Header Ads

KESI YA DK.NAMALA MKOPI YAFIKA PATAMU

Na Happiness Katabazi UPANDE wa jamhuri katika kesi ya kudhalau amri ya Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi inayomkabili Rais wa Chama cha Madaktari nchini(MALT), Dk.Namala Mkopi ulimsomea maelezo ya awali mshitakiwa huyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam. Wakili Mwandamizi wa Serikali, Tumaini Kweka mbele ya Hakimu Mkazi Faisal Kahamba aliikumbusha mahakama kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya upande wa jamhuri kumsomea maelezo ya awali mshitakiwa huyo anayekabiliwa na makosa mawili ya kudharau amri ya Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi kinyume na kifungu cha 124 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 na kosa la pili ni kuwashawishi madaktari wagome. Wakili Kweka alianza kumsomea maelezo ya awali mshitakiwa huyo na kudai kuwa Dk.Mkopo daktari wa binadamu aliyeajiliwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii katika Hospitali ya Taifa ya Mhimbili. Alidai kuwa Dk.Mkopi ni mwanachama (MAT) ambacho kimeanzishwa na madaktari ambacho pia kinaishauri serikali katika mambo ya afya na utabibu na pia kunasimamia na kulinda maadili ya wanachama wake na kwamba mwaka 2011 mshitakiwa huyo alichaguliwa kuwa rais wa chama hicho. “Juni 2012 madaktari wanaofanyakazi katika hospitali za serikali waliingia kwenye mgomo dhidi ya mwajiri wao ambaye ni serikali na mgomo huo uliandaliwa na MAT na madaktari hao waligoma kuwahudumia wagonjwa wakati wakati mkatabao wao waajira waliongia na serikali ni kuwatibia wagonjwa”alidai Kweka. Wakili Kweka alidai kuwa wakati mgomo huo ukiendelea serikali ilipeleka maombi No.73 ya mwaka 2012 katika Mahakama Kuu Diveshini ya Kazi yaliyokuwa yakiomba mahakama hiyo itoe amri ya kuzuia mgomo huo usiendelee hadi pale ule mgogoro baina ya MAT na serikali ulifunguliwa katika Tume ya Usuluhishi wa migogoro (CMA) uliosajiliwa kwa namba CMA/DSM/ILA/145/12 mbele ya Jaji Moshi utakapomalizika. Aidha Kweka alidai kuwa Juni 22 mwaka huu,Mahakama Kuu ilitoa amri ya kuwataka madaktari waliogoma nchi nzima wasitishe mgomo na mahakama hiyo ikampatia nakala ya amri hiyo mshitakiwa (DK.Mkopi) ,Juni 25 mwaka huu. “Licha ya mshitakiwa kupatia amri hiyo ya mahakama ambayo aliipokea yeye na madaktari wenzake waliendeleza mgomo huo na Juni 26 mwaka huu, Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi ilitoa amri nyingine kwa MAT iliyokuwa ikikitaka chama hicho kutekeleza kwa vitendo amri ya mahakama iliyotolewa Juni 22 mwaka huu ambayo ilimtaka Dk.Mkopi kwenda kwenye vyombo vya habari kuwatangazia madaktari wote waliogoma wasitishe mgomo huo; “Lakini Dk.Mkopi alishindwa kutekeleza amri hizo mbili za Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na matokeo yake yeye na madaktari wenzake wakaendelea na mgomo na kwamba Julai 9 mwaka huu, mshitakiwa alikamatwa na kufikishwa mahakamani hapa Julai 10 mwaka huu na kufunguliwa kesi hii iliyopo mbele yako Mheshimiwa Hakimu”alidai Kweka. Kwa upande wake Dk.Mkopi alidai ameyasikia maelezo hayo aliyosomewa wakili Kweka ila anakanusha kuwa yeye siyo daktari wa Hospitali ya Taifa ya Mhimbili ila anakubali kuwa ni kweli yeye ni daktari wa binadamu na anakataa kuwa madaktari hawakugoma kuwatibia wagonjwa na kwamba si kweli kuwa alidharau amri ya mahakama ya Juni 22 mwaka huu iliyomtaka aende kwenye vyombo vya habari kuwatangazia madaktari waache kugoma. Hakimu Kahamba aliarisha kesi hiyo hadi Oktoba 23 mwaka huu, ambapo siku hiyo kesi itakuja kwaajili ya mashahidi wa upande wa jamhuri kuanza kutoa ushahidi wao. Julai 10 mwaka huu, ilidaiwa na wakili wa serikali Lasdiraus Komanya kuwa kati ya Juni 26 na 28 mwaka huu,Dk.Mkopi akiwa ni Rais wa MAT alidharau amri halali ya Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi ya Juni 26 mwaka huu, ambayo ilimtaka mshitakiwa huyo kwenda kwenye vyombo vya habari kuwatangazia wanachama wa chama hicho wasitishe mgomo kwani mgomo ule waliokuwa wakitaka kuufanya ni batili kama ambayo mahakama hiyo ya Divisheni ya Kazi Juni 22 mwaka huu, ilitoa amri kama hiyo ya kuubatilisha mgomo huo, lakini mshitakiwa huyo hakufanya hivyo. Wakili Kweka pia alidai kosa la pili ni kuwashawishi madaktari wagome kinyume na kifungu 390 na 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002, kuwa Juni 27 mwaka huu, mshitakiwa huyo akiwa rais wa chama hicho aliwashawishi madaktari wasitekeleze amri hiyo ya Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi ya Juni 22 mwaka huu,na matokeo yake madaktari hao wakagoma. Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa,Septemba 28 mwaka 2012.

No comments:

Powered by Blogger.