Header Ads

MALUMBANO HAYA HAYANA TIJA

Na Happiness Katabazi
KIFUNGU cha 7(1)(a) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002; kinasema ni wajibu wa kila mwananchi anayefahamu taarifa za kutendeka au kuna mtu anania ya kutenda uhalifu au mauji,anapaswa atoe taarifa hizo kwenye mamlaka husika za dola.


Na endapo mtu huyo atashindwa kutimiza waibu huo anaweza kushtakiwa kwa kosa la kusaidia kutendeka kwa kosa kwa mujibu wa Sheria ya Kanuni ya Adhabu (Penal Code R:E;2002).

Nacho kifungu cha 99(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002,kina mruhusu hakimu kutoa kibali kwa mwananchi aliyeomba mahakama impatie kibali cha kuendesha kesi binafsi bila kuhusisha waendesha mashtaka wa serikali.

Na kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu Toleo la Pili iliyochapishwa na Oxford Universty Press, inatoa maana ya neno Fisadi .Ina sema Fisadi maana yake ni “Mtu mbaya ,mtongozaji,mharibifu,mpotevu,mwasherati;-guberi”.

Nimelazimika kunukuu vifungu hivyo vya sheria na maana ya neno Fisadi ambalo limefafanuliwa kwenye kamusi hiyo kwasababu kwa takribani wiki mbili sasa kumeibuka malumbano ya hoja ndani na nje ya bunge ambayo yanaendeshwa na wazi wazi na wabunge wengi wa Dar es Salaam, dhidi ya Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dk.Didas Masaburi ambayo malumbano hayo yamekuwa yakibebwa kwa mbeleko ya hali ya juu na baadhi ya vyombo vya habari hali inayoleta kichefuchefu kwa jamii ya watu wanaofikiri sawa sawa na wazalendo wa kweli wa taifa hili.

Malumbano hayo ni kwamba mbunge wa Ilala, Zungu, Mbunge wa Temeke, Abasi Mtemvu, Mbunge wa Kawe, Halima Mdee na Mbunge wa Jimbo la Ubungo John Mnyika ambayo wakiwa ndani ya Bunge walitoa kile wao wanachodai ni ufisadi uliofanyika ndani ya Shirika la Uda na kutaka Dk.Masaburi awajibishwe naye hawakutosheka wabunge hao wakasafiri hadi jijini Dar es Salaam, na kuja na nyaraka mbalimbali wakionyesha kuwa wao hawausiki na kile kilichodaiwa na Dk.Masaburi kuwa wamefanya ufisadi katika jengo la Machinga Complex.

Kwa watu wanaofikiri sawa sawa na tunaofahamu vyema hulka na tabia chafu walizonazo wanasiasa wa nchi hii tunapoendelea kusikiliza malumbano hayo uwa tunakereka na kusikia kichefuchefu kabisa.

Kwani tunaamini kabisa hao wabunge ndiyo watunga sheria wetu wameendelea kujigamba kuwa wanaushahidi wa Dk.Masaburi amefanya ufisadi UDA na Zungu amefanya ufisadi Machinga Complex kwanini wasitekeleze matakwa ya vifungu hivyo vya sheria kwa kupeleka huo ushahidi walionao mfukoni kwenye vyombo vya dola ambavyo ndivyo vyenye thamana ya kufanyia uchunguzi tuhuma hizo wanazitumia hivi sasa kupakana matope mbele ya wapiga kura wao na umma?

Na kama hilo litawashinda kwasababu miongoni mwa wabunge hao walishawahi kutamka kuwa hawana imani na TAKUKURU, kwanini wasiende mahakamani kuomba kibali cha kuendesha kesi binafsi kuliko hivi sasa wanavyoendelea kupakana matope na kushushiana heshima mbele ya wapiga kura na jamii kwa ujumla?

Nadiriki kusema kuwa mimi nikiwa ni miongoni mwa waandishi wachache makini ambao wakati malumbano hayo yakitokea nilichukua hatua ya kuwataadharisha wanahabari wenzangu kuwa wawe makini na malumbano hayo yanayoendelea kwani tayari kuna taarifa za Kiichunguzi zimeanza kuusisha malumbano hayo na ubaguzi wa kidini, uasama na kisasi ya kampuni mmoja ambayo nyuma yake yupo mtu ambaye kwa hasira ya kampuni hiyo ambayo inadaiwa kuwa ana mahusiano nayo ndiyo amekuwa akiendesha chini chini malumbano hayo.

Na kwakuwa watanzania huwa atunyimani maneno tunanyimana matonge ya ugali.Muda si mrefu itakuja kubainika wazi kwamba chanzo na nyuma ya mgogoro huo ambayo minasema hauleti tija kwa taifa letu ni wakina nani wapo nyuma ya mgogoro huyo, na ni kwanini wapo nyuma ya malumbano hayo?

Mbaya zaidi wote wanaolumbana kuhusu kutuhumiana ni viongozi waliochaguliwa na wanachi.Sasa sisi wapiga kula umefika wakati tujiulize ni kwanini hawa viongozi wetu ambao wanatuhumia kupitia vyombo vya habari ni kwanini wanashindwa kuomba viongozi wao wajuu wawaite pamoja na kuweza kutatuliwa kero zao kwenye vikao vya ndani?

Malumbano hayo wanayoyaendeleza kupitia vyombo vya habari, yanatupa picha gani sisi wapiga kura wao?Je malumbano hayo yanatumalizia kero za maji, uhaba wa madawa, barabara mbovu kwenye majimbo yetu?

Na sisi waandishi wa habari ifike mahala tuamke na tutafute kilichopo nyuma ya pazia kwani somo zuru kuhusu ushetani wa wanasiasa wetu wa kupenda kuzuliana majungu na kashfa zisizona ukweli na kutaka waungwe mkono na jamii,wakishafanikiwa azma yao hiyo ya kumchafua mwanasiasa mwenzao wanasiasa hao uwaacha solemba wananchi na vyombo vya habari ambavyo vilikuwa vikiwaunga mkono katika usheni huo pasipo kujua na mfano mzuri ni kashfa ya mkataba wa kufua umeme wa Richmond.

Kwahiyo katika malumbano hayo ya UDA ni vyema waandishi wa habari wakaingia msituni kafanya utafiti wa kweli UDA imeuzwa au inataka kuingia ubia na kampuni binafsi?Maana kuuza shirika la umma ama kuuza ni vitu viwili tofauti. Au je utendaji kazi thabiti wa Dk.Masaburi wa kuanza kufumua uozo ndani jiji hili ndiyo umeanza kuwatia matumbo joto wabunge hao?

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika

0716 774494
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Agosti 13 mwaka 2011.




No comments:

Powered by Blogger.