Header Ads

MSAFARA WA JK KUPIGWA MAWE:TUMEVUNA TULICHOPANDA

Na Happiness Katabazi
WIKI iliyopita vyombo vya habari vya hapa nchini viliripoti habari kwamba msafara wa Rais Jakaya Kikwete umepigwa mawe katika kijiji cha Kange wilayani Chunya mkoani Mbeya, ambapo rais alikuwa na ziara ya kikazi mkoani humo.

Hakuna sababu ya kulionea haya tukio hili la msafara wa rais Kikwete kupigwa mawe kwasababu mficha uchi azai.

Hivi sasa Tanzania inavuna ilichopanda.Kuna namna tatu ya kuliangalia tukio hili.Ulipopigwa mawe mkutano wa chama cha CHAUSTA kule Tarime Agosti 29 mwaka huu, hakuna mtu aliyepoga kelele kwasababu mkutano wa chama hicho ni sawa na kifaranga na wala haikuonekana ni ishara mbaya kwa nchi.

Hakuna mtu aliyepiga kelele mkutano wa NCCR-Mageuzi uliofanyika Agosti 31 mwaka huu, huko Tarime kwasababu waliona NCCR-Mageuzi ni kitu gani.

Siku chache baada ya mkutano wa NCCR kupigwa mawe aliyekuwa wakwanza kujibu ni Dk.Willbroad Slaa aliyesema mwanasiasa anayefanya siasa zinzokera unampiga mawe.Hakuna aliyepiga kelele alipopigwa jiwe Mwenyekiti wa (DP) Mchungaji Christopher Mtikila.

Haya mambo wamefanyiwa watu ambao ni wanasiasa wakitekeleza wajibu wao wa kisiasa.Ukishaalalisha hayo huna sababu ya kulaani kupigwa mawe kwa msafara wa Kikwete.
Kwa sababu tumeishajijengea utamaduni wa kupigana mawe kwa kipindi kifupi.

Hiyo ni namna moja ya kuliona hilo jambo.Basi tuvune matunda haya japo ni machungu.Hivyo kukurupuka kwa Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya kwenda kukamata vijana zaidi ya 60 eti ndiyo waliorushia mawe msafara huo,inashangaza sana.

Namna ya pili ya kuliona hilo jambo,ni utendaji kazi wa rais Kikwete na serikali anayoingoza ambayo utendaji wake unakatisha tamaa na kuwakosesha matumaini wananchi kwakuwa inaonekana wazi rais ana huruma na mafisadi lakini hana huruma na wannachi wake wema wanaogelelea kwenye lindi la umaskini.

Rais na serikali yake imekaa kitako na kujadiliana na mafisadi walioiba fedha za EPA, hata fisadi mmoja hadi leo hii ajatajwa kwa hiyo hawa mafisadi ni waheshimiwa.Kwa kuwa rais amewakumbatia mafisadi na kuwatupa mkono raia wake, hivyo raia wake wamebakia na njia ya kufanya vitendo vya kupiga mawe viongozi na kuwazomea.

Ipo siku tutaona watu wakijitoa muhanga wa kujilipua mabomu na hapo ndipo tutakapotambua Watanzania ni binadamu kama binadamu wengine duniani kwamba nao wanapata na kusikia njaa, mateso,wanakata tamaa na wanaweza pia kujilipua na mabomu.

Kwa hiyo cha msingi sio kukataa msafara wa rais Kikwete haujapigwa mawe, tukubali yaliyotokea na tuyatafutie ufumbuzi na yaliyotokea ni ishara ya taifa lililokata tamaa.

Maisha bora kwa kila Mtanzania yako wapi?Wale waliowavalisha wananchi T-shirt,kapero,skafu,kuwalisha pilau wananchi hivi leo wako wapi?Hao ndiyo wanaotakiwa kujibu hoja ya msafara wa rais kupigwa mawe kwa kuwa matumaini yaliyoamshwa na hizo Tshirt,kapero,skafu na pilau yamekufa.

Kama rais anataka aendelee kuwa mpendwa wa watanzania aache kutangatanga nchi za nje, apambane na umaskini unaowakabili wananchi wake ,awape Watanzania matumaini kuwa umaskini unaopindukia sasa utakomeshwa.

Aoneshe hatua za wazi wazi za kukomesha umaskini miongoni mwa watu wakawaida kwa kusimamia miradi ya uzalishaji viwandani,mashambani kwa namna ambayo kukuwa kwa uchumi na kuongezeka kwa ajira na kuongezeka kwa kipato kwa mtu wa kawaida.

Rais Kikwete asisimame na kuona walimu wanateseka akakaa kimya kwani kwenye kampeni za mwaka 2005 alipowaaidi walimu kuwa atawatatulia matatizo yao , alikuwa anaomba kura tu?

Rais Kikwete asisimame na kuona migomo ikisambaa nchi nzima ya walimu,wanafunzi, wafanyakazi wa NMB, na sasa atakuja kupata migomo ya wakulima akazani kila kitu bado kipo shwari.

Rais Kikwete asisimame na kuduwaa anapoona bomoabomoa inayofanywa na vyombo vyake vya serikali na uchukuaji wa ardhi ya wakilima na wafugaji nchini ili kuwapisha wawekezaji akazani kuwa Watanzania watakubali kuishi kama wakimbizi kwenye nchi yao.

Rais Kikwete asifikiri Watanzania wa leo ni sawa na Watanzania wa jana ambao unaweza kuwaundia tume za kuchunguza mikataba ya Richmond,EPA,madini nk.na kisha ukafukia kashfa hizo kwenye mafaili ya Ikulu usichukue hatua zozote.

Rais Kikwete anapojizungushia marafiki ambao wanatuhumiwa kuwa ni mafisadi anatazamia wananchi wamweke kwenye fungu gani?Je si kweli ndege wenye manyoya yanayofanana wanaruka pamoja?

Namna ya tatu ya kuliona jambo hili ni yale mawe yaliyorushwa kwenye msafara aliyataka mwenye rais Kikwete, kwa kuwakorofisha watu wa Mbeya.Kwa sababu mwaka 2005 watu wa Jimbo la Kyela walimkataa John Mwakipesile asiwe mbunge wao wakamchagua Dk.Harrison Mwakyembe awe mbunge wao.

Sasa kama rais aliwapenda kikwelikweli watu wa Mbeya asingemteua Mwakipesile kuwa Mkuu wa Mkoa huo kwasababu kufanya vile ni kugombanisha watu wa Mbeya .Kama anampenda Mwakipesile angemteua kwa nafasi hiyo hata zaidi ya nafasi hiyo katika mkoa mwingine.

Lazima tuwe wa kweli kwa rais wetu, kwa namna mmoja ama nyingine rais anasababisha mgogoro ndani ya mkoa huo.Hao washauri wake hawakwambii ukweli au wanamshauri vizuri anapuuza ushauri wao?.

Hivyo hili la Mbeya hatutaki maelezo ya kipumbavu kwamba waliopiga mawe msafara wa rais walikuwa walevi wa pombe, watu wa Mbeya ninavyowafahamu mimi siyo walevi kihivyo ni watu wenye hoja ambazo rais na serikali yake wanakataa kuzisikiliza.

Ieleweke wazi hatutetei matumuzi ya fujo ,silaha,umwagaji damu katika kutafuta ufumbuzi katika medani ya siasa, tunasema kwamba tulizarau mwiba sasa umetuchoma ,tusiamaki,tuanze upya kwa kuutoa mwiba,kutibu kidonda ,tuendelee.

Na kuondoa mwiba hapa ni kumuondoa Mwakipesile kwa kumuamishia mkoa mwingine na kutibu vidonda ni kuwaachilia huru vijana waliokamatwa na jeshi la polisi mkoani humo ili taifa letu liende mbele.

Mungu Tanzania,Mungu ibariki Afrika

0755 312859
katabazihappy@yahoo.com;www.katabazihappy.blogspot.com
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi,Oktoba 23 mwaka 2008

No comments:

Powered by Blogger.