Header Ads

JEETU AGONGA MWAMBA KORTINI

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, imekataa kutoa uamuzi wa kumruhusu au kutomruhusu mshitakiwa wa kwanza katika kesi ya wizi wa sh bilioni 2.5 za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania BoT), Jayantkumar Chandubhai Patel, maarufu Jeetu Patel, kwenda nchini India kwa ajili ya matibabu ya ugonjwa wa moyo.

Uamuzi huo ulitolewa jana na kiongozi wa jopo la mahakimu wakazi, Rwaichi Meela, anayesaidiana na Msajili wa Mahakama Kuu Kitengo cha Biashara, John Kayohza na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi, Grace Mwakipesile, ambaye alisema licha ya jana kesi hiyo kuja kwa ajili ya kutolewa uamuzi wa ombi hilo la mshitakiwa, wameona ni muhimu, ila linahitaji umakini.

Meela alisema mahakama hiyo ni chombo cha serikali, hivyo haiwezi kupokea taarifa za ugonjwa wa mshitakiwa kutoka hospitali binafsi, na kumtaka kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na kuonana na mtaalamu wa ugonjwa huo, ambaye atamchunguza na kuandika ripoti, kisha kupelekwa mahakamani hapo.

“Ombi la mshitakiwa tumelichukulia kuwa ni muhimu, ila jopo hili leo (jana) haliwezi kupokea taarifa za ugonjwa wake kutoka hospitali binafsi, hivyo tunamwamuru mshitakiwa aende Muhimbili na kuonana na mtaalamu wa ugonjwa unaomsumbua, ili naye aandike ripoti yake kisha iletwe mahakamani, ndipo sisi tutakapotoa uamuzi kuhusu ombi lake,” alisema Meela.

Baada ya kueleza hayo, Meela aliahirisha kesi hadi Aprili 28, itakapotajwa.
Jumatano wiki hii, Wakili Mabere Marando anayemtetea mshitakiwa huyo, aliwasilisha ombi hilo akidai mteja wake anasumbuliwa na maradhi ya moyo, na amekuwa akitibiwa katika Hospitali ya Hindu Mandal.

Marando alidai hospitali hiyo imeandika taarifa mbili za uchunguzi wa ugonjwa unaomsumbua mteja wake, na kupendekeza akatibiwe nchini India, kwani hospitali hiyo haina uwezo wa kumtibu.

Marando alidai licha mteja wake kukabiliwa na kesi nne mahakamani hapo, anaomba aruhusiwe kwenda India kuanzia Aprili 20 hadi Mei 14, kwa ajili ya matibabu.

Mbali na Jeetu Patel, washitakiwa wengine katika kesi hiyo namba 1154/2008 ni Devendra Patel na Amit Nandy, ambao wote wanatetewa na mawakili wa kujitegemea; Marando, Joseph Tadayo na Martin Matunda.

Novemba 16, mwaka jana, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, washtakiwa wote kwa pamoja bila ya halali yoyote, walitumia kampuni yao ya Nobel Azania Investment Ltd kuonyesha kuwa kampuni ya nje ya Bencon Investment, imewapatia idhini ya kurithi deni lake la sh bilioni 2.5.

Wakati huo huo, shahidi wa tisa katika kesi ya wizi wa sh milioni 207 za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) inayomkabili Rajabu Maranda na maofisa wa BoT, Iman Mwakosya, Ester Komu na Bosco Kimela, jana alishindwa kuanza kutoa ushahidi wake baada ya upande wa mashitaka kubadilisha hati ya mashitaka na kumuongeza mshitakiwa Farijala Hussein.

Hussein ambaye kwa sasa atakuwa anakabiliana na kesi nne za EPA mahakamani hapo, aliunganishwa jana baada ya upande wa mashitaka uliokuwa ukiongozwa na Wakili wa Serikali, Vitalis Timon, kuwasilisha ombi la kubadilisha hati na kumsomea mashitaka sita, likiwamo shitaka la kula njama, wizi na kujipatia ingizo isivyo halali.

Jopo la mahakimu wakazi, lililokuwa likiongozwa na Hakimu Mkuu Mfawidhi, Addy Lyamuya na Kitusi, waliahirisha kesi hiyo hadi Jumatatu asubuhi ambapo siku hiyo washitakiwa watasomewa maelezo ya awali.

Mshitakiwa alidhaminiwa baada ya kuwasilisha hati yenye thamani ya sh milioni 20.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, April 18,2009

No comments:

Powered by Blogger.