Header Ads

WAZEE WA BARAZA WAMTETEA ZOMBE

*Waiambia korti hana hatia
*Wengine ushahidi wawabana
*Sasa yasubiriwa hukumu

Na Happiness Katabazi

WAZEE wa Baraza katika kesi ya mauaji ya wafanyabishara watatu na dereva taksi mmoja inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam, ACP Abdallah Zombe na wenzake nane, wameiomba Mahakama Kuu imwachie huru Zombe kwa kuwa hana hatia.


Wazee hao wa baraza, Magreth Mossi na Nicolus Kimolo, walitoa kauli hizo jana alipokuwa wakitoa maoni yao kulingana na ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo na pande zote mbili.

Mbali na kuomba Zombe kuachiwa huru wazee hao pia wameimba mahakama kumwachia huru mshitakiwa mwinigine katika kesi hiyo, Festus Gwasabi (mshitakiwa wa 13) kwa maelezo kuwa ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo dhidi ya washitakiwa hao haukuweza kudhibitisha kuhusika na mauaji hayo.

Kabla ya wazee hao kutoa maoni hayo jana, Jaji wa Mahakam ya Rufani, Salum Massati, anayesikiliza kesi hiyo juzi aliwatahadharisha kutoa maoni yao kwa kutozingatia yaliyoandikwa katika vyombo vya habari kwani yameandikwa mengi kuhusiana na kesi hiyo.

Hata hivyo, katika kutoa hukumu ya kesi hiyo, Jaji anaweza kuzingatia au kutozingatia maoni ya wazee hao.

Mzee wa baraza aliyeanza kutoa maoni yake ni Kimolo ambaye alieleza kuwa kulingana na ushahidi wa upande wa mashitaka, hakuna shahidi aliyedhibitisha kwamba Zombe alishiriki katika mauaji hayo na pia hakuna shahidi aliyethibitisha alimuona Zombe kwenye eneo la tukio.

Mzee wa Baraza Kimolo ndiye aliyaanza kutoa maoni na mapendekezo yake kuhusu mshitakiwa wa kwanza(Zombe), alikumbusha upande wa mashitaka ulileta mashahidi 37 na hakuna udhibitisho kwamba mshitakiwa huyo alishiriki katika mauji hao na kwamba hakuna shahidi hata mmoja aliyeweza kusema wala kuthibitisha kwamba walimuona Zombe kwenye eneo la tukio.

Kimolo alidai kuhusu hoja iliyotolewa na upande wa mashitaka kwamba Zombe alikwenda kituo cha Polisi Urafiki, yeye ameona mshitakiwa huyo alikwenda kutatua utata wa fedha na alitoa amri kwamba kielelezo hicho kitimie na kuongeza hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Zombe aende kituoni hapo.

Kuhusu hoja ya mashitaka kwamba Zombe aliwapa mkono wa pongezi askari kuwa alikuwa anajua kilichokuwa kinaendelea kwani asingeweza kutoa pongezi kwa baadhi ya askari; alidai kwa maoni yake Zombe alikuwa hajui chochote kilichokuwa kinaendelea.

Alikumbusha kuwa mahakama hiyo ilielezwa na mshitakiwa wa 12,Rajabu Bakari jinsi walivyofundishwa na Zombe kujibu maswali kwenye Tume ya ACP-Mgawe na Jaji Mussa Kipenka, pia aliendelea kueleza kuwa mshitakiwa wa kwanza aliwapa vikaratasi vya kujitetea lakini Rajabu wakati akijitetea alidai hata hayo aliyofundishwa kujitetea hayakumsaidia na hata alipotakiwa na mahakama atoe hivyo vikaratasi alishindwa kuwasilisha mahakamani vikaratasi hivyo.

“Maoni yangu katika hilo hilo , kushindwa kwa Rajabu kuwasilisha vikaratasi hivyo hayana ukweli” alidai Kimolo huku akionyesha kujiamini.

Akichambua ushahidi wa shahidi wa 36 wa upande wa mashitaka,Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Sidney Mkumbi ambaye ndiye alikuwa Mpelelezi Mkuu wa kesi hiyo, alikiri mbele ya mahakama hiyo kuwa Zombe akuandika maeleszo ,pia alieleza mahakama kuwa mshitakiwa wa kwanza ameunganishwa tu kwenye kesi hiyo kutokana na maelezo ya nyongeza yaliyotoka kwa washitakiwa wenzake.

“Baada ya washitakiwa wote kupewa haki yao ya msingi ya kujitetea katika mahakama hii tukufu,hatukuweza kusikia hayo maelezo ya nyongeza yaliyofanya Zombe aunganishwe kwenye kesi hii.

“Jaji ili mahakama yako iweze kumtia hatiani kwa kosa kubwa kama hili mauji nilazima upande wa mashitaka uthibitishe bila kuacha shaka yoyote kesi yake.Hivyo basi upande wa mashitaka katika kesi hii umeshindwa kuthibitisha mashitaka manne ya mauji kwa Zombe kwa sababu zifuatazo:alidai Kimolo.

Sababu ya kwanza alieleza kuwa hakuna shahidi hata mmoja katika mashahidi 37 aliyedai Zombe kuwa alihusika.Pili, Tume zote zilizoundwa,hazikupendekeza mshitakiwa huyo wa kwanza ashitakiwa.Tatu, mpelelezi Mkuu wa kesi hiyo, SACP- Mkumbi naye alithibitisha kwamba Zombe aliunganishwa katika kesi hiyo kwa maelezo ya nyongezo yaliyotolewa na washitakiwa wenzake.

“Kwa maoni na mapendekezo yangu, naiomba mahakama hii imuone Zombe hana hatia kwa makosa ya mauji aliyoshitakiwa nayo” alidai Kimolo.

Kwa upande wake Magreth Mossi, akitoa maoni na mapendekezo yake kuhusu Zombe,alieleza kuwa ni ukweli usiopingika mashahidi wote wa upande wa mashitaka ,hakuna shahidi aliyeweza kuthibitisha shitaka hili kuhusu mshitakiwa huyo.

“Jaji, kuanzia kukamatwa kwa marehemu na hadi walipofikwa na umauti wao hata shahidi mmoja hakuweza kumnyoshea kidole Zombe kuwa alikuwepo eneo la tukio.Mahakama hii ilipokea ushahidi wa jinsi mshitakiwa huyo alivyokuwa akitoa taarifa alizokuwa amezipata kutoka kwa askari wake waliokuwa eneo la tukio” alidai Mossi.

Kuhusu hoja ya Zombe aliwapongeza askari kwamba ilionyesha alikuwa akifahamu tukio hilo, alidai ukweli usiopingika kiongozi yoyote anapoona askari wake wamefanyakazi ya ushupavu sio vibaya kutoa mkono wa pongezi,kwani alipata taarifa askari wake walikamata majambazi na silaha waliopora roli la kampuni ya Bidco.

“Naona hicho ndicho kilimfanya Zombe kutoa mkono wa pongezi na tume zote mbili zilioundwa , hazikumuona mshitakiwa huyo ana kesi ya mauji hivyo naungana na mzee wa baraza mwenzangu, kuiomba mahakama hii tukufu umuone mshitakiwa wa kwanza hana hatia” alidai Mosi, na kusababisha Zombe awe anajifuta machozi mara kwa mara kizimbani.

Kuhusu mshitakiwa 13, Festus Gwasabi, wazee hao wote kwa pamoja waliomba mahakama imuone hana hatia kwani ushahidi umeonyesha alishiriki katika upekuzi wa kwa marehemu wakati wakiwa hai Sinza Palestina, na baada ya zoezi hilo alipewa amri na mkubwa wake aendeshe gari la marehemu hao ambapo alipanda gari hilo na aliyekuwa mshitakiwa sita, Moris Nyangerela ambaye aliachiliwa huru na kulipeleka gari hilo kituo cha Urafiki.

Aidha walidai haya Gwasabi wakati akijitetea alikubali kushiriki kukamata na kuwapekua marehemu lakini aliamuriwa na mkuu wake apelike gari hilo Urafiki na mshitakiwa huyo alimleta shahidi wake, Nyangerela ambaye alikuja kudhibitisha hayo.

Hivyo wakaiomba mahakama hiyo itumie kifungu kile kile ilichokitumia kumwachia Nyangerela pia kitumike kumwachia Gwasabi na hivyo maoni na mapendekezo yao kwa mshitakiwa huyo wanaomba mahakama imwone hana hatia.

Wazee hao wakitoa maoni na mapendekezo yao dhidi ya mshitakiwa wa pili,SP-Christopher Bageni, wote kwa kauli moja wanakubaliana na upande wa mashitaka kwamba umeweza kudhibitisha kesi dhidi ya mshitakiwa na wakaiomba mahakama imuone ana hatia ya makosa anayoshitakiwa kwakuwa, ushahidi wa mazingira unaoyesha alitenda kosa hilo.

Kuhusu mshitakiwa tatu,SP- Ahmed Makelle, wazee hao kwa kauli moja waliomba mahakama imwone ana hatia kwasababu mashahidi wa upande wa mashitaka walimtambua mshitakiwa huyo alifika eneo la tukio na wakati mshitakiwa akijitetea alikiri kufika eneo la tukio na kwamba mashahidi hao walieleza walimtambua baada ya Makelle kuwa anagombea fuko la fedha.

Aidha wakitoa maoni yao kuhusu mshitakiwa wa tano, Jane Andrew,wazee hao pia waliomba atiwe hatiani kwani wanakubaliana na mashahidi wa upande wa mashitaka kwamba walimtambua kuwa ndiye aliyefika Sinza Palestina na alikuwa akigombea mfuko wa fedha.

Lakini katika hali isiyo tarajiwa na wengi, wakati wazee hao wa baraza walipomaliza kutoa maoni yao dhidi ya Mabula, Bageni, Makelle na Jane walikuwa wakiangua vicheko kizimbani.

Kuhusu mshitakiwa wa saba,Emmanuel Mabula, wazee hao pia walikubaliana na upande wa mshitaka kuwa umeweza kudhibitisha kesi kwa mshitakiwa huyo, kwani hakuna hata shahidi aliweza kuiambia mahakama siku ya tukio mshitakiwa huyo alipangiwa doria eneo la Makongo Juu.

“Mshitakiwa mwenyewe(Mabula) aliambia mahakama kuwa alikuwa ni miongoni mwa askari walioenda kupewa mkono wa pongenzi wa RCO-Zombe, huku akijua kuwa hakuwa hakuwa katika mapambano na majambazi lakini akakubali pongezi hizo, sisi tunasema aliku na lake jambo alilokuwa akilificha hivyo tunaomba hatiwe hatiani” alidai.

Wazee hao ambao walionyesha kujiamini wakati wakitoa mapendekezo yao, wakitoa maoni yao dhidi ya mshitakiwa tisa, Michael Shonza, walisema maoni yao kwa mshitakiwa hayo yanafanana na maoni waliyoyatoa kwa mshitakiwa saba, kwani siku ya tukio Mabula na Shonza walikuwa pamoja, hivyo wanameomba naye atiwe hatiani.

Aidha kuhusu mshitakiwa kumi, Koplo Abeneth Salo, wazee hao walisema baadhi ya mashahidi wa mashitaka walimtambua japo kuwa Januari 16/1/2006 Sinza Palestina alivalia nguo za kiraia na siku hiyo walimuona akiwa amekaa kwenye gari la mshitakiwa tatu(Makelle) ila mashahidi hao walimwona Jane na Makelle pale Sinza Palestina ila Abeneth alkuwa ndani ya gari.

Walikumbusha kuwa mshitakiwa 12(Rajabu) alieleza mshitakiwa tano(Jane) na Abeneth wote walifika barabara ya Samunujoma kwenye roli la Bidco, vile vile alimshuhudia Jane na Abeneth wakiondoka pamoja na gari la Makelle, na aliendelea kufahamisha mahakama kuwa gari hilo ndiyo lilikuwa la kwanza kuondoka .

Walisema Abeneth alipopewa haki ya kujitetea alidai yeye alishushwa Ubungo Terminal kwaajili ya kuendelea na doria na wala hakuweza kuleta shahidi ili adhibitishe madai hayo, hivyo walidai kushindwa kwa mshitakiwa huyo kufanya hivyo wanakubaliana na upande wa mashitaka kwamba wameweza kuthibitisha kesi dhidi yake na wakaiomba mahakama imwone ana hatia.

Aidha wazee hao wakichambua ushahidi wa mshitakiwa wa 12,Rajabu Bakari, walisema kwa hiari yake mwenye bila kulazimishwa na mtu yoyote ,mshitakiwa huyo akiwa ana akili timamu alikiri kuwa alikuwepo eneo la mauji msitu wa Pande na kwamba alipopewa haki ya kujitetea,mshitakiwa huyo alidai alikuwa chini ya amri ndiyo maana alikwenda katika msitu huo.

“Jaji huyu ni askari polisi na moja ya kazi ya majukumu yake ni kulinda usalama wa raia na mali zake,hivi kweli bosi wake anampa amri ya kuwa watu wasiyo na hatia, akanyamaza kimya?Mtukufu jaji huyu mshitakiwa anahusika moja kwa moja na tukio hili la mauji na tunaomba atiwe hatiani”alidai Magreth Mossi.

Baada ya wazee hao kuitimisha kutoa maoni na mapendekezo yao , Jaji wa Mahakama ya Rufani, Salum Massati, huo ndiyo mwisho wa kesi hiyo na kwamba hukumu ataitoa kutokana tarehe itakayopangwa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Mbali na Zombe, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni SP Christopher Bageni, SP Ahmed Makelle, Jane Andrew, Emmanuel Mabula, Michael Shonza, Koplo Abeneth Saro, Rajabu Bakari na Festus Gwasabi.

Zombe na wenzake, wanadaiwa kufanya mauaji hayo Januari 14 mwaka 2006, eneo la Mbezi Luis, katika msitu wa Pande, ambapo waliwaua Ephraim Chigumbi, Sabinus Chigumbi na Mathias Lukombe, ambao ni wafanyabiashara wa madini kutoka Mahenge, Ulanga na Juma Ndugu, ambaye ni dereva teksi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Juni 27 ,2009

No comments:

Powered by Blogger.