Header Ads

NCCR-Mageuzi imestahimili mawimbi ya kisiasa-Mbatia



MWENYEKITI wa Chama NCCR-Mageuzi, James Mbatia, anasema kutokana na kurekebishwa kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kutungwa kwa sheria Na. 5 ya mwaka 1992 na sheria nyingine zinazoruhusu kuundwa kwa vyama vingi vya siasa nchini, taifa letu limeshuhudia kuibuka kwa vyama ambavyo kwa kiasi fulani vimeleta changamoto na kuchochea maendeleo katika ngazi za jamii ungana na Mwandishi Wetu ,Happiness Katabazi , ambaye alifanya naye mahojiano na kiongozi hivi karibuni.

James Mbatia anasema kutokana na uamuzi huo, vyama 13 vilivyopata usajili wa kudumu kutoka kwa Msajili wa Vyama ni pamoja na Chama Cha Mapinduzi (CCM), National Convetion for Construction and Reform – Mageuzi (NCCR-Mageuzi), Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Civic United Front (CUF) na United Democratic Party (UDP).

Vyama vingine vilikuwa ni TADEA, NRA, UMD, Tanzania Labour Party (TLP), UPDP, PONA na Tanzania Peoples Party (TPP); vyama vingine viliendelea kuandikishwa na kupata usajili wa kudumu baadaye na kujiunga rasmi kwenye mchakato huo wa kisiasa.

Anasema licha ya uchanga wa vyama vya siasa vilivyoundwa kufuatia kutungwa kwa sheria hiyo, chama kikongwe na kinachotawala, Chama cha Mapinduzi ambacho kimekuwa na historia ndefu ya kutoka mwaka 1954, kimekiri kwa nyakati tofauti kutikiswa na chagamoto zilizotokana na vyama hivi vichanga.

Leo hii tunapotafakari kutimia kwa miaka 15 baada ya kuruhusiwa kwa mfumo huo demokrasia ya vyama vingi nchini Tanzania, ni lazima kama wananchi wa taifa hili kuangalia kwa makini tulikotoka, kuanzia enzi za Uhuru chini ya vyama vingi, kufutwa kwa mfumo huo na kuingizwa kwenye mfumo wa utawala wa chama kimoja na baadaye kurejea tena kwenye mfumo huu.

“Historia ni ndefu, na matukio muhimu yaliyotokea katika kipindi hicho ni mengi, lakini lililo la umuhimu wa kipekee na swali la msingi la kujiuliza ni Je, mfumo huu umetimiza kwa kiasi gani matarajio ya watanzania ambao licha ya asilimia 80 kukataa mfumo huo lakini serikali ikaamua kuufuata”anasema James Mbatia.

Anasema kumetokea matukio kadhaa katika historia ya mfumo huu kati ya Julai 1992 na Oktoba 1995 ambapo katika uchaguzi wa kwanza uliofanyika 1993, CCM ilishinda kwa asilimia 97 kwenye kinyang’anyiro cha kutafuta wenyeviti wa vitongoji, vijiji na wajumbe wa serikali za vijiji, chama hicho kiliendelea kuvinyanyasa vyama vingine hadi mwishoni mwa 1995.

Aidha Oktoba 1994, kulikuwa na uchaguzi wa viongozi wa serikali za mitaa kwa maana ya madiwani ambapo kati ya nafasi 2,411 zilizokuwepo, ni nafasi 1,226 zilizoshindaniwa na vyama mbalimbali kutokana na nafasi zingine kunyakuliwa na wagombea wa CCM bila ya kupingwa na mwisho CCM ikajikusanyia viti 2,336 huku vyama vya upinzani vikiambulia viti 75 sawa na asilimia 3.11.

Oktoba mwaka 1995, uchaguzi mkuu wa kwanza uliendeshwa nchini kwa mara ya kwanza na vyama vingi vikashiriki na kupata matokeo kama ifuatavyo kwenye uchaguzi wa Rais wa Jamhuri; CCM 61.96%, NCCR – Mageuzi 27.8%, CUF 6.4% na UDP 4.0%; hii ni kutokana na kura 6,512,745 zilizopigwa.

Na katika uchaguzi wa wabunge jumla ya vyama siasa 13 vilishiriki kuwania kura 6,440,913 zilizopigwa na kupata matokeo kama ifuatavyo; CCM 59.22%, NCCR-Mageuzi 21.83%, CHADEMA 6.16%, CUF 5.02%, UDP 3.32%, TADEA 1.19%, NRA 0.94%, UMD 0.64%, TLP 0.41%, NLD 0.41%, UPDP 0.31%, PONA 0.28% na TPP 0.24%.

Anaeleza kuwa kwa vyovyote vile kutokana na matokeo hayo, chama cha NCCR-Mageuzi kilionekana dhahiri kuwa na ushawishi mkubwa miongoni mwa wapiga kura na kilitoa changamoto kubwa katika siasa na mfumo mpya wa vyama vingi vya siasa nchini; changamoto ambayo miaka takriban 15 baadaye imeonekana kufifia na kukosa matumaini makubwa.

“Nakumbuka tukio moja nililolishuhudia wakati wa kampeni hizo ambazo wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanasema kuwa endapo Rais wa kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Julius Nyerere, asingelichukua hatua ya kukisaidia CCM katika kampeni zake, basi leo historia ingekuwa inasema mambo mengine,” anasema Mbatia.

Mbatia anasema ndicho kipindi ambacho mgombea urais kwa tiketi ya NCCR-Mageuzi, Augustine Mrema, alikuwa ameingia kwenye nyoyo za watanzania kwa kiwango kikubwa nami nilishuhudia hilo kwenye mji mdogo wa Shirati wilayani Tarime, wakati mashabiki na wanachama wa chama hicho walivyojitokeza bila ya woga kumpokea Nyerere wakiwa na bendera na mavazi rasmi ya NCCR-Mageuzi.

“Hakukuwepo na woga tena, walikuwa wakikimbia pande zote mbili za barabara wakiwa na bendera na mabango yanayoonyesha kuwa hawamtaki mgombea wa CCM, Benjamin Mkapa na Nyerere mwenyewe na kufurika kwenye uwanja wa Obwere kumdhihirishia Nyerere kuwa chama chake kimewachosha’ anasema.

Aidha anasema baada ya uchaguzi, chama hicho kilichoasisiwa na Mabere Marando na ambacho kilichoonekana kuwa chama mbadala kwa CCM kilighubikwa na mtafaruku uliopelekea kusambaratika kwa viongozi wake waandamizi na kujikuta kikiwa njia panda kisiasa, jinamizi ambalo licha ya kudhibitisha uongozi uliopo wa chama hicho limeacha kovu kubwa la kisiasa nchini.

Matukio, kupanda na kuporomoka kwa NCCR-Mageuzi katika ulingo wa kiasiasa ni changamoto kwa viongozi wa vyama mbalimbali vya kisiasa nchini, ingawaje yeye binafsi na wanachama na wapenzi wa NCCR , chama hicho kimestahimili mawimbi ya kisiasa na kiko imara zaidi ya kipindi cha nyuma.

Hata hivyo anasema Watanzania ambao walikuwa na matumaini makubwa na mfumo wa vyama vingi, kwa kiasi fulani wameanza kupoteza imani kwa vyama hivyo na walishuhudia wimbi kubwa la wanachama mahiri waliokuwa kwenye upinzani wakikimbilia tena kurejea CCM.

Wanachama na viongozi hawa kwa mujibu wa kiongozi mwandamizi wa NCCR-Mageuzi, Dk. Sengondo Mvungi, wamesahau au hawajui maana ya chama cha kisiasa na ndiyo maana wamekosa misimamo na kuwa ‘malaya’ wa kisiasa.

Itakumbukwa kwamba kwenye semina ya wajumbe wa halmashauri mjumbe akiwasilisha mada kweye semina ya wajumbe wa halmashauri kuu ya chama hicho kwenye hoteli ya Bahari Beach Dar es Salaam mwaka 2006, Dk. Mvungi alisema kuwa chama cha kisiasa ni mjumuiko wa hiari wa wananchi wenye mtizamo mmoja wa kiitikadi ya kisiasa wenye nia ya kujenga hoja ndani ya jamii ili kupata ridhaa ya uongozi wa jamii kwa misingi na malengo ya itikadi yao.

Kwamba chama cha siasa huundwa kwa hiari ya wanachama bila ya shuruti, hivyo wanachama waliobakia ndani ya chama hicho ni wale wanaotekeleza mtazamo wao na hawayumbishwi na matakwa ya viongozi.

Mrema alipofarakana na Marando na baadaye akakihama chama hicho, wanachama wengi walimfuata Mrema na kujiunga na chama cha TLP bila ya kubaini na kukubaliana na itikadi ya chama hicho, matokeo yake tumeshuhudia wanachama hao wakikihama tena TLP na kujiunga na vyama vingine au kurejea CCM.

Aidha kuhama kwa Mrema, kuliangaliwa na baadhi ya watanzania kama mwisho wa NCCR-Mageuzi, lakini chama hicho kikastahimili matokeo ya mtafaruku huo na kuendelea kufanya uchaguzi mkuu ndani ya chama ambapo Mbatia alimshinda muasisi wa chama hicho kwenye uchaguzi wa kidemokrasia.

“NCCR-Mageuzi chini uongozi wa wangu imeendelea kughubikwa na matatizo mbalimbali ndani na nje ya chama, matatizo ambayo kwa kiasi fulani yameonyesha ukomavu wa kisiasa wa chama hicho ukilinganisha na vyama vingine,” anasema.

Chama hiki cho kinaongozwa kwa kufuata itikadi ya demokrasia ya kijamii ambayo lengo lake ni ujenzi wa jamii yenye uhuru, haki za binadamu, usawa na ustawi wa jamii na inayokubali kutegemeana kwa binadamu katika msingi wa mmoja kwa wote na wote kwa mmoja kimeweza kujiendesha bila ya kutegemea ruzuku toka serikali toka mwaka 2000 hadi leo.

Kutokana na mtafaruku uliokikumba, chama hicho kilishindwa kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2000 na kuambulia mbunge mmoja, Gulam Hussein Kiffu, toka jimbo la Kigoma Kusini ambaye hata hivyo aliondolewa katika nafasi hiyo baada ya kupingwa kwa matokeo hayo mahamakani na hivyo kukosa uhalali wa kupatiwa ruzuku na serikali.

“NCCR- Mageuzi imeweza kuweka historia ya kudai mabadiliko ya katiba wakati huo kikundi cha wanaharakati, tulifanikiwa na serikali ikaruhusu mfumo huo, lakini pia tuna historia ya kuwa na mtandao mkubwa nchini baada ya uchaguzi mkuu wa kwanza 1995”. Anasema Mbatia na kuongeza kuwa chama chake ndicho chama pekee kilichoweza kuendesha chaguzi za kidemokrasia ndani ya chama kisheria.

Mbatia anasema hali ya vyama vya upinzani nchini bado inafanana na hali ndani ya CCM ambapo kiongozi wa chama haruhusu kushindana na wanachama wengine wakati wa uchaguzi mkuu, hali ambayo inadhoofisha demokrasia na kuendekeza udumishwaji wa fikra za baadhi ya watu.

Chama hicho kikongwe, pia kimeweza kuandika historia ya kuwa chama cha kwanza cha upinzani kutoa mbunge, Mabere Marando, kuwakilisha kwenye bunge la Afrika Mashariki huku kikiwa kimetumia vizuri michango ya wanachama wake na kununua rasilimali nyingi za kudumu kwenye maeneo mbalimbali nchini.

“Bila ya ruzuku ya serikali, chama chetu kimeweza kutumia michango ya wanachama kuendesha mikutano mikuu ndani ya chama, kampeni kwenye chaguzi mbalimbali, tumenunua magari kadhaa na kununua majengo kwenye wilaya mbalimbali nchini likiwemo jengo la kisasa la ofisi za makao makuu na kununua ardhi kwa ajili ya kujenga chuo kikuu,” anasema Mbatia.

Akizungumzia changamoto kubwa zilizokikabili chama hicho kipindi cha uongozi wake, Mbatia anaeleza kuwa alipata wakati mgumu sana wakati NCCR-Mageuzi kilipoamua kuwawekea pingamizi wagombea wa CUF kwenye uchaguzi wa marudio kwenye mikoa ya Pemba ambapo wananchi walikihukumu chama hicho kuwa ni wakala wa CCM.

Anasema kuwa mbele ya sheria, vyama vyote ni sawa na vyote vinawania kupata ridhaa ya kuongoza na hakuna chama chochote chenye ubia na chama kingine, hivyo kwa kuweka pingamizi dhidi ya wagombea wa CUF, NCCR-Mageuzi ilikuwa ikitekeleza haki yake ya kikatiba na kisheria na kwamba chama hicho kilikuwa na haki zote za kisheria kuwafanya hivyo.

“CUF waliwahi kumuwekea pingamizi mgombea wetu kwenye uchaguzi wa kule Kagera, wananchi hawakulalamika, na hata wakati walipomzuia Mhe. Naila Jidawi kugombea urais wa Zanzibar kupitia chama chetu pia watu walinyamaza, lakini sisi tulipotekeleza wajibu wetu wa kikatiba kuwawekea wagombea wao pingamizi basi tukaonekana wanaCCM, huu ni upuuzi!”. Amesisitiza Mbatia.

Kiongozi huyo amesema kuwa Tanzania ni ya watanzania wote ya vyama vyote, hakuna ngome ya chama Fulani kwasababu vyama vyote vina haki mbele ya sheria na kikatiba hivyo dhana ya kwamba Zanzibar ni ngome ya CCM na CUF pekee inadumaza demokrasia ya vyama vingi na haistahili kuendekezwa.

Licha ya CCM kuhodhi rasilimali nyingi zilizochangiwa na watanzania wote na kutumia fursa ya kuwepo madarakani kwa kipindi kirefu kuvinyanyasa vyama vya upinzani, lakini Mbatia anaamini kuwa mageuzi ya kisiasa yanawezekana kutokana na nguvu za wananchi endapo watazijua haki zao na kusimama kidete kuzidai kwa kujiunga na vyama vya upinzani na kuvipatia nguvu na kutokana na hilo chama chake kimefanya marekebisho kadhaa kwenye katiba yake ya 1992 ili kukiwezesha kujiendesha kisayansi zaidi.

Wananchi wanavikataa vyama vya upinzani nyakati za uchaguzi kutokana na rushwa na vitisho na kutokana na dola kutumiwa na chama hicho tawala lakini mara baada ya uchaguzi wanaanza kukilaani chama hicho kutokana na ubadhirifu na kuingia mikataba mibovu na kutumia vibaya mamlaka zake.

“CCM inatumia mabavu kuvinyanyasa vyama vya upinzani, inatumia vitisho kuwanyakua wanachama wetu, kuna mfano niloutoa wa Mkuu wa wilaya, ya Sumbawanga, C.F.Mwali, alivyotumia madaraka yake vibaya na kupokea vitendea kazi vya NCCR- Mageuzi na kuvikabidhi rasmi kwa Katibu wa CCM kwa barua yenye Kumb. Na. SUMB/SS.20/1 ya 11/11/2003”. Amesema na kuongeza kuwa watanzania wameshuhudia jinsi marais ambao ni viongozi wa CCM wanavyokusanya bendera na mali nyingine za vyama na kuvirundika kwenye ofisi za CCM.

Licha ya vyama vya upinzani kukosa umaarufu uliotarajiwa kutokana na uongozi mbovu kwenye baadhi ya vyama, lakini kumekuwepo na malalamiko mengi kuhusu matumizi ya nguvu za dola katika kuvidhoofisha vyama hivi, hii imetumika mara kadhaa wakati viongozi wa vyama hivyo kikiwemo NCCR-Mageuzi walipopigwa na polisi wakati wa maandamano.

Upungufu wa kutokuwepo kwa katiba mpya pia ni dosari kwasababu mara baada ya madadiliko ya kisiasa kuridhiwa, kulitakiwa kuwepo na katiba mpya ambayo inakidhi matakwa na hali ya kisiasa.

Marekebisho ya katiba yaliyofanywa yalifanywa na bunge lililokuwa limesheheni wabunge wa CCM, hivyo kukubalika kwake na wadau wengine kisiasa ni vigumu kwasababu bunge halina mamlaka ya kuunda katiba kwavile linakuwepo kutokana na katiba iliyotungwa na wadau wote.

Kwa mujibu wa mwanasheria mmoja ambaye sina haja ya kutaja jina lake, Katiba yoyote katika nchi inayotawaliwa kidemokrasia hufaqnyiwa mabadiliko kutokana na mabadiliko ya kiuchumi au kisiasa na sio vinginevyo; hivyo kutokana na badiliko kuu la mfumo wa kisiasa tulilopitia kuna haja kubwa ya kuwepo kwa katiba mpya inayokidhi haja za hali ya sasa ya kisiasa na kiuchumi.

Mfano mmoja wa mabadiliko ya kikatiba kutokana na hali ya kiuchumi ni kuwepo na baadhi ya sheria ambazo zinatoza faini ya sh.200, katika mazingira ya sasa kama mtuhumiwa atatozwa faini ya kiwango hicho kitasaidia nini.

Katika hili, NCCR-Mageuzi inadai kuwepo kwa katiba mpya isiyowekewa viraka ili iweze kukidhi mahitaji na matakwa ya mfumo uliopo, kama chama tawala kitaendelea kung’ang’ania katiba iliyopo basi itashuhudia vyama vya upinzani vikifa kifo vya mende na kurejesha nchi kwenye mfumo wa chama kimoja.

Kuhusu matarajio ya baadaye ya chama, James Mbatia anasema kuwa NCCR-Mageuzi ni chama pekee nchini kilichoandaa Mpango Mkakati wa chama cha umma kwa ajili ya mageuzi ya kidemokrasia nchini Tanzania, mpango ambao umeanza kutekelezwa toka mwaka 2006 kufikia lengo lake 2010 na kwamba mpango huo umekuwa ukiendelea kutekelezwa kama ulivyopangwa.

0755 312859
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano Julai 18,2007

3 comments:

Anonymous said...

Hii imetulia dada Happy! Heko kaka Mbatia! Vyama vya Upinzani kaza kamba ipo siku watanzania wata tambua haki zao katika siasa na Demokrasia, uchumi na kijamii!

Mungu bariki Tanzania, Mungu vibariki Vyama vya Upinzani Tanzania! Amena.

Innocent Kasyate said...

Hongera sana dada Happyness, nafikiri hizi makala zinatuonesha hali halisi nchini mwetu.
Keep it up with vigour, wenye akili tunaelewa na kutambua mchango wa wapinzani.
Bila watu kama wewe, hatutajua ni nini kinaendelea.
Kazi nzuri, nimeikubali..

Anonymous said...

Tunahitaji viongozi waliotulia na wenye kuipenda nchi yao, kwa kuweka maslahi ya taifa mbele kama Mbatia. Tuko pamoja.

Powered by Blogger.