Header Ads

KESI KUBWA YA UFISADI YAFUTWA

•HAKIMU AITAKA SERIKALI KUWA MAKINI NA MIKATABA

Na Happiness Katabazi

HATIMAYE Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, jana iliwaachia huru ofisa ugavi kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Elias Mziray, na maofisa wenzake wanne waliokuwa wakikabiliwa na makosa matatu ya kula njama ya wizi wa sh milioni 119.


Mahakama hiyo, ilifikia uwamuzi huo baada ya kuwaona washtakiwa wote kwa pamoja hawana kesi ya kujibu.

Mbali na Mziray, washtakiwa wengine ni Ofisa Manunuzi, David Kakoti, Gene Moshi na Mhasibu Joseph Rweyemamu ambao wote ni watumishi wa wizara hiyo, ambao walikuwa wakitetewa na wakili wa kujitegemea Hudson Ndusyepo.

Uamuzi huo, ulitolewa jana na Hakimu Mkazi, Stewart Sanga, ambaye bila kumung'unya maneno alisema baada ya kupitia ushahidi wa mashahidi nane na vielelezo vilivyowasilishwa mahakamani hapo na upande wa mashtaka, amebaini kwamba upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha kesi hiyo, kitendo ambacho kinampa msukumo kuifuta kesi hiyo.

Hakimu Sanga, akichambua shtaka la kwanza ambalo ni la kula njama, alisema Jamhuri umeshindwa kuthibitisha shtaka hilo kwa sababu kisheria kosa la kula njama ni lazima washtakiwa wote wakubaliane kutenda, kosa ambalo limekatazwa kisheria lakini katika kesi hiyo, mashahidi wote wa Jamhuri wakati wakitoa ushahidi wao waliambia mahakama kuwa washtakiwa walitenda kazi yao ya kutoa tangazo la zabuni na kumtafuta zabuni, kumlipa fedha mzabuni kwa kufuata sheria hivyo mahakama hiyo haijaona kama washtakiwa walitenda kosa.

Akilichambua shtaka la pili ambalo ni wizi, alisema mashahidi wote wameshindwa kuthibitisha shtaka hilo, kwani kumbukubu za kibenki na hundi ambazo zilitolewa kama vielelezo vinaonyesha wazi mzabuni alilipwa kwenye akaunti yake na hakuna shahidi hata mmoja aliyeieleza mahakama washtakiwa hao walinufaika binafsi na fedha hizo na kuongeza kuwa ni wazi Jamhuri, ilifahamu mapema fedha aliyelipwa ni nani kwani ni Jamhuri hiyo hiyo ndiyo iliyopeleka ‘Bank Statement’ na hundi kama vielelezo ambavyo vyote vinaonyesha jina la mzabuni aliyelipwa fedha hizo.

Hakimu Sanga, akichambua shtaka la tatu ambalo ni la kusababisha hasara, alisema pia Jamhuri imeshindwa kuthibitisha, kwani washtakiwa wote ni watumishi wa umma na walifanya kazi kwa nafasi zao, hivyo walifuata taratibu zilizokuwepo tena kwa kufuata utaratibu wa Sheria ya Manunuzi ya Umma.

Hata hivyo, alikemea mtindo wa wizara kuwaruhusu watumishi wa umma wasio na taaluma ya kuandaa vitu vya kitaaluma, kama mikataba kufanya hivyo ndiko kunakosababisha wizara na serikali kwa ujumla kupata hasara.

Wakati Mhasibu Mkuu wa Wizara, ambaye alikuwa shahidi wa nane, naye aliidhinisha malipo kwa mzabuni huyo bila kuusoma mkataba huo.

Alidai hao, ndiyo walipaswa kuwajibishwa kwanza kwa sababu ndiyo waliyoingiza wizara hiyo kwenye mkataba wenye utata.

“Mtu wa kwanza kulaumiwa kwa kuisababishia wizara hiyo hasara ni Katibu Mkuu ambaye kwa uzembe wake alisaini mkataba bila kuusoma na kujua kuna nini ndani yake, matokeo yake akaidhinisha mzabuni alipwe na mwingine ni Mhasibu Mkuu wa wizara hiyo kwa kupitisha malipo hayo hivyo washtakiwa hao hawawezi kuitwa wezi kwa sababu fedha zinaonekana zilikwenda sehemu husika,” alisema Hakimu Sanga.

Mwaka jana, washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo kwa mbwembwe na upande wa Jamhuri ukidai kuwa mwaka 2005 mpaka sasa Kampuni ya Ostergaad & Invest Ltd iliyoshinda zabuni ya kuiuzia wizara hiyo pikipiki 25 na kulipwa sh 119, 530,000, hazijaleta huku wakidai mmiliki wake Yahaya Mhina alifariki dunia.

Pia Jamhuri ilidai kuwa Juni 17, 2005 katika wizara hiyo,washtakiwa wakiwa ni watumishi wa umma, walishindwa kutekeleza majukumu yao na kuisababishia serikali kupata ya hasara ya kiasi hicho cha fedha.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Julai 3 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.