Header Ads

WAITARA:SITAKI SIASA

*Asema ataendelea kuishi Dar

Na Happiness Katabazi

MKUU wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) mstaafu, Jenerali George Marwa Waitara (57), amesema hana mpango wa kushiriki katika siasa.

Jenerali Waitara alisema hayo jana kwenye lango la kutokea la Kambi ya Jenerali Twalipo, Mgulani jijini Dar es Salaam, muda mfupi baada ya kusukumwa na maofisa wakuu wanane wenye vyeo vya meja jenerali na brigedia jenerali, kama ishara ya kuagwa rasmi jeshini.

Jenerali Waitara ambaye aliagwa kwa kishindo na heshima zote za kijeshi, alisema hata baada ya kustaafu rasmi Septemba 15, ataendelea kuishi Dar es Salaam kwa kuwa familia yake ina makazi ndani ya jiji.

“Ndiyo nimestaafu lakini nitaendelea kuishi hapa hapa jijini kwa kuwa familia yangu ipo hapa, ila wakati mwingine nitakuwa nikienda Tarime ambako nilizaliwa… ila sihami jijini, nitaendelea kuishi hapa hapa,” alisisitiza Jenerali Waitara, huku akicheka na kusababisha maofisa wa jeshi hilo waliokuwa karibu yake na waandishi wa habari kuangua kicheko pia.

Akijibu mwaswali ya mwandishi wa gazeti hili kwamba ana mpango wa kuingia kwenye medani ya siasa na anatarajia kufanya shughuli gani, alisema kazi anayoijua yeye ni moja, na kuitaja kazi hiyo kuwa ni jeshi.

Alisema hana mpango wa kujitumbukiza kwenye siasa kwa kuwa kazi anayoijua yeye ni jeshi, na kuwa tangu azaliwe hajawahi kufikiria wala kuota ndoto ya kujiunga katika siasa.

Kuhusu shughuli gani ya kumuingizia kipato anayotarajia kuifanya baada ya kustaafu, alisema hadi wakati anastaafu alikuwa hajapanga atafanya shughuli gani na akaongeza kuwa, baada ya mapumziko ataangalia na kushauriana na ndugu na jamaa zake kuhusu shughuli atakayoifanya.

Mkuu mpya wa JWTZ, Jenerali Davis Mwamunyage, alimkabidhi mstaafu huyo kitambulisho cha kustaafu, ikiwa ni ishara ya kumuaga na Waitara naye alimkabidhi kitambulisho chake cha kazi, alichokuwa akikitumia kabla ya kustaafu.

“Leo nina furaha kubwa sana ya kukukabidhi hati hii ambayo utaitumia baada ya kustaafu… na ninakukabidhi hati hii kwa niaba ya JWTZ kama ishara ya kutambua na kuheshimu utumishi ndani ya jeshi hili… hongera sana na nina furaha sana kuona unastaafu kwa amani na kuliacha jeshi likiwa imara,” alisema Jenerali Mwamunyange.

“Nami nakukabidhi kitambulisho changu ambacho nilikuwa nikitumia kabla ya kustaafu kazi ya jeshi kama ishara ya kitambulisho hicho kwisha muda wake,” alisema Jenerali mstaafu Waitara.

Sherehe za kuagwa kwa mstaafu huyo zilianza saa 2:30 asubuhi katika Kambi ya Jenerali Twalipo, Mgulani kwa gwaride lililokuwa na gadi sita.

Awali, gadi hizo zilifanya gwaride la kumkaribisha Mkuu mpya wa jeshi hilo, Jenerali Mwamunyange, ambaye aliapishwa Jumamosi iliyopita na Amiri Jeshi Mkuu, Rais Jakaya Kikwete, na kisha kupita mbele kwa ukakamavu na kisha kutoa heshima kwa mwendo wa pole na haraka.

Baada ya kumaliza kutoa heshima, gwaride hilo lililokuwa likiongozwa na Kanali Raphael Mataba, liliumba umbo la Omega ikiwa ni ishara ya utumishi wa mwisho wa Waitara katika jeshi hilo.

Baada ya tukio hilo kumalizika, Waitara alipakiwa kwenye gari maalumu la wazi lililokuwa lilisukumwa na maofisa wa jeshi taratibu. Maofisa hao waliongozwa na mameja jenerali wawili. Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Meja Jenerali Martin Madatta na Meja Jenerali Sylvester Rioba.

Wengine sita waliomsukuma ni wenye vyeo vya brigedia jenerali, Said S. Omar ambaye ni Mkuu wa Kikosi cha Wanamaji (Navy), Seni Hinda, Charles Makakala, Rasul Kilonzo, Kamaro Ileti na Albert Balati.

Sherehe hizo zilihudhuriwa na Kaimu Kamishna Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini, Aziza Murhsal, Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Profesa Juma Kapuya, majenerali wastaafu, waambata wa kijeshi wanaowakilisha nchi zao hapa nchini na wananchi wa kawaida.

Wakati huo huo, maofisa na askari wa kawaida walimmwagia sifa Waitara wakimtaja kama kiongozi imara aliyeliongoza jeshi katika misingi ya haki na maadili mema.

Waitara alistaafu rasmi Septemba 15 mwaka huu. Alizaliwa Septemba 15 mwaka 1950 katika Kijiji cha Itirya, Wilaya ya Tarime, mkoani Mara. Alimaliza masomo yake ya Sekondari katika Shule ya Sekondari ya Minaki mwaka 1969.

Alijiunga rasmi na jeshi hilo mwaka 1970 akiwa ofisa mwanafunzi, na alipata kamisheni mwaka 1971, na kuhudhuria mafunzo mbalimbali ya kijeshi.

Mwaka 1978, katika vita ya Tanzania na Uganda, Waitara alikuwa miongoni mwa makamanda walioongoza vikosi katika vita hiyo.

Wakuu wa majeshi wengine waliomtangulia Waitara ni Sam Hagai, Mrisho Sarakikya, marehemu Abdallah Twalipo, David Musuguri, Ernest Mwita Kiaro na Robert Mboma.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima,Septemba 18,mwaka 2007

No comments:

Powered by Blogger.