Header Ads

ZITTO KABWE UNAJIANDALIA ANGUKO

Na Happiness Katabazi

MTUME  Muhammad S.A.W amewahi kunukuliwa akizitaja sifa kuu tatu za mnafiki. Ambazo ni ; “Mnafiki akisema anasema uongo,mnafiki  akiaidi hatimizi na mnafki akiaminiwa ,haaminiki’.

Nukuu hiyo ya Mtume inapendwa mno kutumiwa na rafiki yangu ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Rombo (Chadema),  Joseph Selasini,katika harakati zake za kisiasa tangu nimfahamu akiwa Chama Cha NCCR-Mageuzi.Na nanukuu hiyo ndiyo imekuwa kama salamu yangu mimi na yeye pindi tunapowasiliana kwa simu au kukutana hana kwa ana na mwishowe tunaishia kucheka sana kutokana na sifa hizo za Mnafiki.

Alhamisi wiki hii huko Bungeni, Mwanasheria Mkuu wa Serikali(AG) , Jaji Fredrick Werema akiwa bungeni alimuumbua  Mbunge wa Kigoma Kaskazini ,Zitto Kabwe kwa vielelezo kuwa Zitto  alishakiri chini ya kiapo ofisini kwa Jaji Werema kwamba hana majina wala akaunti za watu hao , kinyume  cha kauli yake  huko  nyuma  alipowahi kusema  kuwa anawajua.

Jaji Werema alilazimika kusema hayo muda mfupi bungeni baada ya Zitto kusisitiza kuwa  serikali haionyeshi  nia ya kuwachukulia  hatua walioficha  fedha hizo nje ya nchini.

Jaji Werema ambaye ni Mwanasheria Kitaaluma aliigeukia taaluma yake na kuanza kutoa vielelezo vinavyopinga kauli hiyo ya Zitto kwamba serikali haina nia ya kuwawajibisha walioficha fedha hizo, ambapo Jaji huyo alisema Februali 28 mwaka huu, Kamati iliyoundwa  kuchunguza  kama fedha hizo ni haramu , kutambua benki walizoficha , kuandaa mashitaka  na kisha kuisharu serikali.

“Februali 28 mwaka huu, Kama   “Februari 28, mwaka huu, kamati ilikutana hapa bungeni katika ofisi yangu na ilipomuita Mheshimiwa Zitto aje atoe ushahidi, alikuja akatwambia anazo nyaraka na taarifa ila akaomba ahakikishiwe usalama ili pale ambapo angezileta pasingelikuwa na mtu wa kumzonga.

“Pia, alitaka mimi nitoe kiapo ambacho baada ya kutaja hayo majina halafu ikawa siyo kweli, basi yeye awe ‘free’ (huru), kwa hiyo alitaka apewe kinga ya kiapo.
“Machi 23 tulipomuita aje akatukwepa, akasema anakwenda Tanga kwenye mafunzo ya mgambo, kwa hiyo, tukaona tumsubiri hadi atakapomaliza.

“Aprili 12, mwaka huu, tukakutana naye hapa Dodoma katika viwanja vya Bunge, akasema hawezi kutwambia chochote kwa sababu alikuwa akijiandaa kwenda Afrika Kusini.
“Mei 4 tulimuita tena kwenye kamati hapa Dodoma na katikati ya mahojiano alidai ana jambo muhumu lenye maslahi kwa taifa, akasema anaomba aondoke atarudi, kamati ilimruhusu, hata hivyo hakurudi tena.

“Tulipompigia simu alisema alikuwa Dar es Salaam na alikuwa ‘busy’ akijiandaa kwa kongamano la Kigoda cha Mwalimu Nyerere.

 “Mei 24 kamati ilimfuata Dar es Salaam, akasema hana nafasi kwa sababu wakati huo alikuwa akijiandaa kuisaidia Timu ya Taifa,” alisema Jaji Werema na kuongeza:

“Kamati iliamua sheria ichukue mkondo wake kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Kifungu cha sita ndipo tukachukua maelezo ya Zitto Kabwe chini ya kiapo na akatwambia hakuwa na jina, wala akaunti ya Mtanzania yeyote aliyeficha fedha nje.
“Lakini, leo hapa amesema serikali haina nia ya kurudisha fedha zilizofichwa Uswisi. Kwa maana hiyo, Mheshimiwa Naibu Spika, Zitto Kabwe ni mzito na nakubaliana na Lema (Mbunge wa Arusha Mjini) aliyesema hapa, kwamba Zitto alete majina hayo.

Itakumbukwa kuwa kwa takribani mwaka mmoja sasa Zitto amekuwa akilandalanda mitaani na kunukuliwa na vyombo vya habari kuwa kuna vigogo wameficha fedha nchini Uswis na anawajua. Kweli kwa watu wanaopenda kudakia mambo bila kufanyia utafiti nao wakajikuta wanaiomba wimbo huo aliokuwa akiumba Zitto.

Ambapo mwisho wa siku Jaji Werema ,Alhamsi ya wiki hii bungeni alikuja kufumbua macho watanzania kuwa  huyu huyo Zitto aliyekuwa anatamba mitaani kuwa anawajua walioficha fedha, aliitwa kwenye Kamati hiyo maalum ili akaisaidie kutoa hayo majina ya namba za akaunti zao lakini hakwenda na matokeo yake Zitto alikwenda ofisini kwa Jaji Werema chini ya hati ya kiapo kuwa hayafahamu majina wala akaunti za watu hao.

Kisheria tunasema kila tuhuma inayoibuliwa au kesi inayofunguliwa mahakamani lazima iwe na mlalamikaji ambaye mlalamikaji huyo anapaswa kufika katika mamlaka husika kuisaidia kutoa vielelezo anavyodai kuwa watu fulani wamevunja sheria.

Sasa kwa muktadha huu ambapo Zitto aliaminisha umma kuwa kitendo hicho cha kufichwa fedha nje ya nchi kimemkera na ushahidi anao, kwanini Zitto huyu kwa zaidi ya mara nne ameitwa kwenye Kamati hiyo akashindwa kufika kutoa vielelezo hivyo?

Je alikuwa na lengo moyoni na akilini mwake?Maana tuhuma hizo alizoziibua ni kubwa sana na serikali yoyote makini nilazima tu ingeanza kufanyiakazi tuhuma hizo na hivyo ndivyo ilivyofanya serikali ya Tanzania, baada ya Zitto kuibua skendo hiyo , serikali iliamua kuunda kamati ya kuchunguza ukweli wa tuhuma hiyo , lakini cha kustaajabisha muibuaji wa skendo hiyo Zitto ambaye alikuwa akijitapa kuwa ana ushahidi, hakuweza kwenda kwenye Kamati hiyo kutoa ushahidi.

Naweza kusema pia kama yaliyosema na Jaji Werema ni kweli, basi watanzania hatuna budi ya kumwambia Zitto tena bila haya kuwa anaichezea serikali yetu sambamba na kuchezea rasilimali watu na fedha za walipa kodi.

Kwani ni yeye aliyeshupalia skendo hiyo na serikali ikajikuta inatumia fedha za kuunda kamati, kutumia rasilimali watu na muda wa serikali muda kuja kuhoji watu mbalimbali ambapo mwisho wa siku Zitto ndiyo alikuwa mtu muhimu sana wa kuisaidia Kamati hiyo kupata ukweli wa tuhuma hizo lakini cha kushangaza Zitto inaelezwa alishindwa kutoa ushirikiano kwa Kamati hiyo.

Kama kweli maelezo ya Jaji Werema ni ya kweli,Je wananchi wamuite   Zitto ni Mnafiki ,Mzandiki, muongo, msahaulifu, au ni mtu  anayekurupuka?

Maana inashangaza  kwa watu wenye kumbukumbu na Zitto kipindi kile alivyokuwa amekomaa na skendo hiyo, leo hii Jaji Werema anakuja kuliambia Bunge eti Zitto ameeleza chini ya kiapo kuwa hana majina wala hafahamu akaunti za vigogo na kwamba alikwepa kwenda kwenye Kamati kuhojiwa?

Hapo ndiyo ninampomheshimu Mbunge wa Vunjo(TLP), Agustine Mrema enzi zile alipoibua kashfa wa wizi wa Sh.milioni 900 kwa mawaziri wa serikali ya awamu ya tatu iliyokuwa ikiongozwa na Rais Mstaafu Benjamin Mkapa kuwa wametafuna fedha hizo na kweli Mrema alikubali kuhojiwa na Kamati ya Bunge na akafunguliwa kesi hiyo katika Mahakama ya Kisutu na alishinda kesi hiyo.

Mrema aliibua kashfa hiyo iliyomhusisha Rais Mkapa na baadhi ya mawaziri wake kwenye mikutano yake kisiasa , na alipoitwa kuhojiwa kwenye kamati ya bunge kipindi hicho hakukimbia, alikwenda na akahojiwa na mwisho wa siku alifunguliwa kesi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutoka na kuibuka kashfa hiyo ambayo upande wa jamhuri ulidai kashfa hiyo ni uzushi, lakini mahakama ilimwachiria huru Mrema.

Hivyo Mrema awe ni funzo kwa wanasiasa wengine walioibuka hivi sasa ambao wanajifanya mahiri sana wa kudai wanaibua tuhuma za ufisadi lakini wakiitwa katika mamlaka husika kutoa ushahidi huo ,wanakwepa.

Aprili 12 mwaka 2012 gazeti hili lilichapisha makala yangu iliyokuwa na kichwa cha habari kisemacho ‘Zitto Kabwe ,Mbona U msahaulifu?

Maudhui ya makala hiyo nilikuwa namuelezea Zitto  kumbe na yeye ni jamiii ile ya baadhi ya wanasiasa wale wale wenye hulka za kinyang’au ambao wanakasumba ya kuzungumza uongo mbele ya umma, ili umma uwapende na uamini kuwa kiongozi huyo ni mtu safi na mtetezi wa wanyonge, kumbe siyo kweli. Ieleweke wazi hapo nyuma Zitto alipata bahati ya kupata umaarufu  ndani ya jamii kwa kile kilichoelezwa ni mwanasiasa kijana ambaye ana misimamo thabiti na asiyeyumba katika kile anachikiami.

Sisi waumini wa sheria tunasema tuhuma zitabaki kuwa tuhuma hadi pale zitakapothibitika na mahakama au vikao husika vya chama chake.Lakini kwa kuwa mungu ni mwema kadri siku zinavyozidi kwenda mbele atazidi kutuonyesha kama kweli Zitto ni mwanasiasa msafi ,mhadilifu kuliko wanasiasa wenzake wanaotoka katika vyama mbalimbali vya siasa.

Na kweli utabili wangu huo umetimia kwa hivi karibuni Kamati Kuu ya Chadema, ikatangaza  kumvua nyadhifa zote ndani ya chama hicho kwa kile kilichodaiwa kuwa wamebaini kuwa Zitto anakisaliti chama chao.Hali iliyosababisha baadhi ya wanananchi kuanza kumtazama tofauti Zitto.

Itakumbukwa kuwa Zitto alikuwa msatili wa mbele kushinikiza baadhi ya watumishi wa serikali na viongozi wakiwemo mawaziri na Waziri Mkuu Mizengo Pinda wawajibishwe kwa kile alichokuwa akikidai kuwa wameshindwa kutekeleza majukumu yao na wengine wamekuwa wakikabiliwa na tuhuma mbalimbali na kweli kuna mawaziri waliondolewa kwenye baraza la mawaziri kwasababu ya tuhuma hizo zilizokuwa zikiibuliwa na Zitto na mwisho wa siku zikaungwa mkono na wananchi.

Waswahili wanamsemo wao usemao ‘linalomkuta Boko na Mamba pia litamkuta kwasababu wote wanaishi majini’. Kwa  hiyo yaliyowakuta baadhi ya mawaziri kwa kuondolewa kwenye  baraza la mawaziri kwa kigezo cha tuhuma tu...ndicho ambacho kimemkuta Zitto leo hii kwa Kamati Kuu ya chama chake kumvua nyadhifa zake zote kwa tuhuma kuwa ni msaliti.

Iwe Chadema walimsukia  zengwe Zitto na kuamua kumpokonya madaraka kwa kisingizio cha usaliti au ni kweli.Minaona itakuwa ni funzo sasa kwa Zitto kujifunza kuwa siyo jambo jema tena kwake kuendelea na kasumba yake ya kupenda kushinikiza wanasiasa wenzake hasa wa CCM wawajibishwe au kupokonywa madaraka kwasababu wanakabiliwa na tuhuma  za ufisadi na kuutaka urais mwaka 2015.

Kwa uzoefu wangu kwa wanasiasa wengi wa nchi hii ni mabingwa kuwatengenezea wenzao majungu, fitna na mwisho wa siku majungu wanayapeleka kwenye vyombo vya habari kwa kuwatumia baadhi ya waandishi wa habari kuwachafua mahasimu wao na kweli wanafanikiwa na majungu hayo kwa kuwachafua maasimu wao na mwisho wa siku maasimu wao wanachafuka mbele ya jamii na kama asimu wake ni mbunge, wananchi wake katika chaguzi zijazo wananchi wake hawamchagui tena kwa kisingizio kuwa mbunge wao huyo anakabiliwa na tuhuma za ufisadi kumbe wakati mwingine ni uzushi mtupu.

Ushauri wangu kwa Zitto ni kwamba akubali kuwa ule umaarufu aliokuwa nao zamani umeporomoka sana na hakuna ubishi kuwa itamgharimu kipindi kirefu sana kuuurejesha ndiyo atashindwa kabisa kuuresha.

Hivyo ni vyema yeye binafsi ajipe muda na atafakari ni wapi amekosea hadi leo hii kila kukicha umaarufu wake unazidi kuporoka, uadilifu wake unatiliwa shaka na chama chake na baadhi ya wananchi,kwanini Mwanasheria Mkuu wa serikali Jaji Werema ameamua kumtolea uvivu bungeni na kumuumbua kuwa Zitto kuwa aliitwa kwenye Kamati hakufika kuhojiwa na alipoitwa ofisini kwa AG, alitoa maelezo yake chini ya kiapo kuwa hana majina ya vigogo wala majina ya akaunti za vigogo walioficha fedha Uswiss.

Naheshimu mchango wa Zitto katika medani ya siasa nchini ila sipendezwi na tuhuma mbalimbali zilizomzingira Zitto kwani wananchi walionekana kumuani Zitto kuwa ni mwanasiasa msafi kuliko wengine lakini ghafla baadhi ya wananchi wanaripotiwa kwenye vyombo vya habari wakisema hawana imani naye tena.Kwa nini hili Zitto anaruhusu litokee?

Pia namshauri Zitto hivi sasa ni vyema akajiepusha kujadili adharani masuala yanayohusu uadilifu wa wanasiasa wenzake , kwani tayari nayeye hivi sasa anaandamwa na tuhuma hizo za ukosefu wa uadilifu.

Pia awe makini sana na hao watu wanaomshauri kwenda kwenye vyombo vya habari kujadili masuala kadha wa kadhaa kwani hao hao leo hii wanaojifanya kukushauri kujadili masuala kadha wa kadhaa mbele ya adhara ndiyo hao hao mwisho wa siku watakucheka.

Kwa wanaoifahamu jamii ya Watanzania, tunaelewa kuwa Watanzania wengi ni kama tuna ugonjwa wa usahalifu.Tunashikia bango jambo fulani mwisho siku tunalisahau tunadandia hoja nyingine.

Ni sisi watanzania tulishupalia wee Dk.Steven Ulimboka , Absalom Kibanda, mauji ya Daud Mwangosi, Idara ya Usalama wa Taifa livyotuhumiwa na Chadema kuiba kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010,mgomo wa madaktari ,shinikizo la kutaka aliyekuwa Waziri Mkuu Edwar Lowassa, na aliyekuwa waziri Andrew Chenge wajiudhuru na kwamba ni mafisadi, vurugu za kugombea ujenzi wa bomba la gesi Mtwara na vurugu za kisiasa Arusha  lakini leo hii nani tena anazungumzia mambo hayo.Hakuna.

Watoto wa mjini tunasema hivi nyimbo zinazotamba  Tanzania kwa sasa ni  kifo cha Rais wa Zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, kile kinachodaiwa ni mgogoro ndani ya Chadema na Zitto ,Zitto kuvuliwa nyadhifa zake kwa madai kuwa ni msaliti .Kwahiyo ni vema akatulia ,watanzania watasahau tuhuma zake.

Nimalizie kwa kumtaka Zitto Kabwe, asikubali kuingia kwenye nukuu hiyo ya Mtume  Mtume Muhamad kuwa; ‘  “Mnafiki akisema anasema uongo,mnafiki  akiaidi atimizi na mnafki akiaminiwa ,aaminiki’.

Mungu ibariki Tanzania

0716 774494
www.katabazihappy.blogspot.com
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili,Desemba 15 Mwaka 2013.

1 comment:

Anonymous said...

Ukweli umeusema happy akikusikiliza atafika mbali na akipuuza atakukumbuka miaka ijayo.

Powered by Blogger.