Header Ads

RAIS ANZA KUREJESHA NYUMBA YAKO SERIKALINI

Na Happiness Katabazi

UADILIFU wa serikali hautokani na hotuba nzuri za viongozi bali vitendo ambavyo viongozi hao wamevifanya na vinaonekana kwa wananchi.

Hapa nchini, ipo kanuni ya maadili ya viongozi inayosema uongozi ni dhamana.

Maana halisi ya kanuni hii ni kwamba, uongozi si mali ya mtu, wala nchi hii si mali ya kiongozi, bali vyote viwili ni mali ya wananchi.

Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), hasa Serikali ya Awamu ya Tatu na Awamu ya Nne, imeshindwa kutafsiri kanuni hii kwa kivitendo, badala yake viongozi wa CCM wanaamini kwamba uongozi wa nchi ni mali yao, na hakuna binadamu mwingine anayestahili kuupata. Pia nchi hii ni mali yao na wanaweza kufanya watakavyo.

Wanaweza kuuza mali ya serikali na kuuza nchi yenyewe bila kuulizwa na mtu. Aina hii ya mtazamo tumeiona katika uamuzi wa kuuza nyumba za serikali.

Jambo hili limepigiwa kelele sana na watu wenye heshima na maadili mema, wakisema mtumishi wa umma, hawezi kuchukua nyumba ya mwajiri wake na kuifanya yake au hata kuiuza.

Kitendo cha viongozi wa serikali ya CCM kujigawia nyumba za serikali ni aina nyingine ya ufisadi.

Nyumba zile zilianza kujengwa wakati wa mkoloni, zikaongezewa na uongozi wa Awamu ya Kwanza wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Awamu ya Pili.

Haikumithilika kamwe katika awamu hizo mtu kujiuzia nyumba za serikali, lakini, Rais mstaafu Benjamin Mkapa, tuliyeambiwa kuwa ni ‘Bwana Msafi’, ndiye aliyekuwa wa kwanza kuvunja mwiko huo.

Alijichukulia nyumba iliyopo pale Sea View, Upanga na kisha akawaruhusu wenzake wachukue nyumba walizokuwa wanakaa.

Mawaziri, makatibu wakuu, majaji na wakurugenzi, kila mmoja kwa nafasi yake alitafuta nyumba na kuinunua. Nyumba nyingine zilikarabatiwa kwa mamilioni ya fedha za walipa kodi na kisha zikauzwa kwa bei chee.

Je, ni halali nyumba ikarabatiwe kwa sh milioni 300 halafu ije kuuzwa kwa mtumishi wa serikali kwa milioni 30 au 40, tena fedha zenyewe anazilipa kwa awamu?

Kichekesho zaidi ni pale familia nzima, yaani baba, mama na watoto wawili eti kwa vile wote wanafanya kazi serikalini, kila mmoja amenunua nyumba ya serikali. Huu kama si ufisadi ni nini?

Jambo hili lilifanyika kwa usiri mkubwa bila kupata idhini ya Bunge. Tunashangaa hadi sasa hakuna hoja iliyowasilishwa bungeni kujadili ufisadi huu.

Tuelezane ukweli kwamba nyumba za serikali zimejengwa kwa kodi ya wananchi. Si halali watumishi wa serikali kugawana nyumba hizo kwa madai kuwa eti wameuziwa. Huo ni wizi.

Rais Jakaya Kikwete aliiga kampeni za washindani wake wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 kwamba endapo ataingia Ikulu, atazirejesha nyumba hizo.

Mara baada ya kuchaguliwa, Kikwete alilitangazia taifa kuwa yeye amekubali kuuziwa nyumba ya serikali baada ya kulazimishwa, lakini alilaani mpango mzima wa kuuza nyumba za serikali, kwamba ulikuwa mbovu.

Kwa kukubali kuchukua nyumba ya serikali, rais naye alishiriki kwenye dhambi hiyo, akawa mmoja wa waliozawadiwa nyumba hizo.

Rais aonyeshe mfano, aanze kwanza kurejesha serikalini nyumba yake ili wengine wafuate. Watanzania wamechoka kuwalipia viongozi na watendaji wa serikali mabilioni ya fedha kwa kuishi mahotelini, kwani wapo wanaolipiwa sh 300,000 kwa siku kwa kukaa hotelini baada ya serikali kukosa nyumba ya kuwaweka..

Hivi huo ubadhirifu wa kodi ya wananchi utaisha lini? Je, ni lini umaskini tutaupiga vita?

Mara ya mwisho wakati akiadhimisha miaka miwili ya kuwa Ikulu, Rais Kikwete alisema, serikali bado inaendelea na utafiti wa jinsi ya kurejesha nyumba hizo. Napenda kumuuliza, lini utafiti huo utakwisha na lini kazi ya kuanza kurejesha nyumba hizo itaanza?

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika

Simu: 0755 312859.
katabazihappy@yahoo.com;www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Machi 12 mwaka 2008

3 comments:

Anonymous said...

Happy,
Ahsante kwa makala hii inayothibitisha kuwa u miongoni mwa watanzania ambao hatujasahau kiini macho hicho.
Ati wanafanya utafiti! Yamkini kabla ya kugawana walifanya utafiti pia na kugundua kwamba hata wangefanya ufisadi wa kiwango gani, Tanzania ni nchi ya amani

Simon Kitururu said...

Maswala ya kulia serikalini kiujanja ujanja haya ,inabidi yaishe.Mungu Ibariki Tanzania lakini tuondolee Mafisadi!

Adam said...

Dear Happy, Tusife moyo kuyasema tunayoona yanaitafuna au yataitafuna nchi yetu. Ulichokisema sasa kinatukia, Alyce kimaro kafanya kweli (hata kama wanafanya maigizo)mambo hayatakuwa yale yale. Ujumbe umefika, wananchi kupitia wabunge wao, wamepaza sauti zao. Kama serikali ya mpendwa wetu JK itaendelea kushupaza shingo, shauri yake.

Kuhusu JK kukubali nyumba kwa kushurutishwa hizo zilikuwa siasa tu. Alishiriki kikamilifu kama mmoja wa mawaziri katika baraza la mkapa, katika kuukamilisha mpango huo. ALILAZIMISHWA NA NANI? HAKUNA KITU KAMA HICHO.

Hata hivyo, muungwana siku zote hukiri kosa. Akikiri leo kwamba alifanya madhambi, au walau alishiriki madhambi, na awe wa kwanza kurejesha nyumba aliyokwapua, kisha awabane wenzake. Utafiti au uchunguzi, unaolenga kuwabainisha mbuzi chache wa kafara hausaidii sana.

SONGA MBELE HAPPY. MAPAMBANO NDIYO KWANZA YAMEANZA.

Mungu ibariki Tanzania.

Mwl Adam

Powered by Blogger.