Header Ads

MGOMBEA BINAFSI YAIVURUGA SERIKALI

•JAJI MKUU ASEMA HUKUMU YA MAHAKAMA IKO PALE PALE

Na Happiness Katabazi
MAHAKAMA ya Rufani Tanzania imesema hukumu ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam iliyoruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi nchini, itaendelea kuwepo hadi pale mahakama hiyo itakapotoa uamuzi mwingine.


Kiongozi wa jopo la majaji saba, Jaji Mkuu Agustino Ramadhani, alisema hayo jana alipokuwa akiahirisha kusikiliza rufaa ya kupinga mgombea binafsi iliyofunguliwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali dhidi ya Mchungaji Christopher Mtikila.

“Rufaa iliyokatwa katika Mahakama ya Rufani nchini ya kupinga mgombea binafsi, haitengui uamuzi wa Mahakama Kuu ulioruhusu kuwepo mgombea binafsi.

“Hivyo taratibu za uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba, zitafuata hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu na hivyo ndivyo sheria inavyosema....kwa hiyo mgombea binafsi anaendelea kuwepo hadi Mahakama ya Rufani itakapoamua vinginevyo,” alisema Jaji Mkuu Ramadhani.

Majaji wengine wanaosikiliza rufani hiyo ni Eusebio Munuo, Nataria Kimaro, Januari Msofe, Mbarouk Mbarouk, Sauda Mjasiri na Bernad Ruhanda.

Jaji Ramadhani ambaye ni Jaji Mkuu wa Tanzania, alisema wamesikiliza hoja ya upande wa mkata rufani (Mwanasheria Mkuu wa Serikali) ambaye katika rufaa hiyo aliwakilishwa na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju, aliyekuwa akisaidiwa na Methew Mwaimu na Edson Milungwi ambao waliomba usikilizwaji wa kesi hiyo uahirishwe kwa kuwa hawajafanya utafiti wa kutosha kuhusu rufaa hiyo.

Jaji Ramadhani aliahirisha kesi hiyo hadi Aprili 8 itakapokuja kusikilizwa.

Awali, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Masaju, alidai rufaa hiyo inaenda kuweka historia katika Katiba na sheria za nchi, hivyo kuomba mwongozo wa mahakama ni kwa nini rufaa hiyo inasikilizwa na jopo la majaji saba badala ya watano au watatu kama ibara ya 118(1) na 122(1) za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inavyotaka.

Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya Jaji Mkuu na Naibu Mwanasheria Mkuu
Jaji Mkuu:
Nikuulize katika uelewa wako jopo la majaji watano wa mahakama ya rufani linakaa wakati gani?

AG:
Majaji watano wanakaa baada ya majaji watatu kukaa na jopo hilo la majaji watano linafanyia marejeo uamuzi wa majaji watatu kama kulikuwa na malalamiko ya uamuzi uliotolewa na majaji watatu.

Jaji Mkuu: Kesi ikishafunguliwa Mahakama ya Rufani haikatiwi tena kitakachofanyika ni kufanyiwa mapitio ya uamuzi sasa sijui tatizo hapa linatoka wapi! Na Mgombea binafsi ni suala kubwa nchini na ndiyo maana mahakama yetu imepanga idadi kubwa ya majaji na Mahakama ya Rufani ina mamlaka hayo...sasa sijui tatizo linatoka wapi.

AG: Basi Jaji Mkuu nimekuelewa naondoa hoja.

Masaju alidai Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ndiyo iliyokata rufaa na waliwapatia hoja kwa vielelezo upande wa wadaiwa Ijumaa iliyopita na wao wakaturudishia majibu Jumamosi na aliyepewa ni Mwanasheria Mwandamizi wa Serikali, Mwaimu, ambaye anauguliwa.

Kwa upande wake, wakili wa utetezi, Richard Rweyongeza, anayesaidiana na Mpale Mpoki alikiri kupatiwa vielelezo kwa maandishi na upande wa mkata rufani na kwamba wao waliitumia siku ya Jumamosi na Jumapili iliyopita kujiaandaa na wako tayari kuendelea kusikilizwa kwa rufaa hiyo.

Jaji Mkuu: Hivi course list (ratiba ya kikao cha Mahakama ya Rufani) ilitoka lini?

AG: Januari 28 mwaka huu.

Jaji Mkuu: Sasa kilichoifanya ofisi ya AG, muwa-‘save’ wadaiwa hivyo vielelezo vyenu Ijumaa iliyopita ni kitu gani? Na suala la Mwaimu kuuguliwa na baba yake tafadhari naomba liwekwe kando sasa.

AG: Mh! Mheshimiwa Jaji Mkuu hata jopo lako limekubali rufaa hii ni nzito....hivyo bado tunafanyia utafiti hoja zetu tutakazoziwasilisha katika rufani hii.

Jaji Mkuu: Hivi si ni serikali ndiyo iliyokata rufaa, ina maana siku zote hizo hamkufanya utafiti na kama leo hii (jana) mnadai bado hamjafanya utafiti na zile sababu sita mlizoziwasilisha kwenye rufaa yenu nazo ina maana pia hamkuzifanyia utafiti? Na mnakataje rufaa bila kufanya utafiti?

AG: Mhh (kimya).

Jaji Mkuu: Swali langu linabaki palepale inakuaje ofisi ya AG iu-‘save’ vielelezo upande wa mdaiwa Ijumaa iliyopita?

AG: Mhh! Tunaepuka malalamiko kwamba wanasheria wa serikali tumekuwa tukifungua kesi bila kufanya utafiti wa kutosha. Na tunaomba msajili wa Mahakama ya Rufani aipange rufaa hii katika kikao kijacho.

Jaji Mkuu: Kwani Msajili wa Mahakama ya Rufani atajuaje kama mmeishamaliza kufanya utafiti wenu? Kwani Msajili wa Mahakama ya Rufaa akiwa anapanga course list huwa anaihusisha ofisi ya AG?

AG: Hapana.

Jaji Mkuu:
Inasikitisha sana kuona kauli hiyo inatolewa na Naibu Mwanasheria Mkuu anayetokea ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, yaani nyie ndiyo mmekata rufaa halafu mnasema hamjajiandaa! Wenzenu wa utetezi mmewapatia vielelezo vyenu na wamejiandaa ndani ya siku mbili...halafu nyie wanasheria wa serikali ndiyo mnaoingoza bar (meza ya mawakili wa pande zote mbili) sasa sijui mnaongoza nini (watu wakaangua vicheko).

AG: Mi’ najitetea, mi’ niliteuliwa hivi karibuni kuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Jaji Mkuu: Hakuna cha kujitetea hapa. Jopo liko tayari kuahirisha usikilizaji wa rufaa hii sasa nyie semeni tuiahirishe hadi lini?

AG: Tunaomba miezi minne ijayo kuanzia leo.

Jaji Mkuu: Tunaiarisha rufaa hii hadi April 8.

Kwa mujibu wa rufaa hiyo namba 45 ya mwaka jana, inaonyesha serikali iliwasilisha rufaa hiyo, mwishoni mwa Juni mwaka jana, mahakamani hapo ikipinga hukumu iliyotolewa na waliokuwa majaji wa Mahakama Kuu, ambao ni Jaji Mstaafu Amir Manento, Salum Massati (Jaji wa Mahakama ya Rufani) na Thomas Mihayo (Mstaafu), ambao walikubaliana na ombi na Mtikila na kuruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi nchini.

Katika rufaa hiyo, serikali imetoa sababu sita za kukata rufaa hiyo zikiwemo: Mahakama Kuu ilikosea kujipa mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo; ilikosea kutengua vifungu vya Katiba ya nchi; na ilikosea kisheria kwa kupunguza matakwa ya lazima ya Ibara 30(5) na 13(2) ya Katiba ya nchi.

Sababu nyingine ni kujipachika mamlaka ya kibunge ya kutunga sheria, kukosea kisheria kwa kuiweka Katiba ya nchi katika vyombo vya kimataifa na pia ilikosea kuitolea maamuzi kesi hiyo bila kuweka suala hilo bayana.

Mara ya kwanza, serikali ilikata rufaa dhidi ya hukumu ya Mahakama Kuu, katika mahakama hiyo ya rufaa mwaka 2007, ambapo ilidai mahakama hiyo ya chini ilikosea kisheria kutafsiri Ibara ya 21(1)(c), 39(1)(c) (b) na 69(1)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977.

Hata hivyo, rufaa hiyo ilitupwa na Mahakama ya Rufaa baada ya mahakama hiyo kukubaliana na ombi la wakili wa Mtikila, Richard Rweyongeza, kwamba rufaa hiyo haina msingi na kwamba imejaa dosari za kisheria.

Awali katika hukumu ya Mahakama Kuu iliyotolewa Mei 2006, iliruhusu kuwepo kwa mgombea binafsi katika uchaguzi, kwa sababu Katiba ya nchi inatoa haki hiyo.

Mahakama Kuu ilibainisha kuwa Katiba inatamka wazi kuwa kila mwananchi ana haki ya kuchagua au kuchaguliwa kuwa kiongozi na haiweki masharti kuwa hilo lifanyike kwa mtu kujiunga na chama fulani.

Mwaka 1993, Mtikila alishinda kesi kama hiyo katika Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, lakini licha ya uamuzi huo wa mahakama, Bunge lilishindwa kutunga sheria ya kuruhusu mgombea binafsi hivyo alifungua kesi hiyo ya Kikatiba Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na kushinda tena.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Februali 9 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.