Header Ads

MAWAKILI WATAKA LIYUMBA AACHIWE


Na Happiness Katabazi
UPANDE wa utetezi katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumushi na Utawala wa BoT,Amatus Liyumba, umeiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imuone mshitakiwa hana kesi ya kujibu na imuachirie huru kwasababu upande wa mashitaka umeshindwa kuthibitisha kesi yao(prima facie case).


Ombi hilo liliwasilishwa mahakamani hapo jana saa 6:11 mchana kwa njia ya maandishi (written submission) lenye kurasa 16 na wakili wa utetezi Majura Magafu anayesaidiwa na Jaji Mstaafu Hillary Mkate, Onesmo Kyauke na Hudson Ndusyepo ambayo aliikabidhi kwenye chumba cha makarani na ikapokelewa.Kuwasilishwa kwa ombi hilo jana kulitokana na amri iliyotolewa Machi 15 mwaka huu na Kiongozi wa Jopo la Mahakimu Wazki Edson Mkasimongwa ambaye alizitaka pande zote kuwasilisha hoja maombi hayo kwanjia ya maandishi.

Kwa mujibu wa nakala ya ombi hilo ambalo gazeti hili limefanikiwa kupatana nakala yake , Magafu anaomba mteja wao mahakama imuone hana kesi ya kujibu kwani hata mashahidi nane walioletwa na upande wa mashitaka waliambia mahakama hiyo kwamba mshitakiwa hakuwa na mamlaka ya kuidhinisha ujenzi wala mabadiliko ya ujenzi(scope of work) wa ujenzi wa 10 Mirambo office Extension na wala hawajawahi kumuona akiudhulia kwenye vikao vya bodi ya BoT kwasababu hakuwa mjumbe wa bodi hiyo na kuongeza bodi ndiyo iliyoidhinisha ujenzi huo na si Liyumba.

‘Tunaomba mahakama hii tukufu imuone mshitakiwa hana kesi ya kujibu kwani upande wa mashitaka umeshindwa kuthibitisha kesi yake na upande wa mashitaka ushindwa kufahamu mshitakiwa alikuwa anatakiwa ashitakiwe kwa makosa gani ....Naibu gavana Juma Reli wakati anatoa ushahidi alisema wazi kwamba hadi sasa mtu hawezi kujua hasara iliyopatikana katika ujenzi huo kwasababu ripoti ya ujenzi huo haijatoka...na mashahidi wote wa Jamhuri ukiutaza ushahidi wao walimtetea Liyumba;

“Kwa nguvu zote tunarudia kuiomba mahakama imuonesha Liyumba hana kesi ya kujibu kwani pia upande wa Jamhuri umeshindwa kuleta ushahidi unaonyesha serikali imepata hasara na kwamba kwasasa hakuna mtu anayepaswa kusema hasara imepatikana kwasababu ripoti ya ujenzi huo bado haijaandaliwa,kwa mujibu wa shitaka la kusababisha hasara sheria inasema mshitakiwa lazima awe ametenda kosa hilo akiwa na nia mbaya lakini Jamhuri imeshindwa kuleta ushahidi unaounga mkono kosa hilo na kama hivyo ndivyo nia mbaya haipo.

‘Na kushindwa kwa Jamhuri kuleta vielelezo kwamba mshitakiwa alitoa maamuzi kwenye mradi huo upande huo pia umeshindwa kuleta ushahidi kuonyesha uamuzi huo kufanya mabadiliko ya mradi unaodaiwa kufanywa na Liyumba aliufanya akiwa na nia mbaya.ndiyo maana tunaimba mahakama imuone mshitakiwa hana kesi ya kujibu”alidai Magafu.

Akichambua madai ya upande wa mashitaka yaliyodai kwamba Liyumba na aliyekuwa Gavana wa BoT,marehemu Daud Balali ndiyo waliofanya mabadiliko ya ujenzi bila idhini ya bodi ya wakurugenzi ,alidai hakuna upande wa mashitaka umeshindwa kuleta ushahidi wa kuthibitisha tuhuma hiyo na pia umeshindwa kuleta nyaraka kama kielelezo ambacho kingeonyesha saini ya Liyumba kwamba ndiye aliyeidhinisha ujenzi huo.

Alidai kwa mujibu wa kumbukumbu ya ushahidi uliotolewa unaonyesha wazi Liyumba ofisi yake ilikuwa ni kiunganishi (Co-ordinator) kati ya Menejimenti ya Benki hiyo na Meneja Mradi,hivyo shughuli zote za mradi huo alikuwa akizifanya kwa niaba ya benki hiyo na sisi yeye binafsi.

“Ni dhahiri kabisa upande wa Jamhuri katika kesi hii umeshindwa kufahamu walipaswa wamfungulie mshitakiwa mashitaka ya aina gani ni wao walikiri mahakamani hapa kwamba mshitakiwa ofisi aliyokuwa akionga ilikuwa ni kiungo cha mradi huo wa ujenzi..sasa inakuwaje wakati huo huo upande wa Jamhuri udai mshitakiwa huyo alifanya maamuzi ya mabadiliko ya ujenzi na eti mshitakiwa huyo huyo akaidhinisha mabadiliko hayo ;

“Na katika hilo upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha tuhuma hiyo,na kwa akili ya kuzaliwa hivi mtu huyo Bila upande wa mashitaka kuleta ushahidi kuthibitisha tuhuma hiyo?kwa akili ya kuzailiwa mtu mmoja anaweza kuratibu kazi ile ile katika maamuzi na kuwapelekea watu huku tayari maamuzi yalishafanyika.Na licha hivyo BoT ilikuwa ina ngazi ya juu ya kufanya maamuzi ,hivyo BoT haina chumba kilichokuwa kikiitwa chumba cha kuratibu kwaajili ya kufanya maamuzi.”alidai Magafu.

Magafu alidai kwamujibu wa kumbukumbu ya ushahidi,unaonyesha Bodi ya BoT iliiruhusu Menejimenti ya benki hiyo kutoa fedha kwaajili ya ujenzi wa mradi huo na hivyo hakuna ushahidi ulioletwa mahakamani unaonyesha vidole vya mshitakiwa vilitumika kuidhinisha fedha za BoT zitolewe kwaajili ya ujenzi huo.

Upande wa Jamhuri nao utawasilisha hoja zake zitakazomuona mshitakiwa anakesi ya kujibu Machi 29 na mahakama itatoa uamuzi wa mshitakiwa ana kesi ya kujibu au la April 9 mwaka huu.

Januari 27, mwaka jana, Liyumba na Meneja Mradi wa Benki Kuu, Deogratius Kweka, walifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza na kusomewa mashitaka hayo ya kuidhinisha mradi wa majengo ya minara pacha bila idhini ya bodi ya wakurugenzi na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221.

Mei 27 mwaka jana, mahakama hiyo iliwafutia kesi, lakini muda mfupi baada ya kuachiliwa walikamatwa tena mahakamani hapo na Mei 28 mwaka jana Liyumba peke yake ndiye aliyerudishwa mahakamani hapo na kusomewa mashitaka hayo na Kweka akawa ameachiliwa huru.

Tangu kipindi hicho hadi sasa Liyumba anaendelea kusota rumande, baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana, ambapo mahakama ilimtaka atoe fedha taslimu au hati ya mali yenye thamani ya sh bilioni 111.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Machi 23 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.