Header Ads

DPP AZIDI KUMNG'ANG'ANIA LWAKATARE



Na Happiness Katabazi

MKURUGENZI wa Mashitaka (DPP), Dk.Eliezer Feleshi amewasilisha ombi katika Mahakama ya Rufani nchini, akiomba mahakama hiyo itengue uamuzi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, wa Mei 8 mwaka huu, ambao ulimfutia jumla ya mashitaka matatu ya ugaidi Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Wilfred Lwakatare na Ludovick Joseph.

Dk.Feleshi aliwasilisha ombi hiyo juzi jioni katika Mahakama ya rufaa kwa njia ya maandishi ambapo katika maombi yake hayo yanayoomba mahakama hiyo ya juu kabisa nchini iitishe mwenendo wa shauri lilotolewa uamuzi huo na Jaji wa mahakama Kuu Lawrence Kaduri Mei 8 mwaka huu, iiputie upya na iufute uamuzi huo kwasababu una makosa kisheria.

Kwa mujibu wa hati ya madai Dk.Feleshi anadai kuwa sababu kuwasilisha ombi lao katika Mahakama ya Rufaa Lwakatare hakuwai kuomba mahakama kuu imfutie mashitaka kama jaji Kaduri alifikia uamuzi wa kumfutia mashitaka hayo, bali Lwakatare katika maombi yake mahakama Kuu aliomba mahakama Kuu iitishe majadala ya kesi ya msingi iliyofunguliwa Kisutu Machi 18 na 20 mwaka huu dhidi yake na kisha iyapitie kwani wanaamini DPP alitumia madaraka yake vibaya kwa kumfutia kesi Lwakatare Na.37 na kisha machi 20 mwaka huu, kumfungulia tena kesi Lwakatare kwa makosa hayo.

“Kwa kuwa ofisi ya DPP ipo kwaajili ya kusimamia utawala wa sheria ,haujalidhishwa na uamuzi wa mahakama Kuu uliomfutia mashitaka yale matatu Lwakatare hivyo tunaiomba mahakama hii iitishe mwenendo wa kesi ulioamliwa na mahakama kuu uupitie kwani tunaamini kisheria jaji alikosea kutoa uamuzi ule kwani Lwakatare hakuwa ameomba afutiwe mashitaka yanayomkabili”alidai Dk.Feleshi.

Hata hivyo hadi jana mchana, uongozi wa mahakama ya rufaa ulikuwa bado haujapangia majaji wa kusikiliza ombi hilo.

Mei  8 mwaka huu,Jaji Kaduri alitoa uamuzi wa kufutia makosa  matatu ya tuhuma za ugaidi ambapo alisema uamuzi wake huo unafuatia baada ya kusikiliza hoja za mawakili wanaomwakilisha DPP na Lwakatare ambao waliwasilisha hoja zao mbele yake  Aprili 15 mwaka huu, mawakili wa Lwakatare pia walidai DPP alitumia madaraka yake vibaya kwa kuifuta na kufungua kesi upya na kwamba wanaomba mahakama hiyo  itoe amri ya kuifuta kesi ya msingi iliyopo mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu inayowakabili Lwakatare peke yake  kwa sababu mashitaka anayoshtakiwa nayo hayaonyeshi kama mshitakiwa alikuwa  na nia ya kutenda kosa la ugaidi.

Akitoa uamuzi wake Jaji Kaduri alisema  amekubaliana na hoja ya mawakili wa Lwakatare ya kwamba shitaka la pili,tatu na la nne  hayaonyeshi kama Lwakatare  alikuwa na nia ya kutenda koswa la ugaidi na kwasababu hiyo hati ya mashitaka Lwakatare atabakia akikabiliwa na kosa moja   ambalo ni Kosa la kwanza ambalo linawakabili washitakiwa wote kuwa ni la kula njama kutenda kosa la jinai kinyume na kifungu cha 284  cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 , na kwamba mnamo Desemba 28 mwaka jana, huko Kimara King’ong’o  Stopover, wote kwa pamoja walitenda kosa hilo kwa kutaka kutumia  sumu kwa lengo la kumdhuru  Denis Msaki  ambaye ni Mhariri wa habari wa Gazeti la Mwananchi ambalo ni kinyume na kifungu cha 227 cha sheria hiyo.

 “Baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili, mahakama hii inatoa amri ya kumfutia Lwakatare mashitaka matatu yaani kosa la pili, tatu na la nne kwa sababu jamhuri imeshindwa kuonyesha maelezo yanayotesheleza kumshitaki Lwakatare kwa kesi ya ugaidi na hivyo naamuru jalada la kesi ya msingi lilirudishwe mahakama ya Kisutu kwaajili ya mshitakiwa kuendelea kushitakiwa kwa kosa moja la kula njama ambalo linaangukia katika sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002”alisema Jaji Kaduri.

Hata hivyo Jaji Kaduri alitupilia mbali hoja za mawakili wa Lwakatare iliyodai DPP alitumia madaraka yake vibaya ya kufuta kesi na kuifungua upya ambapo alisema anakubaliana na hoja ya mawakili wa serikali  Prudence Rweyongeza na Ponsian Lukosi kuwa uamuzi wa DPP wa kufuta kesi ya Na.37 na kisha kuifungua kesi hiyo kwa mashitaka yale yake ambayo ilipewa Na. zote za mwaka huu,ulikuwa sahihi kisheria na akaamuru washitakiwa warejeshwe rumande.

Itakumbukwa kuwa Aprili 30 mwaka huu, kesi ya msingi inayomkabili Lwakatare katika mahakama ya Kisutu ilikuja kwaajili ya kujatwa na wakili wa Serikali Peter Mahugo alieleza mahakama hiyo kuwa kwa mujibu wa taarifa za jeshi la polisi upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na Hakimu Alocye Katemana aliarisha kesi hiyo hadi Mei 13 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya kutajwa.

Aprili 15 mwaka huu, wakili Wakili Prudence  Rweyongeza akijibu hoja za mawakili wa Lwakatare mbele ya Jaji Kaduri alikanusha hoja za mawakili wa Lwakatare zilizodai kuwa  DPP alitumia madaraka yake vibaya kuifuta kesi ya Na.37/2013 na akazitaja sababu zilizosababisha DPP aifute kesi hiyo na kufungua kesi mpya iliyopewa Na.6/2013 Machi 20 mwaka huu na mashitaka ni yale yale.

Wakili Rweyongeza aliitaja sababu ya kwanza iliyofanya DPP aifute kesi Na.37 /2013 iliyofunguliwa Machi 18 mwaka huu, ni kwamba uongozi wa mahakama ya Kisutu ulikosea na kuifungua kesi hiyo katika jalada la kesi zinazoendeshwa katika mahakama za chini (Subodnate Court) badala ya kuisajili kesi hiyo katika rejista ya kesi zinazopaswa kusikilizwa na Mahakama Kuu.

Sababu ya pili ni kwamba hakimu aliyeisikiliza kesi hiyo Emilius Mchauru alikosea kuwaruhusu washitakiwa hao kujibu mashitaka wakati mahakama ya Kisutu haina mamlaka ya kisheria ya kusikiliza kesi hiyo ya Ugaidi.
‘Kwasababu hizo mbili ndiyo maana DPP-Feleshi Machi 20 , kesi hiyo ilipokuwa inakuja kwaajili ya hakimu Machauru kutoa uamuzi wa ama kuwapatia dhamana au la, DPP akawasilisha hati ya kuifuta kesi na baada ya muda mfupi washitakiwa walikamatwa na kupandishwa kizimbani na kufunguliwa kesi mpya iliyopewa Na. 6/2013 ambayo ilifunguliwa na uongozi wa mahakama ya Kisutu kwa kufuata taratibu zote ,licha mashitaka yalikuwa niyale yale yaliyoyokuwa kwenye kesi iliyofutwa:

Akipangua hoja ya mawakili wa Lwakatare iliyokuwa ikiiomba Mahakama Kuu iifute kesi ya msingi inayowakabili washitakiwa hao kwasababu kosa la pili,tatu na nne hayaonyeshi nia ya washitakiwa hao kutenda makosa ya ugaidi,alidai kuwa hoja hizo zimeletwa wakati usiyo sahihi kwani kesi ya msingi ipo katika hatua za uchunguzi, upelelezi bado haujakamilika  na kwamba uenda siku za usoni DPP akaamua kubadilisha hati ya mashitaka kwahiyo ombi hilo halina msingi na kwamba hata hivyo Sheria ya Kuzuia Ugaidi  inasema kitendo cha kumteka nyara mtu ni kosa la ugaidi  kwahiyo kinachotakiwa kuzingatiwa katika hilo ni suala la ushahidi tu.

Hata hivyo Mei 13 mwaka huu, kesi ya msingi ya Lwakatare ilivyokuja katika Mahakama ya Kisutu kwaajili ya kutajwa, hakimu Alocye Katemana anayesikiliza kesi hiyo hakuwepo na mawakili wa Lwakatare Peter Kibatara aliwasilisha ombi la kuomba mteja wake apatiwe dhamana kwasababu kosa la kwanza la kula njama lilobaki linadhamana kwa mujibu wa sheria lakini hata hivyo wakili wa Serikali Prudence alililipinga ombi hilo kwa madai kuwa shauri hilo lipo hatua za uchunguzi  kilichopo mahakamani hapo ni jalada la tuhuma zinazowakabili washitakiwa ambazo zipo katika hatua za uchunguzi na kwamba tuhuma hizo mwisho wa siku zitakufunguliwa kesi rasmi Mahakama Kuu kwani Mahakama Kuu ndiyo yenye mamlaka ya kuisikiliza hivyo huwezi mahakama haiwezi kutoa dhamana kwa kesi ambayo haipo(Pending Trial) .

“Na kwa mazingira ya shauri linalomkabili Lwakatare hapa Mahakama ya Kisutu,lipo katika hatua za uchunguzi na  bado DPP hajafungua kesi rasmi Mahakama Kuu, sasa tunashangaa mawakili wa washitakiwa wanawasilisha ombi la dhamana leo hii katika mahakama hii wakati maamuzi hayo ya mahakama ya Rufaa yapo na bado hajatenguliwa?

Rweyongeza aliomba mahakama hiyo itupilie mbali maombi ya mawakili wa utetezi kwasababu hakuna kesi rasmi iliyofunguliwa na DPP mahakama Kuu dhidi ya washitakiwa na kwamba shauri lililopo katika mahakama ya Kisutu lipo katika hatua za uchunguzi.

Baada ya mawakili wa pande zote mbili kuwasilisha maombi hayo, Hakimu Fimbo alisema amesikia maombi hayo na ayafikisha kwa hakimu anayesikiliza kesi hiyo ambaye ni Katemana ambaye kwa jana hakuwepo ofisini kwasababu alikuwa na udhuru  na kwamba Katemana ndiyo atakayetolea uamuzi kuhusu maombi hayo na akaiarisha kesi hiyo hadi Mei 27 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya kutajawa na akaamuru washitakiwa warejeshwe rumande na kufanya umati wa wafuasi wake wakiwa wamejiinamia kwa uzuni .

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi Mei 23 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.