Header Ads

KORTI YAMTAKA ZOMBE KUMJIBU AG KWA MAANDISHI

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imemwamuru aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Abdallah Zombe kujibu kwa maandishi hoja za Mwanasheria wa Serikali (AG) ifikapo Mei 23 mwaka huu.


Amri hiyo ilitolewa jana na Jaji Upendo Msuya wakati kesi hiyo namba 35/2011 ya madai ya fidia ya sh bilioni tano iliyofunguliwa na Zombe dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ilipofika kwa mara ya kwanza kwa ajili ya kutajwa.

Katika kesi hiyo Zombe anawakilishwa na wakili wa kujitegemea Nyaronyo Kichere wakati upande wa mdaiwa haukuwa na mwakilishi.

“Kesi hii ilikuja leo kwa ajili ya kutajwa hivyo upande wa mdaiwa ulishawapatia majibu ya hati yenu ya madai, hivyo mahakama inauamuru upande wa mlalamikaji kujibu na kuyaleta majibu yenu Mei 23 na kesi hii itakuja kutajwa tena Juni 20 mwaka huu,” alisema Jaji Upendo.

Hati ya majibu ya mwanasheria mkuu inadai kwamba Zombe hana anachomdai kwa sababu Oktoba 7, 2009 Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) aliwasilisha rufaa katika Mahakama ya Rufani kupinga hukumu ya Mahakama Kuu ya Agosti 17 mwaka 2009 ambayo ilimwachia huru Zombe na wenzake nane waliotuhumiwa kwa mauji na kwamba rufaa hiyo bado haijatolewa maamuzi.

Machi 18 mwaka huu, Zombe alifungua kesi hiyo mahakamani hapo akiomba mdaiwa amlipe sh bilioni tano na riba ya sh milioni 200 kwa sababu polisi ilikiuka sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 wakati wanamkamata.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Mei 17 mwaka 2011.

No comments:

Powered by Blogger.