kwanza kuwa Kombo pamoja na Devotha Soko walikula njama na kughushi kati ya Januari-Machi mwaka 2008.

Wakili Komanya alidai shitaka la pili ni kwamba Machi 25 mwaka 2008 kwa nia ya udanganyifu washitakiwa walighushi mhutasari wa kikao cha Machi 25 mwaka 2008 na kujaribu kuonesha kuwa familia ya marehemu Awadhi Shoo imemteua Devotha Soko kuwa msimamizi wa mirathi.

Katika shitaka la tatu inadaiwa kuwa Aprili 23 mwaka 2008 , Devotha alitoa nyaraka za uongo katika Mahakama ya Mwanzo Sinza jijiini Dar es Salaam, kwa lengo la udanganyifu na akajaribu kuonyesha ameteuliwa kusimamia mirathi ya familia ya marehemu Awadhi Shoo.

Katika shitaka la tano, inadaiwa kuwa Mei 15 mwaka 2008 katika Mahakama ya Mwanzo Sinza , Devotha alimpatia hakimu wa mahakama hiyo taarifa hizo ambazo si za kweli, kuwa marehemu Awadhi Shoo alifariki dunia mwaka 1986 akiacha watoto wawili, Juma na Asha na kwamba mshitakiwa huyo wa pili amesimamia mirathi hiyo huku akijua si kweli.

Imeelezwa kuwa Januari 21 mwaka 2011 kwa nia ya udanganyifu, washitakiwa wote wawili walijipatia sh milioni 100 kutoka kwa Rukia Zidadu baada ya kumuuzia nyumba iliyopo kitalu Na. 281 Block 46 huko Kijitonyama. Washitakiwa wamekana mashitaka na upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika.

Hakimu Lema alikubali dhamana ya fedha taslimu sh milioni 25 au kuwasilisha hati ya mali yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha.

Hata hivyo, Devotha alitimiza masharti hayo ya dhamana lakini Meja Kombo alishindwa kutimiza masharti hayo na amepelekwa rumande hadi Desemba 19 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwa ajili ya kutajwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Desemba 6 mwaka 2011.

MCHINA AHUKUMIWA, AKAMATWA TENA

Na Happiness Katabazi



MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, jana ilimhukumu kifungo cha mwaka mmoja jela au kulipa faini ya sh 100, 000 raia wa China Xuxiab We Ng (26) baada ya mshtakiwa kukiri kutenda kosa la kumzuia ofisa wa Idara ya Uhamiaji asifanye kazi yake.


Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Aloyce Katemana, muda mfupi baada ya Mwanasheria wa Idara ya Uhamiaji Patrick Ngayomela, kumsomea shtaka linalomkabili mshtakiwa ambaye anatetewa na wakili wa kujitegemea, Yassin Memba, na kisha mshtakiwa jana alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza kukiri kutenda kosa hilo.

Hakimu Katemana alisema kwa kuwa mshtakiwa amekiri kosa linalomkabili mahakama hiyo inamtia hatiani kwa kosa hilo ambalo ni kinyume na kifungu cha 31(1)(f) na (2) cha Sheria ya Uhamiaji, hata hivyo mshtakiwa huyo ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Teng Da Foot Wear Co Ltd, alilipa faini hiyo na kuachiliwa huru.

Dakika kumi baada ya raia huyo wa China kulipa faini, alijikuta akikamatwa na askari wa polisi wa mahakamani hapo na kisha kupelekwa kikuo kikuu cha Polisi Kati, kwa ajili ya kufunguliwa kesi mpya ya shambulio la kudhuru mwili.

Awali wakili wa Idara ya Uhamiaji, Ngayomela, akimsomea shtaka lake, alidai kuwa Novemba 30, mwaka huu, huko Kariakoo mshtakiwa huyo alimzuia Ofisa Uhamiaji Koplo Mussa Abdallah Mkubwa, kufanya kazi yake kwa kumshambulia na kumsababishia maumivu makali yaliyompelekea kulazwa hospitali akiwa hajitambui.

Na kwamba baada ya kumpiga mshtakiwa huyo alikamatwa na kupelekwa katika Kituo cha Polisi Kati na kuchukuliwa maelezo na alikiri kosa na iliamuriwa afikishwe mahakamani.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Desemba 3 mwaka 2011.

MAWAKILI WA LIYUMBA WAKWAMISHA KESI

Na Happiness Katabazi


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jana ilijikuta ikishindwa kuanza kusikiliza pingamizi la awali lililotarajiwa kuwasilishwa na mawakili wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba (63), anayekabiliwa na kesi ya kukutwa na simu gerezani kwa sababu ya mawakili hao kutokuwepo mahakamani bila kutoa taarifa rasmi.



Liyumba anayetetewa na mawakili wa kujitegemea Majura Magafu na Hudson Ndusyepo, alifika mahakamani na kudai kuwa Magafu amemweleza kuwa yuko Mahakama Kuu kwenye kesi nyingine na Ndusyepo kampeleka hospitalini baba yake mzazi kwani ni mgonjwa.

Hoja hiyo ilionekana kumkera wakili wa serikali Elizabeth Kaganda, ambaye alidai upande wa jamhuri ulikuwa tayari kwa ajili ya kuanza kusikiliza pingamizi la upande wa utetezi na kwamba anasikitishwa na kitendo cha mawakili hao kutofika mahakamani bila kutoa taarifa za udhuru kwa utaratibu unaostahili.

Kwa upande wake, Hakimu Stewart Sanga, alimweleza mshtakiwa huyo kuwa mawakili wake walipaswa kutoa taarifa mahsusi kama kweli wako Mahakama Kuu na kwa ajili gani kwani wakili kwenda kuhudhuria kesi Mahakama Kuu si jambo la kushtukiza.

Alisema anaiahirisha kesi hiyo hadi Desemba 21, mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwa ajili ya kusikiliza pingamizi la awali ambalo litawasilishwa na mawakili wa utetezi.

Septemba 8, mwaka huu, Liyumba alifikishwa mahakamani akikabiliwa na kesi ya kukutwa na simu gerezani kinyume na sheria za Magereza chini ya kifungu cha 86 (1,2) kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Desemba 3 mwaka 2011.

JERRY MURRO ASHINDA KESI




Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, imemwachilia huru aliyekuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC 1), Jerry Murro (30) na wenzake ambao walikuwa wakikabiliwa na makosa ya kula njama na kuomba rushwa ya sh milioni 10 baada ya upande wa Jamhuri kushindwa kuthibitisha mashitaka yao.

Sambamba na hilo, tayari Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP), Dk. Eliezer Feleshi kupitia Mkurugenzi Msaidizi wa ofisi hiyo, Stanslaus Boniface, jana saa 6:46 mchana aliwasilisha hati ya nia ya kuikatia rufaa hukumu hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na mahakama hiyo imekwisha kuipokea.

Hukumu hiyo iliyokuwa ikisubiriwa kwa shahuku kubwa na umma, ilisomwa jana kwa takriban saa mbili na Hakimu Mkazi, Frank Moshi, ambaye alisema baada ya kupitia kwa kina ushahidi wa mashahidi saba wa upande wa Jamhuri, mashahidi wanne wa upande wa utetezi na vielelezo vilivyotolewa na upande wa Jamhuri, mahakama hiyo imefikia uamuzi wa kuuona upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha kesi yao, kwakuwa ushahidi wao ni dhahifu na umeshindwa kuishawishi mahakama hiyo kuwatia hatiani washitakiwa hao.

Hakimu Moshi alisoma hati ya mashitaka iliyokuwa na jumla ya mashitaka matatu, ambapo shitaka la kwanza ni la kula njama kinyume cha kifungu namba 32, shitaka la pili ni kuomba rushwa ya sh milioni 10 kutoka kwa aliyekuwa mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Wage, kinyume cha kifungu cha 15(1)(a) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007 ambalo wanadaiwa kulitenda Januari 29, mwaka 2010.

Shitaka la tatu ambalo linamkabili mshitakiwa wa pili, Edmund Kapama ‘Dokta’ na mshitakiwa wa tatu, Deogratius Mugassa, ni kudai kuwa wao ni maofisa wa Takukuru kinyume cha kifungu cha 100 B cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007, ambacho kinasomwa pamoja na kifungu cha 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 ya mwaka 2002.

Hakimu Moshi alisema upande wa Jamhuri katika harakati zake za kuthibitisha shitaka la kwanza ilimleta shahidi wa tatu wa upande wa Jamhuri, Michael Wage, ambaye katika ushahidi wake alidai kukutana na washitakiwa hao katika Hoteli ya Sea Cliff Januari 29, mwaka jana, na kielelezo cha tatu ambacho ni picha za kamera ya CCTV ya hoteli hiyo ambayo alidai inaonyesha sura za washitakiwa hao na yeye na kwamba alikuwa akifanya mawasiliano kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu (SMS).

“Sasa mahakama imefikia uamuzi wa kuona ushahidi wa Wage una mapungufu kwani Jamhuri imeshindwa kuleta nakala ya mawasiliano ya ujumbe mfupi ‘print out’ ambazo zingethibitisha Murro alikuwa akiwasiliana na Wage.

“Pia kwa kitendo cha Jamhuri kushindwa kuleta video ya kuona mahakamani, gwaride la utambulisho na nakala halisi ya picha za CCTV zinazoonyesha washitakiwa wote kweli walikutana pamoja na Wage…mahakama hii inatamka wazi kuwa Jamhuri imeshindwa kuthibitisha kosa hili na kwa sababu hiyo inawaachilia huru washitakiwa wote katika kosa hili la kula njama,” alisema Hakimu Moshi.

Akilichambua kosa la pili ambalo ni la kuomba rushwa ambalo pia linawakabili washitakiwa wote watatu, alisema kwa mujibu wa ushahidi wa shahidi wa tatu wa upande wa Jamhuri, Wage alidai kuwa mshitakiwa wa pili na wa tatu (Kapama na Muggasa) walijitambulisha kwake kama wao ni maofisa wa Takukuru na wakamtaka awapatie kiasi hicho cha fedha kwakuwa yeye anakabiliwa na tuhuma za ubadhirifu wa fedha za umma ili wasimkamate na kwamba Murro alimwambia ampatie fedha hizo ili asiende kuzirusha tuhuma hizo kwenye kipindi cha Usiku wa Habari kinachorushwa na Televisheni ya TBC1, na kwamba Kapama alipokea kianzio ambacho ni sh 9,000,000 kwa ahadi kuwa kesho yake angekuja kuwamalizia kiasi kilichosalia katika kiwango cha awali walichokuwa wakikitaka kutoka kwake ambacho ni shilingi milioni 10.

Na kwamba Wage alidai Januari 30, mwaka jana alikwenda kutoa taarifa Kituo Kikuu cha Polisi kuwa kuna watu wanamuomba rushwa na kwamba polisi waliweka mtego ambapo waliondoka na shahidi huyo hadi mgahawa wa City Garden uliopo Mtaa wa Mkwepu jijini Dar es Salaam, na Wage akaamuliwa na polisi hao kumpigia simu Murro ili aje kuchukua kiasi cha fedha kilichosalia na kweli baada ya muda mfupi Murro alifika katika eneo la mgahawa huo na kabla ya kushuka kwenye gari alizingirwa na polisi waliokuwa wamemuwekea mtego waliokuwa wakiongozwa na shahidi wa nne, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Issa Chabu.

Hakimu huyo akilichambua shitaka hilo la pili, alisema mahakama imeshindwa kuelewa ni kwanini polisi hao siku hiyo walimkamata Murro kwa haraka kiasi kile na kwamba zile picha za CCTV kamera ambazo zilipokewa na mahakama kama kielelezo cha tatu hazionekani vizuri na kwamba haziusaidii upande wa Jamhuri kuonyesha uhalisia wa washitakiwa hao.

“Mahakama hii imeona Hoteli ya Sea Cliff ni eneo lenye shughuli nyingi sana na linatembelewa na watu wengi na Murro wakati akijitetea alidai kuwa alifika katika hoteli hiyo kwa ajili ya kusaka habari na kwamba kosa hili liliungwa mkono na ushahidi wa Wage na mahakama hii inasema Jamhuri imeshindwa pia kulithibitisha shitaka hili la pili na hivyo mahakama inawaachiria huru washitakiwa wote katika kosa la pili,” alisema Hakimu Moshi.

Kuhusu shitaka la tatu ambalo ni la kujitambulisha kwa Wage kuwa wao ni maofisa wa Takukuru linamkabili Kapama na Mugassa peke yao, hakimu Moshi alisema mahakama imejiuliza umakini wa Wage uko wapi kwani kama ni kweli washitakiwa walijitambulisha kwake kuwa wao ni maofisa wa Takukuru ni kwanini Wage asingeomba washitakiwa hao wampatie vitambulisho vyao?

Aidha, Hakimu Moshi alidai kuwa wakati Kapama na Mugassa wakijetetea waliyakana majina ya Dokta na Kaimu Mkurugenzi wa Takukuru ambayo upande wa Jamhuri ulidai washitakiwa hao walijitambulisha kwa Wage kwa majina hayo na kuongeza kuwa upande wa Jamhuri ulipaswa ufanye uchunguzi mitaani ili kubaini majina hayo na vyeo hivyo kama kweli washitakiwa hao wanavitumia mitaani.

“Mahakama imeonelea shitaka hili la tatu nalo limeacha mashaka makubwa kwani hakuna vielelezo vinavyoonyesha washitakiwa hao Kapama na Mugassa walijiwakilisha kuwa wao ni maofisa wa Takukuru na kwasababu hiyo mahakama hii inawaachiria huru washitakiwa wote kwenye kosa hili la tatu na makosa mengine yote, hivyo kuanzia sasa washitakiwa wote mpo huru na upande wowote kama haujaridhika na hukumu yangu una haki ya kukata rufaa katika mahakama ya juu,” alisema Hakimu Moshi.

Aidha, hakimu huyo alitoa amri kwamba Murro aliyekuwa anatetewa na mawakili wa kujitegemea, Richard Rweyongeza na Pascal Kamala wakati washitakiwa wengine walikuwa wakitetewa na Majura Magafu arejeshewe pingu na bastola yake ambayo ilitolewa mahakamani hapo na upande wa jamhuri kama vielelezo kwasababu vitu hivyo havikubishaniwa mahakamani hapo.

Baada ya kumalizika kusomwa kwa hukumu hiyo umati wa ndugu na jamaa wa washitakiwa hao waliwalaki kwa furaha ndugu zao hao ambao walishinda kesi hiyo nje ya viwanja vya mahakama hiyo huku ndugu mmoja wa Murro ambaye hakuweza kufahamika jina lake mara moja alikwenda kumkabidhi chupa ya mvinyo ambayo Murro aliipokea kwa furaha.

Akizungumza na waandishi wa habari nje ya viwanja vya mahakama hiyo huku akiwa ameambatana na mkewe Jeniffer John, Murro alisema amewasamehe baadhi ya viongozi wa serikali na maofisa wa Jeshi la Polisi ambao walimbambikizia kesi hiyo na kwamba yote ana mwachia Mungu.

“Natoa ushauri wa bure, wanachi wenzangu na maofisa serikali na polisi tuache kutafutana badala yake tufanye kazi kwa masilahi ya taifa letu, matatizo yaliyonikuta mimi yalikuwa ni yakunitafuta mimi lakini leo hii nashukuru nimeweza kuishinda kesi yangu na ninawashukuru wale wote waliokuwa karibu na mimi katika matatizo haya wakawa wananiombea na kwa moyo mmoja natamka rasmi kuwa nimewasamehe wale viongozi wa serikali na jeshi la polisi ambao walibambikia kesi hii,” alisema Murro huku akijifuta machozi na kisha kuondoka mahakamani hapo.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi Msaidizi katika ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka nchini, Stanslaus Boniface, akizungumza na Tanzania Daima jana mchana alisema Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini inayoongozwa na Dk. Eliezer Feleshi haijaridhika kabisa na hukumu hiyo na kwamba jana hiyo hiyo saa saba mchana walikuwa wameishawasilisha hati ya nia ya kukata rufaa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Februari 5, mwaka 2010, washitakiwa hao walifikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani hapo wakikabiliwa na mashitaka hayo ya kuomba na kupokea rushwa kutoka kwa Michael Wage, mashitaka ambayo waliyakana na kwa wakati wote huo hadi jana kesi hiyo ilipotolewa hukumu washitakiwa hao walikuwa nje kwa dhamana.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Desemba 1 mwaka 2011.