Header Ads

SERIKALI YAMNG'ANG'ANIA LIYUMBA

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa jamhuri katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba umeiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imuone mshitakiwa ana kesi ya kujibu.


Ombi hilo liliwasilishwa mahakamani hapo jana saa tisa alasiri kwa njia ya maandishi yaliyochukua kurasa 29 na Mkuu wa Kitengo cha Sheria cha Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ben Lincoln na wakili wa serikali Prosper Mwangamila.
Kuwasilishwa kwa ombi hilo kulitokana na amri iliyotolewa Machi 15, mwaka huu, na kiongozi wa jopo la mahakimu wakazi wanaosikiliza kesi hiyo, Edson Mkasimongwa ambaye alizitaka pande zote kuwasilisha maombi kwa njia ya maandishi.

Kwa mujibu wa nakala ya ombi hilo ambalo gazeti hili lina nakala yake, upande wa jamhuri umedai kwa mujibu wa vielelezo 12 walivyotoa mahakamani na mashahidi wanane waliowaleta, wameweza kutoa ushahidi thabiti dhidi ya mshitakiwa ambao utaishawishi mahakama hiyo imuone ana kesi ya kujibu na kuongeza kuwa wanaiomba mahakama hiyo itupilie mbali ombi la utetezi lililotaka mahakama imuone mshitakiwa huyo hana kesi ya kujibu kwa sababu halina msingi.

Wakichambua shitaka la matumuzi mabaya ya ofisi ya umma kinyume na kifungu cha 91(1) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002, jamhuri imejigamba kuwa imeweza kuthibitsha shitaka hilo kwa sababu mshitakiwa huyo ni kweli alikuwa mtumishi wa serikali toka mwaka 1971-2007 na kwamba alikuwa na cheo wakati wa mradi wa 10 Milambo Office Extention na alikuwa na jukumu la kuusimamia na kwamba kwa mujibu wa shahidi 1, 2, 3, 5, 6 na 8 waliithibitishia mahakama kuwa mradi huo ulikuwa ukiratibiwa na ofisi aliyokuwa akiongoza Liyumba ya Utumishi na Utawala.

Wakichambua shitaka la pili la kuisababishia serikali hasara, upande wa jamhuri umejigamba kuwa umeweza kuthibitisha shitaka hilo kwa madai kuwa hoja iliyodaiwa na upande wa utetezi kuwa haiwezekani kutambua hasara iliyopatikana bila ripoti ya mwisho ya mradi kukamilika si ya msingi kwani hata ikitolewa haiwezi kubadili makadirio ya gharama za mradi.

‘Kwahiyo hoja kwamba ripoti ya mwisho ya mradi haijatoka na kwamba hiyo ndiyo ingetuwezesha sisi kujua kuna hasara imepatikana si ya msingi..kwani hata hiyo ripoti ya mwisho ya mradi ikitolewa leo haiwezi kubadili gharama zilizokadiliwa na Mkadiliaji majengo hivyo sisi tunagemea ushahidi uliotolewa na shahidi wa saba na tunasisitiza kwamba mshitakiwa huyo ameisababishia serikali hasara kwa kufanya ongezeko la mabadiliko ya mradi na hivyo ongezeko hilo limesababisha serikali kutumia fedha nyingine za ziada kwaajili ya ujenzi huo”alidai.

Kuhusu hoja ya upande wa utetezi iliyodai upande wa mashitaka umeshindwa kuthibisha kwamba mshitakiwa huyo alitenda makosa hayo akiwa na nia ovu, umedai kuwa katika kesi za jinai hoja hiyo haina msingi.

Machi 22 mwaka huu, mawakili wa utetezi Majura Magafu, Onesmo Kyauke, Hudson Ndusyepo na Jaji Mstaafu Hillary Mkate waliwasilisha hoja zao wakitaka mahakama hiyo imuachilie huru mshitakiwa huyo kwa sababu upande wa mashitaka umeshindwa kuthibitisha kesi yao.

Kwa sababu tayari pande zote mbili katika kesi hiyo zimekwisha wasilisha hoja zao, kiongozi wa jopo la mahakimu wakazi, Mkasimongwa, Lameck Mlacha na Benedict Mwingwa, April 9 mwaka huu, wanatarajiwa kutoa uamuzi wao kuhusiana na hoja hizo.

Januari 27, mwaka jana, Liyumba na Meneja Mradi wa Benki Kuu, Deogratius Kweka, walifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza na kusomewa mashitaka hayo ya kuidhinisha mradi wa majengo ya minara pacha bila idhini ya bodi ya wakurugenzi na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221.

Mei 27 mwaka jana, mahakama hiyo iliwafutia kesi, lakini muda mfupi baada ya kuachiliwa walikamatwa tena mahakamani hapo na Mei 28 mwaka jana, Liyumba peke yake ndiye aliyerudishwa mahakamani hapo na kusomewa mashitaka hayo na Kweka akawa ameachiliwa huru. Tangu kipindi hicho hadi sasa Liyumba anaendelea kusota rumande, baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana, ambapo mahakama ilimtaka atoe fedha taslimu au hati ya mali yenye thamani ya sh bilioni 111

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Machi 30 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.