MANJI,MWALUSAKO WAKIMBILIA MAHAKAMA YA RUFAA


Na Happiness Katabazi

MWENYEKITI wa Klabu ya Yanga Yusuph Manji na Katibu Mkuu wake, Lawrence Mwalusako, jana walifika katika Mahakama Kuu Diveshi ya Kazi Dar es Salaam lakini hawakusimama kizimbani kujieleza ni kwanini wasichukuliwe hatua za kisheria  kwa kosa la kudharau amri ya mahakama.

Manji ambaye pia ni mfanyabiashara na Mwalusako walifika mbele ya Msajili wa mahakama hiyo Mohamed Gwae lakini hawakuhojiwa chochote kwasababu jalada la kesi limepelekwa Mahakama ya Rufani  kwaajili ya kufanyiwa marejeo.

Katika kesi hiyo timu ya  Yanga inadaiwa  kukiuka umuzi  uliyokwishatolewa na mahakama hiyo ambayo iliitaka timu hiyo iweke  mahakamani Sh milioni 106, kwasababu ilishindwa kuwalipa walalamikaji  katika kesi hiyo, ambae ni Kipa wa zamani wa timu hiyo  Stephen Marashi na beki raia wa Malawi, Wisdom Ndlovu.

Jalada la kesi hiyo hiyo   limeitwa Mahakama ya Rufaa  baada ya mdaiwa (Timu ya Yanga), kuwasilisha ombi katika mahakama hiyo ya Rufani  linaloiomba mahakama hiyo ifanye marejeo ya uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu Diveshi ya Kazi ambao uliitaka timu hiyo  iweke kiasi hicho cha fedha mahakamani.

Jana Msajili Gwae alisema kuitwa kwa Manji na Mwalusako tena mahakamani hapo, kutategemea uamuzi utakaotolewa na Mahakama ya rufaa.

Ombi hilo la Yanga la linaloomba Mahakama ya Rufaa ifanyie  marejeo uamuzi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi , waliliwasilisha Machi 25 mwaka huu, chini ya hati  ya dharura likiomba mahakama hiyo ya juu kabisa nchini iitishe jalada la kesi ya msingi ili iweze kuupitia mwenendo mzima wa kesi hiyo iliione uamuzi huo ulikuwa sahihi.

Kwa mujibu wa hati ya kiapo kilichoapwa na mdaiwa wa pili ( Mwalusako) inayounga mkono ombi hilo, Oktoba 11 mwaka jana waliwasilisha ombi la marejeo  pamoja na kuwasilisha  ombi la kusitisha utekelezaji wa tuzo ya kuwalipa wachezaji hao.

Kwa mujibu wa hati hiyo, Februali 5 mwaka huu, Msajili Gwae ilikataa ombi la kusitisha utekelezaji wa hukumu hiyo na kuwataka Yanga kuweka fedha hizo mahakamani wakati wakisubiri uamuzi wa ombi la marejeo.

Anadai  kuwa, utekelezaji dhidi ya walalamikaji umekwenda kinyume na utaratibu kwa kuwa msuluhishi alishindwa kuzingatia nafasi ya mlalamikaji katika suala hilo, pia Klabu hiyo haina mali yoyote ya kuweza kutekeleza tuzo hiyo.

Katika kesi ya msingi, Marashi na mwenzake, wameiomba mahakama kumfunga jela mwenyekiti huyo na katibu wake, baada ya timu hiyo kushindwa kutekeleza amri ya mahakama, ikiamuru kiasi hicho kulipwa.

Kamisheni ya Usuluhishi na Upatanishi iliiamuru Yanga iwalipe wachezaji hao fedha hizo kutokana na kukatisha mkataba wao kinyume cha  taratibu, na walitakiwa kulipwa wiki mbili kuanzia tarehe ya hukumu.

Yanga iliingia kwenye mgogoro na wachezaji hao, baada ya kuvunja nao mikataba mwaka 2010 kutokana na sheria mpya ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kuzitaka klabu kuwa na nyota watano tu kutoka nje, hivyo kuwaacha Ndlovu, Mkenya John Njoroge na Mtanzania Marashi. Njoroge alilipwa milioni 17.

Walalamikaji hao wanadai kuwa, walisajiliwa na Yanga kwa mkataba wa miaka miwili kuanzia Machi 18, 2010, wanadai Julai 17, 2010, wakiwa wanajiandaa na kipindi kingine kipya cha msimu wa ligi, Kocha Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic aliwaambia kwa mdomo kwamba wao si wachezaji wa Yanga.

Walidai kwa mujibu wa mkataba, Yanga walitakiwa kuwasiliana nao kuhusu kukatisha mikataba yao ndani ya siku saba kabla ya tarehe iliyokuwa imewekwa na TFF, kwa timu za ligi kuu kuwasilisha majina ya wachezaji watakaoachwa jambo hilo liliwakosesha nafasi ya kucheza katika timu nyingine.

Kamisheni iliamuru, Ndlovu alipwe sh. milioni 57 kama mshahara wa miaka miwili, sh. milioni 1.8 kama gharama za usafiri wa kumrejesha Malawi na sh. milioni 20 kama fidia ya kumkosesha nafasi ya kucheza.

Kwa upande wa Marashi, Yanga iliamriwa imlipe sh. milioni 18 kama gharama za kutia saini mkataba na mshahara kwa miaka miwili, sh. milioni 10 kwa kupoteza nafasi ya kucheza na sh. 500,000 kama malipo aliyopaswa kulipwa wakati anatia saini mkataba wa 2009 hadi 2010.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Machi 28 mwaka 2013.

ANAYEDAIWA KUUMUA TRAFIKI KORTINI


Na Happiness Katabazi 

ANAYEDAIWA kumuua askari wa kikosi cha Usalama Barabarani wiki iliyopita, Elikiza Nnko, Jakson Stephen Fimbo jana alifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni akikabiliwa na makosa ya matatu likiwemo kosa la kuingilia msafara wa kiongozi.

Mbele ya Hakimu Mkazi Kwey Lusema wakili mwandamizi wa serikali Lasdilaus Komanya alilitaja kosa la kwanza  ni la kusababisha  kifo cha trafiki huyo  kupitia kwendesha gari kwa hatari  na kwamba Machi 18 mwaka huu,  katika barabara ya Bagamoyo katika mataa ya Bamaga jijini Dar es Salaam,  mshitakiwa akiwa ni dereva  kiongozi wa gari lenye namba za usajili  T328 BML aina ya Land Lover Discovery.

Wakili Komanya alidai mshitakiwa huyo  aliendesha gari hilo ka mwendo wa hatari  katika barabara hiyo ambayo ni ya umma Mshitakiwa huyo jambo ambalo  lina hatarisha  usalama wa raia  na kutokana na mshitakiwa huyo kuendesha gari hilo kwa mwendo huo wa hatari alimgonga askari huyo ambaye amezikwa alhamisi iliyopita.

Alidai kosa la pili ni  kuingilia msafara  wa kiongozi,kuwa siyo ya Machi 18 mwaka huu, katika eneo hilo la mataa ya Bamaga,mshitakiwa huyo hakutii  maelekezo yaliyokuwa yakitolewa kwa ishara ya askari huyo Elikiza,ambaye alikuwa na wajibu wa kuyasimamisha magari kwa njia ya ishara.

Wakili Komanya alidai shitaka la tatu ni la kushitwa kutoa  taarifa za kusababisha ajali katika barabara hiyo ya umma na kwamba alishindwa kutoa tarifa za kusababisha ajali hiyo katika kituo chochote cha jirani.

Hata hivyo mshitakiwa huyo alikanusha mashitaka hayo na wakili Komanya alidai upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na anaomba tarahe ya kuja kumsomea maelezo ya awali mshitakiwa.
 Kwa upande wake  hakimu Lusema alisema ili apate dhamana ni lazima awe na wadhamini wawili ambao kila mmoja atasaini bondi ya Sh.milioni mbili ,hata hivyo mshitakiwa huyo alitimiza masharti hayo ya dhamana na akapata dhamana na hakimu huyo akaiarisha kesi hiyo  Aprili 15 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya upande wa jamhuri kumsomea maelezo ya awali.

Katika hatua hutua nyinge, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imeshindwa kuendelea kusikiliza kesi ya kuchapisha makala ya uchochezi inayomkabili aliyekuwa Mharii Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima na wenzake,kwasababu Kibanda bado amelazwa katika hospitali moja nchini Afrika Kusini kwaajili ya matibabu na hivyo ameiarisha hadi Aprili 29 mwaka huu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Machi 26 mwaka 2013.

KAJALA ATIWA HATIANI,WEMA SEPETU AMLIPITIA FAINI YA SH.MIL 13




Na Happiness Katabazi

HATIMAYE Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imewahukumu kwenda jela miaka nane au kulipa faini ya Sh.milioni 13 msainii wa Filamu nchini, baada ya kumtia hatiani katika makosa ya kula njama kuamisha umiliki wa nyumba, na kuamisha umiliki wa nyumba iliyokuwa iliyokuwa imezuiwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali isiuzwe.

Hukumu hiyo iliyolewa jana na Hakimu Mkazi Sundi Fimbo ambapo alianza kwa kuikumbusha mahakama hiyo kuwa Kajala na Faraja Chambo walikuwa wakikabiliwa na makosa matatu yaliyofunguliwa mapema mwaka jana mahakamani hapo..

Makosa hayo ni kosa la kwanza ni   la kula njama kinyume na kifungu cha 34 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007, ambako washitakiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo la kula njama la kuhamisha umiliki wa nyumba iliyopo Kunduchi, Salasala eneo ambalo halijapimwa jijini Dar es Salaam.

Shitaka la pili ni kwamba, Aprili 14 mwaka 2010 walihamisha isivyo halali umiliki wa nyumba hiyo, ambayo walikuwa wakiimiliki kwenda kwa Emilian Rugalia, ambaye ndiye walimuuzia kinyume na kifungu cha 34(2)A(3), cha Sheria ya TAKUKURU ya mwaka 2007, na shitaka la tatu ni la kutakatisha fedha, ambalo walilitenda siku hiyo ya Aprili 14 mwaka 2010, huku wakijiua ni kinyume cha sheria hiyo.

Hakimu Fimbo alisema baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote mbili, alisema upande wa Jamhuri umeweza kuithibitisha kesi hiyo na hivyo mahakama hiyo imemtia hatiani Kajala katika kosa la kwanza na la pili tu wakati Chambo amepatikana na hatia katika makosa yote matatu.

Alisema katika kosa la kwanza Kajala na Chambo watatakiwa walipe faini ya Sh.milioni tano kila mmoja au kwenda jela miaka mitatu. Kosa la pili watatakiwa walipe faini ya Sh.milioni nane  aukwenda jela miaka mitano kwa kila mmoja.

Aidha katika kosa la tatu ambayo ni Chambo ndiyo amekutwa na hatia  atatakiwa alipe faini ya Sh.milioni 200 au kwenda jela miaka mitano na kwamba adhabu hizo hazitakwenda pamoja.Hivyo Kajala peke yake  amehukumiwa kwenda jela jumla ya miaka nane  au kulipa jumla ya Sh.milioni 13 .

“Mahakama imewakutana na hatia washitakiwa wote  katika kosa la pili kwasababu ushahidi umethibitisha kuwa washitakiwa wote  walikuwa wakifahamu kuwa kuwaliwa na hati ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali iliyokuwa imezuia nyumba yao waziize kwasababu Taasisi ya Kuzia na Kupambana na Rushwa ilikuwa ikidai kuwa nyumba hiyo imepatikana kwa njia ya utakatishaji fedha,lakini wao wakakaidi amri hiyo wakaamua kuiuza”alisema Hakimu Fimbo.

Akilichambua kosa la kwanza, alisema pia upande wa jamhuri umeweza kulithibitisha  kwasababu kosa la pili limeweza kuthibitishwa .

Kuhusu shitaka la tatu, hakimu huyo alisema amemwachilia huru Kajala kwasababu upande wa jamhuri umeshindwa kuthitisha Kajala alishiriki vipi katika upatikanaji wa fedha haramu  kwasababu ilidaiwa kuwa Chambo alizipata fedha haramu katika maelezo ya onyo  kuwa alizipata fedha za kujengea nyumba hiyo wakati akiwa mfanyakazi wa Benki ya NBC.

‘Na kwa mujibu wa maelezo ya onyo ya Chambo ambaye ni mume wa Kajala, alikiri  kuwa wakati akiwa mfanyakazi wa benki ya NBC alikuwa akichukua fedha na kuzituma kwa baadhi ya watu wa ofisi ya TTCL ,watu ambao hawakuwa wakistahili kulipwa na baada ya vyombo vya dola kuanza kumfuatulia akaamua kuizua nyumba yake hiyo”alisema hakimu Fimbo.

Hata hivyo baada ya hukumu kutolewa wasanii wa filamu nchini walikuwa wamefika mahakamani hapo kufuatilia hukumu ya kesi hiyo, walikusanyika katika viunga vya mahakama hiyo na kuanza kujadiliana ili wachangishane fedha lakini msanii Wema Sepetu aliwataka wenzake wasichanganishane fedha ,badala yake yeye analipa Sh.milioni 13 na akaondoka katika eneo hilo na kisha kurejea mahakamani hapo saa saba mchana na kulipa faini hiyo na kisha kuondika na Kajala ,wakati Chambo akirudishwa gerezani kwani alishindwa kulipa fidia hiyo na pia anakabiliwa na kesi nyingine ya utakatishaji fedha mahakamani hapo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Machi 26 mwaka 2013.

LWAKATARE SASA AKIMBILIA MAHAKAMA KUU


 Na Happiness Katabazi

MAWAKILI wanaomtetea Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), jana wamewasilisha Mahakama Kuu Dar es Salaam, ombi la kuomba mahakama hiyo iitije majadala ya kesi tuhuma za ugaidi zilizofunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwaajili ya kuzifanyia marejeo.

Maombi hayo ambayo tayari yameishapewa namba 14 ya mwaka huu, na yameapwa na wakili wake  wa washitakiwa hao Peter Kibatara   yaliwasilishwa jana mchana na karani wa wakili huyo  mahakamani hapo.

Kwa mujibu wa kiapo kilichoapwa na wakili Kibatara, mawakili hao wanaomba mahakama hiyo ifanyie marejeo wa majadala ya kesi ya ugaidi Na.37/2013 iliyofunguliwa wa Machi 18 mwaka huu na Mkurugenzi wa Mashitaka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu dhidi ya Lwakatare na Ludovick Joseph mbele ya hakimu Emilius Mchauru  ambapo siku hiyo alisikiliza maombi  ya pande mbili.

Maombi ya mawakili wa utetezi yaliomba washitakiwa wapewe dhamana wakati mawakili wakuu wa serikali Ponsian Lukosi, Prudence Rweyongeza na Peter Mahugo waliomba mahakama isitoe dhamana kwasababu kesi makosa yanaoyoangukia katika sheria za ugaidi ya mwaka 2002 hayana dhamana.

Ambapo siku hiyo hakimu Mchauru aliairisha kesi hiyo hadi Machi 20  kwaajili ya kuja kutolea uamuzi wa maombi hayo pamoja na maombi mengine lakini  hakimu huyo alijkuta akishindwa kutoa uamuzi wake kwasababu Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP), Dk.Eliezer  Feleshi amewasilisha  hati ya kuwafutia kesi washitakiwa hao chini ya kifungu cha 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 kwasababu hana  haja ya kuendelea kuwashitaki.

Lakini dakika chache baada ya hakimu Mchauru kuwafutia kesi hiyo, wanausalama waliwakamata tena washitakiwa hao na kisha kuwapandisha mahakamani mbele ya Hakimu mwingine Alocye Katemana na wakili wa serikali  Rweyongeza alianza kuwasomea mashitaka manne mapya katika kesi mpya iliyopewa Na.6/2013 ambayo mashitaka ni yale yale  yaliyokuwa kwenye hati ya mashitaka ya awali  iliyofutwa na DPP,ambapo Katemana aliwataka washitakiwa wasijibu chochote na akaamuru waende gerezani hadi Aprili tatu.

Kwa mujibu wa madai yao mawakili wa Lwakatare wanaomba Mahakama Kuu ipitie uamuzi wa  DPP wa kuifuta hati ya awali ya mashitaka na kisha kuwafungulia kesi upya washitakiwa hao wakati kesi hiyo ilikuwa imekuja kwaajili ya mahakama kuitolea uamuzi lakini mahakama ikashindwa kutoa uamuzi wake kwasababu DPP aliwasilisha hati ya kuifuta kesi hiyo.

Kwa mujibu wa habari za kuaminika toka ndani ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, zimelieleza gazeti hili kuwa tayari uongozi wa mahakama imeishatoa amri ya kuyaitisha majalada hayo mawili ya kesi yanayomkabili Lwakatare na mwenzake yatoke mahakama ya Kisutu yaletwe mahakama kuu kwaajili ya kuyafanyia marejeo.   

Kosa la kwanza ambalo linawakabili washitakiwa wote kuwa ni la kula njama kutenda kosa la jinai kinyume na kifungu cha 284  cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 , na kwamba mnamo Desemba 28 mwaka jana, huko Kimara King’ong’o  Stopover, wote kwa pamoja walitenda kosa hilo kwa kutaka kutumia  sumu kwa lengo la kumdhuru  Denis Msaki  ambaye ni Mhariri wa habari wa Gazeti la Mwananchi ambalo ni kinyume na kifungu cha 227 cha sheria hiyo.

Wakili Rweyongeza alilitaja  kosa la pili kuwa ni la kula njama  ambalo pia ni kwaajili ya washitakiwa wote  ambalo ni kinyume na kifungu cha 24(2) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi Na.21 ya mwaka 2002, ambapo washitakiwa hao walitenda kosa la ugaidi la  kutaka kumteka Msaki  kinyume na kifungu  cha 4(2)(c) (iii) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya mwaka 2002.

Shitaka la tatu ni la washitakiwa wote ambapo wanashitakiwa kwa kosa la  kupanga kufanya makosa ya ugaidi  kinyume na kifungu cha 59(a) cha Sheria ya Kuzuia ugaidi kwamba Desemba 28 mwaka jana,walishiriki katika mkutano wa kupanga kufanya vitendo vya kumteka nyaraka Msaki  kinyume na kifungu 4(2)(c) (iii) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi.

Shitaka la nne, Rweyongeza alidai linamkabili Lwakatare peke yake  ni aliwezesha kutendeka kwa kosa la ugaidi kinyume na kifungu cha 23(a) cha sheria ya kuzuia ugaidi , kwamba Desemba 28 mwaka jana, Lwakatale akiwa ni mmiliki nyumba hiyo ilipo Kimaraka King’ong’o  kwa makusudi  aliliruhusu  kufanyika kwa kikao hicho baina yake na Ludovick  cha kutenda kosa la ugaidi la kutaka kumteka nyara Msaki hata hivyo walikanusha mashitaka hayo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Machi 23 mwaka 2013.