Header Ads

BABA WA TAIFA TUNAENDELEA KUKUENZI


Na Happiness Katabazi

MWALIMU Julias Nyerere Baba wa Taifa letu,leo tunaadhimisha miaka nane tangu ulipotutoka Oktoba 14,1999, na tukakupumzisha kwa amani katika Kijiji ulichozaliwa cha Butiama.

Tunaendelea kukuenzi baba japo kwa staili mbalimbali.Tukikuita baba kwa sababu wewe ni mwasisi wa taifa letu la Tanzania .Baba,ulikuwa Mwalimu wetu na hata leo hii inaendelea kutufundisha katika yale yote uliyotuusia.

Nakuomba baba uchungulie toka uliko utuangalie hapa duniani katika taifa lako la Tanzania uone tunavyokuenzi hususan katika yale mambo kuntu(masuala mazito) sana uliyotufundisha na kutuhusia.

Wasia wako uliukita katika mtindo wako wa maisha binafsi,uongozi wako uliotukuka,matamshi na matendo yako.Miongoni mwa mambo uliyotuusia yanahusu elimu.Ulipenda watu wote wapate elimu na ukatuambia kila apataye elimu afanye nini.

Baba, uliwahi kutuambia kwamba;aliyepata bahati ya kusoma na akapata elimu ni kama mtu ambaye kijiji kimempa chakula chote kilichopo ili ale ashibe,avuke ng’ambo akakiletee kijiji chote chakula ,na asipofanya hivyo akajenga kiburi ni sawa na msaliti.Baba tunakuenzi kwa hilo.

Tunakuenzi kuanzia katika suala la elimu, ambalo baba ulibobea katika hilo ukiwa mwalimu na mwanafalsafa. Ulitufundisha falsafa ya Elimu ya Kujitegemea, uliyoiasisi mwenyewe; ulituusia kwamba elimu itujengee akili za udadisi.Leo tunakuenzi baba kupuuza kuwa wadadisi na wabunifu.Shuleni tunasoma kwa kukariri ili tufaulu mitihani.Baba,hata udadisi wa kisiasa umepigwa marufuku katika taasisi za elimu ya juu, ili tuwe mbumbumbu,mazumbuku,mzungu wa reli,wasioweza kuhoji lolote.

Hukuishia hapo ukaanzisha elimu ya watu wazima. Tunakuenzi baba kwa mipango na mikakati lukuki ya elimu.Baba, kupitia mipango mbalimbali ya elimu kuanzia ya msingi (MMEM), sekondari (MMES) na kadhalika, tumeongeza idadi ya shule nchini hususan za sekondari ambazo baadhi ya wajukuu zako wanaziita eti sekondari za Lowassa,na walimu wake wanaitwa ni ‘voda fasta’ bila shaka utamkumbuka huyu kijana wako,ndiye waziri wetu mkuu wa sasa.

Baba ukichungulia huwezi kuamini wingi wa shule hizo. Si unakumbuka idadi ya kata katika nchi hii uliotuachia. Tumekuenzi kwa kufungua sekondari kwa kutumia kanuni ya kata moja shule moja kama ulivyoacha tumekusudia katika sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995. yaani baba tumeanzisha shule nyingi kwelikweli kiasi kwamba hazina walimu.

Hilo baba usidhani ni tatizo si afadhali tunazo shule angalau tupate mahali ambapo wajukuu zako watakaa wapige soga kuliko kukaa bure nyumbani. Alafu baba kama tusingezifungua si wagombea uongozi wetu watakosa kura katika uchaguzi ujao.

Baba usijali masuala ya kitaaluma, tunaenzi uanasiasa wako kwa kuanzisha shule za kisiasa. Hata zisipozalisha wataalam, si wawekezaji wataendelea kuja na wataalam wao.

Tunajitahidi kwa kuhakikisha angalau kila shule tuliyoianzisha ina mwalimu mmoja,tena huyo huyo ndio mkuu wa shule, wasaidizi wake viranja. Kwa kawaida huyu mwalimu akisafiri usiwe na wasiwasi, anakabidhi mafaili ya ofisi na majukumu yote ya kufundisha kidato cha kwanza hadi cha nne kwa kiranja mkuu.

Usiwe na wasiwasi baba, viranja wanaimudu kazi hiyo vizuri sana, hii ni katika kuakikisha tunaienzi vyema taaluma yako ya ualimu kwa kuifanya si taaluma tena bali kichwa cha mwenda wazimu ambacho hata asiyejua kushika wembe anaweza kukinyoa, kwani baba, lazima mtu ajue kusoma ndio awe mwalimu?

Tunakuenzi baba kwa kuendelea kusoma tukiwa watu wazima na katika siku zote za maisha yetu. Chungulia baba uone jinsi wengi wetu walivyofanikiwa kusoma ukubwani na kujipatia shahada za juu kabisa. Tangia uondoke baba idadi ya wanao wenye shahada za falsafa (PhD) imeongezeka kwa kasi. Usishangae baba tumewezaje hilo, siku hizi kuna shahada tunazipata kiurahiiisi kwenye mtandao. Wenyewe baba wanaziita za ‘on line’.

Kwahiyo tunakuenzi baba kwa kurahisisha mambo, tunatafuta wenzetu wenye uwezo kichwani tunawapa visenti kidogo wanatufanyia ‘assignments’ na kutuandikia thesis, tunawasilisha kwenye vyuo vya ughaibuni, kisha kufumba na kufumbua tunaitwa ‘madokita’. Hicho cheo baba tunakitumia vilivyo kukuenzi katika siasa , maana kitaaluma hatuwezi kukitumia, samahani baba hatuna ujuzi wowote katika nyanja za shahada tunazotunukiwa.

Kukuenzi kwetu hakuishii hapo baba. Si unakumbuka ulituachia vyuo vikuu. Tumekuenzi si tu kwa kuviboresha bali tumeongeza na vingine vingi baba. Kwa sasa baba tuna universities zisizopungua therathini(30). Zaidi baba tumekuenzi kwa kuongeza kwa kiasi kikubwa udahili katika vyuo hivyo.

Hiyo ni mojawapo ya mikakati tunayoitumia kukuenzi kwa kuuporomosha kwa kasi ya roketi ubora wa elimu ya juu uliyotuanzishia baba. Kwa mfano baba katika chuo kikuu cha mlimani, tumekuenzi kwa kukigeuza mfano wa sekondari kuubwa!

Nikufafanulie kidogo baba, chungulia baba uone jinsi tulivyokuenzi kwa kuboresha mazingira ya kazi ya wafanyakazi wa chuo hicho kwa kuwarundika waadhiri na maprofesa watatu watatu au wawili wawili karibu katika kila chumba kinachofanana ofisi japo ni vyumba vidogo vidogo baba. Si unafahamu baba kwamba ualimu ni wito na uadhiri ni wito mkuu na afterall hatuna fedha zilizobaki baada ya kununua mashangingi hata tuwajengee ofisi zenye ‘vipupwe’ na nafasi.

Baba, fedha zimetutindikia tunawalipa mishahara ambayo haina tofauti sana na posho ya siku nne ya mheshimiwa mmoja anayetuwakilisha bungeni. Tumekuenzi enzi baba kwa kutambua kuwa siku moja ya mbunge aliyesinzia kwenye kiti cha kuzunguka kule dodoma ina thamani sawa na wiki nzima ya mhadhiri anayesugua kichwa na kula vumbi la vitabu akitoka jasho kuwaelimisha wanao.

Lakini baba, nisiseme sana maana wahadiri wenyewe baadhi yao wameamua kukuenzi kwa kuweka chaki chini na kukimbilia kuomba kura za wananchi. Wana ka-msemo eti siasa inalipa vizuri hasa ukiweza kupata takrima ya ‘kuinvest’ humo. Wengine wao wanakuenzi kwa kukalia kimya makosa ya watawala.

Wanachelea kufungua midomo yao wasije wakaikosa ahadi ya maisha bora waliyoahidiwa na kijana wako, japo wengi wao hawana nyumba za kuishi tuankaa nao mitaani ‘uswazi’ au ‘madongo poromoka’. Tunashangaa baba,wanawezaje kukaa chini wakafikiri na kuandika mambo ya akili,ya kisomi wakiwa wanaishi huku uswahilini kwetu ambako kila mpangaji ufungulia redio yake.

Wameshindwa baba kuandika chochote cha maana, wanakuenzi kwa kuwaelezea kila siku mawazo yako uliyoandika,wakitoka hapo wanahubiri na kukariri tu nadharia na mawazo ya wasomi wenzao wa nchi za ughaibuni. Si kosa lao baba, hivyo ndivyo watawala wamewataka wawe labda wasije wakahatarisha maslahi ya wenye nacho.

Baba, kwa kushindwa kuwajengea wasomi wetu hawa nyumba za kuishi, hatuwezi kukulaumu wewe,maana enzi zako nyumba zilijengwa pale mlimani zilizowatosheleza waliokuwepo. Na kwa kuona mbali baba ulitenga eneo kubwa la mlima ule kwa ajili ya ujenzi wa baadaye, bila shaka wa vyumba vya mihadhara, ofisi, makazi ya wahadhiri na wanafunzi wao.

Sisi baba, tumeamua kukuenzi kwa kulitumia eneo hilo ulilotutengea kwa staili mbadala kabisaa! Tumewekeza baba kwa kutumia sehemu ya eneo hilo kuwapa wageni makaburu; hapana ni ndugu zetu wa sauzi, wanyonyaji; sio – ni wawekezaji, makupe; no! ni wajasiriamali, tumewapa wajenge maduka ya kisasa ya bei mabaya kwa ajili ya wenyenazo kufanya shoping na walalahoi kwenda kujionea mambo! Usishangae baba, katika maduka hayo miwani ya jua bei yake ni sawa na mshahara wa kima cha chini ongeza noti kadhaa!

Tunaendelea kukuenzi baba kwa kutojali tena mwanafunzi wa chuo kikuu anaishi wapi,ni mtu mzima atajua mwenyewe. Anasomasomaje ‘madesa’ au vitabu shauri yake, anakula au ‘anadeshi’,kalala pazuri au ‘kabebwa’ no bode keaz. Samahani baba hiyo misamiati mitatu hukutuachia,imetungwa na wasomi wenyewe kutokana na maisha magumu yanayowakabili kutokana na harakati za kukuenzi.

Madesa wanasema ni makaratasi ya kuokoteza yanayofanana na kile kilichomo kwenye vitabu wasivyoweza kuvipata; kudeshi baba ni kushinda bila kula nakokufanya msomi ili aweze kumudu uchangiaji wa gharama za elimu ya juu. Wanachangia baba kwa mujibu wa sera iliyotungwa na wale wanaokuenzi kwa vile uliwasomesha bure elimu bora,ukawalisha bure chakula bora, ukawapatia vitabu bora na walimu bora. Wanakuenzi baba kwa kutanguliza adjective bora kabla ya nomino.

Baba, kule Dodoma ulikotuambia viongozi wetu wahamie wakakuenzi kwa kukataa kwenda huko hadi leo,sasa tunapatumia kukuenzi kwa mtindo mpya. Tumeanzisha Chuo Kikuu kipya huko. Hatukupata shida ya majengo ya kuanzia, tumetumia yale yale ambayo waliyatelekeza uliowaagiza waame Magogoni waende Ugogoni.

Eeh, tumetumia na mojawapo ya majengo ya chama ambayo awali kilikataa kuyarejesha kwa umma baada ya kuanzishwa mfumo wa vyama ulivyotwambia visiwe utitiri,mpaka sasa havijawa utitiri baba, tunavyo kumi na saba tu japo vingi vina tatizo la utapiaruzuku.

Baba, ulituachia uhuru wa kutoa kauli na ukavifanya vyuo vikuu mahali huru pa kujieleza. Tunakuenzi baba kwa kuua moyo huo. Kila anpojitokeza anyethubutu kuwa jasiri kama wewe tunamnyamazisha ili wewe tu ubakie mwenye kuenziwa. Kuna mjukuu wako mmoja, labda humjui vizuri kwani ni mdogo sana. Tumemwekea breki ya kuongea kwa niaba ya wananchi katika chombo cha uwakilishi. Haikutosha baba,juzi tu alialikwa chuo kikuu,lakini tukafanikiwa kumdhibiti maana tuliona ana fikra huru kama zako tukakuenzi kwa kumkatalia kuingia chuoni. Chungulia baba umwone huyo kijana.

Vilevile katika uwanja huo huo wa elimu,tunaendelea kukuenzi kwa kufanya midahalo isiyo na tija. Tunatajataja jina la lako,tunakunywa maji ya kilimanjaro,tunagahawana posho,tayari tunakuwa tumekuenzi.

Baba ulituhusia pia tuwe na umoja wa kitaifa,watoto wa baba mmoja wasiokuwa na ubaguzi wa kidini wala kikabila.Baba ukasema katika karne ya 20,wanangu mnazungumzia ukabila,ukatuuliza iwapo tunaka kutambika?Tunakuenzi baba,hasa linapokuja suala la uchaguzi.

Ni hivi juzi tu tu limchagua Rais wa Awamu ya Nne,Jakaya Kikwete, bila wewe kuwepo.Tunakuenzi kwa kukataa ukabila, lakini wapo baadhi ya wanao wanaouendekeza.Baba unamkumbuka yule motto wako kipenzi Dk.Salim Ahmed Salim? Wapo waliompigia kumbo asigombee kiti cha urais kwa sababu ya asili yake, ngozi ya rangi yake.Eti yeye ni Mwarabu,eti alikuwa mwanachama wa Hizbu!

Pia yule mwanao Joseph Mungai ambaye ni waziri tangu enzi za utawala wako hadi sasa, naye ameambia yeye si Mtanzania ni ‘mkikuyu’, na aliambia hivyo baada ya kugombea nafasi ya NEC kupitia mkoa Iringa ambapo mwaka huu chama chako ulichokiasisi kinafanya uchaguzi mkuu.

Dhambi ya pili baba tumetenda,utusamehe na utuombee kama ulivyotuahidi kabla hujatutoka, kuwa unajua tungelia sana baada ya kifo chako,lakini kwamba utatuombea.

Vile vile baba ulituasa kwamba serikali haina dini,na kila mtu awe na uhuru wa kufuata dini anayoipenda.Kwamba dini kamwe isitutenganishe.Baba ulikuwa Mkatoliki mwaminifu, lakini uliwapenda na kuwaheshimu wanao Waislamu na hata wengine waliofikia wakakubatiza jina la Musa!

Baba mwaka huu tunakuenzi kwa kukwaruzana kidini.Tunabisaha juu ya Mahakama ya Kadhi na kunyoosheana vidole machini huku chama ulichokiasisi mwenyewe kikiwa ndicho kinachokonoa udini huu kwa kuwaahidi dada na kaka zetu wa Kiislamu kwamba kina sera ya kuanzisha Mahakama ya Kadhi.Tuombee baba,amani uliyotuachia tusiipoteze kwa kuanzisha taasisi ambazo hukuturithisha na ambazo ni hatari.

Baba katika suala la uchumi tunaendelea kukuenzi kwa kuuza kila raslimali uliyotuachia. Ahsante baba kwa kutuachia mali. Alhamdulilahi hatujaanza kutoana roho – yarabi kwa mali ulizoacha baba. Ila tumeziuza kisawasawa.
Baba zile nyumba ulizotuachia ukasema wakae humo watumishi wa umma tumeziuza na pesa tulizopata tukazitumia kuwapangishia viongozi wetu vyumba katika mahoteli makubwa. Si unaona mwenyewe tulivyo na akili.

Baba yale mabenki uliyotuachia tunaendelea kuyauza, viwanda tunaendelea kuvinadi, mashirika hatujaacha kuyapiga bei, mahoteli hatujachoka kuyabinafsisha na madini tuayatoa zawadi kwa marafiki zetu wa ughaibuni kwa njia ya mikataba yenye kamrabaha. Baba, katika miaka michache ijayo almasi,dhahabu,tanzanite,,bati, uranium na vito vingine vya thamani ulivyotuachia tutakuwa hatunavyo tena. Hizo zote ni harakati za kukuenzi maana ulituachia mali nyingi kiasi kwamba zinatulewesha.

Tunakuenzi baba hata katika suala zima la uongozi bora.Baba,unamkumbuka yule kijana wako uliyempenda sana kwa tabia yake ya utanashati na usafi wa mwili na roho,hata akaitwa Mr.Clean?Naye amekuenzi hivyo.

Amekuenzi Baba kwa kutuhumiwa kufanya Ikulu ni mahala pa ujasiriamali japo wewe ulimhusia kwamba Ikulu ni mahala patakatifu.Uliuliza baba, ikulu pana biashara gani?’ Swali lako .Baba kijana wako kakuenzi kwa kulijibu kwamba ikulu pana biashara ya kutumia dhamana ya ukuu wa nchi kujipatia mikopo bila kuulizwa ulizwa ili ujasiriamali.Tunakuenzi baba,kwa kuisigina vilivyo sheria ya Maadili ya Viongozi.Baba,kalianzisha kaka, wadogo zake unatarajia wafanyeje?

Na wadogo nao wameamua kukuenzi.Wewe baba ulituambia ,’watu safi katika nchi hii wapo chungu nzima’ utuwie radhi baba mpaka sasa hatujaweza kuwatambua.Ila angalau tumewatambua hao wengine.Tumekuenzi baba kwa kuunda timu ya mchezo wa ufisadi, inaitwa”The list of shame’ aka “Jk eleven’.Hii timu inakuenzi vizuri sana baba,kwa kuongeza harufu chafu uliyoisikia uliposema ‘kanchi kananuka rushwa!’. Siku hizi baba siyo kunuka tu, bali ka-nchi kamevunda ufisadi’ kuanzia sebuleni hadi jikoni.Yaani baba huwezi kuamini, uvundo umefika hadi kwenye jiko la uchumi(Benki Kuu ya Tanzania).

Baba ungekuwepo endapo wala rushwa wangetiwa hatiani na vyombo vya sheria ungeamuru wachapwe viboko wakati wakuingia gerezani na wakati wa kutoka ili wakawaonyeshe wake zao makovu ya bakora hizo.Lakini sasa hakuna wakuamuru hilo.

Tunakuenzi Baba, tukikumbuka ulitufundisha hata kutunga mashairi, mfano ni tunaposoma kile kitabu chako cha ‘Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania’.usibishe baba ebu soma shairi hili uone tunavyofuata nyanyo zako:

“Mkataba wa Buzwagi, alisaini Karamagi,
Umezua hoja nyingi,tena hoja za msingi
Kulikoni Karamagi,akaiuza Buzwagi
Mbona hanywi Konyagi,na wala havuti Bangi”?

Buzwagi unaijua baba;ni eneo moja lenye utajiri wa madini uliyotuachia, kijana wako Karamgi kawagawia wazungu kwa kusaini mkataba ambao ukisoma baba utalia machozi.

Baba tunazidi kukuenzi kwelikweli, hadi ndani ya chama ulichotuachia.Baba ulituambia chama kiwe na matawi imara.Tumekuenzi baba kwa kuimarisha matawi hayo., ila si kama yale matawi ya kizamani, tumeanzisha matawi yanayoendana na wakati.Nikutajie matawi hayo Baba japo machache?Haya…moja linaitwa,mtandao-maslahi,jingine mtandao-halisi, la tatu mtandao-matumaini, la nne mtandao-dhuluma—yako mengi baba.

Halafu Baba unajua tunakuenzije kuhusu suala la alama za chama?Baba uliturithisha jembe na nyundo ukasema kwa maana hiyo chama ni cha wakulima na wafanyakazi.

Lakini tumekuenzi Baba, kwa kugundua kwamba hizo alama haziendi na wakati.Hatujazifuta,ila tumekigeuza chama kuwa cha wenye uwezo ,wafanyabiashara na mafisadi.Baba, hakuna wa kukwambia kwamba hili si kweli.

Akikwambia hivyo muulize mweka hazina wa sasa wa chama ni mkulima au mfanyakazi?Je hayumo kwenye Jk eleven? Muulize nini kilitokea kuhusu ufisadi wakati wa uchaguzi ndani ya chama.

Baba , watoto wadogo ambao hakukuona,wanachanganywa sana juu ya sura yazo.Kuna sanamu za ajabu kabisa zinachongwa na kuwekwa mitaani sasa, hadi wengine wakubwa wanakaribia kuisahau sura yako halisi.Wahurumie hao baba, njaa zao zinawatuma vibaya.

Baba, niruhusu niwakumbushe wanao wote kwamba hatuwezi kujivunia wewe kuwa baba yetu na kusema kwamba tunakuenzi, wakati kile tunachokifanya ni kinyume cha mafundisho,wasia na imani yako.

Tuombee baba, ili mfumo wa elimu yetu ukuenzi,ili mfumo wa uchumi wetu nao ukuenzi na mfumo wa siasa ukuenzi.Kadhalika viongozi wetu wakuenzi kwa maneno yao,mawazo yao na matendo yao.

Baba ,viongozi wetu inabidi wakumbuke maneno ya Yesu Kristo aliyowaambia watu wa taifa la Uyahudi,kwamba “Hamjui kwamba mnaye baba mwingine,ninyi si watoto wa Ibrahim,ninyi ni watoto wa ibili,kwa kuwa ibilisi amekuwa mwongo na mnafiki tangu mwanzo,nanyi mnayatenda hayo hayo kama baba yenu”.

Sasa baba ,wanao tunapojivunia ubaba wako,baadhi ya yetu wanaye baba mwingine ambaye si wewe!Baba yao ni beberu(bepari aliyekomaa),kwani bepari amekuwa mnonyaji,tangu mwanzo hata leo hii,angali akinyonya kwa kutumia utandawazi,unafsishaji na kuendekeza masilahi binafsi.

Viongozi wetu wa leo mnamuenzi baba yupi?Baba Mungu alikuumba na ukiisha kuifanya kazi yake hapa kwetu,akakutwaa.Jina la Bwana lihimidiwe na aipumzishe roho yako mahali pema peponi.Amina.

0755 312859:katabazihappy@yahoo.com;www.katabazihappy.blogspot.com

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili , Oktoba 14, 2007

12 comments:

Anonymous said...

CCM na Serikali yake Ndio waseme kuwa wao ndio wanamuenzi baba wa Taifa kwa staili hiyo. then CCM inabidi waseme wako katika sera gani za uchumi>??? Je ubepari Uchura?? au Ujamaa Uchura au Unanzi wenye maslahi kwao?? maana uonaona kuwa hata Katiba ya Taifa inasema inchi inafuata siasa za ujamaa Kweli ndio Hivyo??? Au wanafuata ubepari uchura?? Nasema uchura kwasababu CCM hata wanacheza hawajui misingi yake na kufanya watu kama Makondoo vile.. Hivyo umesema kweli kabisa hivyo ndio hali ya Sasa huko Tanzania. CCM wanahiji kufanya na kuacha kuwadhiaki Watanzania maana yote mabaya ni yao kama wanataka kuwambia mazuri basi na Mabaya ni yao?? Hapa ndipo wamelifikisha Taifa letu.. Then WACCM wanalewa na utajiri wa rasimili za Taifa ndio maana wanakuwa kama vichaa vile.. CCM wasidhani kuwa wao ndio Wana haki pekee yao?? Siasa safi zipi?? CCM wanajijua Siasa safi?? au ni porojo tu??
Joshua Michael
Colorado Marekani

luihamu said...

Dada Katabazi mimi nimsomaji mzuri wa makala unayoandika katika Tanzania daima pamoja na blogu yako.unakaribishwa katika blogu ya rastafarian.Karibu dada Katabazi

Anonymous said...

hilo shairi lako kiboko. hii nimeipenda kwakweli.

Rashid Mkwinda said...

“Mkataba wa Buzwagi, alisaini Karamagi,
Umezua hoja nyingi,tena hoja za msingi
Kulikoni Karamagi,akaiuza Buzwagi
Mbona hanywi Konyagi,na wala havuti Bangi”?

Ni kweli usemayo, Mkataba ulio,
Wananchi wana kiliyo,kutwa wapiga miayo,

Mikataba idhuruyo,waikimbilia mbiyo,
Kisa walizwao,huishia kupiga mayoyo,
Wananchi washangaa hayo,sasa wako mikoani Mbio,

Kuzima kelele zao, Kisa wazomewao, eti mazuri wafanyayo.

Ni mengi yaliyo, bali hayana kimbilio, wananchi waliliayo, hayana matagemeo.

Ni miwili miaka yao, Mitano haijawa hiyo,Ni kilio ni kilio wananchi ni kilio.

Anonymous said...

Haya ni mimi John tena, wenye midomo chongeni zenu. Sasa huyu dada anaandika kuhusu Nyerere kuwa pale mlimani mabakuru wamejenga, tena maduka ya makubwa na vitu bei ya juu, dada acha ushamba, tunaenda na wakati, sasa wewe unataka tuwe na vioski vya soda au nini? namkubali sana Nyerere, lakini dada kwa hili umechemka, hatuwezi kukwepa wawekezaji... wenye midomo chongeni tena.
John

Anonymous said...

Bwana John, I totally agree with you, huyu dada leo kachemsha, she wants to take us back kwa Mwalimu Nyerere? Dada kila nchi kuna maskini na matajiri... John bado hupo Holland or Norway?
Phillip

Rashid Mkwinda said...

Tatizo la Ewe Bwana unaejiita John hutakiwa kuwa wazi na hivyo watu wanashindwa kukutembelea katika Blog yako inawezekana wewee unaandika pumba katika blogu yako hivyo unaona ukijiweka hadhatani tutachungulia uozo wako endelea kujificha lakini watu ashakujua wewe ni nani

Anonymous said...

John kama kweli hilo ni jina lako, basi sinajina jingine la kukupatia zaidi kukuita wewe ni mpuuzi, na mwenye akili za kuvuka barabara usigongwe na magari.
Tumeishagundua kwamba huo utumbo wako unaoandika kwenye blog hii, lengo lako ni kumkatisha tamaa dada happiness, asiendelee kuandika ukweli,ni hivi ushindwe na ulegee kiuno kwa jina la yesu.
Tunaimani na Happy kwamba ni mtu anayejiamini na kusimamia kile anachokiamini, kwahiyo hizo fikra zako za kipuuzi unafikiri zitamdhoofisha katabazi, ulie tu .Kwani anafanyakazi ya kuabarisha umma na umma umekua ukiheshimu na kuthamini mchango wake.Hivyo wewe endelea kubwabwaja lakini usiku utalala.
Wanaume waliokamilika hawana mambo ya kishenzi na kipuuzi kama yako unayoyafanya. Lumbana kwa hoja siyo ngonjera unazoandika.
Kosoa kwa hoja siyo kuandika porojo.Jiheshimu na uheshimu utu na taaluma za watu.
Usikurupuke kama mtu alishinda kutwa nzima akibeba box tupu.
Dada Happiness, songa mbele kwa maslahi ya taifa letu la Tanzania.

By Diana Mwasakyafyuka
Italia

Anonymous said...

John!
dada Happiness amekunyima nini?
Mbona unataka kumvavaa kama suruali yako mbovu uliyoiacha kijijini kwenu baada ya kuukana uraia wa Tz! Mbona wanaume wenzio hatuko hivyo? Usipende kuwa Mtumwa wa mawazo mpaka fikra, tuna wasiwasi na upeo wako wa kufikiri. Hebu tuambie bwamdogo wewe kale ka mshiko ka ndugu yako Karamagi na wewe uli kalamba nini? maana uko mstari wa mbele kukatetea kama kuku anayetaga, Una kiherehere kama mkojo wa asubuhi vile! Dada Happy usife moyo kabisa mdharau huyu FISADI: By Kiboko ya John

Anonymous said...

Hongera Happiness,
Blog yako ni nzuri na nimeitembelea na kusoma makala zote, kwakweli napenda kukupongeza hasa makala hii ya Baba Wa Taifa, ni nzuri kwani umegusa kila eneo.
Tunakuombea mungu akupe afya njema uendelee kutuabarisha umma wa watanzania hasa sisi tunaoishi nje ya nchi.
Wanawake sikuzote wamekuwa wakidharaulika mbele ya jamii kwamba ni watu dhaifu na mfano halisi ni huyu John, ambaye nimeona anaponda makala zako tena mbaya zaidi hatoi hoja mbadala, anaishia kupayuka.
Ni hivi Happiness songa mbele usirudi nyuma. Chonga kalamu barabara kwa maslahi ya umma wa watanzania, panapostahili kukosoa kosa,kukukemea kemea panapostahili kusifia sifia na shauri.
By.Godfrey Chami
London

Anonymous said...

Wewe John,
Licha ya kujinadi kwamba unaishi nje ya nchi na umekana uraia wa Tz, natilia shaka upeo wako wa kufikiri nisamehe katika hilo.
Na hilo limejidhiirisha katika maoni yako katika makala ya nyerere, hivi Happiness katika makala yake ile amepinga wawekezaji? hajapinga wawewekazaji.Happy alichomweleza Baba wa taifa katika makala yake kwamba eneo la Mlimani City kwamba wamepewa makaburu, sasa ni paragraph hipi imeonyesha kwamba amepinga watu hao kuwekeza. Acha upuuzi. Kwa taarifa yako kinachopingwa hapa nyumbani ni sera mbovu za uwekezaji na sheria za madini, hakuna hanayepinga wawekezaji ila watanzania wanataka sheria za sera hizo zirekebishwe ili ziweze kuleta manufaa kwa taifa.Kama wewe umetembea nchi mbalimbali na kusoma historia za nchi hizo baada ya kukaribisha wawekezaji mfano mzuri tembelea Dubai, ujionee walivyopata mafanikio ya kutokana na uwekezaji.Utabaini wawekezaji wanaokuja kuwekeza hapa Tanzania wengi wao ni wawekezaji uchwara, na wapo hapa kwaajili ya faida binafsi na si taifa letu.
Hivyo lumbana kwa hoja siyo umbeya wanaume hawapaswi kuwa hivyo.Tanzania ni yetu sote na itajengwa na watanzania wenyewe, sasa wewe kama utakuwa ukiponda makala za happiness, bila ya wewe kutumia elimu yako kuandika makala zenye hoja mbadala ambazo wewe unaamini zitaleta tija kwa taifa letu ,na kuzituma kwenye vyombo vya habari vya hapa nchini zikachapishwa wananchi na wataalam wakazisoma na kuzichambua kwa kina wanaweza kujifunza kutoka kwako. Lakini kitendo cha wewe ambaye nimeona maoni yako kwenye makala za huyu dada kwamba umejitambulisha kuwa wewe ni mtanzania uliyekana uraia wa Tz,itakuwa haitusaidi sisi watanzania, sana sana tutaendelea kukuchukilia wewe punguani, mhuni na juha fulani.
George Damas
Tanzania

Anonymous said...

Dada Happy, vipi kuhusu Mahakama ya Kadhi? mbona ujasema lolote? au sababu ni Mtikila kasema hivyo nini? nadhani issue ya Mahakama ya kadhi ni muhimu sana kuijadili, lakini naona kimya, kama ingekuwa Zitto Kabwe, basi ungekuwa umeishaandika... chao,
John

Powered by Blogger.