NI MGOMO WA MADAKTARI AU?



Na Happiness Katabazi

KWA takribani wiki moja sasa vyombo vya habari vimekuwa vikipambwa na habari za mvutano baina ya serikali na madaktari kuwa wamegoma kufanyakazi kwa kile wanachodai kupandishiwa mishahara, kujengewa nyumba za kuishi na kuongezewa masurufi yao.

Taarifa za mvutano huo binafsi zimekuwa zikinikosesha raha na kunikera mno na kuanza kutamani kuwa na viongozi madikteta.

Nao baadhi ya madaktari walinukuliwa wakisema wameishapita kiwango cha kuongea na waziri wa afya na Ustawi wa Jamii, Dk.Juma Mponda kwani ameshindwa utatua mwenye uwezo wa kuongea nae hivi sasa ni Waziri Mkuu Mizengo Pinda na kushinikiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Brandina Nyoni, hii ni dharau ya aina yake.

Wakati madaktari hao wakitoa maneno hayo, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk.Mponda, Alhamisi ya wiki iliyopita aliifanya mkutano na waandishi wa habari na kutoa tamko la serikali na ufafanuzi kuhusu madai ya madaktari hao na bila kumung’unya maneno alisema serikali haiwezi kuwaongezea mishahara na kufikia shilingi milioni 3.5 kwa kuwa kada hiyo inalipwa vizuri.

Dk.Mponda alisema mishara ya watumishi wa serikali hufuata miundombinu ya watumishi iliyopo ambayo iliboreshwa kwa sekta ya afya na hivi sasa watumishi wa afya wanapata mishahara mikubwa kuliko watumishi wengine serikalini.

Ieleweke kwamba baadhi ya madai ya madaktari ni ya msingi na tayari serikali imesema inayafanyia kazi.

Ila sikubaliani na hatua ya madaktari hao kukiuka viapo vyao walivyoapa kuwa wataakikisha wanahudumia wagonjwa katika mazingira yoyote yale lakikini hivi sasa wameamua kuwatoroka wagonjwa nakwenda kufanya migomo na kufanya deiwaka katika mahospitali binafsi ili waweze kujiongezea kipato.

Na kitendo hicho hakina tofauti na jambazi ambaye anamwelekezea bunduki kichwani mwananchi akimtaka ampatie fedha ama sivyo anamuua au akina tofauti na daktari ambaye anamtibu mgonjwa halafu anamwambia hawezi kukupatia dawa hadi unipatie hongo..

Kwanza nakubaliana na maelezo ya Waziri Mponda kuwa suala la kupandishiwa mishahara na masurufi mingine kwa watumishi wa umma kuna utaratibu wake.Wafanyakazi wa serikali wanaodai kuongezewa mishahara na masurufi mengine wanapaswa kufuata utaratibu mahususi ulianishwa ndani ya Civil Service Negotiation Machinery Act, na kama serikali itashindwa kutekeleza madai yao yaliyofuata utaratibu wa sheria sheria hiyo wanaruhusiwa kugoma.

Sasa tuwaulize hawa madaktari walifuata utaratibu ulioanishwa katika sheria hiyo hadi wafikie uamuzi wa kugoma ?

Na kama hawakufuata utaratibu sheria za nchi zipo wazi ambazo zinawabana wale wote wanaofanyakazi au kutoa ushahidi chini ya kiapo na pindi wanapokiuka viapo vyao wanatakiwa waadhibiwe mara moja.

Maana ni wenyewe walieleza kuwa madai yao waliyafikisha wizarani na waziri Mponda akasema aliupokea ujumbe wa chama cha madaktari na wakajadiliana na serikali ikaueleza ujumbue huo kuwa baadhi ya madai yao serikali inayafanyia kazi.

Na baada ya Dk. Mponda kutoa ufafanuzi huo,hatujakisikia chama hicho cha madaktari kikipinga maelezo ya waziri huyo kwa kutoa ushahidi mbadala matokeo yake tunakisikia chama hicho kikisema kuwa hadhi hayo kwa sasa si ya kuongea na waziri huyo ,hadhi yao hivi sasa ni yakuzungumza na waziri mkuu.

Haya Pinda waliokuwa wakimtaka alikwenda Karimjee kuzungumza na madaktari hao lakini madaktari hao walishindwa kutokea kwa sababu za kijinga ambazo sasa zimetulazimu tuanze kuwamini huu siyo mgomo wa madaktari bali unaajenda mbaya nyuma yake.

Hivi nani kairoga nchi hii?Madaktari ndiyo wenye shida na waziri Mponda ndiyo waziri wao lakini cha kushangaza madaktari hao ambao ndiyo wenye shida wamegeuka kuwa manyapara wa kutoa amri ya wanataka nini na nani wazungemze na nani na cha ajabu hadi sasa serikali inaendelea kuwakumbatia?

Nyie madaktari kwa akili zenu waziri alichokizungumza mnafikiri kabla ya kukizungumza huyo waziri mkuu Pinda alikuwa akijui? Waziri wenu kasema serikali inayafanyiakazi madai yenu hamsikii sasa mnataka nini?

Tuulize ule ujumbe wa madaktari uliokiwenda kuzungumza na Dk.Mponda kuhusu madai yao na akawasikiliza, walikuwa hawajui waziri huyo siyo saizi yao na kwamba hana huwezo wa kuwatatulia kero zao?Mlimfuatia nini ?

Ni lini wamegundua waziri Mponda siyo saizi yao? Je ni baada ya waziri huyo kuwaambia ukweli kuwa haitaweza kuwapandishia mshahara?

Na wewe Pinda aibu uliyoipata jana ulijitakia kwani haiwezekani wewe ndiyo Waziri Mkuu Mawaziri wote wapo chini yako na wanakusaidia katika utendaji kazi wako wa kila siku, madaktari hao wanamtolea maneno ya shombo waziri wa Afya Dk.Mponda na maofisa wake ambao ndiyo wenye dhamana ya sekta hiyo, halafu na wewe unakubaliana na upuuzi na dharau hiyo ya madaktari kwa waziri wako , unakwenda kuwaona , na matokeo yake na wewe wamekudhalilisha umejikuta ukumbini peke yako.

Nchi hii hivi sasa si ngazi ya familia wala nje ya familia, hatuheshimiani tunadharauliana bila sababu za msingi. Hajulikani baba ni nani, mama ni nani, mkubwa ni nani,mtoto ni nani na kiongozi ni nani kila mtu anaongea na kufanya analotaka.Na hali hii isipotokomezwa ipo siku taifa hili litajikuta limetumbukia mtoni.

Kwa akili yenu nyie madaktari mliogoma, hivi hayo madai mnayodai ya kupandishwa mshahara ndiyo mtapandi leo leo? Je hizo nyumba mnazodai mjengewe ndiyo ujenzi wake utakuwa umekamilika ndani ya siku mbili?

Lakini wafanyakazi wengine kwa uhalisia wa fani zao walioajiriwa serikali hawawezi kufanyakazi kazi serikali na sekta binafsi kwa wakati mmoja lakini wafanyakazi wa aina hiyo hatujawasikia wakigoma.

Sasa kama hivyo ndivyo ni kwanini madaktari mnaofanyakazi sehemu mbili na mwisho wa mwezi mnapata mishahara miwili.Mbona kule kwenye hospitali za sekta binafsi mnapofanyiakazi hamuwagomeagi mnakuja kuigomea serikali?

Na kama mnaona serikali iliyowaajiri haiwalipi vizuri si mtafute sehemu nyingine ambako mtalipwa vizuri kuliko kung’ang’ania kufanyakazi sehemu ambayo hulipwi vizuri ambapo mwishoe mtakuja kuwaua makusudi wagonjwa kwa kuwachoma sindano za mikojo ili wafe?

Na kama siyo ubinafsi na unafki ni nini, kipindi hicho mmeongezewa mishara na masulufi hatukuwasikia mkijitokeza adharani kutangaza mmeongezewa mishahara?
Watanzania wanaheshimu haki za binadamu sote tuamke tuupinge mgomo huo kwani mgomo huo ni haramu na umeanza kuleta madhara makubwa kwa wananchi wetu ambao hawana uwezo wa kwenda kutibiwa hospitali binafsi na nje ya nchi.

Ieleweke wazi kuwa ni kweli gharama za maisha zimepanda na ukali huo wa maisha unatuhumiza wote lakini hicho kisiwe kigezo cha madaktari wetu kutoroka wagonjwa mahospitali na kwenda kufanya migomo huku wananchi wasiyo na hatia wakipoteza maisha kwa kukosa huduma.

Minaamini kuwa kila mtu awe na elimu na asiye na elimu ana umuhimu hapa duniani na wote tunategemeana hivyo ni vyema na haki madaktari wakaacha na kingizio kuwa taaluma yao ni muhimu kuliko taaluma zingine.

Mwisho nimalizie kwa kuishauri serikali ijenge utaratibu wa kuyashughulikia mapema malalamiko ya kada yoyote inayoyalalamikia kabla ya kada hizo kuanza kujichukulia sheria mkononi na kugoma kwani mwisho wa siku wanaothirika ni wananchi na taifa linajikuta likipata sifa mbaya kuwa taifa la Tanzania hivi sasa limekuwa ni taifa la migomo.

0716 774494
www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatatu, Januari 30 mwaka 2012

MLIOADHIBIWA UDSM MMEVUNA MLICHPANDA


Na Happiness Katabazi

MAKAMU Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,Profesa Rwekaza Mukandala ,Januari 10 mwaka huu alitangaza kuwafukuza chuo wanafunzi 13 akiwamo Spika wa Serikali ya Wanafunzi(DARUSO), Peter Arnold na wengine 86 kuwasimamisha miongoni mwao ni Rais wao, Kilawa Simon.


Hatua hiyo ilifikia baada ya hali katika chuo hicho kuwa tete kwa siku tatu mfululizo baada ya wanafunzi wa DARUSO kufukuzwa chuo siku hiyo kwa shinikizo la kuanzisha mgomo wenye nia ya kuwarejesha wenzao 48 na wanne waliosimamishwa Desemba mwaka jana.

Aidha kwa kipindi cha Desemba mwaka jana hadi sasa ni wanafunzi 61 waliofukuzwa na 90 kusimamishwa wakipisha uchunguzi kufanyika na ikigundulika wana makosa watafukuzwa na na watakaoonekana kutokuwa na makosa watarejeshwa kuendelea na masomo.

Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kusema maneno yafuatayo kwamba ‘ukweli una tabia moja nzuri sana hauchagui rafiki wala adui’.

Hivyo kwa nukuu hiyo ya Baba wa Taifa kwanza nafahamu wazi mtazamo huu hautawafurahisha wanafunzi waliofukuzwa na kusimamishwa lakini naomba wanivumilie.
Ikumbukwe kuwa Tanzania ni nchi ambayo inajiongoza kwa utawala wa sheria hivyo kila mwananchi na viongozi wetu wanapotenda kazi au kufanya mambo yao lazima wahakikishe wanafuata na kuzingatia taratibu zote za kisheria.

Hivyo basi hata wale wanafunzi vyuoni hasa baadhi ya wanafunzi wa UDSM pindi wanapokuwa na madai yao wanapaswa kufuata taratibu zote za sheria zilizoanzisha vyuo vyao na sheria nyingine za nchi kudai madai yao na siyo kuamua kujichukulia sheria mkononi kwa kuanzisha migomo haramu, kufunga barabara na kuwacharaza bakora wanafunzi wenzao ambao hawawaungi mkono katika hiyo migomo yao haramu .

Labda tuwakumbushe hao wanafunzi wa UDSM kwamba sheria ni msumeno.Na pindi sheria inapoanza kutumiwa dhidi ya wavunja sheria haibagui kuwa huyu ni mwanachuo asishtakiwe mahakamani au kuadhiwa kwa njia yoyote ile au huyu ni maskini.

Pale UDSM kuna wanafunzi ambao wanafahamu vyema kilichowapeleka pale ni masomo na wengine nafikiri hivi sasa wamesahau kilichowapeleka pale na matokeo yake wamekengeuka na kuanza kila kukicha kuanzisha vurugu kwa kisingizio cha hali ngumu ya maisha kwa Bodi ya Mikopo haijawaingia fedha kwenye akaunti mara wale wenzao wanaokabiliwa na kesi ya mkusanyiko haramu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Desemba mwaka jana eti warudishwe chuo wakati wengine wamesimamishwa na wengine kufukuzwa.

Hivi nyie wanachuo mliokuwa mkiendesha huo mgomo haramu wiki iliyopita aliyewaambia UDSM ina mamlaka ya kuwafutia kesi wanafunzi hao nani?Kwanini msingeenda kumvamia Hakimu Waliarwande Lema anayesikiliza kesi hiyo au ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka(DPP), Dk.Elizer Feleshi kuwashinikiza wafute hiyo kesi kwani ndiyo hasa wenye mamlaka hayo?Ni kiwaita nyie ni wabaguzi na mnalenu jambo nitakuwa nimekosea?

Wale wanafunzi wanaokabiliwa na kesi si watanzania kama wale watanzania wengine ambao kila kukicha wanafunguliwa kesi mahakamani na wengine wanazeekea magerezani, mbona hatujawahi kuwasikia mkijitokeza kuandaa mgomo kushinikiza nao wafutiwe kesi?Maana kinachotuunganisha sisi Utanzania wetu.

Imeanza kuonekana ni kawaida sasa kusikia kila kukicha wanafunzi wa hasa wale wa UDSM wakigoma bila kufuata taratibu na hakuwa hata mzazi mmoja au wale wanaojiita wanaharakati kujitokeza kukemea vitendo hivyo vya ufunjifu wa amani na utovu wa nidhamu unaofanywa na wanafunzi hao kwa kigezo kuwa wanakabiliwa na matatizo mengi likiwemo la bodi ya mikopo kuwacheleweshea fedha zao.

Ieleweke kwamba ni wanafunzi hawa hawa siku za mbele ndiyo wanaweza kuwa viongozi katika taasisi za serikali,siasa na sekta binafsi sasa inapotokea leo hii wanafunzi hawa leo hii hawajahitimu masomo wala kutwaa madaraka wanaanza kufanya vitendo vya kidikteta vya kuwacharaza bakora wanafunzi wenzao ambao hawataki kugoma,inasikitisha na kutisha sana.
Hapo zamani wanafunzi wa UDSM walikuwa ni wanafunzi ambao walikuwa wakishiriki kwenye midahalo na kutoa fikra zao ambazo zilikuwa zikileta changamoto kwenye jamii, licha kulikuwepo pia migomo licha haikuwa ya mara kwa mara kama hii.

Lakini leo hii hayo hayapo tena kwani kuna taarifa za kuaminika kuwa baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakitumiwa na wanasiasa kuanzisha migomo mara kwa mara na bila kufuata taratibu na wanafunzi wengine wanafuata mkumbo na kusahau kuwa kilichowapeleka pale ni kusoma na siyo kutumiwa na wanasiasa na kuanzisha migomo.

Na nyie wanafunzi mnaokubali kutumiwa na wanasiasa mkae mkijua hapo chuoni ulikwenda peke yako na utaondoka peke yako hivyo siku ukifukuzwa chuo hao wanasiasa hawatawasiadia lolote kwani mkae mkijua UDSM ina sheria zake ndogo ndogo ambapo pindi uongozi wa chuo ukiamua kuzitumia ni wazi wale wanafunzi ambao wanashiriki kwenye vitendo vya uvunjifu wa sheria watafukuzwa na hasara wataipata wao na familia zao.
Misioni mankiti
ya wanafunzi hao kila kukicha kuzua migomo, kutoa lugha chafu na kuwachara bakora wenzao na kuwatoa madarasani kwa kigezo kuwa wanashinikiza bodi iwaingizie fedha kwenye akaunti kwa muda wanaoutaka wao wakati wanafunzi hao hao wengine wanawazazi ambao wanauwezo wa kuwalipia ada lakini hawawalipii ada lakini wanafunzi hao hatujawasikia wakiwaletea vurugu au kuwapiga baba zao kwa kigezo cha kushindwa kuwalipia ada.

Tujiulize leo hii ni wanafunzi wangapi ambao wamekosa fursa ya kulipiwa ada ya vyuo vikuu na bodi ya mikopo lakini wanafunzi hao wanasoma katika mazingira magumu sana na wamegeuka kuwa matonya wa kuomba ada huku na kule kwenda kulipa vyuoni lakini hata siku moja hatujawasikia wanafunzi hao wakifanya vurugu?

Ni baadhi ya wanafunzi hawa hawa wa UDSM mwishoni mwa mwaka jana siku ile ya Sherehe ya miaka 50 ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo Rais Jakaya Kikwete, Rais wa Uganda Yoweli Mseveni walikuwepo kwenye sherehe hizo lakini wanafunzi hawa kwa kukosa nidhamu walimzomea kwa mabango rais Kikwete.

Rais Kikwete alivumilia hali hiyo na aliendelea na maadhimisho hayo na ilipofika wakati wa kutoa hotuba yake alisoma hotuba yake ambayo ilionekana kutoa matumaini mapya ya maendeleo kwa chuo hicho kwani ndani ya hotuba hiyo alisema serikali yake itatenga fedha kwaajili ya upanuzi wa ujenzi wa majengo wa chuo hicho hali iliyosababisha wale wale waliokuwa wakimzoea nao kuanza kumpigia makofi.

Katika mila na desturi za Afrika na jamii iliyostaarabika ni lazima mtoto awe na heshima kwa mkubwa wake , lakini kwa kile kitendo kilichofanywa na baadhi ya wanafunzi wale kumzoea rais wan chi Kikwete siku hiyo ni dhahiri kwa watu tunaotazama mbali, kitendo kile kilituthibitishia kuwa wale wanafunzi waliofanya kitendo kile ni wahuni,wasiyoheshimu wakubwa na viongozi na kuwa uenda hata majumbani kwao hawawaheshimu wazazi wao.

Ifike mahala sasa uongozi wa Chuo Kikuu chini ya Profesa Mukandara uamke na kuanza kurejesha na kutetea heshima ya UDSM kwa kuwashughulikia bila huruma wanafunzi wote wanajihusisha na vitendo vya uvunjifu wa sheria chuoni hapo kwa madai kuwa wanakabiliwa na maisha magumu kwani hakuna ubishi kwamba chuo hicho hivi sasa ndani ya nchi za Afrika Mashariki kimeanza kuwa na sifa mbaya ya wanafunzi wake kuanzisha migomo kila kukicha badala ya kuingia madarasani kusoma.

Chuo KIkuu cha Dar es Salaam, kina historia ndefu na kimezalisha wasomi wengi na wazuri ambao hivi sasa wanatamba katika nchi nyingi duniani, sasa serikali na Profesa Mukandara msikubali sifa hiyo ya kitaaluma iliyokuwa nacho chuo hicho ipotee kwaajili ya wanafunzi wachache ambao wana hulka za kihuni ambao wanapoteza muda mwingi wa kuandaa maandamano badala ya kujisomea.

Ni kweli chuo hicho kinakabiliwa na changamoto kadhaa kama uchache wa mabweni, miundombinu ya majitaka,madara na mengineyo lakini changamoto hizo zisiwe kigezo cha wanafunzi hao kudai kwanjia ya uvunjifu wa sheria kutatuliwa kwa changamoto hizo.
Nawataka nyie wanafunzi ambao mnadai mnadai haki zenu kwa njia ya migomo haramu mtambue kuwa hata sisi tunaofanyakazi maofisi tena tunafamilia zinatutegemea pia na sisi tunakabiliwa na changamoto kadhaa ambazo zinatakiwa zitatuliwe na wamiliki au viongozi wa maofisi tunayofanyia kazi, lakini sisi wafanyakazi tumekuwa tukifuata taratibu na njia za amani kufikisha vilio vyetu vya kutaka changamoto hizo zitatuliwe na kweli wakati mwingine zinatatuliwa na nyingine hazitatuliwi kwa muda tunautaka sisi na tunavumilia.

Nimalizie kwa kuwaasa kuwa kumbukeni kuwa nyie baadhi ya wanafunzi mnaoshiliki kwenye migomo kila kukicha pale UDSM ni kusoma na siyo kutumiwa na wanasiasa au kudai haki zenu kwanjia ya uvunjifu wa sheria za nchi mkae mkijua mwisho wa siku mtaangua kwenye mikono ya dola na mtashughulikuwa kama wanashughulikiwa watuhumiwa wengine ambao si wanafunzi.

Kwani inasikitisha sana kuona mzazi kwa moyo mweupe anamruhusu mtoto wake aende kusoma UDSM halafu mtoto huyo anafika chuoni hapo anasahau kilichompeleka pale na dhiki za nyumbani kwao anaanza kujiingiza kwenye makundi ya wanafunzi wapuuzi ambao wanachowaza ni migomo kuliko kusoma mwisho wa siku mzazi anasikia mtoto wake amekamatwa na kufikishwa Mahakamani kwa makosa ya mkusanyiko usiyo halali au kusimamishwa shule au kufukuzwa chuo kabisa.Kwa kweli inaumiza sana.

Na ndiyo maana katika makala yangu ninawaasa wazazi,vyombo vya habari ambao si tu wana watoto wanaosoma pale UDSM kuanza kuwakemea wanafunzi wanaoshiriki kufanya uhuni huo kuliko kila kitu kuuachia uongozi wa chuo na serikali kuwakemea wanafunzi wanaotenda vitendo hivyo kwani kushindwa kufanya hivyo ndiyo kunasababisha wakati mwingine wanafunzi hao kuwa na jeuri ya kuendelea kutenda vitendo hivyo kwani hakuna watu wa kuwakemea.

Leo hii kuna baadhi ya wazazi au wafanyakazi waliojaliwa kuwa na kipato kikubwa wameamua kutotaka watoto wao wakasome UDSM kutokana na uhuni huo ambao ni wazi na taratibu unaanza kuporomosha heshima ya chuo mbele ya jamii jambo ambalo ni hatari kwa chuo kama hicho ambacho kinamilikiwa na serikali yetu.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika

0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne,Januari 17 mwaka 2012.

MGOMBEA URAIS WA UPINZANI BURUNDI,AFIKISHWA KISUTU

Na Happiness Katabazi

ALIYEKUWA mgombea urais wa chama kimoja cha upinzani nchini Burundi, Alex Sinduhnje, jana alifikishwa katika mahabusu ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, lakini hata hivyo hakuweza kupandishwa kizimbani.

Sinduhnje ambaye anatetewa na wakili wa kujitegemea, Hurbet Nyange, alifikishwa majira ya saa tatu asubuhi, katika eneo la mahakama hiyo na makachero wa polisi tayari kwa ajili ya kusubiri kupandishwa kizimbani lakini hata hivyo haikuweza kufahamika angefunguliwa mashtaka gani.

Gazeti hili lilipofika saa 6:47 mchana liliwashuhudia makachero wa Jeshi la Polisi wakimuondoa mtuhumiwa mahakamani hapo na kumpeleka polisi kwa kutumia gari aina ya Discovery lenye namba za usajili 280 AEN.

Baada ya hali hiyo kutokea waandishi wa habari za mahakamani walimfuata Mwendesha Mashtaka Kiongozi wa Mahakama hiyo, Elizabeth Kaganda, ili kupata ufafanuzi ni kwa nini hajapandishwa kizimbani, na kusema kuwa baadhi ya taratibu za kisheria zilikuwa hazijakamilika.

“Kwa kuwa taratibu za kisheria kuhusu tuhuma zinazomkabili Sinduhnje hazijakamilika ofisi yangu imeliagiza Jeshi la Polisi kwenda kufanyia marekebisho hayo na kuondoka na mtuhumiwa huyo na kwenda kumhifadhi katika mikono yao na pindi taratibu hizo zitakapokamilika hatua nyingine zitafuata,” alisema Kaganda.

Kufikishwa kwa Sinduhnje mahakamani hapo, kulimfanya Mwenyekiti wa Chama cha DP, Mchungaji Christopher Mtikila, kufika kwa ajili ya kumsaidia, lakini alidai kuwa makachero wa polisi walimkataza asiende kuzungumza na mtuhumiwa huyo hali iliyomfanya Mtikila kukaa kwenye chumba cha mawakili kwa ajili ya kusubiri taratibu zilizokuwa zikiendelea dhidi ya mshtakiwa huyo.

“Huyu Sinduhnje ni mpinzani ambaye amemsumbua sana Rais wa Burundi, Pier Nkurunzinza, katika uchaguzi uliopita na nimepata taarifa kuwa serikali ya Tanzania inataka imrudishe Burundi na mimi maoni yangu sitaki arudishwe kwao kwani akirudishwa kule anaenda kukatwa kichwa,” alisema Mtikila.

Mtikila alisema kwa taarifa alizonazo ni kwamba serikali ya Burundi inamtaka mtuhumiwa huyo arudishwe Burundi ili akakabiliane na kesi za kubambikwa za mauji kwani uchaguzi ulipomalizika alikimbilia Ulaya akakaa huko na ndiyo hivi karibuni kaingia hapa nchini na kukamatwa, haelewi kama mtuhumiwa huyo aliua kwa kutumia simu au intaneti.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Januari 14 mwaka 2012.

LIYUMBA AOMBA AFUTIWA KESI

Na Happiness Katabazi

ALIYEKUWA Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba, ambaye kwa sasa anakabiliwa na kesi ya kukutwa na simu akiwa katika gereza la Ukonga, ameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, iifute kesi hiyo kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kuisikiliza.

Kesi hiyo ambayo inasikilizwa na Hakimu Mkazi, Stewart Sanga, jana ilikuja kwa ajili ya kusikiliza pingamizi lililowasilishwa na wakili wa Liyumba, Majura Magafu, kwa ajili ya kuwasilisha pingamizi ambalo linataka mteja wake afutiwe kesi hiyo kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kwa sababu taratibu za awali za sheria ya Magereza ya mwaka 2002 hazikufuatwa.

Wakili Magafu alidai kwa mujibu wa sheria ya magereza ya mwaka 2002 inataka mshtakiwa anayeishi mahabusu kabla hajaletwa mahakamani asomewe mashtaka na ofisa wa magereza hukohuko gerezani na endapo atapatikana na hatia atapewa adhabu na aendapo mshtakiwa huyo ataonekana amekuwa mtendaji sugu wa makosa akiwa gerezani ndipo italazimika afunguliwe mashtaka katika mahakama za uraiani.

Akipangua hoja za upande wa utetezi Wakili wa Serikali Eliezabeth Kaganda alianza kwa kusema kuwa kesi ya aina hiyo inayomkabili Liyumba siyo ya kwanza kufunguliwa katika mahakama za hapa nchini.

Kaganda aliitaja kesi ya jinai Na. 472/2009 iliyokuwa ikimkabili Juma Matonya katika Mahakama ya wilaya ya Temeke ambapo hakimu Mzava alimhukumu kifungo cha miezi sita jela baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kukutwa na simu gerezani.

Na kesi nyingine mbili za aina hiyo hiyo, ambazo washtakiwa walitiwa hatiani moja akitakiwa alipe faini ya shilingi 20,000 na nyingine kwenda jela miezi sita.

“Kwa kesi hizo ambazo ni mifano hai, upande wa jamhuri unapinga hoja ya wakili ya utetezi inayotaka sisi tulete vielelezo kuonyesha hatua zilizofanyika kwa kuwa kuna mashahidi wa upande wa mashtaka watakaokuja kueleza kila kitu,” alidai wakili Kaganda.

Wakili Kaganda alieleza kuwa kabla hawajamfikisha Liyumba mahakamani hapo Jeshi la Magereza lilikuwa na mamlaka ya kushughulikia tuhuma zilizokuwa zikimkabili mshtakiwa na kwamba mkurugenzi wa mashtaka, na maofisa wa magereza walikuwa wameishaamua kuifungua kesi hiyo mahakamani hapo, kwa sababu hiyo haikuwa mara ya kwanza kukutwa na simu gerezani na alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa shinikizo la damu hivyo haikuwa rahisi kumpa adhabu akiwa gerezani.

Aidha akijibu hoja za Kaganda, wakili Magafu alieleza kwa kudai kuwa kwanza anamshukuru wakili huyo kukubali hoja yake ya maofisa wa magereza kuwa alikuwa na mamlaka ya kushughulikia tuhuma zilizokuwa zikimkabili mshtakiwa.

Magafu aliipinga hoja ya wakili huyo wa serikali kuwa mshtakiwa alipokuwa gerezani alikuwa ni mtendaji sugu wa makosa hayo ya kukutwa na simu gerezani lakini eti magereza ilishindwa kumwadhibu kwa sababu alikuwa anaugua ugonjwa wa shinikizo la damu kwa sababu haina ushahidi wowote kwani hata kama ni kweli alikuwa akiyatenda makosa hayo hakuna ushahidi unaonyesha alishawahi kufikishwa mbele ya maofisa wa magereza na kuchukuliwa hatua.

Akizungumzia kuhusu kesi zile tatu zilizotolewa hukumu na mahakama ya Temeke, wakili Magafu alidai kuwa upande wa utetezi haufahamu kesi hizo zilifunguliwa katika mazingira gani hivyo Kaganda alipaswa alete nakala za hukumu hizo ili waweze kuzisoma.

Kwa upande wake Hakimu Mkazi Stewart Sanga alisema amesikiliza hoja za pande zote mbili na kwamba atakuja kutoa uamuzi wake Januari 27 mwaka huu.

Septemba 8 mwaka jana, kwa mara nyingine tena Liyumba alifikishwa mbele ya hakimu Sanga akikabiliwa na kosa la kukutwa na kitu kilichokatazwa gerezani chini ya kifungu cha 86 (1,2) cha sheria ya Magereza kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Wakili Kaganda alidai kuwa Liyumba ambaye wakati huo alikuwa ni mfungwa mwenye Na.303/2010, Julai mwaka jana, ndani ya gereza la Ukonga, alikutwa na simu ya Nokia Na.1280 nyeusi iliyokuwa na laini yenye Na. 0653-004662 na IMEI Na. 356273/04/276170/3 ambayo alikuwa akiitumia kufanyia mawasiliano binafsi wakati ni kinyume cha sheria.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Januari 14 mwaka 2012

WANNE UDSM WAENDA JELA KWA KUKOSA DHAMANA

Na Happiness Katabazi

WANAFUNZI wanne kati ya 51 wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), wanaokabiliwa na kesi ya kufanya mkusanyiko haramu wamepelekwa rumande baada ya kushindwa kukamilisha masharti ya dhamana waliyopewa.

Waliopelekwa rumande ni Elias Mwambapa, Alphonce Lusako, Moris Denis na Jabir Ndimbo ambao walishindwa kukamilisha masharti ya dhamana ya kuwa na mdhamini mmoja wa kuaminika na kusaini hati ya dhamana ya Sh 1 milioni kwa kila mshtakiwa.
Hatua hiyo ilikuja baada ya uongozi wa Chuo hicho Kikuu cha Dar es Salaam kujivua udhamini wa wanafunzi 41 kati ya 51, Desemba 20, mwaka jana.

Wakili wa Serikali Elizabeth Kaganda alidai mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Waliarwande Lema kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.

Kaganda alidai kuwa jana kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya washtakiwa kusomewa maelezo ya awali na kupeleka wadhamini wapya baada ya uondozi wa chuo kujitoa.

Baada ya kutolewa kwa maelezo hayo, hakimu Lema aliiahirisha kesi hiyo hadi Januari 23, mwaka huu watakaposomewa maelezo ya awali yanayohusiana na kesi yao.

Katika kesi hiyo, mshtakiwa wa 31, anadaiwa kuwa si mwanafunzi wa chuo hicho, bali ni kibaka aliyetumia jina la mwanafunzi wa chuo hicho la Said John wakati jina lake halisi ni Hassan Suleiman hata hivyo ilibainika kuwa anakabiliwa na kesi nyingine katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni.
Awali, Ambinyiel Maro akiwasilisha barua kutoka kwa uongozi wa chuo hicho mbele ya Hakimu Stewart Sanga alidai kuwa uongozi wa chuo unajivua udhamini kwa wanafunzi 41.

Mahakama hiyo ilipokea maombi hayo, lakini Hakimu Sanga alisema anatoa nafasi mpaka Januari 10, mwaka huu kwa wanafunzi hao 41 kutafuta wadhamini wengine kuliko kuwarudisha rumande.

“Kisheria haitakuwa haki kupokonya udhamini kwa washitakiwa hao kwasababu imekuwa ni ghafla leo hawakujiandaa , hawakujua kama kuna barua hiyo,” alisema Hakimu huyo.

Alitoa tahadhari kwa wanafunzi hao kujiandaa kupeleka wadhamini kwa masharti yale yaliyowekwa awali na ambaye hatayekuwa hana mdhamini atakuwa amevunja masharti ya
dhamana, hivyo ataenda rumande.

Novemba 14, mwaka huu, wanafunzi hao walifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza na kudaiwa kuwa katika eneo la Mlimani, kwa pamoja walifanya mkusanyiko usio wa halali na kusababisha uvunjifu wa amani katika eneo hilo.

Shitaka jingine walidaiwa kukaidi amri ya askari walipoambiwa watawanyike. Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Rwekaza Mukandala wiki iliyopita alifafanua kuwa kati ya wanafunzi 51 waliokuwa wamefikishwa Kisutu, 43 kati yao ndio waliofukuzwa, watatu sio wanafunzi wa chuo
hicho, tisa hawajasikilizwa na Baraza la Chuo hicho na kutolewa mapendekezo.

Alisema matukio yaliyojiri ni mwendelezo wa matukio ya uvunjifu wa amani ambapo kila mara vitendo hivyo vilianzishwa na kikundi kidogo cha wanafunzi na hatimaye kupata wafuasi katika kuvuruga shughuli za chuo.

Alisema madai ya wanafunzi waliokuwa wakiendesha vurugu hizo, yamekuwa yakibadilika kila kukicha ambapo mwanzo walidai mikopo ya wanafunzi waliochaguliwa katika mwaka huu wa masomo na ambao hawakupata mikopo, baadaye dai kubwa likawa ni kuachiwa huru wenzao waliokamatwa na kufunguliwa mashitaka kutokana na kuendesha maandamano kinyume cha sheria na kukaidi amri ya Polisi ya kutawanyika.

Profesa Mukandala alisema katika siku mbili za vurugu madai ya awali yalikuwa kuondolewa kwa adhabu za kinidhamu walizopewa wenzao wachache kwa mujibu wa Kanuni na Sheria za Chuo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Januari 12 mwaka 2012

KESI YA HAMAD RASHID KUSIKILIZWA JANUARI 19

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Dar es Salam imepanga kusikiliza maombi ya Mbunge wa Wawi Zanzibar Hamadi Rashid na wenzake 10 waliofukuzwa uanachama wa Chama cha Wananchi (CUF), juma lijalo.

Rashid na wenzake juzi waliwasilisha maombi mahakamani hapo wakiiomba mahakama hiyo iwamuru waitwe mahakamani wajieleze ni kwa nini wasitiwe hatiani na kufungwa kwa kupuuza amri ya mahakama.

Pia anaiomba mahakama ibatilishe uamuzi wa Baraza Kuu la Chama hicho wa kuwafukuza uanachama na itamke kuwa wao bado ni wanachama halali wa chama hicho.
Habari zilizolifikia Tanzania Daima jana na kuthibitishwa na Wakili wa kina Rashid Agustine Kusalika zinasema kuwa maombi hayo yamepangwa kusukilizwa Alhamisi ijayo Januari 19, 2012 na kwamba maombi hayo yatasikilizwa na Jaji Augustine Shangwa anayesikiliza kesi ya msingi .

Januari 4 Jaji Shangwa wa Mahakama Kuu Dar es Salaam iliagiza Baraza Kuu la CUF lisitishe mchakato wa kuwasimamisha au kuwafukuza uanachama Rashid na wenzake wala kuendelea kuwajadili wakati wa mkutano wake wa Januari 4 uliofanyika Zanzibar.

Mahakama hiyo ilifikia uamuzi huo baada ya Rashid na wenzake kuwasilisha maombi Januari 3, 2012 wakiiomba mahakama hiyo iamuru mkutano huo ambao ulikuwa na lengo la kuwafukuza uanachama usitishwe hadi kesi yao ya msingi itakapomalizika.
Katika kesi yao hiyo ya msingi namba 1 ya mwaka 2012, Rashidi na wenzake wanahoji uhalali wa Kamati ya Nidhamu na Maadili ya chama hicho na uteuzi wa wajumbe wake.
Kamati hiyo ndio iliyowahoji Rashid na wenzake na kisha kupendekeza kwa Baraza Kuu wafukuzwe uanachama.

Akizungumza na waandishi wa habari juzi baada ya kuwasilisha maombi hayo madogo, Rashid alisema CUF wamevunja Katiba ya Nchi kwa kuidharau amri ya Mahakama pamoja na Katiba ya chama chao.

Alisema Ibara ya 4 ya katiba ya chama hicho inasema kuwa mahakama ndio itakayoamua mambo yote yakiwemo yahusuyo migogoro baina ya wanachama bila kuingiliwa isipokuwa kwa kukata rufaa tu na kwamba Ibara ya 5 inasisitiza kuwa juu ya utawala wa Sheria.
Alisema kutokana na chama hicho kukiuka amri halali ya mahakama basi yeye bado ni mbunge halali wa Wawi na kwamba hata kwenye vikao vya kamati za Bunge vitakavyoanza Januari 15 atashiriki.

Alisisitiza kuwa tayari ameshawalisha taarifa na vielelezo kwa Spika Anne Majkinda na kwamba kwa mujibu wa kanuni za bunge kama jambo liko mahakamani haliwezi kuchukua hatua yoyote hadi mahakama itakapokuwa imetoa uamuzi wake.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamsi, Januari 12 mwaka 2012.

HAMAD RASHI AITIA KITANZI CUF KORTINI

Na Happiness Katabazi

HATIMAYE mbunge wa Wawi Hamad Rashid Mohamed(CUF), na wenzake 10 jana waliwasilisha maombi madogo katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, wakiomba mahakama hiyo itamke kuwa uamuzi wa Baraza la Uongozi Taifa la chama hicho uliomvua uanachama yeye na wenzake ni batili.

Mbali na Hamad walalamikaji wengine Shoka Khamisi Juma, Doyo Hassan Doyo, Juma Said Sanani, Yassin Mrotwa,Kirungi Amir Kiurungi,Doni Waziri Mnyamani, Mohamed Faki Albadawi,Tamim Omari Tamim,Nanjase Haji Nanjase na Mohamed Massaga ambao wanatetewa na wakili Augustine Kusilika toka kampuni ya uwakili ya GF Law Chambers dhidi ya Bodi ya Udhamini ya chama hicho.

Ombi hilo ambalo nalo limepewa Na.1/2011 na limewasilisha chini ya hati ya dharula licha bado halijapangiwa tarehe ya kuanza kusikilizwa.

Kwa mujibu wa hati hiyo ya madai ambayo ina maombi manne, ombi la kwanza, Hamad na wenzake wanaiomba mahakama itoe amri kwa bodi ya baraza la wadhamini na wajumbe wa baraza kuu la chama hicho wajieleze ni kwanini wasitiwe hatiani kama wafungwa kesi ya madai kwa kitendo chao cha kudharau uamuzi wa upande mmoja uliotolewa na Januari 4 mwaka huu, ambayo iliwataka wadaiwa hao au mawakala wao wasifanye jambo lolote ambalo lilikuwa na lengo la kuwafukuza uanachama wadaiwa hadi ombi hilo dogo la lilotolewa uamuzi siku hiyo ya Januari 4 mwaka huu, litakapokuja kusikilizwa na pande zote mbili.

Katika ombi la pili, Hamad anaiomba mahakama itamke kuwa utaratibu wote uliofanywa na wadaiwa Januari 4 mwaka huu jioni mjini Zanzibar baada ya Jaji Agustine Shangwa wa Mahakama Kuu, kutoa uamuzi ule wa upande mmoja kuwa ni batili.

Ombi la tatu, walalamikaji hao wanaomba mahakama iwaamuru wadaiwa kulipa gharama za uendeshaji wa ombi hilo dogo na ombi la nne wanaiomba mahakama itoe amri nyingine itakazoona zinafaa.

Januari 4 mwaka huu, saa nne asubuhi Jaji Agustine Shangwa alitoa amri ya kuzuia Hamad Rashid na wenzake wasifukuzwe uanachama hadi maombi hayo madogo Na.1/2012 yatakapokuja kwaajili ya kusikilizwa na pande zote mbili na ilipofika saa 6:30 mchana ya siku hiyo Hatibu Omari ambaye ni mtumishi wa mahakama anayeshughulika na jukumu la kuwapelekea wahusika wa kesi mbalimbali hati za wito wa kuitwa mahakamani au amri zilizokwishatolewa na mahakama.

Na kwa mujibu wa nakala ya kiapo ambacho Tanzania Daima Jumatano inayo nakala yake, kilichoapwa na Omari , Januari 4 mwaka huu, katika kiapo kinamnukuu Omari akisema; “Nathibitisha kwamba nilipeleka uamuzi huo uliotolewa na Jaji Shangwa pale Buguruni kwenye ofisi Kuu ya chama cha CUF na Bwana Mikidadi ambaye nimemkuta hapo ofisini alikataa kupokea uamuzi huo bila sababu za msingi”alisema Omari katika kiapo chake.

Januari 4 mwaka huu, Jaji Shangwa akitoa uamuzi wake siku hiyo alisema Januari 3 mwaka huu, wadaiwa hao waliwasilisha ombi dogo dhidi ya Bodi ya Wadhamini ya chama cha CUF liliomba mahakama hiyo itoe uamuzi wa kwa kusikiliza upande mmoja ambao uamuzi huo utazuia Baraza Kuu la Taifa la CUF ambalo lilikuwa likiketi Januari 4 mwaka huu mjini Zanzibar , lisiwafukuze uanachama walalamikaji kwani endapo watavuliwa uanachama haki zao za Kikatiba kama wanachama wa chama hicho zitakuwa zimevunjwa.

Pia Hamad siku hiyo mbele ya Shangwa kupitia wakili wake wakiwasilisha hoja zao walidai sababu nyingine yakuwasilisha ombi lile ambalo lilikishwa tolewa uamuzi siku hiyo na jaji huyo ni kwamba tayari walishafungua kesi ya msingi mahakamani hapo ambayo bado haijatolewa uamuzi na katika madai yao ya msingi walalamikaji hao wanaipinga uhalali wa Kamati ya Nidhamu na Maadili iliyoundwa nje ya Katiba ya chama na wajumbe wa Kamati Kuu ambao ndani ya wajumbe wa Kamati hiyo tayari walishawahi kutokeza adharani kumuhukumu Hamad Rashid na wenzake kupitia mitandao ya mawasiliano kabla ya hata kamati hiyo ya Nidhamu na Maadili kuundwa ghafla hivi karibuni.

Akitoa uamuzi wa upande mmoja kutokana na maombi hayo yaliyowasilishwa na walalamikaji hao Januari 3 mwaka huu, Jaji Shangwa alisema kwa maoni yake kama kuna taaarifa ya dharula inayotaka walalamikaji kuvuliwa uanachama na kwamba taarifa hiyo itaatarisha haki zake zao za Kikatiba na hadhi ya wadhifa wao wa kisiasa.

“Natoa amri ya kumzuia mdaiwa na mawakala wake kuwavua uachama walalamikaji hadi ombi hili litakapokuja kusikilizwa kwa kudhuliwa na pande zote katika ombi hilo Februlia 13 mwaka huu”alisema Jaji Shangwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania la Jumatano, Januari 11 mwaka 2012.

RAIA WA BURUNDI KORTINI KWAKUKUTWA NA RISASI 682

Na Happiness Katabazi

RAIA wa Burundi, Ismail Stefano (39) jana alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na mashtaka ya kukutwa na silaha mbili aina ya SMG na risasi 682.

Mbele ya Hakimu Mkazi Ritha Tarimo Wakili wa Serikali Cecilia Mkononga alidai kuwa Januari 5, mwaka huu katika stendi ya mabasi yaendayo mikoani ya Ubungo, mshtakiwa huyo alikamatwa akiwa na SMG mbili pamoja na risasi 682 kinyume na kifungu cha 4(1) na 34(1),(2) cha sheria ya Umiliki wa silaha sura ya 223 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Mkononga alidai kuwa silaha hizo alizokamatwa nazo mshtakiwa akizimiliki bila ya kuwa na leseni inayomruhusu kufanya kumiliki , na zilikuwa na namba UC-99611998 na nyingine namba 1992-AET 3837.

Alidai kuwa siku hiyo aliyokamatwa , mshtakiwa huyo pia alikutwa akimiliki risasi hizo 682 wakati akiwa hana kibali kinachomruhusu kuzimiliki.
Hata hivyo mshtakiwa huyo alikana mashtaka hayo na upande wa Jamhuri ulidai upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamalika hivyo wanaiomba mahakama ipange tarehe ya kutajwa.

Akitoa masharti ya dhamana Hakimu Tarimo alimhoji mshtakiwa huyo kuwa ni mwenyeji wa wapi ambapo mshtakiwa huyo alijibu kuwa yeye ni mzaliwa wa Mkoa wa Kigoma na wazazi wake kabila lao ni Wahutu na wakimbizi toka nchini Burundi waliongia nchini mwaka 1972 na kwamba wakati wanaingia nchini mama yake alikuwa na ujauzito wake hivyo yeye amezaliwa mkoani Kigoma.

Aliendelea kudai kuwa licha ya yeye kuzaliwa mkoani Kigoma pia ana uraia wa Tanzania lakini vinashikiliwa na jeshi la polisi na kusisitiza kuwa yeye ni raia wa Tanzania.

Hakimu huyo aliendelea kumuuliza mshtakiwa huyo kuwa anakaa wapi , ambapo alijibu Katumba Mpanda na kuongeza kuwa alikuja Jijini Dar es Salaam na lengo lake ni kufikia nyumba ya kulala wageni.

Baada ya kutoa maelezo hayo, Wakili Mkononga aliiomba mahakama wakati inapotoa masharti ya dhamana izingatie kuwa mshtakiwa huyo haelewi uraia wake kama ni mtanzania au la.

Akitoa masharti ya dhamana, Hakimu Ritha alimtaka mshtakiwa huyo awe na wadhami watatu wanaominika , wanaoishi Dar es Salaam, mmoja wao awe mfanyakazi wa serikali lakini asiwe mwalimu.

Hata hivyo mshtakiwa huyo alishindwa kutimiza masharti hayo ya dhamana na hakimu akaamuru apelekwe gerezani hadi Januari 24 mwaka huu kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya kutajwa.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Januari 11 mwaka 2012

UGUMU WA MAISHA UTATUANGAMIZA


Na Happiness Katabazi

KARIBU kila pembe ya nchini hii wimbo wa gharama za kupanda kwa maisha na mfumuko wa bei umezidi kushika chati katika mawazo na midomoni mwa wananchi wengi.


Wananchi tulio wengi hususani sisi wenye maisha ya hali ya chini tumekuwa tukisurubika na hali hiyo huku tukiona hakuna jitihada za mara moja zinazofanywa na serikali au wamiliki wa makampuni ya sekta binafsi wakikabiliana na hali hiyo.

Matokeo yake wafanyakazi wanaofanya kazi katika serikali, sekta binafsi na wale wasio na ajira za uhakika na wamekuwa wakiimba wimbo huo wa kukabiliwa na hali ngumu ya maisha .

Kwa sisi wanawake ambao mara kwa mara ndiyo tunakwenda kununua bidhaa katika masoko na madukani ndiyo tumekuwa tukishuhudia moja kwa moja upandaji wa bei za nafaka katika kipindi kifupi tu na ukimuuliza muuzaji ni kwanini wiki iliyopita nimekuja kununua mchele au maharage kwa bei ile na leo umepandisha bei kiasi hiki.

Muuzaji anaishia kukupa jibu la mkato kwamba gharama za maisha zimepanda na kwamba kama unataka kununua bidhaa zake nunua hutaki nenda katika masoko mengi.

Mtu unakuwa huna jinsi inabidi ununue bidhaa hiyo kwa huku ukinung’unika moyoni.
Tumewasikia viongozi wa serikali wakitoa bei ya sukari kwa wauzaji kuwa washushe bei hiyo toka shilingi 2500 kwa kilo moja na waizue kwa shilingi 1,700.Lakini maagizo hayo yameshindwa kutekelezeka na wauzaji hao matokeo yake bei ya kilomoja ya sukari inauzwa sh 2500.
Lakini kwa kuwa shida ni mwalimu sisi malofa hivi sasa tunakimbila maduka ya Shoprite kununua sukari kwasababu bei yake ina unafuu.Katika maduka hayo kilo moja ya sukari ni shilingi 1,900.
Kwa maoni yangu serikali kupitia wachumi wake kama hawatakaa kitako na kuweka mikakati ya taifa lake kukabiliana na hali hii, basi ijiandae kuona baadhi ya nguvu kazi yake kubwa mwisho wa siku ikishindwa kuzalisha kutokana na sababu mbalimbali.
Ikiwemo maradhi ya kuambukiza kama ukimwi, magonjwa ya moyo na wananchi wake kuamua kujitumbukiza kwenye vitendo haramu kwa lengo la kujipatia fedha kwa njia ya mkato na mwisho wa siku wakajikuta wakiangukia kwenye mkono wa dola.
Hivi sasa huko mitaani kuna vijana ambao hawana elimu na wengine wenye elimu tena wengine wapo vyuoni, nao wamekuwa wakilalamikia hali hilo hali inayowasababisha wengine kushindwa kujizuia na kuamua kujitumbukiza kwenye kufanya ngono zembe ili waweze kupata fedha za kuendeshea maisha yao.
Na siyo kundi hilo pia kuna baadhi ya wake za watu nao bila haya wamekuwa wakisaliti ndoa zao na kwenda kufanya mapenzi na wanaume wengi ili waweze kupata fedha za kuendeshea maisha yao kwa kisingizio kuwa waume zao fedha wanazowapatia ni ndogo.
Pia kuna wa mama watu wazima nao wamekuwa wakitumia fedha zao kuwarubuni vijana wadogo wa kiume kufanya nao mapenzi kwa kuwahonga fedha ili waweze kuwatimizia haja zao za kimapenzi.

Licha tabia hizi chafu hazikuanza leo zimeanza siku nyingi lakini hivi sasa zimeshika kasi na zinafanyika kwa uwazi bila kificho kwa kila mmoja wao kutumia udhaifu wa mwenzie uwe wa kimapenzi au kifedha.

Tukiachana na hilo hivi sasa mitaani kutokana na baadhi ya vijana kutaka kujipatia fedha kwa njia za mkato na kukata tamaa,miongoni mwao mitaani wamekuwa wakiishi maisha ya kifahari kuliko hali halisi zinazowazunguka na wengine wamekuwa wakinyoshewa vidole kuwa wanajiusisha na kufanyabiashara haramu kama kuuza unga kwa kigezo cha kujifanya wao ni wafanyabiashara wa kwenda kununua bidhaa kama nguo nje ya nchi na kuzileta hapa nchini.

Ni rai yangu pia kwa waendeshaji wa maofisi ya sekta binafsi nao wabadilike hivi sasa wasiangalie faida tu wanayoingiza tu makampuni na viwanda vyao pia wakae chini watafakari ni jinsi gani wanaboresha maisha ya wafanyakazi wao kwani hakuna ubishi mfumuko wa bei pia unawaathiri hata wafanyakazi wa sekta binafsi.

Pia na serikali nayo iweke utaratibu sasa huko mbele ya safari wa kuweza kuwabana wauzaji wa bidhaa mbalimbali ambao kila kukicha wanapandisha bei kwani hiki kisingizio cha serikali cha soko huria ndiyo maana inashindwa kuwabana ipo siku watu watachoka kukisikia.

Na pia serikali iendelee kupanua wigo wa ajira za uhakika kwa vijana ili waweze kuondoka vitendo hivyo haramu ambavyo mwisho wa siku vitafupisha maisha yao.

Tunaamini serikali yoyote makini ina uthubutu na ina mkono mrefu na inapoamua jambo lake lifanyike na litekelezwe, linatekelezwa sasa ni sisi wenyewe tumeridhia serikali yetu ituongoze hivyo serikali hii haina budi sasa kuakikisha inaweka taratibu za kuweza kukabiliana na hali hii ya wananchi wengi kuimba wimbo huu wa ukali wa maisha.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika
0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Januari 10 mwaka 2012

MNALENU JAMBO,SIO BEI MPYA YA KIVUKO




Na Happiness Katabazi

MWISHONI mwa wiki iliyopita Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, alitangaza kupanda kwa nauli za vivuko hususan vivuko vya serikali vya Kigamboni.
Alisema kuanzia siku hiyo abiria wangeanza kulipa nauli ya sh 200 badala ya sh 100 ya zamani.


Hata hivyo tangazo hilo lilionekana kuwakera baadhi ya watumiaji wa huduma hiyo na wengine kufikia hatua ya kumtolea maneno yasiyofaa na kupinga wakati abiria wengine wakitekeleza agizo hilo kwa vitendo kwa kuanza kutumia huduma hiyo kwa nauli mpya.

Baada ya baadhi ya wananchi kulipinga tangazo hilo, Magufuli aliwapasha wananchi hao kwamba asiyetaka kulipa nauli mpya ajifunze kupiga mbizi au asitumie kivuko hicho na badala yake azungukie Kongowe.
Aidha juzi tulishuhudia baadhi ya wabunge wa Dar es Salaam wakinukuliwa na vyombo vya habari wakiishutumu kauli ya Magufuli na kudai kwamba upandaji wa nauli utawaumiza abiria na kuomba uongozi wa juu wa nchi kumuonya waziri kutokana na maamuzi ya kupandisha nauli.

Binafsi naunga mkono tangazo la Waziri Mafuguli la kupandisha nauli na ushauri alioutoa kwa abiria wanaopinga ongezeko hilo la nauli kwamba kama hawataweza kulipa basi wajifunze kupiga mbizi au wazungukie Kongowe.

Nimelazimika kuunga mkono agizo hilo kwa sababu Watanzania wengi tunapenda kuambiwa uongo na viongozi wetu, hivyo anapotokea kiongozi anayetuambia ukweli ili tujiandae kukabiliana na utekelezwaji wa ukweli huo, huwa tunamuona ni mbaya na hafai.

Kutokana na tabia hii ambayo imejengeka akilini mwetu, ndio maana nyakati za uchaguzi, wagombea wengi wa ubunge, urais na udiwani toka vyama vya siasa wamekuwa wakitumia uongo kunadi sera zao na hatimaye wananchi wanaopenda kudanganywa huona wanasiasa hao wanafaa na kuwapa kura za ndiyo.

Nina uzoefu na hilo nililolisema kwani nimezunguka nchi nzima mara tatu na wagombea wa urais toka vyama mbalimbali na baadhi ya ahadi walizokuwa wakizitoa kwenye majukwaa zilikuwa hata hazimo kwenye ilani za vyama vyao.

Nakumbuka kampeni za urais mwaka 2005, ahadi mbalimbali zilitolewa na viongozi wa kisiasa kama vile kila kata kungejengwa chuo kikuu; maisha bora kwa kila mmoja; milo mitatu kwa kila mtu; pamoja na wananchi kusoma bure hadi chuo kikuu.

Wakati viongozi hao tofauti wakitoa ahadi hizo kwenye mikutano ya hadhara tulikuwa tukiwashangilia sana lakini leo hii tumegeuka na kuanza kuwashambulia kwa ahadi hizo.

Sasa kwa muktadha huo nawataka wananchi tunaotumia kivuko cha Kigamboni tujiulize hivi katika akili zetu siku zote za maisha tulikuwa tukifikiri ile nauli ya sh 100 ya kivuko haitapanda?

Ni nyie abiria mliokuwa mkilia usiku na mchana kuhusu ubovu wa kivuko cha zamani na hatimaye alipoingia madarakani Rais Jakaya Kikwete na serikali yake wakafanya jitihada hadi wakawaletea kivuko kipya cha Mv. Magogoni; leo hii mnavuka usiku na mchana na kwa usalama zaidi kwa sababu kivuko hicho kipya ni cha uhakika.

Lakini hamjiulizi serikali ilipataje fedha hadi ikawaletea kivuko hicho hapo Kigambo?
Inashangaza kwa ongezeko hilo la nauli ambayo kwa sasa ni sh 200 hadi mnataka kuandamana wakati bidhaa na huduma mbalimbali zimepanda bei kama nafaka, dawa, kondomu, matibabu, vinywaji, nauli za kwenda mikoani, ada na vifaa vya shule.

Wabunge wa Dar es Salaam mnaoingilia kati jambo hili, napenda kutoa ushauri wa bure kwenu kwamba tekelezeni ile dhana ya uwajibikaji wa pamoja na achaneni na porojo za kisiasa.

Naamini Magufuli sio chizi kwa kutoa agizo lile, hivyo ni vema na mna haki, wabunge kwenda ofisini kwa Magufuli kimya kimya ili awaeleze sababu zilizosababisha yeye kufikia uamuzi huo na sio kujitokeza hadharani na kuanza kumhukumu kuwa anatumia madaraka yake vibaya kupandisha nauli.

Sote tunafahu waziri ana mamlaka ya kutunga sheria ndogondogo muda wowote anapoona inafaa.

Serikali kupitia Magufuli haijawalazimisha mtumie kivuko hicho, hivyo wale wanaopenda kutumia kivuko hicho kwa nauli mpya watumie na wasiotaka watafute njia nyingine.
Magufuli aliposema kama hamtaki kulipa bei mpya basi mjifunze kupiga mbizi au kuzungukia Kongowe sio lugha ya kuudhi, bali ametoa ushauri mzuri tu.

Kwa nini Watanzania hatupendi mtu anayeliita jembe ni jembe? Kwa nini tunawapenda watu wanaotudanganya kwa kanga, pilau na kofia wakati wa uchaguzi wakati tunajua ni waongo?

Magufuli tafadhali kaza uzi! Na nyie wanasiasa wa Dar es Salaam acha unafiki na uzandiki.

Kama hili la kupanda bei limewakera andikeni michanganuo kwa hao wafadhili wenu wanaowachangieni hela za kampeni kisirisiri ili muweze kununua kivuko binafsi ili wananchi waweze kupanda bure kama mtaweza!

Mungu ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika

0716 774494 www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Januari 4 mwaka 2011.