Header Ads

HONGERA DK.KAHANGWA KUWA MGOMBEA URAIS WA NCCR- MAGEUZI



 *Tujikumbushe mahojiano yangu na Dk.Kahangwa ya mwaka 2009.

Na Happiness Katabazi

JANA  Chama Cha NCCR Mageuzi, kilipitisha jina la Kada wake ambaye ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk.George Kahangwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya chama hicho.

Awali ya yote naomba nitangaze maslahi yangu kwa Dk.Kahangwa.

 Dk.Kahangwa toka zamani hadi hivi sasa ni rafiki yangu,Kaka yangu kwasababu wote tunatokea Mkoa mmoja wa Kagera, Kaka yangu pia kwasababu mimi na Dk.Kahangwa na baadhi ya vijana wengine wote sisi Baba yetu mlezi ni marehemu Dk.Sengondo Mvungi ambaye  alikuwa akitulea na kutufunza pamoja mambo mbalkmbali yakiwemo siasa za kimageuzi ,sheria,kutusisitiza tujiendeleze kielimu  na mambo mengine ya kufikirisha akili  tangu mwaka 2003 hadi Dk.Mvungi anafariki Dunia Novemba 12 mwaka 2012.

Na katikati ya mwaka 2012 kaka Kahangwa alirejea nchini kutoka  masomoni  huko Ughaihuni  baada ya kutunukiwa Shahada ya Uzamili (PhD)   na hivyo kufanya tuanze kumuita Dk.George Kahangwa na siyo George Kahangwa, licha hadi sasa imekuwa ikiniwia kumuita Dk.George namuita Kaka George kwasababu tangu akiwa ajaoa,Mwalimu wa Shule ya Green Acress,Mwanafunzi wa Shahada ya Pili ya Ualimu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,nikawa nakaa nae chini ya miti eneo la UDSM tunajadili mambo ya mustakabali  wa taifa letu huku tukimsubiri Dk.Mvungi arudi ofisini kwakwe ili twende tukamuone maana Dk.Mvungi nae alikuwa ni Mhadhiri wa sheria wa UDSM.

Namfahamu vizuri Dk.Kahangwa kabla ajaoa na kuajiriwa kama Mhadhiri wa UDSM alikuwa akiishi Mwananyamala nyumba moja ha uswahili ambayo mvua ikinyesha eneo la uwanja wa nyumba ile aliyokuwa akiishi ina geuka bahari hadi alipopapata ajira UDSM na kubahatika kuoa na kupata watoto wawili na kuhama Mwananyamala kuamia nyuma za UDMS zilizopo eneo la Mwenge na kwenda nchini Ughaibuni kusoma shahada ya tatu.

Dk.Kahangwa aliporejea nchini Agosti mwaka   2013 , tulikutana nae kwa mara ya kwanza katika ofisini za iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, kwa aliyekuwa Mjumbe wa Tume hiyo,marehemu Dk.Mvungi ,na mimi bila kujua nilifika siku hiyo ofisini kwa Dk.Mvungi na tukakutana pale na kuongea mambo mengi na kufurahi pamoja.

Nilimpongeza kwa kutunukiwa shahada ya Udaktari kwani alikuwa ametima ndoto yake ya kuwa Daktari wa Elimu kama alivyowahi kunieleza katika mahojiano yangu niliyofanya nae ambayo ipo chini kama kielelezo cha aliyowahi kuyasema na mipango ambayo  ameanza kuitimiza hatua kwa hatua.

Kwa wale walioshiriki siku ya kuaga mwili wa marehemu Dk.Mvungi katika uwanja wa Karimjee, lazima walipatiwa nakala ya kitabu kidogo cha historia ya marehemu Dk.Mvungi ambacho kiliandikwa na Dk.Kahangwa kama mchango wa kumuhenzi mzee wetu Dk.Mvungi.

Dk.Kahangwa moja ya ndoto yake ni kuwa na PhD , kuwa mgombea urais wa Tanzania.

Na kupitia ndoto zake hizo tayari ndoto ya kupata PhD kaishaitimiza, ndoto ya kugombea urais kupitia NCCR imetimia kwani NCCR imeteua jina lake kuwa mgombea urais ambalo jina hilo litapelekwa UKAWA ambapo UKAWA itaketi na kupitisha jina moja la mgombea urais kati ya majina yaliyoletwa na vyama vjnavyounda umoja huo na kisha kupitisha jina moja la mgombea urais atakaye iwakirisha UKAWA.

Dk.Kahangwa ambaye yeye upenda kuniita mimi kwa jina Mpambanaji au First Lady wa Dk.Mvungi, ninavyomfahamu mimk Dk.Kahangwa ni kijana mwenye hofu ya Mungu,mpenda haki na asiyependa siasa chafu.

Dk.Kahangwa aamini katika siasa chafu, yeye anaamini msomi aliyefundwa kisomi anaweza kufanya siasa safi na kufanikiwa kuleta mageuzi ya kimaendeleo katika taifa letu.

Dk.Kahangwa ni msomi anayejiamini na asiyeteteleka katika kile anachokiamini, siyo mpenda makuu ila ni mtu ambaye moyo na fikra zake tangu nianze kufahamiana naye ni kijana ambaye anaipenda nchi yake na anayetaka kuitumikia zaidi kupitia ulingo wa siasa na tangu mapema amekuwa akifanya hivyo ushahidi huo ni nao na anatabia moja ya kutopenda kuonekanaonekana kwenye vyombo vya habari.

Ulipokuwa ukimsikia Dk.Mvungi au baadhi ya viongozi wa Chama cha NCCR - Mageuzi, wanazungumzia mfumo wa elimu nchi huku wakionyesha takwimu ,uzuri na ubaya wa mfumo wa elimu hapa nchini na hadi sasa ukisikia wanaongelea kuhusu hilo, ujue ni Dk.Kahangwa aliwaandikia andiko la kitaalamu linalohusu elimu na viongozi wakalisemee majukwaani.

Nakumbuka mwaka jana Dk.Kahangwa alikwazwa na kitu kimoja kilichotokea ndani ya chama chake akaanza kuingiwa na mawazo mabaya ambayo sitayataja hapa kwenye hii makala ,alinishirikisha nimsaifie ushauri.

Mimi nilimjibu kuwa asichukue uamuzi wowote wakati ana jazba, atulie akishatulia hasira zitaisha na atakumbuka nasaha na  mafunzo ya kwa sisi wanamageuzi,aliyokuwa akitufundisha mzee wetu Dk.Mvungi ya kuipambanaji na kwamba uamuzi ambao angeuchukua ni kama angekuwa amepuuza mafunzo tuliokuwa tukipewa nyumbani,na ofisini kwa  Dk.Mvungi mara kwa mara ya jinsi ya kufanya siasa za mageuzi nchini.

Alielewa na akaachana na mawazo yake akasonga mbele na hadi alipopata amefika.

Kukaa kwangu kote na Kaka Kahangwa kumenifundisha mambo mengi kwanza kumenifundisha elimu haimtupi mtu kwani maisha aliyokuwa nayo awali Kahangwa kabla ya kujiendeleza kielimu zaidi siyo maisha aliyonayo sasa, uvumilivu, kumcha Mungu, kupenda watu na kuheshimu mkubwa na mdogo na kusikiliza maoni ya watu ambao amewazidi elimu,kuwa na msimamo katika masuala ya msingi.

Kaka George na kupa hongera kwa NCCR Mageuzi kwa kuonyesha imani na wewe hadi wamepitisha jina lako uwe mgombea urais kupitia chama hicho,ni hatua nzuri.

Lakini nakutaka utambue kuwa utakuna na changamoto nyingi katika safari yako, usikate tamaa , pambana kadri ya uwezo wako utakapofikia ndiyo Mungu atakuwa alikuwa amekuandikia ufikie hapo katika  safari yako hiyo ya kuutaka urais wa taifa hili .

Kwani kumbuka wakati tulikuwa tunaketi kitako na Dk.Mvungi alikuwa akituambia kuwa yeye katika maisha yake alishaweka nia ya kuwa siku moja agombee nafasi ya Rais ili aweze kuwatumikia vyema ,na kwamba suala la kushinda au kushindwa yeye lilikuwa halimpi shida kwani ndoto yake ya kugombea urais aitimize na aliitimiza.

Namalizia kuandika makala hii kwa kusema nimefarijika kuona kijana alitengenezwa na kupitia katika mikono ya Dk.Mvungi yaani Kahangwa naye leo hii ameweza kupanda juu na kufikia hadhi aliyowahi kuipata Dk.Mvungi toka NCCR Mageuzi ya kuteuliwa kuwa  mgombea urais mwaka mwaka 2005 , jana kijana wa Dk.Mvungi ,Dk.Kahangwa nae ameweza kupata hadhi hiyo ya kuwa mgombea urais kwa tiketi ya NCCR Mageuzi.

Mungu amrehemu Dk.Mvungi kwani watu wengi walipita mikononi mwake na aliwafundisha mema na leo hii wanachomoza katika nyanja mbalimbali.

Chanzo: Blogg:www. katabazihappy.blogspot.com
Facebook: Happy Katabazi
0716 774494
Aprili 25 mwaka 2015.

******************I
(Tujikumbushe mahojiano niliyowahi kufanya na George na Kahangwa  enzi hizo mimi nikiwa Mwandishi wa Gazeti la Tanzania Daima  ambapo makala hiyo ilichapishwa katika  Gazeti la Tanzania Daima la  Mei 27 mwaka 2009)

ELIMU, MAARIFA NA UCHUMI

Na Happiness Katabazi

Ni jinsi gani elimu inaweza kulisaidia taifa letu kiuchumi na kijamii katika ulimwengu wa sasa?

Takribani nyakati zote katika historia ya mwanadamu, elimu imekuwa ya manufaa sana kwa mtu mmoja mmoja anayeipata na kwa jamii ambayo mpata elimu anaishi. Leo hii zinapoendelea jitihada za kihimizana katika ngazi ya familia na taifa kwamba hapana budi kuwekeza sana katika suala la elimu bila suluhu, kimsingi sababu kuu ni hilo kwamba elimu ina manufaa kwa mtu binafsi (private returns) na kwa jamii (social returns). Ni dhahiri basi kwamba anapoelimika mtanzania mmoja ananufaika yeye na linanufaika taifa zima la Tanzania.

Katika ulimwengu wa sasa unaouzungumzia, manufaa hayo ya elimu yanazidi kutambulika na kuongezeka kiasi kwamba katika mataifa mbali mbali hususan ya ulimwengu wa kwanza elimu inatazamwa kuwa ndilo tumaini la kipekee kiuchumi na kimaendeleo kwa sasa na kwa siku nyingi za usoni.

Utakumbuka kwamba uchumi wa nchi moja moja una msingi wake, matharani hapa Tanzania kwa miongo kadhaa tunazungumza kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa taifa,kwa maneno mengine msingi mkuu wa uchumi wetu ni kilimo. Utakuwa unafahamu pia kwamba mataifa kadhaaa yaliyoendelea kiviwanda yanazungumzia uzalishaji wa viwandani kuwa ndio msingi mkuu wao kiuchumi (industrial economy)
Mtazamo wa kidunia sasa hivi ni kwamba uchumi wa ulimwengu hususan wa mataifa yanayoitwa yaliyoendelea unahama katika kutegemea zaidi viwanda na sekta nyinginezo za uzalishaji, tegemeo kubwa sasa ni maarifa ambayo chimbuko lake ni elimu. Kwa kifupi tunaweza kusema kuwa dunia ya leo na kesho inaelekea zaidi katika uchumi wa maarifa (knowledge economy)

Nchi za ulimwengu wa tatu, ikiwemo Tanzania yetu zimedumu katika kutegemea kilimo, zikashindwa kuingia katika uchumi wa viwanda. Kwa sasa nchi hizi zinayo fursa ya kujikwamua na kutoka katika maendeleo duni endapo zitajielekeza katika kuutafuta uchumi wa maarifa. Kwa mantiki hiyo nchi yetu inayo fura ya kuingia katika ulimwengu wa kwanza, bila kulazimika kutafuta ufalme wa viwanda mama, yatosha tukiuendea sasa kwa udi na uvumba uchumi wa maarifa. Elimu ndio chombo pekee cha kutupeleka huko.

Ni nini hasa unachokimaanisha kwa kusema uchumi wa maarifa na una uhakika gani kwamba kwa kuutafuta uchumi huo taifa letu litaondoka katika ulimwengu wa tatu?

Ndugu mwandishi, upo ushahidi usiotiliwa shaka kutoka katika mataifa mbali mbali ambayo awali hayakufanikiwa sana katika uchumi wa viwanda yakaja kupata maendeleo makubwa sana kutokana na maarifa. Tuchukulie kwa mfano nchi ya Finland, kwa miongo kadhaa taifa hilo lilikuwa halina mafanikio makubwa kiuchumi, wafinland walitegemea sana zao la mbao na mara kwa mara uchumi wao uliyumba. Lakini tokea serikali ya nchi hiyo ilipofunguka macho ikawekeza kwa nguvu katika maarifa, Finland kwa sasa limekuwa taifa lenye mafanikio makubwa sana kiuchumi kwa kiasi kilichoushangaza ulimwengu. Kwa sasa finland ni moja ya nchi chache sana duniani zinzoweza kutoa kwa raia wake elimu bure kuanzia elimu ya msingi hadi vyuo vikuu. Mataifa yaliyoko katika umoja wa nchi za Ulaya yanaendelea kujifunza kwa bidii kile ambacho finland imekifanya, wakijua fika kuwa katika ulimwengu wa utandawazi ni maarifa pekee yatakaloliwezesha taifa kuwa na nguvu kubwa kiuchumi.

Kwa ufupi uchumi wa maarifa ni uchumi unaotegemea maarifa kama raslimali kuu. Unajua maliasili kama madini na ardhi ni rasilimali, fedha ni rasilimali hali kadhalika watu ni raslimali. Hizo ni raslimali zinazoshikika na kuonekana wazi (tangible resources) lakini maarifa ni tofauti kidogo maana ni intangible. Viel vile wakati rasilimali tangible hutumika na kuisha, rasilimali ya maarifa haiwezi kuisha bali huwa bora zaidi na kuongezeka kadiri inavyotumika.
Uchumi huu wa maarifa unaeleweka zaidi unapochanganuliwa katika zile zinazoitwa nguzo zake kuu nne. Hizo nguzo ni Elimu na uendelezi wa rasilimali watu; pili, Utafiti, uvumbuzi na ubunifu; tatu, Tekinolojia na mawasiliano; na nne ,ni Mfumo wa utawala na nyenzo sahihi.

Katika nguzo ya elimu na uendelezi wa rasilimali watu, ili taifa liufikie uchumi wa maarifa linatakiwa kuhakikisha kuwa elimu inayotolewa ina ubora wa hali ya juu na watu wa nchi husika wanaendelezwa kwa wingi, kama sio wote ili wafikie viwango vikubwa vya elimu na kuyapata maarifa watakayoyatumia kuujenga uchumi wao.

Taifa halina budi kuhakikisha si tu kwamba halina raia yoyote mjinga bali pia asilimia kubwa ya raia ni wahitimu wa vyuo vikuu katika fani mbali mbali na ni wasiokoma kutafuta maarifa hata wawapo kazini na katika maisha yao yote ili wazidi kupata ujuzi wa kazi, wawe wazalishaji zaidi na washindani.

Katika nguzo ya utafiti, uvumbuzi na ubunifu taifa linatakiwa kuwa na mchakato endelevu wa kufanya tafiti zinazolenga kugundua maarifa mapya, suluhu za matatizo mbalimbali, ugunduzi wa nyenzo na uboreshaji wa zana za kazi. Tafiti za namna hiyo zitalifanya taifa kuboresha kila sekta ya uzalishaji na zaidi sana zitalinufaisha taifa kwa njia ya kuuza maarifa yaliyogunduliwa kwa mataifa mengine. Nadhani unafahamu ni kiasi gani wagunduzi wa vitu mbali mbali wanazinufaisha nchi zao kwa kile wanachokigundua.

 Chukulia mfano wa ugunduzi wa simu za mkononi unavyozinufaisha nchi zinazozalisha simu hizo. Ni wazi kuwa elimu yetu inapaswa kuwa na mkono katika hili, tunatakiwa kuwa na elimu inayomfanya mwanafunzi awe na uwezo wa kutafiti na kugundua maarifa mapya au kuwa mbunifu hata akaboresha yale yaliyopo.

Kuhusu nguzo yya teknolojia na mawasiliano, taifa linapaswa kuwa la watu wenye kupata kwa wingi habari sahihi na zenye manufaa, wawe na mawasiliano ya kutosha tena ya haraka na wawe watumiaji wazuri wa teknolojia ya habari na mawasiliano kiasi kwamba njia hizo zinawasaidia kuzalisha mali zaidi, na kwa wakati muafaka. Fikiria kwa mfano, unapokuwa na mkulima au mfanya biashara anayeweza kupata mtandao unaomwezesha kupata habari za soko la mazao yake au bidhaa zake kutoka ulimwengu mzima, ni dhahiri mtu huyu akitumia habari hizo vizuri kamwe hatakuwa sawa na yule anayejua tu habari za soko la kijijini kwake. Hata katika hili elimu ina jukumu muhimu kwani ni kupitia katika elimu watu hujifunza matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano.

Nguzo ya nne ya mfumo wa utawala na nyenzo sahihi. Katika hili taifa linahitaji kuwa na mfumo unaowezesha maarifa yanayopatikana yanatumika vilivyo katika sekta za uzalishaji. Ili kufanikisha hilo hapana budi kuwe na uhusiano wa maana kati ya taasisi za elimu na sekta mbali mbali za uzalishaji. Matharani, kuwepo kwa uhusiano wa vyuo vikuu na sehemu za ajira ili kinachofunzwa vyuoni kiwe ni chenye manufaa mahali pa uzalishaji. Vile vile kuwe na mfumo unaowezesha maarifa kuzalishwa na kutumika katika nchi. Mfumo huo uwezeshe mambo kadhaa kama vile upatikanaji wa nyenzo za kufanyia tafiti, uhuru wa kujiendeleza kimaarifa mahali pa kazi na uhuru wa watu kufanya ugunduzi majaribio na ubunifu.

Unafikiri nguzo hizo za uchumi wa maarifa ziko katika hali gani hapa nchini, taifa letu linawezesha hayo unayoyasema?

Nchi yetu Tanzania, kwa kweli ina hali mbaya sana katika nguzo zote nne. Laiti kama tungekuwa vizuri katika japo nguzo mbili, uchumi wetu ungekuwa na hali nzuri kiasi chake. Elimu yetu imeendelea kuyumbisha na kuwa na hali duni kuanzia kile tunachokiamini na kukitekeleza kama falsafa ya elimu nchini, sera za elimu, mitaala, mchakato wa kufundisha na kujifunza, uwezeshaji wa watendaji katika elimu na suala zima la utadhimini wa elimu.

Ukiangalia katika takwimu zilizotolewa hivi karibuni na benki ya dunia, Tanzania ina alama 7 kwa mia katika elimu na uendelezaji wa rasilimali watu, asilimia 17 katika utafiti na ugunduzi, asilimia 8 katika teknolojia ya habari na mawasiliano, na asilimia 34 katika mfumo na nyenzo. Kwa hiyo uchumi wetu unaitegemea rasilimali ya maarifa kwa asilimia takribani 17 tu, wakati yapo mataifa yamekwisha kufikia asilimia 90 na zaidi.

Unaweza kung’amua kwa takwimu hizo jinsi taifa letu lilivyo na elimu isiyokidhi. Vile vile licha ya kwamba watanzania sasa tunakadiriwa kuwa milioni 39 watu wetu wengi hawajaendelezwa kiasi cha kulinufaisha taifa kiuchumi, tunayo rasilimali watu ya kutosha lakina bahati mbaya iliyokosa maarifa. Mwalimu Nyerere aliwahi kutuambia kwamba, ili nchi iendelee inahitaji pamoja na vitu vingine, watu wake. Lakini watu bila maarifa ni hasara tupu.
Kwa upande wa tafiti nako hatuko vizuri kwa sababu nyingi, kwanza matharani katika vyuo vikuu, utakuta tafiti zinafanyika ndio, lakini si kwa maslahi ya taifa bali kwa wafadhili wan je wanaotoa fedha kwa ajili ya tafiti hizo. Ninachosema hapa ni kwamba watafiti wachache tulionao badala ya kutumiwa na taifa wanatumiwa na mashirika ya nje kufanya tafiti ambazo hao wageni wana maslahi nazo, na watafiti wetu wanakubali maana wanataka pesa. Laiti kama Taifa letu, hususan serikali kuu, ingeona haja ya kuwekeza katika utafiti na kuwawezesha watafiti wetu kutumia umahili wao katika kutafuta maarifa mapya, na kutafiti suluhu za matatizo yetu yote sisi wenyewe.

Kibaya zaidi hata tafiti chache zilizokwisha fanyika nchini, matokeo ya tafiti hizo ni nadra kusikia yakitumiwa vilivyo katika sekta za uzalishaji. Ripoti nyingi za tafiti zimeishia kujaa vumbi katika shelf za maktaba za vyuo vikuu bila kutumiwa.

Ama kwa suala la teknolojia ya habari na mawasiliano, licha ya kwamba hatujamudu kuingiza jambo hili katika shule zetu za sekondari, wengi miongoni mwa vijana wanaojua kutumia intertnet na vitu kama simu za mkononi bahati mbaya hawazitumii katika kiwango kizuri cha kuwanufaisha . Kwa walio wengi internet ni kwa ajili ya kutumiana ujumbe wa kirafiki, kuangalia picha za pono, hali kadhalika simu ni kusalimiana tu. Wachache sana wanaotumia mawasiliano kujiendeleza kielimu, kutafuta maarifa na au kupata habari za masoko na biashara.

Unafikiri ni nini kifanyike?
Yapo mengi ya kufanya, labda mimi nizungumze kupitia jicho la taaluma yangu. Hatuna budi kuwa na sera za elimu zitakazotuhakikishia kwamba kila mwenye uwezo wa kupata elimu ya juu anaipata bila vikwazo vya karo, nafasi kidogo na kadhalika. Tunatakiwa kuongeza fursa kwa gharama yoyote ile, huo ni uwekezaji utakaotuletea manufaa makubwa sana kiuchumi kama nilivyoeleza.

Hatuna budi pia kuwa na mitaala inayomwezesha mwanafunzi kuwa wa manufaa kabisa katika ulimwengu wa kisasa. Tunahitaji wahitimu wanaoajirika, tuahitaji elimu ituzalishie wagunduzi na wabunifu mahiri, watafiti wachapa kazi na watu wanaodumu katika kuyatafuta maarifa kwa bidii katika maisha yao yote.

Kadri tutakavyoendelea na sera za kukopesha watu wachache waingie vyuo vikuu ndivyo tutakavyolididmiza taifa. Kadri tutakavyoipuuza taaluma ya ualimu ndivyo tutakavyo dunisha elimu yenyewe na kubaki kuwa wasindikizaji katika ulimwengu wa utandawazi.

Hujazungumzia manufaa ya elimu kijamii, unasemaje hapo?

Nimetaja jambo la social returns, lakini kwa upande mwingine elimu inapaswa kuinufaisha jamii kwa kuzalisha wahitimu waadilifu.kwa sasa mitaala yetu haijakaza sana suala la maadili na shule nyingi hazionekani zikiwaadilidha watanzania. Yamkini ndio sababu tuanpata wingi wa watumishi na viongozi wala rushwa, wabadhilifu na mafidsadi.

Laiti kama mitaala yetu yote kuanzia elimu ya awali hadi vyuo ingesisitiza vya kutosha elimu ya maadili. Tunatakiwa kuwa waadilifu katika mahusiano, katika kazi, katika utunzaji wa mazingira, katika utumiaji wa rasilimali na katika mwenendo kwa ujumla. Elimu inalojukumu la kutuhakikishia hilo.

Nini historia yako kwa ufupi?

Mimi ni mzaliwa wa mkoa wa Kagera. Umri wangu ni miaka 39 sasa. Nimesoma elimu ya msingi katika shule ya Omurushenye na baadaye Bilele ya mjini Bukoba. Nilipata elimu ya sekondari katika shule ya Sekondari Bukoba. Nilisomea ualimu katika chuo cha ualimu Korogwe. Kwa miaka kadhaa nilikuwa mwalimu wa elimu ya Msingi. Baada ya kujiendeleza na kupata shahada ya kwanza ya ualimu katika chuo kikuu cha Dar es salaam, nilifungisha kwa miaka miwili mara hii elimu ya sekondari. Nilifanikiwa pia kusoma shahada ya uzamili katika elimu, hapa hapa chuo kikuu cha Dar es salaam, na hatimaye kuajiriwa na chuo hiki katika kitivo cha elimu, ambapo kazi yangu ni unadhiri katika masuala ya utawala wa elimu, mipango na sera. Nimepata pia mafunzo ya elimu na Utandawazi katika chuo Kikuu cha Oulu nchini Finland. Nimeoa na tuna watoto wawili.

Ni nini matarajio yako ya baadaye?

Kwa taaluma yangu, inanipasa kujiendeleza zaidi na zaidi katika kuyatafuta maarifa. Natarajia kuanza masomo ya shahada ya juu ya falsafa huko ughaibuni mwishoni mwa mwezi huu. Bila shaka ninalo jukumu la kuitumia elimu yangu katika utumishi kwa taifa langu.

 Ndoto yangu ni kupata fursa pana za kuwahudumia na kuwatumikia watanzania wengi zaidi kama sio wote kwa kadri Mungu atakavyonipa kibali.

Chanzo: Gazeti la Tanzania Daima la Mei 27 mwaka 2009 .

0716 774494

No comments:

Powered by Blogger.