Header Ads

RAIS MWINYI APANDA KIZIMBANI KUTOA USHAHIDI KATIKA KESI YA KUIBIWA SH.MIL 37


Na Happiness Katabazi
RAIS mstaafu wa awamu ya pili, Ally Hassan  Mwinyi amefuata nyayo za Rais wa awamu ya tatu,Benjamin Mkapa kwa kufika katika Mahakama ya Hakimu MKazi Kisutu Dar es Salaam, na kupanda kizimbani na kutoa ushahidi katika kesi za jinai zilizofunguliwa mahakamani hapo na Mkurugenzi wa Mashitaka nchini(DPP), Dk.Eliezer Feleshi dhidi ya washitakiwa wa kesi hizo za jinai.
Rais Mwinyi jana alitua katika mahakama hiyo huku akiongozwa na maofisa Usalama wa Taifa(TISS)  kuja kutoa ushahidi katika kesi ya jinai Na. 201/2012 iliyofunguliwa na upande wa Jamhuri dhidi ya wakala wa Mwinyi Abdallah  Nassoro  Mzombe(39),mbele ya Hakimu Mkazi Genivitus Dudu  ambapo mshitakiwa huyo ambaye ni Mfanyabiashara  na mkazi wa Kinondoni Mkwajuni anashitakiwa kwa makosa ya   kumuibia Rais Mwinyi Sh. 37,440,000 zikiwa ni kodi ya pango  katika nyumba mbili zinazomilikiwa na rais huyo mstaafu.
Kabla ya Mwinyi kuanza kwa kesi hiyo jana, rais huyo mstaafu alipelekwa kna kuifadhiwa kwa muda kwenye chumba namba moja cha mahakama hiyo kwaajili wakili wa serikali  Charles Anindo kumuandaa kiongozi huyo kutoa ushahidi huo na wakati huo huo  maafisa wanne wa usalama wa taifa walikuwa wakifanya dolia kali ndani na nje ya chumba hicho alichokuwa ameifadhiwa kiongozi huyo.
Ilipofika saa   5:05 asubuhi, askari mmoja wa jeshi la Magereza alimtoa mshitakiwa Zombe katika mahabusu ya mahakama hiyo na kisha kumpandisha kizimbani kwaajili ya kesi yake kuanza kusikilizwa.
Baada ya mshtakiwa huyo kupandishwa kizimbani na askari huyo wa Jeshi la Magereza, waandishi wa habari za mahakamani tuliokuwepo mahakamani hapo nao walijiandaa kuingia katika chumba cha kuendeshea kesi hiyo ili waweze kusikiliza kesi hiyo,  lakini waandishi hao walipowakaribia maofisa usalama hao ,wanausalama hao waliwazuia kuingia ndani  ya chumba cha kusikilizia kesi hiyo  na wanausalama hao wakawahoji wanahabari hao kuwa wao ni wakinanani?

Miongoni mwa maofisa usalama hao ,mmoja wao aliwauliza waandishi wa habari kuwa wanakwenda wapi?
Waandishi wa habari: Tunataka kuingia kwenye hicho chumba kusikiliza kesi hiyo ya mshitakiwa anayedaiwa kumibia rais Mwinyi.
Afisa usalama: Nyie ni wakina nani?
Jibu :  Waandishi wa habari za mahakamani.
Afisa usalama: mmeambiwa kuna mahakama humu?
Jibu: Ndiyo hiyo ni mahakama.
Baada ya waandishi wa habari kumjibu hiyo,  afisa  huyo wa usalama alinyoosha mkono na kuzuia waandishi  kuingia kwenye mahakama hiyo. “Msiingie humu ndani  haiwahusu”.  Baada ya kuambiwa hivyo na mwanausala huyo ilitubidi  tukaa nje hadi saa 6:21 mchana na muda huo ndiyo kesi hiyo ilipamalizika kusikilizwa na tukamuona  rais Mwinyi akitoka ndani ya chumba hicho na kuongozwa na maafisa usalama hao kwenda nje ya mahakama hiyo na kisha kupanda gari aina ya Land Cruiser lenye namba za usajili T 914 BJT na kisha kuondoka katika viwanja vya mahakama hiyo.
Licha ya jitihada hizo za wanausalama kuzuia waandishi wa habari za mahakama kuingia ndani ya chumba cha mahakama kusikiliza ushahidi uliokuwa ukitolewa na rais Mwinyi, lakini waandishi hao nao walitumia mbinu zao na wakafanikiwa kupata hati ya mashitaka ya kesi hiyo ambayo ilifunguliwa mahakamani hapo Agosti  21 mwaka huu, na waandishi wa habari za mahakamani kwa kipindi chote hicho hawakuwa wakifahamu kuna kesi ya aina hiyo ilikuwa imefunguliwa mahakamani hapo.
Kwa mujibu wa hati hiyo ya mashitaka ambayo waandishi wa habari za mahakama walifanikiwa kuipata mahakamani hapo jana ,upande wa Jamhuri unadai  Mzombe anadaiwa kufanya makosa hayo kinyume na kifungu cha 258 na 273 (b) (e) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya Sura ya 16 ya mwaka 2002.
  
Siku hiyo ya Agosti 21 mwaka huu, ilidaiwa  kuwa  kati ya Januari Mosi, mwaka 2011 na Julai 2012 huko Mikocheni ,  Mzombe akiwa Wakala wa rais huyo mstaafu, alimwibia  Sh 17,640,000  ambazo ni pato la kodi ya nyumba yake  iliyopo eneo la Mikocheni  wilaya ya Kinondoni.
Iliendelea kudai kuwa kiasi hicho cha fedha ambacho Mzombe alimwibia rais Mwinyi kilikuwa ni kodi ya pango la nyumba namba 481,  iliyopo kwenye ploti A ,huko Mikocheni ya mwaka 2011/2012 na 2012/2013.
Aidha Mbali anadaiwa kuwa  kati ya Januari Mosi, mwaka 2011 na Julai 10, mwaka huu huko Msasani Village  wilaya ya Kinondoni, mshtakiwa  huyo alimwibia tena rais huyo mstaafu Sh 19,800,000  ambayo ilikuwa ni kodi ya nyumba namba 55 iliyopo kwenye Kitalu C .
Iliongezwa kudaiwa kuwa kiasi hicho cha fedha kilikuwa ni kodi ya pango la nyumba hiyo la mwaka  2011/2012 na 2012/2013, hata hivyo mshitakiwa huyo alikana mashitaka yote  na yupo rumande hadi oktoba 22 mwaka,itakapokuja kuendelea kusikilizwa.
Itakumbukwa kuwa Mei 7 mwaka Rais Mkapa alifika mbele ya Hakimu Mfawidhi  wa mahakama ya Kisutu,  Elvin Mugeta m katika kesi ya uhujumu uchumi iliyokuwa ikimkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu na Grace Martin kutoa ushahidi katika kesi hiyo ambapo alikuwa alikuwa ni shahidi wa Mahalu  ambapo Agosti 9 mwaka huu, Hakimu Mugeta alitoa hukumu ya kesi hiyo ya kihistoria na kuwaachiria huru washitakiwa wote kwa madai kuwa upande wa jamhuri wameleta ushahidi dhahifu ambao umeshindwa kuishawishi mahakama imtie hatiani Mahalu na Grace.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Oktoba 10 mwaka 2012.
 
 


No comments:

Powered by Blogger.