Header Ads

Ukimya wa wazazi wa wanafunzi wa elimu ya juu unamaanisha nini?

Na Happiness Katabazi

ELIMU, kama zilivyo sekta nyingine ina wadau ambao si haba. Wadau hao uhusika kwa namna moja au nyingine katika kuamua mustakabari wa sekta husika.

Hapa nchini, wadau wa Elimu ni pamoja na Serikali Kuu, Serikali za Mitaa, Jumuiya za wahisani, Taasisi na Mashirika mbalimbali, Taasisi za elimu, Wazazi, walimu na wanafunzi,asasi za kidini.

Mchango wa kila mdau katika ya elimu katu haupuuziki kwa kuwa ni mkubwa na wa maana sana. Matharani, wadau hawa wanawajibika kugharimia elimu, kuendesha mchakato wa siku hadi siku mashuleni au vyuoni, na vilevile kushawishi (influence) mitaala itumikayo mashuleni.

Lakini, mara kadhaa baadhi ya wadau wameonekana kusahau wajibu wao huo na kukaa pembeni, hata wasijihusishe katika mambo yanayoipata sekta ya Elimu kana kwamba ama hayawahusu au hakuna umuhimu wa wao kuyashughulikia.

Nitoe mfano wa ambayo yamekuwa yakijiri hapa nchini katika vyuo vyetu vya Elimu ya Juu. Vyuo hivi vimekumbwa na matatizo mengi tokea enzi za uongozi wa Baba wa Taifa Mwalimu Julias Nyerere hata leo. Kumekuwa na matatizo kama vile migomo ya wanafunzi ambavyo sasa imegeuka kuwa kana kwamba ni moja ya sifa kuu za vyuo vikuu vya Tanzania.

Katika tukio la hivi karibuni (mwezi huu April, 2007), wanafunzi wa vyuo hivyo waligoma kuingia madarasani wakipinga kulipia moja kwa moja asilimia arobaini (40%) ya karo yao ya kila mwaka wa masomo. Mgomo huo ulisababisha vyuo vifungwe na baadaye wanafunzi wakatangaziwa masharti mazito yapatayo tisa (9) ambayo pasipo kutimizwa kuyatimiza, katu mwanafunzi asiote kurejea masomomi katika chuo husika.

Naam, nafasi za baadhi ya wadau wa Elimu katika kushughulikia masuala ya elimu ilijionesha wazi katika hili. Mdau serikali, kipitia mamlaka aliyopewa Makamu Mkuu wa Chuo aliwatimua wanafunzi, kisha kupitia Naibu waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia na Waziri Mkuu, mdau Serikali akawalaumu wanafunzi kwa kugoma na akabariki hatua ya kutimuliwa kwao.

Kwa upande wake wadau taasisi na mashirika, matharani vyama vya siasa CUF, TLP, NCCR, CHADEMA na NGOs kama TANLET, wakapinga kufukuzwa kwa wanafunzi na kuwataka wahusika wavifungue vyuo bila masharti.
Kinachogomba hapa ni kwamba, yu wapi mdau/wadau wakuu waitwao WAZAZI katika hili? Mbona wazazi mko kimya mara zote katika matatizo ya watoto wenu wanaosoma vyuo vikuu?

Siamini kwamba nafasi yenu wazazi inaishia katika kuwagombeza wana wenu wanaporejeshwa mara kwa mara majumbani mwenu eti kisa wamegoma. Haiingii akilini mwa mtu anayefikiri vizuri kwamba wazazi mnaona ni vyema kunyamaza kimya ilihali mnajua kabisa kwamba baadhi yenu watoto wenu hamjawaona huko nyumbani tokea wafukuzwe.

Sijui mnajisikiaje mnaposikia kwamba baadhi ya wanafunzi hao wanazagaa jijini Dar es Salaam ama wakiuza mali zao na pengine miili yao ili wajikimu katika kipindi ambacho hata hawajui ni kirefu kiasi gani.

Dhalau (kudharirishwa) hii inayowapata wana na mabinti zenu si tu itakiongezea kizazi hiki laana bali itawafanya hao wanafunzi wajapohitimu, virusi vya ukimwi wanavyovichota katika kipindi hiki havitawaruhusu walitumikie taifa na wala hawatakuwa na nguvu za kurejesha hiyo mikopo wanayopewa ili wasome.

Sidhani mko tayari kuuza mashamba yenu ili mlipe, mikopo waliyopewa watoto wakaaga dunia kabla ya kuirejesha kupitia nguvu kazi zao.Pengine kwa kuwa kuna baadhi ya watanzania hatupendi kufikiri juu ya kesho, hayo madhara ya baadaye twaweza kuyapuuza.

Lakini lipo ambalo wazazi hamtalipuuza maana linawahusu ninyi moja kwa moja; nalo ni masharti 9 waliyopewa wanafunzi.Mojawapo ya masharti hayo ni kwamba watoto wenu hawatarejea vyuoni hadi walipe 40%.

Ukweli ni kwamba sharti hii hawajapewa wanafunzi bali ninyi wazazi na walezi. Kazi kwenu, mnatakiwa mlipe hizo fedha japo watoto wenu waligoma wakidai ninyi wazazi mlio wengi hamna uwezo wa kulipa kiasi hicho.

Pengine baadhi yenu mmeshaanza kulipa au mnakusudia kufanya hivyo. Fanyeni hima basi ili ithibitike kwamba wanafunzi ni waongo na wakorofi tu maana kumbe wazazi mnao uwezo wa kulipa bila matatizo.

Au ithibitike vinginevyo, kwamba wanafunzi walisema ukweli maana wanazijua fika hali za familia walikotokea. Naamini katika upande wa kwamba, wanafunzi walisema UKWELI. Ni mtanzania yupi asiyejua kwamba nchi hii licha ya kubarikiwa kwa utajiri wa Rasilimali, wanaoufaidi utajiri huo ni tabaka dogo la walanchi na maswahiba wao kutoka nchi za nje, wanaoifyonza nchi hii hadi inyauke kwa kisingizio cha soko huria na uwekezaji.
Wazazi (wananchi) wa kitanzania walio wengi ni wakulima hohehahe ambao licha ya uduni wa zana zao za uzalishaji, kizalishwacho mashambani kinakosa soko, kiasi kwamba kumudu maisha ya kila siku ni msamiati mgumu kwa familia nyingi, sembuse kulipia elimu ya chuo kikuu!

Ama si ninyi wazazi mlioshindwa kulipa UPE na UMITASHUMTA wa shilingi 2000/= tu hata ada hiyo ikafutwa, mtayaweza ya laki tano (500.000/=) na ushehe, jumlisha na mkopo wa asilimia sitini (60%) juu?Yamkini yote haya wazazi hamyaoni hata mngali mwaendelea kunyamaza. Mjapo lipa hiyo 40% kumbukeni yafuatayo.

Mosi, mtakuwa mmebariki Serikali ijitoe moja kwa moja katika kugharimia elimu ya juu maana sasa kila mzazi atamsomesha mwanae chuo kikuu kwa kugharimia asilimia 100% ya mahitaji, wakati huo huo mkilipa Serikali kodi sijui ikatumie fungu hilo kufanyia ziara za ughaibuni na manunuzi ya mashangingi,kujenga mahekaru,rada butu na madege ya anasa.

Pili, kwa kuwa alipiaye kilo moja ya Sukari dukani hamtarajii mwenye duka ampimie nusu kilo, na katu hata mtoto mdogo hataondoka penye dirisha la duka hadi apewe kiasi timilifu cha bidhaa aliyolipia, ni wakati wenu sasa wazazi kwa kushirikiana na wanafunzi watoto wenu, kuhakikisha kwamba hiyo elimu mtakayokubali kuilipia 100% ubora wake usiwe chini ya thamani hiyo. Itakuwa ni “uzumbukuku” endapo mtagharimika kiasi hicho alafu watoto wenu waendele kupatiwa elimu isiyowawesha kuajirika au kujiajiri.

Eti mlipe gharama hizo, alafu wana na mabinti zenu waendelee kujifunza wakiwa wamesimama nje ya vyumba vya madarasa wanasikiliza Mhadhara (Lecture) kwa kuwa madarasa yamejaa pomoni!

Ati mlipe mamilioni, alafu katika mabweni watoto wenu walale ‘mzungu mchongoma’ kana kwamba wako gerezani. Mtoe fedha lukuki alafu wanafunzi wapatiwe muda kichele wa mafunzo kwa vitendo. Waulizeni wakupeni ‘orodha mnyororo’ ya matatizo yanayowasibu wawapo masomoni.

Mjikamue kisawasawa alafu kizazi chenu kipate huduma mbovu za maktaba zenye vitabu na vifaa visivyotosheleza. Mjitoe mhanga kugharimia alafu wasomi wenu wagombanie komputa chache zilizopo vyuoni kana kwamba ni wa cheza mpira na refa kaamuru kona. Mtoe fedha za kilo moja ya mchele, mnyamaze kimya msiwaulize wana wenu iwapo mwenye duka ni kweli kapima kila moja, sufuria jikoni ikipwaya msimlaumu mtu bali ukimya wenu.

Nikusihi au nikuulize ewe mzazi, wapi udau wako katika elimu; ni upi msimamo wako kuhusu migomo ya wanafunzi na hatua ambazo serikali inawachukulia. Wapi sauti ya Jumuiya ya Wazazi Tanzania , wapi kauli ya umma wa watanzania. Mwathubutuje kunyamaza wakati mustakabari wa watoto wenu na taifa kwa ujumla uko mashakani! Haifai mkanyamaza kama kwamba kuna mliyemwajiri awasemee.

0755312859;katabazihappy@yahoo.com;www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Tanzania Daima la Jumatano, April 25,2007.

No comments:

Powered by Blogger.