Header Ads

VIONGOZI WA DINI AMKENI MUIKOE JAMII

Happiness Katabazi
KWA takriban miaka miwili sasa viongozi wa madhehebu ya dini mbalimbali hapa nchini wamekuwa wakiitumia kikamilifu ibara ya 18(a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.


Ibara hiyo inasema ‘kila mtu anao uhuru wa kutoa maoni na kueleza fikra zake’.

Viongozi hao wa dini wamekuwa wakiitumia vyema ibara hiyo kwa kupaza sauti kwa kukemea wakidai ufisadi umeshamiri nchini hasa katika utawala wa Rais Jakaya Kikwete, hadi kufikia hatua ya viongozi hao kutofautiana kimsimamo na wanasiasa wakongwe akiwemo Kingunge Ngombare Mwiru.

Kingunge aliwataka viongozi wa dini kuacha kujiingiza kwenye ulingo wa siasa kwani endapo wataendelea kufanya hivyo wanaweza kuvuruga amani ya taifa letu. Hata hivyo viongozi hao wa dini waliweka pamba masikioni; waliendelea na msimamo wao kupinga ufisadi kwa matamshi yao na maovu mengine ambayo walipaswa wawafundishe waumini wao wasiyatende, wala hawakuyapigia kelele kama walivyopogia kelele ufisadi.

Leo katika makala hii nitazungumzia aina mpya ya mahusiano yaliyozuka kwenye jamii yetu ambayo yameanza kutishia amani, mila na desturi zenu: ushoga na usagaji.

Kwa mujibu wa kifungu cha 138A na kifungu cha 157 CAP 15, Offence Against Morality of Tanzania Penal Code, 2002, vinakataza vitendo hivyo vya kibazazi.

Lakini kuna aina mpya ya mahusiano ya kubadilisha jinsia imezuka; mwanaume anabadili jinsia, anaweka ya kike!

Hili ni tatizo na halijatungiwa sheria, linatishia usalama wa jamii na mila zetu kwani haiwezekani watoto katika familia ambayo baba au mama wanamuona mtoto wao akibadilisha jinsia.

Hakika hii ni dhambi na itatupeleka motoni; na tukae tukijua watoto wetu pindi washuhudiapo ufedhuli huu ni wazi wataathirika kisaikolojia.

Hapa viongozi wetu wa dini wanatakiwa kutusaidia kukomesha mambo haya ili maadili yasiteketee.

Viongozi wa dini wanatakiwa wajue wajibu wao kwa jamii, watumie muda mwingi kufikiri mbinu sahihi za kuifundisha jamii ili iweze kuelewa kwa urahisi.

Leo inawezekana tutaliona ni tatizo dogo lakini tutakapogundua kua si dogo litakuwa limetuzidi nguvu.

Aidha, kumekuwepo na madai kwamba baadhi ya viongozi wa dini nao wamekumbwa na mmomonyoko wa maadili kwa kujihusisha na dhambi ya uzinzi ambayo imekemewa vikali kabisa katika vitabu vitakatifu vya Mungu hususan ndani ya Biblia katika kitabu cha Mithali 6:36 inayosema ‘Yeyote aziniye hana akili kabisa tena afanya jambo litakaloangamiza nafsi yake’.

Kufanya ngono zembe na waumini wao au wake za waumini wao, wanatumia nguvu za giza kuendesha nyumba za ibada, wanatumiwa na wanasiasa, wanaishi maisha ya hali ya juu kuliko waumini wao, kwa wale viongozi wadini waliokatazwa kuoa au kuolewa wamekuwa na mahusiano ya kimapenzi hadi kufikia kuzaa watoto kinyemela na kuwatunza kwa siri kubwa.

Lakini pamoja na kujifanya wanaficha dhambi za uzinifu wao, jamii imeshawang’amua na ile heshima waliyokuwa wakipewa zamani imepungua au kumalizika na wanaonekana ni viongozi wa dini wanaotumia dini kuficha maovu wanayoyafanya.

Tukubaliane kuwa kuna mmonyoko wa maadili kwa baadhi ya viongozi wetu wa dini, ni vizuri wakatambua nafasi yao kwa waumini wao na ikiwezekana waache mambo yanayowashushia heshima mbele ya umma kwa kuwa wao ni kioo.

Mtu anapokuwa kioo ni lazima atende matendo ya kuigwa badala ya kufanya mambo yanayodhalilisha cheo chake pamoja na taasisi anayoiongoza.

Napenda kutoa rai kwa viongozi wa dini kwamba nguvu zile walizozitumia kupaza sauti kuhusu ufisadi nchini, basi wazitumie kupaza sauti kukemea ushoga, usagaji, uzinzi, mauaji dhidi ya binadamu wenzetu, nguvu za giza, pepo wa tamaa ya mali na madaraka.

Huko nyuma tulipokuwa tukihudhuria nyumba za ibada, viongozi wa dini hususan sisi waumini wa Kanisa la Kiinjili ya Kilutheri tulikuwa tukihamasishwa mno kuheshimu amri za Mungu zisemazo usitamani mwanamke wa mwenzio, usimshuhudie jirani yako uongo, usitamani mali ya jirani yako wala ng’ombe, punda, au mjakazi wake, usilitaje bure jina la bwana Mungu wako.

Leo hii ukihudhuria kwenye nyumba za ibada au ukiwa na mazungumzo na viongozi wa dini, ni nadra mno kuwasikia viongozi hao wa dini wakizitaja amri hizo…utawasikia wakitaja ufisadi umeshamiri.

Hakuna asiyefahamu kwamba nchi yetu nayo inakabiliwa na maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi ambao kwa asilimia kubwa chanzo chake ni ngono zembe.

Umefika wakati kwa viongozi wa dini kuelekeza nguvu zao kwa kupiga vita maovu hayo na kuwakumbusha mara kwa mara waumini wa dini husika amri hizo za Mungu naamini mioyo ya watu na akili zao zitabadilika na kuwa na hofu ya Mungu na kuachana na madhambi hayo.

Naomba kutoa hoja.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili la Machi 7 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.