Header Ads

USHAHIDI KESI YA MRAMBA UTATA MTUPU

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa utetezi wa kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 11.9 inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba, na wenzake, jana uliushutumu vikali upande wa jamhuri katika kesi hiyo kuwa umepeleka mahakamani vielelezo vya kughushi.


Mbali na Mramba, washtakiwa wengine ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona, na Katibu Mkuu mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja.

Shutuma hizo zilitolewa jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam mbele ya jopo la Mahakimu Wakazi John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela na mawakili wa utetezi, Hurbet Nyange, Peter Swain a Elisa Msuya, wakati wakipinga kielelezo ambacho ni barua iliyoandikwa na Mamlaka ya Mapato (TRA) kwenda kwa Mramba ambapo kwa mujibu wa barua hiyo, TRA ilikataa kampuni ya Alex Stewart Government Bussiness Corporation kupewa msamaha wa kodi.

Wakili Nyange kwa niaba ya mawakili wengine wa utetezi alitoa shutuma hizo muda mfupi baada ya Wakili Mwandamizi wa Serikali Fredrick Manyanda ambaye alikuwa akimuongoza shahidi wake wa sita, Ludovick Kandege, kutoa ushahidi wake alipoiomba mahakama ipokee barua kama hiyo ambayo iliandikwa na shahidi huyo mwaka 2003 kama kielelezo.

“Kwa ujumla tunapinga kielelezo hicho (orginal) kisipokelewe kwa sababu ni cha kughushi na kimetofautiana kabisa na nakala ya kielelezo walichonacho upande wa utetezi ambacho walipewa na upande huo wa mashtaka…kwani zinatofauti kubwa sana; nakala tuliyopewa sisi haina ‘indosement’ lakini kielelezo hiki kinachotaka kutolewa na shahidi huyu kina indosement. Kielelezo tulichopewa sisi kinaonyesha barua hiyo iliandikwa Oktoba 7 mwaka 2003 lakini kielelezo kinachotaka kutolewa sasa kinaonyesha barua hiyo iliandikwa Septemba 7 mwaka 2003.


“Kielelezo tulichopewa sisi kinaonyesha namba ya Faksi ya TRA ni tofauti na namba ya Faksi ya TRA kwenye kielelezo kinachotaka kutolewa leo(jana),na hata saini za mwandishi wa barua hiyo zinapishana herufu…licha maudhui ya vielelezo hivyo halisi na nakala yanafanana,kwenye kielelezo walichopewa wao chini TRA inanukta lakini kwenye kielelezo halisi kwenye neno TRA hakuna nukta…kwa sababu hizo sisi tunataka kielezo hicho kisipokelewe kwani hakifanani na nakala ya kielezo tulichopewa na upande wa mashitaka na tunachokiona upande wa Jamhuri umenza kuleta vielelezo vya kughushi.

“Na tunapinga kwamba TRA haijawahi kumwandikia mshitakiwa wa kwanza hiyo hiyo barua ya iliyokuwa ikimshauri asitoe msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo….na ninarudia tena kwa tofauti hizo nilizozianisha nadiriki kutamka kwamba kuna namna fulani ya kughushi katika kuleta kielelezo hiki mahakamani.

“Upande wa mashitaka wenyewe hapo mahakamani umekiri kwamba ni wao ndiyo umetupa nakala ya barua hiyo …swali la kujiuliza hivi mtu anapoenda kutoa fotokopi siinatoka nakala ile ile sasa kwani upande wa mashitaka katika kesi hii unaleta barua halisi ambayo inatofautiana na nakala halisi?alidai Nyange na kusababisha watu kuangua vicheko mahakamani

Akijibu shutuma hizo, Wakili Manyanda alidai kielelezo hicho kinafanana na nakala waliyowapatia upande wa utetezi na kuamua kueleza kweli ila mchapishaji wa barua hiyo alikosea kuandika mwezi na usahihi ni kwamba barua hiyo iliandikwa Septemba 7 mwaka 2003 na siyo Oktoba 7 mwaka huo kama inavyosomeka kwenye nakala ya barua hiyo ambayo upande wa Jamhuri ndiyo uliwapatia upande wa utetezi.

Hata hivyo jopo la mahakimu hao, lilisema uamuzi wa barua hiyo ipokelewe kama kielezo au la itautoa Aprili 15 mwaka huu kesi hiyo itakapokuja kwa ajili ya kutajwa na akautaka upande wa utetezi usimuulize maswali shahidi huyo ambayo yatatokana na barua hiyo hadi hapo jopo hilo litakapotoa uamuzi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Machi 20 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.