Header Ads

'NILIKUTA PINGU,MIWANI KWENYE GARI LA MURRO

Na Happiness Katabazi

MKUU wa Upelelezi wa Mkoa wa Ilala, Duani Nyanda, jana ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jinsi alivyopekua gari la Jerry Murro, anayetuhumiwa kuomba rushwa ya sh milioni 10 ambapo alikuta pingu na miwani ya kusomea.


Nyanda ambaye ni Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, ambaye pia ni shahidi wa sita katika kesi hiyo inayomkabili Murro, Kapama na Deo Mgassa, wanaotetewa na mawakili wa kujitegemea Richard Rweyongeza na Majura Magafu, alitoa ushahidi huo akiongozwa na Naibu Mkurugenzi wa Mashitaka nchini, Stanslaus Boniface, mbele ya Hakimu Gabriel Mirumbe.

Alieleza kuwa Januari 31 mwaka jana saa 12 jioni akiwa ofisini aliamriwa na aliyekuwa Mkuu wake, Charles Mkumbo, kwenda kulipekua gari la Murro lenye namba za usajili T 545 BEH Toyota Cresta lililoegeshwa kwenye viunga vya Kituo Kikuu cha Polisi.

“Baada ya kupewa jukumu hilo nilimchukua Murro ambaye alikuwa ofisini kwa Mkumbo na mashahidi wengine akiwamo Koplo Lugano Mwampeta na waandishi wa habari, nikaenda nao kwenye gari lake lilipokuwa limeegeshwa.

“Baada ya Murro kulifungua nikaanza upekuzi wa gari lile, kwa sababu polisi tulipata malalamiko kutoka kwa aliyekuwa Mhasibu wa Halmashauri ya Bagamoyo, Michael Wage, kwamba kuna watu akiwamo Murro walimtishia kwa pingu, bastola na kumwomba rushwa na kwamba Wage alisahau miwani yake katika gari la Murro,” alidai SSP Nyanda.

Nyanda alieleza kuwa katika upekuzi wake alifanikiwa kupata pingu ambazo Wage alizibaini ndizo alizotishiwa nazo na Murro na miwani ya kusomea ambayo anadai ni yake aliisahau kwenye gari hilo Januari 30 mwaka jana na kuongeza kuwa alikuwa na hati ya polisi ambayo Murro na Wage walisaini kuthibitisha kushuhudia upekuzi huo na kuitoa mahakamani kama kielelezo namba tano kilichopokewa.

Pamoja na hati hiyo, pingu na miwani pia vilitolewa mahakamani kama vielelezo namba sita na saba. Kesi hiyo iliahirishwa hadi Machi 8 na 9 mwaka huu, ambapo shahidi wa saba ataanza kutoa ushahidi wake.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Januari 27 mwaka 2011

No comments:

Powered by Blogger.