Header Ads

CUF KUBALINI YAISHE

Na Happiness Katabazi

BABA wa Taifa Julias Kambarage Nyerere aliwahi kusema kwamba ‘ukweli una tabia moja nzuri sana.Haujali mkubwa wala mdogo , haujali adui wala rafiki’.

Hivi karibuni Chama cha Wananchi (CUF) kimeingia kwenye malumbano na Chama cha Mapinduzi (CCM) kuhusu namna ya utekelezaji wa makubaliano ya rasimu ya mwafaka wa tatu.

Sasa CCM imesema majadiliano ya mwafaka yaliyochukua miezi 14 ya pelekewe kwa wananchi ili wapige kura za maoni .CUF kwa upande wake inapinga na kusema kuwa hivyo sivyo walivyokubaliana na kwamba walichokubaliana ni mwafaka kutiwa saini.

Awali ya yote, wananchi hawajui kwa kina kanuni za majadiliano hayo wala ajenda kwani miezi 14 vyama hivyo viwili vilifanya majadilino hayo kuwa siri kubwa baina yao.

Na vyama hivyo vilichangamkia mazungumzo hayo kwasababu walipewa donge nono na wafadhili.Kuna mambo kadhaa ya msingi yanayojitokeza kutokana na malumbano hayo.

Moja,mwafaka huu uliotegemewa kutiwa saini kati ya CCM na CUF baada ya mwafaka wa mwaka 1995 na 2000 kushindwa.Mara zote vyama vya upinzani vilikishauri Chama cha CUF kutoshiriki kwenye mazungumzo ya mwafaka peke yake.

Vilipendekeza kwamba vyama vyote vya upinzani viunde timu moja ya kuikabili CCM kwenye mazungumzo ya mwafaka.CUF ilikataa hoja hiyo ikisema kwamba mazungumzo hayo hayavihusu hivyo vyama vingine kwakuwa CUF ina ajenda binafsi isiyo vihusu vyama hivyo vingine kwenye mazungumzo ya mwafaka.

Matokeo yamekuwa kwamba CCM iliihadaa CUF katika mwafaka wa kwanza, ikarudia tena kuihadaa katika mwafaka wa pili na sasa ama kwa hakika hata huu mwafaka wa tatu yawezekana usipatikane.

Sasa imefika wakati tunaweza kuamini kwamba CUF ni CCM B. Kama CUF siyo CCM B, kwanini inaruhusu kuibiwa kwa kura zake ili ishirikishwe kwenye serikali shirikishi?.Na kwa nini mara zote imekuwa ikikataa vyama vingine vya upinzani visishirikishwe kwenye mazungumzo ya mwafaka isipokuwa chama hicho pekee cha upinzani?

Kwa yoyote anayejua siasa za Zanzibar ni wazi sasa kwamba CUF imekata tamaa ya kupata madaraka na njaa yake ya madaraka imekuwa kali mno.Baadhi ya viongozi wako tayari kupewa Umakamu wa rais bandia ili mradi wajulikane nao wapo serikalini.

Ukiliangalia hili kwa undani utaona kwamba miafaka yote mitatu imelenga maslahi binafsi ya baadhi ya viongozi wa CUF wanaotamani uongozi kwa gharama yoyote ile kuliko kutanguliza maslahi ya wananchi wenzetu wa Zanzibar ambao ndiyo wanateswa moja kwa moja na mpasuko huo .Kumbe wenzetu hawapiganii mageuzi bali vyeo?

Tunajua kwamba baada ya kumalizika kwa mchakato wa mwafaka wa pili , Maalim Seif Sharif Hamad alirejeshewa kiinua mgongo chake na marupurupu ya Waziri Kiongozi Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Sasa katika mwafaka huu Seif anataka kuwa Makamu wa Rais wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar?Kama ni hivyo Wanzanzibar waamue kusuka au kunyoa .

Nilazima Wazanzibar waamke na kuibua chama kitakacho jipambanua kama nguvu ya tatu Zanzibar.Wakati CUF inajigeuza CCM B lazima harakati za mageuzi ziendelee kupitia vyama vingine .

Chaguzi zote CUF imekuwa ikilalamika kuibiwa kura na CCM sasa CUF ina ng’ang’ania kuingia kwenye serikali kwa stahili hii itailetea tija gani?.Sote tunakumbuka ni CUF hii hii muda mfupi baada ya kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi wa mwaka 2005 ilitangaza haitambui urais wa Rais Aman Abeid Karume kwakuwa umetokana na wizi wa kura na hadi sasa haijafuta kauli hiyo.

Kitendo cha CUF kung’ang’ania mwafaka unaokidharirisha chama hicho na kuchora taswira kwamba CCM ndiyo itakayoingiza chama hicho madarakani na siyo kura za wananchi ni kitendo cha usaliti kwa wananchi waliokuwa wanakiunga na wanaoendelea kukiunga mkono.

Ikumbukwe kwamba mamlaka ya kisiasa Zanzibar yanatoka kwa umma wa wananchi wa Zanzibar na wala siyo kwenye mikoba ya CCM.Kwa hiyo CUF kama inafikiri CCM ndiyo itawaingiza madarakani, nasema hivi imepotea njia tena sana tu.

CUF haina mbadala, ila lazima kurudi kwenye majadiliano, kwasababu miezi 14 ilikubali kulala kwenye kitanda kimoja cha mwafaka na CCM , sasa mtoto amezaliwa CCM inamwambia CUF wamtoe mtoto nje ili ndugu ,jamaa na marafiki wamfahamu mtoto huyo ,CUF ina kataa inang’ang’ania mtoto abaki ndani .Je CUF ni kwasababu ina uhakika kwamba mtoto aliyezaliwa ni mwanaharamu?

Kwa nyakati tofauti wiki iliyopita Mwenyekiti wa (CCM) Rais Jakaya Kikwete na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba walitueleza mazungumzo hayo yaliyochukua miezi 14 na kwa mujibu wa maelezo yao.

Kumbe walichokuwa wanazungumzia kwa kipindi chote hicho ni jinsi ya vyama vyao kugawana madaraka katika serikali iliyopo hivi sasa, badala ya kuzungumzia wizi wa kura usije tokea Zanzibar.

Kwa hiyo, suala la kwenda kwa wananchi binafsi naona ni la msingi, kwasababu linatupeleka mbele kidemokrasia, kwa kuwa ni haki ya wananchi kuulizwa kauli yao kabla ya kufanyika maamuzi mazito yanayohusu taifa lao.

Naamini kabisa kwamba kule Zanzíbar kuna Wazanzibar ambao si wanachama wa chama chote kile cha siasa lakini pia kuna wananchi wengine siyo wanachama wa CCM wala CUF ni wanachama wa vyama vingine vya siasa.

Hivyo na sisitiza zoezi la upigaji wa kura za maoni likifanyika kama lilivyokusudiwa,litaleta maslahi kwa wananchi, kuliko masilahi ya vyama hivi viwili.

Ieleweke wazi kwamba Tanzania Bara na Visiwani si mali ya wanasiasa, bali ni mali ya wananchi wote hivyo tunataka kuona endapo maoni ya wananchi yatatolewa,yaheshimiwe kwa maslahi ya wananchi wa pande hizi mbili za muungano.

Umoja ni nguvu ,wabinafsi ni adui zetu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano ,April 9 mwaka 2008

No comments:

Powered by Blogger.