Header Ads

WAZIRI APINGA KULIPA MILIONI 100/=

Na Happiness Katabazi

NAIBU Waziri wa Wizara ya Sayansi na Teknolojia na Mawasiliano, Dk.Maua Daftari amewasilisha rasmi hati ya nia ya kukata rufaa katika Mahakama ya Rufani nchini,akipinga hukumu ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,iliyotolewa mwishoni mwa wiki ambayo ilimwamuru alimpe aliyekuwa mlalalamikaji Fatma Said, Sh milioni 100.7


Hati hiyo iliwasilishwa jana chini ya hati ya kiapo kupitia wakili wa Dk.Daftari, Peter Swai ambapo amedai anakusudia kukata rufaa katika mahakama hiyo ya juu nchini na kuonyesha kasoro zilizopo kwenye hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu ambayo ilisomwa kwa mara ya pili Ijumaa iliyopita na Jaji Fedrica Mgaya na kwamba endapo atakubali kutekeleza amri hiyo ataathirika mno.

“Endapo nitakubali kulipa kiasi hicho cha fedha nitaathirika sana kwani hakuna ubishi mimi nimtumishi wa umma na kiwango hicho nilichoamuriwa nikilipe nikikubwa ambacho kitaniliazimu kuuza vifaa vyangu vyote ikiwemo nyumba ninayokaa na familia yangu…na mdaiwa hatapata hasara yoyote endapo rufaa yangu sitashinda hivyo mimi ni mtumishi wa umma na anwani yangu inafahamika ila huyo mdaiwa anwani yake haifahamiki”alidai Waziri Maua Daftari.

Aidha aliomba mahakama ya rufaa itoe amri ya kusitisha utekelezwaji wa hukumu ya Mahakama Kuu kwani endapo uamuzi huo utabaki kama ulivyo, ataathirika zaidi nakuongeza kuwa anaomba apatiwe nakala ya hukumu hiyo ili aweze kuisoma na kuandaa rufaa yake ambayo ataiwasilisha mahakamani hapo ndani ya kipindi kifupi kwani anaamini hukumu ya mahakama kuu haijamtendea haki na imejaa makosa.

Ijumaa iliyopita Jaji Mgaya alisoma hukumu hiyo kwa mara ya pili, mara ya kwanza ilisomwa na Jaji Laurian Kalegeya ambapo alimwamuru Dk.Daftari amlipe Fatma Salim, kiasi hicho cha fedha baada ya kubaini alivunja mkataba na mlalamikaji huyo. Jaji Fedrica, alisema amefikia uamuzi wa kutoa amri ya kumtaka mdaiwa (Dk. Daftari), alipe kiasi hicho cha fedha mdaiwa badala ya sh milioni 410, kiasi ambacho mdaiwa aliomba amlipe, baada ya kubaini madai mengine katika hati ya madai, Dk. Daftari ameshindwa kupeleka ushahidi wa kuthibitisha madai hayo.

Jaji Mgaya, alisema dai la sh milioni 1,760 ni dai ambalo limeweza kuthibitishwa kwa vielelezo kwa sababu mdaiwa na mlalamikaji waliandikishiana kisheria na ndiyo maana ameamuru mdaiwa amlipe kiasi hicho.Matukio hayo, yalitendeka kati ya mwaka 1994-1996 na kesi hiyo ilifunguliwa mahakamani hapo mwaka 1999 na mlalamikaji dhidi ya naibu waziri huyo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Julai 14 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.