Header Ads

MWAKALUKWA:NILIHISI KIASI KILICHOTOZWA NI KIKUBWA

Na Happiness Katabazi

ALIYEKUWA Kamishna wa Madini katika Wizara ya Nishati na Madini, Gray Mwakalukwa (58), ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kuwa alihisi kiasi cha ada asilimia 1.9 kilichotozwa na Kampuni ya Alex Stewart Government Business Corporation kwa serikali ni kikubwa.


Mwakalukwa ambaye ni shahidi wa tano alieleza hayo jana baada ya kubanwa maswali na mawakili wa utetezi, Hurbet Nyange, Peter Swai, Profesa Leonard Shahidi na Elisa Elia, ambao wanamtetea aliyekuwa Waziri wa Fedha wa zamani, Basil Mramba, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja, mbele ya jopo la mahakimu wakazi, John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela.

Mwakalukwa ambaye sasa ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) baada ya kusema hayo, wakili wa utetezi Peter Swai, alimtaka shahidi huyo atoe vielelezo vya kiasi cha gharama zinazotozwa na makampuni ya ukaguzi wa dhahabu katika nchini nyingine, lakini hata hivyo shahidi huyo aliiambia mahakama kuwa hana ulinganisho wa nchi nyingine, hali iliyosababisha watu waliohudhuria kesi hiyo kuangua vicheko.

“Wakati huo mimi nilikuwa kamishna wa madini pale wizarani, kiasi hicho kweli nilihisi ni kikubwa, licha ya kuwa sikuwa nimefanya utafiti katika nchi nyingine, lakini kiasi hicho kiliwekwa kwenye mkataba na mimi sikuhusika kuandaa mkataba, hivyo sijui chochote kuhusu mkataba huo ila baada ya BoT kwa niaba ya serikali kuingia kwenye mkataba na kampuni hiyo na kusainiwa Julai 2003, uliletwa kwangu kama sheria ya madini inavyotaka.

“Baada ya kuona, niliteua mtu akafanye ukaguzi kwenye migodi kwa niaba yangu (Kamishna wa Madini) na kampuni hiyo ya ukaguzi wa madini ilikwenda kufanya kazi hiyo na sijahusika kuandaa kipengele cha ada ya ukaguzi wa dhahabu kilichowekwa kwenye mkataba huo wala kuandika barua ya kuiombea msamaha wa kodi kampuni hiyo, kwakuwa yeye alikuwa akishughulika na utoaji wa msamaha wa mirahaba wa makampuni ya madini,” alidai Mwakalukwa.

Alisema yeye akiwa kamishna wa madini, alitoa ushauri mapema kwa Yona kabla ya mkataba huo kusainiwa na alitoa ushauri huo kwa maandishi, aliangalia maeneo matatu, ambapo aliangalia kampuni hiyo baada ya kuingia mkataba na serikali itaingiaje kwenye migodi au serikali itatumia sheria ya madini au ya ukaguzi kutoa mapendekezo ya tozo kwa kampuni hiyo na alishauri hayo malipo yalipwe na kampuni ya madini au serikali.

Kiongozi wa Jopo la mahakimu wakazi, John Utamwa, aliahirisha kesi hiyo hadi kesho ambapo shahidi wa sita ataanza kutoa ushahidi wake.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Machi 18 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.