Header Ads

Kamishna wa kwanza mwanamke wa Jeshi la Magereza Tanzania

Aziza Mursali
Kamishna wa kwanza mwanamke wa Jeshi la Magereza
*Ndiye alikuwa Naibu Kamishna Mwanamke Pekee
*Aeleza siri ya mafanikio yake jeshini
*Awaonya wanawake kutojilegeza

AZIZA Mursali (57) ni mmoja kati ya wanawake wachache waliopata mafanikio makubwa yaliyotokana na bidii na kujituma katika kazi. Akiwa miongoni mwa askari wachache wa kike waliojiunga na Jeshi la Magereza mwishoni mwa miaka ya 1960, alifanikiwa kupanda ngazi za kijeshi hadi kufikia cheo cha Kamishan na kuwa mwanamke wa kwanza katika historia ya jeshi hilo kutunukiwa wadhifa huo. Katika makala hii, Mwandishi Wetu Happiness Katabazi, anamuhoji mwanamama huyo siri ya mafanikio na misukosuko aliyokutana nayo katika maisha yake ya kazi ndani ya jeshi hilo.

Swali: Kitu gani kilikusukuma kujiunga na Jeshi la Magereza?

Jibu: Nilikuwa na mapenzi ya Jeshi la Magereza tangu nilipokuwa msichana mdogo bila kujua ni kwa sababu gani, lakini ilitokea tu nikawa napenda kuwa Askari wa Magereza.
Kama Mungu alijua kuwa nalipenda jeshi, baada tu ya kumaliza masomo yangu nililetewa barua ya kutakiwa kujiunga na Jeshi la Magereza kutoka iliyokuwa Idara ya Kazi wakati huo. Enzi hizo kulikuwa na utaratibu wa vijana wanaomaliza shule kupangwa kufanya kazi katika idara mbalimbali au kujiunga na kozi. Bila kusita niliikubali nafasi hiyo, ndiyo hivyo.

Swali: Wewe ni mwanamke mwenye mafanikio makubwa ndani ya Jeshi la Magereza, siri ya mafanikio yako ni nini?

Jibu: Siri ya mafanikio yangu ni utii, uaminifu, ukweli, juhudi na bidii kazini, lakini kikubwa ni kujiendeleza. Katika maisha yangu nimekuwa nikijiendeleza bila kuchoka, imani niliyojijengea kuwa elimu haina mwisho ndiyo iliyonisaidia na kufika hapa nilipo.

Swali: Wewe ni kiongozi wa kijeshi, kwa cheo chako haina shaka una majukumu mengi na makubwa, unaweza kumudu kazi yako na kutunza familia yako?

Jibu: Ukitaka mafanikio katika kazi yoyote ni lazima ujiwekee taratibu ambazo ni lazima uzifuate, kwa kuzingatia taratibu nilizojiwekea nimekuwa nikipanga ratiba ya kazi zangu na za familia yangu. Ninachofanya ni kuhakikisha ratiba zangu za nyumbani hazivurugi taratibu ya kazi za mwajiri wangu. Ingawa kazi za jeshi ni amri, lakini ninao muda mwafaka wa kuwa na familia yangu, mara nyingi natumia muda wa jioni, siku za sikukuu na likizo. Mwanamke hatakiwi kubweteka, kama tunapiga kelele za usawa ni lazima tuonyeshe kweli tunaweza, na nimekuwa nikifanya kazi kwa bidii siku zote ili kuthibitisha hilo.
Imenisaidia na hata kama ningekuwa si askari na kuwa ninaishi kijiji, ningelima kwa bidii, ni mpangalio tu na uamuzi, kama mtu umeamua kweli kufanya na kazi kuachana na uzembe na utegemezi hakuna kinachoshindikana.

Swali: Kuna madai kuwa nafasi za kujiunga na jeshi zinatolewa kwa upendeleo, ni lazima muombaji awe na mtu anayemjua wa kumfanyia mpango, unalizungumziaje hili?

Jibu: Huo ni uongo. Ajira kwa vijana wanaotaka kujiunga na jeshi zinatangazwa magazetini, pia kuna matangazo mbalimbali yanayobandikwa hadi vijijini kuelezea sifa zinazotakiwa kwa waombaji.
Waombaji hujadiliwa na Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya na wanaochaguliwa huchujwa na Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa, wenye sifa huchaguliwa na Magereza huwa hawabadili uamuzi wa vikao vya Ulinzi na Usalama vya mikoa.

Swali: Kwa mtizamo wako, viongozi wanawake ndani na nje ya jeshi hapa wanatosha?

Jibu: Idadi ya wanawake viongozi hapa nchini haina uwiano sawa na wanaume, hilo liko wazi. Wito wangu kwa Watanzania, kila mtu kwa nafasi yake aone umuhimu wa kuwapa elimu wasichana. Ni lazima tukubali kuwa wanawake wanaweza kuwa viongozi wazuri, inategemea na malezi na jinsi wanavyowezeshwa. Mfano hai ni mimi. Pamoja na wengine ambao tunalitumikia taifa letu katika ngazi mbalimbali za uongozi, wanawake tupo na hivi sasa tunajivunia kuwa na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha-Rose Migiro. Kikubwa, nasisitiza hili, ni malezi na kuwezeshwa.

Swali: Ukiangalia enzi ulizojiunga na jeshi na sasa, ukakamavu mliokuwa nao wanawake wakati huo ni sawa na walionao wasichana wa sasa.

Jibu: Sioni tofauti kubwa kati ya askari wa kike wa karne ya 20 na wa karne ya 21, tofauti ndogo iliyopo ni kwamba askari wa kike wa enzi zetu ni wavumilivu sana. Unajua wakati huo wasichana wengi wasomi hawakutaka kujiunga na Magereza, tuliojiunga tulikuwa na nia na dhamira ya kweli ya kulitumikia jeshi, ndio maana tumefanya kazi katika mazingira magumu kwa miaka mingi kwa uaminifu bila kukata tamaa. Lakini kwa hivi sasa watu wanaangalia maslahi kwanza, ule moyo wa kujituma kizalendo umefifia.

Swali: Ni tukio gani kubwa katika maisha yako jeshini au kabla hujajiunga na jeshi ulilokutana nalo ambalo hutalisahau.

Jibu: Ni kifo cha Mwalimu Julius Nyerere…Unajua yule alikuwa kiongozi kweli, ninaweza kusema hata moyo wa kujiunga na jeshi mimi na baadhi ya wenzangu tuliupata kwake. Alikuwa kiongozi aliyekuwa akiwajenga vijana wa Kitanzania kuipinda nchi yao, kuwa na moyo wa kizalendo, tulikuwa tunaipenda kweli Tanzania yetu.

Swali: Kuna haya madai ya kuwapo kwa unyanyasaji wa kijinsia kwa askari wa kike kunakofanywa na askari wa kiume jeshini. Je, madai haya yana ukweli wowote?

Jibu: Ninalolifahamu mimi ni Jeshi la Magereza, hivyo nitalizungumzia hilo. Kwanza kunyanyaswa kijinsia ni udhaifu binafsi. Ukweli ni kwamba ndani ya Jeshi la Magereza hakuna huo unyanyasaji, wala askari wa kike kunyanyaswa na askari wa kiume hakuna Tatizo hapo ni moja nililoligundua mimi - kudeka! Baadhi ya wanawake wanapenda kudeka, na jeshini ni amri ndugu yangu, sasa kama mtu ana tabia ya kudekadeka au kujirahisirahisi, popote pale watadhani kuwa ananyanyaswa.

Swali: Mabadiliko yanayofanywa sasa na serikali katika Jeshi la Magereza unayaonaje, yanawaridhisha ninyi askari?

Jibu: Sana, tena kwa kiasi kikubwa sana. Unajua mahali popote kama unawataka watu wafanye kazi vizuri, ni lazima uwawezesha, si siri, hapo nyuma askari tulikuwa na hali mbaya sana lakini sasa hali imebadilika, serikali inawatupia jicho askari wake na ninaomba iendelee kufanya hivyo.
Tuna mafanikio mengi, mfano tumepewa zabuni ya ujenzi wa nyumba za serikali na tumemudu kuzijenga kwa ubora wa hali juu, magereza mapya yamejengwa sehemu mbalimbali nchini sambamba na upanuzi na ukarabati wa magereza ya zamani.
Lakini hata wafungwa hali zao zimeboreshwa, sasa wanavaa shati na suruali badala ya kaptura zilizokuwa zinadhalilisha utu wao, sasa magereza yana radio za kisasa na televisheni zinazotoa mafunzo burudani kwa wafungwa, haya yote ni mafanikio.
Lakini pia serikali imewakumbuka zaidi wanawake. Sasa yupo mkuu wa Magereza wa mkoa mmoja - Boharia Mkuu wa Jeshi la Magereza mmoja ambaye ni Kamishna Msaidizi Mwandamizi Edith Malya, Mkuu wa Chuo cha Udereva mmoja, yeye ni Kamishna Msaidizi Grace Ungani, pia yupo Katibu wa Bodi ya Parole Magereza nchini, Kamishna Msaidizi Mwandamizi Simfroza Bondo pamoja na maofisa nidhamu wa mikoa wawili. Hizi zote ni jitihada za serikali kulifanyia mabadiliko Jeshi la Magereza.

Swali: Tueleze historia ya maisha yako.

Jibu: Nizaliwa 1950 katika Kijiji cha Mazombe, Wilaya ya Iringa Vijijini. Mimi pamoja na ndugu zangu tisa tulilelewa na mama baada ya baba kufariki mwaka 1958 tukiwa bado wadogo.
Mama ni mkulima, aliolewa na mwanamume mwingine baadaye, baba yetu huyo wa kambo alitusomesha mimi, kaka yangu na wadogo zangu watatu hadi elimu ya sekondari, huwa tunamshukuru sana baba huyu.
Nilihitimu masomo ya sekondari mwaka 1968 katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Mtwara. Na mwaka huo huo nilijiunga na Jeshi la Magereza. Kituo changu cha kwanza cha kazi kilikuwa Gereza la Wanawake KPF – Morogoro.
Mwaka 1969 nilihudhuria mafunzo ya uaskari katika Chuo cha Magereza Ukonga kwa muda wa mwaka mmoja. Mwaka 1971 nilirudi tena katika Chuo cha Magereza Ukonga kwa kozi fupi ya uongozi na mwaka huo huo nilikwenda kusoma Elimu ya Siasa katika Chuo cha Kivukoni. Baadaye mwaka 1974 nilijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kama mwanafunzi wa nje wa chuo, ambako nilisoma kozi ya sheria na nilihitimu na kutunukiwa cheti mwaka 1976.
Mwaka 1976 nilikwenda tena Ukonga kusoma kozi ya Gazzetted Officer na baadaye mwaka 1981 nikarudi Kivukoni kwa ajili ya kozi ndefu elimu ya siasa na kisha mwaka 1984 nilikwenda nchini Burgaria kwa ajili ya kozi ya mwaka mmoja ya Social Science & Management course.
Hivi sasa ninasomea Shahada ya Sheria (LLB) katika Chuo Kikuu Huria cha Tanzania nikiwa mwaka wa mwisho.
Katika kipindi changu cha utumishi ndani ya Jeshi la Magereza nilishika pia wadhifa wa Katibu Msaidizi Mkuu wa Chama wa Mkoa wa Majeshi kwa muda wa miaka mitano Nilikuwa Katibu Mkuu Msaidizi wa Chama wa Mkoa wa Majeshi kabla ya Tanzania haijaingia katika mfumo wa vyama vingi vya siasa 1992.
Mkoa wa Majeshi ilikuwa ukiundwa na vikosi vya Ulinzi kutoka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Polisi na Magereza.
Katika vipindi tofauti nimefundisha katika vyuo vya kijeshi kikiwamo Chuo cha Usalama Moshi na Chuo cha Maofisa wa Magereza Ukonga. Aidha, nimewahi kuwa Mkuu wa viwanda vya Magereza nchini, hivyo naamini nina sifa za kuwa kiongozi.
Niliteuliwa kuwa Kamanda wa Magereza Mkoa wa Kagera Oktoba 17, 2003. Nimeolewa na Said Kangwi, mwenyeji wa Kijiji cha Mkanyageni, Wilaya ya Muheza, mkoani Tanga. Nina watoto wanne - wasichana watatu na mvulana mmoja.
Katika maisha yangu ya utumishi jeshini nimetunukiwa medali mbalimbali ikiwamo ya utumishi uliotukuka niliyotunukiwa mwaka 1996 na nishani ya utumishi wa muda mrefu mwaka 1999.Na Agosti mwaka huu nilipandishwa cheo na kuwa Kamishna mwanamke pekee magereza, kabla ya kupandishwa cheo hiki nilikuwa na Cheo cha Naibu Kamishna ambacho nimedumu nacho kwa miaka mitatu na wakati wote nikiwa na cheo hicho cha DCP nilikuwa nacho mwanamke peke yangu.

0755 312859:katabazihappy@yahoo.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima, la Jumapili April 29,2007

1 comment:

yussufu said...

Aziza Mursali ni mwanamke wa shoka.
Nilitaraji angekuwa PCP

Powered by Blogger.