Header Ads

SERUKAMBA AIBWAGA CHADEMA

Na Happiness Katabazi MAHAKAMA ya rufaani nchini, imetupilia mbali kwa gharama maombi ya kufanyiwa mapitio ya hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Tabora Machi 28 mwaka huu, ambayo ilisema kuwa taratibu za sheria ya uchaguzi na matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 yaliomtangaza Peter Serukamba (CCM), kuwa Mbunge wa Kigoma Mjini, hayakukiuka sheria. Agosti mwaka huu, aliyekuwa mgombea wa CHADEMA katika jimbo hilo, Ally Mleih, aliwasilisha Mahakama ya Rufaa, ombi la kuiomba ifanye mapitio ya hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Tabora iliyotolewa na Jaji Stella Mgasha. Uamuzi huo wa jana ulitolewa na majaji watatu wa Mahakama ya Rufaa, Jaji Edward Rutakangwa, Bernard Luanda na Salum Massati, baada ya kusikiliza hoja za pande mbili katika shauri hilo. Jaji Rutakangwa alisema jopo lake limekubaliana na hoja zilizowasilishwa mbele yao na wakili wa Serukamba, Kennedy Fungamtama, kuwa mrufani alipaswa afungue rufaa katika mahakama hiyo na si kuwasilisha ombi linalotaka mahakama hiyo ifanyie mapitio ya hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Tabora. “Baada ya kupitia hoja za pande zote mbili, mahakama hii imekubaliana na hoja za Wakili Fungamtama na kwamba imebaini mrufani alipitia mlango wa nyuma kuwasilisha ombi lake hilo, jambo ambalo ni kinyume cha sheria na Katiba ya nchi. Kwa sababu hiyo inatupilia mbali kwa gharama,” alisema. Jaji Rutakangwa alisema kuomba rufaa ni haki ya kikatiba na haki hiyo imeainishwa bayana katika ibara ya 83 (4) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977. Alisema kwa mujibu wa matakwa ya ibara hiyo mrufani, Mleih ana haki ya kukata rufaa na si kuwasilisha ombi la mapitio kama alivyofanya hivi sasa. Mapema Machi 28 mwaka huu, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, Mgasha alitupilia mbali kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi ya mwaka 2010 ya Kigoma Mjini yaliyomtangaza Serukamba kuwa mshindi kwa maelezo kuwa mlalamikaji alishindwa kuthibitisha madai aliyoyafungua mahakamani. Chanzo:Gazeti la Tanzania la Alhamis Septemba 6 mwaka 2012.

No comments:

Powered by Blogger.