BALALI ATAJWA TENA KESI YA EPA
Na Happiness Katabazi
MSHTAKIWA wanne katika kesi ya wizi wa zaidi ya  sh.bilioni 3.9 katika  Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania,  Imani Mwakosya (54) jana ameileleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salama, kuwa aliyekuwa gavana wa wakati huo marehemu Daudi Balali  ndiye aliyeidhinisha kiasi hicho cha fedha kilipwe kwa kampuni ya  Mibare Farm kwakuwa ilionekana ni deni halali.
Mwakosya anayetetewa na wakili wa kujitegemea Majura Magafu alitoa maelezo hayo mbele ya jopo la majaji Samuel Kalua,Beatrice Mutungu na Hakimu Mfawidhi Ilvin Mugeta wakati akitoa utetezi wake 
Mshtakiwa huyo ambaye alikuwa kifanya kazi idara ya Madeni BoT,alidai kuwa nyaraka  mbalimbali vilizowasilishwa BoT na kampuni hiyo wakati ikiombwa   kulipwa fedha hizo,zilionekana ni halali baada ya kupitiwa na maofisa mbalimbali wa benki hiyo.
Mwakosya alizitaja baadhi ya nyaraka hizo kuwa  ni pamoja na hati ya makabidhiano ya kuamisha  deni hilo baina ya Kampuni ya Mibare Farm na Kampuni ya Lackshim Textile Mills Ltd ya India.
Alidai kuwa deni hilo pia lilionekana katika mtandao wa BoT huku taarifa zake zikionekana kulingana na vielelezo zilivyowasilishwa na kampuni ya Mibare Farm wakati wakidai deni hilo.
"Napenda  mahakama ielewe kuwa  malipo yalifanyika kihalali kwasababu vithivitisho vyote  vilivyotakiwa kuthibitisha deni vililetwa BoT na vilitiwa na vikaonekana halali na ndipo gavana alipitisha malipo hayo"alidai Mwakosya.
Alidai kuwa katika mchakato wa ulipwaji wa deni hilo yeye aliwahi kuandika dokezo la kulipwa kwa deni hilo kwenda kwa gavana.
Alidai kuwa kampuni ya Kampuni ya Lackshmi Textile Mills Ltd ya India ilikuwa inaidai  serikali ya Tanzania Yeni milioni 307,595,400 pamoja na fedha za india rupia milioni 29,220,686.92 ambazo ni sawa na sh.bilioni 3,868,805,737.13
Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Kada wa CCM Rajabu Maranda,Farijala Hussein ambao tayari wameishafungwa jela jumla ya miaka nane katika kesi mbili tofauti za EPA, Ajay Somani, Ester Komu na Sophia Lalika.
Katika kesi hiyo washitakiwa hao wanadaiwa  kula njama,kugushi na kuiba zaidi ya Shbilioni 3 .8 kutoka BoT, baada kudanganya kuwa imepewa deni na Kampuni ya Lackshim Textile Mills Ltd ya India na kujipatia inginzo hilo.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Julai 31 mwaka 2012
 
 
 
No comments:
Post a Comment