Header Ads

Ukaidi wa Malima,unabomoa nguvu za Bunge?

(Sauti ya Jumapili) April 8,2007,Easter day

Na Happiness Katabazi

HIVI karibuni baadhi ya vyombo vya habari vilimkariri Mbunge wa Mkuranga Adamu Malima, kwamba hayupo tayari kwenda ofisini kwa Spika wa Bunge Samwel Sitta, kwaajili ya kupatanishwa na Mwenyekiti wa Makapuni ya IPP, Reginald Mengi, kwakuwa hana ugomvi naye.

Vyombo hivyo vya habari kwa nyakati tofauti pia vilimkariri Mbunge huyo, kwamba akubaliani na uamuzi wa Spika, na badala yake amewasilisha malalamiko yako kwa Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yusuf Makamba, ya kwamba amezalishwa na uamuzi ulitolewa Spika Sitta bungeni hivi karibuni.

Pia vyombo hivyo vilimkariri Makamba, ambaye alikiri kupokea malalamiko ya Malima, dhidi ya Spika Sitta kwakuwa hawa wote ni viongozi ndani ya CCM, ambaye hata hivyo alisema lalamiko hilo litaongelewa katika vikao husika vya chama.

Kwa wale kama mimi tunaofuatilia masuala ya siasa za hapa nchini na mustakabali wanchi yetu mtakuwa mmesikia na kuzisoma kauli za viongozi hao kupitia vyombo vya habari hivi karibuni.

Uamuzi uliotolewa bungeni hauwezi kupingwa kwenye chombo cha chama siasa na hilo likifaulu ni kuvunja mamlaka ya bunge na kufanya bunge letu tukufu kuwa ni kichekesho kubwa sana.

Ieleweke kwamba wabunge na hata Spika wa bunge ni wanachama wa vyama vyao lakini ikiwa vikundi ndani ya Chama Tawala (CCM) , kinatumika kudhoofisha mamlaka ya bunge ni hatari kwa demokrasia hapa nchini.

Inawezekana kwamba uamuzi wa Sitta, kuhusu sakata la mbunge huyo na Mengi,aliutoa bungeni mapema mwaka huu, haukukubaliwi na kundi la Malima ambaye hivi sasa anatazamwa kuwa yeye ni chambo,kuadi wa vigogo ndani ya CCM katika kupigania madaraka siku za usoni.

Lakini kubomolewa kwa Spika Sitta ni kubomolewa kwa mamlaka ya bunge na inawezekana kuleta mtafaruku mkubwa ndani ya CCM.Na si mtafaruku pekee, pia linadharirisha CCM, na viongozi wa chama hicho ambao wengine ni viongozi wa kuu ndani ya serikali.

Pia kutaitimisha minong'ono inayoongelewa chini chini hivi sasa,ya kwamba viongozi wengi wa awamu hii ni wasanii na wanaendesha nchi hii kisanii na ambao nyoyo zao zimejawa na uchu wa madaraka na wapo madarakani kwaajili ya maslahi yao binafsi.

Lile sakata la Malima na Mengi, lilionyesha mgawanyiko mkubwa katika vigogo ndani ya CCM na kilichokuwa kinaonekana wazi ni makundi ambayo yalikuwa yanajipendekeza na kujikomba kwa Rais Jakaya Kikwete, kwa kisingizio cha kumtetea Rais hatangazwi vizuri na apewi muda wa kutosha na vyombo vya habari vinavyomilikiwa na Mengi.

Sasa kama Malima anafikiri hilo linaweza kutatuliwa kwa siri ndani ya CCM amekosea sana.Binafisi si mtetei Sitta wala Mengi, lakini umbeya na uzandiki wa jambo lenyewe hautoshi katika vita vya kumng’oa Sitta katika cheo chake cha Uspika.

Na ninashanga hadi sasa Sitta kutomchukulia hatua mbunge huyo baada ya kukaidi amri ya bunge. Kwa hili Malima kukataa amri ya Sitta inavyoonekana vita vya kugombea urais ndani ya CCM vimeanza na bila shaka Malima ni kuadi au mpiga debe wa mgombea urais ajaye na ndiye anayempa jeuri na kibri.

Viongozi wetu mtambue hili kwamba lengo la kuwa viongozi ni kuongoza wananchi ili wajiletee maendeleo na kazi ya kiongozi ni kuwafikisha hapo wananchi.

Sasa kiongozi anapozua mjadala ya kitaifa isiyo na kichwa wala miguu ni kuiletea taifa hasara.Watanzania ebu tufikirie hoja ya Malima na Mengi imetughalimu fedha kisasi gani za walipa kodi? Ebu angalia Taifa limetumia muda gani wa watu walioshiriki katika hoja hiyo?.

Ebu fikiria tu wananchi huko mitaani walioshiriki katika hoja hiyo badala ya kufanya shughuli za maendeleo. Narudia tena Malima hoja yako siyo ya msingi na kamwe haileti tija kwa taifa hili.

Malima alikuwa akimtuhumu Mengi kuwa anatumia muda mwingi kujitangaza yeye kwenye Televisheni yake ya ITV kuliko viongozi wa nchi, lakini kwasasa tunachokishuhudia kufanywa na mbunge huyo ni anatumia muda mwingi wa wananchi kumjadili tena yeye anatumia vyombo vingi vikiwemo vya habari na CCM.

Nimalizie kwakumwambia Malima, kuwa mwisho wa ubaya ni aibu kwahiyo usipoangalia utakuja kuumia kwa aibu kwani unaweza kuwa unatumiwa bila wewe kujua na wajanja wakawa wamevuna wakakuacha kwenye mataa.

Mungu ibariki Afrika, Mungu inusuru Tanzania
0755 312859;katabazihappy@yahoo.com;www.katabazihappy@blogspot.com

Chanzo;Gazeti la Tanzania Daima

No comments:

Powered by Blogger.