AKIBA BENKI KORTINI KWA UPOTEVU WA FEDHA ZA MTEJA WAKE



Na Happiness Katabazi

MKURUGENZI wa Kampuni ya Principal Company Limited, Godfrey Mosha ameieleleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam jinsi  Benki ya Akiba Commercial  Tawi la Ubungo ilivyoidhinisha malipo ya fedha  kwa mtu mwingine kutoka katika akaunti yake ndani ya benki hiyo, bila yeye kuwa na taarifa wala kuridhia.

Katika kesi hiyo ya madai ya uzembe iliyofunguliwa na Mosha dhidi ya Benki ya Akiba, inayosikilizwa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Warialwande Lema, Mosha anaomba Benki hiyo imlipe  Sh.milioni 46.8 , zilizolipwa kwa mtu asiyemfahamu kwa kutumia hundi nne tofauti na kwa tarehe tofautitofauti ambazo alidai hundi hizo zimeghushiwa.

Akiongozwa na wakili wake Michael Ngaro kutoa ushahidi wake mbele ya Hakimu Lema, Mosha ambaye ni mlalamikaji katika kesi hiyo, alidai kuwa aligundua  hamisho hilo la kiasi hicho cha fedha katika akaunti ya kampuni yake Na. 0400438671, Novemba 15, 2011, alipochukua taarifa ya kibenki (Bank Statement).

Mosha alidai kuwa  baada ya kubaini hamisho hilo , alikwenda makao makuu ya benki hiyo ambako alimuona Meneja wa Fedha, Vicent Antony na kumwalifu kuhusu  tukio hilo wakati yeye hajawahi kuidhinisha hamisho hilo.

“Vicent aliniambia kuwa siyo transfer (hamisho) bali ni malipo yaliyofanyika kwa kutumia cheque. Aliniambia namba za hundi hizo na ikaonekana kuwa zililipwa kwa Rafael John Mkwabi, mwenye namba ya akaunti 11000787541.”, alidai Mosha na kuongeza:

“Binafsi huyo John  sijawahi kumwandikia hundi wakati wowote ule , wala sijawahi kufanya naye biashara, sijawahi kukutanana naye, wala simfahamu kabisa.”

Mosha alidai kuwa hundi hizo zilikuwa zimesainiwa na Vicent na Meneja Mkuu, Salehe Ramadhani, huku akidai kuwa saini inayoonekana katika hundi hizo si yake.

Alizitaja hundi hizo kuwa ni hundi namba 083722, ya Sh11.6 milioni iliyolipwa Novemba 11, 2011 na  hundi namba 083723, ya Sh 9 milioni, pia iliyolipwa tarehe hiyo.Hundi nyingine  ina namba   083724 , ya Sh milioni 14.4  iliyolipwa Desemba 2011, na hundi namba 083725, ya Sh.milioni 11.8  iliyolipwa Desemba 3, 2011.

Mosha kupitia wakili wake Ngaro alizitoa hundi hizo na nyaraka nyingine mbalimbali   na kuomba zipokelewe kama vielelezo.Na baada ya kumaliza kutoa ushahidi wake, wakili , Ngalo alifunga ushahidi na hakimu Lema aliarisha kesi hiyo hadi Julai 8 mwaka huu, iyakapokuja kwaajili ya mdaiwa ambaye ni benki ya Akiba inayotetewa na wakili wa kujitegemea Karoli Tarimo  waanze kujitetea.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatatu, Juni 24 mwaka 2013.

HEKO MIZENGO PINDA KWA AGIZO HILO KWA JESHI LA POLISI






Na Happiness Katabazi
JUNI 20 mwaka huu, Waziri Mkuu Mizengo Pinda akiwa bungeni alitoa agizo wa Jeshi la Polisi kutumia nguvu kuwashughulikia wale wote wanaojihusisha na vitendo vya uvunjifu wa sheria ikiwemo kukaidi amri zinazotolewa na jeshi la polisi.

Kauli hiyo ya Pinda imekuja hasa kutokana na vurugu zilizotokea Arusha kuanzia wiki iliyopita ambapo watu watatu wamepoteza maisha na wengine kujeruhiwa vibaya kutokana na mtu asiyejulikana kurusha bomu la mkono katika mkutano wa siasa uliokuwa ukifanyika katika viwanja vya Soweto wilaya ya Arusha mjini, muda mfupi baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe kumaliza kuwahutubia wafuasi wake na hivyo kusababisha taharuki kubwa.

Wakati mauji hayo ya kitokea huko jimbo la Monduli jumapili iliyopita kuliwa na uchaguzi wa Udiwani, ambapo Mbunge wa Chadema,(Arumeru Mashariki), Joshua Nansari, ilidaiwa alipigwa na watu wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa CCM hadi kulazwa kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kupishana kauli na mfuasi mmoja wa CCM na mbunge huyo hali iliyosababisha Nansari kupigwa.

Juni 16 na 17 mwaka huu,  kwa nyakati tofauti  Mbowe alizungumza na waandishi wa habari na kusema tukio lile lilipangwa na kwamba anaoushahidi wa aliyefanya tukio lile.Na baadhi ya watu wengine walinukuliwa wakisema Jeshi la polisi linamfahamu aliyefanya unyama ule ila imeamua kumficha.

Baada ya Mbowe na baadhi ya wananchi hao kusema hayo, Kamisha wa Oparesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Paul Chagonja, aliibuka na kusema wanamtaka Mbowe ajisalimishe polisi na aelete huo ushahidi anaosema anao, na akatoa rai kwa mwananchi yoyote  mwenye kuhafamu aliyerusha bomu hilo aende kutoa taarifa na zitafanyiwa kazi kwani tukio lile lina uvunjifu wa sheria na limesababisha watu kupoteza maisha na wengine kujeruhiwa vibaya.

Juni 20 mwaka huu, Mbowe alijisalimisha Polisi na kuhojiwa na kisha kuzungumza na waandishi wa habari yale aliyoyazungumza na muda mfupi baada ya Mbowe kuzungumza aliyoyazungumza kwa waandishi wa habari, Kamishna Changonja naye aliwaambia waandishi wa habari kuwa kilichoelezwa na Mbowe kwa vyombo vya habari ni tofauti na kile alichokieleza Mbowe wakati akihojiwa na jeshi la polisi.

Na kwa kauli hiyo ya Kamishna Chagonja inatutaka wananchi wenye akili timamu kutumia ule msemo wa watoto wa mjini usemao ‘akili kumkichwa’.

Baada ya hapo kumekuwa na kauli ya za kama kurushia vijembe kama vya ‘mtu na mke mwenzie’ baina  ya polisi na viongozi wa Chadema, jambo ambalo hivi sasa limeonyesha nchi hii hatuheshimiani,hakuna mkubwa wala mdogo, baba ,mama, mwanamke ,mwanaume hajulikani, askari  ,raia hajulikani.Kila mtu anataka kujifanya ana sauti na madaraka hata kama hana madaraka ya kijeshi na kiserikali.

Jeshi la polisi linapofanyakazi yake kwa mujibu wa sheria utawasikia wanaharakati na wanasiasa uchwara wakishinikiza jeshi la polisi lipanguliwe,lina kiuka haki za binadamu wakati ni baadhi ya hawa hawa wanasiasa uchwara wa hapa nchini ndiyo chanzo madhara yote yanayotokea hivi sasa.Ina kera sana.

Lakini yote hii imesababishwa  na baadhi ya viongozi  ndani ya  CCM, serikalini na vyama vya upinzani ni mandumila kuwili, wanafki, wasaliti, wasiyo na maadili,wanajikomba ili wapate vyeo na wapendwe na wananchi, wavivu wa kufikiri na ndiyo maana hii leo hapa nchini baadhi ya wananchi wamefikia hatua ya kuonyesha dharau hii kwa askari wetu wa jeshi la polisi wazi wazi hata kama jeshi la polisi linatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa  sheria licha ni kweli kuna baadhi ya askari wa jeshi la polisi wamekuwa wakijihusisha na vitendo vya utovu wa maadili hata Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali (IGP), Said Mwema amekuwa akikiri hilo ana amekuwa akiagiza mamlaka zake kuwachukulia hatua askari hao wanaojihusisha na vitendo hivyo vya kuonea raia, ujambazi na mfano si wa kutafuta .

Kwani   Machi 13 mwaka huu, mbele ya Hakimu Mkazi Emilius Mchauru , Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP), aliwafikishwa jumla ya askari Polisi mkoa wa Dar es Salaam.Washitakiwa hao  ni Sajenti Dancan Mwasabila (43) mkazi wa Kiwalani, Koplo Geofrey (39) Mbezi Luis, Koplo Rajab Nkurukwa (46) mkazi wa Buguruni, Kolpo Kawanani Humphrey (34) mkazi wa Kijitonyama na Koplo Kelvin Mohamed (49) mkazi wa Gongo la Mboto.

Wakili wa serikali Bernad  Kongola alidai kuwa Desemba 18 mwaka jana katika eneo la Kariakoo Wilaya ya Ilala Dar es salaam waliiba sh,milioni 150 . Na kesi hiyo inaendelea mahakamani hapo. Na  si kesi hiyo tu , pia  hata yule  askari polisi Pacificus Cleophase Simon (23)  anayedaiwa kumuua marehemu Daudi Mwangosi aliyekuwa Mtangazi wa Chanel Ten, naye amefunguliwa kesi ya mauaji katika mahakama ya Mkoa Iringa na kesi yake inaendelea.Na bado washitakiwa hao ambao ni askari polisi watabaki kuitwa ni watuhumiwa kwani bado mahakama haijawakuta na hatia.

Lakini kwa sinema hii inayoendelea kuchezwa na jeshi la polis, ofisi ya DPP na Chadema kwa zaidi ya miaka minne sasa imeanza kunifanya nianze kujiuliza maswali mengi yasiyo na majibu.

Mosi, nimejiuliza na bado naendelea kujiuliza hii ‘sinema’ inayochezwa na jeshi la polisi, viongozi wa juu wa Chadema na ofisi ya DPP , ina nini nyuma yake?

Maana ‘sinema’ ambayo inaendelea kuchezwa na makundi hayo matatu kwa zaidi ya miaka mitatu sasa, itakamilika lini?Kwani itakumbukwa kuwa miaka mitatu iliyopita Chadema walifanya mkutano wa hadhara Arusha mjini na kusababisha polisi kutumia nguvu na watu zaidi ya wawili wakajikuta wanapoteza maisha na mwishowe Mbowe, Slaa,Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Arusha, Simson Mwigamba na viongozi wengine walikamatwa na kufunguliwa kesi ya uchochezi katika mahakama ya Mkoa wa Arusha. Wala Mwanasheria Mkuu wa Serikali Kanda ya Arusha hakuwasilisha hati ya kuwafungia dhamana watuhumiwa hao.

Na matukio mengine kama matatu ambayo polisi iliwatuhumu viongozi wa Chadema kutoa maneno ya uchochezi na kufanya mikusanyiko haramu mkoani Arusha, ambapo Mbowe,Godbles Lema na vingozi wengine wana kabiliwa na kesi za tuhuma kufanya uchochezi zaidi ya moja.Na hadi leo kesi zao zinaendeshwa kwa kasi ya kinyonga tofauti na kesi nyingine.

Lakini hata siku moja hatujawai kumsikia Mwanasheria Mkuu wa Serikali Kanda ya Arusha, kuwasilisha mahakamani hati ya kuwafungia dhamana washitakiwa hao, au Kamanada wa polisi Mkoa wa Arusha kuwanyima dhamana ya polisi watuhumiwa hao ambao jeshi la polisi kila kukicha limekuwa likisema halimuogopi mtu na alimpendelei mtu.

Wakati viongozi hao wa juu wa Chadema wakiipata pepo hiyo, tungali tukikumbuka hapa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Sheikh Ponda Issa Ponda na Mukadamu Swalehe ambao walikuwa wakishitakiwa na wenzao 47 walifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Oktoba 18 mwaka jana, wakikabiliwa na makosa matano ya kula njama,kuingia kwa jinai, kujimilikisha kwa nguvu kiwanja cha Chang’ombe Markas mali ya kampuni ya Agritanza Ltd , wizi wa Sh.milioni 59 na uchochezi ambalo lilikuwa linamkabili Ponda na Mukadamu peke yao.

DPP alimfungia dhamana Ponda na Mukadamu na kweli walikaa gerezani tangu Oktoba 18 mwaka jana  hadi kesi yao hiyo ilipotolewa hukumu Mei 9 mwaka huu, ambapo Hakimu Mkazi Victoria Nongwa aliwaachiria huru washitakiwa wote 48 na akamtia hatia Ponda peke yake tena kwa kosa moja tu la kuingia kwa jinai na akamfunga kifungo cha nje cha mwaka mmoja.

Itakumbukwa kuwa Machi 21 mwaka huu, Hakimu Mkazi wa mahakama ya Kisutu ,Sundi Fimbo aliwahukumu adhabu ya kwenda jela mwaka mmoja jumla ya wafuasi 53 wa Sheikh Issa Ponda ,baada ya kuwakuta na hatia ya kufanya kosa la kula njama kutenda kosa kinyume na kifungu 384 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002, kosa la pili ni la kufanya mkusanyiko haramu kinyume na kifungu cha 74 na 75 cha sheria hiyo  ambavyo vinasomwa pamoja na kifungu cha 43(2)(4) na 46 cha Sheria ya Jeshi la Polisi ya mwaka 2002 , kuwa Februali 15 mwaka huu, walitenda kosa hilo la kutaka kuandamana kwenda katika ofisi ya Mkurugenzi Mkuu wa Mashitaka ,Dk.Eliezer Feleshi kumshinikiza ampatie dhamana Sheikh Ponda,kwani Feleshi alimfungia dhamana Ponda tangu Oktoba 18 mwaka jana hadi Mei 9 mwaka huu, alipohukumiwa kifungo cha nje kwa mwaka mmoja.

Wafuasi hao wa Ponda walifikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani hapo Februali 18 mwaka huu, na nilikuwepo mwanzo hadi mwisho wa kesi hiyo,na siku ya kwanza tu katika hali iliyotushitua wengi,wakili Mwandamizi wa Serikali Bernad Kongora alidai kuwa upelelezi umekamilika na kesho yake yaani Februali 19 mwaka huu, upande wa jamhuri ukawasomea maelezo ya awali washitakiwa na siku hiyo hiyo shahidi wa kwanza wa upande wa jamhuri (ZDCO) Mkoa wa Dar es Salaam, Msangi alipanda kizimbani na kuanza kutoa ushahidi wake.

Hakika kesi ya wafuasi hao wa Ponda na kesi ya Ponda iliendeshwa kwa kasi sana ambayo ilitufanya tujiulize ni kwanini kesi hizi mbili zinaendeshwa kwa kasi hiyo, askari wengi zaidi ya 30 kutanda mahakamani hapo kila siku kesi hizo zinapokuja kusikilizwa. Na katika kesi hii ya wafuasi 53 wa Ponda, DPP aliwafungia dhamana washitakiwa watatu wengine wakapewa dhamana na mahakama baadaye kwani mahakama hapo mwanzo iliwanyima dhamana kwasababu ya hali ya usalama mkoani Dar es Salaam,iliuwa haijatengamaa.

Na itakumbukwa kuwa wafuasi wa Ponda hawakupewa dhamana ya polisi kwani walikamatwa Ijumaa na Jumatatu  yake waliletwa mahakamani , pia wafuasi wa Ponda walikamatwa Februlia 15 mwaka huu, tena kama Mukadamu alikaa mikononi mwa jeshi la polisi kwa siku tano tena bila kupewa dhamana na kisha akafikishwa mahakamani na DPP akamfungia dhamana kama alivyopewa mamlaka hayo kwa mujibu wa kifungu cha 148(4) cha Sheria ya Mwendeno wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002.

Na baadhi ya madai ya Ponda na wafuasi wenzake ni kwamba serikali inawaonea Waislamu na inawapendelea wakristo,mali za waislamu zinafujwa na viongozi wa Bakwata na madai mengine mengi.

Sote ni mashahidi kuwa tuhuma zilizokuwa zikielekezwa na jeshi la Polisi kwa Ponda na wafuasi wake ambao walishitakiwa nao hazikuweza kusababisha watu kupoteza maisha, ni vurugu ambazo zilisababisha uvunjifu wa amani wa watu kushindwa kufanya shughuli zao kwa amani kwa kuhofia maandamano ya wafuasi wale ambayo yalikuwa hayana kibali cha polisi.

Watu tunaofiriki sawa sawa tumeanza kujiuliza ni kwanini basi wanapoandamana watu wanajitambulisha kuwa ni waumini wa dini ya kiislamu bila kufuata sheria za nchi, jeshi la polisi linawakamata haraka haraka na DPP anaibukia mahakamani na kuwafungia dhamana washitakiwa hao?

Kwa nini baadhi ya wafuasi wa Chadema wanapofanya kile kinachodaiwa na jeshi la polisi kuwa ni mikusanyiko,maandamano haramu ambayo imepigwa marufuku na jeshi la polisi na polisi wamekuwa wakidai kuwa baadhi ya wafuasi wa chama hicho wamekuwa wakipambana na polisi, jeshi la polisi linasuasua kuwakamata na likiwakamata utasikia muda mfupi limewapa dhamana, na hatumsikii DPP wala Mwanasheria wa Serikali Kanda ya Arusha akiwasilisha hati ya kuzuia dhamana kwa baadhi ya viongozi hao wa Chadema  ambao kila kukicha tumekuwa tukilisikia  jeshi la polisi likiwatuhumu kufanya vurugu na kuwafungulia kesi za uchochezi lakini kesi hizo zinakwenda mwenendo wa kinyonga ukilinganisha na kesi nyingine kama hizo za Ponda na wafuasi wake, watuhumiwa ambao wanaelezwa kuwa ni waumini wa dini ya Kiislamu ambao wanadaiwa kuchoma makanisa eneo la Mbagala?

Au kwa sinema hii, mnataka waamini ile minong’ono inayoenezwa chini chini kuwa baadhi ya viongozi wa Chadema ambao wanatuhumiwa na jeshi hilo kufanya vitendo vya uvunjifu wa sheria wanapata jeuri hiyo kwasababu eti baadhi ya viongozi wa juu wa jeshi hilo la polisi wanatoka wote mikoa ya Kanda ya Kaskazini ndiyo maana wanawalea?

Binafsi siamini katika minong’o hii kwani ninapinga upendeleo wa aina yoyote ile,ubaguzi wa aina yoyote na uonevu pia.Na ninavyomfahamu IGP-Mwema si mtu wa kuendekeza ujinga huo na ndiyo maana katika utawala wake ndani ya jeshi hilo, ameweza kuruhusu askari wengi tu kushitakiwa katika mahakama za kijeshi na mahakama za uraiani.

Na mimi nikiwa mwandishi wa habari za mahakamani ni shahidi katika hilo.Na katika hilo amejitofautisha na watangulizi wake ambapo licha wananchi walikuwa wakilalamika kuwa kuna baadhi ya askari polisi wanaonea raia, wanashiriki katika vitendo vya utovu wa nidhamu lakini watangulizi wa IGP-Mwema waliweka pamba masikioni ,hawakuwachukulia hatua askari polisi wao.

Watanzania tunapwasa tujiulize kunanini hapa? Kwa nini wananchi wengine wakituhumiwa kufanya vitendo vya uvunjifu wa sheria,hata kama hakuna ushahidi wa moja kwa moja wa kuhusika kutenda uhalifu huo, hatusikii polisi ikiwabembeleza wananchi hao kwa kuwatangazia kupitia umma kuwa wajisalimishe, ila inapotokea polisi inawatuhumu viongozi wa Chadema kuhusika kutenda vitendo vya uvunjifu wa sheria ,basi utalisikia jeshi la polisi likijitokeza hadharani kutoa rai ya kutaka Mbowe na Lema wajisalimishe.

Ninavyofahamu mimi serikali ina mkono mrefu pindi inapoamua kuweka unafki, ghiliba pembeni na kuamua kufanyakazi yake, na serikali inamfahamu kila mwananchi nyendo zake na anapoishi.

Lakini itakumbukwa kuwa mwaka juzi, Mwenyekiti wa Chama Cha Demokratic,Mchungaji Christopha Mtikila aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya kuchapisha wakala wa uchochezi ambao alimuita Rais Kikwete ni gaidi anaungamiza ukristo, kesi hiyo mwanzoni ilikuwa kwa hakimu Waliarwande Lema, na siku hiyo ya kesi Mtikila alichelewa kwa zaidi ya saa mbili kuingia mahakamani akakuta kesi hiyo imeishahairishwa na hakimu Lema kato amri ya Mtikila akamatwe, na ilipofika saa tano, Mtikila alifika mahakamani hapo akajikuta amewekwa chini ya ulinzi na wanausalama  na Mtikila alivyopelekwa mbele ya Hakimu Lema ajieleze kwanini alichelewa kufika ,Mtikila alijitetea kuwa wakati akiwa njiani kuja kwenye kesi yake suruali yake ilichanika hivyo alilazimika kurudi nyumbani kubadilisha nguo kisha ndiyo aje mahakamani lakini utetezi huo ulikataliwa na alipelekwa rumande.  

Hata hivyo mwaka jana, Hakimu Mugeta ambaye alikuwa akisikiliza kesi hiyo ya Mtikila baada ya Mtikila kumkataa Lema asiendelee na kesi yake kwani hana imani naye na akamtaja hakimu Lema kuwa ni mtu katili asiyejali utu wa watu wengine ,alimwachilia huru Mtikila kwa maelezo kuwa upande wa jamhuri umeshindwa kuthibitisha kesi hiyo.

Turejee kwenye kauli ya ‘Msomi wa Sheria ’ Mizengo Pinda,kwanza binafsi ninaunga mkono kauli hiyo  na ninaamini  wale wenye akili timamu, ambao hawajawahi kupata magonjwa yanaombatana na mtikisiko wa ubongo na elimu zao siyo za kugelezea mitihani watakubaliana na makala yangu hii ambayo inaunga mkono kauli hiyo Pinda. 
Na kwa wale mambumbumbu wa sheria watampinga Pinda tena bila kutoa vielelezo vya kumpinga au watajitutumua kwa kutumia Ibara 13(6) (b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. Ambapo ibara hiyo inasema ‘mshitakiwa yoyote anayeshitakiwa kwa makosa ya jinai asichukuliwe kuwa ana hatia  hadi pale mahakama itakapomkuta na hatia’.

Lakini atakayetumia ibara hiyo kumpinga kauli ya Pinda atakuwa amekosea , kwani Ibara hiyo inatumika pale tu mshitakiwa aliyeshitakiwa kwa makosa ya jinai.Na kwa mujibu wa agizo la Pinda ni amewataka polisi kutumia nguvu kuwakamata wale wote wanaokaidi amri za jeshi hilo na kuvunja sheria za nchi na kisha kuwafikisha kwenye ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa  Mkoa  husika kwaajili ya ofisi hiyo ya Mwanasheria Mkuu wa serikali iwafikishe mahakamani.

Kwani kwa zaidi ya miaka mitano sasa, Jeshi la polisi limeondolewa jukumu la kuwafungulia kesi washitakiwa wa makosa ya jinai badala yake limebakidhiwa majukumu mengine yakiwemo majukumu ya kupeleleza matukio ya uhalifu,kuwakamata.

Na hivyo basi jukumu la kuwafikisha watuhumiwa wa kesi za jinai mahakamani limekabidhiwa kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kama ilivyoanishwa kwenye kifungu cha 90 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002.

Binafsi nasema kauli hiyo ya  Pinda ni kauli  yenye  afya na imekidhi  kiu ya watanzania wengi wenye akili timamu tuliokuwa tukiisubiri kwa hamu na ama kwa hakika kauli hiyo inaungwa mkono na kifungu cha 21(2) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002,  ambacho kifungu hicho kinawataka polisi kutumia nguvu kuwakamata wale wote wanavunja kwa makusudi  sheria za nchi.

Lakini licha ya  mimi binafsi kuunga mkono kauli hiyo ya Pinda, lakini napenda niseme wazi baadhi ya viongozi wa serikali ya awamu ya nne inayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete wamekuwa ni ndumila kuwili, hawana msimamo na maelekezo wanayoyatoa kwa watendaji wao wa chini, kwani  ni aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Rick Mahalu  ambaye alifunguliwa  kesi ya uhujumu uchumi na wizi Euro milioni 3 katika ununuzi wa jengo la ubalozi wetu nchini Italia,muda mfupi tu tangu serikali ya Rais Kikwete iingie madarakani.

Na  mawakili wa TAKUKURU  walidai Mahalu  hakupewa idhini na serikali ya kununua jengo hilo kwa njia ya mikataba miwili na kwamba serikali ilikuwa haina taarifa za yeye kununua jengo hilo kwa njia ya mikataba miwili.

Lakini katika utetezi wake Mahalu na shahidi wake Rais Mstaafu Benjamin Mkapa  mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu , Ilvin Mugeta,binafsi nilikuwepo kwani nimeudhuria kesi hiyo mwanzo hadi mwisho. Mahalu alionyesha vielelezo vyake vinavyoonyesha kuwa serikali ilibariki ununuzi wa jengo hilo kwa njia ya mikataba miwili, na Rais Kikwete ambaye wakati huo alikuwa ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,ndiye aliyempa nguvu ya kisheria (Power of Attoney), Mahalu kuendelea na shughuli zote za ununuzi wa jengo hilo.

Na Rais Mkapa katika ushahidi wake, alieleza kuwa yeye ndiye aliyekuwa kiongozi mkuu wa mhimili wa serikali na kwamba serikali yake ya awamu ya tatu ilimwagiza Mahalu anunue jengo la ubalozi wetu kwanjia ya mikataba miwili na kwamba anashangazwa ni kwanini Mahalu ameshitakiwa kwa makosa hayo wakati ni serikali yake ya awamu ya tatu ambayo Kikwete alikuwa ni mjumbe wa Baraza la mawaziri na baraza hilo la mawaziri ililidhia  Mahalu aendelee na ununuzi wa jengo la ubalozi wetu kwa utaratibu alioutumia Mahalu kununua jengo hilo.

Lakini Agosti 9 mwaka jana, Hakimu Mugeta alitoa hukumu ya kesi hiyo ya kihistoria na kumwachiria huru Mahalu na Grace Martin  baada ya kuona upande wa jamhuri umeshindwa kuthibitisha kesi hiyo.Hata hivyo Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP), Dk.Eliezer Feleshi hajaridhishwa na hukumu hiyo na amekata rufaa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, na rufaa hiyo itaanza kusikilizwa rasmi Julai Mosi mwaka huu, mbele  ya Jaji John Utamwa.

Kwa hiyo hukumu hiyo ya kesi ya Mahalu, imetufundisha kuwa ndani ya serikali kuna viongozi au watendaji ambao hawapo njia moja, wanafki na wazandiki wanatoa maelekezo kwa watendaji wao wa chini watekeleze jambo fulani, na watendaji hao wakishatekeleza jambo hilo mwisho wa siku ama wanawaundia tume kuwachunguza, kuwafukuza kazi,au kuwafikisha mahakamani kitendo ambacho hivi sasa kimewafanya baadhi ya watendaji wa baadhi ya vyombo vya dola tunaozungumza nao kutotilia mkazo maelekezo yanayotolewa kwao na viongozi wa kisiasa na wanawadharau sana viongozi wa kisiasa.

Nimalizie kwa kusema hivi Chadema, CUF, CCM, NCCR na viongozi wa vyama vyote vya siasa vitapita, ila Tanzania yetu itabaki. Hivyo watanzania wote tuukatae  uhuni na umwagaji damu wa aina yoyote unaofanywa ama na wanasiasa, wananchi wanaokubali kutumiwa na wanasiasa uchwara, au njaa zao zinawatuma kufanya matendo ya uvunjifu wa amani ili wapate ujira. 

Na vyombo vya dola bado ninaimani navyo kuwa vinapoamua kufanyakazi yake kikamilifu vinafanya.Na viomba vitambue kuwa hivi sasa tayari sifa ile ya amani ambayo Tanzania tuliyokuwa tukijivunia imeishaingiwa na doa ,hivyo ni kazi kwenu wanausalama na wananchi kwa ujumla kukomesha wale wote wanaotia doa amani yetu kwa gharama zozote ilimradi amani yetu iendelee kudumu.
Baba wa Taifa, marehemu Julias Nyerere na makomredi wenzake wakati wanatafuta uhuru wa Taifa la Tanganyika, hawakutumia silaha  kutafuta uhuru, walitumia  akili, weledi na siasa safi hadi wakatuletea uhuru. 

Sasa inakuwaje leo hii wanatokea wahuni wachache tu ambao hata mkononi hawajai ,hawana hata uwezo wala kufanya ushawishi wa kutengeneza uasi ndani ya majeshi yetu wakaweza kupata silaha na kwenda kujificha msituni, wawe na jeuri ya kila kukicha kuanzisha matukio ya uvunjifu wa amani ambayo yanasababisha pia wananchi wenzetu kupoteza maisha, kujeruhiwa,makazi ya watu kuharibiwa, shughuli za kiuchumi kusimama, watu kuanza kuishi kwa hofu utafikili wanaopa Barazani.Maana siku zote mtu anayeoga barazani anakuwa na wasiwasi kuwa kuna mtu anaweza kupita akamtazama maungo yake.

Vyombo vya dola mmeapa kuilinda serikali ya Jamhuri ya Muungano na wananchi wake kwa hali yoyote ile, sasa tunawaomba sasa mtumie mafunzo yenu mliyopewa mkiwa katika vyuo vya kijeshi kuwashughulikia wale wote wanaojihusisha na uvujifu wa amani kwani wahalifu kama wahalifu wengine bila kujali mharifu huyo ni kiongozi wa serikali, chama cha siasa au mhalifu huyo anafahamiana na kiongozi fulani.Tumechoka na matukio haya ya kishenzi na kikatili.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika

Facebook: happy katabazi
0716 774494
Juni 21 mwaka 2013.    

ALIYEJIFANYA MWANDISHI WA HABARI JELA MIAKA MITATU





Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala Dar es Salaam, imemhukumu kwenda jela miaka mitatu au kulipa faini ya Sh.500,000  Msambazaji wa Gazeti la Mtandao,Salum Hassan Goko baada ya kumkuta na hatia ya kujifanya Mwandishi wa habari wa gazeti hilo na kuomba na kupokea rushwa ya Sh.200,000 kutoka kwa Meneja wa Kampuni ya Vinywaji Baridi aina ya Pepsi, Rashid Chenja.

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu wa Jocye Minde ambaye alisema amefikia uamuzi huo kwani mawakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoa wa Ilala Dar es Salaam, uliokuwa ikiliwakilishwa na  Sarha  Abdallah na Sophia Gula wameweza kuithibitisha kesi hiyo  ya tuhuma za rushwa Na.24/2008 bila ya kuacha mashaka yoyote na kwamba mshitakiwa huyo alikuwa akikabiliwa na makosa ya kuomba na kupokea rushwa ya Sh.200,000 kinyume na kifungu cha 15(1) A cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na.11 ya mwaka 2007.

Hakimu Minde alisema kwa mujibu wa maelezo ya mashahidi na vielelezo vilivyotolewa mahakamani hapo vilionyesha wazi kuwa mshitakiwa Goko alikuwa ni mfanyakazi idara ya Usambazaji wa gazeti hilo la Mtandao lakini alijifanya yeye ni mwandishi wa habari wa gazeti hilo na akamfuata Chenja na kumweleza kuwa wanataarifa zake kuwa anatembea na mke wa mtu hivyo wakamtaka Chenja awapatie fedha ili wasichapishe habari hizo na endapo asingewapatia fedha hizo wangeenda kuzichapisha na zingemchafulia jina lake.

“Chenja alikubaliana na maelekezo hayo ya Goko na akamtaka Goko aje mwisho wa mwezi ili ampatie fedha ili asiandike habari yake na ushahidi wa mawasiliano ya simu unaonyesha Goko na Chenja walikuwa wanawasiliana na Chenja alienda kutoa taarifa Takukuru na ndipo Takukuru walimpatia Sh.200,000 za mtego wa Rushwa na Goko alipokwenda kuzipokea fedha hizo alikamatwa na maofisa wa Takukuru na kisha kufikishwa mahakamani”alisema Hakimu Minde.

Hakimu huyo alisema amefikia uamuzi wa kuukataa utetezi wa Goko ambaye alikuwa akitetewa na wakili wa kujitegemea Tuliamwesige kwasababu ushahidi wake ni dhahifu  hivyo mahakama yake imeridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa jamhuri na kwamba imemkutana na hatia ya makosa hayo na hivyo inamhukumu kwenda jela miaka mitatu au kulipa faini y a Sh.500,000. Hadi saa nane mchana jana Goko alikuwa chini ya ulinzi mahakamani hapo.

 Katika hatua nyingine mhariri  Mtendaji wa Kampuni ya New Habari ,Absalom Kibanda ambaye Machi mwaka huu alitekwa na kujeruhiwa vibaya na watu wasiyojulikana na hivyo kusababisha kushindwa kuudhiria katika kesi ya kuandika na kuchapisha makala ya uchochezi, jana kwa mara ya kwanza aliweza kufika katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam, kuudhulia kesi yake.

Mbali na Kibanda katika kesi hiyo washitakiwa wengine ni aliyekuwa Kaimu Mhariri wa gazeti la Mwananchi , Theophil Makunga na mwandishi wa makala hiyo Simon Mwigamba ambao wanatetwa na mawakili wa kujitegemea Isaya Matambo, John Mhozya.

Hakimu Mkazi Waliarwande Lema alisema kesi hiyo ilikuwa imekuja kwaajili ya kitajwa lakini amepokea taarifa kutoka kwa mdhamini wa Mwigamba kuwa Mwigamba ameshindwa kuudhulia jana mahakamani hapo kwasababu ni mgonjwa hivyo anaiarisha kesi hiyo hadi Julai 17 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya kuendelea kusikilizwa.

Disemba mwaka 2011 ilidaiwa mahakamani hapo na mawakili wa upande wa jamhuri kuwa washitakiwa hao walitenda makosa hayo ya kuruhusu na kuchapisha makala ya uchochezi katika gazeti la Tanzania Daima iliyokuwa na kichwa cha habari “Wakala Maalum kwa askari wote’.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Juni 21 mwaka 2013.

IDD SIMBA AFUTIWA KESI YA UHUJUMU UCHUMI







Na Happiness Katabazi

HATIMAYE Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imemwachiria huru Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la UDA,Idd Simba, na wenzake watatu waliokuwa wakikabiliwa na makosa mbalimbali likiwemo kosa la uhujumu uchumi kwa maelezo kuwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Dk.Eliezer Feleshi amewasilisha hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea kuwashitaki.

Mbali na Simba ambaye anatetewa na wakili maarufu nchini Alex Mgongolwa ambaye ni Mwenyekiti wa Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam na mwanasiasa mkongwe nchini,wengine ni Mkurugenzi Salum Mwaking’inda, Meneja wa shirika hilo Victor Milanzi na Mkurugenzi wa Kampuni ya Simon Group  Ltd, Simon Kisena ambao wanatetewa na Romani Masumbuko .

Amri ya kufutiwa kesi hiyo ya uhujumu uchumi Na.3/2013 ilitolewa jana asubuhi na Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo Ilvin Mugeta muda mfupi baada ya wakili wa serikali Awamu Mbagwa kuikumbusha mahakama kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya upande wa jamhuri kuwasomea maelezo ya awali washitakiwa na kuwa hata hivyo upande wa jamhuri hautaweza kuwasomea tena maelezo hayo ya awali kama  ilivyokuwa imepangwa na mahakama kwasababu Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP), Dk.Elizer Feleshi amewasilisha mahakamani hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea kuwashitakiwa washitakiwa wote chini ya kifungu cha 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002.

 Baada ya wakili huyo wa serikali Mbagwa kutoa hati hiyo , wakili Mugeta alimpatia fursa wakili wa Idd Simba, Alex Mgongolwa azungumzie hati hiyo, Mgongolwa alieleza kuwa upande wa utetezi hawana pingamizi la hati hiyo  idi mradi tu upande wa jamhuri usije kuwasumbua tena wateja wao.

Akitoa amri ya mahakama, Hakimu Mugeta alisema kwasababu kesi hiyo ni ya jinai na ilifunguliwa na upande wa jamhuri na upande huo wa jamhuri kupitia DPP-Dk.Feleshi amewasilisha hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea kuwashitaki washitakiwa hao, mahakama yake haina mamlaka ya kupingana na hati hiyo ya DPP  hivyo mahakama yake kwa kauli moja inatamka kuwafitia kesi hiyo ya uhujuju uchumi  washitakiwa wote hivyo kuanzia jana washitakiwa hao wapo huru.

Hata hivyo wakati hakimu huyo akitoa amri hiyo Kisena hakuwepo mahakamani hapo bila ya kutoa taarifa yoyote  na itakumbukwa kuwa Mei  20 mwaka huu, Hakimu Mugeta alitoa hati ya kukamatwa kwa Kisena ili aje aunganishwe kwenye kesi hiyo mpya Na.3/2013 iliyofunguliwa  Aprili 30 mwaka huu, ambapo Kisena aliongezwa katika kesi hiyo na kufanya idadi ya washitakiwa kuwa wanne kwani Mei 28 mwaka jana wakati kesi hiyo ilipofunguliwa rasmi washitakiwa walikuwa ni watatu tu yaani Simba, Mwaking’inda na Milanzi.

Mei 20 mwaka huu, kesi hiyo ilikuja kwaajili ya kuwasomea maelezo ya awali washitakiwa lakini ilishindikana kwasababu Kisena hakuwa amefika mahakamani licha ya Aprili 30 mwaka huu, aliunganishwa katika kesi hiyo ya jinai, hali iliyosababisha siku hiyo ya Mei 20 mwaka huu, wakili wa serikali Mbagwa kuiomba hati ya kukamatwa kwa Kisena na mawakili wa utetezi nao kugeuka mbogo na kuungana na upande wa jamhuri kutaka Kisena akamatwe aje aunganishwe na kesi hiyo ili washitakiwa wote kwa pamoja waweze kusomewa maelezo ya awali kwani wanaamini serikali inafahamu Kisena anapoishi na anapofanyia shughuli zake, hoja ambayo ilikubaliwa na hakimu Mugeta ambaye alitoa amri ya kukamatwa kwa Kisena na siku hiyi hakimu Mugeta aliarisha kesi hiyo hadi Juni 4 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwaajili ya washitakiwa kusomewa maelezo ya awali.

Mwandishi wa habari hii ambaye ameifuatilia kesi hii tangu ilipofunguliwa kwa mara ya kwanza mahakamani hapo hapo

Mei 29 mwaka jana hadi jana kesi hiyo imefikia tamati,Juni 4 mwaka huu kesi hiyo ilipokuja kwaajili ya kusomewa maelezo ya awali lakini pia ,washitakiwa hakuweza kusomewa kwasabababu hakimu Mugeta alikuwa nje ya ofisi kikazi, Kisena hakufika mahakamani na kesi hiyo iliarishwa hadi jana ilipokuja kwaajili ya washitakiwa kusomewa maelezo ya awali na maelezo hayo ya awali hayakuweza kusomewa kwasababu DPP aliwasilisha hati ya kuwafutia kesi washitakiwa hao kwasababu hana haja ya kuendelea kuwashitaki , pia Kisena hakuwa amekamatwa na wanausalama kama amri ya mahakama ilivyokuwa imeelekeza na wala hakuwepo mahakamani hapo.

 Akizungumzia uamuzi huo wa DPP-Dk.Feleshi wa kuwafutia kesi wateja wake, nje ya viwanja vya mahakama hiyo,  Wakili Mgongolwa alisema anapongeza uamuzi huo wa DPP kwani ni uamuzi mzuri na pia ni matumizi mazuri ya sheria pale tu DPP anapoona  hana mashahidi thabiti wa kuja kujenga kesi yake atumie kifungu hicho kufuta kesi kwani DPP kuendelea kuwa na kesi za jinai mahakamani ambazo anaona kabisa hana mashahdi thabiti wa kuwaleta mahakamani kuja kujenga kesi yake ,hayo ndiyo matumuzi mabaya ya sheria kwani pia hali hiyo itaisababishia serikali gharama za kuwaleta mashahidi na kuongeza mrundikano wa mashauri mahakamani.

‘Minampongeza Dk.Feleshi kwa uamuzi wake huu wa kuwafutia wateja wetu kesi hii ambayo ilikuwa ikifuatiliwa na umma wa watanzania wengi…..DPP ametumia sheria vizuri tena kwa maslahi ya taifa hili kwa kuamua kuifuta kesi hii na ninamshauri pia pale DPP anapoona kuna mashauri mengine ambayo hana hajaya kuendelea nayo pia atumie kifungu hicho kuzifuta ‘alisema wakili Mgongolwa.

Aprili 30 mwaka huu, upande wa jamhuri uliifuta kesi ya awali  ya matumuzi mabaya ya madaraka iliyokuwa ikimkabili Simba na wenzake wawili na kisha kufungua kesi mpya yenye mashitaka sita yakiwemo mashitaka ya rushwa na uhujumu uchumi  na kisha kumuunganisha Kisena katika kesi hiyo ambapo katika kesi ya awali iliyofutwa Kisena alikuwa ni shahidi wa upande wa jamhuri na hivyo kufanya kesi hiyo ya makosa ya rushwa, uhujumu uchumi kuwa na jumla ya washitakiwa wa nne hivi sasa.  

Wakili Mwandamizi wa Serikali Oswalid Tibabyekomya akiwasomea upya mashitaka yao katika kesi hiyo mpya Na.3/2013 alidai washitakiwa wanakabiliwa na  makosa ya rushwa,uhujumu uchumi,matumizi mabaya ya madaraka na kulisababishia shirika hilo hasara ya Sh. Bilioni 8.4. Na kwamba Tibabyekomya alieleza kuwa baada ya kuyachambua makosa hayo wamebaini kuwa yanaangukia katika Sheria ya Uhujumu Uchumi

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka ya kesi mpya , shtaka la kwanza la kula njama linawahusu Simba na Milanzi na Kisena.

Washtakiwa hao wanadaiwa kuwa kati ya Septemba 2009 na Januari 2010, jijini Dar es Salaam, kwa pamoja walikula njama za kutenda kosa la vitendo vya rushwa, kinyume cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa.

Kwa mujibu wa hati hiyo ya mashtaka, shtaka la pili la vitendo vya rushwa linamhusu Kisena peke yake, hata hivyo shtaka hilo halikusomwa kutokana na mshtakiwa huyo kutokuwapo mahakamani.

Shtaka la tatu ni la vitendo vya rushwa ambalo linawahusu Simba na Milanzi. Wakili Mbagwa alidai kuwa kati ya Septemba 2009 na Januari 2010, walikubali kupokea  Sh. Milioni 320 milioni kutoka kwa Kisena ushawishi wa kuiuzia Simon Group hisa za UDA ambazo zilikuwa bado hazijagawiwa.Katika shtaka la nne ambalo ni la matumizi mabaya ya madaraka, linawahusu Simba , Mwaking’inda na Milanzi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Juni 20 mwaka 2013.