Header Ads

SERIKALI ISIFUNGUE KESI KWA KUKURUPUKA

Na Happiness Katabazi

JULAI 2, mwaka huu, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, Stewart Sanga alimwachia huru ofisa ugavi wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Elias Mziray, na maofisa wenzake wanne waliokuwa wakikabiliwa na makosa matatu ya kula njama ya wizi wa sh milioni 119.


Mbali na Mziray, washitakiwa wengine ni Ofisa Manunuzi, David Kakoti, Gene Moshi na Mhasibu, Joseph Rweyemamu, ambao wote ni watumishi wa wizara hiyo, ambao walikuwa wakitetewa na wakili wa kujitegemea, Hudson Ndusyepo.

Uamuzi huo, ulitolewa siku hiyo na Hakimu Mkazi Sanga, bila kumung'unya maneno alisema baada ya kupitia ushahidi wa mashahidi wa nane na vielelezo vilivyowasilishwa mahakamani hapo na upande wa Jamhuri, ameona washitakiwa hawana kesi ya kujibu kwasababu amebaini kwamba upande wa Jamhuri ulishindwa kuthibitisha kesi hiyo, kitendo ambacho kilimpa msukumo kuifuta kesi hiyo ya jinai namba 117 ya mwaka 2009.

Hakimu Sanga, akichambua shitaka la kwanza ambalo ni la kula njama, alisema Jamhuri ilishindwa kuthibitisha shitaka hilo kwa sababu kisheria kosa la kula njama ni lazima washitakiwa wote wakubaliane kutenda kosa ambalo limekatazwa kisheria lakini katika kesi hiyo, mashahidi wote wa Jamhuri wakati wakitoa ushahidi wao waliieleza mahakama kuwa washitakiwa walitenda kazi yao ya kutoa tangazo la zabuni na kumtafuta mzabuni, kumlipa fedha mzabuni kwa kufuata sheria hivyo mahakama hiyo haijaona kama washitakiwa walitenda kosa.

Akilichambua shitaka la pili ambalo ni wizi, alisema mashahidi wote wameshindwa kuthibitisha shitaka hilo, kwani kumbukumbu za kibenki na hundi ambazo zilitolewa kama vielelezo vinaonyesha wazi mzabuni alilipwa kwenye akaunti yake na hakuna shahidi hata mmoja aliyeieleza mahakama washitakiwa hao walinufaika binafsi na fedha hizo na kuongeza kuwa ni wazi Jamhuri, ilifahamu mapema fedha aliyelipwa ni nani kwani ni Jamhuri hiyo hiyo ndiyo iliyopeleka ‘Bank Statement’ na hundi mahakamani hapo ili zitumike kama vielelezo, ambapo vielelezo hivyo viwili vyote vinaonyesha jina la mzabuni ambaye ndiye aliyelipwa fedha hizo.

Hakimu Sanga akichambua shitaka la tatu, ambalo ni la kusababisha hasara, alisema pia Jamhuri imeshindwa kulithibitisha, kwani washitakiwa wote ni watumishi wa umma na walifanya kazi kwa nafasi zao, hivyo walifuata taratibu zilizokuwepo tena kwa kufuata utaratibu wa Sheria ya Manunuzi ya Umma.

Hata hivyo ambaye ni miongoni mwa mahakimu vijana mahakamani hapo, alikemea vikali mtindo wa wizara kuwaruhusu watumishi wa umma wasio na taaluma ya kuandaa masuala ya kitaaluma, kwani kufanya hivyo ndiko kuna kosababisha wizara na serikali kwa ujumla kupata hasara na kuongeza kuwa washitakiwa hao hawakupaswa kutuhumiwa kwa kosa la wizi.

Wakati Mhasibu Mkuu wa Wizara, ambaye alikuwa shahidi wa nane, naye aliidhinisha malipo kwa mzabuni huyo bila kuusoma mkataba huo.

Alisema hao ndio walipaswa kuwajibishwa kwanza kwa sababu ndio walioiingiza wizara hiyo kwenye mkataba huo wenye utata.

Mwaka jana washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo kwa mbwembwe na upande wa Jamhuri ukidai kuwa mwaka 2005 mpaka sasa Kampuni ya Ostergad & Invest Ltd iliyoshinda zabuni ya kuiuzia wizara hiyo pikipiki 25 na kulipwa sh 119, 530,000, hazijaletwa huku wakidai mmiliki wake Yahaya Mhina alifariki dunia.

Pia wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Kyando alidai kuwa Juni 17, 2005 katika wizara hiyo, washtakiwa wakiwa ni watumishi wa umma, walishindwa kutekeleza majukumu yao na kuisababishia serikali kupata hasara ya kiasi hicho cha fedha.

Katika hatua nyingine, Fukuto la Jamii linawakumbusha wasomaji wake kuwa Juni 16 mwaka huu, mahakama hiyo ilimfutia kesi Naibu Mkurugenzi wa Misitu na Nyuki, Dk. Ismail Kelly Alloo, baada ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kuwasilisha mahakamani hapo hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea kumshitaki mshitakiwa huyo.

Itakumbukwa Alloo naye alifikishwa kwa mbembwe na makachero na wanasheria wa Takukuru mahakamani hapo Novemba mwaka jana, mbele ya Hakimu Mkazi Paul Kimicha na wakili wa taasisi hiyo Kasuni Nkya alidai kuwa Mei 2, mwaka 2005, mshitakiwa anadaiwa kutenda kosa la matumizi mabaya ya ofisi ya umma kwa kuruhusu mauzo ya magogo kinyume cha sheria.

Shitaka la pili, ni kuwa Machi 17 mwaka 2005 katika ofisi za makao makuu ya Takukuru jijini Dar es Salaam, wakati wa uchunguzi wa matumizi mabaya ya rushwa, mshitakiwa alitoa taarifa za uongo kuhusu tangazo la mazao ya misitu mali ya Kampuni ya Aqeel Traders Ltd. Pamoja na kwamba upande wa Jamhuri ulidai upelelezi wa kesi hiyo ulikuwa umekamilika, kesi hiyo ilikuwa ikitajwa mahakamani hapo hadi mshitakiwa alipofutiwa kesi hiyo na DPP.

Fukuto la Jamii linapenda kumpongeza Hakimu Mkazi Stewart Sanga kwa ujasiri wake wa kuweza kufuata sheria na haki kama ambavyo taaluma yake inavyomtaka katika kuifuta kesi hiyo ambayo ni miongoni mwa kesi zilizopewa jina la ‘kesi za ufisadi’, ambazo kwa sisi waandishi wa habari za mahakamani tumeshuhudia kesi hizo zikifunguliwa mahakamani hapo kwa mbwembwe nyingi na kufuatiliwa kwa karibu na mashushushu ambao walikuwa wakihudhuria kesi hizo kwa mitindo mbalimbali, hali ambayo baadhi ya mahakimu wengine wamekuwa wakijikuta wakiogopa kutoa haki katika baadhi ya aina hiyo ya kesi kwa kigezo kuwa kesi hizo zinafuatiliwa na ‘manusanusa’.

Fukuto la Jamii linampongeza Hakimu Sanga kwani yote hayo hakuyajali, alichozingatia ni sheria na maadili ya kazi yake na si kisingizo cha maslahi ya taifa, kisingizio cha sasa hivi taifa lipo kwenye mapambano dhidi ya wabadhirifu wa fedha za umma.

Alichozingatia ni matakwa ya sheria na hivyo ndivyo tunataka mahakimu na majaji wetu wazingatie hilo kama taaluma yao inavyowataka na si vinginevyo.

Tunaamini kabisa wachunguzi wa TAKUKURU waliopeleleza kesi hiyo walitumia rasilimali na muda wa walipa kodi kupeleleza kesi hiyo, hivyo nasisitiza wananchi tuna haki ya kuwalaumu na kuhoji ni kwanini wameshindwa kufanya vizuri katika kesi hii licha ya kwa mujibu wa dhana ya sheria, kesi inapofunguliwa mahakamani kuna kushinda kesi au kushindwa.

Kwa muktadha huo hapo juu, Fukuto la Jamii linahoji umakini na weledi wa wachunguzi toka TAKUKURU ambao walipeleleza kesi Na. 117/2010 uko wapi?

Hivi hawa wapelelezi wa kesi na mawakili wa serikali wanafahamu kwamba ukosefu wao wa umakini katika kupeleleza kesi au kuendesha kesi ambapo mwisho wa siku wanamfungulia kesi mtu ambaye hakustahili kufunguliwa kesi.

Wananchi tujiulize hivi mchunguzi aliyefundwa chuoni, anaweza kufanya upelelezi wa kesi kama hiyo ambayo matokeo yake tumeona wachunguzi hao walikusanya vielelezo ambavyo ni hundi na bank statements ambazo hazioani na sheria waliyoitumia kuwashitaki washitakiwa hao?

Kwa mujibu wa kesi hiyo, upande wa Jamhuri ulileta bank Stament na hundi kama vielelezo ili viweze kusaidia kesi yao kushinda, wakati vielelezo hivyo vimeonyesha wazi wizara hiyo ilimlipa kiasi hicho cha fedha mzabuni na wakati huo hati ya mashitaka inadai washitakiwa walikula njama, waliiba na kusababisha hasara ya sh milioni119.

Hivi tuiulize Takukuru na ofisi ya DPP iliamua kuifungua kesi hiyo mahakamani kwa sababu gani?

Je, walifungua kweli kwakutaka kuona haki inatendeka au waliamua kuwafungulia kesi hiyo kwa ajili ya mashinikizo ya wanasiasa?

Au taasisi hizo zilihakikishiwa na wazandiki na wambeya kwamba wafungue kesi hiyo haraka, mbele ya safari wazandiki hao wangezipelekea taasisi hizo ushahidi mzito ambao ungeweza kuwabana washtakiwa hao?

Au Watanzania tuziulize taasisi hizo mbili, shitaka la kusababisha hasara linawababaisha hawa wapelelezi wetu na waendesha mashitaka wetu au shitaka hilo limekuwa ni fasheni sasa ya kuwaumiza watu ambao hawana hatia ila tu taasisi hizo zinaamua kuwafungulia kesi wananchi wenzetu kwa ajili ya majungu au kujipatia umaarufu wa kipuuzi? Fukuto la Jamii linapata wakati mgumu kuelewa hilo.

Watanzania huu ni mzaha mbaya katika matumizi ya rasilimali za walipa kodi na muda wa mahakama kusikiliza kesi zisizokuwa na kichwa wala miguu kama hiyo iliyoandaliwa ovyo ovyo na upande wa Jamhuri ambapo mwisho wa siku Rais Jakaya Kikwete akiwa nyumbani kwa Baba wa Taifa-Butiama mwaka jana, aliwahutubia wana CCM na wananchi kwa ujumla akiwaeleza wananchi hao kwamba mtu akiwauliza wananchi serikali ya awamu ya nne imefanya nini tangu iingine madarakani, wamjibu serikali yake imeweza kufungua kesi za ufisadi mahakamani.

Sasa kama rais wa nchi anatamba kwamba uongozi wake umeweza kuimarisha utawala wa sheria ikiwa ni pamoja na kufungua kesi za ufisadi mahakamani zinazowahusu vigogo na matokeo yake baadhi ya kesi hizo kumbe zimeandaliwa ovyo ovyo na wapelelezi na waendesha mashitaka, ina leta picha gani kwa umma?

Aiingii akilini mchunguzi na mwanasheria makini na anayethamini utu wake na utu wa binadamu mwenzake kukubali kupeleleza na kufungua kesi hiyo kwa kigezo cha kuwa na vielelezo kama hivyo ambayo mwisho wa siku serikali yetu imejikuta imepoteza fedha za walipa kodi kwa ajili ya kuwawezesha wachunguzi.

Na mahakama imepoteza muda wa kusikiliza kesi kama hiyo na mwisho wa serikali ya awamu ya nne chini ya Rais Jakaya Kikwete imeendelea kusukumiwa kwa chini chini zigo la tuhuma kuwa ni serikali ya kionevu, kwani imekuwa ikiwabambikia kesi baadhi ya maofisa wa serikali kwa uonevu na visasi ili serikali ijipatie umaarufu wa kwamba inapambana na ufisadi.

Na siyo siri tuhuma hiyo kila kukicha imekuwa ikiwahusisha baadhi ya viongozi wakuu wa nchi kwamba kuna baadhi ya washtakiwa wanafikishwa mahakamani kwa kukomolewa kwa sababu wakati wapo serikalini walikuwa mabingwa wa kupora mahawala wa vigogo wenzao.
Tuhuma hizi zinazoelekezwa kwa serikali ya awamu ya nne ziwe na ukweli ndani yake au la, Fukuto la Jamii linasema tuhuma hiyo inaipaka matope, kwani si nzuri na inaamsha chuki baina ya ndugu, jamaa wa washitakiwa waliofunguliwa kesi na wale walioshinda kesi hizo dhidi ya serikali ya awamu ya nne.

Sasa ili serikali kujiondoa katika tuhuma hiyo, ione wakati umefika wa kupeleka muswada bungeni utakaoweza kuwabana wapelelezi wanaopeleleza kesi za jinai bila umakini na ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) ambayo ndiyo yenye dhamana ya kutoa kibali cha kesi za jinai kufunguliwa mahakamani ambapo mwisho wa siku serikali inashindwa vibaya kesi hizo.

Naamini hilo likifanikiwa hawa wapelelezi na ofisi ya DPP ambao wamepewa dhamana hizo watakuwa makini na kamwe hawatakubali kufungua kesi mahakamani kwa mashinikizo ya wanasiasa ili wakubwa wao wazione taasisi hizo zinafanya kazi kwa kupeleka baadhi mahakamani kumbe ni upuuzi mtupu wanaoupeleka mahakamani ambao haulisaidii taifa badala yake unaliumiza taifa letu na washitakiwa na ndugu zao.

Hakuna ubishi kwamba kila kukicha wananchi mbalimbali akiwemo Mkurugenzi wa Takukuru, Dk. Edward Hosea ambaye kwa zaidi ya mara mbili amenukuliwa kwenye vyombo vya habari akiilalamikia mahakama kwamba inachelewesha kumalizika na wala mahakama hiyo haitoi kipaumbele kwa kushughulikia haraka kesi kubwa ambazo ni za kifisadi na kwamba DPP - Eliezer Feleshi, amekalia kesi zaidi ya 60 za ufisadi ambazo taasisi yake ilishakamilisha upelelezi na kuzikabidhi ofisini kwa DPP.

Lakini cha kushangaza hadi sasa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeshatolea uamuzi kesi tatu ambazo aliziita kesi kubwa ambazo zimepelelezwa na ofisi yake lakini hadi sasa hatujamsikia kiongozi huyo akijitokeza hadharani kuupongeza mhimili wa mahakama kwa kuweza kuzimaliza kesi hizo ndani ya kipindi kifupi ukilinganisha na kesi nyingine za walalahoi ambazo zinachukua zaidi ya miaka minne na kuendelea mahakamani.

Mfano, kesi ya matumizi mabaya ya ofisi za umma iliyokuwa ikimkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu, Amatus Liyumba, ambayo ilifunguliwa mahakamani hapo Januari 27 mwaka jana na ikamalizika Mei 24 mwaka huu.

Kesi nyingine ni Na. 117/2009 iliyomalizika Julai 2 mwaka huu, kesi iliyokuwa ikimkabili Naibu Mkurugenzi wa Misitu na Nyuki, Dk. Ismail Kelly Alloo ambayo ilifunguliwa Novemba mwaka jana na ikamalizika Juni mwaka huu.

Siku mbili baadaye baada ya Liyumba aliyefungwa miaka miwili jela, tulimsikia Dk. Hosea kupitia vyombo vya habari akishangilia hukumu hiyo na kujigamba kwamba hukumu hiyo ni matunda ya kazi nzuri ya upelelezi iliyofanywa na taasisi yake.

Lakini chakushangaza, Dk. Hosea hatujamsikia tena akichomoza kwenye vyombo vya habari akiwaeleza wananchi kuhusu uamuzi wa Hakimu Sanga uliowaachiria huru maofisa wanne wa Wizara ya Maliasili wala uamuzi wa DPP wa kumfutia kesi Dk. Alloo.

Tumuulize Dk. Hosea ameamua kukaa kimya kwa sababu upelelezi uliofanywa na taasisi yake umeshindwa kufurukuta kwenye kesi hizo mbili ambayo moja imefutwa na mahakama baada ya kubaini ushahidi ulioletwa na upande wa mashitaka ni dhahifu na kesi nyingine ilifutwa na mahakama hiyo baada ya DPP-Feleshi kuwasilisha hati ya kuondoa kesi hiyo kwasababu hana haja kuendelea na kesi hiyo?

Namshauri Dk. Hosea asijitokeze kwenye vyombo vya habari kushangilia kesi wanazoshinda tu , awe mwepesi pia kujitokeza na kueleza umma pindi baadhi ya kesi zake zinaposhindwa kufurukuta mahakamani ili umma ujue ni kwanini ushahidi uliokusanywa na vijana wake ulikuwa ni dhahifu, kwasababu binafsi naamini kiongozi huyo ameishajiwekea utamaduni wa kwenda kwenye vyombo vya habari kutoa malalamiko yake dhidi ya taasisi nyingine ambazo anaamini zinamkwaza kiutendaji.Naamini huo ndio uwajibikaji wa kweli wa kukubali kushindwa, kushinda na kukosolewa.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili,Julai 11 mwaka 2010

No comments:

Powered by Blogger.