Header Ads

MSHITAKIWA ALIKIRI KUHUSIKA-SHAHIDI

Na Happiness Katabazi

SHAHIDI wa pili katika kesi ya wizi wa sh bilioni 2.2 wa Fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki ya Tanzania, inayomkabili Kada wa CCM, Rajabu Maranda na mpwa wake, Farijara Hussein, SSP-Salum Kisai, ameiambia mahakama Farijara alikiri kuhusu na kesi hiyo.


SSP-Kisai ambaye alikuwa akiongozwa kutoa ushahidi wake na Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, Fredrick Manyanda,Oswald Tibabyekoma na Michael Lwena, alidai kuwa Oktoba 20 mwaka jana, akiwa katika ofisi za Kikosi Kazi kilichoundwa na Rais Jakaya Kikwete kuchunguza wizi wa EPA, aliandika maelezo ya onyo ya Farijara na kwamba alifuata taratibu zote za kisheria zinazotakiwa kuchukua maelezo ya onyo kwa mshitakiwa.

Kisai ambaye ni Mtaalamu wa Maandishi toka Makao Makuu ya Upelelezi ya Jeshi la Polisi, alidai kuwa kimsingi maelezo Farijara alikiri kuhusika na wizi huo na akaomba mahakama ipokea maelezo hayo ya onyo ya mshitakiwa huyo kama kielelezo.

Lakini hata hivyo wakili wa mshitakiwa Majura Magafu alipinga kupokelewa kwa maelezo hayo kwasababu hati hiyo ya onyo haijakidhi matakwa ya kifungu cha 46 na 58 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya 2002.

Magafu alidai kuwa shahidi huyo wakati akichukua maelezo ya mshitakiwa alimfanyia ulaghai mteja wake kwani pia alipaswa kumweka sehemu nzuri mshitakiwa na angempatia peni na karatasi ili aweze kuandika maelezo yake mwenyewe na angemjulisha kuwa maelezo hayo yangekuja kutumika mahakamani.

“Hivyo napinga maelezo ya onyo yasipokelewe kwasababu Farijara alirubuniwa na shahidi huyu ambaye ni ofisa wa polisi wakati akimhoji mteja wangu kule katika ofisi za Kikosi Kazi” alidai Magafu.

Pingamizi lilosababisha jopo la mahakimu wakazi linaloongozwa na Fatma Masengi, Catherine Revocate na Benedict Muigwa,kukubaliana na pingamizi la Magafu na kutoa amri ya kusimamisha uendeshaji wa kesi ya msingi na kuamua kufanyika kwa kesi ndogo ambayo itaanza leo ambapo kila upande utaleta mashahidi wake kudhibitisha kama maeleazo hayo ya onyo hayakufuata taratibu za kisheria.

Novemba mwaka jana, ilidaiwa kuwa washitakiwa hao kati 2004-2005 walitumia kampuni yao hewa ya Money Planner Consaltant kuibia Benki Kuu, sh bilioni 2.2.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa,Julai 10,2009

No comments:

Powered by Blogger.