Header Ads

Tukubali, si kila mtu anafaa kuwa kiongozi



Na Happiness Katabazi

KWA muda mrefu miongoni mwa wasomi na wananchi wa kawaida wamekuwa na mawazo tofauti kuhusu viongozi wanapatikanaje na ni hasa anastahili kuwa kiongozi.

Wapo wanaoamini kwamba uongozi ni karama au kipaji anachozaliwa nacho mtu, lakini kuna wengine wanaamini mtu anaweza kufundishwa kuwa kiongozi.

Kwa upande mwingine wapo wanaoamini kwamba akiwa na sifa za kuzaliwa na akapewa mafunzo ya uongozi huyo ndiye kiongozi anayefaa.
Lakini wote hawa hikubaliana jambo moja kwamba sikila mtu hata asiyekuwa na sifa anaweza kuwa kiongozi. Kimsingi kiongozi lazima awe na sifa zinastahili ikiwa ni pamoja na uelewa wa mambo, maono, awe ni mfano bora kwa wanaowaongoza na asiyetanguliza maslahi yake binafsi kabla ya awali anaowaongoza na kadhalika.

Dunia imebahatika kupata viongozi wenye sifa za namna hii na mifano hao viongozi si ya kutafuta kwa maana ni wengi. Kule Afrika Kusini, kulikuwa na Nelson Mandela, alikuwa na uelewa wa mambo na msomi wa hali ya juu alitanguliza maslahi ya watu wa taifa lake weupe kwa weusi hata akafungwa gerezani miaka 27 kwa sababu hiyo.

Waliopata fursa ya kuisoma hotuba yake aliyoitoa mwaka 1964 kabla ya kuingizwa gerezani alisema hivi. :” My life time I have dedicated my self to this struggle of the Afrivan people. There fought again in black domination, I have ideal of decratic and free society in which al persons live together in hormony and with equal opputunities.
“It is an ideal which hope to live for and achive.But if I needs be, it is an ideal for which I am prepares to die.” mwisho wa nukuu.
Tunaweza kuchukua mfano wa Alexander The Great, aliyeishi kati ya mwaka 356-323, ambaye wakati fulani akiwa kwenye mapambano na vikosi vyake alikataa kunywa maji kidogo yaliyokuwepo kwa sababu yasingewatosha yeye na na askari wake na akaamuru vikosi visonge mbele katika mstari wa mapambano na askari wake walimtii baada ya kuona ana moyo wa kutanguliza maslahi ya watu wake badala ya maslahi yake binafsi.
Sasa tukirejea Tanzania tunaweza kumtaja Baba wa Taifa Julius Nyerere, ambaye aliipenda watu na taifa lake na hata muda mfupi ya kuaga dunia alitamka wazi atawaombea wananchi wa taifa hili kwa mwenyezi mungu.

Vile vile Nyerere aliwahi kusema Ikulu ni mahali patakatifu na pana mzigo mzito wa kuwatumikia wananchi waliona matatizo mbalimbali kama umaskini na kadhalika.

Nyerere alikuwa msomi aliyebobea na mwenye shahada kadhaa za vyuo vikuu, mwenye maono na mwenye msimamo dhabiti katika yale aliyoyaamini. Kiongozi huyu aliyeweza kuibua viongozi wengine wenye sifa kama za kwake na pengine ni za kipekee mathalani marehemu Moringe Sokoine, ambaye aliwahi kuwa Waziri Mkuu wa nchi hii.

Mwalimu alifikia hatua ya kuwafunza watu uongozi akijua kwamba anatengeneza uongozi wa baadaye wa taifa lake kwa bahati wanafunzi wake wengi (kwa leo sitawataja ila wanajijua), wamesaliti mafunzo aliyowapa. Taifa letu la Tanzania lilipata bahati kubwa wakati wa uongozi wa Nyerere, viongozi waliheshimika ndani na nje ya nchi.

Waliheshimika kwa sababu walijiheshimu, walifuata maadili, walikuwa na moyo wazalendo na kutanguliza maslahi ya taifa mbele na hawakuwa wabinafsi. Viongozi hawa walipokuwa wakitamka jambo au kutoa maelekezo kwa watendakazi chini yao, wananchi kwa ujumla walisikilizwa na maelekezo yalikuwa yakitekelezwa bila kupuuzwa.

Leo hii viongozi wetu wanatoa maelekezo wanaishiwa kukosolewa na wananchi na watalaamu mbalimbali.

Enzi hizo lilipotangazwa Azimio la Arusha, Musoma na Nyerere taifa zima lilizima na kuitikia wito wa kiongozi muda mfupi na utekelezaji ulioneka hadharani.

Lakini kama alivyoimba mwanamuziki maarufu wa muziki wa kizazi kipya Lady J Dee, ‘Siku hazigandi’, enzi za uongozi na viongozi walio na uwezo wa kutupeleka kule kunakostahili hivi leo zinaoneka kama zimetoweka.
Leo hii sifa na vigezo vya mtu kuchaguliwa kuwa kiongozi si tena zile sifa njema, taifa hili sasa linashuhudia watu wakipata uongozi kwa sababu ya mahusiano yao na watu fulani wenye sauti katika jamii.

Mifano si ya kutafuta viongozi wetu wa ngazi ya kitaifa, mikoa, wilaya hata kata na wataasisi mbalimbali wametumia mgongo wa ‘uana mtandao’ kukalia viti vya uongozi walivyonavyo sasa.

Wengine wana kuwa viongozi kwa sababu hapo zamani au hata sasa wana uhusiano wa kimapenzi na wenye mamlaka ya kuteua. Kwa upande mwingine wapo viongozi ambao madaraka yao yametokana na undugu na kiongozi fulani mkubwa, wengine kwa kisingizio cha kufuata nyayo za wazazi wao, waume zao au wake zao.

Kadhalika wapo waliopewa uongozi kwa sababu sifa za kung’ara katika sanaa za maonyesho mathalani uimbaji kwaya, maigizo, mashairi, mipasho na au kwa sifa ya kupiga porojo na kuwa bingwa wa fitna.

Wengine wameteuliwa, kuchaguliwa kwa sababu ya kutoa michango mikubwa katika misiba, nyumba za ibada, kweye vyama vya siasa hususani chama tawala hata hakuna aliye na uhakika kama mapesa hayo wanayochangia hayatokani na baishara za haramu ya dawa za kulevya na hujuma zingine.

Maadamu hizi ndizo zimekuwa ni kisasa za kupata uongozi katika taifa letu hii leo tunashuhudia uongozi uliolegalega kwa namna ambayo haijawahi kutokea katika historia ya nchi yetu.

Leo hii viongozi wetu hawasemi kitu kikasikilizwa na watendaji waliopo chini yao wala kikatekelezwa na wananchi ipasavyo. Viongozi wengi wanaonekana kupwaya katika nafasi zao, kwani wengi wanadaiwa hawana uwezo kuwashawishi utendaji kazi na wao wenyewe hawaonekani kumudu majukumu yao.

Hali hiyo inaipa taifa letu hasara za siku hadi siku maana tunalazimika kuingia gharama zisizokoma za kuwakumbusha na kuwafundisha viongozi waandamizi majukumu yao.
Cha kustaabisha zaidi hata viongozi wakuu wa nchi hawaonekani kuwa na mvuto tena wa kusikilizwa na kupata utii unaostahili kutoka kwa wananchi.
Hayo yote ni kwa sababu ya viongozi wetu kukosa sifa machoni pa jamii na katika viongozi wengi tulionao si viongozi wenye uelewa mpana wa mambo, maono, uzalendo na maadili.

Katika hali hii ni dhahiri taifa linakoelekea ni kubaya sana kama vile ilivyo meli baharini inapokosa nahodha mahiri itapoteza dira na mwelekeo kama alivyowahi kusema aliyekuwa kuwa Katibu Mkuu wa CCM, Horace Kolimba, siku chache kabla ya kutoweka ghafla bin vuu duniani ambalo alisema “CCM imepoteza dira”.

Ni kama vile mashirika na makampuni ya umma yalivyokosa dira na mwelekeo hadi serikali ikaamua kubinafsisha kwa wageni. Kwa bahati mbaya hatuwezi kulibinafsisha taifa japo zipo dalili za kutuletea uchuro huo.
Tutajisikiaje watanzania, viongozi wa taifa hili watakuwa ni wageni na wafanya maamuzi muhimu wa nchi hii watakuwa si wazawa tena bali wageni?

Endapo tutaendelea kuwa na viongozi wanaopwaya kiasi hiki, taifa letu litasahau habari ya kutokomeza umaskini na kusonga mbele kimaendeleo sana sana tutapiga hatua kurudi nyuma siku hadi hadi siku.

Lakini hatima ya nchi hii katika suala la uongozi lipo mikononi mwa wananchi,wananchi ndiyo tunatakiwa tusimame sasa na kusema uongozi usio na sifa sasa basi.

Tufike mahali ambapo hatutamchagua kamwe kiongozi mbinafsi, fisadi, mlaghai, mbumbumbu, asiye na dira wa mwelekeo eti kwasababu tu ana uwezo wa kuwapatia wapiga kura sukaru kilo moja, doti za kanga, kapelo, fulana na vijisenti.

Tena sasa hivi imeibuka mchezo wa baadhi ya watu wenye fedha zao utoa fedha kidogo kwa wanamuziki wa bendi za dansi hapa nchi, ma DJ wa redio mbalimbali kuwarusha hewani, ili majina yao yazoeleke mbele ya jamii na kujipatia umaarufu wa chee, ili wakati wa uchaguzi waweze kutumia umaarufu huo kugombea nafasi za uongozi na kweli wanafanikiwa, Tuwakatae kwa nguvu zote viongozi wa aina .

Tufike mahala wananchi tumkatae kiongozi yoyote atakayeteuliwa ati kwa sababu ni mpenzi, ndugu au swahiba wa karibu wa anayemteua.

Kama wananchi hatutajali, tukumbuke kuwa dereva asiye na sifa za kuwa dereva akiendelea kupewa usukuni siku atakaposababisha ajali likawa janga la kitaifa, tutakaopoteza uhai ni sisi wananchi na dereva (kiongozi) huyo atatokomea kusikojulikana atakimbilia kule alikohifadhi fedha ambazo yeye na wenzake waliuibia umma.

Nasi tutabaki kuoza katika makaburi ya upweke ilhali vizazi vyetu vya baadaye vikaendelea kuteseka katika ufukara, dhiki kuu na aibu ya kutawaliwa na wageni kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni.

Hatuna budi kusimama na kuwakemea sasa viongozi wanaotaka kuturejesha katika enzi za utawala wa Kifalme ambapo uongozi uliaminiwa upo kwenye damu na ukoo au nasaba ya mhusika badala ya sifa zinazostahili.

Wakati umefika kila aliyempiga kura asiliangamize taifa kwa kumchagua mtu eti ni kwa sababu ni mtoto au mjukuu wa fulani. Wakati umefika viongozi wote mliochaguliwa kwa mizengwe kwa namna isiyostahili muone haja ya kujiuzulu na wa wananchi tutawaheshimu kwa kitendo hicho cha kiungwana.

Ni kweli jamii za wanadamu zinahitaji viongozi na viongozi hao lazima wawe watu. Hivyo ingawa viongozi wote ni watu lakini kila si kila mtu anafaa kuwa kiongozi.

Yule ambaye hawawezi kufikiri kwamba jamii anayokusudia kuiongoza atafanyia nini, bali anafikiri jamii imfanyie nini hatufai. Yule ambaye yupo tayari kuuza mwili wake ili apate nafasi ya uongozi hatufai. Yule ambaye yupo tayari kutoa na kupokea rushwa ili apate uongozi hatufai.

Yule ambaye anaghushi vyeti na kujipachika shahada za udaktari wa Falsafa (PhD) hatufai. Hakika Watanzania tumechoka kulaghaiwa na vyeo vya kitaaluma ilhali uongozi wenu kiutendaji ni sawa tu na mtu aliyeishia darasa la pili, tena katika shule isiyokuwa na walimu wala viti,vitabu na chaki.

Mungu Ibariki Afrika, Mungu inusuru Tanzania

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili Uk.10. Julai 8,2007

1 comment:

Anonymous said...

Ni kweli si kila mtu anafaa kuwa kiongozi. Vilevile si kila mtoto wa kiongozi anaweza kuwa kiongozi! hili linaonekana katika siasa ya Tanzania. Hivi sasa kumekuwa na mtindo wa watoto wa viongozi kudai kuwa kwa sababu wamelelewa ndani ya chama, basi wanaweza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi! Kuna wachache wanaweza kufuata 'nyayo' za wazazi wao, lakini si wote!

Kibaya zaidi, tumepoteza mwelekeo wa maana ya uongozi. Tunafikiri uongozi ni nafasi ya kuboresha maisha yetu na ya familia zetu kiuchumi, na ndio maana tuko tayari hata kughushi vyeti ili tupate cheo!

Uongozi ni kuwafungulia njia wananchi. Kuna wengine wansema "Utafunguaje mlango wa neema na wewe usitangulie kuingia?"
Tatizo la viongozi wetu wanaingia, halafu wanasahau kwamba walipewa jukumu la kufungua mlango ili wananchi waingie na kujikuta wamejifungia wenyewe!
"CHEO NI DHAMANA"

Powered by Blogger.