Header Ads

KESI YA CHE MUNDUGWAO YAZIDI KUSOMBA WASHITKIWA



Na Happiness Katabazi

WAKAZI wawili wa Dar es Salaam,jana walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu  kwaajili  ya hapo baadae kuja kuunganishwa katika kesi ya wizi wa Paspoti 26 inayomkabili Msainii wa Muziki wa asili, Chingwele Che Mundugwao na wenzake wanne.

Wakili wa serikali  Aidah Kisumo mbele Hakimu Mkazi Sundi Fimbo aliwataja washitakiwa hao walifikishwa jana kwa mara ya kwanza mahakamani hapo wakikabiliwa na makosa yanayofanana ambayo yanamkabili Chemundugwao na wenzake ni  Rajab Momba na Haji Mshamu.

Akiwasomea mashitaka Momba na Mshamu, Wakili Kisumo alidai kuwa tarehe isiyofahamika washitakiwa walikula njama ya kutenda kosa. Aidha tarehe tofauti Dar es Salaam, Momba aliiba hati ya kusafiria yenye namba AB 651926 mali ya serikali.

Alidai Momba, Mshamu na Iqbal wanadaiwa tarehe isiyofahamika Dar es Salaam, walighushi hati ya kusafiria yenye namba hiyo, kuonesha ni halali na imetolewa na Idara ya Uhamiaji ya Tanzania jambo ambalo si kweli.

Mbali na Che mundugwao washitakiwa hao wataunganishwa na Raia wa Uingereza Ahsan Iqbal au Ali Patel, Ofisa  Ugavi wa  Idara ya Uhamiaji Shemweta Kiluwasha, Injinia Keneth Pius wa Kikosi  cha Zimamoto na Uokoaji na mfanyabiashara Ally Jabir.

Hata hivyo washitakiwa  hao walikana mashitaka na kurudishwa rumande kwa kuwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP),Dk.Eliezer Feleshi  aliwasilisha hati ya kuwafungia dhamana washitakiwa hao wawili kama alivyofanya kwa kina Chemunduwao na wenzake na kwamba  upelelezi bado haujakamilika na kesi itatajwa tena Julai 22, mwaka huu, ili waunganishwe na Chemundugwao ambapo kesi yao nayo imepangwa kuja kutajwa Julai 22 mwaka huu.

Juni 3 mwaka huu, Chemundugwao na wenzake walifikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani hapo wakikabiliwa na makosa mbalimbali yakiwemo kosa la wizi wa paspoti 26, ambapo hata hivyo DPP aliwasilisha hati ya kuwafungia dhamana ambapo hadi sasa wapo gerezani.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Julai 19 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.