Na Happiness
Katabazi
KATIBU Mkuu
wa Baraza la Kuu la Waislamu(BAKWATA), Suleman Said Lolila(61),amekanusha madai
yaliyotolewa na Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh
Ponda Issa Ponda na wenzake 49 wanaokabiliwa na kesi uchochezi na wizi wa Sh milioni 59 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es
Salaam, kuwa Baraza Kuu la Waislamu nchini(BAKWATA), siyo chombo cha
kuwakilisha waislamu wote hapa nchini.
Sambamba na waandishi
wa habari za mahakamani walipongeza
hatua iliyochukuliwa na wana usalama ya jana kuzuia umati wa wafuasi wa Ponda
kuingia ndani ya chumba kinachoendeshewa kesi kwani hapo awali wafuasi hao
walikuwa wakifurika hali iliyosababisha waandishi wa habari,wanausalama
kushindwa kufanyakazi yao kwa nafasi na kupata hewa ya kutosha kwani kesi hiyo
kwanza ina washtakiwa wengi ambao ni 50.
Suleiman
ambaye ni shahidi wa kwanza wa upande wa jamhuri katika kesi hiyo, alitoa
maelezo hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi Victoria Nongwa wakati akiongozwa na
wakili mwandamizi wa serikali Tumaini Kweka kumuongoza kutoa ushahidi ambapo
jana shahidi huyo alimaliza kutoa ushahidi wake.
Itakumbukwa
kuwa Novemba 15 mwaka huu, wakili Mwandamizi wa Serikali Tumaini Kweka
aliwasomea maelezo ya awali washtakiwa hao ambapo alidai Bakwata ni chombo
ambacho kinawawakilisha waislamu wote, lakini Ponda na wenzake walikanusha
madai yao na kusema kuwa Bakwata haipo kwaajili ya kuwawakilisha waislamu wote.
Suleiman
alitoa maelezo hayo baada ya kuulizwa swali na wakili Kweka kuwa BAKWATA ni
chombo gani?kipo kwaajii ya waumini wa dini gani?Mali za waislamu zinamilikiwa
na nani kwa niaba yao?Na na ninani hivi sasa ni mmilikiwa wa kiwanja kiwanja Kitalu 311/3/4 Block T ,kilichopo eneo la Chang’ombe Markas jijini
Dar es Salaam?
Akijibu
maswali hayo shahidi huyo ambaye alidai yeye ndiye mtendaji mkuu wa BAKWATA
alieleza kama ifuatavyo:
“BAKWATA ni
chombo kilichoundwa kwa Korani na Sunaa
na imesajiliwa na Wizara ya Mambo ya Ndani, na Bakwata ni chombo
kilichoanzishwa kwa kwaajili ya kuwawakilisha waumini wa dini ya Kiislamu hapa
nchini na mali za waislamu zinamilikiwa
kwa niaba yao na Bodi ya Wadhamini ya Bakwata ;
“Na mmiliki
halali wa kiwanja hicho hivi sasa ni kampuni ya Agritanza Ltd , kwani Serikali
ya Misri ilitoa wazo ya kuwasaidia waislamu wa Tanzania kielimu na ikafanya
mazungumzo na viongozi wa serikali ya Tanzania ,serikali ya Tanzania ikaipatia
serikali ya Misri eneo hilo la Chang’ombe Markas kiwanja hicho ili kiweze
kujenga chuo kikuu cha Waislamu lakini baadaye serikali ikaja kuwagawai baadhi
ya maeneo taasisi ya YCC na mfanyabashara Yusuf Manji:
“Ikabakia
eneo jingine ambalo mwisho wa siku BAKWATA ikiaamua eneo hilo wabadilishane na
kampuni ya Agritanza Ltd kwa mikataba halali kisheria , hivyo makubaliano
yalifikishwa tena kwa maandishi BAKWATA ikaridhia kubadilisha na kampuni hiyo
hivyo Agritanza hivi sasa ndiye mmiliki halali wa kiwanja hicho na si
vinginevyo na alipata Baraka zote za Bakwata ambayo ni chombo kinachosimamia
mali na waislamu wote’alidai shahidi huyo.
Kwa upande
wake wakili utetezi Nassor Mansoor akimhoji shahidi huyo alimuuliza kama anafahamu
alikuwa akifahamu hati ya umiliki wa kwanza wa kiwanja hicho ulikuwa
ukimilikiwa na nani na kwamba kabla ya kiwanja hicho kugawiwa kwa baadhi ya
watu kilikuwa na ukubwa gani na kwamba kama alikuwa akiwafahamu washtakiwa .
Akijibu
maswali hayo alidai yeye hafahamu awali kiwanja hicho kilikuwa kikimilikiwa na
nani na kilikuwa na ukubwa gani na kuhusu kuwafahamu washtakiwa alidai
anamfahamu Sheikh Ponda kwani amekuwa akimuona kupitia vyombo vya habari na
kisha shahidi huyo akainuka akawasalimia washtakiwa na kusema “Asalmayek nao
washtakiwa wakamjibu kwa sauti Alykmsalamu hali iliyosababisha Hakimu Mkazi
Victoria Nongwa kumwaleza shahidi kuwa mahakamani hapo watu huwa hawasalimiani
na kusababisha watu kuangua vicheko.
Baada ya
Shahidi huyo kumaliza kutoa ushahidi wake, Hakimu Nongwa alisema anaiarisha
kesi hiyo hadi Desemba 13 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya shahidi wa pili
kuja kuanza kutoa ushahidi wake na akamuamuru mshtakiwa wa kwanza Ponda na Mukadam Abdal Swalehe(45)
ambaye ni mshtakiwa wa tano katika kesi
hiyo ya jinai Na.245/2012 warudishwe gerezani kwasababu bado Mkurugenzi wa
Mashtaka(DPP), Dk.Eliezer
Feleshi hajaiondoa hati yake aliyoiwasilisha ambayo
imefunga dhamana za washtakiwa hao wawili.
Baada ya
hakimu Nongwa kuarisha kesi hiyo, ndugu na jamaa na washtakiwa ambao wapo nje
kwa dhamana walijipanga katika viunga vya mahakama hiyo na kumpungia mkono
Mukadam na Ponda ambao walikuwa wamepandishwa kwenye gazeti la Jeshi la
Magereza lilokuwa likilindwa na kuongozwa na msafara wa magari ya ina ya Defenda za jeshi la Polisi na gari mmoja
lililokuwa limebebeba maji ya kuwasha ‘kikojozi’ na kuanza safari ya kumrejesha
katika gereza la Segerea na wafuasi hao ambao kadri siku zinavyozidi kusonga
mbele wanapungua kuja mahakamani kuudhulia kesi hiyo walisikika wakisema ‘Takbiri,Takbir’
huku wakiwapungia mkono Ponda na Mukadam ambao walikuwa wakiondoshwa kwenye
eneo hilo la Mahakama kupelekwa gereza
la Segerea.
Awali Oktoba 18 mwaka huu, ilidaiwa na wakili Kweka kuwa kosa la kwanza alidai ni la kula njama ambalo linawakabili washitakiwa wote,kosa la pili ni kwaajili ya washitakiwa wote ambalo ni la kuingia kwa nguvu kwa nia ya kutenda kosa kinyume na kifungu cha 85 na 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002, kuwa Oktoba 12 mwaka huu huko Chang’ombe Markas, wasipokuwa na sababu za msingi waliingia kwa jinai kwenye kiwanja kinachomilikiwa na kampuni ya Agritanza Ltd, kujimilikisha kiwanja hicho kwa njia ya iloyopelekea uvunjifu wa amani,wizi ambapo baada ya kuvamia waliiba vifaa na malighafi ikiwemo nondo, kokoto zenye jumla ya thamani ya Sh. 59,650,000 mali ya kampuni ya Agritanza na kosa la tano ni la uchochezi kinyume na kifungu cha 390 na 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, ambalo sasa kosa hili la uchochezi litamkabili Mukadamu na Ponda peke yao kuwa wakiwa ni viongozi wa jumuiya hiyo , Oktoba 12 mwaka huu ,waliwashawishi wafuasi wao watende makosa hayo hata hivyo walikanusha mashtaka yote.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Novemba 30 mwaka
2012